Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Kuyaimarisha Makutaniko”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 15

      ‘Kuyaimarisha Makutaniko’

      Waangalizi wa mzunguko huyasaidia makutaniko yawe na imani yenye nguvu

      Matendo 15:36–16:5

      1-3. (a) Paulo anasafiri na nani, na mwandamani huyo ni mtu wa aina gani? (b) Tutajifunza nini katika sura hii?

      WANAPOVUKA milima na mabonde kutoka mji mmoja hadi mwingine, mtume Paulo anamfikiria kijana anayesafiri pamoja naye. Kijana huyo ni Timotheo mwenye umri wa miaka 20 hivi. Kadiri kijana huyo anavyotembea katika safari hii ndivyo anavyokuwa mbali zaidi na nyumbani kwao. Kadiri siku inavyopita, ndivyo wanavyozidi kuwa mbali na majiji ya Listra na Ikoniamu. Ni mambo gani yatakayotokea? Huenda Paulo alijua kwa sababu hii ni safari yake ya pili ya umishonari. Anajua kwamba kutakuwa na hatari na matatizo mengi. Timotheo atatendaje atakapokabili hali hizo?

      2 Paulo anamwamini Timotheo, labda kuliko Timotheo anavyojiamini. Matukio ya karibuni yalimfanya Paulo aone umuhimu wa kuchagua mwandamani anayefaa. Paulo anajua kwamba kazi ya kutembelea makutaniko na kuyatia nguvu, inahitaji waangalizi walio thabiti na wenye nia moja. Kwa nini? Huenda sababu moja ni kutoelewana kati ya Paulo na Barnaba kulikosababisha mgawanyiko.

      3 Katika sura hii tutajifunza mengi kuhusu njia bora ya kutatua kutoelewana. Pia, tutajua ni kwa nini Paulo alichagua kusafiri na Timotheo, nasi tutajifunza mengi kuhusu kazi muhimu inayotimizwa na waangalizi wa mzunguko.

      “Turudi Tukawatembelee Akina Ndugu” (Mdo. 15:36)

      4. Paulo alikusudia kufanya nini katika safari yake ya pili ya umishonari?

      4 Katika sura iliyotangulia tuliona jinsi ndugu wanne, Paulo, Barnaba, Yuda, na Sila, walivyolitia nguvu kutaniko la Antiokia kwa kulijulisha uamuzi wa baraza linaloongoza kuhusu suala la tohara. Paulo alifanya nini baadaye? Alimwendea Barnaba akiwa na mikakati mipya ya safari, akamwambia: “Turudi tukawatembelee akina ndugu katika kila jiji ambalo tulitangaza neno la Yehova tuone jinsi wanavyoendelea.” (Mdo. 15:36) Paulo hakuwa akipendekeza wawatembelee Wakristo hao wapya kirafiki tu. Kitabu cha Matendo kinaonyesha wazi kusudi halisi la safari ya pili ya umishonari ya Paulo. Kwanza, kuyajulisha makutaniko maagizo yaliyotolewa na baraza linaloongoza. (Mdo. 16:4) Pili, akiwa mwangalizi wa mzunguko, Paulo alikuwa ameazimia kuyajenga makutaniko kiroho, na kusaidia kuimarisha imani yao. (Rom. 1:11, 12) Tengenezo la Mashahidi wa Yehova linafanyaje hivyo leo?

      5. Baraza Linaloongoza huwasiliana na makutaniko na kuyatia moyo jinsi gani?

      5 Leo, Kristo anatumia Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova kuongoza kutaniko lake. Kupitia barua, machapisho ya mtandaoni na yaliyochapishwa, mikutano, na njia nyingine, ndugu hao watiwa-mafuta huyaongoza na kuyatia moyo makutaniko ulimwenguni pote. Pia, Baraza Linaloongoza hujitahidi kudumisha mawasiliano pamoja na kila kutaniko. Ili kufanya hivyo, wanatumia waangalizi wa mzunguko. Baraza Linaloongoza huwaweka rasmi maelfu ya wazee wanaostahili ulimwenguni pote kuwa waangalizi wa mzunguko.

      6, 7. Waangalizi wa mzunguko wana majukumu gani?

      6 Waangalizi wa mzunguko leo huwahangaikia na kuwatia moyo wote katika makutaniko wanayotembelea. Jinsi gani? Kwa kufuata kielelezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza kama Paulo. Alimhimiza hivi mwangalizi mwenzake: “Lihubiri neno; fanya hivyo kwa uharaka katika nyakati zinazofaa na nyakati ngumu; karipia, kemea, himiza, kwa subira yote na ustadi wa kufundisha. . . . Fanya kazi ya mweneza-injili.”​—2 Tim. 4:2, 5.

      7 Waangalizi wa mzunguko—pamoja na wake zao ikiwa wameoa—hutii maneno hayo kwa kushiriki katika huduma ya shambani pamoja na wahubiri wa kutaniko wanalotembelea. Kwa sababu wao ni walimu stadi, na wanapenda huduma, mfano wao unawachochea ndugu na dada. (Rom. 12:11; 2 Tim. 2:15) Waangalizi wa mzunguko huonyesha upendo usio na ubinafsi na kujidhabihu. Huwatumikia wengine kwa hiari, nyakati nyingine wanasafiri wakati ambapo kuna hali mbaya ya hewa na hata katika maeneo yenye hatari. (Flp. 2:3, 4) Pia, waangalizi wa mzunguko hutia moyo, hufundisha, na kuonya makutaniko kupitia hotuba zinazotegemea Biblia. Ni vizuri kwa wote kutanikoni kutafakari mfano mzuri wa waangalizi hao na kujitahidi kuiga imani yao.​—Ebr. 13:7.

      “Wakagombana kwa Ukali” (Mdo. 15:37-41)

      8. Barnaba aliitikiaje mwaliko wa Paulo?

      8 Barnaba alikubali pendekezo la Paulo la ‘kuwatembelea akina ndugu.’ (Mdo. 15:36) Wawili hao walifanya kazi bega kwa bega wakisafiri pamoja, na tayari walijua maeneo na watu waliohitaji kutembelewa. (Mdo. 13:2–14:28) Kwa hiyo, huenda waliona ingefaa wasafiri pamoja kwa ajili ya mgawo huo. Hata hivyo, tatizo likatokea. Andiko la Matendo 15:37 linasema: “Barnaba alikuwa ameazimia kwenda na Yohana, aliyeitwa Marko.” Barnaba hakuwa akitoa pendekezo. “Alikuwa ameazimia” waende pamoja binamu yake, Marko, katika safari hiyo ya umishonari.

      9. Kwa nini Paulo na Barnaba hawakuelewana?

      9 Paulo hakukubali. Kwa nini? Masimulizi yanasema: “Lakini Paulo hakutaka waende pamoja naye [Marko], kwa sababu alikuwa amewaacha huko Pamfilia na hakuenda pamoja nao kwenye kazi.” (Mdo. 15:38) Marko alikuwa amesafiri pamoja na Paulo na Barnaba katika safari yao ya kwanza ya umishonari lakini hakuendelea na safari hiyo mpaka mwisho. (Mdo. 12:25; 13:13) Mwanzoni katika safari yao ya kwanza, wakiwa Pamfilia, Marko aliuacha mgawo wake na kurudi nyumbani Yerusalemu. Biblia haisemi ni kwa nini aliondoka, lakini inaonekana kwamba mtume Paulo alimwona Marko kuwa mtu asiyechukua mambo kwa uzito. Huenda Paulo alikuwa na mashaka kuhusu kutegemeka kwa Marko.

      10. Kutoelewana kati ya Paulo na Barnaba kulisababisha nini, na matokeo yalikuwa nini?

      10 Hata hivyo, Barnaba alikuwa ameazimia kwenda na Marko. Na Paulo alikataa kwenda naye. Matendo 15:39 inasema: “Ndipo wakagombana kwa ukali hivi kwamba wakaachana.” Barnaba akapanda meli kuelekea Kipro, kisiwa cha nyumbani kwao, akiwa pamoja na Marko. Naye Paulo akaenda zake. Masimulizi hayo yanasema: “Paulo akamchagua Sila na kuondoka baada ya akina ndugu kumkabidhi kwenye fadhili zisizostahiliwa za Yehova.” (Mdo. 15:40) Wakasafiri pamoja ‘kupitia Siria na Kilikia, wakiyaimarisha makutaniko.’​—Mdo. 15:41.

      11. Ni sifa gani zinazohitajiwa ili kudumisha urafiki na mtu aliyetukosea?

      11 Huenda masimulizi hayo yakatukumbusha hali yetu ya kutokamilika. Paulo na Barnaba walikuwa wamewekwa rasmi kuwa wawakilishi wa pekee wa baraza linaloongoza. Inaonekana baadaye Paulo aliwekwa rasmi kuwa mshiriki wa baraza hilo. Hata hivyo, ingawa Paulo na Barnaba walikuwa ndugu wazuri sana, wakati huu walishindwa kudhibiti hasira yao. Je, wangeruhusu hali hiyo ivunje kabisa urafiki wao? Ingawa hawakuwa wakamilifu, Paulo na Barnaba walikuwa wanyenyekevu, na walikuwa na akili ya Kristo. Ndiyo sababu baada ya muda mfupi, walionyesha roho ya undugu wa Kikristo na kusameheana. (Efe. 4:1-3) Baadaye, Paulo na Marko walifanya kazi pamoja katika migawo mingine ya Kikristo.a—Kol. 4:10.

      12. Kama Paulo na Barnaba, waangalizi wanapaswa kuwa na sifa gani?

      12 Tukio hilo moja halimaanishi kwamba Barnaba na Paulo walikuwa na utu huo. Barnaba alikuwa mwenye upendo na mkarimu sana hivi kwamba badala ya mitume kumwita kwa jina lake, Yosefu, walikuwa wakimwita Barnaba, yaani, “Mwana wa Faraja.” (Mdo. 4:36) Paulo alikuwa mpole na mwenye upendo mwororo. (1 The. 2:7, 8) Waangalizi Wakristo leo, kutia ndani waangalizi wa mzunguko, wanapaswa kujitahidi kuwa wanyenyekevu na kuwatendea wazee wenzao na kundi zima kwa wororo.​—1 Pet. 5:2, 3.

      “Alishuhudiwa Vema” (Mdo. 16:1-3)

      13, 14. (a) Timotheo alikuwa nani, na alikutana jinsi gani na Paulo? (b) Kwa nini Paulo alipendezwa na Timotheo? (c) Timotheo alipewa mgawo gani?

