-
Yehova Hutoa Amani na Kweli kwa WingiMnara wa Mlinzi—1996 | Januari 1
-
-
Yehova Hutoa Amani na Kweli kwa Wingi
“Nitawaponya; nami nitawafunulia wingi wa amani na kweli.”—YEREMIA 33:6.
1, 2. (a) Kuhusu amani, mataifa yana rekodi gani? (b) Katika 607 K.W.K., Yehova alifundisha Israeli somo jipi kuhusu amani?
AMANI! Hiyo yatamanika kama nini, nayo imekuwa nadra kama nini katika historia ya kibinadamu! Hasa karne ya 20 haijawa karne ya amani. Badala ya hivyo, imeona vita viwili vyenye uharibifu zaidi katika historia ya kibinadamu. Baada ya vita ya ulimwengu ya kwanza, Ushirika wa Mataifa ulisimamishwa ili kudumisha amani ya ulimwengu. Shirika hilo lilishindwa. Baada ya vita ya ulimwengu ya pili, shirika la Umoja wa Mataifa lilianzishwa likiwa na lengo lilelile. Twahitaji tu kusoma magazeti ya kila siku kuona jinsi hilo pia linavyoshindwa vibaya.
2 Je, tushangae kwamba mashirika ya kibinadamu hayawezi kuleta amani? La hasha. Zaidi ya miaka 2,500 iliyopita, wachaguliwa wa Mungu, Israeli, walifundishwa somo kwa habari hii. Katika karne ya saba K.W.K., amani ya Israeli ilitishwa na Babiloni, lililokuwa likiinuka kuwa mamlaka kuu ya ulimwengu. Israeli lilitazamia Misri ili kupata amani. Misri lilishindwa. (Yeremia 37:5-8; Ezekieli 17:11-15) Katika 607 K.W.K., majeshi ya Babiloni yalibomoa kabisa kuta za Yerusalemu na kuchoma hekalu la Yehova. Hivyo Israeli likajifunza kwa dhiki ubatili wa kutegemea mashirika ya kibinadamu. Badala ya kufurahia amani, taifa hilo lililazimishwa kwenda uhamishoni Babiloni.—2 Mambo ya Nyakati 36:17-21.
3. Katika utimizo wa maneno ya Yehova kupitia Yeremia, ni matukio gani ya kihistoria yaliyofundisha Israeli somo la pili lililo muhimu kuhusu amani?
3 Hata hivyo, kabla ya kuanguka kwa Yerusalemu, Yehova alikuwa amefunua kwamba yeye, wala si Misri, angeleta amani halisi Israeli. Kupitia Yeremia aliahidi: “Nitawaponya; nami nitawafunulia wingi wa amani na kweli. Nami nitawarudisha wafungwa wa Yuda, na wafungwa wa Israeli, na kuwajenga kama kwanza.” (Yeremia 33:6, 7) Ahadi ya Yehova ilianza kutimizwa katika 539 K.W.K. Babiloni liliposhindwa, na Waisraeli waliokuwa uhamishoni kupewa uhuru. (2 Mambo ya Nyakati 36:22, 23) Kufikia sehemu ya mwisho ya 537 K.W.K., kikundi cha Waisraeli kiliadhimisha Msherehekeo wa Mabanda katika Israeli kwa mara ya kwanza kwa miaka 70! Baada ya msherehekeo huo, walianza kujenga upya hekalu la Yehova. Walihisije kuhusu hilo? Rekodi yasema: ‘Walipaza sauti zao, na kupiga kelele, walipomhimidi BWANA, kwa sababu msingi wa nyumba ya BWANA ulikwisha kuwekwa.’—Ezra 3:11.
4. Yehova aliwaamshaje Waisraeli wafanye kazi ya kujenga hekalu, naye alitoa ahadi gani kuhusu amani?
4 Hata hivyo, baada ya mwanzo huo wenye furaha Waisraeli walivunjwa moyo na wapinzani wakaacha kazi ya kujenga hekalu. Miaka kadhaa baadaye, Yehova aliwainua manabii Hagai na Zekaria waamshe Waisraeli ili wakamilishe kazi ya kujenga upya. Ni lazima walisisimuka kama nini kumsikiliza Hagai akisema hivi kuhusu hekalu ambalo lingejengwa: “Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza, asema BWANA wa majeshi; na katika mahali hapa nitawapa amani.”—Hagai 2:9.
Yehova Hutimiza Ahadi Zake
5. Ni jambo gani linalotokeza kuhusu sura ya nane ya Zekaria?
5 Katika kitabu cha Biblia cha Zekaria, sisi husoma juu ya maono na unabii mwingi mbalimbali wenye kupuliziwa ambao uliwaimarisha watu wa Mungu huko nyuma katika karne ya sita K.W.K. Unabii uo huo mbalimbali huendelea kutuhakikishia utegemezaji wa Yehova. Huo hutupa sababu nyingi za kuamini kwamba Yehova atawapa watu wake amani katika siku yetu pia. Kwa kielelezo, katika sura ya nane ya kitabu kinachotajwa kwa jina lake, nabii Zekaria atamka maneno haya mara kumi: ‘BWANA asema hivi.’ Kila wakati, usemi huo watanguliza tangazo la kimungu linalohusu amani ya watu wa Mungu. Baadhi ya ahadi hizo zilitimizwa huko nyuma katika siku ya Zekaria. Zote zimetimizwa au zinaendelea kutimizwa leo.
‘Nitakuwa na Wivu kwa Ajili ya Sayuni’
6, 7. Ni katika njia gani Yehova alikuwa ‘mwenye wivu kwa ajili ya Sayuni kwa ghadhabu kuu’?
6 Usemi huo watokea mara ya kwanza kwenye Zekaria 8:2, ambapo twasoma hivi: ‘BWANA wa majeshi asema hivi, Mimi nitakuwa na wivu kwa ajili ya Sayuni, wivu mkuu, nami nitakuwa na wivu kwa ajili yake kwa ghadhabu kuu.’ Ahadi ya Yehova ya kuwa mwenye wivu, kuwa na bidii sana, kwa ajili ya watu wake ilimaanisha kwamba angekuwa macho ili awarudishie amani. Kurudishwa kwa Israeli katika bara lalo na kujengwa upya kwa hekalu kulikuwa uthibitisho wa bidii hiyo.
7 Lakini, vipi juu ya wale ambao walikuwa wamepinga watu wa Yehova? Bidii yake kwa ajili ya watu wake ingetoshana na ‘ghadhabu yake kuu’ juu ya maadui wake. Wayahudi waaminifu walipoabudu kwenye hekalu lililojengwa upya, wangeweza kufikiria yale yaliyopata Babiloni lenye nguvu, ambalo sasa lilikuwa limeanguka. Pia waliweza kufikiria juu ya kushindwa kabisa kwa maadui waliojaribu kuzuia kujengwa upya kwa hekalu. (Ezra 4:1-6; 6:3) Nao waliweza kumshukuru Yehova kwamba alikuwa ametimiza ahadi yake. Bidii yake iliwaletea ushindi!
“Mji wa Kweli”
8. Katika siku za Zekaria, Yerusalemu ungekuwaje mji wa kweli tofauti na nyakati za mapema?
8 Mara ya pili Zekaria aandika: “BWANA asema hivi.” Yehova asema nini pindi hii? ‘Nitarudi Sayuni, nami nitakaa katikati ya Yerusalemu; na Yerusalemu utaitwa, Mji wa kweli; na Mlima wa BWANA wa majeshi utaitwa, Mlima mtakatifu.’ (Zekaria 8:3) Kabla ya 607 K.W.K., hakika Yerusalemu haukuwa mji wa kweli. Makuhani na manabii wao walikuwa wafisadi, na watu wao hawakuwa waaminifu. (Yeremia 6:13; 7:29-34; 13:23-27) Sasa watu wa Mungu walikuwa wakijenga upya hekalu, wakionyesha hali yao ya kujitoa kwa ibada safi. Katika roho Yehova alikaa tena Yerusalemu. Kweli za ibada safi zilisemwa tena humo, hivyo Yerusalemu ungeweza kuitwa “mji wa kweli.” Mahali payo palipoinuka paliweza kuitwa “mlima wa BWANA.”
9. Ni badiliko gani la hali lenye kutokeza lililopatwa na “Israeli wa Mungu” katika 1919?
9 Ingawa matangazo hayo mawili yalikuwa na umaana katika Israeli la kale, hayo pia yana umaana sana kwetu sisi wakati karne hii ya 20 iendeleapo kumalizika. Karibu miaka 80 iliyopita, wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza, maelfu machache ya watiwa-mafuta ambao wakati huo waliwakilisha “Israeli wa Mungu” walienda katika utekwa wa kiroho, kama tu Israeli la kale lilivyoenda katika utekwa Babiloni. (Wagalatia 6:16) Kiunabii, wao walifafanuliwa kuwa maiti zenye kulala barabarani. Na bado, wao walikuwa na tamaa yenye unyoofu ya kumwabudu Yehova “katika roho na kweli.” (Yohana 4:24) Hivyo, katika 1919, Yehova aliwafungua kutoka utekwani, akiwainua kutoka kwa hali yao ya kuwa wafu kiroho. (Ufunuo 11:7-13) Hivyo, Yehova alijibu kwa Ndiyo kubwa sana swali hili la kiunabii la Isaya: “Je, kweli bara litazaliwa kwa utungu katika siku moja? Au kweli taifa litazaliwa kwa wakati mmoja?” (Isaya 66:8, NW) Katika 1919, watu wa Yehova walikuwapo tena wakiwa taifa la kiroho katika “bara” lao wenyewe, au hali ya kiroho duniani.
10. Kuanzia 1919, Wakristo watiwa-mafuta wamekuwa wakifurahia baraka zipi katika “bara” lao?
10 Wakiwa salama katika bara hilo, Wakristo watiwa-mafuta walitumikia katika hekalu kubwa la kiroho la Yehova. Wao waliitwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” wakikubali daraka la kutunza mali za kidunia za Yesu, pendeleo ambalo wangali wanafurahia karne ya 20 ikaribiapo mwisho. (Mathayo 24:45-47) Walijifunza vema somo la kwamba Yehova ndiye “Mungu wa amani mwenyewe.”—1 Wathesalonike 5:23.
11. Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wamejionyeshaje kuwa maadui wa watu wa Mungu?
