Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Mungu Hupenda Mpaji Mchangamfu”
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Novemba 1
    • Lakini baadaye Wayudea hao wakarimu walipatwa na umaskini. Biblia haisemi kihususa ni kitu gani hasa kilichosababisha hiyo hali yao. Wasomi fulani husema kwamba huenda ikawa njaa kubwa irejezewayo kwenye Matendo 11:28, 29 ndiyo iliyokuwa kisababishi. Kwa vyovyote vile, Wakristo hao Wayudea walikuwa katika hali yenye kukatisha tumaini, naye Paulo alitaka kuhakikisha kwamba mahitaji yao yangeshughulikiwa. Angefanyaje hivyo?

      Mchango kwa Ajili ya Wenye Uhitaji

      Paulo alipata msaada kutoka kwa makutaniko yaliyokuwa mbali sana kama vile Makedonia, naye alipanga mchango utolewe kwa niaba ya Wakristo wa Yudea waliokumbwa na umaskini. Kwa Wakorintho, Paulo aliandika: “Kama vile nilivyoyapa maagizo makutaniko ya Galatia, nyinyi wenyewe pia fanyeni kwa njia hiyohiyo. Kila siku ya kwanza ya juma acheni kila mmoja wenu kwenye nyumba yake mwenyewe aweke kando kitu fulani katika akiba kama aelekeavyo kuwa anafanikiwa.”a—1 Wakorintho 16:1, 2.

      Paulo alikusudia kwamba fedha hizo zipelekwe upesi kwa ndugu waliokuwa Yerusalemu, lakini Wakorintho hawakuitikia kwa uharaka maagizo ya Paulo. Kwa nini? Je, walikuwa bila hisia yoyote kuelekea hali mbaya ya ndugu zao Wayudea? La, kwa maana Paulo alijua kwamba Wakorintho “[wali]zidi katika kila jambo, katika imani na neno na ujuzi na hali yote ya bidii.” (2 Wakorintho 8:7) Yaelekea, walikuwa na shughuli nyingi kuhusiana na mambo mengine muhimu ambayo Paulo alitaja katika barua yake ya kwanza kwao. Lakini sasa hali katika Yerusalemu ilikuwa yenye uharaka. Kwa hiyo, Paulo alitaja suala hilo katika barua yake ya pili kwa Wakorintho.

      Wasihiwa Wawe Wakarimu

      Kwanza, Paulo aliwaambia Wakorintho juu ya Wamakedonia, ambao itikio lao kwa jitihada ya kutoa msaada lilikuwa kielelezo chema. “Wakati wa jaribu kubwa chini ya taabu kubwa,” Paulo aliandika, “wingi wao wa shangwe na umaskini wa kina kirefu ulifanya utajiri wa ukarimu wao kuzidi.” Wamakedonia hawakuhitaji kusihiwa kutoa. Kinyume cha hilo, Paulo alisema kwamba “wa[li]fuliza kwa hiari yao wenyewe kutuomba kwa kusihi sana wapate pendeleo la kutoa kwa fadhili.” Ukarimu mchangamfu wa Wamakedonia ni wenye kutokeza zaidi tufikiriapo kwamba wao wenyewe walikuwa katika hali ya “umaskini wa kina kirefu.”—2 Wakorintho 8:2-4.

      Je, Paulo alikuwa akijaribu kuchochea roho ya mashindano miongoni mwa Wakorintho kwa kuwasifu Wamakedonia? Sivyo kabisa, kwa maana alijua kwamba hiyo haikuwa njia ifaayo ya kuwachochea. (Wagalatia 6:4) Zaidi ya hayo, alijua kwamba Wakorintho hawakuhitaji kuaibishwa ili kufanya lililofaa. Badala yake, alikuwa na uhakika kwamba Wakorintho waliwapenda kikweli ndugu zao Wayudea na walitamani kuchangia jitihada hiyo ya kutoa msaada. “Tayari mwaka mmoja uliopita,” akawaambia, “nyinyi mlianzisha si kule kufanya tu bali pia kule kutaka kufanya.” (2 Wakorintho 8:10) Kwa kweli, kwa njia fulani Wakorintho walikuwa kielelezo chema katika jitihada hiyo ya kutoa msaada. “Najua utayari wenu wa akili ambao juu ya huo najisifu kwa Wamakedonia juu yenu,” Paulo akawaambia, akiongeza kusema hivi: “Bidii yenu imechochea walio wengi kati yao.” (2 Wakorintho 9:2) Ingawa hivyo, sasa Wakorintho walihitaji kubadili bidii yao na utayari wao wa akili uwe matendo.

      Kwa sababu hiyo, Paulo aliwaambia: “Acheni kila mmoja afanye kama vile ameazimia moyoni mwake, si kwa kinyongo au kwa shurutisho, kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Kusudi la Paulo wakati huo halikuwa kuwashurutisha Wakorintho, kwa maana mtu hawezi kuwa mpaji mchangamfu akishurutishwa. Kwa wazi, Paulo alidhani kwamba nia ifaayo ilikuwepo tayari, kwamba kila mtu alikuwa tayari ameazimia kutoa. Kwa kuongezea, Paulo aliwaambia: “Kwa maana ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika hasa kulingana na alicho nacho mtu, si kulingana na kile ambacho mtu hana.” (2 Wakorintho 8:12) Naam, utayari ukiwepo—mtu anapochochewa na upendo—anachotoa kitakubaliwa na Mungu, hata kiwe chaonekana kidogo kadiri gani.—Linganisha Luka 21:1-4.

  • “Mungu Hupenda Mpaji Mchangamfu”
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Novemba 1
    • a Ingawa Paulo ‘alitoa maagizo,’ hilo halimaanishi kwamba alitoa madai ya lazima, yasiyo na msingi maalumu. Badala yake, Paulo alikuwa tu akisimamia mchango, uliohusisha makutaniko kadhaa. Kwa kuongezea, Paulo alisema kwamba kila mmoja “kwenye nyumba yake” angetoa “kama aelekeavyo kuwa anafanikiwa.” Yaani, kila mchango ungetolewa faraghani na kwa hiari. Hakuna aliyelazimishwa.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki