Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mbona Leo Hakuna Majirani Wanaojali?
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Septemba 1
    • Mbona Leo Hakuna Majirani Wanaojali?

      “Jamii ya kisasa haimtambui jirani,” akasema Benjamin Disraeli, mwanasiasa mashuhuri wa karne ya 19 kutoka Uingereza.

      WAKUBA walio wazee huboresha maisha yao kwa njia isiyo ya kawaida: wana vikundi vinavyoitwa círculos de abuelo yaani, vikundi vya mababu na nyanya. Kulingana na ripoti moja ya mwaka wa 1997, Mkuba 1 kati ya kila Wakuba 5 wazee ni mshiriki wa vikundi hivyo. Kwenye vikundi hivyo wazee hao hupata marafiki, utegemezo na msaada ambao huwawezesha kuishi maisha bora. ‘Madaktari wa familia wanapotaka kusambaza habari kuhusu chanjo ya kuzuia ugonjwa fulani, wao huwaendea wazee wa vikundi hivyo ambao wako tayari na wanaweza kuwasaidia,’ linasema gazeti World-Health.

      Hata hivyo, inasikitisha kwamba katika nchi nyingi za ulimwengu, hakuna vikundi kama hivyo vinavyojali hali ya wazee. Kwa mfano, fikiria kisa chenye kuhuzunisha cha Wolfgang Dircks, aliyeishi katika nyumba fulani za kupanga huko Ulaya magharibi. Miaka kadhaa iliyopita, gazeti The Canberra Times liliripoti kwamba ingawa familia 17 zilizoishi katika nyumba hizo pamoja na Wolfgang hazikuwa zikimwona, ‘hakuna hata mtu mmoja aliyefikiria kubisha mlango wake.’ Hatimaye wakati mwenye nyumba hizo alipokuja, “aliipata mifupa ya Wolfgang ikiwa imeketi mbele ya televisheni.” Kwenye mapaja yake kulikuwa na orodha ya vipindi vya televisheni ya Desemba 5, 1993. Wolfgang alikuwa amekufa kwa muda wa miaka mitano. Huo ni uthibitisho ulioje kwamba majirani hawajali wenzao! Si ajabu kwamba mwandishi mmoja alisema katika makala moja kwenye gazeti The New York Times Magazine kwamba watu wa mahali anapoishi, sawa na watu wa sehemu nyingine nyingi, ‘hawajuani.’ Je, hali iko hivyo mahali unapoishi?

      Ni kweli kwamba jamii fulani za mashambani bado zinafurahia ujirani wa kweli nazo jamii nyingine mijini zinajitahidi kuwasaidia watu wawe wenye kuwajali majirani. Hata hivyo, wakazi wengi wa mijini huhisi wametengwa na pia huhisi wanaweza kupatwa na hatari fulani katika ujirani wao. Wanahisi hivyo kwa kuwa hawajui majirani wao. Jinsi gani?

      Kuishi Bila Kujua Jirani

      Bila shaka wengi wa majirani wetu wanaishi karibu nasi. Mmemeto wa televisheni, vivuli vya watu wakipita karibu na dirisha, kuwashwa na kuzimwa kwa taa, mngurumo wa magari yakiingia na kutoka, sauti za nyayo za watu wakipitapita ushorobani, milango ikifunguliwa na kufungwa, ni ishara kwamba majirani bado wako “hai.” Hata hivyo, hakuwezi kuwa na ujirani wa kweli ikiwa watu wanaoishi karibu-karibu hawajuani au wanapuuzana kwa sababu ya hekaheka za maisha. Huenda watu wakahisi kwamba hakuna haja ya kujishughulisha na majirani au kuhisi wana daraka lolote kuwaelekea. Gazeti Herald Sun la Australia linakiri hivi: ‘Watu hawajui kinachotendeka katika ujirani wao, na hivyo hawahisi wana daraka lolote kuelekea jamii. Sasa ni rahisi kupuuza au kuwaepuka watu wasiopendeza katika jamii.’

      Hali hiyo haishangazi. Katika ulimwengu ambapo watu ni “wenye kujipenda wenyewe,” majirani wameanza kupata matokeo ya maisha yao ya ubinafsi. (2 Timotheo 3:2) Matokeo hayo ni kwamba watu wengi wanakuwa wapweke na wanahisi wametengwa. Hali hiyo hutokeza kutoaminiana, hasa ikiwa kuna jeuri au uhalifu katika ujirani. Nayo hali hiyo ya kutoaminiana hufanya watu wasioneane huruma.

      Hata hali iweje katika ujirani wako, bila shaka unakubali kwamba majirani wema wanafaa katika jamii. Watu hutimiza mambo mengi wanaposhirikiana wakiwa na lengo moja. Majirani wema wanaweza pia kuwa baraka. Makala inayofuata itaonyesha jinsi majirani wanavyoweza kuwa baraka.

  • Majirani Wema Wanafaa
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Septemba 1
    • Majirani Wema Wanafaa

      “Afadhali jirani aliye karibu kuliko ndugu aliye mbali.”—Mithali 27:10.

      MSOMI mmoja wa karne ya kwanza W.K. alimwuliza Yesu hivi: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Katika jibu lake, Yesu hakumweleza tu ni nani aliye jirani yake, bali alimweleza jambo ambalo humfanya mtu awe jirani wa kweli. Yaelekea unajua mfano huo wa Yesu. Wengi wanauita mfano wa Msamaria mwema nao unapatikana katika kitabu cha Injili ya Luka. Yesu alisimulia hivi:

      “Mtu fulani alikuwa akiteremka kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko akaanguka miongoni mwa wapokonyaji, ambao walimvua nguo na pia kumpiga, wakaenda zao, wakimwacha yeye nusura kufa. Sasa, kwa sadfa, kuhani fulani alikuwa akiteremka katika barabara hiyo, lakini, alipomwona, akaenda kupita kando upande wa pili. Hivyohivyo, Mlawi pia, alipofika chini kwenye mahali hapo na kumwona, akaenda kupita kando upande wa pili. Lakini Msamaria fulani mwenye kusafiri katika ile barabara alikuja akamkuta na, alipomwona, akasukumwa na sikitiko. Kwa hiyo akamkaribia akafunga majeraha yake, akimwaga mafuta na divai juu yayo. Kisha akampandisha juu ya hayawani wake mwenyewe akamleta kwenye hoteli ndogo na kumtunza. Na siku iliyofuata akatoa dinari mbili, akampa hizo mtunza-hoteli, na kusema, ‘Mtunze, na chochote kile utumiacho mbali na hiki, mimi nitakulipa nirudipo hapa.’ Ni nani kati ya watatu hawa aonekana kwako kuwa alijifanya mwenyewe jirani kwa mtu aliyeanguka miongoni mwa wapokonyaji?”—Luka 10:29-36.

      Yaelekea msomi huyo alielewa kiini cha mfano huo kwa kuwa alitaja bila kusita ni nani kati ya watu hao aliyekuwa jirani kwa mtu huyo aliyejeruhiwa: “Yeye aliyetenda kwa rehema kumwelekea.” Kisha Yesu akamwambia: “Shika njia yako uende na uwe ukifanya hilohilo wewe mwenyewe.” (Luka 10:37) Huo ni mfano wenye nguvu kama nini kuhusu kuwa jirani wa kweli! Huenda mfano wa Yesu hata ukatuchochea kujiuliza: ‘Mimi ni jirani wa aina gani? Je, mimi huwaona watu wa jamii yangu au taifa langu kuwa tu ndio majirani? Je, mambo hayo hunizuia kuona kwamba nina daraka la kuwasaidia watu wenye matatizo? Je, ninajitahidi niwezavyo kuwa jirani mwema?’

      Uanzie Wapi?

      Ikiwa tunaona kuna uhitaji wa kufanyia jambo hilo maendeleo, basi ni lazima tuanze na maoni yetu. Tunapaswa kuhangaikia kuwa majirani wema. Jambo hilo pia linaweza kuchangia kuwa na majirani wema. Karibu miaka elfu mbili iliyopita, Yesu alikazia kanuni hiyo muhimu kuhusu uhusiano wa wanadamu katika Mahubiri yake maarufu ya Mlimani. Alisema hivi: “Mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.” (Mathayo 7:12) Kuwatendea wengine kwa heshima na fadhili huwachochea wakutendee vivyo hivyo.

