-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kisha Tom na Rowena wakahamia Hanuabada, jina linalomaanisha “Kijiji Kikubwa” katika lugha ya wenyeji ya Motu. Kijiji hicho kilifika hadi kwenye Bandari ya Port Moresby na kilikuwa na mamia ya nyumba zilizotengenezwa juu ya nguzo za mbao na kuunganishwa na vijia virefu vya mbao vinavyofika hadi ufuoni. “Watu walituzunguka ili wasikilize habari njema,” anaandika Rowena. “Watu wengi sana walipendezwa hivi kwamba tulirudi kila jioni kuongoza mafunzo ya Biblia, tulikosa kurudi jioni mbili tu katika miezi miwili.” Tom anaongeza hivi: “Tumaini la ufufuo na kuishi katika paradiso duniani liliwavutia sana watu hawa. Wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo na polisi wa eneo hilo walijaribu kuwafanya waache kujifunza, lakini waliendelea kuwa imara. Kweli ilikuwa imeingia ndani sana ya mioyo yao.”
Raho na Konio Rakatani, Oda Sioni, Geua Nioki na mume wake, Heni Heni aliyekuwa amepata vichapo kutoka kwa wahubiri waliowasili katika mashua inayoitwa Lightbearer miaka 16 mapema, ni baadhi ya wale ambao walichukua msimamo imara kwa ajili ya kweli. Punde si punde, watu 30 hivi walikuwa wakihudhuria mikutano kwa ukawaida katika nyumba ya Heni Heni. “Wanaume waliketi upande mmoja na wanawake upande ule mwingine katika chumba hicho,” anakumbuka Oda Sioni, ambaye alikuwa kijana wakati huo. “Wanawake walivalia sketi za nyasi na hawakuwa na blauzi na waliwabeba watoto katika mifuko yenye kuvutia iliyofumwa kwa nyuzi na ilining’inizwa kwenye nguzo za chumba hicho. Baada ya kuwanyonyesha watoto, waliwatia ndani ya mifuko hiyo na kuibembeza polepole hadi watoto walipolala.”
Tom Kitto aliongoza mikutano hiyo akisaidiwa na mtafsiri. Nyakati nyingine mambo yalienda mrama. “Katika mkutano mmoja, ndugu ya Heni Heni, Badu Heni, alikuwa akitafsiri,” anaeleza Don Fielder, aliyefika huko katika mwaka wa 1953. “Mwanzoni ilionekana kwamba mambo yalikuwa shwari, kwa kuwa Badu alitafsiri maneno ya Tom na hata aliiga ishara zake. Baadaye tu ndipo Badu alimwambia Tom kuwa hakuelewa chochote ambacho alikuwa akisema. Alisema tu kweli alizokuwa amejua hapo awali na kuiga ishara za Tom ili ionekane kwamba hivyo ndivyo hotuba ilivyosema.” Licha ya hali hizo ngumu, kikundi hicho kilikua upesi, na baada ya muda kikundi cha pili kilianzishwa katika nyumba ya Raho Rakatani, ambayo pia ilikuwa kwenye kijiji cha Hanuabada.
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 79]
Kijiji cha Hanuabada na sehemu fulani ya Port Moresby inaonekana upande wa nyuma
-