-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Wamishonari fulani hutumika katika kazi ya kuzungukia makutaniko. Ili kutembelea makutaniko, huenda wakatumia usafiri wowote unaopatikana. Mambo yalikuwa hivyo kwa Edgar Mangoma. Mizunguko aliyotembelea ilitia ndani Mto Fly na Ziwa Murray. “Nilipotembelea makutaniko mawili yaliyo kando ya ziwa, nilisafiri kwa mitumbwi ambayo nyakati nyingine ilikuwa na injini au nyakati nyingine haikuwa nayo. Niliposafiri kwa mtumbwi ambao haukuwa na injini, ingenichukua saa nane kutoka kutaniko moja hadi lile lingine. Kwa kawaida, ndugu watatu au wanne waliandamana nami, ili warudi na mtumbwi baada ya kunifikisha nilikokuwa nikienda. Niliwathamini sana ndugu hao!”
Kielelezo kizuri cha wamishonari, kutia ndani unyenyekevu na upendo wao kwa watu, ulikuwa na matokeo mazuri. Mwangalizi mmoja wa mzunguko anasema hivi: “Wanakijiji walishangaa kuniona nikiishi na watu wanaopendezwa na kula pamoja nao. Hata baadhi yao wameniambia: ‘Wewe unamwabudu Mungu kwa njia inayofaa. Makasisi wetu hawashirikiani nasi kama vile wewe unavyofanya.’”
Je, dada wamishonari wanaotumika Papua New Guinea huona ikiwa vigumu kuzoea maisha ya huko? “Kwa miezi michache ya kwanza ilikuwa vigumu kwangu,” anasema Ruth Boland, ambaye aliambatana na mume wake, David, katika kazi ya kusafiri. “Mara nyingi nilijihisi siwezi kuendelea. Lakini ninafurahi kwamba sikuacha, kwa kuwa nimekuja kuwathamini na kuwapenda ndugu na dada. Mimi na mume wangu hatukujifikiria sana bali tuliwafikiria wengine. Kwa kweli, shangwe tuliyopata haina kifani. Hatukuwa na vitu vya kimwili, lakini tulikuwa matajiri kiroho. Na tuliona jinsi ambavyo Yehova alibariki kazi ya kuhubiri habari njema na pia maisha yetu. Usipokuwa na vitu vya kimwili, unamtegemea Yehova zaidi na kupata baraka zake.”
-
-
Papua New Guinea2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 147, 148]
“Yehova Ndiye Mwalimu Wetu Mkuu Zaidi”
JOHN TAVOISA
ALIZALIWA 1964
ALIBATIZWA 1979
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alipokuwa mtoto aliteswa kikatili na walimu na wanafunzi wenzake na akalazimika kuacha shule baada ya kusoma kwa miaka miwili tu. Sasa anatumika akiwa mwangalizi wa mzunguko.
◼ NILIZALIWA katika kijiji cha Govigovi kwenye Mkoa wa Milne Bay. Baba yangu alianza kujifunza Biblia nilipokuwa na umri wa miaka saba na alinifundisha mambo aliyokuwa akijifunza.
Huo ndio wakati nilipoanza masomo yangu kwenye shule ya umma. Walimu wangu wawili, ambao walikuwa Waanglikana, walipogundua kwamba nilikuwa nikishirikiana na Mashahidi, walianza kunitesa. Wanafunzi wengine wakafanya hivyo pia, nyakati nyingine wakinipiga kwa fimbo. Kwa sababu hiyo nililazimika kuacha shule baada ya miaka miwili tu.
Mwaka mmoja hivi baadaye, nilikutana na mmoja kati ya walimu hao sokoni. “Wewe ni mwanafunzi mwerevu na ungefanya vizuri sana shuleni,” akaniambia. “Lakini kwa sababu ya dini yako, utakuwa mtumishi wa wanafunzi wenzako.” Nilipomwambia baba yangu kile ambacho mwalimu huyo alikuwa amesema, aliniambia maneno yenye kutia moyo sana. “Ikiwa ulimwengu hautakuelimisha,” akasema, “Yehova atafanya hivyo.”
Baba na ndugu mmoja painia wa pekee walinisaidia nipate elimu yenye thamani zaidi ya zote—ujuzi unaoongoza kwenye uzima wa milele. (Yoh. 17:3) Lugha yangu ya mama ni Dawawa, lakini walinifundisha Biblia katika Kihiri Motu, ambayo ilikuwa lugha yangu ya pili, na pia katika Kitok Pisin, ambayo ikawa lugha yangu ya tatu. Nilibatizwa nikiwa na umri wa miaka 15. Miaka miwili baadaye nikawa painia.
Mnamo 1998, nilialikwa kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Wakati huo sikujua Kiingereza vizuri. Kwa hiyo, ili nijitayarishe kwa ajili ya shule hiyo, ofisi ya tawi iliniambia nishirikiane na kutaniko la Kiingereza huko Port Moresby. Kwa hiyo, Kiingereza kikawa lugha yangu ya nne.
Baada ya kuhitimu, nilitumwa katika Kutaniko la Alotau kwenye Mkoa wa Milne Bay. Miezi sita baadaye, nilishangaa na kufurahi sana nilipowekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko. Mzunguko wangu wa kwanza ulitia ndani New Britain, New Ireland, Kisiwa cha Manus, na visiwa vingine vya karibu. Katika mwaka wa 2006, nilimwoa Judy, na tukawa mapainia wa pekee kwa mwaka mmoja, na baada ya hapo tukaendelea na kazi ya mzunguko.
Ninapoyazuru makutaniko, mara nyingi mimi huwaambia vijana: “Yehova ndiye Mwalimu wetu mkuu zaidi. Kwa hiyo mwache akufundishe, kwa sababu anaweza kukusaidia upate mafanikio ya kweli maishani.” Kwa kweli, hilo ni somo muhimu sana ambalo nimejifunza.
[Picha]
Nikiwa na mke wangu, Judy
-