11 Lakini, namna gani juu ya maadui wa Israeli wa Mungu? Bidii ya Yehova kwa ajili ya watu wake yalingana na ghadhabu yake dhidi ya wapinzani. Wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza, viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo walileta mkazo mkubwa sana walipojaribu—na kushindwa—kuondoa kabisa kikundi hiki kidogo cha Wakristo wenye kusema kweli. Wakati wa vita ya ulimwengu ya pili, wahudumu wa Jumuiya ya Wakristo waliungana katika jambo moja tu: Katika pande zote mbili zilizokuwa zikipambana, walihimiza serikali ziwakandamize Mashahidi wa Yehova. Hata leo, katika nchi nyingi viongozi wa kidini wanachochea serikali mbalimbali kuwekea vikwazo au kupiga marufuku kazi ya Kikristo ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova.
12, 13. Ghadhabu ya Yehova yaonyeshwaje dhidi ya Jumuiya ya Wakristo?
12 Hilo halijakosa kuonwa na Yehova. Baada ya vita ya ulimwengu ya kwanza, Jumuiya ya Wakristo, pamoja na sehemu iliyobaki ya Babiloni Mkubwa, ilianguka. (Ufunuo 14:8) Uhalisi wa kuanguka kwa Jumuiya ya Wakristo ukaja kuwa jambo la kujulikana kwa wote wakati, kuanzia 1922, mfululizo wa mapigo ya mifano yalipomwagwa, yakifunua peupe hali yake ya kufa kiroho na kuonya juu ya uharibifu wake unaokuja. (Ufunuo 8:7–9:21) Huku kukiwa na uthibitisho kwamba kumwagwa kwa mapigo hayo kwaendelea, hotuba “Mwisho wa Dini Bandia U Karibu” ilitolewa ulimwenguni pote katika Aprili 23, 1995, ikifuatwa na kugawanywa kwa mamia ya mamilioni ya nakala za toleo la kipekee la Habari za Ufalme.
13 Leo, Jumuiya ya Wakristo iko katika hali ya kusikitisha. Kotekote katika karne ya 20, washiriki wayo wameuana katika vita vikatili vilivyobarikiwa na makasisi na wahudumu wayo. Haina uvutano wowote katika nchi fulani. Inaelekea kuharibiwa pamoja na sehemu inayobaki ya Babiloni Mkubwa.—Ufunuo 18:21.
Amani kwa Ajili ya Watu wa Yehova
14. Ni picha gani ya maneno ya kiunabii inayoonyeshwa ya watu wenye amani?
14 Kwa upande mwingine, katika mwaka huu wa 1996, watu wa Yehova hufurahia amani nyingi sana katika bara lao lililorudishwa, kama ielezwavyo katika tangazo la tatu la Yehova: “BWANA wa majeshi asema hivi, Wazee wanaume na wazee wanawake watakaa tena katika njia za Yerusalemu, kila mtu ana mkongojo wake mkononi, kwa kuwa ni mzee sana. Na hizo njia za mji zitajaa wavulana, na wasichana, wakicheza katika njia zake.”—Zekaria 8:4, 5.
15. Japo vita za mataifa, watumishi wa Yehova wamefurahia amani gani?
15 Picha hiyo ya kupendeza ya maneno yaonyesha jambo moja la kutokeza katika ulimwengu huu wenye vita nyingi—watu wenye amani. Tangu 1919, maneno ya kiunabii ya Isaya yametimizwa: “Amani, amani, kwake yeye aliye mbali, na kwake yeye aliye karibu; asema BWANA; nami nitamponya. Bali . . . hapana amani kwa wabaya; asema Mungu wangu.” (Isaya 57:19-21) Bila shaka, ingawa watu wa Yehova si sehemu ya ulimwengu, hawawezi kuepuka kuathiriwa na fujo za mataifa. (Yohana 17:15, 16) Katika nchi fulani, hao huvumilia magumu makali sana, na wachache hata wameuawa. Na bado Wakristo halisi wana amani katika njia mbili zilizo kubwa. Kwanza, wana “amani kwa Mungu, kwa njia ya Bwana [wao] Yesu Kristo.” (Warumi 5:1) Pili, wana amani miongoni mwao wenyewe. Wao husitawisha “hekima itokayo juu,” ambayo “kwanza ni safi, tena ni ya amani.” (Yakobo 3:17; Wagalatia 5:22-24) Isitoshe, wao hutazamia kupata amani katika maana kamili wakati ‘wenye upole watakapoirithi nchi, na kujifurahisha kwa wingi wa amani.’—Zaburi 37:11.
16, 17. (a) “Wazee wanaume na wazee wanawake” pamoja na ‘wavulana na wasichana’ wameimarishaje tengenezo la Yehova? (b) Ni nini kionyeshacho amani ya watu wa Yehova?
16 Bado kuna “wazee wanaume na wazee wanawake” miongoni mwa watu wa Yehova, watiwa-mafuta wakumbukao ushindi mbalimbali wa mapema wa tengenezo la Yehova. Uaminifu na uvumilivu wao wathaminiwa sana. Watiwa-mafuta wachanga zaidi walichukua uongozi katika siku moto-moto za miaka ya 1930 na za Vita ya Ulimwengu 2, na vilevile katika miaka yenye msisimuko ya ukuzi iliyofuata. Zaidi, hasa tangu 1935, “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” umejidhihirisha. (Ufunuo 7:9, NW; Yohana 10:16) Kadiri Wakristo watiwa-mafuta wamekuwa na umri mkubwa zaidi na kuwa wachache zaidi, kondoo wengine wametwaa kazi ya kuhubiri na wameieneza kotekote duniani. Katika miaka ya majuzi kondoo wengine wamekuwa wakijaza bara la watu wa Mungu. Kwani, mwaka uliopita pekee, 338,491 walibatizwa katika wonyesho wa wakfu wao kwa Yehova! Wapya hao ni wachanga kwelikweli, tukisema kiroho. Hali yao ya kuwa wapya na shauku yao yathaminiwa waongezapo idadi ya wale waimbao sifa zenye shukrani kwa “Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo.”—Ufunuo 7:10.
17 Leo, ‘njia za mji zimejaa wavulana na wasichana,’ Mashahidi walio na nguvu ya ujana. Katika mwaka wa utumishi wa 1995, ripoti zilipokewa kutoka mabara na visiwa vya bahari 232. Lakini hakuna upinzani wa kimataifa, wala chuki ya kikabila, wala wivu usiofaa, kati ya watiwa-mafuta na kondoo wengine. Wote hukua pamoja kiroho, wakiungana katika upendo. Kwa kweli udugu wa ulimwenguni pote wa Mashahidi wa Yehova ni wa kipekee sana ulimwenguni.—Wakolosai 3:14; 1 Petro 2:17.
Je, Ni Vigumu Mno kwa Yehova?
18, 19. Katika miaka ya tangu 1919, Yehova ametimizaje lile ambalo huenda lilionekana kuwa gumu mno kwa maoni ya kibinadamu?
18 Huko nyuma katika 1918 mabaki ya watiwa-mafuta walipokuwa tu maelfu machache ya nafsi zilizovunjika moyo katika utekwa wa kiroho, hakuna mtu ambaye aliweza kuona kimbele mwendo wa matukio. Hata hivyo, Yehova alijua—kama ionyeshwavyo na tangazo lake la nne la kiunabii: “BWANA wa majeshi asema hivi, Ingawa hili ni neno lililo gumu [“laweza kuonekana kuwa gumu mno,” NW] mbele ya macho ya mabaki ya watu hawa katika siku hizo, je! liwe neno gumu [“gumu mno,” NW] mbele ya macho yangu? asema BWANA wa majeshi.”—Zekaria 8:6.
19 Katika 1919, roho ya Yehova ilihuisha watu wake kwa ajili ya kazi iliyokuwa mbele. Lakini, imani ilihitajika kushikamana kabisa na tengenezo dogo la waabudu wa Yehova. Walikuwa wachache sana, na mambo mengi hayakuwa wazi. Hata hivyo, polepole Yehova aliwaimarisha kitengenezo na kuwaandaa wafanye kazi ya Kikristo ya kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. (Isaya 60:17, 19; Mathayo 24:14; 28:19, 20) Polepole, aliwasaidia watambue masuala muhimu kama vile kutokuwamo na enzi kuu ya ulimwengu wote mzima. Je, ilikuwa vigumu mno kwa Yehova kutimiza mapenzi yake kwa kupitia kikundi hicho kidogo cha Mashahidi? Hakika jibu ni la! Hilo laonyeshwa katika kurasa 12 hadi 15 za gazeti hili, zionyeshazo chati ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova ya mwaka wa utumishi wa 1995.
“Nami Nitakuwa Mungu Wao”
20. Kukusanywa kwa watu wa Mungu kulitolewa unabii kuwa kungeenea kwa kiasi gani?
20 Tangazo la tano laonyesha zaidi hali yenye furaha ya Mashahidi wa Yehova leo: “BWANA wa majeshi asema hivi, Tazama, nitawaokoa watu wangu toka nchi ya mashariki, na toka nchi ya magharibi; nami nitawaleta, nao watakaa katikati ya Yerusalemu; nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao, katika kweli na katika haki [“uadilifu,” NW].”—Zekaria 8:7, 8.
21. Ni katika njia zipi amani nyingi ya watu wa Yehova imedumishwa na kuenezwa?
21 Katika 1996 twaweza kusema bila kusita kwamba habari njema imehubiriwa ulimwenguni kote, toka “nchi ya mashariki” hadi “nchi ya magharibi.” Watu wa mataifa yote wamefanywa kuwa wanafunzi, nao wameona utimizo wa ahadi hii ya Yehova: “Watoto wako wote watafundishwa na BWANA; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” (Isaya 54:13) Tuna amani kwa sababu tunaelimishwa na Yehova. Na kwa kusudi hilo, fasihi zimetangazwa katika lugha zaidi ya 300. Mwaka uliopita pekee, lugha 21 zaidi ziliongezwa. Gazeti la Mnara wa Mlinzi sasa hutangazwa sawia katika lugha 111, na Amkeni! katika lugha 54. Mikusanyiko ya kitaifa na ya kimataifa huandaa wonyesho wa peupe wa amani ya watu wa Mungu. Mikutano ya kila juma hutuunganisha na kutupa kitia-moyo tunachohitaji ili tuwe imara. (Waebrania 10:23-25) Ndiyo, Yehova anaelimisha watu wake “katika kweli na katika uadilifu.” Anawapa watu wake amani. Tuna baraka kama nini kushiriki katika hiyo amani nyingi!
-
-
‘Penda Kweli na Amani’!Mnara wa Mlinzi—1996 | Januari 1
-
-
‘Penda Kweli na Amani’!
“Neno la Yehova wa majeshi likaendelea kunijia, likisema: ‘. . . Pendeni kweli na amani.’”—ZEKARIA 8:18, 19, NW.
1, 2. (a) Mwanadamu ana rekodi gani kuhusu amani? (b) Kwa nini ulimwengu huu wa sasa hautaona amani halisi?
“ULIMWENGU haujapata kamwe kuwa na amani. Mahali fulani—na mara nyingi katika sehemu nyingi wakati uleule—sikuzote kumekuwa na vita.” Ndivyo alivyosema Profesa Milton Mayer wa Chuo Kikuu cha Massachusetts, Marekani. Hayo ni maelezo ya kuhuzunisha kama nini juu ya ubinadamu! Ni kweli kwamba watu wametaka amani. Wanasiasa wamejaribu njia nyingi za kuidumisha, tokea ile Pax Romana (amani ya Roma) ya nyakati za Waroma hadi ile sera ya “Uhakikishiano wa Kuangamizana” ya nyakati za Vita Baridi. Hata hivyo, hatimaye jitihada zao zote zilishindwa. Kama Isaya alivyoeleza jambo hilo karne nyingi zilizopita, ‘wajumbe wa amani wamelia kwa uchungu.’ (Isaya 33:7) Kwa nini?
2 Ni kwa sababu amani ya kudumu ni lazima itoke kwa hali isiyo na chuki na pupa; ni lazima itegemee kweli. Amani haiwezi kutegemea uwongo. Hiyo ndiyo sababu Yehova alisema hivi alipoahidi Israeli la kale urudisho na amani: ‘Namwelekezea amani kama mto, na utukufu wa mataifa kama kijito kifurikacho.’ (Isaya 66:12) Mungu wa mfumo huu wa mambo, Shetani Ibilisi, ni “muua-binadamu kikatili,” muuaji kimakusudi, na ‘mwongo na baba ya uwongo.’ (Yohana 8:44, NW; 2 Wakorintho 4:4) Ulimwengu wenye mungu kama huyo wawezaje kupata amani?
3. Yehova amewapa watu wake zawadi gani yenye kutokeza, wajapoishi katika ulimwengu wenye matatizo?
3 Hata hivyo, kwa kutokeza Yehova huwapa watu wake amani hata waishipo katika ulimwengu wa Shetani wenye kukumbwa na vita. (Yohana 17:16) Katika karne ya sita K.W.K., alitimiza ahadi yake kupitia Yeremia na kutoa “amani na kweli” kwa taifa lake la kipekee alipolirudisha katika bara lalo. (Yeremia 33:6) Na katika siku hizi za mwisho, amewapa watu wake “amani na kweli” katika “bara” lao, au hali yao ya kiroho, hata ingawa wameishi kupitia wakati mbaya zaidi wa matatizo ambao ulimwengu huu umepata kuona kufikia sasa. (Isaya 66:8; Mathayo 24:7-13; Ufunuo 6:1-8) Tuendeleapo na mazungumzo yetu juu ya Zekaria sura ya 8, tutafahamu kwa kina amani na kweli kutoka kwa Mungu na kuona kile ambacho ni lazima tufanye ili kudumisha ushiriki wetu kwayo.
“Mikono Yenu na Iwe Hodari”
4. Zekaria alitia moyo Israeli litende kwa njia gani ili kupata amani?
4 Kwa mara ya sita katika Zekaria sura ya 8, twasikia tangazo lenye kusisimua kutoka kwa Yehova: “BWANA wa majeshi asema hivi, Mikono yenu na iwe hodari, ninyi mnaosikia siku hizi maneno haya kwa vinywa vya manabii, waliokuwapo siku hiyo ulipowekwa msingi wa nyumba ya BWANA wa majeshi; yaani, hekalu hilo; ili lijengwe. Maana kabla ya siku zile hapakuwa na ijara kwa mwanadamu, wala hapakuwa na ijara kwa mnyama; wala hapakuwa na amani kwake yeye aliyetoka, wala kwake yeye aliyeingia, kwa sababu ya adui; nami nalimwacha kila mtu kugombana na jirani yake.”—Zekaria 8:9, 10.
5, 6. (a) Kwa sababu ya Waisraeli kuvunjika moyo, kulikuwa na hali gani katika Israeli? (b) Yehova aliahidi Israeli badiliko gani likitanguliza ibada yake?
5 Zekaria alisema maneno haya hekalu lilipokuwa likijengwa Yerusalemu. Awali, Waisraeli waliokuwa wamerudi kutoka Babiloni walivunjika moyo na kuacha kazi ya kujenga hekalu. Kwa sababu wao waligeuza uangalifu wao kwa anasa zao wenyewe, hawakuwa na baraka wala amani kutoka kwa Yehova. Hata ingawa walilima mashamba yao na kutunza mashamba yao ya mizabibu, hawakupata ufanisi. (Hagai 1:3-6) Ilikuwa kana kwamba walikuwa wakifanya kazi ‘bila ijara.’
6 Kwa vile sasa hekalu lilikuwa likijengwa, Zekaria aliwatia moyo Wayahudi ‘wawe hodari,’ kwa moyo mkuu wakitanguliza ibada ya Yehova. Ni nini lingetokea ikiwa wangefanya hivyo? “Sasa sitakuwa kwa mabaki ya watu hawa kama nilivyokuwa siku zile za kwanza, asema BWANA wa majeshi. Kwa maana itakuwako mbegu ya amani; mzabibu utatoa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake, na hizo mbingu zitatoa umande wake; nami nitawarithisha mabaki ya watu hawa vitu hivi vyote. Kisha itakuwa, kama vile mlivyokuwa laana katika mataifa, Ee nyumba ya Yuda, na nyumba ya Israeli, ndivyo nitakavyowaokoa, nanyi mtakuwa baraka; msiogope, lakini mikono yenu na iwe hodari.” (Zekaria 8:11-13) Ikiwa Israeli lingetenda kwa kuazimia, lingefanikiwa. Mapema, mataifa yalipotaka kutaja kielelezo cha laana, yaliweza kutaja Israeli. Sasa Israeli lingekuwa kielelezo cha baraka. Hiyo ilikuwa sababu bora kama nini ya ‘kuacha mikono yao iwe hodari’!
7. (a) Ni mabadiliko gani yenye kusisimua ambayo watu wa Yehova wamepata, yakifikia upeo katika mwaka wa utumishi wa 1995? (b) Kwa kutazama ripoti ya kila mwaka, ni nchi zipi unazoona kuwa zina rekodi ya kutokeza ya wahubiri, mapainia, na wastani wa saa?
7 Namna gani leo? Katika miaka ya kabla ya 1919, kwa njia fulani watu wa Yehova hawakuwa na bidii. Hawakuchukua msimamo thabiti wa kutokuwamo katika vita ya ulimwengu ya kwanza, nao walikuwa na mwelekeo wa kufuata mwanadamu badala ya Mfalme wao, Yesu Kristo. Tokeo likawa kwamba wengine walivunjwa moyo na upinzani kutoka ndani na nje ya tengenezo. Kisha, katika 1919, wakiwa na msaada wa Yehova wao waliacha mikono yao iwe hodari. (Zekaria 4:6) Yehova aliwapa amani, nao walisitawi sana. Hilo laonekana katika rekodi yao ya miaka 75 ambayo imepita, ifikiayo upeo katika mwaka wa utumishi wa 1995. Wakiwa kikundi, Mashahidi wa Yehova huepuka utukuzo wa taifa, ukabila, upendeleo, na vyanzo vingine vyote vya chuki. (1 Yohana 3:14-18) Wao humtumikia Yehova kwa bidii ya kweli katika hekalu lake la kiroho. (Waebrania 13:15; Ufunuo 7:15) Mwaka uliopita pekee, walitumia zaidi ya muda wa saa bilioni moja wakizungumza na wengine kuhusu Baba yao wa kimbingu! Kila mwezi, waliongoza mafunzo ya Biblia 4,865,060. Wastani wa 663,521 walishiriki katika utumishi wa painia. Wahudumu wa Jumuiya ya Wakristo watakapo kutoa kielelezo cha watu ambao kwa kweli ni wenye shauku katika ibada yao, nyakati nyingine wao hutaja Mashahidi wa Yehova.
8. Kila Mkristo aweza kunufaikaje na “mbegu ya amani”?
8 Kwa sababu ya bidii yao, Yehova huwapa watu wake “mbegu ya amani.” Kila mtu asitawishaye mbegu hiyo ataona amani ikikua moyoni mwake na maishani mwake. Kila Mkristo anayeamini ambaye hufuata amani pamoja na Yehova na pamoja na Wakristo wenzake hushiriki kweli na amani ya watu waitwao kwa jina la Yehova. (1 Petro 3:11; linganisha Yakobo 3:18.) Je, hiyo si ajabu?
“Msiogope”
9. Yehova aliahidi badiliko gani katika shughuli zake pamoja na watu wake?
9 Sasa twasoma tangazo la saba kutoka kwa Yehova. Ni lipi hilo? “BWANA wa majeshi asema hivi, Kama vile nilivyoazimia kuwatenda ninyi mabaya, baba zenu waliponikasirisha, asema BWANA wa majeshi, wala mimi sikujuta; vivyo hivyo nimeazimia katika siku hizi kuutendea Yerusalemu mema, na nyumba ya Yuda pia; msiogope.”—Zekaria 8:14, 15.
10. Ni rekodi gani ya Mashahidi wa Yehova ionyeshayo kwamba wao hawajaogopa?
10 Hata ingawa watu wa Yehova walitawanyika katika maana ya kiroho katika vita ya ulimwengu ya kwanza, mioyoni mwao walitaka kufanya yaliyo sawa. Hivyo, baada ya kuwatia nidhamu kidogo, Yehova alibadili njia yake ya kushughulika nao. (Malaki 3:2-4) Leo, sisi hutazama nyuma na kumshukuru sana kwa yale ambayo amefanya. Ni kweli, tumekuwa “watu wa kuchukiwa na mataifa yote.” (Mathayo 24:9) Wengi wamefungwa gerezani, na wengine hata wamekufa kwa ajili ya imani yao. Mara nyingi sisi hukabili ubaridi au uhasama. Lakini hatuogopi. Twajua kwamba Yehova ana nguvu kushinda upinzani wowote ule, uonekanao au usioonekana. (Isaya 40:15; Waefeso 6:10-13) Hatutaacha kutii maneno haya: “Tumaini katika Yehova; uwe na moyo mkuu na moyo wako uwe na nguvu.”—Zaburi 27:14, NW.
“Semezaneni Kweli”
11, 12. Sisi mmoja-mmoja twapaswa kukumbuka nini ikiwa tunataka kushiriki kikamili katika baraka ambazo Yehova huwapa watu wake?
11 Ili kushiriki kikamili katika baraka zinazotoka kwa Yehova, kuna mambo tupaswayo kukumbuka. Zekaria asema hivi: “‘Nyinyi watu mwapaswa kutenda mambo haya: Semezaneni kweli. Kwa kweli na hukumu ya amani mfanye hukumu zenu malangoni mwenu. Na msitungiane msiba mioyoni mwenu, na msipende kiapo bandia; kwa kuwa nimeyachukia hayo yote,’ ndilo tamko la Yehova.”—Zekaria 8:16, 17, NW.
12 Yehova atuhimiza tuseme kweli. (Waefeso 4:15, 25) Yeye hasikii sala za wale watungao mambo yenye kudhuru, wafichao kweli kwa sababu ya kufaidika kibinafsi, au kuapa kwa ubandia. (Mithali 28:9) Kwa kuwa yeye huchukia uasi-imani, atutaka tushikamane na kweli ya Biblia. (Zaburi 25:5; 2 Yohana 9-11) Na zaidi, kama wanaume wazee kwenye malango ya jiji la Israeli, wazee wanaoshughulikia kesi za kihukumu wapaswa kutegemeza shauri lao na maamuzi yao kwenye kweli ya Biblia, wala si kwenye maoni ya kibinafsi. (Yohana 17:17) Yehova huwataka watafute “hukumu ya amani,” wakijaribu, wakiwa wachungaji Wakristo, kurudisha amani kati ya watu wanaozozana na kuwasaidia watenda dhambi wenye toba wapate tena amani pamoja na Mungu. (Yakobo 5:14, 15; Yuda 23) Wakati uo huo, wao huhifadhi amani ya kutaniko, kwa moyo mkuu wakiondosha nje wale wanaoharibu amani hiyo kwa kuendelea kutenda makosa kimakusudi.—1 Wakorintho 6:9, 10.
“Mchachao na Shangilio”
13. (a) Zekaria alitoa unabii wa badiliko gani kuhusu kufunga? (b) Ni mfungo gani uliofanywa katika Israeli?
13 Sasa, twasikia tangazo la nane lenye uzito: “Yehova wa majeshi amesema hivi, ‘Mfungo wa mwezi wa nne, na mfungo wa mwezi wa tano, na mfungo wa mwezi wa saba, na mfungo wa mwezi wa kumi utakuwa mchachao na shangilio na pindi ya msherehekeo kwa ajili ya nyumba ya Yuda. Hivyo pendeni kweli na amani.’” (Zekaria 8:19, NW) Chini ya Sheria ya Kimusa, Waisraeli walifunga kwenye Siku ya Kufunika ili kuonyesha huzuni juu ya dhambi zao. (Mambo ya Walawi 16:29-31) Mifungo minne iliyotajwa na Zekaria yaonekana ilifanywa ili kuomboleza juu ya matukio yaliyohusika na kushindwa na kuharibiwa kwa Yerusalemu. (2 Wafalme 25:1-4, 8, 9, 22-26) Hata hivyo, sasa hekalu lilikuwa likijengwa upya na Yerusalemu kukaliwa tena. Ombolezo lilikuwa likibadilishwa kuwa shangilio, na mifungo kuwa pindi za sherehe.
14, 15. (a) Sherehe ya Ukumbusho ilikuwaje chanzo kikubwa cha shangilio, nayo yapasa kutukumbusha nini? (b) Kama ionekanavyo katika ripoti ya mwaka, ni nchi zipi zilizokuwa na mahudhurio yenye kutokeza ya Ukumbusho?
14 Leo, sisi hatufanyi mifungo iliyotajwa na Zekaria au mfungo uliotajwa na Sheria. Kwa kuwa Yesu alitoa uhai wake kwa ajili ya dhambi zetu, tunafurahia baraka za Siku ya Kufunika iliyo kubwa zaidi. Dhambi zetu hufunikwa, si kidogo tu, bali kabisa. (Waebrania 9:6-14) Kufuatia amri ya Kuhani wa Cheo cha Juu wa kimbingu, Yesu Kristo, sisi huadhimisha Ukumbusho wa kifo chake ukiwa sherehe ya pekee yenye uzito katika kalenda ya Wakristo. (Luka 22:19, 20) Je, hatupati “mchachao na shangilio” tukusanyikapo pamoja kila mwaka kwa ajili ya sherehe hiyo?
15 Mwaka uliopita, watu 13,147,201 walikusanyika ili kusherehekea Ukumbusho, wakiwa 858,284 wengi zaidi kuliko 1994. Huo ni umati ulioje! Ebu wazia shangilio lililokuwa katika makutaniko 78,620 ya Mashahidi wa Yehova wakati idadi kubwa isivyo kawaida za watu zilipomiminika katika Majumba ya Ufalme yao kwa ajili ya sherehe hiyo. Hakika, wote waliokuwapo walisukumwa ‘kupenda kweli na amani’ walipokumbuka kifo cha Yule aliye “njia, na kweli, na uzima” na ambaye sasa atawala akiwa “Mwana-Mfalme wa Amani” wa Yehova aliye mkubwa! (Yohana 14:6; Isaya 9:6, NW) Sherehe hiyo ilikuwa na umaana wa kipekee kwa wale walioiadhimisha katika nchi zilizokumbwa na msukosuko na vita. Baadhi ya ndugu zetu waliona maogofyo yasiyoweza kufafanuliwa katika 1995. Na bado, ‘amani ya Mungu, ipitayo akili zote, iliwahifadhi mioyo yao na nia zao kupitia Kristo Yesu.’—Wafilipi 4:7.
“Tuombe Fadhili za BWANA”
16, 17. Watu wa mataifa wawezaje ‘kuomba fadhili za Yehova’?
16 Lakini, hayo mamilioni yote ya watu waliohudhuria Ukumbusho yalitoka wapi? Tamko la tisa la Yehova laeleza: “BWANA wa majeshi asema hivi, Itatokea halafu ya kwamba watakuja mataifa na wenyeji wa miji mingi; wenyeji wa mji huu watauendea mji huu, wakisema, Haya! twendeni zetu kwa haraka tuombe fadhili za BWANA, na kumtafuta BWANA wa majeshi; Mimi nami nitakwenda. Naam, watu wa kabila nyingi na mataifa hodari watakuja Yerusalemu kumtafuta BWANA wa majeshi, na kuomba fadhili za BWANA.”—Zekaria 8:20-22.
17 Watu waliohudhuria Ukumbusho walitaka ‘kumtafuta Yehova wa majeshi.’ Wengi wao walikuwa watumishi wake waliojiweka wakfu na kubatizwa. Mamilioni ya wengine waliohudhuria hawakuwa wamefikia hatua hiyo. Katika nchi fulani hudhurio la Ukumbusho lilikuwa mara nne au tano kuliko idadi ya wahubiri wa Ufalme. Wengi hawa wanaopendezwa wahitaji msaada wa kuendelea kufanya maendeleo. Na tuwafundishe kuchachawa katika ujuzi wa kwamba Yesu alikufa kwa ajili ya dhambi zetu na sasa anatawala katika Ufalme wa Mungu. (1 Wakorintho 5:7, 8; Ufunuo 11:15) Na tuwatie moyo wajiweke wakfu kwa Yehova Mungu na kunyenyekea Mfalme wake aliyewekwa rasmi. Kwa njia hiyo wao ‘wataomba fadhili za BWANA.’—Zaburi 116:18, 19; Wafilipi 2:12, 13.
‘Watu Kumi wa Lugha Zote za Mataifa’
18, 19. (a) Katika utimizo wa Zekaria 8:23, ni nani leo aliye “Myahudi”? (b) Ni nani leo walio “watu kumi” ambao ‘washika upindo wa nguo ya Myahudi’?
18 Kwa mara ya mwisho katika sura ya nane ya Zekaria, twasoma hivi: “BWANA wa majeshi asema hivi.” Tangazo la mwisho la Yehova ni nini? “Siku hizo watu kumi, wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naam, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.” (Zekaria 8:23) Katika siku ya Zekaria, Israeli la asili lilikuwa taifa lililochaguliwa la Mungu. Hata hivyo, katika karne ya kwanza, Israeli lilimkataa Mesiya wa Yehova. Kwa hiyo, Mungu wetu akachagua “Myahudi”—Israeli jipya—kuwa watu wake wa kipekee, “Israeli wa Mungu” waliofanyizwa kwa Wayahudi wa kiroho. (Wagalatia 6:16; Yohana 1:11; Warumi 2:28, 29) Idadi ya mwisho ya hawa ilikuwa iwe 144,000, waliochaguliwa kutoka miongoni mwa wanadamu ili kutawala pamoja na Yesu katika Ufalme wake wa kimbingu.—Ufunuo 14:1, 4.
19 Wengi wa hawa 144,000 tayari wamekufa wakiwa waaminifu nao wameenda kwenye thawabu yao ya kimbingu. (1 Wakorintho 15:51, 52; Ufunuo 6:9-11) Wachache wamebaki duniani nao hushangilia kuona kwamba “watu kumi” wanaochagua kuenda pamoja na “Myahudi” hakika ni “mkutano mkubwa sana [“umati mkubwa,” NW] . . . wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.”—Ufunuo 7:9; Isaya 2:2, 3; 60:4-10, 22.
20, 21. Mwisho wa ulimwengu huu ukaribiapo zaidi, twaweza kukaaje kwa amani pamoja na Yehova?
20 Mwisho wa ulimwengu huu ukaribiapo zaidi na zaidi bila kukosa, Jumuiya ya Wakristo ni kama Yerusalemu katika siku ya Yeremia: “Tulitazamia amani, lakini hayakuja mema yo yote, tulitazamia wakati wa kupona, na tazama, kufadhaika [“ogofyo,” NW] tu!” (Yeremia 14:19) Ogofyo hilo litafikia upeo mataifa yatakapogeukia dini bandia na kuleta mwisho wayo wenye jeuri. Muda mfupi baadaye, mataifa yenyewe yatapatwa na uharibifu katika vita ya mwisho ya Mungu, Har–Magedoni. (Mathayo 24:29, 30; Ufunuo 16:14, 16; 17:16-18; 19:11-21) Huo utakuwa wakati wa fujo kama nini!
21 Kupitia hayo yote, Yehova atawahifadhi wale wapendao kweli na kusitawisha “mbegu ya amani.” (Zekaria 8:12; Sefania 2:3) Basi, na tukae salama katika bara la watu wake, tukimsifu kwa bidii na kuwasaidia wengi kadiri iwezekanavyo ‘kuomba fadhili za Yehova.’ Tukifanya hivyo, sikuzote tutafurahia amani ya Yehova. Ndiyo, “BWANA atawapa watu wake nguvu; BWANA atawabariki watu wake kwa amani.”—Zaburi 29:11.
-