Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Fundisho la Ufufuo Linakuhusu
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Mei 1
    • 1. Ufufuo ulipataje kuwa suala la kujadiliwa mbele ya Sanhedrini?

      MTUME Paulo alikuwa Yerusalemu mwishoni mwa safari yake ya tatu ya umishonari mwaka wa 56 W.K. Baada ya kukamatwa na Waroma, aliruhusiwa kwenda mbele ya Sanhedrini, mahakama kuu ya Wayahudi. (Matendo 22:29, 30) Paulo alipowatazama washiriki wa mahakama hiyo, aliona Masadukayo na Mafarisayo. Kulikuwa na tofauti moja kubwa sana kati ya vikundi hivyo viwili. Mafarisayo waliamini kuna ufufuo, nao Masadukayo walisema hakuna ufufuo. Ili kuonyesha msimamo wake kuhusu suala hilo, Paulo alisema: “Wanaume, akina ndugu, mimi ni Farisayo, mwana wa Mafarisayo. Ninahukumiwa juu ya tumaini la ufufuo wa wafu.” Maneno hayo ya Paulo yalisababisha mvurugo katika mahakama hiyo!—Matendo 23:6-9.

      2. Kwa nini Paulo alikuwa tayari kutetea imani yake kuhusu ufufuo?

      2 Miaka kadhaa awali, alipokuwa njiani kwenda Damasko, Paulo aliona maono na kusikia sauti ya Yesu. Paulo hata alimuuliza Yesu: “Nitafanya nini, Bwana?” Yesu akamjibu: “Simama, ondoka uende Damasko, na huko utaambiwa kila kitu ambacho umewekewa kufanya.” Paulo alipofika Damasko, Anania, mwanafunzi Mkristo mwenye kujali, alimtafuta Paulo na kumweleza hivi: “Mungu wa mababu zetu amekuchagua upate kujua mapenzi yake na kumwona yule Aliye mwadilifu [Yesu aliyefufuliwa] na kuisikia sauti ya kinywa chake.” (Matendo 22:6-16) Basi, haishangazi kwamba Paulo alikuwa tayari kutetea imani yake kuhusu ufufuo.—1 Petro 3:15.

      Atangaza Waziwazi Tumaini la Ufufuo

      3, 4. Paulo aliliteteaje fundisho la ufufuo kwa uthabiti, na mfano wake unaweza kutufunza nini?

      3 Baadaye, Paulo alipelekwa mbele ya Gavana Feliksi. Pindi hiyo, Tertulo, “msemaji wa hadharani” aliyewasilisha kesi ya Wayahudi dhidi ya Paulo, alimshtaki kuwa mchochezi wa uasi na kiongozi wa madhehebu fulani. Kwa kujibu, Paulo alitangaza hivi waziwazi: “Ninakiri jambo hili kwako, kwamba, kulingana na ile njia wanayoiita ‘madhehebu,’ kwa namna hii mimi ninatoa utumishi mtakatifu kwa Mungu wa mababu zangu.” Kisha akaeleza suala kuu lililohusika kwa kusema: “Nina tumaini kwa Mungu, tumaini ambalo watu hawa pia wanalo, kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 23:23, 24; 24:1-8, 14, 15.

      4 Miaka miwili hivi baadaye, Porkio Festo, aliyekuwa Gavana baada ya Feliksi, alimwalika Mfalme Herode Agripa ajiunge naye kumhoji Paulo, aliyekuwa mfungwa. Festo alieleza kwamba wale waliomshtaki Paulo walikataa dai lake kwamba “mtu fulani anayeitwa Yesu aliyekuwa amekufa . . . alikuwa hai.” Paulo alijitetea kwa kuuliza hivi: “Kwa nini mnaamua kwamba ni jambo lisiloaminika kwamba Mungu hufufua wafu?” Kisha akasema: “Kwa sababu nimeupata msaada kutoka kwa Mungu ninaendelea mpaka leo kutoa ushahidi kwa wadogo na wakubwa pia, lakini bila kusema lolote ila mambo ambayo Manabii na vilevile Musa walisema yatatukia, kwamba Kristo angeteseka na, akiwa wa kwanza kufufuliwa kutoka kwa wafu, angetangaza nuru kwa watu hawa na pia kwa mataifa.” (Matendo 24:27; 25:13-22; 26:8, 22, 23) Paulo alikuwa mteteaji thabiti sana wa tumaini la ufufuo. Kama Paulo, sisi pia tunaweza kutangaza kwa uhakika kwamba kutakuwa na ufufuo. Lakini tunaweza kutazamia watu waitikieje? Yaelekea itikio litakuwa sawa na lile ambalo Paulo alipata.

      5, 6. (a) Watu waliitikiaje mitume walipotetea tumaini la ufufuo? (b) Tunapoendelea kuwaeleza watu kuhusu tumaini letu katika ufufuo, ni jambo gani lililo muhimu?

      5 Fikiria mambo yaliyotukia mapema katika safari ya pili ya Paulo ya umishonari (yapata mwaka wa 49-52 W.K.) alipotembelea jiji la Athene. Alijadiliana na watu walioamini katika miungu mingi na kuwahimiza wafikirie kusudi la Mungu la kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia mwanamume ambaye Amemweka rasmi. Mwanamume huyo ni Yesu. Paulo alieleza kwamba Mungu alitoa uhakikisho wa jambo hilo kwa kumfufua Yesu. Watu waliitikiaje? Tunasoma hivi: “Basi, waliposikia juu ya ufufuo wa wafu, wengine kati yao wakaanza kudhihaki, huku wengine wakisema: ‘Tutakusikiliza tena juu ya jambo hili wakati mwingine.’”—Matendo 17:29-32.

  • Fundisho la Ufufuo Linakuhusu
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Mei 1
    • Imani na Ufufuo

      7, 8. (a) Kama inavyoonyeshwa katika barua iliyoandikiwa kutaniko la Korintho katika karne ya kwanza, imani inawezaje kuwa bure? (b) Kulielewa tumaini la ufufuo kwa usahihi hutofautishaje Wakristo wa kweli na wa uwongo?

      7 Si Wakristo wote katika karne ya kwanza W.K. waliokubali kwa urahisi tumaini la ufufuo. Baadhi ya Wakristo hao walikuwa katika kutaniko la Korintho. Paulo aliwaandikia hivi: “Niliwapa ninyi, kati ya mambo ya kwanza, yale niliyopokea pia, kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba alifufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko.” Kisha Paulo akathibitisha jambo hilo kwa kusema kwamba Kristo aliyefufuliwa “aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano,” naye akaongeza kwamba wengi wao bado walikuwa hai. (1 Wakorintho 15:3-8) Paulo pia alitoa hoja hii: “Ikiwa Kristo anahubiriwa kwamba amefufuliwa kutoka kwa wafu, kwa nini wengine kati yenu wanasema hakuna ufufuo wa wafu? Ikiwa, kwa kweli, hakuna ufufuo wa wafu, basi Kristo hakufufuliwa. Lakini ikiwa Kristo hakufufuliwa, hakika kuhubiri kwetu ni bure, na imani yetu ni bure.”—1 Wakorintho 15:12-14.

      8 Kwa kweli, fundisho la ufufuo ni muhimu sana hivi kwamba imani ya Kikristo ni bure ikiwa ufufuo haukubaliwi kuwa jambo halisi. Naam, kuuelewa ufufuo kwa usahihi hutofautisha Wakristo wa kweli na wa uwongo. (Mwanzo 3:4; Ezekieli 18:4) Kwa hiyo, Paulo anataja ufufuo kuwa sehemu ya “fundisho la msingi” la Ukristo. Na tuazimie ‘kusonga mbele kuelekea ukomavu.’ Paulo anatuhimiza hivi: “Na hili tutalifanya, ikiwa kwa kweli Mungu ataruhusu.”—Waebrania 6:1-3.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki