-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
UVUMILIVU LICHA YA HALI NGUMU
Dini mbalimbali zilizo huko Papua New Guinea zilikuwa na mkataba usio rasmi wa mahali ambapo kila dini ilipaswa kuendesha shughuli zake. Kila kikundi cha kanisa kilikuwa na eneo lake na ilitarajiwa kwamba dini nyingine hazitaingilia eneo hilo. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova huwahubiria habari njema watu wote wanaotaka kusikiliza, haidhuru wanaishi wapi. Viongozi wa kidini walikasirika sana kwa kuwa Mashahidi walifanya hivyo na pia kwa sababu watu wengi walisikiliza kweli.
“Baada ya kuhamia kisiwa kidogo cha Kurmalak, kilicho kwenye mkoa wa West New Britain, mtu wa kwanza aliyenitembelea alikuwa kasisi wa Kianglikana,” anasema Norm Sharein. “‘Huna ruhusa ya kuhubiri katika eneo langu,’ akasema. ‘Watu hawa tayari ni Wakristo!’
“Baadaye nilimwona mtu mmoja niliyekuwa nikijifunza naye Biblia akipiga makasia ya mtumbwi wake kwa kasi katika mvua nyingi na bahari iliyochafuka akielekea ufuoni. Kwa kweli, alikuwa akihatarisha uhai wake kwa kusafiri katika hali hiyo mbaya ya hewa. Alivuta mtumbwi wake kwenye ufuo na, huku akipumua kwa nguvu, akaniambia kwamba Wakatoliki waliojaa katika mashua moja wakiongozwa na mwalimu wao wa katekisimu, walikuwa wakija kunipiga. Sikuwa na mahali pa kukimbilia, kwa hiyo nikamwomba Yehova anipe hekima na nguvu.
“Mashua hiyo ilipowasili, wanaume 15 hivi walishuka, wakiwa na nyuso zilizopakwa rangi nyekundu—jambo lilionyesha wazi kwamba walitaka kunidhuru. Badala ya kungoja waje kwangu, nilienda kukutana nao. Mapema nilikuwa na woga, lakini sasa sikuhisi woga. Nilipowakaribia, walinitukana wakifikiri kwamba hilo lingenichochea kupigana nao, lakini nilibaki nikiwa mtulivu.
“Pia, kati ya watu waliokusanyika mahali hapo, kulikuwa na mwanamume mwingine mzee ambaye nilijifunza naye Biblia, naye ndiye aliyemiliki kisiwa hicho. Akiwa na nia nzuri, aliwaambia hivi wanaume hao: ‘Mashahidi wa Yehova hawapigani. Hebu mpigeni mjionee wenyewe!’
“‘Sasa mtu huyu yuko upande wa nani?’ nilijiuliza, nikitamani anyamaze.
“Baada ya kuzungumza nao kwa dakika kadhaa, niliwaomba waondoke, na kama ishara ya kwamba sikuwa na uhasama wowote, nilimnyoshea kiongozi wao mkono wangu wa kulia. Akiwa ameshangaa, aliwatazama wenzake, nao wakamtazama. Kisha akanisalimu. Hilo lilifanya kila mtu astarehe, na sote tukasalimiana. Baadaye waliondoka na nikatulia sana! Nilikumbuka maneno ya Paulo kwa Timotheo: ‘Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote, . . . akiendelea kujizuia chini ya uovu.’”—2 Tim. 2:24.
Berndt Andersson anakumbuka kwamba katika kijiji kimoja kilichokuwa mlimani, kasisi mmoja wa Kilutheri na kikundi chenye ghasia cha wanaume 70 hivi kutoka kijiji kingine walijaribu kuwafukuza Mashahidi na kuharibu Jumba lao la Ufalme. Wanaume hao walishangaa Berndt alipoenda kukutana nao. Alimkaribia kasisi huyo na kumwuliza kwa nini misheni ya Kilutheri inasema kwamba Mungu anaitwa Anutu, jina la kienyeji ambalo lilianza kutumiwa na Wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo. Kasisi huyo alisema kwamba jina hilo linapatikana katika Biblia, hivyo Berndt akamwomba amwonyeshe linapatikana wapi. Kasisi huyo alifungua Biblia yake, na aliposhindwa kulipata, Berndt akamwomba asome Zaburi 83:18. Baada ya kumsaidia kupata andiko hilo, kasisi alianza kulisoma kwa sauti. Alipofikia jina Yehova, alifunga Biblia yake na kusema kwa sauti, “Huo ni uwongo!” Aligundua kwamba tayari alikuwa ameishutumu Biblia yake mwenyewe. Baada ya kisa hicho, wafuasi wake wengi walibadili mtazamo wao kuwaelekea Mashahidi.
Nyakati nyingine wapinzani wa kidini waliteketeza Majumba ya Ufalme yaliyojengwa kwa nyasi, kama ilivyotukia katika kijiji cha Agi, katika Mkoa wa Milne Bay. Hata hivyo, katika kisa hicho, mmoja wa watu walioteketeza jumba hilo, alikuwa mlevi wakati huo, na alijuta sana. Baadaye aliwafikia akina ndugu na kukubali kujifunza Biblia, naye akawa painia. Isitoshe, alikubaliwa kuishi katika nyumba ya mapainia iliyokuwa kando ya jumba hilo lililojengwa upya. Hivyo akawa mtunzaji wa jumba lililojengwa mahali palepale alipoteketeza lile la kwanza!
Leo, mateso yanayochochewa na dini yamepungua. “Tumeingia katika kipindi cha amani,” anasema Craig Speegle.
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Muda mfupi baadaye, nilianza kujifunza Biblia na familia 12 katika Kisiwa cha Bagabag. Tulifanya mikutano kwa ukawaida katika nyumba ya mjomba wangu, kwa kutumia njia ileile ya kujifunza Biblia niliyokuwa nimeona huko Madang. Baba yangu aliyekuwa na cheo cha juu katika Kanisa la Kilutheri, alikasirishwa sana na jambo hilo. “Mimi ninamjua Yahweh lakini simjui Yehova,” alifoka. Nilifungua Biblia yangu ya Kitok Pisin na kumwonyesha maelezo ya chini yanayopatikana katika andiko la Kutoka 3:15, ambayo yanaeleza kuhusu jina la Mungu. Baba yangu hakuwa na la kusema.
Alinipeleka mara tatu mbele ya viongozi wa kanisa ili niitetee imani yangu. Mkutano mmoja kati ya hiyo ulifanywa katika kanisa kubwa zaidi kwenye kisiwa hicho. Zaidi ya watu mia moja walihudhuria. Kila mtu alikuwa na wasiwasi. Mwenyekiti aliniuliza, “Utajitetea jinsi gani?” “Ninataka tu kufanya kama Mathayo 6:33 inavyosema na kuutanguliza Ufalme wa Mungu,” nikajibu huku nikiwa nimeshikilia Biblia yangu kwa nguvu. Baba yangu alisimama kwa ghafula na kwa hasira nyingi akasema hivi kwa sauti kubwa, “Unajaribu kutufundisha?” Mjomba wangu mmoja alisimama ili anipige, lakini mtu fulani wa ukoo akamzuia mara moja. Fujo zikaanza katika mkutano huo. Mwishowe, niliambiwa niondoke.
-