Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kushinda Vizuizi vya Mawasiliano Huko Panama
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 15
    • Kushinda Kizuizi cha Kutosikia

      Huko Panama, familia nyingi zenye viziwi huaibika. Wakati mwingine viziwi hawaelimishwi. Viziwi wengi huhisi kwamba wametengwa na kukataliwa kwa kuwa si rahisi kuwasiliana nao.

      Hivyo, ilikuwa wazi kwamba jambo fulani lilihitaji kufanywa ili kuwahubiria habari njema watu wenye matatizo ya kusikia. Kwa kutiwa moyo na mwangalizi anayesafiri, mapainia wenye bidii pamoja na wengine waliamua kujifunza Lugha ya Ishara ya Panama. Walipata matokeo kwa sababu ya ubunifu wao.

      Kufikia mwisho wa mwaka wa 2001, kikundi cha lugha ya ishara kilikuwa kimeanzishwa huko Panama City. Wahudhuriaji walikuwa 20 hivi. Kadiri ndugu na dada walivyoendelea kuwa stadi katika lugha hiyo, ndivyo walivyoweza kuwahubiria watu wengi ambao kwa mara ya kwanza “walisikia” kweli ya Biblia katika lugha yao. Pia, Mashahidi wengi walio na watoto wenye matatizo ya kusikia walianza kuhudhuria mikutano na wakatambua kwamba watoto wao walielewa mafundisho ya Biblia kwa urahisi na walifurahia kweli. Mara nyingi wazazi walijifunza lugha ya ishara, na hivyo waliwasiliana na watoto wao vizuri. Wazazi hao waliweza kuwasaidia watoto wao kiroho na familia ziliimarika. Kisa cha Elsa na binti yake Iraida kinathibitisha jambo hilo vizuri.

      Shahidi mmoja katika kikundi cha lugha ya ishara alipata habari kumhusu Iraida, akamtembelea, na kumwachia broshua Furahia Milele Maisha Duniani!c Iraida alifurahia sana yale aliyojifunza kutokana na picha za ulimwengu mpya. Funzo la Biblia lilianzishwa katika broshua hiyo. Baada ya kumaliza kujifunza broshua hiyo, walijifunza broshua Mungu Anataka Tufanye Nini?d Wakati huo, Iraida alianza kumwomba mama yake amsaidie kutayarisha na kumweleza habari aliyojifunza.

      Elsa alikuwa na matatizo mawili: Kwa sababu hakuwa Shahidi, hakujua kweli ya Biblia, wala hakuelewa lugha ya ishara. Alikuwa ameambiwa kwamba hapaswi kuwasiliana na binti yake kwa lugha ya ishara bali kwamba binti huyo anapaswa kujifunza kuzungumza. Hivyo, waliwasiliana mara chache sana. Akichochewa na ombi la Iraida la kutaka msaada, Elsa alimwomba Shahidi fulani kutanikoni ajifunze na Iraida. Elsa alisema hivi: “Nilifanya hivyo kwa faida ya binti yangu kwa kuwa sijawahi kumwona Iraida akifurahia sana chochote.” Elsa alijiunga na binti yake katika funzo na akajifunza lugha ya ishara. Kadiri Elsa alivyotumia muda mwingi pamoja na binti yake, ndivyo walivyowasiliana vizuri nyumbani. Iraida alianza kuwa mwangalifu kuhusu watu aliofanya urafiki nao, naye akashirikiana na kutaniko. Sasa, mama huyo na binti yake wanahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Elsa alibatizwa hivi karibuni, na Iraida anafanya maendeleo kufikia hatua hiyo. Elsa anasema kwamba kwa mara ya kwanza sasa amepata kumwelewa binti yake na wanaweza kuzungumzia mambo mengi muhimu yanayowapendeza.

      Kikundi cha lugha ya ishara ambacho kimekuwa kutaniko tangu Aprili 2003, sasa kina wahubiri wa Ufalme 50, na wale wanaohudhuria mikutano ni zaidi ya 50. Zaidi ya thuluthi moja ni viziwi. Vikundi vingine vya lugha ya ishara vimeanzishwa katika majiji mengine matatu nje ya jiji kuu la Panama City. Ijapokuwa bado kuna mengi ya kufanya katika eneo la lugha ya ishara, ni wazi kwamba hatua kubwa imepigwa katika kushinda kizuizi cha mawasiliano kati ya viziwi na Muumba wao mwenye upendo, Yehova Mungu.

  • Kushinda Vizuizi vya Mawasiliano Huko Panama
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Aprili 15
    • [Picha katika ukurasa wa 12]

      Funzo la “Mnara wa Mlinzi” katika lugha ya ishara

      [Picha katika ukurasa wa 12]

      Elsa na binti yake, Iraida, wanafurahia kuwasiliana

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki