-
Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya KweliMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Hawa Wanafunzi wa Biblia hawakuwa na uhakika kabisa ni jambo gani lingetukia. Walisadikishwa kwamba tokeo halingekuwa kuteketezwa kwa dunia na kufutiliwa mbali kwa uhai wa kibinadamu. Badala ya hivyo, walijua kwamba ingeonyesha hatua yenye maana katika utawala wa kimungu. Mwanzoni, walifikiri kwamba kufikia tarehe hiyo Ufalme wa Mungu ungekuwa umepata udhibiti kamili, wa ulimwengu wote mzima. Wakati jambo hilo halikutukia, uhakika wao katika unabii mbalimbali wa Biblia ulioonyesha tarehe hiyo haukuyumbayumba. Walifikia mkataa kwamba, badala ya hivyo, tarehe hiyo ilionyesha tu mwanzo kwa habari ya utawala wa Ufalme.
-
-
Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya KweliMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Je, “Kengele ya Saa” Ililia Mapema Mno?
Bila shaka msukosuko mkubwa ulikumba ulimwengu katika 1914 kwa kufyatuka kwa Vita ya Ulimwengu 1, ambayo kwa miaka mingi iliitwa tu ile Vita Kuu, lakini haikuongoza mara hiyo kwenye kupinduliwa kwa tawala zote za kibinadamu zilizokuwako. Kadiri matukio kuhusiana na Palestina yalivyositawi kufuatia 1914, Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba waliona uthibitisho wa mabadiliko ya maana kwa ajili ya Israeli. Lakini kadiri miezi na kisha miaka ilivyopita, Wanafunzi wa Biblia hawakupokea thawabu yao ya kimbingu, kama walivyokuwa wametarajia. Waliitikiaje jambo hilo?
The Watch Tower la Februari 1, 1916, lilivuta fikira hususa kwenye Oktoba 1, 1914, kisha likasema: “Hiyo ilikuwa ndiyo hatua ya mwisho ya wakati ambayo kronolojia ya Biblia ilielekeza kwetu kuwa ilihusiana na mambo ambayo yangelipata Kanisa la Katoliki ya Roma. Je, Bwana alituambia kwamba tungechukuliwa huko [mbinguni]? Hapana. Yeye alisema nini? Neno lake na matimizo ya unabii yalionekana yakielekeza bila kukosea kwamba tarehe hiyo ilionyesha mwisho wa Nyakati za Mataifa. Sisi tuliamua kutokana na hilo kwamba ‘badiliko’ la Kanisa lingetukia katika au kabla ya tarehe hiyo. Lakini Mungu hakutuambia kwamba ingekuwa hivyo. Yeye alituruhusu tufikie uamuzi huo; nasi tunaamini kwamba umethibitika kuwa mtihani uliohitajiwa juu ya watakatifu wapendwa wa Mungu kila mahali.” Lakini je, matukio hayo yalithibitisha kwamba tumaini lao tukufu lilikuwa limekuwa la bure? Hapana. Ilimaanisha tu kwamba si kila kitu kilikuwa kikitukia upesi kama walivyokuwa wametarajia.
Miaka kadhaa kabla ya 1914, Russell alikuwa ameandika hivi: “Kwa wazi kronolojia (unabii wa wakati kwa ujumla) haikukusudiwa kuwapa watu wa Mungu habari sahihi ya kronolojia muda wa karne zote. Kwa wazi ilikusudiwa zaidi itumike kama kengele ya saa iwaamshe na kuwatia nishati watu wa Bwana katika wakati ufaao. . . . Lakini tuseme, mathalani, kwamba Oktoba, 1914, ungepita na kusitukie anguko kubwa la serikali za Mataifa. Hilo lingethibitisha au lisingethibitisha nini? Lisingeondoa uthibitisho wa sehemu yoyote ya Mpango wa Kimungu wa Zile Enzi. Bei ya fidia iliyokamilishwa huko Kalvari bado ingekuwa uthibitisho wa utimizo wa mwisho wa Programu ya Kimungu iliyo kubwa kwa ajili ya rudisho la wanadamu. Ule ‘mwito wa juu’ wa Kanisa lipate kuteseka pamoja na Mkombozi na kutukuzwa pamoja naye likiwa washiriki wake au likiwa Bibi-Arusi wake bado ungekuwa vile vile. . . . Jambo pekee lililoathiriwa na kronolojia lingekuwa wakati wa kutimizwa kwa matumaini hayo matukufu kwa ajili ya Kanisa na kwa ajili ya ulimwengu. . . . Na tarehe hiyo ikipita ingethibitisha tu kwamba kronolojia yetu, ‘kengele ya saa’ yetu, ililia mapema kidogo kabla ya wakati. Je, sisi tungefikiri kwamba ni msiba mkuu ikiwa kengele ya saa yetu ingetuamsha nukta chache mapema zaidi asubuhi ya siku fulani kuu yenye kujawa na shangwe na furaha? Hakika sivyo!”
Lakini hiyo “kengele ya saa” haikuwa imelia mapema mno. Kwa kweli, mambo waliyoona ambayo “saa” ilikuwa imewaamsha ndiyo hayakuwa mambo barabara waliyokuwa wametarajia.
Miaka fulani baadaye, wakati nuru ilipokuwa imekuwa nyangavu zaidi, wao walikiri hivi: “Walio wengi kati ya watakatifu hao wapendwa walifikiri kwamba kazi yote ilikuwa imefanywa. . . . Walishangilia kwa sababu ya uthibitisho ulio wazi kwamba ulimwengu ulikuwa umekwisha, kwamba ufalme wa mbingu ulikuwa umekaribia, na kwamba siku ya ukombozi wao ilikaribia. Lakini walikuwa wamekosa kuona jambo jingine ambalo lazima lifanywe. Habari njema ambazo walikuwa wamepokea lazima wangeambia wengine; kwa sababu Yesu alikuwa ameamuru: ‘Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.’ (Mathayo 24:14)”—The Watch Tower, Mei 1, 1925.
Kadiri matukio yaliyofuata 1914 yalivyoanza kufunuka, nao Wanafunzi wa Biblia wakayalinganisha na yale ambayo Bwana-Mkubwa alikuwa ametabiri, walikuja kuthamini hatua kwa hatua kwamba walikuwa wakiishi katika siku za mwisho za mfumo wa kale na kwamba zilianza 1914. Pia walikuja kuelewa kwamba katika mwaka 1914 ndipo kuwapo kusikoonekana kwa Kristo kulipokuwa kumeanza na kwamba, huko hakukuwa katika maana ya kurudi kwake binafsi (hata kwa kutoonekana) kwenye ujirani wa dunia, bali kwa kuelekeza uangalifu wake kwenye dunia akiwa Mfalme anayetawala. Waliona nao wakakubali daraka muhimu lililokuwa lao la kupiga mbiu ya hii “habari njema ya ufalme” kwa ajili ya ushahidi kwa mataifa yote katika huu wakati wa hatari wa historia ya kibinadamu.—Mt. 24:3-14.
Ujumbe ambao wangehubiri juu ya Ufalme ungekuwa nini hasa? Je, ulikuwa tofauti na ujumbe wa Wakristo wa karne ya kwanza?
Ufalme wa Mungu, Tumaini Pekee la Wanadamu
Kama tokeo la funzo la uangalifu la Neno la Mungu, Wanafunzi wa Biblia walioshirikiana na Ndugu Russell walielewa kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali ambayo Yehova aliahidi kusimamisha kwa njia ya Mwanae ili kubariki wanadamu. Yesu Kristo, akiwa mbinguni, angekuwa na washirika pamoja naye wakiwa watawala, “kundi dogo” lililoteuliwa na Mungu kutoka miongoni mwa wanadamu. Walielewa kwamba serikali hiyo ingewakilishwa na wanaume waaminifu wa kale ambao wangetumikia wakiwa wakuu katika dunia yote. Hao walirejezewa kuwa “wakuu wa kale.”—Luka 12:32; Dan. 7:27; Ufu. 20:6; Zab. 45:16.
Kwa muda mrefu Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imefundisha nadharia ya kwamba ‘wenye kumiliki hupokea haki ya kuwa wafalme kutoka kwa Mungu,’ kuwa njia ya kufanya watu watii. Lakini hao Wanafunzi wa Biblia waliona kutoka Maandiko kwamba wakati ujao wa serikali za kibinadamu haukufanywa salama na uhakikisho wowote wa kimungu. Kupatana na yale waliyokuwa wakijifunza, Watch Tower la Desemba 1881 lilitaarifu: “Bila shaka kusimamishwa kwa ufalme huu, kutahusisha kupinduliwa kwa falme zote za dunia, kwa kuwa zote—hata zile bora kati yazo—zimetegemezwa juu ya utovu wa haki na haki zisizo sawa na uonevu wa wengi na kupendelea wachache—kama tusomavyo: ‘Utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.’”—Dan. 2:44.
Kwa habari ya njia ambayo falme hizo zenye uonevu zingevunjwavunjwa, hao Wanafunzi wa Biblia bado walikuwa na mengi ya kujifunza. Bado wao hawakuelewa waziwazi jinsi manufaa za Ufalme wa Mungu zingeenea kwa wanadamu wote. Lakini wao hawakuchanganyikiwa juu ya Ufalme wa Mungu wakifikiri kwamba ulikuwa hisi isiyoeleweka iliyo ndani ya moyo wa mtu au kuwa ndio ule utawala wa viongozi wa kidini uliotumia Serikali ya kilimwengu kuwa mkono wayo.
Kufikia 1914, watumishi waaminifu wa Mungu wa nyakati za kabla ya Ukristo hawakuwa wamefufuliwa duniani wakiwa wakuu wenye kuwakilisha Mfalme wa Kimesiya, kama ilivyokuwa imetarajiwa, wala wabakio wa “kundi dogo” hawakuwa wamejiunga na Kristo katika Ufalme wa kimbingu katika mwaka huo. Hata hivyo The Watch Tower la Februari 15, 1915, lilitaarifu kwa uhakika kwamba 1914 ulikuwa ndio wakati uliowekwa “wa Bwana wetu kutwaa uweza Wake mkuu na kuanza kutawala,” hivyo kumaliza zile mileani nyingi za utawala usiokatizwa wa Mataifa. Katika toleo lalo la Julai 1, 1920, The Watch Tower lilithibitisha tena msimamo huo na kuushirikisha na zile habari njema ambazo Yesu alikuwa ametabiri kwamba zingehubiriwa duniani pote kabla ya mwisho. (Mt. 24:14) Kwenye mkusanyiko wa Wanafunzi wa Biblia huko Cedar Point, Ohio, katika 1922, uelewevu huo ulitaarifiwa upya katika azimio la ujumla, na Ndugu Rutherford akahimiza wakusanyikaji hivi: “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.”
Hata hivyo, wakati ule Wanafunzi wa Biblia walihisi kwamba kuanzishwa kwa Ufalme, kusimamishwa kwao kikamili mbinguni, hakungetukia mpaka washiriki wa mwisho wa bibi-arusi wa Kristo watukuzwe. Kwa hiyo, hatua kubwa ya kweli ilifikiwa katika 1925, wakati The Watch Tower la Machi 1, lilipotoa makala “Uzaliwa wa Taifa.” Ilitoa funzo lenye kufungua macho juu ya Ufunuo sura ya 12. Makala hiyo ilionyesha uthibitisho wa kwamba Ufalme wa Kimesiya ulikuwa umezaliwa—ukasimamishwa—katika 1914, kwamba wakati huo Kristo alikuwa ameanza kutawala katika kiti chake cha kifalme mbinguni, na kwamba baada ya hapo Shetani alikuwa amevurumishwa chini kwenye ujirani wa dunia kutoka mbinguni. Hizo ndizo zilizokuwa habari njema ambazo zilipasa kupigiwa mbiu, habari za kwamba Ufalme wa Mungu ulikuwa tayari unatenda. Lo, jinsi uelewevu huo uliotiwa nuru ulivyochochea hao wapiga-mbiu wa Ufalme wahubiri hata kwenye miisho ya dunia!
Kwa kila njia ifaayo, watu wa Yehova walitoa ushahidi kwamba Ufalme wa Mungu pekee ndio ungeleta kitulizo cha kudumu na kutatua matatizo yaliyoimarika sana yenye kutaabisha wanadamu. Katika 1931 ujumbe huo ulitolewa kupitia usambazaji wa redio na J. F. Rutherford katika mfumo wa kimataifa wenye kuenea zaidi uliokuwa umepata kutangazwa hewani. Maandishi ya usambazaji huo yalikuwa pia yametangazwa katika lugha nyingi katika kijitabu The Kingdom, the Hope of the World (Ufalme, Tumaini la Ulimwengu)—mamilioni ya nakala zacho yaligawanywa kwa muda wa miezi michache tu. Kuongezea ugawanyaji kwa umma wenye kuenea pote, jitihada za pekee zilifanywa kutia nakala mikononi mwa wanasiasa, wanabiashara mashuhuri, na makasisi.
Miongoni mwa mambo mengine, kijitabu hicho kilisema hivi: “Serikali za ulimwengu za sasa ambazo si zenye uadilifu haziwezi kutoa tumaini lolote kwa watu. Hukumu ya Mungu dhidi yazo yajulisha kwamba lazima ziharibiwe. Kwa hiyo, tumaini la ulimwengu, na tumaini pekee, ni ufalme wenye uadilifu au serikali ya Mungu, Kristo Yesu akiwa Mtawala wayo asiyeonekana.” Walitambua kwamba, Ufalme huo, ungeleta amani na usalama wa kweli kwa wanadamu. Chini ya utawala wao dunia ingekuwa paradiso halisi, na magonjwa na kifo havingekuwapo tena.—Ufu. 21:4, 5.
Habari njema za Ufalme wa Mungu huendelea kuwa imani kuu ya Mashahidi wa Yehova. Tangu toleo la Machi 1, 1939, gazeti lao kuu, ambalo sasa hutangazwa kwa lugha 112, limekuwa na kichwa Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova.
Lakini kabla utawala wa Ufalme haujageuza sura ya dunia iwe paradiso, ingekuwa sharti huu mfumo mwovu wa mambo utoweke. Hilo lingetimizwaje?
Vita ya Ile Siku Kubwa ya Mungu Mweza Yote
Ile vita ya ulimwengu iliyoanza katika 1914 ilitikisa mfumo wa mambo ulioko hadi kwenye misingi yao. Kwa wakati fulani ilionekana kana kwamba matukio yangesonga mbele kama vile Wanafunzi wa Biblia walivyokuwa wametarajia.
Huko nyuma katika Agosti 1880, Ndugu Russell alikuwa ameandika hivi: “Sisi twaelewa kwamba kabla familia ya kibinadamu haijarudishwa au hata kuanza kubarikiwa, serikali za dunia ambazo sasa hufunga na kuonea wanadamu zitapinduliwa zote na kwamba ufalme wa Mungu utatwaa udhibiti na kwamba baraka na rudisho zitakuja kupitia huo ufalme mpya.” ‘Kupinduliwa kwa falme’ kungetukiaje? Akitegemea hali ambazo angeweza kuona wakati ule zikitukia katika ulimwengu, Russell aliamini kwamba wakati wa vita ya Har–Magedoni, Mungu angetumia vikundi vyenye kuzozana vya wanadamu kupindua mipango iliyoko. Alisema hivi: “Kazi ya kubomoa milki ya kibinadamu inaanza. Mamlaka itakayozipindua inatenda kazi sasa. Tayari watu wanapanga majeshi yao chini ya jina la Wakomunisti, Wasosholisti, na Wanamapinduzi, n.k.”
Kitabu The Day of Vengeance (baadaye kiliitwa The Battle of Armageddon), kilichotangazwa katika 1897, kiliongeza habari zaidi juu ya njia ambayo Wanafunzi wa Biblia wakati ule walielewa jambo hilo, kikisema hivi: “Bwana, kwa maongozi yake ya kimungu yenye kushinda, atatwaa uongozi wa ujumla wa jeshi hili kubwa la wasioridhika—wazalendo, warekebishaji, wasosholisti, wateteaji-maadili, wanamachafuko, wajinga na wasio na tumaini—na kutumia matumaini yao, hofu, upumbavu na ubinafsi, kulingana na hekima yake ya kimungu, kutimiza makusudi yake mwenyewe makuu katika kupindua mipango ya sasa, na katika kutayarisha binadamu kwa ajili ya Ufalme wa Uadilifu.” Hivyo wao walielewa kwamba vita ya Har–Magedoni ingeshirikishwa na mapinduzi ya kijamii yenye jeuri.
Lakini je, Har–Magedoni ingekuwa mng’ang’ano tu kati ya vikundi vyenye kuzozana vya wanadamu, mapinduzi ya kijamii yenye kutumiwa na Mungu kupindua mipango iliyoko? Kadiri uangalifu zaidi ulivyokazwa juu ya maandiko yaliyohusu habari hiyo, The Watch Tower la Julai 15, 1925, lilivuta fikira kwenye Zekaria 14:1-3 na kusema: “Kwa hilo tungeelewa kwamba mataifa yote ya dunia, chini ya mwelekezo wa Shetani, yangekusanywa kwenye vita dhidi ya jamii ya Yerusalemu, yaani, wale ambao huchukua msimamo wao upande wa Bwana . . . Ufunuo 16:14, 16.”
Mwaka uliofuata, katika kitabu Deliverance, uangalifu ulikazwa juu ya kusudi la kweli la vita hiyo, kusema: “Sasa Yehova, kulingana na Neno lake, atafanya wonyesho wa nguvu zake kwa wazi sana na kwa njia isiyo na shaka hivi kwamba watu wataweza kusadikishwa juu ya mwendo wao usio wa kimungu na waweze kuelewa kwamba Yehova ndiye Mungu. Hiyo ndiyo sababu iliyofanya Mungu alete lile furiko kuu, aangushe chini Mnara wa Babeli, aharibu jeshi la Senakeribu yule mfalme wa Ashuru, na kumeza Wamisri; na ndiyo pia sababu sasa ataleta taabu nyingine kuu juu ya ulimwengu. Maafa hayo ya hapo kwanza yalikuwa vivuli tu vya lile linalokuja sasa. Kukusanywa huko ni [kuletwa] kwenye siku ile kuu ya Mungu Mweza Yote. Ndiyo ile ‘siku kuu na itishayo ya Bwana’ (Yoe. 2:31), wakati ambapo Mungu atajifanyia mwenyewe jina. Katika pambano hilo kuu na la mwisho vikundi vya watu wa kila taifa, kabila na lugha vitajifunza kwamba Yehova ndiye mwenye nguvu zote, mwenye hekima yote na Mungu mwenye haki.” Lakini watumishi wa Yehova duniani walitahadharishwa hivi: “Katika vita hiyo kuu hakuna Mkristo atakayerusha ngumi. Sababu inayofanya wasifanye hivyo ni kwamba Yehova amesema: ‘Vita si yenu, bali ya Mungu.’” Vita inayozungumzwa hapa kwa wazi si ile ambayo ilipiganwa miongoni mwa mataifa, kuanzia 1914. Ilikuwa ingali inakuja.
Bado kulikuwa na maswali mengine yaliyohitaji kutatuliwa kwa msingi wa Maandiko. Moja la hayo lilihusu utambulisho wa Yerusalemu ambao ungekanyagwa chini ya miguu mpaka mwisho wa Nyakati za Mataifa, kama ilivyotaarifiwa kwenye Luka 21:24; na uliohusiana na huo ulikuwa utambulisho wa Israeli warejezewao katika unabii mwingi sana juu ya kurudishwa.
-