-
Kuwatambua Waabudu wa Kweli Katika Wakati wa MwishoSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
21. (a) Kile kipindi cha wakati kilichotabiriwa katika Danieli 12:11 kingeanza wakati ambapo hali gani zingetokea? (b) Ile “sadaka ya kuteketezwa daima” ilikuwa nini, nayo iliondolewa lini? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 298.)
21 Danieli aliambiwa hivi: “Tangu wakati ule ambapo sadaka ya kuteketezwa ya daima itaondolewa, na hilo chukizo la uharibifu litakaposimamishwa, itapata siku elfu na mia mbili na tisini.” Kwa hiyo, kipindi hicho cha wakati kingeanza wakati ambapo hali fulani zingekuwa zimetokezwa. “Sadaka ya kuteketezwa ya daima”a ilikuwa imeondolewa. (Danieli 12:11) Malaika huyo alimaanisha dhabihu gani? Si dhabihu ya wanyama iliyotolewa kwenye hekalu lolote la kidunia. Kwani, hata hekalu ambalo wakati mmoja lilikuwa Yerusalemu lilikuwa “nakala ya uhalisi”—hekalu kuu la kiroho la Yehova, lililoanza kutumika wakati Kristo alipopata kuwa Kuhani wa Cheo cha Juu wa hekalu hilo mwaka wa 29 W.K.! Katika hekalu hilo la kiroho, lenye kuwakilisha mpango wa Mungu wa ibada safi, hakuna uhitaji wa matoleo yenye kuendelea ya dhambi, kwa kuwa ‘Kristo alitolewa mara moja kwa wakati wote ili kuchukua dhambi za wengi.” (Waebrania 9:24-28) Hata hivyo, Wakristo wote wa kweli hutoa dhabihu kwenye hekalu hilo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kupitia [Kristo] acheni sikuzote tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani.” (Waebrania 13:15) Kwa hiyo, hali hiyo ya kwanza ya unabii huo—kule kuondolewa kwa “sadaka ya kuteketezwa daima”—ilitimizwa katikati ya mwaka wa 1918 wakati ambapo kazi ya kuhubiri ilionekana kana kwamba ilikuwa imekomeshwa kwa muda.
22. (a) “Chukizo” la uharibifu ni nini, nalo lilisimamishwa lini? (b) Kile kipindi kilichotabiriwa katika Danieli 12:11 kilianza lini, na kiliisha lini?
22 Hata hivyo, vipi juu ya hali ya pili—‘kusimamishwa,’ au kuwekwa kwa “chukizo la uharibifu”? Kama tulivyoona tulipozungumzia Danieli 11:31, chukizo hilo mwanzoni lilikuwa Ushirika wa Mataifa na kisha likatokea tena likiwa Umoja wa Mataifa. Mashirika yote mawili yanachukiza kwa kuwa yatangazwa kuwa tumaini pekee la amani duniani. Kwa hiyo, mioyoni mwa watu wengi, mashirika hayo kwa hakika yametwaa mahali pa Ufalme wa Mungu! Ushirika wa Mataifa ulipendekezwa rasmi Januari 1919. Basi, wakati huo hali zote mbili za Danieli 12:11 zilitimizwa. Kwa hiyo, zile siku 1,290 zilianza mapema mwaka wa 1919 na kuendelea hadi vuli (kwenye Kizio cha Kaskazini) ya mwaka wa 1922.
23. Watakatifu wa Mungu walielekeaje kupata msimamo safi wakati wa zile siku 1,290 zilizotabiriwa katika Danieli sura ya 12?
23 Wakati huo, je, watakatifu walifanya maendeleo kuelekea kufanywa weupe na kutakaswa machoni pa Mungu? Bila shaka! Machi 1919 msimamizi wa Watch Tower Society na washiriki wake wa karibu walifunguliwa kutoka gerezani. Baadaye wakaondolewa mashtaka yote ambayo hayakuwa ya kweli. Wakijua kwamba bado walikuwa na kazi nyingi, mara moja wakaanza shughuli, wakipanga mkusanyiko wa Septemba 1919. Mwaka huohuo, gazeti-jenzi la The Watch Tower likachapishwa kwa mara ya kwanza. Mwanzoni likiitwa The Golden Age (sasa laitwa Amkeni!), sikuzote limetegemeza Mnara wa Mlinzi katika kufichua bila woga ufisadi wa ulimwengu huu na katika kusaidia watu wa Mungu wadumishe usafi. Kufikia mwisho wa zile siku 1,290 zilizotabiriwa, watakatifu walikuwa wakielekea kutakaswa na kuwa na msimamo mpya. Septemba 1922, wapata wakati barabara ambapo kipindi hicho kiliisha, walifanya mkusanyiko wa pekee huko Cedar Point, Ohio, Marekani. Ulichochea sana kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, bado kulikuwa na uhitaji wa kufanya maendeleo zaidi. Hayo yangefanywa katika kipindi cha pekee kilichofuata.
-
-
Kuwatambua Waabudu wa Kweli Katika Wakati wa MwishoSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
Siku 1,290: Januari 1919 hadi
Danieli 12:11 Septemba 1922
(Wakristo watiwa-mafuta waamka
na kuendelea kiroho.)
-