Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Endelea Kuushinda Uovu Kwa Wema”
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Julai 1
    • “Alikasirika na Kuudhika Sana”

      5, 6. (a) Maadui wa Nehemia walifanya nini kuelekea kazi ya ujenzi? (b) Kwa nini Nehemia hakuogopeshwa na wapinzani?

      5 Kwa ujasiri, Nehemia aliwatia moyo hivi watu wake: “Tujenge upya ukuta wa Yerusalemu.” Wakamwambia: “Tukajenge.” Nehemia anasema hivi: “Wakaitia mikono yao nguvu kwa ajili ya kazi hiyo njema,” lakini wapinzani “wakaanza kutudhihaki na kutudharau wakisema: ‘Ni nini hili mnalofanya? Je, mnamwasi mfalme?’” Nehemia hakuogopeshwa na dhihaka zao na mashtaka yao ya uwongo. Aliwaambia hivi wapinzani hao: “Mungu wa mbinguni, Yeye ndiye atakayetupatia mafanikio, na sisi watumishi wake, tutasimama, nasi tutajenga.” (Nehemia 2:17-20) Nehemia aliazimia kuendelea na “kazi hiyo njema.”

      6 Mmoja wa wapinzani hao, Sanbalati, “alikasirika na kuudhika sana” naye akazidi kuwashambulia kwa maneno. “Hawa Wayahudi wanyonge wanafanya nini?” akawadhihaki. “Je, watafufua mawe kutoka kwenye marundo ya takataka chafu?” Tobia alijiunga naye katika kuwadhihaki akisema: “Mbweha akipanda juu yake, ataubomoa ukuta wao wa mawe.” (Nehemia 4:1-3) Nehemia alitenda jinsi gani?

      7. Nehemia alitenda jinsi gani kuelekea mashtaka ya wapinzani wake?

      7 Nehemia alipuuza tu dhihaka zao. Alifuata amri ya Mungu naye hakujaribu kulipiza kisasi. (Mambo ya Walawi 19:18) Badala yake, aliacha mambo mikononi mwa Yehova, na akasali hivi: “Sikiliza, Ee Mungu wetu, kwa maana tumedharauliwa; na uzirudishe shutuma zao juu ya vichwa vyao wenyewe.” (Nehemia 4:4) Nehemia alisadiki uhakikisho huu wa Yehova: “Kisasi ni changu, na malipo.” (Kumbukumbu la Torati 32:35) Zaidi ya hayo, Nehemia na watu wake ‘waliendelea kujenga ukuta.’ Hawakujiruhusu wakengeushwe. Kwa hiyo, “ukuta mzima ukaungana kufikia nusu ya kimo chake, watu nao wakaendelea kuwa na moyo wa kufanya kazi.” (Nehemia 4:6) Maadui wa ibada ya kweli walishindwa kusimamisha kazi hiyo ya ujenzi! Tunaweza kumwiga Nehemia jinsi gani?

      8. (a) Tunaweza kumwiga Nehemia jinsi gani wapinzani wanapotushtaki kwa uwongo? (b) Simulia jambo uliloona au kusikia ambalo linaonyesha hekima ya kutolipa kisasi.

      8 Leo, wapinzani shuleni, kazini, au hata nyumbani wanaweza kutudhihaki na kutushtaki. Hata hivyo, mara nyingi njia nzuri ya kushughulikia mashtaka hayo ya uwongo ni kwa kufuata kanuni hii ya Maandiko: “Kuna . . . wakati wa kukaa kimya.” (Mhubiri 3:1, 7) Kwa hiyo, kama Nehemia, hatulipizi kisasi kwa kusema maneno yenye kuumiza. (Waroma 12:17) Tunasali kwa Mungu na kumtumaini yule ambaye anatuhakikishia hivi: “Mimi nitalipa.” (Waroma 12:19; 1 Petro 2:19, 20) Kwa njia hiyo, hatuwaruhusu wapinzani wetu watukengeushe kuacha kazi ya kiroho ambayo inapaswa kufanywa leo, kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kila wakati tunaposhiriki katika kazi ya kuhubiri na kutoruhusu upinzani utuzuie, tunaonyesha roho ileile ya uaminifu ambayo Nehemia alionyesha.