      13 Katika safari yake ya pili ya umishonari, Paulo alienda Galatia, mkoa wa Roma, ambako makutaniko kadhaa yalikuwa yameanzishwa. Mwishowe, “akafika Derbe na pia Listra.” Simulizi hilo linaendelea kusema hivi: “Huko kulikuwa na mwanafunzi aliyeitwa Timotheo, mama yake alikuwa Myahudi aliyekuwa mwamini, lakini baba yake alikuwa Mgiriki.”​—Mdo. 16:1.b

      14 Inaonekana kwamba, Paulo alikuwa amekutana na familia ya Timotheo alipotembelea eneo hilo karibu mwaka wa 47 W.K. Baada ya miaka miwili au mitatu hivi, wakati wa safari yake ya pili, Paulo alipendezwa kwa njia ya pekee na kijana Timotheo. Kwa nini? Kwa sababu Timotheo “alishuhudiwa vema na akina ndugu.” Sifa nzuri za Timotheo zilijulikana kutanikoni kwao na hata katika makutaniko mengine. Masimulizi ya Matendo yanasema kwamba akina ndugu wa Listra na Ikoniamu, waliokuwa umbali wa kilomita 30 hivi, walijua sifa nzuri za Timotheo. (Mdo. 16:2) Wakiongozwa na roho takatifu, wazee walimpa kijana Timotheo mgawo mzito wa kusafiri pamoja na Paulo na Sila ili kufanya kazi nao.​—Mdo. 16:3.

      15, 16. Timotheo aliwezaje kupata sifa nzuri?

      15 Timotheo alipataje sifa nzuri hivyo akiwa kijana? Je, ni kwa sababu alikuwa na akili nyingi, sura nzuri, au vipawa vyake? Mara nyingi wanadamu huvutiwa na mambo kama hayo. Hata nabii Samweli alidanganyika wakati fulani kwa kuangalia mwonekano wa nje. Hata hivyo, Yehova alimkumbusha: “Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona ndani ya moyo.” (1 Sam. 16:7) Timotheo alikuwa na sifa za ndani zilizowavutia Wakristo wenzake.

      16 Miaka kadhaa baadaye, mtume Paulo alirejelea sifa fulani za Timotheo. Paulo alitaja mtazamo wake mzuri, upendo wake wa kujidhabihu, na bidii yake katika kushughulikia migawo ya kiroho. (Flp. 2:20-22) Timotheo alijulikana pia kwa kuwa na ‘imani isiyo na unafiki.’​—2 Tim. 1:5.

      17. Vijana wanawezaje kumwiga Timotheo?

      17 Leo, vijana wengi humwiga Timotheo kwa kusitawisha sifa zinazompendeza Mungu. Wanajifanyia jina zuri pamoja na Yehova na watu wake, hata wakiwa na umri mdogo. (Met. 22:1; 1 Tim. 4:15) Wanaonyesha imani isiyo na unafiki. (Zab. 26:4) Hivyo, vijana wengi, kama Timotheo, wanaweza kutimiza mengi katika kutaniko. Wanapostahili kuwa wahubiri wa habari njema na hatimaye kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, wao huwatia moyo wote wanaompenda Yehova!

      “Kuimarishwa Katika Imani” (Mdo. 16:4, 5)

      18. (a) Paulo na Timotheo walilisaidiaje baraza linaloongoza wakiwa wahudumu wanaosafiri? (b) Makutaniko yalipata baraka gani?

      18 Paulo na Timotheo walifanya kazi pamoja kwa miaka mingi. Wakiwa wahudumu wanaosafiri, walifanya mambo mbalimbali waliyoagizwa na baraza linaloongoza. Biblia inasema: “Walipokuwa wakipita katika majiji, walikuwa wakiwapa maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wazee waliokuwa Yerusalemu ili wayashike.” (Mdo. 16:4) Bila shaka makutaniko yalifuata mwongozo wa mitume na wazee waliokuwa Yerusalemu. Kwa sababu ya kutii “makutaniko yakaendelea kuimarishwa katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.”​—Mdo. 16:5.

      19, 20. Kwa nini Wakristo wanapaswa kuwatii “wale wanaoongoza”?

      19 Leo pia Mashahidi wa Yehova hupata baraka nyingi wanapofuata mwongozo wa “wale wanaoongoza” kati yao. (Ebr. 13:17) Kwa kuwa tamasha ya ulimwengu huu inabadilika, Wakristo wanapaswa kukubali na kujitiisha chini ya mwongozo wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45; 1 Kor. 7:29-31) Tukifanya hivyo tutaepuka madhara ya kiroho na kubaki bila doa kutokana na ulimwengu.​—Yak. 1:27.

      20 Waangalizi Wakristo leo kutia ndani washiriki wa Baraza Linaloongoza si wakamilifu kama walivyokuwa Paulo, Barnaba, Marko na wazee wengine watiwa mafuta wa karne ya kwanza. (Rom. 5:12; Yak. 3:2) Hata hivyo, Baraza Linaloongoza linategemeka kwa sababu linashikamana kabisa na Neno la Mungu na kufuata mfano uliowekwa na mitume. (2 Tim. 1:13, 14) Matokeo ni kwamba makutaniko yanatiwa nguvu na kuimarishwa katika imani.

      TIMOTHEO ATUMIKA “KATIKA KUENDELEZA HABARI NJEMA”

      Paulo alithamini sana kazi nzuri iliyofanywa na Timotheo. Baada ya kufanya kazi pamoja kwa miaka 11 hivi, Paulo aliandika hivi kuhusu Timotheo: “Sina mtu mwingine aliye na mwelekeo kama wake atakayejali kwa unyoofu mahangaiko yenu. . . . Ninyi mnajua jinsi alivyojithibitisha mwenyewe, kwamba kama mtoto na baba yake alitumikia pamoja nami katika kuendeleza habari njema.” (Flp. 2:20, 22) Timotheo alijitolea ili kuendeleza kazi ya kuhubiri, na kwa sababu hiyo Paulo alimpenda sana naye ni mfano mzuri sana kwetu.

      Timotheo.

      Inaonekana kwamba Timotheo, ambaye baba yake alikuwa Mgiriki na mama yake Myahudi, alilelewa Listra. Tangu utotoni, Timotheo alikuwa amefundishwa Maandiko na mama yake, Eunike, na nyanya yake Loisi. (Mdo. 16:1, 3; 2 Tim. 1:5; 3:14, 15) Huenda Eunike, Loisi, na Timotheo walikubali kuwa Wakristo, Paulo alipotembelea Listra kwa mara ya kwanza.

      Paulo aliporudi miaka kadhaa baadaye, Timotheo, ambaye huenda alikuwa na umri wa miaka 20 hivi wakati huo, “alishuhudiwa vema na akina ndugu huko Listra na Ikoniamu.” (Mdo. 16:2) Roho ya Mungu iliongoza kutolewa kwa “unabii” kumhusu kijana huyo, na kulingana na unabii huo, Paulo na wazee wengine walipendekeza Timotheo afanye utumishi wa pekee. (1 Tim. 1:18; 4:14; 2 Tim. 1:6) Alipaswa kwenda pamoja na Paulo akiwa mmishonari. Timotheo angeiacha familia yao na pia alikubali kutahiriwa ili Wayahudi wasiwe na sababu yoyote ya kulalamika.​—Mdo. 16:3.

      Timotheo alisafiri sana. Alihubiri pamoja na Paulo na Sila huko Filipi, halafu akahubiri Beroya akiwa na Sila, kisha akahubiri Thesalonike akiwa peke yake. Walipokutana tena katika jiji la Korintho, Timotheo alimjulisha Paulo kuhusu upendo na uaminifu wa Wathesalonike licha ya dhiki walizokabili. (Mdo. 16:6–17:14; 1 The. 3:2-6) Paulo aliposikia habari mbaya kuhusu kutaniko la Korintho, alifikiria kumtuma Timotheo aende Korintho ili akawasaidie. (1 Kor. 4:17) Baadaye, Paulo akiwa Efeso aliwatuma Timotheo na Erasto waende Makedonia. Paulo aliwaandikia Waroma akiwa Korintho na alikuwa pamoja na Timotheo, aliyekuwa amerudi tena Korintho. (Mdo. 19:22; Rom. 16:21) Hayo ni baadhi ya maeneo ambayo Timotheo alienda ili kutimiza migawo yake.

      Inaonekana kwamba Timotheo alisita kwa kiasi fulani kutumia mamlaka yake, ndiyo sababu Paulo alimtia moyo hivi: “Usiruhusu kamwe mtu yeyote audharau ujana wako.” (1 Tim. 4:12) Hata hivyo, Paulo alimwamini Timotheo naye alimtuma aende katika kutaniko lililokuwa na matatizo na kumwagiza: “Uwaamuru watu fulani wasifundishe mambo tofauti.” (1 Tim. 1:3) Pia, Paulo alimpa Timotheo mamlaka ya kuwaweka rasmi waangalizi na watumishi wa huduma katika makutaniko.​—1 Tim. 5:22.

      Paulo alimpenda sana Timotheo kwa sababu ya sifa zake nzuri. Maandiko yanaonyesha kwamba kijana huyo alikuwa kama mwana kwa sababu alishirikiana na Paulo kwa ukaribu, uaminifu na kwa upendo. Paulo aliandika kwamba anakumbuka machozi ya Timotheo, anatamani kumwona, na anasali kwa ajili yake. Pia, akiwa kama baba mwenye kujali, Paulo alimpa Timotheo ushauri kuhusu ‘ugonjwa wake wa mara kwa mara’​—huenda ulikuwa ugonjwa wa tumbo.​—1 Tim. 5:23; 2 Tim. 1:3, 4.

      Paulo alipofungwa kwa mara ya kwanza huko Roma, Timotheo alikuwa pamoja naye. Timotheo pia alifungwa kwa muda fulani. (Flm. 1; Ebr. 13:23) Ni wazi kwamba wanaume hao walipendana kikweli, kwa sababu Paulo alipotambua kwamba anakaribia kufa, alimtumia Timotheo ujumbe huu: “Jitahidi kabisa ili uje kwangu upesi.” (2 Tim. 4:6-9) Maandiko hayasemi ikiwa Timotheo alifika kabla ya Paulo kufa, na kumwona tena mshauri wake mpendwa.

      MARKO APATA MAPENDELEO MENGI

      Injili ya Marko inasimulia kwamba wale waliomkamata Yesu walijaribu pia kumkamata “kijana fulani” aliyeponyoka, “akakimbia akiwa uchi.” (Marko 14:51, 52) Kwa kuwa Marko, ambaye pia anaitwa Yohana Marko, ndiye peke yake aliyeandika kuhusu tukio hilo, huenda kijana huyo ni yeye mwenyewe. Ikiwa ndivyo, basi Marko alikuwa amekutana kibinafsi na Yesu.

      Marko akisikiliza na kuandika mwanamume mzee anapoongea.

      Miaka 11 hivi baadaye, Herode Agripa alipokuwa akiwatesa Wakristo, “watu wengi” waliokuwa washiriki wa kutaniko la Yerusalemu walikuwa wamekusanyika katika nyumba ya Maria, mama ya Marko, wakisali. Petro alienda katika nyumba hiyo alipofunguliwa kimuujiza kutoka gerezani. (Mdo. 12:12) Hivyo, inawezekana kwamba Marko alilelewa katika nyumba ambayo baadaye ilitumiwa kwa ajili ya mikutano ya Kikristo. Huenda aliwafahamu wanafunzi wa mwanzoni wa Yesu, nao walimsaidia sana kufanya maendeleo ya kiroho.

      Marko alitumikia bega kwa bega na waangalizi kadhaa wa kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza. Inaonekana mgawo wake wa kwanza ulikuwa katika jiji la Antiokia ya Siria alipotumikia pamoja na binamu yake, Barnaba, na mtume Paulo. (Mdo. 12:25) Barnaba na Paulo walipoanza safari yao ya kwanza ya umishonari, Marko alisafiri pamoja nao, kwanza walienda Kipro kisha Asia Ndogo. Wakiwa huko, Marko akarudi Yerusalemu kwa sababu zisizojulikana. (Mdo. 13:4, 13) Baada ya Barnaba na Paulo kutoelewana kwa sababu ya Marko, kama inavyosimuliwa katika Matendo sura ya 15, Marko na Barnaba waliendelea na kazi ya umishonari katika kisiwa cha Kipro.​—Mdo. 15:36-39.

      Inaonekana kufikia mwaka wa 60 au 61 W.K., tayari walikuwa wametatua kutoelewana kwao kwa sababu Marko anatajwa kwa mara nyingine kwamba alikuwa akitumikia pamoja na Paulo jijini Roma. Paulo aliyekuwa mfungwa katika jiji hilo, aliliandikia hivi kutaniko la Kolosai: “Aristarko, mateka mwenzangu anawatumia salamu zake, na pia Marko, binamu ya Barnaba, (ambaye mlipokea maagizo ya kumkaribisha ikiwa atakuja kwenu).” (Kol. 4:10) Kwa hiyo, Paulo alikuwa akifikiria kumtuma Yohana Marko aende Kolosai, akamwakilishe.

      Kati ya mwaka 62 na 64 hivi, Marko alitumikia pamoja na mtume Petro katika jiji la Babiloni. Kama tulivyoona katika Sura ya 10 ya kitabu hiki, walikuwa na uhusiano wa karibu, kwa kuwa Petro anamwita kijana huyo “Marko, mwanangu.”​—1 Pet. 5:13.

      Mwishowe, mwaka wa 65 W.K. hivi, mtume Paulo alipofungwa kwa mara ya pili jijini Roma, alimwandikia hivi Timotheo, mtumishi mwenzake aliyekuwa Efeso: “Mchukue Marko uje pamoja naye, kwa maana ni mwenye faida kwangu katika huduma.” (2 Tim. 4:11) Bila shaka Marko alikubali mwaliko huo na kurudi Roma. Ndiyo sababu Barnaba, Paulo, na Petro walimthamini sana kijana huyo!

      Pendeleo kubwa zaidi la Marko ni lile la kuongozwa na roho ya Yehova kuandika masimulizi ya Injili. Inaaminika kwamba Marko alipata habari nyingi kutoka kwa mtume Petro. Kuna mambo yanayounga mkono wazo hilo. Kwa mfano, masimulizi ya Marko yanataja mambo fulani hususa ambayo yangeweza kusimuliwa tu na mtu aliyejionea matukio hayo, kama vile Petro. Hata hivyo, inaonekana Marko aliandika Injili yake akiwa Roma bali si akiwa Babiloni pamoja na Petro. Marko anatumia maneno mengi ya Kilatini na kutafsiri maneno ya Kiebrania ili watu wasio Wayahudi waelewe kwa urahisi. Kwa hiyo inaonekana aliandika hasa kwa ajili ya Watu wa Mataifa.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Marko Apata Mapendeleo Mengi.”

      b Ona sanduku lenye kichwa “Timotheo Atumika ‘Kuendeleza Habari Njema’.”

  • “Vuka Uingie Makedonia”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 16

      “Vuka Uingie Makedonia”

      Baraka zinazotokana na kukubali mgawo na kuvumilia mateso kwa shangwe

      Matendo 16:6-40

      1-3. (a) Roho takatifu iliwaongozaje Paulo na wenzake? (b) Tutachunguza mambo gani?

      KIKUNDI cha wanawake kinaondoka jijini Filipi, huko Makedonia. Baada ya muda mfupi wanawake hao wanafika kwenye mto mdogo unaoitwa Gangites. Kama ilivyo desturi yao, wanaketi kwenye ukingo wa mto huo ili kusali kwa Mungu wa Israeli. Yehova anaona wanalofanya.​—2 Nya. 16:9; Zab. 65:2.

      2 Wakati huohuo, zaidi ya kilomita 800 upande wa mashariki wa Filipi, kikundi cha wanaume kinaondoka katika jiji la Listra, lililo upande wa kusini mwa Galatia. Siku kadhaa baadaye, wanaume hao wanafika kwenye barabara kuu ya Roma inayoelekea upande wa magharibi katika eneo la wilaya ya Asia lenye idadi kubwa zaidi ya watu. Wanaume hao—Paulo, Sila, na Timotheo—wana hamu ya kutembelea Efeso na miji mingine ambayo maelfu ya watu wanahitaji kusikia kumhusu Kristo. Lakini, kabla ya kuondoka, roho takatifu inawazuia kwa njia fulani. Wanazuiwa kuhubiri Asia. Kwa nini? Kwa sababu Yesu anatumia roho ya Mungu kukiongoza kikundi hicho cha Paulo kupitia Asia Ndogo na kuvuka Bahari ya Aegea ili kwenda kwenye kingo za mto huo mdogo unaoitwa Gangites.

      3 Tunaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na jinsi Yesu alivyowaongoza Paulo na wenzake katika safari hiyo ya pekee ya kwenda Makedonia. Kwa hiyo, tuchunguze mambo fulani yaliyotukia katika safari hii ya pili ya Paulo ya umishonari, iliyoanza mwaka wa 49 hivi W.K.

      “Mungu Alikuwa Ametuita” (Mdo. 16:6-15)

      4, 5. (a) Ni nini kilichotokea Paulo na wenzake walipokaribia Bithinia? (b) Wanafunzi hao waliamua kufanya nini, na matokeo yalikuwa nini?

      4 Walipozuiwa kuhubiri Asia, Paulo na wenzake walienda upande wa kaskazini ili kuhubiri katika majiji ya Bithinia. Huenda walitembea kwa siku kadhaa kwenye vijia katika maeneo yasiyo na watu wengi ya Frigia na Galatia ili wafike huko. Hata hivyo, walipokaribia Bithinia, Yesu alitumia tena roho takatifu kuwazuia. (Mdo. 16:6, 7) Kufikia wakati huo, huenda wanaume hao hawakuelewa wafanye nini. Walikuwa na ujumbe wa kuhubiri, walijua jinsi ya kuhubiri, lakini hawakujua mahali pa kuhubiri. Ni kana kwamba walikuwa wamepiga hodi kwenye mlango wa kuingia Asia, lakini hawakuruhusiwa kuingia. Walipiga hodi kwenye mlango wa kuingia Bithinia, na hapo pia, hawakuruhusiwa kuingia. Paulo alikuwa ameazimia kuendelea kupiga hodi mpaka apate mlango utakaofunguka. Kisha, wanaume hao wakafanya uamuzi ambao huenda ukaonekana kuwa usiopatana na akili. Waliamua kwenda upande wa magharibi na kutembea kilomita 550, wakipita majiji mengi mpaka wakafika bandari ya Troa, ambako wangeweza kusafiri baharini kwenda Makedonia. (Mdo. 16:8) Naam, kwa mara ya tatu, Paulo alipiga hodi na mlango ukafunguka wazi kabisa.

      5 Luka, mwandishi wa Injili, aliyejiunga na Paulo na wenzake huko Troa, aliandika kilichotokea: “Paulo akaona maono usiku—mwanamume Mmakedonia alikuwa amesimama hapo akimsihi: “Vuka uingie Makedonia utusaidie.” Mara tu alipoona maono hayo, tukajaribu kuingia Makedonia, tukikata kauli kwamba Mungu alikuwa ametuita tuwatangazie habari njema.”a (Mdo. 16:9, 10) Sasa, Paulo alijua mahali pa kuhubiri. Bila shaka alifurahi sana kwa sababu hakukata tamaa alipokuwa njiani! Mara moja, wanaume hao wanne wakasafiri kwa mashua kwenda Makedonia.

      Mtume Paulo na Timotheo wakiwa wamesimama kwenye meli. Timotheo akionyesha kitu fulani kilicho mbali huku wafanyakazi wa meli wakiendelea na kazi.

      “Basi tukatoka Troa na kusafiri . . . baharini.”—Matendo 16:11

      6, 7. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo yaliyotokea katika safari ya Paulo? (b) Tunaweza kuwa na uhakika gani kutokana na mambo yaliyompata Paulo?

      6 Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi hayo? Kumbuka jambo hili: Roho ya Mungu iliingilia kati baada ya Paulo kufunga safari kwenda Asia. Yesu aliingilia kati baada ya Paulo kukaribia Bithinia. Na Yesu alimwelekeza Paulo aende Makedonia, baada ya Paulo kufika Troa. Yesu akiwa Kichwa cha kutaniko anaweza kutuongoza kwa njia kama hiyo pia. (Kol. 1:18) Kwa mfano, huenda tumefikiria kuwa mapainia au kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Hata hivyo, Yesu anaweza kutumia roho ya Mungu kutuongoza baada ya sisi kuchukua hatua zinazohitajika ili kutimiza malengo yetu. Kwa nini? Fikiria mfano huu: Dereva anaweza kuongoza gari kuelekea upande wa kushoto au kulia likiwa mwendoni, lakini hawezi kufanya hivyo ikiwa gari hilo limesimama. Vivyo hivyo, Yesu hutusaidia kupanua utumishi wetu, ikiwa tuko mwendoni, yaani, tunajitahidi kabisa kufikia malengo yetu.