      Katika makala “Kumpenda Jirani Yako,” iliyokuwa katika gazeti The Nation Since 1865, Lise Funderburg, mwandishi wa habari na vitabu alitaja mambo madogo-madogo yanayoweza kufanywa ili kuchochea ujirani mwema. Aliandika hivi: ‘Nataka majirani wawasiliane kupitia mambo mengi madogo-madogo yenye fadhili ambayo wanaweza kuwatendea wenzao, kama kuwatunzia watoto au kuwanunulia vitu dukani. Nataka majirani wadumishe uhusiano huo katika ulimwengu unaozidi kutengana na jamii kuvunjika kwa sababu ya woga na uhalifu.’ Kisha anaendelea kusema: “Lazima uanzie mahali fulani. Na huenda ikawa utaanza na jirani yako wa karibu.”

      Gazeti Canadian Geographic pia lilitaja jambo jingine linalofaa ambalo linaweza kuwasaidia majirani wasitawishe maoni yanayofaa kati yao. Mwandishi Marni Jackson alisema: “Huwezi kuchagua majirani wako kama vile huwezi kuchagua washiriki wa familia yako. Unahitaji kuwa na busara, adabu nzuri na uvumilivu ili uwe na uhusiano mzuri na majirani.”

      Majirani Wema Ni Wakarimu

      Ni kweli kwamba wengi wetu husita kuwafikia majirani na kuzungumza nao. Huenda tukaona ikiwa rahisi zaidi kuwaepuka au kujitenga nao. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Kwa hiyo, jirani mwema hujitahidi sana kuwajua majirani wenzake. Ingawa hatataka hasa kusitawisha urafiki wa karibu, atajitahidi kuzungumza nao mara kwa mara, labda akianza kwa tabasamu au kuwapungia mkono kwa urafiki.

      Kama ilivyotajwa juu, ‘mambo hayo madogo-madogo’ ambayo majirani hufanyiana ni muhimu sana katika kuanzisha na kudumisha ujirani mwema. Kwa hiyo, inafaa kujitahidi kumfanyia jirani yako mambo fulani ya fadhili, kwa kuwa mara nyingi kufanya hivyo kutakuza roho ya ushirikiano na kuheshimiana. Zaidi ya hayo, kwa kufanya hivyo, tutakuwa tukifuata ushauri huu wa Biblia: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.”—Mithali 3:27, Yakobo 2:14-17.

      Majirani Wema Wana Shukrani

      Ingefaa kama kila mtu anayesaidiwa au kupokea zawadi angeonyesha shukrani. Inasikitisha kwamba watu hawafanyi hivyo sikuzote. Misaada na zawadi nyingi ambazo zimetolewa kwa nia njema zimepokewa pasipo shukrani, kwa hiyo huenda mtu ambaye alifanya hivyo kwa unyofu akawaza, ‘Sitafanya hivyo tena!’ Mara kwa mara, huenda majirani wako wakaitikia kwa ubaridi tu jitihada zako za kuwasalimu au kuwapungia mkono kwa urafiki.

      Hata hivyo, ingawa mtu anayefanyiwa jambo fulani anaweza kuonekana kana kwamba hana shukrani, mara nyingi hiyo huwa si kweli. Labda huenda kwa sababu ya malezi yake akasita au akaona haya, na hivyo kuitikia kwa ubaridi, bila uchangamfu. Kwa upande mwingine, katika ulimwengu huu usio na shukrani, huenda wengine wakaona urafiki wako kuwa jambo lisilo la kawaida, au wakatilia shaka nia yako. Huenda wakahitaji kupata uhakikisho zaidi. Hivyo, huenda ikachukua muda na pia subira kuanzisha urafiki. Hata hivyo, majirani wakarimu na wenye shukrani watachangia roho ya ujirani mwema, wenye amani na furaha.

      Msiba Unapotokea

      Jirani mwema anafaa sana hasa wakati wa msiba. Wakati wa msiba watu huonyesha roho ya ujirani wa kweli. Wakati huo ripoti nyingi hutolewa kuhusu majirani wanaotenda bila ubinafsi. Msiba unapowapata wote, inaonekana majirani hushirikiana, huku wakijitahidi kuwasaidia wenzao. Mara nyingi hata wale wenye maoni yanayotofautiana hushirikiana.

      Kwa mfano, gazeti The New York Times liliripoti kwamba wakati tetemeko la ardhi lilipoikumba nchi ya Uturuki mwaka wa 1999, watu waliokuwa maadui kwa muda mrefu walishirikiana. “Tumefundishwa kwa miaka mingi tuwachukie Waturuki,” akaandika Anna Stergiou, mwandishi Mgiriki wa makala fulani maalum katika gazeti moja huko Athens. “Lakini hatufurahishwi na msiba mkubwa uliowapata. Tuliguswa moyo sana, na tulilia kana kwamba chuki ambayo tumekuwa nayo kwa muda mrefu ilitoweka tulipoona watoto waliokufa.” Hata baada ya kazi ya kutafuta watu walionusurika kukomeshwa rasmi, vikundi vya waokoaji kutoka Ugiriki viliendelea tu kutafuta walionusurika.

      Bila shaka, kushiriki kazi ya kuokoa watu baada ya misiba ni kitendo kinachofaa cha ujasiri na ujirani mwema. Hata hivyo, kuokoa uhai wa jirani kwa kumwonya kabla msiba haujatokea ndicho kitendo kinachofaa zaidi cha ujirani mwema. Kwa kusikitisha, historia inaonyesha kwamba mara nyingi wale wanaowaonya majirani wenzao kuhusu misiba inayokaribia hawakaribishwi vizuri, kwa kuwa wakati wanapotoa onyo msiba huo unaokaribia huwa hautambuliki kwa urahisi. Mara nyingi watu hawaamini watu hao wenye kutoa onyo. Lazima wale wanaojaribu kuwasaidia watu wasiojua hatari wanayokabili wawe wenye bidii na kujitolea.

      Tendo Kuu Zaidi la Ujirani Mwema

      Leo, kuna tukio fulani kuu zaidi kuliko msiba wa kiasili ambalo litawapata wanadamu hivi karibuni. Tukio hilo ni hatua iliyotabiriwa ya Mungu Mweza Yote ya kuondoa duniani uhalifu, uovu, na matatizo yote yanayohusiana na mambo hayo. (Ufunuo 16:16; 21:3, 4) Tukio hilo kuu si la kuwaziwa tu bali ni hakika kabisa! Mashahidi wa Yehova wana hamu ya kushiriki na watu wengi iwezekanavyo ujuzi unaohitajiwa ili kuokoka tukio hilo linalokaribia ambalo litautikisa ulimwengu. Hiyo ndiyo sababu wao huendelea bila kuacha kufanya kazi yao inayojulikana sana ya kuhubiri ulimwenguni pote. (Mathayo 24:14) Wao hufanya hivyo kwa hiari kwa kuwa wanampenda Mungu na jirani.

      Kwa hiyo, usiruhusu ubaguzi au kuudhika kukuzuie usiwasikilize Mashahidi watakapokuja nyumbani kwako au kuzungumza nawe mahali penginepo. Wao wanajitahidi tu kuwa majirani wema. Kwa hiyo, usikatae wanapojitolea kujifunza Biblia pamoja nawe. Jifunze juu ya uhakikisho unaotolewa na Neno la Mungu kwamba wakati ujao karibuni, majirani wataishi pamoja kwa furaha. Wakati huo, uhusiano wa kirafiki ambao wengi wetu hutamani sana hautavunjwa na ubaguzi wa kijamii, kidini, au kitabaka.

      [Picha katika ukurasa wa 6, 7]

      Inafaa kujitahidi kufanya mambo fulani ya fadhili katika ujirani wako

      [Hisani]

      Tufe: Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki