Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Wafu Watafufuliwa”
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
    • 5. Wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza walitolewa tumaini gani?

      5 Si Yesu pekee ambaye angefufuliwa kwenye uhai wa kimbingu. Paulo aliwaambia Wakristo wenzake katika Roma kwamba walikuwa wametiwa mafuta kwa roho wawe wana wa Mungu na warithi-washirika pamoja na Kristo ikiwa wangethibitisha kutiwa mafuta kwao kwa kuvumilia mpaka mwisho. (Waroma 8:16, 17) Paulo pia alieleza hivi: “Ikiwa tumekuwa wenye kuungana pamoja naye katika ufanani wa kifo chake, hakika sisi pia tutaunganishwa pamoja naye katika ufanani wa ufufuo wake.”—Waroma 6:5.

      Kutetea Tumaini la Ufufuo

      6. Kwa nini imani katika ufufuo ilishambuliwa katika Korintho, na mtume Paulo aliitikiaje?

      6 Ufufuo ni sehemu ya “fundisho la msingi” la Ukristo. (Waebrania 6:1, 2) Hata hivyo, fundisho hilo lilikuwa likishambuliwa huko Korintho. Watu fulani katika kutaniko, waliokuwa kwa wazi wameathiriwa na falsafa za Kigiriki, walikuwa wakisema hivi: “Hakuna ufufuo wa wafu.” (1 Wakorintho 15:12) Wakati ripoti za usemi huo zilipomfikia mtume Paulo, alitetea tumaini la ufufuo, hasa tumaini la Wakristo watiwa-mafuta. Acheni tuchunguze maneno ya Paulo kama yalivyorekodiwa katika 1 Wakorintho sura ya 15. Litakuwa jambo lenye kusaidia ukiwa umesoma hiyo sura yote, kama ambavyo ilipendekezwa katika makala iliyotangulia.

      7. (a) Ni suala gani kuu ambalo Paulo alikazia? (b) Ni nani waliomwona Yesu aliyekuwa amefufuliwa?

      7 Katika mistari ya kwanza miwili ya 1 Wakorintho sura ya 15, Paulo ataja kichwa cha mazungumzo yake: “Nawajulisha nyinyi, akina ndugu, habari njema niliyowatangazia, mliyoipokea pia, ambayo katika hiyo mwasimama pia, ambayo kupitia hiyo nyinyi pia mnaokolewa, . . . isipokuwa, kwa kweli, mwe mlipata kuwa waamini bila kusudi lolote.” Wakorintho walikuwa wameipokea kweli bure, ikiwa walishindwa kusimama imara katika habari njema. Paulo aliendelea kusema hivi: “Niliwapa nyinyi, miongoni mwa mambo ya kwanza, lile nililolipokea pia, kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba amefufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko; na kwamba alionekana kwa Kefa, kisha kwa wale kumi na wawili. Baada ya hilo alionekana kwa zaidi ya ndugu mia tano kwa wakati mmoja, ambao walio wengi kati yao wabaki hadi wakati wa sasa, lakini baadhi yao wamelala usingizi katika kifo. Baada ya hilo alionekana kwa Yakobo, kisha kwa mitume wote; lakini mwisho wa wote alionekana pia kwangu kama kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati wake.”—1 Wakorintho 15:3-8.

      8, 9. (a) Itikadi katika ufufuo ni ya maana kadiri gani? (b) Yaelekea ni wakati gani Yesu alionekana kwa “zaidi ya ndugu mia tano”?

      8 Kwa waliokuwa wamepokea habari njema, imani katika ufufuo wa Yesu halikuwa jambo la kuchagua. Kulikuwa na mashahidi wengi waliojionea kwa macho waliothibitisha kwamba “Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu” na kwamba alikuwa amefufuliwa. Mmoja wao alikuwa Kefa, au Petro, jina linalojulikana zaidi. Baada ya Petro kumkataa Yesu usiku wa kusalitiwa na kukamatwa kwa Yesu, lazima awe alifarijiwa sana kumwona Yesu. Pia Yesu aliyekuwa amefufuliwa aliwatembelea “wale kumi na wawili,” yaani wale mitume wakiwa kikundi—jambo lililoonwa ambalo bila shaka liliwasaidia kushinda hofu yao na kuwa mashahidi wajasiri wa ufufuo wa Yesu.—Yohana 20:19-23; Matendo 2:32.

      9 Kristo pia alionekana kwa kikundi kikubwa zaidi, “ndugu zaidi ya mia tano.” Kwa kuwa ni katika Galilaya tu alikokuwa na idadi kubwa hivyo ya wafuasi, huenda huo ukawa ni ule wakati ambao umeelezwa kwenye Mathayo 28:16-20, Yesu alipotoa amri ya kufanya wanafunzi. Hao watu wangeweza kutoa ushuhuda wenye nguvu kama nini! Baadhi yao walikuwa bado hai mwaka wa 55 W.K. wakati Paulo alipotunga barua yake ya kwanza kwa Wakorintho. Ingawa hivyo, ona kwamba wale waliokuwa wamekufa walitajwa kuwa “wamelala usingizi katika kifo.” Walikuwa bado hawajafufuliwa ili kupokea thawabu yao ya kimbingu.

      10. (a) Mkutano wa mwisho wa Yesu pamoja na wanafunzi wake ulikuwa na matokeo gani? (b) Yesu alionekanaje kwa Paulo “kama kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati”?

      10 Shahidi mwingine mwenye kutokeza wa ufufuo wa Yesu alikuwa Yakobo, mwana wa Yosefu na Maria, mama yake Yesu. Kabla ya huo ufufuo ni wazi kwamba Yakobo hakuwa amekuwa mwamini. (Yohana 7:5) Lakini baada ya Yesu kuonekana kwake, Yakobo akawa mwamini na labda akatimiza fungu fulani katika kugeuza imani ya ndugu zake. (Matendo 1:13, 14) Katika mkutano wake wa mwisho pamoja na wanafunzi wake, wakati alipopaa kwenda mbinguni, Yesu aliwapa utume wa ‘kuwa mashahidi wake hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.’ (Matendo 1:6-11) Baadaye, alionekana kwa Sauli wa Tarso, aliyekuwa mnyanyasaji wa Wakristo. (Matendo 22:6-8) Yesu alionekana kwa Sauli “kama kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati wake.” Ilikuwa kama kwamba Sauli alikuwa tayari amefufuliwa kwenye uhai wa roho na angeweza kumwona Bwana aliyetukuzwa, karne nyingi kabla ya ufufuo huo kutokea. Jambo hilo lilifanya Sauli aache mara moja upinzani wa hata kuua kimakusudi washiriki wa kutaniko la Kikristo na kufanya badiliko lenye kutokeza. (Matendo 9:3-9, 17-19) Sauli alipata kuwa mtume Paulo, mmojawapo wa watetezi mashuhuri wa imani ya Kikristo.—1 Wakorintho 15:9, 10.

      Imani Katika Ufufuo Ni Muhimu

      11. Paulo alifichuaje kosa la kusema kwamba “hakuna ufufuo”?

      11 Kwa hiyo kufufuliwa kwa Yesu kulikuwa jambo la hakika lililothibitishwa vizuri. “Sasa ikiwa Kristo anahubiriwa kwamba amefufuliwa kutoka kwa wafu,” Paulo atoa hoja, “ni jinsi gani wengine miongoni mwenu husema hakuna ufufuo wa wafu?” (1 Wakorintho 15:12) Watu hao hawakuwa na shaka za kibinafsi au maswali kuhusu ufufuo tu, bali pia walisema waziwazi kwamba hawauamini. Hivyo Paulo afichua kusababu kwao kwenye kosa. Alisema kwamba ikiwa Kristo hakufufuliwa, ule ujumbe wa Kikristo ulikuwa uwongo, na walioshuhudia kufufuliwa kwa Kristo walikuwa “mashahidi wasio wa kweli wa Mungu.” Ikiwa Kristo hakuwa amefufuliwa, Mungu hakuwa amelipwa fidia yoyote; Wakristo walikuwa ‘bado wamo katika dhambi zao.’ (1 Wakorintho 15:13-19; Waroma 3:23, 24; Waebrania 9:11-14) Na Wakristo waliokuwa “wamelala usingizi katika kifo” katika visa vingine wakiwa wafia-imani, walikuwa wameangamia bila tumaini la kweli. Wakristo wangekuwa katika hali yenye kusikitisha kama nini ikiwa uhai huu ndio tu wangeweza kutarajia! Kuteseka kwao kwote hakungekuwa na maana.

      12. (a) Ni nini linalodokezwa na kumwita Kristo “matunda ya kwanza katika wale wamelala usingizi katika kifo?” (b) Kristo alifanyaje ufufuo uwezekane?

      12 Hata hivyo, hali haikuwa hivyo. Paulo aendelea kusema hivi: “Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu.” Zaidi ya hayo, yeye ni “matunda ya kwanza kati ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.” (1 Wakorintho 15:20) Yehova aliwabariki Waisraeli kwa mavuno makubwa, wakati ambapo walimpa kwa utii matunda ya kwanza ya mazao yao. (Kutoka 22:29, 30; 23:19; Mithali 3:9, 10) Kwa kumwita Kristo “matunda ya kwanza,” Paulo adokeza kwamba mavuno zaidi ya watu wangefufuliwa kutoka kwa wafu wakaishi mbinguni. “Kwa kuwa kifo ni kupitia mwanadamu,” Paulo asema, “ufufuo wa wafu pia ni kupitia mwanadamu. Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, ndivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.” (1 Wakorintho 15:21, 22) Yesu alifanya ufufuo uwezekane kwa kutoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu ukiwa fidia, ikiwafungulia wanadamu njia watoke katika utumwa wa dhambi na kifo.—Wagalatia 1:4; 1 Petro 1:18, 19.a

      13. (a) Ufufuo wa kimbingu unatukia lini? (b) Inakuwaje kwamba watiwa-mafuta fulani ‘hawalali usingizi katika kifo’?

      13 Paulo aendelea kusema hivi: “Lakini kila mmoja katika daraja lake mwenyewe: Kristo aliye matunda ya kwanza, baadaye wale walio wa Kristo wakati wa kuwapo kwake.” (1 Wakorintho 15:23) Kristo alifufuliwa mwaka wa 33 W.K. Hata hivyo, wafuasi wake watiwa-mafuta—“wale walio wa Kristo”—wangelazimika kungoja hadi punde baada ya Yesu kuanza kuwapo kwake kwa kifalme, ambako unabii wa Biblia waonyesha kulitukia mwaka wa 1914. (1 Wathesalonike 4:14-16; Ufunuo 11:18) Namna gani wale ambao wangekuwa hai wakati wa kuwapo kwake? Paulo asema hivi: “Tazama! Nawaambia nyinyi siri takatifu: Hatutalala usingizi katika kifo sisi sote, bali sisi sote tutabadilishwa, kwa dakika, katika kupepeseka kwa jicho, wakati wa tarumbeta ya mwisho. Kwa maana hiyo tarumbeta itavuma, na wafu watafufuliwa wakiwa wasioharibika, nasi tutabadilishwa.” (1 Wakorintho 15:51, 52) Kwa wazi, si watiwa-mafuta wote ambao hulala kaburini wakingojea ufufuo. Wanaokufa wakati wa kuwapo kwa Kristo hugeuzwa umbo mara moja.—Ufunuo 14:13.

      14. Watiwa-mafuta ‘hubatizwaje kwa kusudi la kuwa wafu’?

      14 “Kama sivyo,” Paulo auliza, “watafanya nini wao wanaobatizwa kwa kusudi la kuwa wafu? Ikiwa wafu hawapaswi kufufuliwa hata kidogo, kwa nini pia wanabatizwa kwa kusudi la kuwa hivyo? Kwa nini sisi pia tumo hatarini kila saa?” (1 Wakorintho 15:29, 30) Paulo hakumaanisha kwamba watu waliokuwa hai walibatizwa kwa niaba ya wafu, kama vile tafsiri nyingine za Biblia hufanya jambo hilo lionekane. Hata hivyo, ubatizo wahusiana na uanafunzi wa Kikristo, na nafsi zilizokufa haziwezi kuwa wanafunzi. (Yohana 4:1) Badala yake, Paulo alikuwa akizungumza juu ya Wakristo waliokuwa hai, ambao wengi wao, kama Paulo mwenyewe, walikuwa “hatarini kila saa.” Wakristo watiwa-mafuta ‘walibatizwa katika kifo cha Kristo.’ (Waroma 6:3) Tangu walipotiwa mafuta, walikuwa ‘wakibatizwa’ kitamathali, na kuingia katika mwendo ambao ungewaongoza kwenye kifo kama kile cha Kristo. (Marko 10:35-40) Wangekufa wakiwa na tumaini la ufufuo mtukufu wa kimbingu.—1 Wakorintho 6:14; Wafilipi 3:10, 11.

      15. Huenda Paulo alipatwa na hatari gani, na imani katika ufufuo ilitimizaje fungu katika kuzivumilia?

      15 Paulo sasa aeleza kwamba yeye mwenyewe alikuwa amekabili hatari kiasi cha kuweza kusema hivi: “Kila siku nakabili kifo.” Ili wengine wasije wakamshtaki kuwa mwenye kutia chumvi, Paulo aongeza kusema hivi: “Hili nathibitisha kwa mchachawo nilio nao juu yenu, akina ndugu, katika Kristo Yesu Bwana wetu.” Biblia Habari Njema hutafsiri mstari huu hivi: “Ndugu, mimi ninakabili kifo kila siku! Fahari niliyo nayo juu yenu katika kuungana na Kristo Yesu Bwana wetu inanifanya nitangaze jambo hili.” Ukiwa mfano wa hatari alizokabili, katika mstari wa 32, Paulo asema juu ya ‘kupigana na mahayawani-mwitu katika Efeso.’ Mara nyingi Waroma walifisha wahalifu kwa kuwatupa kwa mahayawani-mwitu katika viwanja vya michezo. Ikiwa Paulo alivumilia pigano na mahayawani-mwitu halisi, angeweza kuwa aliokoka tu kwa msaada wa Yehova. Bila tumaini la ufufuo, kuchagua njia ya maisha iliyomweka katika hatari kama hiyo kwa kweli kungalikuwa kujihatarisha kipumbavu. Bila tumaini la uhai wa wakati ujao, kuvumilia shida na kujidhabihu kulikoambatana na kumtumikia Mungu hakungekuwa na maana. “Ikiwa wafu hawapaswi kufufuliwa,” Paulo asema, “‘acheni tule na tunywe, kwa maana kesho tutapaswa kufa.’”—1 Wakorintho 15:31, 32; ona 2 Wakorintho 1:8, 9; 11:23-27.

      16. (a) Huenda usemi “acheni tule na tunywe, kwa maana kesho tutapaswa kufa” ukawa umetokana na nini? (b) Ni zipi zilizokuwa hatari za kukubali maoni hayo?

      16 Huenda ikawa Paulo alinukuu andiko la Isaya 22:13, ambalo lafafanua mtazamo wa nadharia-ajali wa wakazi wa Yerusalemu wasiotii. Au huenda akawa alikuwa akifikiria yale Waepikurea waliyoamini, waliodharau tumaini lolote la uhai baada ya kifo na kuamini raha ya kimwili ndiyo iliyokuwa jambo lenye faida kubwa maishani. Kwa vyovyote vile, “tule na tunywe” ilikuwa falsafa ya kutomwogopa Mungu. Kwa sababu hiyo Paulo aonya hivi: “Msiongozwe vibaya. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33) Kushirikiana na wale ambao walikataa ufufuo kungeweza kuwa jambo lenye sumu. Kushirikiana kama huko kulitimiza fungu fulani katika matatizo ambayo Paulo alikuwa ashughulikie katika kutaniko la Korintho, kama vile ukosefu wa adili katika ngono, migawanyiko, mashtaka ya kisheria, na kutostahi Mlo wa Jioni wa Bwana.—1 Wakorintho 1:11; 5:1; 6:1; 11:20-22.

      17. (a) Paulo aliwatolea Wakorintho onyo gani lenye upole? (b) Ni maswali gani yanayobaki kujibiwa?

      17 Hivyo Paulo awapa Wakorintho himizo hili lenye upole ambalo lafaa: “Amkeni mwe na utimamu wa akili katika njia ya uadilifu na msizoee dhambi, kwa maana wengine hawana ujuzi juu ya Mungu. Ninasema ili kuwasukuma mwone aibu.” (1 Wakorintho 15:34) Maoni yasiyofaa juu ya ufufuo yaliongoza wengine kuingia katika kuzubaa kiroho, kama kwamba walikuwa wamelewa. Walihitaji kuamka, kuwa timamu kiakili. Hivyohivyo, Wakristo watiwa-mafuta leo wanahitaji kuwa macho kiroho, bila kuathiriwa na maoni yenye kutilia shaka ya ulimwengu. Lazima washikamane kabisa na tumaini lao la ufufuo wa kimbingu. Lakini maswali bado yalibaki—kwa Wakorintho wakati huo na kwetu wakati wa sasa. Kwa kielelezo, wale 144,000 hufufuliwa kwenda mbinguni katika umbo gani? Na namna gani mamilioni ya wengine waliomo kaburini na ambao hawana tumaini la kimbingu? Ufufuo utamaanisha nini kwa watu kama hao? Katika makala yetu inayofuata, tutachunguza mazungumzo ya Paulo yanayobaki juu ya ufufuo.

  • “Kifo Kitafanywa Kuwa Si Kitu”
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Julai 1
    • “Kifo Kitafanywa Kuwa Si Kitu”

      “Kikiwa ni adui wa mwisho, kifo kitafanywa kuwa si kitu.” —1 WAKORINTHO 15:26.

      1, 2. (a) Mtume Paulo aliwatolea wafu tumaini gani? (b) Paulo alizungumzia swali gani kuhusu ufufuo?

      “NINAAMINI katika . . . ufufuo wa mwili, na uhai udumuo milele.” Hivyo ndivyo isemavyo ile taarifa ya itikadi iitwayo Imani ya Mitume. Wakatoliki na vilevile Waprotestanti huikariri kwa utiifu, wasing’amue kwamba mambo wanayoamini yafanana zaidi na falsafa za Kigiriki kuliko chochote kile ambacho mitume waliwahi kuamini. Hata hivyo, mtume Paulo alikataa falsafa ya Kigiriki na hakuamini kwamba nafsi haiwezi kufa. Hata hivyo, aliamini kwa dhati kuwako kwa uhai wakati ujao na kupuliziwa kuandika hivi: “Kikiwa ni adui wa mwisho, kifo kitafanywa kuwa si kitu.” (1 Wakorintho 15:26) Hilo lamaanisha nini hasa kwa wanadamu wanaokufa?

      2 Kwa kujibu, acheni turudi kwenye mazungumzo ya Paulo juu ya ufufuo yaliyorekodiwa katika 1 Wakorintho sura 15. Utakumbuka kwamba katika mistari ya kufungua, Paulo alithibitisha ufufuo kuwa sehemu muhimu ya fundisho la Kikristo. Sasa anazungumzia swali mahususi: “Hata hivyo, mtu fulani atasema: ‘Wafu watafufuliwaje? Ndiyo, wanakuja wakiwa na mwili wa namna gani?’”—1 Wakorintho 15:35.

      Mwili wa Aina Gani?

      3. Kwa nini watu fulani waliukataa ufufuo?

      3 Kwa kuzusha swali hilo, huenda Paulo akawa alinuia kukinza uvutano wa falsafa ya Plato. Plato alifundisha kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa ambayo hubaki hai baada ya mwili kufa. Wale waliokua wakiwa na wazo kama hilo, bila shaka fundisho la Kikristo la ufufuo halikuonekana kuwa jambo la lazima. Ikiwa nafsi iliendelea kuwa hai baada ya kifo, ufufuo una maana gani? Na zaidi, yaelekea ufufuo ulionekana kuwa jambo lisilo la akili. Mwili unapooza na kuwa mavumbi, kunaweza kuwaje na ufufuo? Mwelezaji wa Biblia, Heinrich Meyer, asema kwamba ugomvi wa Wakorintho fulani labda ulitegemea “msingi wa falsafa ya kwamba, lilikuwa jambo lisilowezekana kurudisha vitu vinavyoufanyiza mwili.”

      4, 5. (a) Kwa nini vipingamizi vya wasio na imani vilikuwa mambo yasiyo ya akili? (b) Eleza kielezi cha Paulo cha “punje tupu.” (c) Mungu huwapa watiwa-mafuta wenye kufufuliwa miili ya aina gani?

      4 Paulo afichua upumbavu wa kusababu kwao: “Wewe mtu asiye na akili! Kile upandacho hakifanywi kuwa hai isipokuwa kwanza kife; na kwa habari ya kile upandacho, wapanda, si mwili utakaositawi, bali punje tupu, huenda ikawa, ya ngano au yoyote moja kati ya zile nyingine; lakini Mungu huipa mwili kama vile imempendeza, na kwa kila moja ya hizo mbegu mwili wayo yenyewe.” (1 Wakorintho 15:36-38) Mungu hangefufua miili ambayo watu walikuwa nayo walipokuwa duniani. Badala yake, kungekuwa na mgeuzo umbo.

      5 Paulo alinganisha ufufuo na kumea kwa mbegu. Mbegu ndogo ya ngano huwa haifanani kwa vyovyote na mmea utakaoota kutoka kwake. Kichapo The World Book Encyclopedia chasema hivi: “Mbegu ianzapo kuota, hufyoza maji mengi sana. Hayo maji husababisha mabadiliko mengi ya kemikali ndani ya hiyo mbegu. Pia husababisha sehemu ya ndani ya mbegu kuvimba na kupasua ngozi ya nje ya mbegu.” Kwa kweli hiyo mbegu hufa ikiwa mbegu na kuwa mmea unaoibuka. “Mungu huipa mwili” kwa kuwa alizipanga sheria za kisayansi zinazoongoza kusitawi kwake, na kila mbegu hupokea mwili kulingana na aina yake. (Mwanzo 1:11) Vivyo hivyo, Wakristo watiwa-mafuta kwanza hufa wakiwa binadamu. Kisha, kwenye wakati wa Mungu uliowekwa, yeye huwafufua katika miili mipya kabisa. Kama vile Paulo alivyowaambia Wafilipi, “Yesu Kristo . . . ataufanya upya mwili wetu uliotwezwa ili upatanishwe na umbo la mwili wake wenye utukufu.” (Wafilipi 3:20, 21; 2 Wakorintho 5:1, 2) Wao hufufuliwa katika miili ya roho na huishi katika makao ya roho.—1 Yohana 3:2.

      6. Kwa nini ni jambo la akili kuamini kwamba Mungu aweza kuwapa wenye kufufuliwa miili ifaayo ya roho?

      6 Je, jambo hilo ni gumu mno kuamini? La. Paulo anasababu kwamba, wanyama wana miili mingi tofauti. Kwa kuongezea, yeye atofautisha malaika wa kimbingu na wanadamu wenye nyama na damu, akisema: “Kuna miili ya kimbingu, na miili ya kidunia.” Pia kuna tofauti kubwa kati ya uumbaji wa vitu visivyo na uhai. “Nyota hutofautiana na nyota kwa utukufu,” Paulo akasema, muda mrefu kabla sayansi haijagundua nyota kubwa kwa ndogo na zenye rangi tofauti-tofauti. Kwa kufikiria hilo, je, si jambo la akili kwamba Mungu aweza kuandaa miili ya roho ifaayo kwa ajili ya watiwa-mafuta wenye kufufuliwa?—1 Wakorintho 15:39-41.

      7. Ni nini maana ya kutoharibika? na ya kutoweza kufa?

      7 Kisha Paulo asema hivi: “Ndivyo pia ulivyo ufufuo wa wafu. Hupandwa katika uharibifu, hufufuliwa katika kutoharibika.” (1 Wakorintho 15:42) Mwili wa kibinadamu, hata unapokuwa mkamilifu, waweza kuharibika. Waweza kuuawa. Kwa mfano, Paulo alisema kwamba Yesu aliyefufuliwa “[ali]kusudiwa asirudi tena kwenye uharibifu.” (Matendo 13:34) Hangefufuliwa katika mwili wa kibinadamu wenye kuharibika, hata ingawa ni mkamilifu. Mungu huwapa watiwa-mafuta wenye kufufuliwa miili isiyoharibika—isiyoweza kufa au kuoza. Paulo aendelea kusema hivi: “Hupandwa katika fedheha, hufufuliwa katika utukufu. Hupandwa katika udhaifu, hufufuliwa katika nguvu. Hupandwa ukiwa mwili wa nyama, hufufuliwa ukiwa mwili wa kiroho.” (1 Wakorintho 15:43, 44) Na zaidi, Paulo asema hivi: “Huu uwezao kufa lazima uvae hali ya kutokufa.” Kutokufa humaanisha uhai wa milele usioweza kuhabiriwa. (1 Wakorintho 15:53; Waebrania 7:16) Katika njia hiyo, wenye kufufuliwa huchukua “mfano wa yule wa kimbingu,” yaani Yesu, aliyewezesha kufufuliwa kwao.—1 Wakorintho 15:45-49.

      8. (a) Twajuaje kwamba wenye kufufuliwa watakuwa watu walewale waliokuwa hai duniani? (b) Ni unabii gani mbalimbali unaotimizwa ufufuo utokeapo?

      8 Licha ya mgeuzo umbo huo, wenye kufufuliwa bado watakuwa watu walewale waliokuwa kabla ya kufa. Watafufuliwa na kumbukumbu zilezile na sifa zilezile bora za Kikristo. (Malaki 3:3; Ufunuo 21:10, 18) Katika hilo wanafanana na Yesu Kristo. Umbo lake la roho lilibadilika kuwa la kibinadamu. Kisha akafa na kufufuliwa akiwa roho. Hata hivyo, “Yesu Kristo ni yuleyule jana na leo, na milele.” (Waebrania 13:8) Watiwa-mafuta wana pendeleo lililoje! Paulo asema hivi: “Lakini wakati huu ulio wenye kuharibika uvaapo kutoharibika na huu uwezao kufa uvaapo hali ya kutokufa, ndipo usemi utakapotukia ambao umeandikwa: ‘Kifo kimemezwa milele.’ ‘Kifo, ushindi wako uko wapi? Kifo, kichomeo chako kiko wapi?’”—1 Wakorintho 15:54, 55; Isaya 25:8; Hosea 13:14.

      Ufufuo wa Kidunia?

      9, 10. (a) Katika muktadha wa 1 Wakorintho 15:24, “mwisho” ni nini, na ni matukio gani yatokeayo kuhusiana na huo? (b) Ni lazima jambo gani litokee ili kifo kifanywe kuwa si kitu?

      9 Je, kuna wakati ujao wowote kwa mamilioni yasiyo na tumaini la uhai wa roho usioweza kufa? Kwa kweli kunao! Baada ya kueleza kwamba ufufuo wa kimbingu hutukia wakati wa kuwapo kwa Kristo, Paulo atoa muhtasari wa matukio yanayofuata kuwapo kwa Kristo, akisema: “Halafu, mwisho, wakati amkabidhipo ufalme Mungu wake aliye Baba, wakati akiwa amefanya serikali yote na mamlaka yote na nguvu kuwa si kitu.”—1 Wakorintho 15:23, 24.

      10 “Mwisho” ni mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, wakati Yesu amkabidhipo Ufalme Mungu wake aliye Baba, kwa unyenyekevu na kwa uaminifu-mshikamanifu. (Ufunuo 20:4) Kusudi la Mungu “kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo” litakuwa limetimizwa. (Waefeso 1:9, 10) Ingawa hivyo, kwanza Kristo atakuwa ameharibu “serikali yote na mamlaka yote” yenye kupinga mapenzi ya Enzi Kuu ya Mungu. Hilo lahusisha mengi zaidi ya uharibifu utakaotekelezwa kwenye Har–Magedoni. (Ufunuo 16:16; 19:11-21) Paulo asema hivi: “Ni lazima [Kristo] atawale akiwa mfalme mpaka Mungu awe ameweka maadui wote chini ya miguu yake. Kikiwa ni adui wa mwisho, kifo kitafanywa kuwa si kitu.” (1 Wakorintho 15:25, 26) Naam, alama zote za dhambi na kifo cha Kiadamu zitakuwa zimeondolewa. Basi, kwa sababu ya uhitaji, Mungu atakuwa ameyaacha “makaburi ya ukumbusho” yakiwa tupu kwa kuwafufua wafu.—Yohana 5:28.

      11. (a) Twajuaje kwamba Mungu aweza kuumba tena nafsi zilizokufa? (b) Watakaofufuliwa duniani watapewa miili ya aina gani?

      11 Hilo lamaanisha kuumba tena nafsi za kibinadamu. Je, ni jambo lisilowezekana? La, kwa kuwa andiko la Zaburi 104:29, 30 latuhakikishia kwamba Mungu aweza kufanya hivyo: “Waiondoa pumzi yao, wanakufa, na kuyarudia mavumbi yao, waipeleka roho yako, wanaumbwa.” Ingawa wenye kufufuliwa watakuwa watu walewale waliokuwa kabla ya kufa, hawatahitaji kuwa na miili ileile. Sawa na wale watakaofufuliwa kwenda mbinguni, Mungu atawapa mwili kama vile impendezavyo. Bila shaka miili yao mipya itakuwa yenye afya na kwa kufaa itakuwa sawa na miili yao ya hapo awali, hivi kwamba wapendwa wao wataweza kuwatambua.

      12. Ufufuo wa kidunia unatokea lini?

      12 Ufufuo wa kidunia utatokea lini? Martha alisema hivi kumhusu ndugu yake Lazaro: “Najua atafufuliwa katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yohana 11:24) Alijuaje hilo? Ufufuo ulikuwa jambo lenye kubishaniwa katika siku yake, kwa kuwa Mafarisayo waliamini katika ufufuo ilhali Masadukayo hawakuamini katika huo. (Matendo 23:8) Hata hivyo, ni lazima Martha awe aliwajua mashahidi wa kabla ya Ukristo waliotumaini katika ufufuo. (Waebrania 11:35) Pia, angeweza kutambua kutoka katika kitabu cha Danieli 12:13 kwamba ufufuo utatokea siku ya mwisho. Huenda hata akawa alijifunza jambo hilo kutoka kwa Yesu mwenyewe. (Yohana 6:39) “Siku [hiyo] ya mwisho” yasadifiana na Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. (Ufunuo 20:6) Ebu wazia msisimko katika “siku” hiyo wakati ambapo tukio hilo tukufu linaanza!—Linganisha Luka 24:41.

      Ni Nani Wanaofufuliwa?

      13. Ni ono gani la ufufuo linalorekodiwa kwenye Ufunuo 20:12-14?

      13 Ono la Yohana juu ya ufufuo wa kidunia limerekodiwa kwenye Ufunuo 20:12-14 hivi: “Nikaona wafu, wakubwa na wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha ufalme, na hati-kunjo zikafunguliwa. Lakini hati-kunjo nyingine ikafunguliwa; hiyo ndiyo hati-kunjo ya uhai. Na hao wafu wakahukumiwa kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika hizo hati-kunjo kulingana na vitendo vyao. Nayo bahari ikawatoa hao wafu waliokuwa ndani yayo, na kifo na Hadesi vikawatoa wafu ndani yavyo, nao walihukumiwa mmoja-mmoja kulingana na vitendo vyao. Na kifo na Hadesi vikavurumishwa ndani ya ziwa la moto. Hili humaanisha kifo cha pili, ziwa la moto.”

      14. Ni nani watakaokuwa miongoni mwa wale wenye kufufuliwa?

      14 Ufufuo utatia ndani “wakubwa na wadogo,” wanadamu mashuhuri na wasio mashuhuri, walioishi na kufa. Naam, hata vitoto vichanga vitakuwa miongoni mwa watakaofufuliwa! (Yeremia 31:15, 16) Kwenye Matendo 24:15, habari nyingine ya maana inafunuliwa: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Watu mashuhuri miongoni mwa “waadilifu” watakuwa wanaume na wanawake waaminifu wa zamani kama vile Abeli, Enoki, Noa, Abrahamu, Sara, na Rahabu. (Waebrania 11:1-40) Ebu wazia kuweza kuongea na mashahidi hao wa kujionea na kupata habari nyingi za matukio ya Biblia ya zamani za kale! “Waadilifu” pia watatia ndani maelfu ya watu wenye kuhofu Mungu ambao wamekufa nyakati za karibuni zaidi na ambao hawakuwa na tumaini la kimbingu. Je, una mshiriki wa familia au mpendwa ambaye huenda akawa miongoni mwao? Inafariji kama nini kujua kwamba unaweza kuwaona tena! Hata hivyo, ni nani hao “wasio waadilifu” ambao watafufuliwa pia? Wanatia ndani mamilioni, labda mabilioni, ambao walikufa bila kuwa na fursa ya kujifunza na kutumia kweli ya Biblia.

      15. Yamaanisha nini kusema kwamba wanaofufuliwa “[watahukumiwa] kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika hizo hati-kunjo”?

      15 Wenye kufufuliwa “[watahukumiwaje] kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika hizo hati-kunjo kulingana na vitendo vyao”? Hati-kunjo hizo si rekodi ya vitendo vyao vya wakati uliopita; walipokufa, waliondolewa hatia ya dhambi walizofanya maishani mwao. (Waroma 6:7, 23) Hata hivyo, wanadamu wenye kufufuliwa bado watakuwa chini ya dhambi ya Kiadamu. Basi, ni lazima iwe kwamba hati-kunjo hizo zitaeleza kikamili maagizo ya kimungu ambayo wote lazima wafuate ili wanufaike kikamili na dhabihu ya Yesu Kristo. Alama ya mwisho ya dhambi ya Kiadamu inapofutwa, “kifo kitafanywa kuwa si kitu” katika maana kamili. Kufikia mwisho wa miaka elfu, Mungu “[ata]kuwa vitu vyote kwa kila mtu.” (1 Wakorintho 15:28) Mwanadamu hatahitaji tena uingiliaji-kati wa Kuhani wa Cheo cha Juu au Mfidi. Wanadamu wote watarudishwa kwenye hali ya ukamilifu ambayo Adamu alifurahia hapo awali.

      Ufufuo Wenye Utaratibu

      16. (a) Kwa nini ni jambo la akili kuamini kwamba ufufuo utafanywa kwa utaratibu? (b) Yaelekea ni nani watakaokuwa miongoni mwa watu wa kwanza kufufuliwa?

      16 Kwa kuwa ufufuo wa kimbingu ni wenye utaratibu, “kila mmoja katika daraja lake mwenyewe,” ni wazi kwamba ufufuo wa kidunia hautatokeza ongezeko la ghafula la idadi ya watu lisilo na utaratibu. (1 Wakorintho 15:23) Ni jambo lenye kueleweka kwamba, wenye kufufuliwa karibuni watahitaji kutunzwa. (Linganisha Luka 8:55.) Watahitaji riziki ya kimwili na msaada wa kiroho ambao ni wa maana zaidi katika kupata ujuzi wenye kutoa uhai juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Yohana 17:3) Kama wote wangefufuliwa wakati uleule, haingewezekana kuwatunza vya kutosha. Ni jambo la akili kukata kauli kwamba ufufuo utatokea hatua kwa hatua. Wakristo waaminifu waliokufa punde kabla ya mwisho wa mfumo wa Shetani yaelekea watakuwa miongoni mwa wale watakaofufuliwa kwanza. Twaweza pia kutarajia ufufuo wa mapema wa wanaume waaminifu wa zamani watakaotumikia wakiwa “wakuu.”—Zaburi 45:16.

      17. Ni masuala gani kuhusiana na ufufuo ambayo Biblia haisemi chochote kuyahusu, na ni kwa nini Wakristo hawapaswi kuhangaika isivyofaa kuhusu mambo hayo?

      17 Hata hivyo, hatupaswi kuwalazimisha watu wafuate maoni yetu juu ya mambo hayo. Biblia haisemi chochote juu ya masuala mengi. Haina habari nyingi zilizo wazi juu ya vipi, lini, au mahali ambapo huo ufufuo wa watu utatokea. Haituambii jinsi wanaofufuliwa watakavyopewa makao, chakula, na nguo. Wala hatuwezi kusema kwa uhakika jinsi Yehova atakavyotatua masuala kama vile kulea na kutunza watoto wenye kufufuliwa wala jinsi atakavyoshughulikia hali fulani ambazo huenda zikahusisha marafiki na wapendwa wetu. Ni kweli ni jambo la kawaida kujiuliza maswali kuhusu mambo hayo; lakini halingekuwa jambo la hekima kupoteza wakati ukijaribu kuyajibu maswali ambayo kwa sasa hayawezi kujibiwa. Twapaswa kukaza fikira zetu juu ya kumtumikia Yehova kwa uaminifu na juu ya kupata uhai udumuo milele. Wakristo watiwa-mafuta huweka tumaini lao katika ufufuo wa kimbingu. (2 Petro 1:10, 11) “Kondoo wengine” hutumaini kupata urithi udumuo milele katika makao ya kidunia ya Ufalme wa Mungu. (Yohana 10:16; Mathayo 25:33, 34) Kuhusu hizo habari nyingi ambazo hazijulikani juu ya ufufuo, tutamtumaini Yehova. Furaha yetu ya wakati ujao iko salama katika mikono ya Yule awezaye ‘kushibisha kila kilicho hai matakwa yake.’—Zaburi 145:16; Yeremia 17:7.

      18. (a) Paulo akazia ushindi gani? (b) Kwa nini tuko na tumaini hakika katika ufufuo?

      18 Paulo amalizia kutoa hoja zake kwa kutangaza hivi: “Shukrani kwa Mungu, kwa maana yeye hutupa sisi ushindi kupitia Bwana wetu Yesu Kristo!” (1 Wakorintho 15:57) Naam, kifo cha Kiadamu hushindwa kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, na watiwa-mafuta na pia “kondoo wengine” hushiriki ushindi huo. Bila shaka, “kondoo wengine” walio hai leo wana tumaini ambalo ni la pekee kwa kizazi hiki. Wakiwa sehemu ya “umati mkubwa,” unaozidi kuongozeka huenda wakaokoka “dhiki kubwa” inayokuja, na kutopatwa kamwe na kifo cha mwili! (Ufunuo 7:9, 14) Hata hivyo, hata wale wanaokufa kwa sababu ya “wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” NW]” au wakiwa mikononi mwa wawakilishi wa Shetani, wanaweza kuweka uhakika wao katika tumaini la ufufuo.—Mhubiri 9:11.

      19. Ni himizo gani lenye bidii ambalo Wakristo wote wapaswa kusikiza leo?

      19 Kwa hiyo, twangojea kwa hamu siku hiyo tukufu kifo kitakapofanywa kuwa si kitu. Kutumaini katika ahadi ya Yehova ya ufufuo bila kuyumbayumba hufanya mambo yaonekane halisi. Chochote kitupatacho katika maisha haya—hata ikiwa tutakufa—hakuna chochote kiwezacho kutupokonya thawabu ambayo Yehova ameahidi. Kwa sababu hiyo, himizo lenye bidii la Paulo kwa Wakorintho lafaa leo kama vile lilivyofaa miaka elfu mbili iliyopita: “Kwa sababu hiyo, ndugu zangu wapendwa, iweni imara, wasioondoleka, sikuzote mkiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.”—1 Wakorintho 15:58.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki