-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Huko Goroka, kwenye Mkoa wa Nyanda za Juu za Mashariki, kutaniko dogo lilikutana nyumbani kwa mtu fulani. Baadaye, walijenga mahali pa kukutania kwa kutumia vifaa walivyopata msituni. Kisha, mnamo 1967, walijenga Jumba la Ufalme lenye kuvutia lililokuwa na viti 40. “Nilitania kwamba tutajaza viti hivyo wakati wa Har–Magedoni,” anasema George Coxsen, aliyetumika kwenye nyanda za juu kwa miaka kumi. “Nilikosea kama nini! Katika muda wa miezi 12, watu wengi sana walikuwa wakihudhuria mikutano hivi kwamba tulihitaji kuanzisha kutaniko la pili!”
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mbali zaidi upande wa mashariki, karibu na Kainantu, Norm Sharein alijifunza Biblia na zaidi ya wanakijiji 50 ambao walikuja nyumbani kwake kila siku. Baadaye, mapainia Berndt na Erna Andersson walitunza kikundi hicho kwa muda wa miaka miwili na nusu. “Mara nyingi watu hawakuoga, walivalia mavazi machache, hawakujua kusoma na kuandika, na walijihusisha sana na uchawi,” anaeleza Erna. “Hata hivyo, kwa sababu ya kusaidiwa kwa subira na upendo, baadhi yao walianza kukariri na kueleza maandiko 150.”
Berndt na Erna walikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na kikundi hicho. “Tulipopewa mgawo wa kwenda Kavieng, wanawake walinizunguka wakilia, na kuomboleza kwa sauti kubwa!” anasema Erna. “Mmoja baada ya mwingine, walishika mikono yangu na kunigusa usoni huku machozi yao yakitiririka. Tena na tena, nilirudi ndani ya nyumba na kulia huku Berndt akijaribu kuwatuliza, lakini hawangeweza kufarijika. Mwishowe, tulipoanza kuondoka, umati mkubwa ulifuata gari letu lilipokuwa likiteremka mlimani, wanawake wakilia kwa sauti kubwa. Bado mimi hushindwa na hisia ninapoeleza jinsi nilivyohisi siku hiyo. Tunatamani kama nini kuwaona watu hao tuliowapenda sana katika ulimwengu mpya!” Mapainia wengine waliendeleza kazi ya Berndt na Erna, na kutaniko zuri likaanzishwa huko Kainantu.
-