-
Kupiga Mbiu ya Kurudi kwa BwanaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Kufungua Mlango wa “Kueneza Gospeli Kupitia Magazeti ya Habari”
Kufikia mwisho wa karne ya 19, ulimwengu ulikuwa umeenezwa nyuzi za simu. Mawasiliano ya simu yalikuwa si ghali na yalikuwa ya kasi; yalikuwa yamebadili sana uchapishaji wa magazeti ya habari. Habari zingeweza kupelekwa kwa haraka katika umbali mrefu na kuchapishwa katika magazeti ya habari. Katika sehemu ya mapema ya karne ya 20, C. T. Russell na washirika wake waliona magazeti ya habari kuwa njia yenye matokeo ya kufikia idadi kubwa za watu. Baadaye Russell alisema hivi: “Magazeti ya habari yamekuwa jambo kubwa katika maisha ya kila siku katika ulimwengu uliostaarabika.”
Toleo la Desemba 1, 1904, la Watch Tower lilitangaza kwamba mahubiri ya C. T. Russell yalikuwa yakitokea katika magazeti ya habari matatu. Toleo lililofuata la Watch Tower, chini ya kichwa “Kueneza Gospeli Kupitia Magazeti ya Habari,” liliripoti hivi: “Mamilioni ya mahubiri yametawanywa hivyo karibu na mbali; na angalau baadhi yayo yametokeza mema. Ikiwa Bwana apenda tutaterema kuona ‘mlango’ huu ukiendelea kufunguka, au hata ufunguke zaidi.” Mlango wa “kueneza gospeli kupitia magazeti ya habari” ulifunguka hata zaidi. Kwa kweli, kufikia 1913 ilikadiriwa kwamba kupitia magazeti ya habari 2,000 mahubiri ya Russell yalikuwa yakifikia wasomaji 15,000,000!
Ingawa hivyo, Russell aliweza kuhakikishaje kwamba mahubiri ya kila juma yalichapishwa hata wakati alipokuwa akisafiri? Kila juma alipelekea shirika la magazeti ya habari, barua ya simu ya mahubiri (yenye urefu upatao safu mbili za gazeti). Nalo shirika hilo, likapelekea upya kwa njia ya simu wachapaji wa magazeti ya habari mahubiri hayo katika Marekani, Kanada, na Ulaya.
Russell alisadikishwa kwamba Bwana alikuwa amesukuma mlango wa kuhubiri kupitia magazeti ya habari ukawa wazi kabisa. Wakati wa mwongo wa kwanza wa karne ya 20, ujumbe wa Biblia ambao Russell na washirika wake walikuwa wakipigia mbiu ulipata kujulikana kwa mapana sana kupitia mahubiri hayo ya magazeti ya habari. Pindi moja kichapo kimoja kiitwacho The Continent kilitaarifu hivi kuhusu Russell: “Maandishi yake yasemekana kuwa na mwenezo mkubwa zaidi kupitia magazeti ya habari kila juma kuliko yale ya mtu mwingine yeyote aliye hai; labda, mkubwa zaidi ya mwenezo uliojumlishwa pamoja wa maandishi ya makasisi na wahubiri wote katika Amerika Kaskazini.”
-
-
Kupiga Mbiu ya Kurudi kwa BwanaMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Picha katika ukurasa wa 58]
Ilikadiriwa kwamba mwaka mmoja, kupitia magazeti ya habari 2,000, mahubiri ya C. T. Russell yalikuwa yakifikia wasomaji 15,000,000
-