-
Albania2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mwaka wa 1947, Albania ikajiunga na Muungano wa Sovieti na Yugoslavia na kuanza kuzozana na Ugiriki. Mwaka uliofuata, Albania ikakata mahusiano kati yake na Yugoslavia na kuboresha uhusiano wake na Muungano wa Sovieti. Yeyote ambaye hakuunga mkono maoni ya serikali alifukuzwa nchini. Kwa sababu ya msimamo ambao akina ndugu walichukua, walikumbwa na upinzani mkali na kuchukiwa.
Kwa mfano, mwaka wa 1948, ndugu na dada sita walikuwa wamekusanyika kwa ajili ya Ukumbusho katika kijiji kidogo. Polisi wakaingia ghafula mahali walipokuwa wakikutania na kuwapiga kwa saa nyingi kabla ya kuwaruhusu waondoke. Majuma kadhaa baadaye, polisi walimkamata ndugu aliyetoa hotuba ya Ukumbusho na kumlazimisha asimame kwa saa 12. Usiku wa manane, mkuu wa polisi akafoka, “Kwa nini ulivunja sheria?”
“Kwetu sisi, sheria ya Bwana ni muhimu zaidi kuliko sheria ya nchi!” ndugu huyo akamjibu.
Akiwa na ghadhabu, polisi huyo akamzaba kofi, kisha alipoona ndugu huyo akigeuza kichwa chake akamuuliza, “Unafanya nini?”
“Nimekuambia sisi ni Wakristo,” ndugu huyo akasema. “Yesu alitufundisha kwamba mtu akikupiga shavu moja, mgeuzie la pili.”
“Kwa sababu hiyo ni amri ya Bwana wenu,” akasema polisi huyo mwenye ghadhabu, “sitamtii, sitakupiga! Ondoka!”
-
-
Albania2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Idara ya Usalama wa Nchi, Sigurimi, ndiyo iliyokuwa na jukumu la kulinda usalama wa taifa katika miaka hiyo. Kwa kuwa sikuzote idara hiyo ilikuwa chonjo kuona tisho lolote dhidi ya Ukomunisti, Sotir aliyekuwa na bidii ya kuhubiri hangeweza kuwaponyoka. Walimkamata, wakamfungia kwa saa nyingi, wakampiga, na kumwamuru asihubiri.
Sotir alipoachiliwa, aliwasiliana na Leonidha, ambaye alimpeleka kwa Spiro Karajani, daktari aliyekuwa amejifunza kweli miaka kadhaa awali. Mbali na kumtibu, Spiro alimsaidia Sotir kuielewa kweli vizuri zaidi.
“Ukikamatwa tena,” Spiro akamshauri Sotir, “kabla ya kutia sahihi chochote, hesabu kila neno na kila mstari. Tia mstari mwishoni mwa maneno yao. Usiache nafasi yoyote. Soma kila kitu kwa uangalifu. Hakikisha kwamba kile unachotia sahihi ndicho ulichosema.”
Siku mbili tu baadaye, polisi wakamkamata Sotir akihubiri tena. Kwenye kituo cha polisi, maofisa walimwamuru atie sahihi taarifa ya polisi. Kabla tu ya kutia sahihi, akakumbuka shauri la Spiro. Licha ya kushinikizwa na polisi afanye haraka, Sotir alihakikisha kwamba amesoma kila neno.
“Samahani,” akasema, “Siwezi kutia sahihi. Sikusema maneno haya. Nikitia sahihi taarifa hii, nitakuwa nasema uwongo, nami siwezi kusema uwongo.”
Polisi hao waliposikia hivyo, wakatengeneza mjeledi wa kamba na kuanza kumpiga Sotir. Alipozidi kukataa, wakamlazimisha ashike nyaya za umeme na kuanza kumpiga kwa umeme.
“Maumivu yaliponizidia,” Sotir akumbuka, “nilisali kwa machozi. Kisha ghafula, mlango ukafunguka. Nikamwona afisa mkuu. Alitupa jicho kisha akageuka. ‘Acheni!’ akaamuru. ‘Mnavunja sheria!’” Walijua vizuri kwamba mateso ni kinyume cha sheria. Polisi wakaacha kumtesa, lakini hawakuacha kumshinikiza Sotir atie sahihi taarifa hiyo. Hata hivyo, alikataa katakata.
Mwishowe wakasema: “Sawa basi!” Kisha, shingo upande, wakaandika taarifa ya Sotir mwenyewe iliyokuwa na ushahidi mzuri. Wakamkabidhi. Licha ya kupigwa kwa saa nyingi na kupigwa kwa umeme, Sotir alisoma kila neno kwa makini. Sentensi ilipoishia katikati ya mstari, alitia mstari mwishoni mwa sentensi hiyo.
“Ulijifunzia wapi kufanya hivi?” maafisa hao wakauliza kwa mshangao.
“Yehova alinifundisha kutotia sahihi mambo ambayo sikusema,” akajibu Sotir.
“Haya, na ni nani anayekupa hiki?” afisa mmoja akamuuliza huku akimpa kipande cha mkate na jibini. Ilikuwa mwendo wa saa tatu usiku, naye Sotir alikuwa na njaa kali, kwa kuwa hakuwa ameonja chochote siku nzima. “Ni Yehova? Hapana. Ni sisi.”
“Yehova ana njia nyingi,” Sotir akajibu. “Yeye ndiye ameichochea mioyo yenu.”
“Tutakuacha uende zako,” wakasema maafisa hao waliokuwa wametamauka, “lakini ukihubiri tena, utakiona.”
“Kama ni hivyo, msiniachilie kwa sababu mkiniachilia, nitaendelea kuhubiri.”
“Na usithubutu kumwambia yeyote mambo yaliyokupata hapa!” afisa akamwamuru.
“Nikiulizwa,” akasema Sotir, “siwezi kudanganya.”
Polisi akamfukuza, “Ondoka!”
Sotir ni mmoja tu kati ya wengi walioteswa kwa njia hiyo.
-