Je, Vyote Ni Ufunuo Mbalimbali wa Kimungu?
JE, ROHO ya Mungu, iliyopulizia Biblia Takatifu, iliweza pia kuhusika katika vile vitabu vingine ambavyo watu fulani huviona kuwa vitakatifu? (2 Timotheo 3:16) Swali hilo lilizushwa na jarida la Kiitalia la Wayesuiti (La Civiltà Cattolica) lililochapishwa “chini ya uangalizi wa Ofisi ya Katibu ya Serikali [ya Vatikani]” na hivyo kuonwa kuwa lenye mamlaka katika nyanja za Ukatoliki.
“Mungu, kupitia utendaji wa Roho Takatifu, alisambaza mbegu ya Neno hata katika vitabu fulani vitakatifu visivyo vya asili ya Kiyahudi wala ya Kikristo,” likasema hilo jarida la Wayesuiti. Kwa Wayesuiti, vitabu “vitakatifu,” kama vile Avesta cha Zoroaster au Vitabu Vinne vya Confucius, havikuandikwa “bila uvutano fulani mahususi wa Roho Takatifu, na hivyo, kwa kiasi fulani vina ‘ufunuo wa kimungu.’”
Hata hivyo, hiyo makala yabainisha. “Baadhi ya maandishi yaliyo katika hivyo vitabu vitakatifu si neno la Mungu,” yataarifu, na kuongeza kwamba huenda ikawa walioviandika vitabu hivyo “walipatwa na uvutano wa mazingira ya ibada ya miungu mingi au uvutano wa mazingira ya kifalsafa” ambamo waliishi na kutenda. Kulingana na Marco Politi, mleta-habari wa mambo ya Vatikani wa gazeti la habari la Italia La Repubblica, msimamo huo “huruhusu mahusiano ambayo zamani yalionwa kuwa yasiyowezekana kati ya Kanisa Katoliki na dini kubwa za kihistoria,” na kurudia ile roho ya ile mikutano mbalimbali ya sala ya mchanganyiko wa dini nyingi kama ule wa Assisi katika mwaka wa 1986, ambao uliendelezwa kwa bidii na John Paul 2.
Yehova si Mungu wa kukosa utaratibu na wa vurugu. (1 Wakorintho 14:33) Kwa hiyo hatuwezi kwa kufaa kukata kauli kwamba roho takatifu yake, au kani ya utendaji, ingepulizia hata sehemu ya vitabu vyovyote ambavyo havipatani kabisa na Neno lake, Biblia. Badala ya kutia moyo hatua za kuungana kwa “desturi [mbalimbali] za kidini,” mtume Mkristo Paulo aliandika kwamba kuna “tumaini moja . . . , Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja.”—Waefeso 4:4, 5.
“Tumaini [hilo] moja” hutegemea kuweka imani katika Yesu Kristo. Biblia hutaarifu hivi kwa kufaa: “Hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina jingine chini ya mbingu ambalo limepewa miongoni mwa watu ambalo kwalo lazima sisi tupate kuokolewa.” (Matendo 4:12) Hakuna “kitabu kitakatifu” kingine chochote ambacho humtokeza Yesu kuwa mtu mwenye fungu kubwa katika kutimizwa kwa makusudi ya Mungu. Tukubalipo Biblia kuwa Neno la Mungu ndipo tu iwezapo kutufundisha juu ya uandalizi wenye upendo wa Yehova Mungu wa kupata wokovu.—Yohana 17:3; 1 Wathesalonike 2:13.