      “Nasi Tutawaua”

      9. Maadui wa Nehemia walitokeza upinzani wa aina gani, na Nehemia alichukua hatua gani?

      9 Wapinzani wa ibada ya kweli katika siku za Nehemia waliposikia kwamba kazi ya “kurekebisha kuta za Yerusalemu imesonga mbele,” walichukua panga zao ili “kupiga vita juu ya Yerusalemu.” Hali hiyo iliwafadhaisha sana Wayahudi. Wasamaria walikuwa upande wa kaskazini, Waamoni upande wa mashariki, Waarabu upande wa kusini, na Waashdodi upande wa magharibi. Yerusalemu lilizingirwa; ilionekana kwamba wajenzi hawakuwa na njia ya kutokea! Wangefanya nini? Nehemia anasema: “Tulisali kwa Mungu wetu.” Maadui waliwatisha hivi: “Nasi tutawaua na kuikomesha kazi.” Nehemia alichukua hatua ya kuwapa wajenzi kazi ya kulinda jiji hilo “wakiwa na panga zao, mikuki yao na pinde zao.” Ni kweli kwamba kwa maoni ya wanadamu, kikundi hicho kidogo cha Wayahudi hakingeweza kamwe kushinda jeshi kubwa la maadui, lakini Nehemia aliwahimiza hivi: “Msiogope . . . Mkumbukeni Yehova, Yeye ambaye ni mkuu na Mwenye kuogopesha.”—Nehemia 4:7-9, 11, 13, 14.

      10. (a) Ni nini kilichosababisha badiliko la ghafula miongoni mwa maadui wa Nehemia? (b) Nehemia alichukua hatua gani?

      10 Mambo yalibadilika ghafula. Maadui waliamua kutoshambulia. Kwa nini? Nehemia anaripoti hivi: “Mungu wa kweli amevunja shauri lao.” Hata hivyo, Nehemia alitambua kwamba bado maadui walikuwa tishio. Kwa hiyo, kwa hekima alibadili njia ya wajenzi hao ya kufanya kazi. Tangu wakati huo na kuendelea, “kila mmoja alikuwa akifanya kazi kwa mkono wake mmoja, na mkono wa pili ukiwa umeshika silaha.” Nehemia pia alimpa mtu mmoja kazi ya “kupiga baragumu” ili kuwaonya wajenzi kuhusu shambulizi la maadui. Zaidi ya yote, Nehemia aliwahakikishia watu hivi: “Mungu wetu mwenyewe atatupigania.” (Nehemia 4:15-20) Wakiwa wametiwa moyo na kutayarishwa kupambana na mashambulizi, wajenzi hao waliendelea na kazi. Tunajifunza mambo gani kutokana na simulizi hilo?

      11. Ni nini kinachowawezesha Wakristo wa kweli kuushinda uovu katika nchi ambako kazi ya Ufalme imepigwa marufuku, nao wanashinda uovu kwa wema jinsi gani?

      11 Nyakati nyingine, Wakristo wa kweli wanapingwa kijeuri. Kwa kweli, katika nchi fulani wapinzani wakali sana wa ibada ya kweli wanakuwa jeshi kubwa la maadui. Kwa maoni ya wanadamu, waamini wenzetu katika nchi hizo hawawezi kuwashinda maadui hao. Hata hivyo, Mashahidi hao wana hakika kwamba ‘Mungu atawapigania.’ Kwa kweli, wale ambao wameteswa kwa sababu ya imani yao wameona mara nyingi kwamba Yehova anajibu sala zao na ‘kuvunja shauri’ la maadui wenye nguvu. Hata katika nchi ambako kazi ya Ufalme imepigwa marufuku, Wakristo wanatafuta njia za kuendelea kuhubiri habari njema. Kama vile wajenzi wa Yerusalemu walivyobadili njia yao ya kufanya kazi, ndivyo Mashahidi wa Yehova leo wanavyobadili kwa hekima njia zao za kuhubiri wanaposhambuliwa. Bila shaka, wanajiepusha kutumia silaha halisi. (2 Wakorintho 10:4) Hata wanapotishwa kushambuliwa kwa ujeuri, hawaachi kuhubiri. (1 Petro 4:16) Badala yake, ndugu na dada hao wenye ujasiri ‘wanaendelea kuushinda uovu kwa wema.’

      “Njoo, Tukutane”

      12, 13. (a) Wapinzani wa Nehemia walitumia mbinu gani? (b) Kwa nini Nehemia alikataa mwaliko wa kukutana na wapinzani wake?

      12 Baada ya maadui wa Nehemia kutambua kwamba mashambulizi yao ya moja kwa moja hayakufanikiwa, walianza kupanga mbinu za werevu zaidi za kumpinga. Kwa kweli, walijaribu mbinu tatu. Ni mbinu gani hizo?

      13 Kwanza, maadui wa Nehemia walijaribu kumdanganya. Walimwambia hivi: “Njoo, tukutane pamoja kwa mapatano katika vijiji vya nchi tambarare ya bondeni ya Ono.” Nchi ya Ono ilikuwa kati ya Yerusalemu na Samaria. Kwa hiyo, maadui walipendekeza kwamba Nehemia akutane nao katikati ili watatue matatizo. Nehemia angefikiri hivi: ‘Hilo ni jambo la busara. Ni afadhali kuongea kuliko kupigana.’ Lakini Nehemia alikataa. Alieleza kwa nini alikataa: “Walikuwa wanapanga kuniumiza.” Alitambua njama yao naye hakudanganyika. Mara nne aliwaambia hivi wapinzani wake: “Siwezi kushuka. Kwa nini kazi isimame kwa kuiacha ili nije kwenu?” Jitihada za maadui za kumfanya Nehemia alegeze msimamo wake zilishindwa. Alikazia macho kazi ya ujenzi.—Nehemia 6:1-4.

      14. Nehemia alichukua hatua gani ili kukabiliana na wale waliomshtaki kwa uwongo?

      14 Pili, maadui wa Nehemia walianza kueneza uvumi wa uwongo, wakidai kwamba Nehemia alikuwa ‘anapanga kumwasi’ Mfalme Artashasta. Kwa mara nyingine tena walimwambia Nehemia hivi: “Tushauriane pamoja.” Nehemia akakataa tena, kwa kuwa alitambua nia ya maadui hao. Nehemia alieleza hivi: “Wote walikuwa wakijaribu kututia woga, wakisema: ‘Mikono yao italegea waache kazi, hivi kwamba haitafanywa.’” Hata hivyo, wakati huu, Nehemia alipinga mashtaka ya maadui wake, akisema: “Mambo kama hayo unayosema hayajatokea, bali unayatunga moyoni mwako mwenyewe.” Zaidi ya hayo, Nehemia alimwomba Yehova msaada, naye alisali hivi: “Itie mikono yangu nguvu.” Alisadiki kwamba kwa msaada wa Yehova angeweza kushinda njama hiyo ya uovu na kuendelea na kazi ya ujenzi.—Nehemia 6:5-9.

      15. Nabii wa uwongo alitoa pendekezo gani, na kwa nini Nehemia hakukubali pendekezo hilo?

      15 Tatu, maadui wa Nehemia walitumia msaliti, Mwisraeli aliyeitwa Shemaya, ili wajaribu kumfanya Nehemia avunje Sheria ya Mungu. Shemaya alimwambia hivi Nehemia: “Tukutane kwa mapatano katika nyumba ya Mungu wa kweli, ndani ya hekalu, halafu tufunge milango ya hekalu; kwa maana wanakuja kukuua.” Shemaya alisema kwamba Nehemia angeuawa lakini angeweza kuokoa uhai wake kwa kujificha hekaluni. Lakini, Nehemia hakuwa kuhani. Angetenda dhambi kwa kujificha katika nyumba ya Mungu. Je, angevunja Sheria ya Mungu akijaribu kuokoa uhai wake? Nehemia alimjibu hivi: “Ni nani kama mimi anayeweza kuingia hekaluni kisha akaishi? Sitaingia!” Kwa nini Nehemia hakunaswa na mtego ambao aliwekewa? Kwa sababu alijua kwamba ingawa Shemaya alikuwa Mwisraeli mwenzake, “si Mungu aliyemtuma.” Kwa vyovyote vile, nabii wa kweli hangeweza kamwe kumshauri avunje Sheria ya Mungu. Tena, Nehemia hakujiruhusu ashindwe na wapinzani waovu. Muda mfupi baadaye aliripoti hivi: “Mwishowe ukuta ukakamilika siku ya 25 ya mwezi wa Eluli, katika muda wa siku 52.”—Nehemia 6:10-15; Hesabu 1:51; 18:7.

      16. (a) Tunapaswa kushughulika kwa njia gani na marafiki wa uwongo, washtaki wa uwongo, na ndugu wa uwongo? (b) Unaonyesha jinsi gani kwamba unakataa kulegeza msimamo wako wa imani nyumbani, shuleni, au kazini?

      16 Kama Nehemia, huenda sisi pia tukakabili wapinzani ambao ni marafiki wa uwongo, washtaki wa uwongo, na ndugu wa uwongo. Huenda watu fulani wakatualika tusikilizane nao na kulegeza msimamo wetu. Huenda wakajaribu kutusadikisha kwamba tukimtumikia Yehova bila bidii nyingi, tunaweza kufuatia miradi ya kilimwengu wakati huohuo. Hata hivyo, tunakataa kulegeza msimamo wetu kwa sababu tunatanguliza Ufalme wa Mungu katika maisha yetu. (Mathayo 6:33; Luka 9:57-62) Wapinzani pia wanaeneza mashtaka ya uwongo kutuhusu. Katika nchi fulani, tunashtakiwa kwamba sisi ni tishio kwa Serikali, kama Nehemia alivyoshtakiwa kwamba anamwasi mfalme. Tumefanikiwa kupinga mashtaka fulani katika mahakama. Lakini, haidhuru tunapata matokeo gani katika hali mbalimbali, tunasali tukiwa na uhakika kwamba Yehova ataelekeza mambo kupatana na mapenzi yake. (Wafilipi 1:7) Tunaweza pia kupingwa na wale wanaojifanya wanamtumikia Yehova. Kama vile tu Nehemia alivyoshawishiwa na Myahudi mwenzake avunje Sheria ya Mungu ili kuokoa uhai wake, ndivyo waasi-imani ambao walikuwa Mashahidi wanavyoweza kujaribu kutushawishi ili tulegeze msimamo wetu kwa njia moja au nyingine. Hata hivyo, tunawakataa kabisa waasi-imani kwa sababu tunajua kwamba tunaweza kuokoa uhai wetu kwa kutii sheria za Mungu wala si kwa kuzivunja! (1 Yohana 4:1) Ndiyo, kwa msaada wa Yehova tunaweza kuushinda uovu wa aina yoyote ile.

  • “Endelea Kuushinda Uovu Kwa Wema”
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Julai 1
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29]

      Mambo Tunayojifunza Katika Kitabu cha Nehemia

      Watumishi wa Mungu wanakabili

      • dhihaka

      • vitisho

      • udanganyifu

      Udanganyifu unatumiwa na

      • marafiki wa uwongo

      • washtaki wa uwongo

      • ndugu wa uwongo

      Watumishi wa Mungu wanaushinda uovu kwa

      • kuendelea kufanya kazi waliyopewa na Mungu

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki