Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Papua New Guinea
    2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • ‘WAPIGENI MARUFUKU MASHAHIDI’

      Wapinzani wetu hawakufurahia maendeleo hayo. Kuanzia 1960 na kuendelea, muungano wa makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo, shirika la kuwategemeza wanajeshi waliostaafu na wanajeshi wengine wa Australia (Returned Services League, RSL), na vyombo vya habari vilianza kampeni iliyopangwa ya kuwavunjia heshima na kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova.

      Mambo yalifikia kilele wakati ambapo karatasi iliyochapishwa kuhusu msimamo wetu juu ya kutiwa damu mishipani iliposambazwa kwa madaktari, makasisi, na maofisa wa serikali. Kama kawaida, makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo ndio waliokuwa wa kwanza kusema. Agosti 30, 1960, gazeti South Pacific Post lilikuwa na kichwa “Makanisa Yakasirishwa na Suala la Damu.” Katika makala inayokuwa ndani, viongozi wa kanisa walisema kuwa Mashahidi ni “wapinga-Kristo [na] maadui wa Kanisa.”

      Makala zilizofuata zilidai kwa uwongo kwamba Mashahidi wa Yehova ni wachochezi na kwamba mafundisho yao yaliwachochea watu wasiende shuleni, wasilipe kodi, wajiunge na madhehebu ya waabudu-mali, na wasidumishe usafi. Ripoti nyingine za uwongo ziliwashtaki kwa kutumia vibaya kupatwa kwa jua ili kuwaogopesha na “kuwadhibiti wenyeji wasio na elimu.” Gazeti moja hata liliwazomea Mashahidi kwa “kuishi, kula, na kufanya kazi pamoja na wanakijiji.” Gazeti South Pacific Post liliwachambua kwa kufundisha kwamba “watu wote wako sawa” na likadai kwamba Mashahidi ni “tisho kubwa kuliko Ukomunisti.”

      Mwishowe, Machi 25, 1962, RSL iliwaomba wenye mamlaka wakoloni wawapige Mashahidi marufuku. Hata hivyo, serikali ya Australia ilikataa waziwazi ombi hilo. “Tangazo hilo lilikuwa na matokeo mazuri katika nchi yote,” anasema Don Fielder. “Watu wenye akili zilizofunguka wangeweza kuona kwamba madai ya wapinzani hayakuwa ya kweli.”

  • Papua New Guinea
    2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Ninakumbuka pindi moja nilikuwa nikihubiri karibu na Rabaul. Mwanamume mmoja Mtolai aliniomba Biblia yangu ili aishike na kujisomea mwenyewe andiko fulani. Nilipompa, aliirarua vipande-vipande na kuitupa chini. Badala ya kumkasirikia, niliripoti kisa hicho kwa kamanda wa polisi, ambaye alimtuma afisa mmoja wa polisi amkamate bwana huyo mara moja. Kamanda huyo alimwambia yule bwana: “Wewe ni mtu mbaya. Ulivunja sheria ya Mungu na ya serikali. Kesho lazima umnunulie mtu huyo Biblia mpya, la sivyo utafungwa jela.” Baada ya hayo kamanda huyo aliniambia nirudi kwenye kituo hicho cha polisi saa 4 kamili asubuhi iliyofuata ili nichukue pesa za kununua Biblia nyingine. Nilipofika kesho yake, pesa zilikuwa tayari. Tangu wakati huo, watu wengi Watolai wamejifunza kweli.

      Katika pindi nyingine, nilikuwa pamoja na kikundi cha Mashahidi tukigawa trakti Habari za Ufalme katika eneo la magharibi ya Wewak. Mashahidi wale wengine walinitangulia. Hata hivyo, kiongozi mmoja wa kijiji, aliwaona akina ndugu wakigawa nakala za trakti hiyo na kuzikusanya. Ni kana kwamba alijua kwamba nilikuwa nikiwafuata kwa sababu alisimama katikati ya barabara na kuningoja, mikono yake ikiwa kiunoni huku akiwa ameshika zile nakala za Habari za Ufalme. Nilimuuliza ikiwa kulikuwa na shida yoyote. Akanikabidhi trakti zile na kusema, “Mimi ndiye ninayesimamia eneo hili, na sitaki kukuona ukigawa makaratasi haya.”

      Nikazichukua kutoka kwake. Wakati huo wanakijiji walikuwa wamekusanyika mahali pale. Niliwatazama na kuwauliza, “Ikiwa mnataka kulima mashamba yenu au kwenda kuvua samaki, je, mnahitaji kupata ruhusa rasmi?”

      “Hapana!” akasema mwanamke mmoja.

      Kisha nikawauliza, “Mngependa kusoma trakti hizi?”

      “Ndiyo,” wakasema. Kwa hiyo nikawagawia tena zile trakti za Habari za Ufalme bila upinzani wowote. Hata hivyo, nilihitaji kujitetea baadaye mbele ya jopo la wazee 20 wa kijiji. Jambo la kupendeza ni kwamba 18 kati yao walikubali tuendelee na kazi yetu ya kuhubiri.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki