Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kushinda Vizuizi vya Mawasiliano Huko Panama
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 15
    • Kushinda Vizuizi Huko Comarca

      Kabila la Wangobe ndilo kubwa zaidi kati ya makabila manane nchini Panama. Kabila hilo lina watu 170,000, wengi wao wakiishi katika eneo ambalo hivi karibuni lilipewa jina la comarca, au eneo lililotengwa. Sehemu kubwa ya eneo hilo ni msitu wenye milima-milima ambayo hufikiwa tu kwa miguu, na pia una pwani maridadi zinazoweza kufikiwa kwa meli. Mara nyingi jamii za watu huishi karibu na pwani, na pia karibu na mito ambayo hutumiwa kwa usafiri. Wakaaji wengi wa comarca hupata mapato kidogo kwa kufanya kazi katika mashamba ya kahawa huko milimani, kuvua samaki, au kupitia ukulima. Wengi wanashirikiana na dini zinazodai kuwa za Kikristo. Hata hivyo, kuna wafuasi wa dini ya eneo hilo inayoitwa Mama Tata. Baadhi yao huwaendea sukias (makasisi ambao hutumia mizungu) kwa ajili ya uponyaji au wanapohisi kwamba wanasumbuliwa na roho waovu. Ingawa watu wengi huzungumza Kihispania, Kingobere ndiyo lugha inayoeleweka zaidi.

      Kusafiri kwa Mitumbwi ili Kuhubiri

      Mashahidi wa Yehova wanajua kwamba ni muhimu kuwasaidia watu kujifunza kweli kwa njia ambayo itawasaidia kuielewa na wakati huohuo kufikia mioyo yao. Kweli inapofikia mioyo yao inaweza kuwachochea kufanya mabadiliko ili kupatanisha maisha yao na kanuni za Biblia. Hivyo, mapainia wa pekee waliotumwa katika sehemu nane za eneo hilo lililotengwa, wamesaidiwa na Mashahidi wenye ujuzi wa eneo hilo kujifunza Kingobere.

      Kuanzishwa kwa makutaniko 14 katika eneo hilo kunaonyesha kwamba kuna uwezekano mkubwa wa ukuzi. Kwa mfano, miaka michache iliyopita, Dimas na Gisela ambao ni wenzi wa ndoa wanaotumikia wakiwa mapainia wa pekee, walipewa mgawo katika kutaniko moja dogo la wahubiri 40 hivi kwenye pwani ya Tobobe. Haikuwa rahisi kwao kuzoea kusafiri kila mara kwa mtumbwi ili kuwahubiria watu wanyenyekevu walio kwenye Pwani ya Atlantiki. Dimas na Gisela walitambua kwamba maji matulivu ya bahari yanaweza kuwa mawimbi hatari. Mara nyingi mikono na migongo yao iliuma kwa sababu ya kupiga makasia kutoka kijiji kimoja hadi kingine. Tatizo lingine lilikuwa kujifunza lugha ya wenyeji. Hata hivyo, kwa sababu ya kujidhabihu na kuvumilia, walibarikiwa wakati watu 552 hivi walipohudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo mwaka wa 2001.

      Upande ule mwingine wa ghuba kutoka Tobobe kuna kijiji cha Punta Escondida. Kwa kawaida kikundi kidogo cha wahubiri kilivuka ghuba hiyo kwa mtumbwi, hali ya hewa ilipowaruhusu ili kuhudhuria mikutano huko Tobobe. Ripoti zilionyesha kwamba kuna uwezekano wa kuanzisha kutaniko jipya katika eneo hilo. Kwa sababu hiyo, Dimas na Gisela waliombwa wahamie Punta Escondida. Baada ya muda usiozidi miaka miwili, kikundi cha Punta Escondida kikawa kutaniko la wahubiri 28 wenye bidii, na kwa wastani watu 114 walihudhuria hotuba ya watu wote ya kila juma. Mwaka wa 2004 kutaniko hilo jipya lilifurahi wakati jumla ya watu 458 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo.

      Kushinda Kizuizi cha Kutojua Kusoma na Kuandika

      Kujua kusoma na kuandika kumewasaidia watu wengi wenye mioyo minyoofu kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Fermina, mwanamke kutoka sehemu yenye milima-milima ya comarca. Wamishonari waliokuwa wakihubiri katika eneo la mbali karibu na mahali alikoishi walitambua kwamba alisikiliza ujumbe wa Ufalme kwa makini. Alipoulizwa iwapo angependa kujifunza Biblia, alisema kwamba angependa kujifunza zaidi. Hata hivyo, kulikuwa na tatizo. Alijua kuzungumza Kihispania na Kingobere lakini hakujua kusoma wala kuandika lugha hizo. Mmishonari mmoja alijitolea kumfundisha akitumia broshua Jitahidi Kusoma na Kuandika.a

      Fermina alikuwa mwanafunzi mzuri, alijitayarisha kwa ajili ya funzo, alitimiza kazi ya ziada aliyopewa, na alikuwa na bidii ya kufanya mazoezi ya kuandika. Katika mwaka mmoja, alikuwa amefanya maendeleo ya kutosha kujifunza broshua Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!b Mikutano ilipopangwa, Fermina alianza kuhudhuria. Hata hivyo, kwa sababu familia yao ilikuwa maskini, ilikuwa vigumu sana kupata nauli ya kwenda mikutanoni pamoja na watoto wake. Painia mmoja aliyejua hali yake, alimshauri Fermina afanye kazi ya kushona na kuuza nguo za kitamaduni za wanawake wa Kingobe. Fermina alifanya hivyo, na ingawa alikuwa na mahitaji mengine ya kimwili, alihakikisha kwamba anatumia pesa alizopata kuhudhuria mikutano ya Kikristo tu. Sasa yeye na familia yake wamehamia eneo lingine, na anaendelea kufanya maendeleo ya kiroho. Wanafurahi kwamba mbali na kushinda kizuizi cha kutojua kusoma na kuandika, wamemjua Yehova.

  • Kushinda Vizuizi vya Mawasiliano Huko Panama
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 15
    • [Picha katika ukurasa wa 8]

      Wanawake Wakuna wakiwa na vitambaa vyenye mapambo ya rangi mbalimbali

      [Picha katika ukurasa wa 9]

      Mmishonari amhubiria mwanamke Mngobe

      [Picha katika ukurasa wa 10]

      Mashahidi kutoka Ngobe wasafiri kwa mtumbwi kuhudhuria kusanyiko la pekee

      [Picha katika ukurasa wa 11]

      Watu wamejifunza kweli ya Biblia nchini Panama licha ya tofauti za utamaduni na lugha

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki