-
Timotheo—Msaidizi Mpya wa PauloKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 110
Timotheo—Msaidizi Mpya wa Paulo
KIJANA unayeona hapa pamoja na mtume Paulo ni Timotheo. Timotheo anakaa pamoja na jamaa yake Listra. Jina la mama yake ni Eunike na nyanya yake Loisi.
Hii ndiyo mara ya tatu ya Paulo kutembelea Listra. Mwaka mmoja uliotangulia, Paulo na Barnaba walifika huku mara ya kwanza katika safari ya kuhubiri. Na sasa Paulo amerudi tena huko akiwa na rafiki yake Sila.
Unajua Paulo anamwambia Timotheo nini? ‘Ungependa kwenda pamoja na Sila na mimi?’ anauliza. ‘Ungeweza kutusaidia kuhubiri watu wa mbali.’
‘Ndiyo,’ Timotheo ajibu, ‘ningependa kwenda.’ Basi upesi baada ya hapo Timotheo aacha jamaa yake na kwenda pamoja na Paulo na Sila. Lakini kabla ya kujifunza juu ya safari yao, na tujifunze ambayo yamekuwa yakimpata Paulo. Imekuwa miaka 17 tangu Yesu alipomtokea akienda Damasko.
Adui fulani wanafanya mpango wa kumwua Paulo kwa sababu hawataki mafundisho juu ya Yesu. Lakini wanafunzi wanamsaidia Paulo aokoke. Wanamweka katika kikapu na kumtelemsha nje ya ukuta wa mji.
Baada ya hayo Paulo aenda Antiokia kuhubiri. Huko ndiko kwa mara ya kwanza, wafuasi wa Yesu wanaitwa Wakristo. Ndipo Paulo na Barnaba wanatumwa kutoka Antiokia waende katika safari ya kuhubiri nchi za mbali sana. Mji mmoja ambao wanatembelea ni Listra, nyumbani kwa Timotheo.
Baadaye, kama mwaka mmoja, Paulo anarudi Listra katika safari ya pili. Timotheo anapokwenda na Paulo na Sila, unajua wanakwenda wapi? Angalia ramani, tujifunze sehemu chache.
Kwanza, wanakwenda kwenye mji wa Ikonio, kisha mji wa pili wa Antiokia. Baada ya hapo wanasafiri kwenda Troʹa, kisha Filipi, Thesalonike na Beroya. Unaona Athene katika ramani? Paulo anahubiri huko. Kisha wanakaa mwaka mmoja na nusu wakihubiri Korintho. Mwishowe wanasimama kidogo katika Efeso. Kisha wanarudi Kaisaria kwa meli, na kusafiri kwenda juu Antiokia, ambako Paulo anakaa.
Hivyo Timotheo anasafiri mamia na mamia ya kilomita akimsaidia Paulo azihubiri “habari njema” na kuanza makundi mengi ya Kikristo. Utakapokuwa mkubwa, je! utakuwa mtumishi mwaminifu wa Mungu kama Timotheo?
-
-
Mvulana Aliyelala UsingiziKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 111
Mvulana Aliyelala Usingizi
MAMA WEE! Haya ni mambo gani? Mvulana aliye chini ameumizwa vibaya? Tazama! mmoja wa watu wanaotoka nyumbani ni Paulo! Unamwona Timotheo pia? Mvulana huyo alianguka kutoka dirisha?
Ndivyo ilivyokuwa. Paulo alikuwa akitolea wanafunzi hotuba katika Troa. Alijua kwamba hangewaona tena kwa muda mrefu kwa sababu kesho yake angeondoka kwa meli. Hivyo akaendelea kuzungumza wee mpaka saa sita za usiku.
Basi, mvulana huyo Eutiko aliketi penye dirisha, akalala usingizi. We! akaanguka kutoka dirishani, orofa tatu mpaka chini! Basi unajua sababu gani watu hawa wana wasiwasi. Watu wanapomwinua mvulana, amekufa kitambo!
Paulo anapoona mvulana amekufa, anamlalia na kumkumbatia. Kisha anasema: ‘Msitie shaka. Yuko salama!’ Na ni kweli! Ni mwujiza! Paulo amemfufua! Watu wengi wanaanza kufurahi.
Wote wanapanda juu tena na kula chakula. Paulo anaendelea kuzungumza mpaka asubuhi. Lakini Eutiko halali usingizi tena! Ndipo Paulo, Timotheo na wasafiri wenzao wanapanda meli. Unajua wanaenda wapi?
Sasa Paulo anamalizia safari yake ya tatu ya kuhubiri, anarudi nyumbani. Katika safari hii Paulo alikuwa amekaa miaka mitatu katika mji wa Efeso peke yake. Hii ni safari yake ndefu sana kuliko ile ya pili.
Baada ya kutoka Troa, meli inasimama kidogo Mileto. Kwa kuwa Efeso ni mwendo wa kilomita chache, Paulo anapeleka habari ili wazee katika kundi waje Mileto aweze kusema nao mara ya mwisho. Wakati wa meli kuondoka unapofika, wanahuzunika sana kumwona Paulo akienda!
Mwishowe meli yarudi Kaisaria. Paulo anapokaa huku katika nyumba ya mwanafunzi Filipo, nabii Agapo anamwonya Paulo. Anasema kwamba Paulo atafungwa akifika Yerusalemu. Na kwa hakika, inakuwa hivyo.
-