      7 Tufanye nini ikiwa mwanzoni hatupati matokeo yoyote? Je, tukate tamaa tukifikiri kwamba hatuna roho ya Mungu? Hapana. Kumbuka kwamba haikuwa rahisi pia kwa Paulo kufikia malengo yake. Lakini aliendelea kutafuta mpaka alipopata mlango uliofunguka. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu tukivumilia na kuendelea kutafuta “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.”​—1 Kor. 16:9.

      8. (a) Filipi lilikuwa jiji la aina gani? (b) Ni jambo gani lenye kufurahisha lililotokea baada ya Paulo kuhubiri “mahali pa sala”?

      8 Baada ya kufika wilaya ya Makedonia, Paulo na wenzake walielekea Filipi, jiji lenye wakaaji waliojivunia kuwa raia wa Roma. Askari-jeshi Waroma waliostaafu waliishi huko na waliona jiji hilo kuwa Italia ndogo, Roma ndogo ya Makedonia. Wakiwa nje ya lango la jiji, kando ya mto mwembamba, wamishonari hao walifika katika eneo ambalo walifikiri ni “mahali pa sala.”b Walipoenda huko siku ya Sabato, waliwakuta wanawake kadhaa waliokuwa wamekusanyika hapo ili kumwabudu Mungu. Wanafunzi hao wakaketi chini na kuzungumza nao. Mwanamke aliyeitwa Lidia “alikuwa akisikiliza, na Yehova akaufungua moyo wake.” Lidia alichochewa sana na mambo aliyojifunza kutoka kwa wamishonari hao hivi kwamba yeye na watu wa nyumba yake wakabatizwa. Kisha, Lidia akamsihi Paulo na wenzake wakae nyumbani kwake.c—Mdo. 16:13-15.

      9. Wengi leo wanafuata mfano wa Paulo jinsi gani, na wamepata baraka gani?

      9 Wazia shangwe iliyotokea Lidia alipobatizwa! Bila shaka Paulo alifurahi sana kwamba alikubali mwaliko wa ‘kuvuka na kuingia Makedonia’ na Yehova aliona inafaa kumtumia yeye na wenzake kujibu sala za wanawake hao wanaomwogopa Mungu! Leo, ndugu na dada wengi, vijana kwa wazee, waliofunga ndoa kwa waseja, uhamia maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Ni kweli kwamba kuna hali nyingi ngumu, hata hivyo, haziwezi kulinganishwa na uradhi unaotokana na kuwapata watu kama Lidia, ambao hukubali kweli za Biblia. Je, unaweza kufanya marekebisho ili ‘uvuke na kuingia’ katika eneo lenye uhitaji? Utapata baraka nyingi. Kwa mfano, mfikirie Aaron, ndugu mwenye umri wa miaka 20 hivi, ambaye alihamia nchi moja ya Amerika ya Kati. Maoni yake yanafanana na ya wengi, anaposema: “Kutumikia nchi ya kigeni kumenisaidia kukua kiroho na kumkaribia Yehova zaidi. Na utumishi wa shambani unafurahisha—ninaongoza mafunzo nane ya Biblia!”

      Dada wawili wakimhubiria mwanamke mtaani. Kijana anajaribu kuangalia ili aone wanachozungumzia.

      Tunawezaje ‘kuvuka na kuingia Makedonia?’

      “Umati Ukasimama . . . Dhidi Yao” (Mdo. 16:16-24)

      10. Roho waovu walijaribu kuzuia kazi ya Paulo na wenzake jinsi gani?

      10 Shetani alikasirika sana kuona watu wakijifunza habari njema na kubatizwa katika eneo ambalo yeye na roho wake waovu hawakuwa na upinzani. Si ajabu kwamba roho waovu walihusika kusababisha kipingamizi katika kazi ya kuhubiri ya Paulo na wenzake! Walipokuwa wakienda mahali pale pa kusali, kijakazi fulani mwenye roho mwovu, aliyewapatia mabwana zake faida nyingi kwa kubashiri, alikuwa akimfuata Paulo na wenzake na kusema kwa sauti kubwa: “Watu hawa ni watumwa wa Mungu Aliye Juu Zaidi nao wanawatangazia ninyi njia ya wokovu.” Huenda roho huyo mwovu alimfanya msichana huyo aseme maneno hayo ili ionekane kana kwamba mabashiri yake na mafundisho ya Paulo yanatoka katika chanzo kimoja. Kwa kufanya hivyo, watazamaji wangekengeushwa wasiwasikilize wafuasi wa kweli wa Kristo. Lakini Paulo alimnyamazisha msichana huyo kwa kumfukuza roho huyo mwovu.​—Mdo. 16:16-18.

      11. Baada ya roho mwovu kufukuzwa, ni nini kilichowapata Paulo na Sila?

      11 Mabwana wa kijakazi huyo walipoona kwamba njia yao ya kupata faida imetoweka, wakakasirika sana. Wakawakamata Paulo na Sila na kuwapeleka sokoni, mahali ambapo mahakimu—maofisa wanaowakilisha Roma—walikuwa wakihukumu. Kwa kuwa mabwana hao walijua kwamba mahakimu waliwachukia Wayahudi na walijivunia kuwa Waroma, walitoa madai yanayoonyesha kuwa Paulo na Sila wanasumbua. Ni kana kwamba walisema: ‘Wayahudi hawa wanasumbua kwa kufundisha mapokeo ambayo sisi Waroma hatuwezi kuyakubali.’ Matokeo ya maneno yao yalionekana mara moja. “Umati [uliokuwa sokoni] ukasimama pamoja dhidi yao [Paulo na Sila],” nao mahakimu wakatoa amri “wapigwe kwa fimbo.” Kisha, Paulo na Sila wakapelekwa gerezani. Mlinzi akawatupa ndani ya gereza la ndani zaidi na kuifunga miguu yao katika mikatale. (Mdo. 16:19-24) Mlinzi huyo alipoufunga mlango wa gereza, kulikuwa giza zito hivi kwamba Paulo na Sila hawangeweza kuonana. Hata hivyo, Yehova alikuwa akitazama.​—Zab. 139:12.

      12. (a) Wanafunzi wa Kristo waliyaonaje mateso na kwa nini? (b) Shetani na wale walio chini ya uvutano wake wanawapingaje wafuasi wa Kristo leo?

      12 Miaka kadhaa iliyotangulia, Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Watawatesa ninyi.” (Yoh. 15:20) Hivyo, Paulo na wenzake walipovuka ili kuingia Makedonia, walitarajia kukabili upinzani. Walipoanza kuteswa walijua kwamba ni kwa sababu ya hasira ya Shetani na haimaanishi walipoteza kibali cha Yehova. Leo, watu walio chini ya uvutano wa Shetani wanatenda kama watu waliompinga Paulo katika jiji la Filipi. Tukiwa shuleni au kazini, wapinzani hao wasio wanyoofu husema mambo yalipotoka kutuhusu ili kuwachochea wengine watupinge. Katika nchi fulani, wapinzani wa kidini wanatushtaki mahakamani, ni kana kwamba wanasema: ‘Mashahidi hawa wanasumbua kwa kufundisha mapokeo ambayo sisi “waumini wa zamani” hatuwezi kuyakubali.’ Katika maeneo mengine, waabudu wenzetu hupigwa na kutupwa gerezani. Hata hivyo, Yehova anatazama.​—1 Pet. 3:12.

      “Wakabatizwa Bila Kukawia” (Mdo. 16:25-34)

      13. Kwa nini mlinzi aliuliza: “Nifanye nini ili niokolewe?”

      13 Paulo na Sila walihitaji wakati wa kutafakari mambo yaliyowapata. Hata hivyo, kufikia usiku wa manane, walijihisi nafuu kutokana na maumivu hivi kwamba “walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo.” Kisha, ghafla, tetemeko la ardhi likatikisa gereza! Mlinzi akaamka, na alipoona milango ya gereza imefunguka, akafikiri wafungwa wametoroka. Akijua kwamba ataadhibiwa kwa kuwaacha wafungwa watoroke, “akauchomoa upanga wake naye karibu ajiue.” Lakini Paulo akamwambia kwa sauti kubwa: “Usijiumize, kwa maana sisi sote tupo hapa!” Mlinzi huyo mwenye wasiwasi akauliza: “Mabwana zangu, nifanye nini ili niokolewe?” Paulo na Sila hawangeweza kumwokoa lakini Yesu pekee angeweza. Kwa hiyo, wakamjibu: “Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokolewa.”​—Mdo. 16:25-31.

      14. (a) Paulo na Sila walimsaidiaje mlinzi wa jela? (b) Paulo na Sila walipata baraka gani kwa kuvumilia mateso kwa shangwe?

      14 Je, mlinzi huyo aliuliza swali hilo kwa unyoofu? Paulo hakutilia shaka unyoofu wake. Mlinzi huyo alikuwa Mtu wa Mataifa, asiyejua Maandiko. Kabla ya kuwa Mkristo, alihitaji kujifunza na kukubali kweli za msingi za Maandiko. Hivyo, Paulo na Sila walitumia wakati ‘kumhubiria neno la Yehova.’ Kwa kuwa walikazia fikira kumfundisha mtu huyo Maandiko huenda walisahau maumivu waliyokuwa nayo. Hata hivyo, mlinzi huyo aliona vidonda migongoni mwao, naye akaviosha. Kisha yeye na familia yake “wakabatizwa bila kukawia.” Paulo na Sila walipata baraka kubwa sana kwa kuvumilia mateso kwa shangwe!—Mdo. 16:32-34.

      15. (a) Mashahidi wengi leo wanafuata mfano wa Paulo na Sila jinsi gani? (b) Kwa nini tuwatembelee tena na tena watu wanaoishi katika eneo letu?

      15 Kama Paulo na Sila, leo, Mashahidi wengi waliofungwa kwa sababu ya imani yao wamepata matokeo mazuri kwa kuhubiri habari njema wakiwa gerezani. Kwa mfano, wakati mmoja kulikuwa na asilimia 40 ya Mashahidi waliojifunza ukweli kumhusu Yehova wakiwa gerezani katika nchi moja ambayo utendaji wetu ulipigwa marufuku. (Isa. 54:17) Pia, kumbuka kwamba mlinzi huyo aliomba msaada baada ya tetemeko la ardhi. Vivyo hivyo, watu fulani leo ambao hawajawahi kukubali ujumbe wa Ufalme huenda wakaukubali baada tu ya ulimwengu wao kutikiswa na jambo fulani lenye kuhuzunisha. Kuwarudia tena na tena watu wanaoishi katika eneo letu, huonyesha kwamba tuko tayari kutoa msaada wakati wowote unapohitajika.

      “Je, Sasa Wanatufukuza kwa Siri?” (Mdo. 16:35-40)

      16. Ni nini kilichotokea siku moja baada ya Paulo na Sila kupigwa viboko?

      16 Siku iliyofuata mahakimu waliamuru Paulo na Sila wafunguliwe. Lakini Paulo akasema: “Walitupiga viboko hadharani bila kutuhukumu, ingawa sisi ni Waroma, na wakatutupa gerezani. Je, sasa wanatufukuza kwa siri? Hapana, haiwezekani! Acha waje watutoe nje wao wenyewe.” Baada ya kutambua kwamba wanaume hao wawili ni raia wa Roma, mahakimu hao “wakaogopa,” kwa sababu walikuwa wamekiuka haki zao.d Mambo yakageuka. Wanafunzi hao walipigwa viboko hadharani; sasa mahakimu walilazimika kuwaomba msamaha hadharani. Wakawasihi Paulo na Sila waondoke Filipi. Walikubali, lakini kwanza wakakitia moyo kikundi kipya cha wanafunzi kilichokuwa kikikua. Kisha wakaondoka.

      17. Uvumilivu wa Paulo na Sila ungeweza kuwafundisha nini wanafunzi wapya?

      17 Ikiwa Paulo na Sila wangesema mwanzoni kwamba wao ni raia wa Roma, huenda hawangepigwa viboko. (Mdo. 22:25, 26) Hata hivyo, huenda wanafunzi wa Filipi wangefikiri kwamba Paulo na Sila walitumia uraia wao kuepuka kuteseka kwa ajili ya Kristo. Kufanya hivyo kungeathirije imani ya wanafunzi ambao hawakuwa raia wa Roma? Sheria haingewazuia wao wasipigwe viboko. Hivyo, kwa kuvumilia adhabu ya viboko Paulo na mwenzake waliwawekea waabudu hao wapya kielelezo kwamba wafuasi wa Kristo wanaweza kusimama imara licha ya mateso. Isitoshe, kwa kusisitiza uraia wao utambuliwe, Paulo na Sila walitaka ijulikane hadharani kwamba mahakimu hao wametenda kinyume cha sheria. Kufanya hivyo kungeweza kuwazuia wasiwatendee vibaya waamini wengine na badala yake kuwapa ulinzi wa kisheria mashambulizi kama hayo yatakapotokea wakati ujao.

      18. (a) Waangalizi Wakristo leo hufuata kielelezo cha Paulo jinsi gani? (b) Tunawezaje “kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema?”

      18 Leo, waangalizi katika kutaniko la Kikristo huliwekea kutaniko kielelezo cha kufuata. Chochote wanachotazamia waabudu wenzao wafanye, Wachungaji hao Wakristo wako tayari kufanya. Kama Paulo, sisi pia huchunguza mambo kwa uangalifu kabla ya kutumia haki zetu za kisheria. Ikihitajika, sisi hukata rufaa katika mahakama za kitaifa na hata za kimataifa ili kutetea uhuru wetu wa ibada. Tunapofanya hivyo, lengo letu si kuleta mapinduzi ya kijamii, bali “kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema” kama Paulo alivyoliandikia kutaniko la Filipi miaka kumi hivi baada ya kufungwa huko. (Flp. 1:7) Hata mahakama itoe uamuzi gani, tumeazimia kuendelea ‘kutangaza habari njema’ popote ambapo roho ya Mungu itatuongoza kama Paulo na wenzake walivyofanya.​—Mdo. 16:10.

      LUKA—MWANDISHI WA KITABU CHA MATENDO

      Kuanzia sura ya 1 hadi sura ya 16 mstari wa 9 wa kitabu cha Matendo, mwandishi wa kitabu cha matendo anazungumzia mambo ambayo wengine wanasema na kufanya. Hata hivyo, kuanzia Matendo 16:10, 11, mtindo wa uandikaji unabadilika. Kwa mfano, katika mstari wa 11, mwandishi anasema: “Tukatoka Troa na kusafiri moja kwa moja baharini hadi Samothrake.” Hapa ndipo mwandishi Luka, alianza kujihusisha katika matukio yanayosimuliwa. Hata hivyo, kwa kuwa jina la Luka halipatikani mahali popote katika kitabu cha Matendo ya Mitume, tunajuaje kwamba yeye ndiye mwandishi wa kitabu hicho?

      Luka amekaa akiandika kwenye kitabu cha kukunjwa kilicho mezani.

      Tunaweza kupata jibu kwa kuchunguza utangulizi wa kitabu cha Matendo na Injili ya Luka. Utangulizi wa vitabu vyote viwili unataja mtu anayeitwa “Theofilo.” (Luka 1:1, 3; Mdo. 1:1) Utangulizi wa kitabu cha Matendo unasema: “Lile simulizi la kwanza, ewe Theofilo, niliandika kuhusu mambo yote ambayo Yesu alianza kufanya na kufundisha.” Kwa kuwa wasomi wenye kutegemeka wamekubali kwa muda mrefu kwamba “lile simulizi la kwanza,” yaani, Injili, liliandikwa na Luka, basi lazima pia aliandika kitabu cha Matendo.

      Hatujui mengi kumhusu Luka. Jina lake linapatikana mara tatu tu katika Biblia. Mtume Paulo anamwita Luka “daktari mpendwa” na ‘mfanyakazi mwenzake.’ (Kol. 4:14; Flm. 24) Sehemu za kitabu cha Matendo ambazo Luka anajihusisha katika masimulizi zinaonyesha kwamba Luka alisafiri pamoja na mtume Paulo kutoka Troa mpaka Filipi mwaka wa 50 W.K. hivi, lakini Paulo alipoondoka Filipi, Luka hakusafiri pamoja naye. Wanaume hao wawili walikutana tena Filipi mwaka wa 56 W.K. hivi na kusafiri pamoja na ndugu wengine saba kutoka Filipi kwenda Yerusalemu, ambapo Paulo alikamatwa. Miaka miwili baadaye, Luka alisafiri pamoja na Paulo, akiwa mfungwa, kutoka Kaisaria kwenda Roma. (Mdo. 16:10-17, 40; 20:5–21:17; 24:27; 27:1–28:16) Paulo alifungwa Roma kwa mara ya pili, na hata alipotambua kwamba anakaribia kuuawa, ni “Luka tu” ndiye aliyekuwa pamoja naye. (2 Tim. 4:6, 11) Ni wazi kwamba Luka alisafiri maeneo ya mbali na alikuwa tayari kuteseka kwa ajili ya habari njema.

      Luka hakudai kwamba alijionea mambo aliyoandika kumhusu Yesu. Badala yake, anasema kwamba alijitahidi ‘kukusanya habari kuhusu mambo aliyosadiki kabisa’ yaliyosimuliwa na “mashahidi wa kujionea.” Anaendelea kusema, “nimefuatilia mambo yote kwa usahihi tangu mwanzo, nami nimeamua kukuandikia mambo hayo kwa utaratibu mzuri.” (Luka 1:1-3) Kitabu cha Luka kinaonyesha wazi kwamba alifanya utafiti kwa makini. Huenda alimhoji Elisabeti, Maria, mama ya Yesu, na wengine ili kukusanya habari za kuandika. Mambo mengi aliyoandika hayapatikani katika vitabu vingine vya Injili.​—Luka 1:5-80.

      Mtume Paulo alisema kwamba Luka alikuwa daktari, na masimulizi yake ya Injili yanaonyesha wazi alihangaishwa na afya ya watu walioteseka. Kwa mfano: Luka aliandika kwamba Yesu alipomponya mtu aliyesumbuliwa na roho mwovu, “yule roho mwovu akamtoka bila kumuumiza.” Pia, aliandika kwamba mama mkwe wa mtume Petro alikuwa na “homa kali,” na kwamba mwanamke ambaye Yesu alimsaidia alisumbuliwa na “roho ya udhaifu kwa miaka 18, mwili wake ulikuwa umepindika na hangeweza kusimama wima.”​—Luka 4:35, 38; 13:11.

      Luka alitanguliza “kazi ya Bwana” maishani mwake. (1 Kor. 15:58) Lengo lake lilikuwa kuwasaidia wengine wamjue na kumtumikia Yehova bali si kutafuta utajiri au umashuhuri.

      LIDIA—MUUZAJI WA BIDHAA ZA RANGI YA ZAMBARAU

      Lidia aliishi Filipi, jiji mashuhuri katika wilaya ya Makedonia. Alitoka Thiatira, jiji lililokuwa magharibi mwa Asia Ndogo katika eneo linaloitwa Lidia. Ili kuendeleza biashara yake, Lidia alihamia eneo la ng’ambo ya Bahari ya Aegea. Inawezekana aliuza bidhaa mbalimbali za rangi ya zambarau, kama vile mazulia, mapambo, vitambaa, na hata rangi yenyewe. Maandishi yaliyopatikana Filipi yanathibitisha kwamba kulikuwa na kikundi cha wauzaji wa bidhaa za zambarau katika jiji hilo.

      Lidia akionyesha kitambaa.

      Kwa kuwa Lidia anatajwa kuwa “mwabudu wa Mungu,” huenda aligeuzwa imani na kuwa mfuasi wa dini ya Kiyahudi. (Mdo. 16:14) Inawezekana alikuwa amepata habari fulani kuhusu ibada ya Yehova katika jiji la nyumbani kwao. Tofauti na Filipi, jiji la kwao lilikuwa na sinagogi la Wayahudi. Watu fulani wanaamini kwamba Lidia lilikuwa jina la utani—linalomaanisha “Mwanamke kutoka Lidia”​—ambalo alipewa alipokuwa Filipi. Hata hivyo, kuna uthibitisho unaoonyesha kwamba kulikuwa na wanawake wengine walioitwa Lidia.

      Tangu siku za Homer, katika karne ya tisa au nane K.W.K., watu wa Lidia na majirani zao walijulikana kwa ustadi wao wa kutia rangi ya zambarau kwenye vitambaa. Maji ya Thiatira yalijulikana kwa kutokeza “rangi nyangavu na zinazodumu sana.”

      Bidhaa za zambarau zilikuwa ghali sana na zingeweza kununuliwa na matajiri tu. Ingawa rangi ya zambarau ingeweza kupatikana kutoka katika vitu mbalimbali, rangi bora na iliyokuwa ghali zaidi—iliyowekwa kwenye vitambaa laini—ilitokana na samaki-gamba wa Mediterania. Kila samaki angeweza kutokeza tone moja tu la rangi hiyo, na ili kupata gramu moja ya rangi hiyo ya pekee, samaki 8,000 hivi walihitajika. Ndiyo sababu nguo za rangi hiyo zilikuwa ghali sana.

      Inawezekana Lidia alikuwa mfanyabiashara tajiri kwa sababu biashara yake ilihitaji awe na pesa nyingi na pia alikuwa na nyumba kubwa ambapo Paulo, Sila, Timotheo, na Luka wangeweza kukaa. Biblia inataja “watu wa nyumbani mwake,” huenda alikuwa anaishi na watu wake wa ukoo, au alikuwa na vijakazi na watumishi. (Mdo. 16:15) Na kwa kuwa kabla ya kuondoka katika jiji hilo, Paulo na Sila walikutana na ndugu kadhaa katika nyumba ya mwanamke huyo mkarimu, inawezekana kwamba baadaye nyumba hiyo ilikuwa mahali ambapo Wakristo wa kwanza katika jiji la Filipi walikutana kwa ajili ya ibada.​—Mdo. 16:40.

      Miaka kumi baadaye, Paulo alipoliandikia barua kutaniko la Filipi, hakumtaja Lidia. Kwa hiyo habari pekee tulizo nazo kumhusu ni zile zinazopatikana katika sura ya 16 ya kitabu cha Matendo.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Luka—Mwandishi wa Kitabu cha Matendo.”

      b Huenda Wayahudi hawakuruhusiwa kuwa na sinagogi katika jiji la Filipi kwa sababu lilikuwa jiji la kijeshi. Au labda jiji hilo halikuwa na angalau wanaume kumi Wayahudi—idadi ya chini zaidi iliyohitajiwa ili kuwa na sinagogi.

      c Ona sanduku lenye kichwa “Lidia—Muuzaji wa Bidhaa za Rangi ya Zambarau.”

      d Kulingana na sheria ya Roma, raia alikuwa na haki ya kusikilizwa kabla ya kuhukumiwa naye hakupaswa kamwe kuadhibiwa hadharani kabla ya kuthibitishwa kuwa mwenye hatia.

  • “Vuka Uingie Makedonia”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 16

      “Vuka Uingie Makedonia”

      Baraka zinazotokana na kukubali mgawo na kuvumilia mateso kwa shangwe

      Matendo 16:6-40

      1-3. (a) Roho takatifu iliwaongozaje Paulo na wenzake? (b) Tutachunguza mambo gani?

      KIKUNDI cha wanawake kinaondoka jijini Filipi, huko Makedonia. Baada ya muda mfupi wanawake hao wanafika kwenye mto mdogo unaoitwa Gangites. Kama ilivyo desturi yao, wanaketi kwenye ukingo wa mto huo ili kusali kwa Mungu wa Israeli. Yehova anaona wanalofanya.​—2 Nya. 16:9; Zab. 65:2.

      2 Wakati huohuo, zaidi ya kilomita 800 upande wa mashariki wa Filipi, kikundi cha wanaume kinaondoka katika jiji la Listra, lililo upande wa kusini mwa Galatia. Siku kadhaa baadaye, wanaume hao wanafika kwenye barabara kuu ya Roma inayoelekea upande wa magharibi katika eneo la wilaya ya Asia lenye idadi kubwa zaidi ya watu. Wanaume hao—Paulo, Sila, na Timotheo—wana hamu ya kutembelea Efeso na miji mingine ambayo maelfu ya watu wanahitaji kusikia kumhusu Kristo. Lakini, kabla ya kuondoka, roho takatifu inawazuia kwa njia fulani. Wanazuiwa kuhubiri Asia. Kwa nini? Kwa sababu Yesu anatumia roho ya Mungu kukiongoza kikundi hicho cha Paulo kupitia Asia Ndogo na kuvuka Bahari ya Aegea ili kwenda kwenye kingo za mto huo mdogo unaoitwa Gangites.

      3 Tunaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na jinsi Yesu alivyowaongoza Paulo na wenzake katika safari hiyo ya pekee ya kwenda Makedonia. Kwa hiyo, tuchunguze mambo fulani yaliyotukia katika safari hii ya pili ya Paulo ya umishonari, iliyoanza mwaka wa 49 hivi W.K.

      “Mungu Alikuwa Ametuita” (Mdo. 16:6-15)

      4, 5. (a) Ni nini kilichotokea Paulo na wenzake walipokaribia Bithinia? (b) Wanafunzi hao waliamua kufanya nini, na matokeo yalikuwa nini?

      4 Walipozuiwa kuhubiri Asia, Paulo na wenzake walienda upande wa kaskazini ili kuhubiri katika majiji ya Bithinia. Huenda walitembea kwa siku kadhaa kwenye vijia katika maeneo yasiyo na watu wengi ya Frigia na Galatia ili wafike huko. Hata hivyo, walipokaribia Bithinia, Yesu alitumia tena roho takatifu kuwazuia. (Mdo. 16:6, 7) Kufikia wakati huo, huenda wanaume hao hawakuelewa wafanye nini. Walikuwa na ujumbe wa kuhubiri, walijua jinsi ya kuhubiri, lakini hawakujua mahali pa kuhubiri. Ni kana kwamba walikuwa wamepiga hodi kwenye mlango wa kuingia Asia, lakini hawakuruhusiwa kuingia. Walipiga hodi kwenye mlango wa kuingia Bithinia, na hapo pia, hawakuruhusiwa kuingia. Paulo alikuwa ameazimia kuendelea kupiga hodi mpaka apate mlango utakaofunguka. Kisha, wanaume hao wakafanya uamuzi ambao huenda ukaonekana kuwa usiopatana na akili. Waliamua kwenda upande wa magharibi na kutembea kilomita 550, wakipita majiji mengi mpaka wakafika bandari ya Troa, ambako wangeweza kusafiri baharini kwenda Makedonia. (Mdo. 16:8) Naam, kwa mara ya tatu, Paulo alipiga hodi na mlango ukafunguka wazi kabisa.

      5 Luka, mwandishi wa Injili, aliyejiunga na Paulo na wenzake huko Troa, aliandika kilichotokea: “Paulo akaona maono usiku—mwanamume Mmakedonia alikuwa amesimama hapo akimsihi: “Vuka uingie Makedonia utusaidie.” Mara tu alipoona maono hayo, tukajaribu kuingia Makedonia, tukikata kauli kwamba Mungu alikuwa ametuita tuwatangazie habari njema.”a (Mdo. 16:9, 10) Sasa, Paulo alijua mahali pa kuhubiri. Bila shaka alifurahi sana kwa sababu hakukata tamaa alipokuwa njiani! Mara moja, wanaume hao wanne wakasafiri kwa mashua kwenda Makedonia.

      Mtume Paulo na Timotheo wakiwa wamesimama kwenye meli. Timotheo akionyesha kitu fulani kilicho mbali huku wafanyakazi wa meli wakiendelea na kazi.

      “Basi tukatoka Troa na kusafiri . . . baharini.”—Matendo 16:11

      6, 7. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo yaliyotokea katika safari ya Paulo? (b) Tunaweza kuwa na uhakika gani kutokana na mambo yaliyompata Paulo?

      6 Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi hayo? Kumbuka jambo hili: Roho ya Mungu iliingilia kati baada ya Paulo kufunga safari kwenda Asia. Yesu aliingilia kati baada ya Paulo kukaribia Bithinia. Na Yesu alimwelekeza Paulo aende Makedonia, baada ya Paulo kufika Troa. Yesu akiwa Kichwa cha kutaniko anaweza kutuongoza kwa njia kama hiyo pia. (Kol. 1:18) Kwa mfano, huenda tumefikiria kuwa mapainia au kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Hata hivyo, Yesu anaweza kutumia roho ya Mungu kutuongoza baada ya sisi kuchukua hatua zinazohitajika ili kutimiza malengo yetu. Kwa nini? Fikiria mfano huu: Dereva anaweza kuongoza gari kuelekea upande wa kushoto au kulia likiwa mwendoni, lakini hawezi kufanya hivyo ikiwa gari hilo limesimama. Vivyo hivyo, Yesu hutusaidia kupanua utumishi wetu, ikiwa tuko mwendoni, yaani, tunajitahidi kabisa kufikia malengo yetu.

      7 Tufanye nini ikiwa mwanzoni hatupati matokeo yoyote? Je, tukate tamaa tukifikiri kwamba hatuna roho ya Mungu? Hapana. Kumbuka kwamba haikuwa rahisi pia kwa Paulo kufikia malengo yake. Lakini aliendelea kutafuta mpaka alipopata mlango uliofunguka. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu tukivumilia na kuendelea kutafuta “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.”​—1 Kor. 16:9.

      8. (a) Filipi lilikuwa jiji la aina gani? (b) Ni jambo gani lenye kufurahisha lililotokea baada ya Paulo kuhubiri “mahali pa sala”?

      8 Baada ya kufika wilaya ya Makedonia, Paulo na wenzake walielekea Filipi, jiji lenye wakaaji waliojivunia kuwa raia wa Roma. Askari-jeshi Waroma waliostaafu waliishi huko na waliona jiji hilo kuwa Italia ndogo, Roma ndogo ya Makedonia. Wakiwa nje ya lango la jiji, kando ya mto mwembamba, wamishonari hao walifika katika eneo ambalo walifikiri ni “mahali pa sala.”b Walipoenda huko siku ya Sabato, waliwakuta wanawake kadhaa waliokuwa wamekusanyika hapo ili kumwabudu Mungu. Wanafunzi hao wakaketi chini na kuzungumza nao. Mwanamke aliyeitwa Lidia “alikuwa akisikiliza, na Yehova akaufungua moyo wake.” Lidia alichochewa sana na mambo aliyojifunza kutoka kwa wamishonari hao hivi kwamba yeye na watu wa nyumba yake wakabatizwa. Kisha, Lidia akamsihi Paulo na wenzake wakae nyumbani kwake.c—Mdo. 16:13-15.

      9. Wengi leo wanafuata mfano wa Paulo jinsi gani, na wamepata baraka gani?

      9 Wazia shangwe iliyotokea Lidia alipobatizwa! Bila shaka Paulo alifurahi sana kwamba alikubali mwaliko wa ‘kuvuka na kuingia Makedonia’ na Yehova aliona inafaa kumtumia yeye na wenzake kujibu sala za wanawake hao wanaomwogopa Mungu! Leo, ndugu na dada wengi, vijana kwa wazee, waliofunga ndoa kwa waseja, uhamia maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Ni kweli kwamba kuna hali nyingi ngumu, hata hivyo, haziwezi kulinganishwa na uradhi unaotokana na kuwapata watu kama Lidia, ambao hukubali kweli za Biblia. Je, unaweza kufanya marekebisho ili ‘uvuke na kuingia’ katika eneo lenye uhitaji? Utapata baraka nyingi. Kwa mfano, mfikirie Aaron, ndugu mwenye umri wa miaka 20 hivi, ambaye alihamia nchi moja ya Amerika ya Kati. Maoni yake yanafanana na ya wengi, anaposema: “Kutumikia nchi ya kigeni kumenisaidia kukua kiroho na kumkaribia Yehova zaidi. Na utumishi wa shambani unafurahisha—ninaongoza mafunzo nane ya Biblia!”

      Dada wawili wakimhubiria mwanamke mtaani. Kijana anajaribu kuangalia ili aone wanachozungumzia.

      Tunawezaje ‘kuvuka na kuingia Makedonia?’

      “Umati Ukasimama . . . Dhidi Yao” (Mdo. 16:16-24)

      10. Roho waovu walijaribu kuzuia kazi ya Paulo na wenzake jinsi gani?

      10 Shetani alikasirika sana kuona watu wakijifunza habari njema na kubatizwa katika eneo ambalo yeye na roho wake waovu hawakuwa na upinzani. Si ajabu kwamba roho waovu walihusika kusababisha kipingamizi katika kazi ya kuhubiri ya Paulo na wenzake! Walipokuwa wakienda mahali pale pa kusali, kijakazi fulani mwenye roho mwovu, aliyewapatia mabwana zake faida nyingi kwa kubashiri, alikuwa akimfuata Paulo na wenzake na kusema kwa sauti kubwa: “Watu hawa ni watumwa wa Mungu Aliye Juu Zaidi nao wanawatangazia ninyi njia ya wokovu.” Huenda roho huyo mwovu alimfanya msichana huyo aseme maneno hayo ili ionekane kana kwamba mabashiri yake na mafundisho ya Paulo yanatoka katika chanzo kimoja. Kwa kufanya hivyo, watazamaji wangekengeushwa wasiwasikilize wafuasi wa kweli wa Kristo. Lakini Paulo alimnyamazisha msichana huyo kwa kumfukuza roho huyo mwovu.​—Mdo. 16:16-18.

      11. Baada ya roho mwovu kufukuzwa, ni nini kilichowapata Paulo na Sila?

      11 Mabwana wa kijakazi huyo walipoona kwamba njia yao ya kupata faida imetoweka, wakakasirika sana. Wakawakamata Paulo na Sila na kuwapeleka sokoni, mahali ambapo mahakimu—maofisa wanaowakilisha Roma—walikuwa wakihukumu. Kwa kuwa mabwana hao walijua kwamba mahakimu waliwachukia Wayahudi na walijivunia kuwa Waroma, walitoa madai yanayoonyesha kuwa Paulo na Sila wanasumbua. Ni kana kwamba walisema: ‘Wayahudi hawa wanasumbua kwa kufundisha mapokeo ambayo sisi Waroma hatuwezi kuyakubali.’ Matokeo ya maneno yao yalionekana mara moja. “Umati [uliokuwa sokoni] ukasimama pamoja dhidi yao [Paulo na Sila],” nao mahakimu wakatoa amri “wapigwe kwa fimbo.” Kisha, Paulo na Sila wakapelekwa gerezani. Mlinzi akawatupa ndani ya gereza la ndani zaidi na kuifunga miguu yao katika mikatale. (Mdo. 16:19-24) Mlinzi huyo alipoufunga mlango wa gereza, kulikuwa giza zito hivi kwamba Paulo na Sila hawangeweza kuonana. Hata hivyo, Yehova alikuwa akitazama.​—Zab. 139:12.

      12. (a) Wanafunzi wa Kristo waliyaonaje mateso na kwa nini? (b) Shetani na wale walio chini ya uvutano wake wanawapingaje wafuasi wa Kristo leo?

      12 Miaka kadhaa iliyotangulia, Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Watawatesa ninyi.” (Yoh. 15:20) Hivyo, Paulo na wenzake walipovuka ili kuingia Makedonia, walitarajia kukabili upinzani. Walipoanza kuteswa walijua kwamba ni kwa sababu ya hasira ya Shetani na haimaanishi walipoteza kibali cha Yehova. Leo, watu walio chini ya uvutano wa Shetani wanatenda kama watu waliompinga Paulo katika jiji la Filipi. Tukiwa shuleni au kazini, wapinzani hao wasio wanyoofu husema mambo yalipotoka kutuhusu ili kuwachochea wengine watupinge. Katika nchi fulani, wapinzani wa kidini wanatushtaki mahakamani, ni kana kwamba wanasema: ‘Mashahidi hawa wanasumbua kwa kufundisha mapokeo ambayo sisi “waumini wa zamani” hatuwezi kuyakubali.’ Katika maeneo mengine, waabudu wenzetu hupigwa na kutupwa gerezani. Hata hivyo, Yehova anatazama.​—1 Pet. 3:12.

      “Wakabatizwa Bila Kukawia” (Mdo. 16:25-34)

      13. Kwa nini mlinzi aliuliza: “Nifanye nini ili niokolewe?”

      13 Paulo na Sila walihitaji wakati wa kutafakari mambo yaliyowapata. Hata hivyo, kufikia usiku wa manane, walijihisi nafuu kutokana na maumivu hivi kwamba “walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo.” Kisha, ghafla, tetemeko la ardhi likatikisa gereza! Mlinzi akaamka, na alipoona milango ya gereza imefunguka, akafikiri wafungwa wametoroka. Akijua kwamba ataadhibiwa kwa kuwaacha wafungwa watoroke, “akauchomoa upanga wake naye karibu ajiue.” Lakini Paulo akamwambia kwa sauti kubwa: “Usijiumize, kwa maana sisi sote tupo hapa!” Mlinzi huyo mwenye wasiwasi akauliza: “Mabwana zangu, nifanye nini ili niokolewe?” Paulo na Sila hawangeweza kumwokoa lakini Yesu pekee angeweza. Kwa hiyo, wakamjibu: “Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokolewa.”​—Mdo. 16:25-31.

      14. (a) Paulo na Sila walimsaidiaje mlinzi wa jela? (b) Paulo na Sila walipata baraka gani kwa kuvumilia mateso kwa shangwe?

      14 Je, mlinzi huyo aliuliza swali hilo kwa unyoofu? Paulo hakutilia shaka unyoofu wake. Mlinzi huyo alikuwa Mtu wa Mataifa, asiyejua Maandiko. Kabla ya kuwa Mkristo, alihitaji kujifunza na kukubali kweli za msingi za Maandiko. Hivyo, Paulo na Sila walitumia wakati ‘kumhubiria neno la Yehova.’ Kwa kuwa walikazia fikira kumfundisha mtu huyo Maandiko huenda walisahau maumivu waliyokuwa nayo. Hata hivyo, mlinzi huyo aliona vidonda migongoni mwao, naye akaviosha. Kisha yeye na familia yake “wakabatizwa bila kukawia.” Paulo na Sila walipata baraka kubwa sana kwa kuvumilia mateso kwa shangwe!—Mdo. 16:32-34.

      15. (a) Mashahidi wengi leo wanafuata mfano wa Paulo na Sila jinsi gani? (b) Kwa nini tuwatembelee tena na tena watu wanaoishi katika eneo letu?

      15 Kama Paulo na Sila, leo, Mashahidi wengi waliofungwa kwa sababu ya imani yao wamepata matokeo mazuri kwa kuhubiri habari njema wakiwa gerezani. Kwa mfano, wakati mmoja kulikuwa na asilimia 40 ya Mashahidi waliojifunza ukweli kumhusu Yehova wakiwa gerezani katika nchi moja ambayo utendaji wetu ulipigwa marufuku. (Isa. 54:17) Pia, kumbuka kwamba mlinzi huyo aliomba msaada baada ya tetemeko la ardhi. Vivyo hivyo, watu fulani leo ambao hawajawahi kukubali ujumbe wa Ufalme huenda wakaukubali baada tu ya ulimwengu wao kutikiswa na jambo fulani lenye kuhuzunisha. Kuwarudia tena na tena watu wanaoishi katika eneo letu, huonyesha kwamba tuko tayari kutoa msaada wakati wowote unapohitajika.

      “Je, Sasa Wanatufukuza kwa Siri?” (Mdo. 16:35-40)

      16. Ni nini kilichotokea siku moja baada ya Paulo na Sila kupigwa viboko?

      16 Siku iliyofuata mahakimu waliamuru Paulo na Sila wafunguliwe. Lakini Paulo akasema: “Walitupiga viboko hadharani bila kutuhukumu, ingawa sisi ni Waroma, na wakatutupa gerezani. Je, sasa wanatufukuza kwa siri? Hapana, haiwezekani! Acha waje watutoe nje wao wenyewe.” Baada ya kutambua kwamba wanaume hao wawili ni raia wa Roma, mahakimu hao “wakaogopa,” kwa sababu walikuwa wamekiuka haki zao.d Mambo yakageuka. Wanafunzi hao walipigwa viboko hadharani; sasa mahakimu walilazimika kuwaomba msamaha hadharani. Wakawasihi Paulo na Sila waondoke Filipi. Walikubali, lakini kwanza wakakitia moyo kikundi kipya cha wanafunzi kilichokuwa kikikua. Kisha wakaondoka.

      17. Uvumilivu wa Paulo na Sila ungeweza kuwafundisha nini wanafunzi wapya?

      17 Ikiwa Paulo na Sila wangesema mwanzoni kwamba wao ni raia wa Roma, huenda hawangepigwa viboko. (Mdo. 22:25, 26) Hata hivyo, huenda wanafunzi wa Filipi wangefikiri kwamba Paulo na Sila walitumia uraia wao kuepuka kuteseka kwa ajili ya Kristo. Kufanya hivyo kungeathirije imani ya wanafunzi ambao hawakuwa raia wa Roma? Sheria haingewazuia wao wasipigwe viboko. Hivyo, kwa kuvumilia adhabu ya viboko Paulo na mwenzake waliwawekea waabudu hao wapya kielelezo kwamba wafuasi wa Kristo wanaweza kusimama imara licha ya mateso. Isitoshe, kwa kusisitiza uraia wao utambuliwe, Paulo na Sila walitaka ijulikane hadharani kwamba mahakimu hao wametenda kinyume cha sheria. Kufanya hivyo kungeweza kuwazuia wasiwatendee vibaya waamini wengine na badala yake kuwapa ulinzi wa kisheria mashambulizi kama hayo yatakapotokea wakati ujao.

      18. (a) Waangalizi Wakristo leo hufuata kielelezo cha Paulo jinsi gani? (b) Tunawezaje “kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema?”

      18 Leo, waangalizi katika kutaniko la Kikristo huliwekea kutaniko kielelezo cha kufuata. Chochote wanachotazamia waabudu wenzao wafanye, Wachungaji hao Wakristo wako tayari kufanya. Kama Paulo, sisi pia huchunguza mambo kwa uangalifu kabla ya kutumia haki zetu za kisheria. Ikihitajika, sisi hukata rufaa katika mahakama za kitaifa na hata za kimataifa ili kutetea uhuru wetu wa ibada. Tunapofanya hivyo, lengo letu si kuleta mapinduzi ya kijamii, bali “kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema” kama Paulo alivyoliandikia kutaniko la Filipi miaka kumi hivi baada ya kufungwa huko. (Flp. 1:7) Hata mahakama itoe uamuzi gani, tumeazimia kuendelea ‘kutangaza habari njema’ popote ambapo roho ya Mungu itatuongoza kama Paulo na wenzake walivyofanya.​—Mdo. 16:10.

      LUKA—MWANDISHI WA KITABU CHA MATENDO

      Kuanzia sura ya 1 hadi sura ya 16 mstari wa 9 wa kitabu cha Matendo, mwandishi wa kitabu cha matendo anazungumzia mambo ambayo wengine wanasema na kufanya. Hata hivyo, kuanzia Matendo 16:10, 11, mtindo wa uandikaji unabadilika. Kwa mfano, katika mstari wa 11, mwandishi anasema: “Tukatoka Troa na kusafiri moja kwa moja baharini hadi Samothrake.” Hapa ndipo mwandishi Luka, alianza kujihusisha katika matukio yanayosimuliwa. Hata hivyo, kwa kuwa jina la Luka halipatikani mahali popote katika kitabu cha Matendo ya Mitume, tunajuaje kwamba yeye ndiye mwandishi wa kitabu hicho?

      Luka amekaa akiandika kwenye kitabu cha kukunjwa kilicho mezani.

      Tunaweza kupata jibu kwa kuchunguza utangulizi wa kitabu cha Matendo na Injili ya Luka. Utangulizi wa vitabu vyote viwili unataja mtu anayeitwa “Theofilo.” (Luka 1:1, 3; Mdo. 1:1) Utangulizi wa kitabu cha Matendo unasema: “Lile simulizi la kwanza, ewe Theofilo, niliandika kuhusu mambo yote ambayo Yesu alianza kufanya na kufundisha.” Kwa kuwa wasomi wenye kutegemeka wamekubali kwa muda mrefu kwamba “lile simulizi la kwanza,” yaani, Injili, liliandikwa na Luka, basi lazima pia aliandika kitabu cha Matendo.

      Hatujui mengi kumhusu Luka. Jina lake linapatikana mara tatu tu katika Biblia. Mtume Paulo anamwita Luka “daktari mpendwa” na ‘mfanyakazi mwenzake.’ (Kol. 4:14; Flm. 24) Sehemu za kitabu cha Matendo ambazo Luka anajihusisha katika masimulizi zinaonyesha kwamba Luka alisafiri pamoja na mtume Paulo kutoka Troa mpaka Filipi mwaka wa 50 W.K. hivi, lakini Paulo alipoondoka Filipi, Luka hakusafiri pamoja naye. Wanaume hao wawili walikutana tena Filipi mwaka wa 56 W.K. hivi na kusafiri pamoja na ndugu wengine saba kutoka Filipi kwenda Yerusalemu, ambapo Paulo alikamatwa. Miaka miwili baadaye, Luka alisafiri pamoja na Paulo, akiwa mfungwa, kutoka Kaisaria kwenda Roma. (Mdo. 16:10-17, 40; 20:5–21:17; 24:27; 27:1–28:16) Paulo alifungwa Roma kwa mara ya pili, na hata alipotambua kwamba anakaribia kuuawa, ni “Luka tu” ndiye aliyekuwa pamoja naye. (2 Tim. 4:6, 11) Ni wazi kwamba Luka alisafiri maeneo ya mbali na alikuwa tayari kuteseka kwa ajili ya habari njema.

      Luka hakudai kwamba alijionea mambo aliyoandika kumhusu Yesu. Badala yake, anasema kwamba alijitahidi ‘kukusanya habari kuhusu mambo aliyosadiki kabisa’ yaliyosimuliwa na “mashahidi wa kujionea.” Anaendelea kusema, “nimefuatilia mambo yote kwa usahihi tangu mwanzo, nami nimeamua kukuandikia mambo hayo kwa utaratibu mzuri.” (Luka 1:1-3) Kitabu cha Luka kinaonyesha wazi kwamba alifanya utafiti kwa makini. Huenda alimhoji Elisabeti, Maria, mama ya Yesu, na wengine ili kukusanya habari za kuandika. Mambo mengi aliyoandika hayapatikani katika vitabu vingine vya Injili.​—Luka 1:5-80.

      Mtume Paulo alisema kwamba Luka alikuwa daktari, na masimulizi yake ya Injili yanaonyesha wazi alihangaishwa na afya ya watu walioteseka. Kwa mfano: Luka aliandika kwamba Yesu alipomponya mtu aliyesumbuliwa na roho mwovu, “yule roho mwovu akamtoka bila kumuumiza.” Pia, aliandika kwamba mama mkwe wa mtume Petro alikuwa na “homa kali,” na kwamba mwanamke ambaye Yesu alimsaidia alisumbuliwa na “roho ya udhaifu kwa miaka 18, mwili wake ulikuwa umepindika na hangeweza kusimama wima.”​—Luka 4:35, 38; 13:11.

      Luka alitanguliza “kazi ya Bwana” maishani mwake. (1 Kor. 15:58) Lengo lake lilikuwa kuwasaidia wengine wamjue na kumtumikia Yehova bali si kutafuta utajiri au umashuhuri.

      LIDIA—MUUZAJI WA BIDHAA ZA RANGI YA ZAMBARAU

      Lidia aliishi Filipi, jiji mashuhuri katika wilaya ya Makedonia. Alitoka Thiatira, jiji lililokuwa magharibi mwa Asia Ndogo katika eneo linaloitwa Lidia. Ili kuendeleza biashara yake, Lidia alihamia eneo la ng’ambo ya Bahari ya Aegea. Inawezekana aliuza bidhaa mbalimbali za rangi ya zambarau, kama vile mazulia, mapambo, vitambaa, na hata rangi yenyewe. Maandishi yaliyopatikana Filipi yanathibitisha kwamba kulikuwa na kikundi cha wauzaji wa bidhaa za zambarau katika jiji hilo.

      Lidia akionyesha kitambaa.

      Kwa kuwa Lidia anatajwa kuwa “mwabudu wa Mungu,” huenda aligeuzwa imani na kuwa mfuasi wa dini ya Kiyahudi. (Mdo. 16:14) Inawezekana alikuwa amepata habari fulani kuhusu ibada ya Yehova katika jiji la nyumbani kwao. Tofauti na Filipi, jiji la kwao lilikuwa na sinagogi la Wayahudi. Watu fulani wanaamini kwamba Lidia lilikuwa jina la utani—linalomaanisha “Mwanamke kutoka Lidia”​—ambalo alipewa alipokuwa Filipi. Hata hivyo, kuna uthibitisho unaoonyesha kwamba kulikuwa na wanawake wengine walioitwa Lidia.

      Tangu siku za Homer, katika karne ya tisa au nane K.W.K., watu wa Lidia na majirani zao walijulikana kwa ustadi wao wa kutia rangi ya zambarau kwenye vitambaa. Maji ya Thiatira yalijulikana kwa kutokeza “rangi nyangavu na zinazodumu sana.”

      Bidhaa za zambarau zilikuwa ghali sana na zingeweza kununuliwa na matajiri tu. Ingawa rangi ya zambarau ingeweza kupatikana kutoka katika vitu mbalimbali, rangi bora na iliyokuwa ghali zaidi—iliyowekwa kwenye vitambaa laini—ilitokana na samaki-gamba wa Mediterania. Kila samaki angeweza kutokeza tone moja tu la rangi hiyo, na ili kupata gramu moja ya rangi hiyo ya pekee, samaki 8,000 hivi walihitajika. Ndiyo sababu nguo za rangi hiyo zilikuwa ghali sana.

      Inawezekana Lidia alikuwa mfanyabiashara tajiri kwa sababu biashara yake ilihitaji awe na pesa nyingi na pia alikuwa na nyumba kubwa ambapo Paulo, Sila, Timotheo, na Luka wangeweza kukaa. Biblia inataja “watu wa nyumbani mwake,” huenda alikuwa anaishi na watu wake wa ukoo, au alikuwa na vijakazi na watumishi. (Mdo. 16:15) Na kwa kuwa kabla ya kuondoka katika jiji hilo, Paulo na Sila walikutana na ndugu kadhaa katika nyumba ya mwanamke huyo mkarimu, inawezekana kwamba baadaye nyumba hiyo ilikuwa mahali ambapo Wakristo wa kwanza katika jiji la Filipi walikutana kwa ajili ya ibada.​—Mdo. 16:40.

      Miaka kumi baadaye, Paulo alipoliandikia barua kutaniko la Filipi, hakumtaja Lidia. Kwa hiyo habari pekee tulizo nazo kumhusu ni zile zinazopatikana katika sura ya 16 ya kitabu cha Matendo.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Luka—Mwandishi wa Kitabu cha Matendo.”

      b Huenda Wayahudi hawakuruhusiwa kuwa na sinagogi katika jiji la Filipi kwa sababu lilikuwa jiji la kijeshi. Au labda jiji hilo halikuwa na angalau wanaume kumi Wayahudi—idadi ya chini zaidi iliyohitajiwa ili kuwa na sinagogi.

      c Ona sanduku lenye kichwa “Lidia—Muuzaji wa Bidhaa za Rangi ya Zambarau.”

      d Kulingana na sheria ya Roma, raia alikuwa na haki ya kusikilizwa kabla ya kuhukumiwa naye hakupaswa kamwe kuadhibiwa hadharani kabla ya kuthibitishwa kuwa mwenye hatia.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki