-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Baadaye, painia mwingine kijana kutoka Australia, Glenn Finlay, alichukua mahali pa Jim na Lionel na akahubiri peke yake kwa miezi 18 huko Kerema. “Ulikuwa wakati mgumu sana kwangu,” anasema Glenn, “na nyakati nyingine nilijiuliza ikiwa nilikuwa nikitimiza jambo lolote kupitia kazi yangu. Lakini tukio fulani lenye kunyenyekeza lilibadili maoni yangu.
“Mmoja wa wanafunzi wangu wa Biblia alikuwa mzee anayeitwa Hevoko, aliyekuwa mwokaji katika kijiji hicho. Hakujua kusoma wala kuandika na baada ya miezi kadhaa alikuwa ameelewa kweli chache tu za msingi. Nilijiuliza ikiwa kulikuwa na faida yoyote kumfundisha. Kisha asubuhi moja, nilipokaribia nyumba yake, nilisikia sauti yake na nikasimama ili nisikilize. Hevoko alikuwa akisali kwa sauti kwa Yehova, akimshukuru kutoka moyoni kwa sababu amemfundisha ukweli kuhusu jina na Ufalme wake. Sala hiyo ya unyoofu ilinikumbusha kwamba Yehova hutazama mioyo ya watu, si akili. Anajua vizuri ni nani wanaompenda.”—Yoh. 6:44.
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Maeneo mapya yalipofunguka, mapainia walifanya kazi ngumu na kwa muda mrefu kutafsiri vichapo katika lugha nyingine za kienyeji. Jim Smith anaeleza hivi: “Kwa kuandika maneno mapya, nilifanya kazi kubwa sana kutokeza kamusi ya Kitairuma na maandishi kuhusu sarufi, ambayo tulitumia kutafsiri makala za funzo la Mnara wa Mlinzi. Mara nyingi nilifanya kazi hadi usiku nikipiga chapa makala zilizotafsiriwa ili kuwapa watu watakaohudhuria mikutano. Baadaye nilitafsiri trakti na kijitabu katika Kitairuma. Vichapo hivyo vya mapema viliwasaidia watu wengi wa Kerema kujifunza kweli.”
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
KAZI YA KUHUBIRI YAENEA KASKAZINI
Mnamo Juni 1956, Ken na Rosina Frame, mapainia waliokuwa wametoka tu kuoana walikuwa Mashahidi wa kwanza kuhamia New Ireland, kisiwa kimoja kati ya Visiwa vya Bismarck vilivyoko kaskazini-mashariki mwa Papua New Guinea. Ken, aliyekuwa mhasibu, alifanya kazi katika kampuni kubwa huko Kavieng, mji mkuu wa kisiwa hicho. “Kabla ya kuondoka Sydney,” Ken anaeleza, “tulishauriwa kwamba tuwaache watu watuzoee kabla ya kuanza kuhubiri hadharani. Rosina alikuwa mshonaji stadi wa nguo na baada ya muda mfupi alikuwa na wateja wengi. Tuliwahubiria kwa njia isiyo rasmi, na baada ya muda kukawa na kikundi kidogo cha watu waliopendezwa ambao walikutana kwa siri nyumbani kwetu mara moja kwa juma.
“Miezi 18 baadaye, mwangalizi wa mzunguko, John Cutforth, alitutembelea na kuuliza ikiwa angeonyesha sinema yenye kichwa The Happiness of the New World Society. Nilizungumza na mmiliki wa jumba la sinema, naye akakubali kuonyesha sinema yetu ya bila malipo. Lazima wafanyakazi wake waliwaambia watu wengine kuhusu sinema hiyo kwani tulipofika kwenye jumba hilo, lango lake lilikuwa limejaa watu, na tulihitaji msaada kutoka kwa polisi ili tufaulu kuingia ndani. Zaidi ya watu 230 walikuja kuitazama, bila kuhesabu watu waliochungulia kwenye madirisha yaliyokuwa wazi. Baada ya hapo tulihubiri waziwazi.”
Mnamo Julai 1957, kutaniko lilianzishwa huko Rabaul, New Britain, mji maridadi wa bandarini uliokuwa katikati ya milima miwili ya volkano hai. Kutaniko la Rabaul lilikutana nyuma ya nyumba iliyokodishwa na mapainia wa pekee. “Zaidi ya watu 100 walikuja kwenye nyumba hiyo kila usiku ili kujifunza Biblia,” anasema painia Norm Sharein. “Tuliwapanga katika vikundi vya watu 20 hivi na kuwafundisha kwa kutumia taa za mafuta chini ya miti.”
Kutaniko lilipokuwa na kusanyiko la kwanza la mzunguko, watu saba walibatizwa ufuoni. Mara moja watano kati yao wakawa mapainia. Lakini ni wapi ambapo wangetumika vizuri zaidi? Ofisi ya tawi ya Australia ilitoa jibu—Madang.
Huko Madang, mji ulioko kaskazini-mashariki mwa pwani, “mashamba” yalikuwa tayari kuvunwa. (Yoh. 4:35) Kwa kweli, kikundi hicho kidogo cha wahubiri hakingeweza kushughulikia watu wote waliopendezwa. Painia Mkanada Matthew Pope na familia yake walipofika na kununua nyumba yenye vyumba kadhaa upande wa nyuma, njia ilifunguka ya kuwatuma mapainia wengi zaidi huko.
Mapainia wanane waliwasili kutoka Rabaul na wakaishi katika sehemu mbalimbali za Wilaya ya Madang. Mmoja wao, Tamul Marung, alinunua baiskeli na kusafiri kwa kutumia mashua hadi Basken, kijiji cha nyumbani kwao, kilomita 48 kaskazini ya Madang. Baada ya kuhubiri huko Basken, alipanda baiskeli yake na kurudi Madang, akihubiri njiani. Kisha alirudi Basken, akaanzisha kutaniko, na kufanya upainia kwa miaka mingine 25. Katika kipindi hicho, alioa na akapata watoto. Baadaye, binti na mpwa wake wa kike walitumika Betheli.
-