Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Maamuzi Mazuri Yalileta Baraka za Kudumu
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Januari 1
    • Siku moja, Ndugu Knorr aliniuliza ikiwa ningekubali kwenda nchini Ubelgiji. Hata hivyo, baada ya siku kadhaa, aliniuliza ikiwa ningekubali mgawo wa kwenda Uholanzi. Nilipopokea barua ya mgawo, ilisema kwamba nimepewa “mgawo wa kuwa mtumishi wa ofisi ya tawi.” Sikuamini macho yangu.

      Mnamo Agosti 24, 1950 (24/8/1950), nilifunga safari ya siku 11 kwa meli kuelekea Uholanzi. Ulikuwa wakati wa kutosha kusoma Biblia mpya ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Nilifika Rotterdam Septemba 5, 1950 (5/9/1950), ambako nilikaribishwa kwa uchangamfu na familia ya Betheli. Ingawa Vita vya Pili vya Ulimwengu vilisababisha uharibifu mkubwa, akina ndugu walijitahidi sana kuanzisha tena utendaji wa Kikristo. Nilipokuwa nikiwasikiliza wakisimulia jinsi walivyodumisha utimilifu wakati wa mateso makali, niliwazia kwamba ingekuwa vigumu kwao kufanya kazi chini ya mtumishi wa ofisi ya tawi asiye na uzoefu. Hata hivyo, baada ya muda ilionekana wazi kwamba sikuwa na sababu yoyote ya kuwa na wasiwasi.

      Bila shaka, mambo fulani yalihitaji kushughulikiwa. Nilifika kabla tu ya kusanyiko, nami nilivutiwa kuona jinsi maelfu ya wajumbe walivyotayarishiwa mahali pa kulala kwenye uwanja wa kusanyiko. Nilipendekeza kwamba katika kusanyiko litakalofuata wajumbe wakaribishwe katika nyumba za watu. Akina ndugu waliona pendekezo hilo kuwa zuri, lakini lisilofaa katika nchi yao. Baada ya kujadiliana kuhusu jambo hilo, tulikubaliana kwamba nusu ya wajumbe walale kwenye uwanja wa kusanyiko na nusu wakaribishwe kwenye nyumba za watu ambao hawakuwa Mashahidi. Nikiwa mwenye shangwe, nilimweleza Ndugu Knorr matokeo ya mpango wetu alipohudhuria kusanyiko hilo. Hata hivyo, baadaye shangwe yangu ilipotea mara tu niliposoma ripoti kuhusu kusanyiko hilo katika Mnara wa Mlinzi. Ripoti hiyo ilisema: “Tuna hakika kwamba wakati ujao ndugu watakuwa na imani na hivyo kuwatafutia wajumbe mahali ambapo wataweza kutoa ushahidi kwa matokeo zaidi, yaani, katika nyumba za watu.” Hivyo ndivyo hasa tulivyofanya “wakati ujao” ulipofika!

      Mnamo Julai (Mwezi wa 7) 1961, wawakilishi wawili wa ofisi yetu ya tawi walialikwa kuhudhuria mkutano huko London pamoja na wawakilishi wa ofisi nyingine. Ndugu Knorr alitangaza kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko Matakatifu ingepatikana katika lugha zaidi, kutia ndani Kiholanzi. Habari hizo zilitusisimua kama nini! Hatukujua mradi huo ulihusisha nini. Miaka miwili baadaye, mnamo 1963, nilifurahi kushiriki katika programu ya kusanyiko huko New York ambako Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kiholanzi ilitolewa.

      Maamuzi na Migawo Mipya

      Mnamo Agosti (Mwezi wa 8) 1961, nilimwoa Leida Wamelink. Familia yao yote ilikuwa imekubali kweli mwaka wa 1942 wakati wa mateso ya Wanazi. Leida alianza kufanya upainia mwaka wa 1950 na kuanza utumishi wa Betheli mwaka wa 1953. Bidii yake Betheli na kutanikoni ilinisadikisha kwamba angekuwa mshiriki mshikamanifu katika huduma yangu.

      Mwaka mmoja hivi baada ya kufunga ndoa, nilialikwa Brooklyn kwa ajili ya mazoezi ya ziada ya miezi kumi. Wakati huo, wake hawakwenda pamoja na waume zao. Ingawa Leida alikuwa na afya mbaya, kwa upendo alikubali niitikie mwaliko huo. Baadaye, afya ya Leida ilizidi kuwa mbaya. Tulijaribu kuendelea na utumishi wa Betheli lakini mwishowe tukaamua ingefaa zaidi kuendelea na utumishi wa wakati wote shambani. Hivyo, tukaanza kazi ya mzunguko. Muda mfupi baadaye, mke wangu alifanyiwa upasuaji mkubwa. Marafiki walitutegemeza kwa upendo, hivyo tukafaulu kukabiliana na hali hiyo, na mwaka mmoja baadaye tulikubali kutumika katika kazi ya wilaya.

      Kwa muda wa miaka saba, tulifurahia kazi yenye kuchangamsha ya kusafiri. Kisha, tukahitajika kufanya uamuzi mzito nilipopewa mgawo wa kufundisha Shule ya Huduma ya Ufalme iliyofanyiwa Betheli. Tulikubali, ingawa ilikuwa vigumu kufanya mabadiliko kwa kuwa tulipenda kazi ya kusafiri. Madarasa 47 ya shule hiyo, ambayo yalichukua majuma mawili kila moja, yalitupa nafasi ya kushiriki baraka za kiroho pamoja na wazee wa makutaniko.

      Wakati huo, nilikuwa nikifanya mipango ya kumtembelea mama yangu mwaka wa 1978. Lakini kwa ghafula, mnamo Aprili 29, 1977 (29/4/1977), tulipokea telegramu iliyotujulisha kwamba Mama amekufa. Nilihuzunika sana kwa sababu singesikia tena sauti yake changamfu wala kumwambia tena jinsi ninavyothamini yote aliyonifanyia.

      Mwishoni mwa Shule ya Huduma ya Ufalme, tuliombwa tuwe washiriki wa familia ya Betheli. Miaka iliyofuata, nilitumika kwa miaka kumi nikiwa mratibu wa Halmshauri ya Tawi. Baadaye, Baraza Linaloongoza liliweka rasmi mratibu mpya, ambaye angeweza kushughulikia daraka hilo vizuri zaidi. Ninashukuru sana kwa jambo hilo.

      Kutumika Kadiri Umri Unavyoruhusu

      Mimi na Leida tuna umri wa miaka 83 sasa. Nimefurahia kutumika katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 60, na kwa miaka 45 iliyopita nimetumika pamoja na mke wangu mshikamanifu. Ameona utegemezo ambao amenipa katika migawo yetu yote kuwa sehemu ya utumishi wake mtakatifu kwa Yehova. Kwa sasa, tukiwa Betheli na pia katika kutaniko, tunafanya kadiri tunavyoweza.—Isaya 46:4.

      Mara kwa mara, tunafurahia kukumbuka matukio mazuri maishani mwetu. Hatujuti kamwe kwa sababu ya yale ambayo tumefanya katika utumishi wa Yehova, na tuna hakika kwamba maamuzi tuliyofanya mapema maishani yalikuwa bora kabisa. Tumeazimia kuendelea kumtumikia na kumheshimu Yehova kwa nguvu zetu zote.

  • Maamuzi Mazuri Yalileta Baraka za Kudumu
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Januari 1
    • [Picha katika ukurasa wa 15]

      Siku yetu ya arusi, Agosti 1961

      [Picha katika ukurasa wa 15]

      Nikiwa na Leida leo

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki