Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yesu Alikuwa na Maoni Gani Kuhusu Siasa?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Mei 1
    • Yesu Alikuwa na Maoni Gani Kuhusu Siasa?

      WAANDIKAJI wa Vitabu vya Injili wanataja matukio kadhaa katika huduma ya Yesu ambayo yalifanya akabiliane moja kwa moja na siasa. Kwa mfano, muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa akiwa na umri wa miaka 30 hivi, Ibilisi alitaka kumpa cheo cha kuwa mtawala wa ulimwengu. Kisha, katika huduma yake, umati ulitaka kumfanya kuwa mfalme. Pia baadaye, watu walijaribu kumlazimisha kuwa mwanasiasa. Yesu alitendaje? Acha tuchunguze matukio hayo.

      Mtawala wa Ulimwengu. Vitabu vya Injili vinataja kwamba Ibilisi alitaka kumpa Yesu utawala juu ya “falme zote za ulimwengu.” Fikiria mambo ambayo Yesu angefanya ili kuwaondolea wanadamu mateso ikiwa angetumia mamlaka ya mtawala wa ulimwengu! Bila shaka, mtu anayeamini kwamba siasa ndiyo inayoweza kusuluhisha matatizo ya wanadamu na anatamani kuyaondoa, hangekataa cheo kama hicho. Lakini Yesu alikataa.​—Mathayo 4:8-11.

      Mfalme. Watu wengi walioishi wakati wa Yesu walitamani sana kuwa na mtawala ambaye angeweza kutatua matatizo yao ya kiuchumi na kisiasa. Kwa sababu walipendezwa na uwezo wa Yesu, walitaka ajihusishe na siasa. Yesu alitendaje? Yohana, mwandikaji wa Injili anasema: “Yesu, akijua walikuwa karibu kuja kumkamata wamfanye kuwa mfalme, akaondoka tena kwenda mlimani akiwa peke yake.” (Yohana 6:10-15) Ni wazi kwamba Yesu alikataa kujihusisha na siasa.

      Mwanasiasa. Ona kilichotokea siku kadhaa kabla ya kifo cha Yesu. Wanafunzi wa Mafarisayo, ambao walitaka kupata uhuru kutoka kwa Milki ya Roma, wakishirikiana na Waherode ambao walikuwa wafuasi wa chama cha kisiasa kilichounga mkono Waroma, walienda kuzungumza na Yesu. Walitaka kumlazimisha aonyeshe msimamo wake kisiasa. Walimuuliza ikiwa Wayahudi walipaswa kulipa kodi kwa Waroma.

      Marko aliandika jibu hili la Yesu: “‘Kwa nini mnanijaribu? Nileteeni dinari niitazame.’ Wakaleta moja. Naye akawaambia: ‘Sanamu hii na mwandiko huu ni za nani?’ Wakamwambia: ‘Ni za Kaisari.’ Ndipo Yesu akasema: ‘Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.’” (Marko 12:13-17) Kitabu Church and State​—The Story of Two Kingdoms kinasema hivi kuhusu jibu la Yesu: “Alikataa kutenda kama masihi wa kisiasa na kwa busara akaweka mipaka kati ya Kaisari na Mungu.”

      Hata hivyo, Yesu alisikitishwa na matatizo yaliyowapata wanadamu kama vile umaskini, ufisadi, na ukosefu wa haki. Hata Biblia inaonyesha kwamba aliguswa sana na hali yenye kuhuzunisha ya watu waliomzunguka. (Marko 6:33, 34) Lakini Yesu hakuanzisha kampeni ya kuondoa ukosefu wa haki duniani, ingawa watu fulani walijaribu kumshawishi ajiingize katika siasa.

      Kama vile mifano hiyo inavyoonyesha, ni wazi kwamba Yesu alikataa kujihusisha na mambo ya kisiasa. Lakini vipi kuhusu Wakristo leo? Wanapaswa kufanya nini?

  • Wakristo Wanapaswa Kufanya Nini Leo?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Mei 1
    • Wakristo Wanapaswa Kufanya Nini Leo?

      WAKRISTO wa kweli leo hawashiriki katika siasa. Kwa nini? Kwa sababu wanaiga mfano wa Yesu. Alisema hivi kujihusu: “Mimi si sehemu ya ulimwengu.” Na akasema hivi kuwahusu wafuasi wake: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19; 17:14) Fikiria sababu kadhaa kwa nini Wakristo hawapaswi kujiingiza katika siasa.

      1. Wanadamu hawana uwezo kamili. Biblia inasema kwamba wanadamu hawana uwezo wala haki ya kujitawala. Nabii Yeremia aliandika: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”​—Yeremia 10:23.

      Kama vile ambavyo wanadamu hawakuumbwa wakiwa na uwezo wa kupaa angani kwa nguvu zao wenyewe, vilevile hawakuumbwa wakiwa na uwezo wa kujitawala wenyewe kwa mafanikio. Akionyesha kwamba serikali hazina uwezo kamili, mwanahistoria David Fromkin alisema hivi: “Serikali hufanyizwa na wanadamu; hivyo basi mara nyingi hazifaulu na wakati wao ujao haujulikani. Zina nguvu kwa kiasi fulani, lakini si kikamili.” (The Question of Government) Ndiyo sababu Biblia inatuonya tusiwategemee wanadamu!​—Zaburi 146:3.

      2. Roho waovu wanaongoza wanadamu. Shetani alipotaka kumpa Yesu utawala wa dunia, Yesu hakusema kwamba Ibilisi hakuwa na mamlaka ya kumpa falme zote za ulimwengu. Baadaye, hata Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu.” Miaka kadhaa baadaye mtume Paulo alisema kwamba Shetani ni “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (Yohana 14:30; 2 Wakorintho 4:4) Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Tuna kushindana mweleka . . . juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12) Roho waovu ndio wanaotawala ulimwengu ingawa watu wengi hawafahamu hivyo. Jambo hilo linapaswa kufanya tuwe na maoni gani kuhusu siasa?

      Fikiria ulinganisho huu: Kama vile mashua ndogo zinavyoweza kusukumwa na upepo wa baharini, ndivyo mifumo ya kisiasa ya wanadamu inavyoongozwa na nguvu za roho waovu. Na kama vile mabaharia katika mashua hizo wasivyoweza kubadili upepo huo wenye nguvu, ndivyo pia wanasiasa wasivyoweza kubadili nguvu za roho hao waovu. Roho hao waovu wameazimia kuwapotosha wanadamu kabisa na kusababisha ‘ole kwa dunia.’ (Ufunuo 12:12) Kwa hiyo, badiliko la kweli linaweza kuletwa tu na mtu mwenye nguvu kuliko Shetani na mashetani wake. Mtu huyo ni Yehova Mungu.​—Zaburi 83:18; Yeremia 10:7, 10.

      3. Wakristo wa kweli wanaunga mkono Ufalme wa Mungu peke yake. Yesu na wanafunzi wake walijua kwamba Mungu alikuwa amepanga wakati ambao atasimamisha serikali mbinguni itakayotawala dunia nzima. Biblia inasema serikali hiyo ni Ufalme wa Mungu na inafunua kwamba Yesu Kristo ndiye aliyechaguliwa kuwa Mfalme. (Ufunuo 11:15) Kichwa kikuu cha mahubiri ya Yesu kilikuwa “habari njema ya ufalme wa Mungu,” kwa sababu alijua kwamba Ufalme huo unawahusu wanadamu wote. (Luka 4:43) Pia, aliwafundisha wanafunzi wake kusali: “Ufalme wako na uje.” Kwa nini? Kwa sababu chini ya ufalme huo, bila shaka, mapenzi ya Mungu yatatimia mbinguni na duniani.​—Mathayo 6:9, 10.

      Hivyo basi, serikali za wanadamu zitapatwa na nini? Biblia inajibu kwamba serikali za “dunia nzima inayokaliwa,” zitaharibiwa. (Ufunuo 16:14; 19:19-21) Ikiwa kwa kweli mtu anaamini kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa serikali zote za wanadamu, basi itakuwa jambo la busara kutounga mkono mifumo ya kisiasa. Zaidi ya hayo, ikiwa mtu ataunga mkono serikali za wanadamu ambazo zitaharibiwa, basi atakuwa akimpinga Mungu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki