Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb04 kur. 43-64
  • Ripoti ya Ulimwenguni Pote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ripoti ya Ulimwenguni Pote
  • 2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
yb04 kur. 43-64

Ripoti ya Ulimwenguni Pote

◼ ULAYA

Idadi ya nchi: 46

Idadi ya watu: 728,162,887

Idadi ya wahubiri: 1,476,554

Idadi ya mafunzo ya Biblia: 697,044

Nyakati nyingine inaweza kuchukua muda mrefu sana kwa mtu ambaye amejifunza kweli kuwa Shahidi wa Yehova. Steponas alikuwa amefungwa kwa sababu za kisiasa katika kambi fulani huko Kazakhstan mwaka wa 1951. Alifanya kazi pamoja na Edvardas, Shahidi kijana mwenye bidii kutoka Lithuania, ambaye alikuwa amefungwa kwa sababu ya kuchapa gazeti la Mnara wa Mlinzi. Edvardas alimweleza kuhusu tumaini lake linalotegemea Biblia, na Steponas alisadikishwa kwamba alikuwa amepata kweli. Steponas aliachiliwa mwaka wa 1955. Walipoachana, Edvardas alimwambia hivi: “Huenda tukakutana tena siku moja.” Ijapokuwa Steponas hakuwa amebatizwa, maafisa wa Halmashauri ya Usalama ya Kitaifa ya Sovieti walifikiri kwamba alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Polisi walipekua nyumba yake na kuchukua karatasi zilizokuwa na anwani za ndugu. Hivyo, hakuweza kuwasiliana tena na watu wa Mungu.

Miaka 47 ilipita. Kwa muda huo wote Steponas aliishi katika kijiji kidogo kaskazini mwa Lithuania ambako hakukuwa na Mashahidi. Kisha mapema mwaka wa 2002 alipata vitabu fulani na aliiandikia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Lithuania kuomba kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia. Anaeleza hivi: “Nilituma barua hiyo nikitumaini kwamba ningeweza kuwasiliana tena na akina ndugu.” Wenzi wa ndoa walio mapainia wa pekee walisafiri hadi kwenye kijiji chake ili kujifunza Biblia naye. Kabla ya mwaka kwisha, Steponas alibatizwa akiwa na umri wa miaka 80.

Je, alikutana tena na Edvardas ambaye karibu miaka 50 iliyopita alikuwa amesema: “Huenda tukakutana tena siku moja”? Ndiyo! Siku iliyofuata ubatizo wake, watu hao wawili ambao sasa ni ndugu wa kiroho, walikumbatiana kwa shauku na furaha nyingi.

Nchini Uingereza, Tim na Sam, wahubiri wasiobatizwa wenye umri wa miaka 11, walikuwa wakihubiri pamoja na mama ya Tim. Wavulana hao walihitaji mikoba mipya ya mahubiri, lakini hawakuwa na pesa. Mapema siku hiyo, kabla ya kwenda shambani, mama za wahubiri hao wachanga walisali kuhusu jambo hilo. Katika nyumba ya mwisho waliyotembelea asubuhi hiyo, Tim aliongea na mwenye nyumba na kumsomea andiko moja la Biblia. Mwenye nyumba huyo alimkatiza na kumwuliza dini yake. Tim alimjibu kwamba yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Mwanamke huyo alimkemea Tim na kumwambia mama yake kwamba hawezi kuelewa ni kwa nini Mashahidi huwaacha watoto wao wafe badala ya kukubali watiwe damu mishipani.

Mama ya Tim alimwambia mwanamke huyo awaulize wavulana maoni yao kuhusu jambo hilo. Aliwauliza swali hilo na Tim alimweleza kwamba yeye angechagua matibabu mengine badala ya kutenda kinyume cha dhamiri yake iliyozoezwa kupatana na Biblia. Kisha, Sam alisema kwamba dada yake alitibiwa bila kutiwa damu mishipani, naye alipona haraka kuliko wagonjwa ambao walikuwa wametiwa damu.

Mwenye nyumba huyo alimgeukia tena mama ya Tim. Wakati huu alilalamika kwamba Mashahidi wa Yehova huwapeleka watoto wachanga katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Wavulana wote wawili walijibu kwamba wao hufurahia kazi ya kuhubiri na wanapenda kufanya kazi hiyo kuliko kuzurura-zurura mitaani kama vijana wengine wa rika lao. Mwenye nyumba huyo alivutiwa na majibu yao na kuwaomba wangoje kidogo, kisha akaingia katika nyumba yake. Walishangaa sana aliporudi na kuwapa mikoba miwili mipya maridadi sana, inayofaa kabisa kazi ya kuhubiri! Mwanamke huyo hujiruzuku kwa kuuza mikoba. Kwa sababu mtazamo wake ulibadilika, wavulana hao walipanga kumrudia. Walipokuwa wakiondoka, mama ya mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 94, ambaye alikuwa akisikiliza, alikuja mlangoni na kumwomba mama ya Tim amtembelee nyumbani kwake.

Dada wawili waliokuwa shambani waliona ujumbe huu uliobandikwa kwenye kituo cha basi huko Ureno: “Mimi ninajifunza saikolojia na ninafanya utafiti kuhusu ushirikina. Ukiweza kunisaidia tafadhali niandikie barua-pepe kwa kutumia anwani ifuatayo . . .” Alasiri hiyo, dada hao walikuwa wakigawa gazeti la Mnara wa Mlinzi lenye kichwa, “Je, Ushirikina Unaongoza Maisha Yako?” Kwa hiyo, waliamua kuandika barua-pepe na kumtolea mwanamke huyo gazeti hilo.

Juma moja baadaye mwanamke aliyekuwa amebandika ujumbe kwenye kituo cha basi aliwajibu hivi: “Asanteni kwa kujibu ombi langu. Nawaomba radhi kwa kuchelewa kujibu. Ningependa kupata gazeti mlilotaja. Sijapata nafasi ya kuongea na Mashahidi hivi karibuni kwa sababu kila mara wanaponijia na kutaka kuongea nami, mimi huwa na haraka sana kwenda kazini au ninakimbia kupata basi. Ninaona kwamba ninyi huongoza mafunzo ya Biblia, ningependa kuwa na funzo kama hilo.”

Dada hao walisema hivi: “Tulipomtembelea kwa mara ya kwanza alikuwa na maswali mengi sana. Tulimpa kitabu Ujuzi na kupanga kujifunza Biblia pamoja naye. Sikuzote anatayarisha funzo vizuri sana na sasa yeye huhudhuria mikutano yote.”

Lina, ambaye ni mhubiri katika jiji moja kusini mwa Ujerumani, alikuwa akihubiri barabarani wakati mwanamke anayeitwa Tatjana alipoanza kuzungumza naye. Tatjana alimwuliza: “Je, unanikumbuka?” Lina hakumtambua. Tatjana alisema: “Si ajabu, kwa kuwa tulikutana mara moja tu miaka mitano iliyopita.” Kisha akaongeza: “Uliongea nami barabarani mapema mwaka wa 1998, na kunitolea broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Nilikujibu kwa madharau, lakini ulikuwa mwenye fadhili na urafiki sana hivi kwamba nilivutiwa kuisoma broshua hiyo. Habari zake zilinigusa sana.” Baadaye, Mashahidi wawili wasiomfahamu Lina walimtembelea Tatjana nyumbani. Kwa sababu alipendezwa na yale aliyosoma katika broshua, Tatjana alikubali funzo la Biblia. Alipokutana na Lina tena mwaka wa 2003, tayari alikuwa Shahidi aliyebatizwa. Na wote wawili, Tatjana na Lina, walikuwa mapainia wasaidizi mwezi huo!

Ofisi ya tawi ilimtumia dada mmoja huko Pskov, Urusi, anwani ya mtu ambaye anaishi katika eneo la mbali. Ilimchukua dada huyo muda mrefu kusafiri hadi eneo hilo. Alipofika hatimaye, aligundua kwamba mtu huyo hakujua kwamba alikuwa ameomba funzo la Biblia. Alikuwa amenunua kitabu fulani katika kibanda kimoja, na ndani ya kitabu hicho alipata kisehemu cha trakti kinachomtolea msomaji kitabu fulani. Mtu huyo alisema kwamba alidhani zawadi fulani ilikuwa ikitolewa, kwa hiyo, alituma kikaratasi hicho akifikiri atashinda zawadi. Dada alimjibu hivi: “Umeshinda funzo la Biblia bila malipo!” Mtu huyo na familia yake walipendezwa na funzo la Biblia likaanzishwa. Dada huyo huongoza funzo hilo mara mbili kwa mwezi kwa sababu familia hiyo wanaishi mbali na nyumbani kwake.

◼OCEANIA

Idadi ya nchi: 30

Idadi ya watu: 34,355,946

Idadi ya wahubiri: 93,718

Idadi ya mafunzo ya Biblia: 47,270

Alyce mwenye umri wa miaka 14, ambaye anaishi Australia, alitumia habari zilizo katika magazeti yetu kuandika insha. Juma moja aliandika insha kuhusu swali, “Ni Nini Kitakachoupata Ulimwengu Huu?” Insha hiyo ilieleza maana ya nyakati zetu kulingana na unabii wa Biblia. Mwalimu alitaka kujua dini yake. Alyce alimweleza kwamba alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, kisha akampa mwalimu wake magazeti kadhaa.

Ingawa mwalimu wa Alyce alipendezwa, mwalimu mwingine alimshauri asishirikiane na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, baada ya kuuchunguza mwenendo wa Alyce kwa miezi kadhaa, mwalimu wake aliamua kufanya utafiti zaidi. Akiwa na wasiwasi kwamba huenda Alyce anashirikiana na madhehebu hatari, alienda kwenye maktaba na kuazima kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu. Alikisoma kitabu chote mwishoni mwa juma! Akisadiki kwamba alikuwa amepata kweli, alimpigia simu mama ya Alyce na kumwomba vitabu vingine na akaanza kujifunza Biblia na Mashahidi. Baada ya mwezi mmoja, alikuwa akihudhuria mikutano yote na alikuwa amemsadikisha mume wake na mama yake wahudhurie mikutano ya Jumapili. Wao pia walianza kujifunza Biblia na wanafanya maendeleo. Baada ya miezi mitatu, mwalimu huyo akawa mhubiri asiyebatizwa na akatoa hotuba yake ya kwanza katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Miezi michache baadaye, Alyce na mwalimu wake, Linda, walibatizwa siku ileile.

Hebu wazia ukiwa mwabudu pekee wa Yehova katika kisiwa fulani! Dada mmoja wa Visiwa vya Marshall, alijikuta katika hali hiyo. Mumewe anafanya kazi kwenye kisiwa cha matumbawe cha Mejatto. Majirani walimwalika dada huyo kwenye kanisa la Kiprotestanti, lakini alikataa. Badala yake, alijitahidi kuwafundisha watoto wake akitumia Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Aliwaeleza majirani wake kuhusu imani yake, na kuhubiri nyumba kwa nyumba akiwa amembeba mtoto wake mchanga. Hatimaye, baadhi yao walipendezwa, na dada huyo sasa anaongoza mafunzo kadhaa ya Biblia akitumia broshua Anataka. Kila mwezi, yeye hutuma ripoti yake ya utumishi wa shambani kwenye kutaniko lake la zamani. Yeye, pamoja na watoto wake husafiri mbali sana kwa mashua ili kuhudhuria Ukumbusho na makusanyiko kwenye kisiwa cha Ebeye. Ndugu na dada wa kutaniko la Ebeye humtumia barua za kumtia moyo, wakisimulia mambo yaliyoonwa katika utumishi wa shambani na mambo wanayojifunza mikutanoni. Nao hutiwa moyo na uaminifu wa dada huyo aliye peke yake kisiwani.

Vijiji vingi vya mbali nchini Papua New Guinea havina umeme. Watu hutumia jenereta au betri kuendesha vifaa vya umeme. Ili kuwasaidia wanakijiji wenzake kuielewa Biblia vizuri, dada mmoja aliyebatizwa karibuni alitaka kuwaonyesha video kadhaa za Mashahidi wa Yehova. Alipata pesa kwa kuuza mazao, kisha akamwendea mwanamke mmoja mfanyabiashara ili kukodi televisheni, mashine ya video, na jenereta. Dada yetu alimweleza kwamba alitaka kuwaalika wanakijiji wote watazame video kadhaa za Biblia ambazo alisadiki zingewasaidia kiroho. Mara moja mfanyabiashara huyo alipunguza kabisa bei ya kukodi vifaa hivyo, huku akisema kwamba yeye pia angependa kutazama video hizo. Karibu kila mtu kijijini alikuja. Baadaye, wengi walisema kwamba hawakujua kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imeenea sana hivyo. Walivutiwa pia na undugu wa ulimwenguni pote, jambo ambalo hawajawahi kuona katika kanisa lao. Watu wengi ambao hapo awali walikataa kuongea na Mashahidi walimwalika dada huyo nyumbani mwao kwa sababu walitaka kujua mengi zaidi kuhusu mafundisho yetu.

Huko Savaii, kisiwa kikubwa zaidi cha Samoa, viongozi fulani wa vijiji wamewapiga marufuku Mashahidi wa Yehova wasihubiri katika vijiji vyao. Dada mmoja anayeishi kwenye kijiji kimoja huko alishikilia kweli kwa uthabiti alipokuwa akipanga mazishi ya mwanaye. Kwa kuwa mazishi hayo yangefanywa nyumbani kwake, ndugu na dada kutoka makutaniko mawili yaliyo kisiwani walimsaidia kusafisha nyumba na ua na kutafuta jenereta. Wanakijiji waliona jinsi ndugu walivyomsaidia kwa upendo na jinsi walivyopanga na kufanya mazishi tofauti kabisa na desturi za Wasamoa.

Siku mbili baada ya mazishi, baraza la kijiji lilikutana ili kuzungumzia tukio hilo. Wanachama wote wa baraza walivutiwa na jinsi Mashahidi walivyoisaidia familia hiyo kabla na baada ya mazishi. Machifu wa kijiji hicho waliguswa moyo sana na mazishi hayo hivi kwamba wote walikubaliana kubadili desturi za mazishi ili zipatane na Faa-Molimau a Ieova (Njia ya Mashahidi wa Yehova). Siku mbili baadaye, Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Kristo ulifanywa katika Jumba dogo la Ufalme lililo mbali kidogo. Magari matatu ya mizigo yalipeleka familia kadhaa za kijiji hicho kwenye mwadhimisho huo. Sasa ndugu na dada zetu wanaweza kuhubiri kwa uhuru katika kijiji hicho, ambacho ni mojawapo ya vijiji vikubwa zaidi kisiwani. Mapainia wawili wa pekee huongoza mafunzo sita ya Biblia katika kisiwa hicho. Chifu mmoja wa kijiji anahudhuria Funzo la Kitabu la Kutaniko pamoja na wanakijiji wanaopendezwa.

Nchini Fiji, kijana mmoja alikuwa ameketi chini ya mti akiwaza kuhusu maisha yake na wakati ujao. Alimwomba mpita-njia mmoja aketi pamoja naye. Mpita-njia huyo alikuwa ndugu, hivyo alitumia nafasi hiyo kumhubiria. Ingawa tayari kijana huyo alikuwa amesikia ahadi ya Biblia ya kwamba dunia itakuwa paradiso, mazungumzo pamoja na ndugu huyo yaliamsha tena upendezi wake. Aliamua kurudi kisiwani ambako mama yake aliishi na akaanza kujifunza Biblia. Baada ya kuwasili huko, watu wa familia yao ambao walipinga imani yake mpya waliharibu mimea aliyokuwa amepanda. Kisha wasimamizi wa kijiji walimwamuru aondoke, na kusema kwamba hawataruhusu dini yoyote isipokuwa dini yao. Kwa hiyo alihamia kijiji cha baba yake katika kisiwa kingine kidogo. Akiwa huko, alitengeneza chombo kwa mabati yaliyochakaa, na kila juma alikitumia kusafiri kilometa kadhaa kwenye bahari yenye mchafuko ili akutane na Mashahidi. Familia iliendelea kumpinga, na hakuwa na la kufanya ila kuishi peke yake katika sehemu isiyo na watu kisiwani. Mwishowe, alifaulu kuhamia kisiwa kikuu, na kuishi karibu na kutaniko kubwa. Anafanya maendeleo ya kiroho akiwa mhubiri asiyebatizwa.

◼ AMERIKA

Idadi ya nchi: 56

Idadi ya watu: 857,137,983

Idadi ya wahubiri: 3,095,083

Idadi ya mafunzo ya Biblia: 2,898,369

Jumapili moja asubuhi, mnamo Septemba 2002, dada mmoja nchini Marekani alimrudia mwenye duka fulani. Mwenye duka alikuwa akiwahudumia wateja wakati huo, hivyo dada huyo alitembea-tembea dukani. Alimwona mwanamke mmoja akiingia haraka dukani kununua mala, shanga za Wahindu zinazofanana na rozari ya Wakatoliki. Mala ni shanga zenye rangi ya kahawia zinazotumiwa kurudia-rudia sala kwa miungu mingi ya Kihindu. Ilionekana kwamba mwanamke huyo anayeitwa Shwe, alipata mala aliyotaka. Dada yetu alimkaribia na kusema: “Tafadhali, nauliza, Je, mala hiyo imetengenezwa kwa mbao ya msandali?”

“Ndiyo! Nimekuwa nikimwomba mungu nipate mala nzuri, na leo nimeipata. Hebu inuse!”

“Ooh, ina harufu nzuri sana! Utaitumia kusali kwa mungu yupi?”

“Eeh, nyakati nyingine kwa Ganesa au Siva au Durga. Nitatumia mala hii kusali kwa miungu hiyo.”

“Hebu nikuulize, Je, umewahi kufikiria ni mungu yupi aliye mkuu?”

“Hilo linanitatanisha. Sijui ni mungu yupi aliye mkuu.”

“Jambo hilo lilinitatanisha pia nilipokuwa Mhindu na nilipoabudu miungu hiyo. Lakini sasa ninajua Mungu mweza-yote ni yupi. Hebu nikuonyeshe. [Asoma Zaburi 83:18.] Yehova Mungu ndiye Mweza-Yote juu ya dunia yote. Yeye ni mkuu kuliko Siva, Ganesa, na Durga. Ninaweza kukufundisha kumhusu Mungu mweza-yote bila malipo yoyote.”

“Je, kweli utanifundisha kumhusu Mungu wa kweli? Leo sala zangu zote zimejibiwa!”

“Zimejibiwaje?”

“Nimekuwa nikisali kila siku nipate mala nzuri ili niitumie kumtafuta Mungu wa kweli. Nilisali pia nipate rafiki wa kweli ambaye anaweza kunisaidia kwa sababu sina rafiki yeyote. Jina lako ni nani?”

“Jina langu ni Mala, ninaweza kuwa rafiki ambaye atakufundisha Biblia.”

“Siamini kwamba Mungu amenipa Mala hai!”

Wanawake hao wawili walipanga kujifunza broshua Anataka. Shwe anahudhuria mikutano kwa ukawaida na ana mradi wa kubatizwa.

Huko Honduras, dada mmoja mishonari ambaye alikuwa akijitahidi kujifunza Kihispania aliingia kwenye ofisi moja na kumwachia mpokea-wageni magazeti. Kisha simu ya ofisi ikalia, na dada huyo mishonari akaketi huku akifiri kwamba mpokea-wageni alimwomba aketi. Kumbe hakumwelewa. Mpokea-wageni alikuwa amemwambia aondoke. Wakati huohuo, mwanamke mwingine katika ofisi jirani alikuwa akisali ili apate msaada wa kuvunja uhusiano usio wa kimaadili na mwanamume aliyeoa na alitaka pia kujua njia inayofaa ya kumwabudu Mungu. Alipomsikia dada akiongea na mpokea-wageni, aliamini kwamba sala yake imejibiwa. Hata hivyo, alipomsikia yule mpokea-wageni akimwambia dada aondoke, alikuwa na wasiwasi kwamba huenda mishonari huyo angeondoka kabla hajazungumza naye. Lakini, mishonari huyo alisema hivi baadaye: “Kwa sababu ya kutomwelewa mpokea-wageni, bado nilikuwa ofisini humo mwanamke huyo alipoingia haraka ili kuzungumza nami. Sote wawili tunasadiki kwamba ni Yehova aliyefanya tukutane.” Miaka kadhaa iliyopita, mwanamke huyo alikuwa amesoma vichapo vya Mashahidi wa Yehova, na sasa aliamua kuchukua mambo ya kiroho kwa uzito. Tayari amevunja uhusiano wake na yule mwanamume aliyeoa na anajifunza Biblia na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida.

Dada mmoja ambaye ni painia wa pekee huko El Salvador alitumwa kwenye kutaniko linalohubiri eneo ambalo lina watu wengi wasiopendezwa na kweli. Alimwomba Yehova amsaidie kuwapata watu wanaopendezwa. Jumapili moja alikutana na kijana mmoja na akazungumza naye kuhusu Biblia. Kijana huyo alichukua kitabu Ujuzi na akakubali dada huyo amtembelee tena. Dada huyo alirudi mara nyingi lakini hakumpata nyumbani. Hata hivyo, alikutana na mke wake ambaye hakupendezwa sana na Biblia. Katika ziara ya tano, mke alimkaribisha dada huyo nyumbani, ingawa alisema, “ni kwa dakika kumi tu.” Dada alimuuliza kama kitabu Ujuzi kilikuwa karibu. Mwanamke huyo alikileta, na dada akazungumzia kwa ufupi mambo machache kutoka kwenye kitabu hicho na akamwonyesha mpango wa kujifunza Biblia. Baada ya kujifunza kwa miezi mitatu, mwanamke huyo alianza kuhudhuria mikutano na akaanza kufanya maendeleo. Vipi mume wake? Baada ya muda, alianza kushiriki katika funzo hilo. Kisha akaanza kuhudhuria mikutano pamoja na familia yake. Sasa wanapanga kuhalalisha ndoa yao. Dada alipata matokeo mazuri kwa sababu ya bidii yake pamoja na sala.

Margarita, anayeishi Mexico, anaeleza matokeo aliyopata alipomhubiria mwanafunzi mwenzake: “Kwenye shule ya kujifunza kushona, nilizungumza na mwanafunzi mwenzangu kuhusu Biblia. Alisema kwamba yeye huziona familia za Mashahidi wa Yehova zikiwa na furaha, kwa sababu sikuzote wanatabasamu na huonekana wakiwa wachangamfu sana. Nilimwambia hakukosea na kwamba wale wanaomtumaini Yehova na kufuata kanuni za Biblia hupata furaha ya kweli.” Margarita alianza kujifunza Biblia na mwanafunzi huyo ambaye sasa anahudhuria mikutano kwa ukawaida na anaendelea kujifunza kweli.

Katika Jamhuri ya Dominika, Ana alimwachia mwanamume mmoja aliyekuwa na wasiwasi broshua Anataka. Mke wake alikuwa amelazwa hospitalini ili afanyiwe upasuaji kwa sababu ya kansa. Alisema kwamba mke wake anapenda kusoma, kwa hiyo angempelekea broshua hiyo hospitalini. Baadaye Ana alikutana na mke wa mwanamume huyo. Mke huyo alisema hivi: “Tunaweza kuanza kujifunza. Niko tayari.” Baadaye alimweleza kwamba alipokuwa hospitalini, alimsihi Mungu amsaidie kupata dini ya kweli. Wakati huohuo, mume wake alimletea broshua Anataka. Aliisoma, akatambua kwamba Mungu amejibu sala yake, na mara moja akajiwekea mradi wa kuwa Shahidi wa Yehova. Ingawa alihitaji kutembea kwa muda wa saa moja ili kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme, alifanya maendeleo ya haraka na punde si punde akastahili kuwa mhubiri. Alisema hivi: “Sasa ninaweza kutimiza nadhiri yangu kwa Mungu.” Katika muda usiozidi miezi sita, alibatizwa kwenye kusanyiko la wilaya, na sasa anaendelea kumtumikia Yehova kwa shangwe.

Martin, mhubiri mwenye umri wa miaka 13 ambaye anaishi Paraguai, hufurahia mahubiri yasiyo rasmi. Siku moja alipokuwa akielekea nyumbani kutoka shuleni huku akimhubiria mtu fulani, aliona kifurushi barabarani. Martin alikiokota na akagundua kwamba kilikuwa na pesa. Alikiweka mfukoni kwa sababu hakumwona yeyote akikitafuta. Alipokuwa akitembea, alijiambia: ‘Ninaweza kutumia pesa hizi kulipa karo ya shule kwa miezi mitatu ambayo ninadaiwa na pia kulipa gharama fulani za wazazi wangu.’ Bila kutarajia, aligeuka na kupitia barabara ambayo kwa kawaida huwa hapitii. Mara alimwona mtu ambaye alikuwa akitafuta kitu fulani. Alimsikia akisema kwamba alikuwa amepoteza guarani 115,000 (dola 18.25 za Marekani) na kwamba hizo ndizo pesa tu alizobaki nazo kwa ajili ya mahitaji yake ya mwezi huo. Mara moja Martin alikumbuka maneno ya mzee mmoja aliyemuuliza maswali ya ubatizo. Mzee huyo alisema: “Utakumbana na majaribu mengi, na hasa wakati huu unapokaribia kubatizwa.”

Martin alihitaji sana pesa hizo. Siku hiyo hata hakuwa na pesa za kutosha kununua chakula, sembuse pesa za kulipa karo ya shule. Hata hivyo, akiwa na uhakika kwamba alikuwa akifanya jambo linalofaa, Martin alimuuliza mtu huyo kiasi cha pesa alizopoteza. Kiasi hicho kilikuwa sawa kabisa na kile ambacho Martin aliokota. Martin alimpa pesa hizo pamoja na trakti na kumwambia kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova. Mtu huyo alifurahi sana na kumshukuru Martin tena na tena na kumkumbatia. Mtu huyo alimpa Martin anwani yake ili amtembelee. Martin alibatizwa pamoja na wazazi wake kwenye kusanyiko la mzunguko hivi majuzi.

◼ ASIA NA MASHARIKI YA KATI

Idadi ya nchi: 47

Idadi ya watu: 3,931,574,927

Idadi ya wahubiri: 568,370

Idadi ya mafunzo ya Biblia: 417,308

Kumiko, dada painia anayeishi karibu na Tokyo huko Japani, hakuweza kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa sababu ya matatizo ya afya. Kwa hiyo, alitumia wakati mwingi kuhubiri kwa njia ya barua. Wahubiri wa kutaniko lao walimpa anwani za watu wasiopatikana nyumbani kwa urahisi. Aliandika barua, na wahubiri wa kutaniko walizipeleka kwenye nyumba za watu hao. Kwa zaidi ya mwaka mmoja, hakupokea majibu yoyote. Lakini bado aliendelea kuandika bila kuacha. Hatimaye, baada ya kuandika barua 1,500 hivi, alipokea kadi iliyosema: “Asante kwa barua yako. Ninapendezwa mno na mambo uliyotaja. Ninapatikana siku zifuatazo, na nitangoja uwasiliane nami.” Alimtembelea mtu huyo huku machozi ya furaha yakimtiririka, akaanzisha funzo la Biblia mara moja. Dada huyo anasema hivi: “Mwanzoni, niliogopa kuandika barua, lakini sasa nina hakika kwamba tukiwatafuta watu wenye mfano wa kondoo kwa subira, bila shaka Yehova atabariki jitihada zetu.”

Asubuhi moja, dada alibisha mlango alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba huko India. Mwanamke mwenye huzuni alifungua mlango. Watoto wawili wadogo walikuwa wameketi sakafuni wakiwa na sahani tupu mbele yao. Dada yetu alimweleza ujumbe wenye kufariji wa Ufalme wa Mungu na baraka utakazoleta, na mwanamke huyo alisikiliza kwa makini sana. Wakati huo, watoto wake wenye njaa waliendelea kumsihi mama awapakulie chakula. Mama alikataa. Dada huyo alisema kwamba anaweza kungoja hadi watoto wale chakula. Mwanamke huyo alianza kulia, na kusema kwamba chakula hicho kilikuwa na sumu. Alitaka kuwapakulia watoto chakula hicho aliposikia mlango ukibishwa. Alikuwa ameamua kujiua na kuwaua binti zake wawili wadogo kwa sababu mume wake alikuwa mlevi na walikuwa na matatizo ya familia. Aliposikia hivyo, dada huyo alitupa chakula hicho, akakimbia kwenye duka la karibu na kununulia familia hiyo chakula. Walipika chakula hicho pamoja na kuwapa watoto. Ujumbe wa Ufalme ulimfariji sana mwanamke huyo. Alikubali funzo la Biblia, na sasa ni Shahidi aliyebatizwa. Watoto wake wawili huandamana naye mikutanoni. Hivi karibuni, mume wake alianza kuhudhuria mikutano na anafanya maendeleo mazuri.

SARS! Neno hilo liliwatia woga watu wengi nchini Taiwan. Kwa wasiwasi, wakazi walitazama ripoti kuhusu athari za ugonjwa huo nchini Hong Kong. Kisha ukafika Taiwan! Hospitali kadhaa zilitengwa kwa sababu ya ugonjwa huo, na watu wengi waliogopa kwamba huenda wakaambukizwa. Hata kabla serikali haijatoa maagizo, ofisi ya tawi iliyasaidia makutaniko kununua vipima-joto ili akina ndugu wampime kila mtu anayehudhuria mikutano.

Serikali iliomba dini zote zilizosajiliwa ziepuke kuhubiri katika maeneo fulani ya makazi. Mkutano wa pekee wa Utumishi uliwasaidia akina ndugu kufanya marekebisho katika utendaji wao ili kuepuka matatizo. Painia mmoja wa pekee alifuata dokezo la kuwarudia hata watu waliopendezwa kidogo tu. Kwa kufanya hivyo, alipata mafunzo mengi ya Biblia. Baadhi ya wanafunzi hao wapya wanafanya maendeleo mazuri. Alisema hivi: “Hali mbaya ilinisaidia kuwa na matokeo mazuri zaidi katika huduma.”

Alipokuwa katika utumishi wa shambani huko Cyprus, dada mmoja alikutana na mwanamke aliyesema kwamba ana shughuli. Dada huyo alizungumza naye kwa ufupi kupitia dirisha la jikoni lililokuwa wazi, akasoma Zaburi 72:12-14, akapanga kurudi tena wakati unaofaa. Dada aliporudi, alishangaa mwanamke huyo alipomwambia kwamba alikuwa akimngoja kwa hamu. Kwa nini? Andiko hilo lilimfariji sana mwanamke huyo na alikuwa amelifikiria siku yote. Dada alijitolea kujifunza Biblia pamoja na mwanamke huyo, naye akakubali. Sasa mwanamke huyo anathamini sana yale anayojifunza katika Neno la Mungu.

Polo, ambaye anaishi Kambodia, alianza kujifunza na mishonari fulani na alifanya maendeleo mazuri. Alikuwa akihudhuria mikutano yote mitano huko Phnom Penh. Kisha mwajiri wake alimwambia ahamie jiji la Battambang lililo karibu na mpaka wa Thailand. Hakuna kutaniko huko, kwa hiyo Polo alimpa mwalimu wake wa Biblia nambari yake ya simu ya mkononi, na wakaendelea kujifunza kupitia simu kwa dakika 30 kila Jumatano na Ijumaa. Polo alitaka pia kutoa maelezo kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi. Kwa sababu kutaniko lilikuwa mbali, aliandika majibu matatu au manne na kumwachia mwangalizi wao wa Funzo la Kitabu la Kutaniko ili yasomwe kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi juma hilo. Bidii yake imewatia moyo wahubiri wa kutaniko. Yeye hujaribu pia kuwahubiria wale anaokutana nao. Anaposafiri kwa basi kwenda na kutoka Phnom Penh, yeye huwahubiria watu wengi na kuwatia moyo wahudhurie mikutano. Mradi wake sasa ni kuwa mhubiri asiyebatizwa.

Huko Mongolia, dada wawili walikutana na mwanamume mwenye umri wa miaka 30 hivi. Aliwaambia wangoje, akaingia nyumbani na kuleta vitabu viwili: Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu na Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi. Alisema kwamba alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova huko Poland miaka 12 iliyopita. Aliporudi Mongolia mnamo mwaka wa 1993, mara moja aliwaandikia Mashahidi barua akiwaomba wamtembelee. Hata hivyo, wakati huo hakukuwa na Mashahidi nchini Mongolia, kwa hiyo hakutembelewa. Baadaye, alijiunga na chuo kikuu nchini India, ambako aliishi kwa miaka mitano. Katika miaka hiyo, kuanzia 1994 hadi 1998, hakukutana na Mashahidi wa Yehova. Kisha alirudi Mongolia, ambako hatimaye alikutana na akina ndugu. Alianza tena kujifunza Biblia na mnamo Aprili 2003, alihudhuria mkutano wake wa kwanza. Sasa anafurahia kujifunza broshua Anataka.

Mwanamke mmoja Mbudha huko Sri Lanka aliwashangaza Mashahidi wawili alipowakaribisha kwa uchangamfu nyumbani mwake, huku akisema kwamba sala yake imejibiwa! Alieleza kwamba binti yake mdogo alijiua hivi majuzi kwa sababu alimtia nidhamu. Alipoenda kumwona kuhani Mbudha ili apate faraja, kuhani huyo alimwambia kwamba binti yake angezaliwa upya na kurudi kulipiza kisasi. Jambo hilo lilimwogopesha sana. Rafiki yake mmoja alimwambia kwamba Wakristo hawaamini mambo hayo. Kwa hiyo mwanamke huyo alimwomba Mungu ili akutane na Mkristo wa kweli, huku akifikiri kwamba huenda Mkatoliki ndiye angetumwa. Badala yake, Mashahidi wawili wa Yehova walimtembelea na kumfariji kwa kumweleza kweli ya Biblia. Sasa anajifunza Biblia ajapopingwa na yule kuhani Mbudha.

Huko Kyrgyzstan, mwanamke mmoja kijana alikuwa mfuasi wa kanisa la Kiinjilisti kwa miaka mingi. Aliposoma Biblia, aliona kwamba kuna tofauti kati ya mambo anayofundishwa kanisani na yale yaliyo katika Biblia. Kwa mfano, hakuelewa fundisho la kanisa la kwamba Yesu Kristo ni Baba na pia ni Mwana. Huku akiamini kwamba lazima mwana awe na baba, alisali kutoka moyoni kwa Baba ya Yesu Kristo, akimwomba amsaidie kupata majibu ya maswali yake ya Biblia. Siku iliyofuata, Mashahidi wawili wa Yehova walimtembelea. Walimuuliza: “Unaonaje? Yesu Kristo aliwafundisha wanafunzi wake wasali kwa nani, na aliwahimiza watakase jina gani?” Alishangaa sana alipokumbuka kwamba siku iliyotangulia alikuwa amemwomba Baba ya Yesu Kristo ajibu maswali hayohayo. Baada ya mazungumzo, hakuwa na shaka yoyote kwamba Mungu alikuwa amejibu sala yake. Mwanamke huyo alikubali kujifunza Biblia kwa ukawaida na akaanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Alipojifunza kwamba Yehova ndiye Baba ya Yesu, alianza kusali kwa Yehova akitumia jina lake. Sasa anafanya maendeleo ya kiroho naye huwaeleza watu wake wa ukoo ujuzi ambao amepata.

◼ AFRIKA

Idadi ya nchi: 56

Idadi ya watu: 755,145,559

Idadi ya wahubiri: 950,321

Idadi ya mafunzo ya Biblia: 1,666,518

Kwenye mabasi mengi nchini Zambia, abiria hutumbuizwa kwa video ambazo mara nyingi huonyesha jeuri na ukosefu wa adili. Wenzi wawili mishonari waliokuwa kwenye basi moja lililokuwa likielekea jiji kuu waliuliza ikiwa video fulani inayozungumzia jinsi Biblia inavyoweza kubadili maisha ya mtu (The Bible—Its Power in Your Life) ingeweza kuonyeshwa. Dereva alikubali. “Tuliona kwamba abiria waliitazama kwa uangalifu na kusikiliza kwa makini,” akasema Ruth. “Baadaye, tulizungumza nao na kuwapa trakti na magazeti. Walifurahi sana.” Wenzi hao walimuuliza dereva ikiwa angeirudia video hiyo, wakifikiri kwamba angefanya hivyo baadaye. Papo hapo aliionyesha tena video hiyo. Richard alisema hivi: “Abiria walifurahia video hiyo kwa mara ya pili, nasi tulifurahi kwamba tulimwomba dereva aonyeshe video hiyo.”

Miranda, ambaye ni mwanafunzi nchini Malawi, alikuwa akimwonyesha mwanafunzi mwenzake kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia wakati wa mapumziko shuleni. Mwalimu alisikia mazungumzo yao na akamwita Miranda ofisini mwake. Alimuuliza ni kwa nini alimwambia rafiki yake aolewe. Miranda akamjibu kwamba hakumwambia rafiki yake aolewe bali alikuwa akimweleza jinsi kitabu hicho kinavyoweza kusaidia familia zipate furaha ya kweli. Mwalimu alimfokea Miranda kwa hasira: “Wewe ni mchanga mno kutoa mashauri kuhusu ndoa!”

Miranda aliondoka ofisini akiwa amehuzunika na akitetemeka. Siku mbili baadaye mwalimu alimwita tena ofisini. Miranda anaeleza kilichotukia: “Mwalimu huyo aliniomba radhi kwa sababu ya kunifokea kwa hasira, na akaniambia kwamba yeye na mke wake waligombana daima na mwishowe wakatengana. Aliniomba nakala ya kitabu nilichomwonyesha mwanafunzi mwenzangu. Nilifurahi kumpa kitabu hicho. Majuma mawili baadaye aliniambia kwamba kitabu hicho kilimsaidia sana na alikuwa amemwonyesha mke wake. Hatimaye, yeye na mke wake walirudiana.”

Huko Afrika Kusini, mtu mmoja mzee anayeitwa Eric, alikuwa amejifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova kwa miaka mingi, lakini hakufanya maendeleo ya kiroho kwa sababu ya zoea la kuvuta sigara. Baada ya mke wake kubatizwa, aliamua kujiwekea mradi huo pia. Alitengeneza nakala kadhaa kubwa za Andiko la 2 Wakorintho 7:1, linalosema hivi: “Wapendwa, kwa kuwa tuna ahadi hizi, acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.” Eric aliweka nakala hizo sehemu mbalimbali nyumbani mwake ambapo zingeonekana wazi. Kila mara alipotamani kuvuta sigara, alisoma andiko hilo na kumwomba Yehova amsaidie kuacha kuvuta sigara. Tokeo ni kwamba ameacha kuvuta sigara kwa zaidi ya miezi kumi. Hivi sasa Eric ni mhubiri asiyebatizwa na anapanga kubatizwa kwenye kusanyiko la wilaya linalokuja.

Alipokuwa akingoja feri kwenye visiwa vya Shelisheli, dada mmoja mishonari alimwona mwanamke aliyekuwa ameketi peke yake. Ingawa dada huyo alikuwa amechoka baada ya kuhubiri siku nzima, alimkaribia mwanamke huyo na kumpa trakti. Aliikubali na kusema kwamba yeye ni Mhindu. Siku chache baadaye, walikutana tena barabarani na dada akapanga kujifunza Biblia pamoja naye. Mume wa mwanamke huyo ambaye alikuwa Mkatoliki na daktari, alikubali kushiriki katika funzo baada ya kusoma kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu na kitabu Ujuzi. Jioni moja, wenzi hao wa ndoa walimkaribisha dada huyo pamoja na mumewe kula nyama choma. Wenzi hao waliteketeza sanamu zao za kidini na kuchoma nyama juu ya moto huo! Muda si muda walianza kuhudhuria mikutano na kushiriki katika utumishi wa shambani. Baada ya kubatizwa, wote wawili walianza kufanya upainia msaidizi. Ndugu huyo anajulikana sana kwa sababu kisiwa hicho ni kidogo. Baadhi ya watu husema hivi kwa ucheshi: “Sasa daktari amekuwa kasisi.” Sasa yeye anatumikia akiwa mtumishi wa huduma, na mke wake anafurahia utumishi wa painia wa kawaida.

Ishmael alijifunza lugha ya ishara ili awasaidie viziwi kujifunza kweli huko Zimbabwe. Siku moja alipokuwa akisafiri kwa basi, alimwona mwanamke mmoja kiziwi akiwaomba abiria pesa. Ishmael alimhubiria, akapanga kukutana naye tena. Mwanamke huyo alipoulizwa kanisa lake hufundisha nini kuhusu hali yake ya kuwa kiziwi, alijibu: “Wanasema ni mapenzi ya Mungu niwe kiziwi.” Ishmael alimweleza kwamba si mapenzi ya Mungu watu wawe viziwi lakini hali kama hizo husababishwa na kutokamilika na dhambi tuliyorithi. Pia alimweleza kwamba hivi karibuni Mungu ataondoa magonjwa yote. Mwanamke huyo akamjibu hivi: “Ningependa kujua kwa nini kanisa langu lilinifundisha uwongo.” Ishmael alipokutana naye mara ya tatu, mwanamke huyo alisema: “Kuanzia sasa mimi ni mmoja wenu. Sitaki kusikiliza uwongo tena.” Anajifunza Biblia na amekuwa akihudhuria mikutano kwa ukawaida na anatarajia kuwa mhubiri asiyebatizwa hivi karibuni.

Huko Ghana, watu wengi hawapati wakati wa kufikiria mambo ya kiroho kwa sababu ya hekaheka za kutafuta riziki. Alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, dada mmoja ambaye ni painia wa kawaida alimpata kijana fulani, akamuuliza kama wanaweza kuzungumzia Biblia kwa dakika tano tu. Mwanamume huyo alimjibu hivi: “Kwa kawaida mimi huwa na shughuli nyingi sana wakati wa mchana. Ninarudi nyumbani baada ya saa mbili usiku ili kulala.”

Dada alimuuliza: “Je, unaweza kujifunza Biblia kwa dakika chache tu kabla ya kulala?”

Akamwambia: “Itawezekana ukija tu baada ya saa mbili usiku.” Siku iliyofuata, dada huyo na mumewe walimtembelea mwanamume huyo saa mbili kamili usiku. Alikuwa ameingia tu kutoka kazini. Alianza kujifunza Biblia na punde si punde akaanza kuhudhuria mikutano. Baadaye alistahili kuwa mhubiri asiyebatizwa na mwishowe akabatizwa. Mabadiliko aliyofanya maishani yalimvutia sana mkewe hivi kwamba alikubali kujifunza Biblia na baada ya muda akastahili kuwa mhubiri asiyebatizwa. Majirani na watu wengi waliojua maisha ya awali ya kijana huyo hawakuamini macho yao walipomwona akihubiri nyumba kwa nyumba. Wengi wao walitaka kujua kilichombadili mtu huyo aliyekuwa mlevi, mwizi, na mtumiaji wa dawa za kulevya. Tokeo ni kwamba watu 22 katika mji huo waliomba kujifunza Biblia. Tayari watu 12 kati yao wanahudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida na huenda wakastahili kuwa wahubiri wasiobatizwa hivi karibuni.

[Picha katika ukurasa wa 43]

Steponas na Edvardas, Lithuania

[Picha katika ukurasa wa 47]

Alyce akiwa na mwalimu wake, Linda, huko Australia

[Picha katika ukurasa wa 51]

Mala, Marekani

[Picha katika ukurasa wa 56]

Kumiko, Japani

[Picha katika ukurasa wa 61]

Ruth na Richard, Zambia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki