-
Unaweza Kufaidika Kutokana na Agano JipyaMungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
-
-
16. Andiko la Ufunuo 7:9, 14 linawatia moyo jinsi gani washiriki wa “umati mkubwa”?
16 Andiko la Ufunuo 7:9, 14, linaonyesha “umati mkubwa” ukiwa ‘umevikwa kanzu nyeupe,’ zinazowakilisha msimamo safi mbele za Mungu. Umati huo mkubwa unakusanywa sasa ili kuwa tayari kuokoka “dhiki kuu.” Hivyo basi, kwa kiasi fulani hata sasa, umati huo una msimamo wa uadilifu mbele za Mungu. Wanatangazwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Yehova. (Rom. 4:2, 3; Yak. 2:23) Hiyo ni faida iliyoje! Ikiwa wewe ni sehemu ya umati mkubwa, unaweza kuwa na hakika kwamba Mungu yuko tayari kukusaidia unapoendelea kujitahidi kubaki safi machoni pake.
17. Ni kwa njia gani Yehova ‘hakumbuki’ dhambi tena?
17 Inakuwaje baada ya Mungu kusamehe dhambi za wale wenye kibali chake? Kama tulivyokwisha kuona, Yehova alisema kupitia Yeremia: “Nitalisamehe kosa lao, na dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yer. 31:34) Mungu anawasaheme watiwa-mafuta kwa msingi wa dhabihu ya Yesu. Vivyo hivyo, Mungu anaweza kusamehe dhambi za umati mkubwa kwa msingi wa ‘damu ya agano’ hilohilo. Yeremia anaposema kwamba Mungu ‘hatazikumbuka’ dhambi tena haimaanishi kwamba Mungu ni msahaulifu na hivyo hataweza kukumbuka dhambi zao. Badala yake, inamaanisha kwamba Yehova akiisha kutoa nidhamu inayohitajiwa na kumsamehe mkosaji mwenye kutubu, Mungu anaitupa dhambi hiyo nyuma yake. Fikiria dhambi ambazo Mfalme Daudi alifanya kuhusiana na Bath-sheba na Uria. Daudi alipata nidhamu na kuvuna matokeo ya dhambi zake. (2 Sam. 11:4, 15, 27; 12:9-14; Isa. 38:17) Hata hivyo, Mungu hakuendelea kumhesabia Daudi dhambi hizo. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 7:17, 18.) Kama inavyoonyeshwa katika agano jipya, Yehova akishasamehe dhambi kwa msingi wa dhabihu ya Yesu, hazikumbuki tena.—Eze. 18:21, 22.
18, 19. Tunaweza kujifunza nini kuhusu msamaha katika agano jipya?
18 Agano jipya linakazia jinsi Yehova ameshughulika na wanadamu wenye dhambi, watiwa-mafuta walio katika agano hilo, na wale walio na tumaini la kuishi duniani. Unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova akishakusamehe, hatakumbuka dhambi zako tena.
-
-
Unaweza Kufaidika Kutokana na Agano JipyaMungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
-
-
BARAKA ZA SASA NA ZA WAKATI UJAO ZA AGANO JIPYA
20. Mtazamo wetu leo unatofautiana jinsi gani na mtazamo wa watu wengi katika siku za Yeremia?
20 Katika siku za Yeremia, ni kana kwamba Wayahudi wengi walikuwa wakisema: “Yehova hatatenda mema, wala hatatenda mabaya.” (Sef. 1:12) Ijapokuwa walikuwa na ujuzi fulani kumhusu Yehova, walihisi kwamba hangechukua hatua; wala hakutazamia waishi kulingana na viwango vyovyote. Hata hivyo, tunajua kwamba Mungu anaona mambo yote. Tunamwogopa Mungu kwa njia inayofaa na bila shaka tungependa kuepuka kufanya mambo mabaya. (Yer. 16:17) Wakati uleule, tunajua kwamba Yehova ni Baba mwenye fadhili. Yeye hutambua matendo yetu mema, iwe wengine wanaona au hapana.—2 Nya. 16:9.
Wale ambao wamemtumikia Mungu kwa uaminifu watafurahia baraka zake za wakati ujao
21, 22. Kwa nini huhitaji kuendelea kuambiwa: ‘Mjue Yehova’?
21 Jambo moja lenye kutokeza kuhusu agano jipya ni hili: “Nitaitia sheria yangu ndani yao, nami nitaiandika katika moyo wao. Nami nitakuwa Mungu wao, . . . Nao hawatafundishana tena kila mtu na mwenzake wala kila mtu na ndugu yake, wakisema, ‘Mjueni Yehova!’ kwa maana wote watanijua mimi.” (Yer. 31:33, 34) Watiwa-mafuta walio duniani leo wameonyesha kwamba wana sheria ya Mungu ndani yao. Wanapenda kweli wanazopata ndani yake, badala ya kutegemea mafundisho ya wanadamu. Nao wanafurahia kushiriki ujuzi wa Biblia pamoja na wale wa umati mkubwa. Hivyo, wale wenye tumaini la kuishi duniani wamepata pia kumjua na kumpenda Yehova. Wanajitiisha chini ya mwongozo wake na wanaamini ahadi zake. Huenda wewe ni mmoja wao. Umepata kumjua vizuri na kujenga uhusiano wa kibinafsi pamoja naye. Hilo ni pendeleo kubwa kama nini!
22 Umeweza kuimarisha uhusiano wako pamoja na Yehova jinsi gani? Bila shaka unakumbuka pindi ambazo ulihisi kwamba amejibu sala zako. Hali kama hizo zilikusaidia kumthamini Mungu hata zaidi. Huenda ulihisi kuwa anakusaidia ulipokumbuka andiko fulani ambalo lilikusaidia kukabiliana na shida fulani. Zithamini sana pindi kama hizo. Unapoendelea kujifunza Neno lake, ujuzi wako utaendelea kuongezeka, nawe utazidi kufaidika.
23. Kumjua Yehova kunaweza kukuondolea jinsi gani hisia zenye kusumbua?
23 Hata hivyo, kuna baraka nyingine inayohusianishwa na agano jipya ambayo tunaweza kupata leo. Kujua kwamba Yehova ndiye anayesamehe kupatana na agano hilo kunaweza kutuondolea hisia za hatia zinazotusumbua. Kwa mfano, wengine ambao walitoa mimba kabla ya kujua kanuni za Mungu huenda wakajiona kuwa wenye hatia na kuhuzunika kwa sababu waliua kimakusudi. Wengine wanahisi hivyo kwa sababu waliua walipokuwa vitani. Dhabihu ya fidia ya Yesu, sehemu muhimu ya agano jipya, inaandaa msamaha kwa wale wanaotubu kikweli. Basi je, hatupaswi kuwa na hakika kwamba ikiwa Yehova ametusamehe dhambi zetu, jambo hilo limesahaulika? Hatupaswi kuendelea kuweka akilini dhambi ambazo Yehova amesamehe kabisa.
24. Masimulizi ya Yeremia 31:20 yanakutia moyo kwa njia gani?
24 Tunapata uthibitisho ulio wazi wa msamaha wa Mungu kwenye Yeremia 31:20. (Soma.) Makumi ya miaka kabla ya siku za Yeremia, Yehova aliliadhibu taifa la makabila kumi ya ufalme wa kaskazini wa Israeli (lililowakilishwa na Efraimu, kabila mashuhuri) kwa sababu ya ibada ya sanamu. Walipelekwa uhamishoni. Hata hivyo, Mungu aliwapenda sana watu wa taifa hilo na akawaonyesha upendo mwororo. Bado aliwapenda kama “mtoto anayetendewa kwa upendo.” Alipowafikiria, matumbo yake ‘yalikuwa na msukosuko,’ yaani, hisia zake za ndani zilichochewa. Masimulizi hayo, yanayozungumziwa kuhusiana na agano jipya, yanaonyesha kwamba Yehova huwa tayari kuwasamehe wale wanaotubu kwa sababu ya makosa yao ya wakati uliopita.
25. Kwa nini unapaswa kumshukuru Yehova kwa sababu ya agano jipya?
25 Ahadi ya Yehova ya kusamehe dhambi kupitia agano jipya itatimizwa kikamili mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Yesu Kristo, pamoja na makuhani 144,000 walio chini yake, watakuwa wamewarudisha wanadamu washikamanifu watakaopita lile jaribu la mwisho kwenye ukamilifu. Baada ya mtihani wa mwisho, wanadamu watakuwa washiriki kamili wa familia ya Yehova ya ulimwenguni pote. (Soma Waroma 8:19-22.) Kwa karne nyingi, wote wamekuwa wakiugua kwa kulemewa na dhambi. Hata hivyo, wakati huo, uumbaji wa Yehova utakuwa na “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu,” uhuru kutokana na dhambi na kifo. Hivyo basi, uwe na hakika kwamba kupitia mpango wenye upendo wa agano jipya, unaweza kupata faida nyingi. Unaweza kufaidika sasa na milele kupitia “chipukizi” la Daudi na kufurahia “uadilifu katika nchi.”—Yer. 33:15.
-