-
Wanyama Ni Zawadi Kutoka kwa MunguAmkeni!—2004 | Februari 22
-
-
Wanyama Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu
JE, UMEWAHI kutembelea bustani ya wanyama au kwenda kwenye sarakasi? Je, ulitamani kumshika au kumpapasa mnyama mzuri, kama vile simba au simbamarara mkubwa? Labda ulifurahia kumwona mtunzaji akiwashika. Miaka karibu 2,000 iliyopita, mwandishi mmoja wa Biblia alisema hivi: “Kila aina ya mnyama-mwitu na vilevile ndege na kitu kinachotambaa na kiumbe cha baharini ni vya kufugwa navyo vimefugwa na binadamu.”—Yakobo 3:7.
Wanyama wote wanafurahia kupendwa na kutunzwa. Unaweza kufurahia kuwaona wakichangamana na watunzaji wao. Mwandishi Mroma Pliny, aliyeandika karibu na wakati ambapo mwandishi wa Biblia Yakobo aliandika, alizungumzia ufugaji wa tembo, simba, simbamarara, tai, mamba, nyoka, na hata samaki.
Kwa kweli, watu walianza kufuga wanyama zamani sana. Muda mrefu kabla ya Yakobo na Pliny kuandika, Wamisri waliwafuga wanyama wa mwituni. Katika sehemu fulani leo, wanyama wengi wanaopatikana katika bustani za wanyama hufugwa nyumbani pia.
Jinsi Walivyoishi na Wanadamu Zamani
Biblia, ambacho ni kitabu cha zamani zaidi cha historia ya wanadamu, husema kwamba mtu wa kwanza, Adamu, aliwapa wanyama majina. Biblia inasema hivi: “Jina ambalo huyo mtu aliita kila nafsi hai, kila mmoja, hilo likawa jina lake. Basi huyo mtu alikuwa akiita majina wanyama wote wa kufugwa na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila mnyama wa mwituni.” (Mwanzo 2:19, 20) Yamkini Adamu aliwachunguza wanyama kwa makini sana ili awape majina yanayowafaa. Lakini hakuhitaji ulinzi, hata kutokana na wanyama wa mwituni. Aliishi kwa amani pamoja nao, na bila shaka alifurahia kuwa nao!
Mungu aliwapa Adamu na mke wake, Hawa, daraka la kuwatunza wanyama. Kupatana na kusudi la Mungu linaloonyeshwa katika Biblia, wanadamu walipaswa “watawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na wanyama wa kufugwa na dunia yote na kila mnyama anayetembea juu ya dunia.”—Mwanzo 1:26.
Uhusiano wa Karibu Wenye Kudumu
Watu wanapowaongoza wanyama vizuri, matokeo huwa mazuri. Mnyama anayependwa anaweza kuonwa kuwa rafiki anayethaminiwa, hata kuonwa kuwa mshiriki wa familia. Ilikuwa hivyo pia maelfu ya miaka iliyopita kama inavyoonyeshwa katika simulizi la Biblia kuhusu “mwana-kondoo jike mmoja, aliye mdogo” wa mtu mmoja maskini. Nabii Nathani alimweleza Mfalme Daudi jinsi mtu huyo maskini alivyomtunza mwana-kondoo aliposema: “Kondoo huyo alikuwa akila tonge lake, na kunywa kutoka katika kikombe chake, naye alikuwa akilala kifuani pake, na kondoo huyo akawa kama binti kwake.”—2 Samweli 12:1-3.
Watu wengi leo wanaweza kuelewa jinsi mnyama anavyoweza kupendwa kama mshiriki wa familia. Fikiria familia moja inayoishi karibu na Harare, jiji kuu la Zimbabwe. Wazazi walimnunulia kila mmoja wa watoto wao mbwa. Mvulana wao mmoja mwenye umri wa miaka minane hivi alipokuwa akitembea na mbwa wake, kwa ghafula nyoka mkubwa mwenye sumu anayeitwa songwe alianguka mbele yake kutoka mtini. Nyoka huyo alimshambulia mtoto, lakini mbwa aliingilia kati upesi na kumwokoa. Je, unaweza kuwazia jinsi mbwa huyo alivyothaminiwa na familia hiyo?
Viziwi wanawathamini sana mbwa waliozoezwa kuwasaidia. Mwanamke mmoja anasimulia hivi: “Twinkie anaposikia kengele, yeye huja na kunigusa mguuni na kunipeleka kwenye mlango wa mbele. Anaposikia saa ya joko ikilia, Twinkie hunikimbilia, nami humfuata. Kukiwa na king’ora cha moshi au moto, Twinkie amezoezwa kunionya na kisha hulala chini kuonyesha kuna hatari.”
Kuna uhusiano wa pekee kati ya vipofu na mbwa wa kuwaelekeza. Mwandishi wa kitabu The Eyes That Lead, Michael Tucker ambaye huwazoeza mbwa, anasema kwamba mbwa aliyezoezwa kumwongoza kipofu anaweza kubadili kabisa maisha yake, na kumfanya “awe huru, ajitegemee, aweze kutembea, na awe na mwandamani.” Ama kweli, uhusiano mzuri kati ya mbwa hao na wenyewe ni jambo la kupendeza!
Hivyo ndivyo watu ambao wamelemaa katika njia nyinginezo huhisi pia kuhusu mbwa wao. Mwanamke mmoja anayelazimika kutumia kiti cha magurudumu, ana mbwa ambaye amezoezwa kuinua kipokezi cha simu na kuramba stempu za barua! Mbwa mwingine anajua amri 120, hata kuchukua mikebe na pakiti kutoka kwenye rafu za duka. Mwenye mbwa huyo ni mlemavu na hutumia kifaa cha leza kuonyesha bidhaa ambazo amechagua, na mbwa huyo humpelekea bidhaa hizo.
Wanyama-vipenzi huwafaidi wazee pia. Daktari wa wanyama alisema kwamba wanyama-vipenzi, kutia ndani mbwa, “huwasaidia wazee kuwa na kusudi maishani wakati huu ambapo jamii imewapuuza.” Gazeti The Toronto Star linaripoti hivi: “Wanyama-vipenzi huwasaidia watu wasifadhaike, wasiugue mara nyingi, na hata wapone baada ya kupatwa na mshtuko wa moyo.”
Kitabu The New Encyclopædia Britannica kinatoa maelezo haya ya kupendeza: “Kuwatunza wanyama-vipenzi hutoa fursa ya kuwafundisha watoto kwamba kuna faida kuchukua madaraka kwa uzito na pia kuwafundisha kuhusu ngono. Watoto huwaona wanyama hao wakijamiiana, na baadaye kupata mimba na matatizo mbalimbali wanayopata wakati wa kuzaa na kuwatunza watoto.”
Kuwapenda na Kuwatunza Wanyama-Vipenzi
Watu fulani huwapenda wanyama kuliko watu wa familia kwa sababu wanyama hao ni waaminifu sana. Katika kesi za talaka, wakati mwingine wanyama huonwa kuwa sehemu ya mali zinazogawanywa kati ya wenzi. Hata wengine wameandika katika wasia kwamba sehemu kubwa ya mali zao nyingi irithiwe na wanyama-vipenzi.
Basi haishangazi kwamba kuna biashara nyingi zinazohusiana na wanyama-vipenzi! Kuna vitabu na magazeti ambayo yanaeleza mambo mengi sana kuhusu wanyama-vipenzi. Wanapotambua kwamba watu wenye wanyama-vipenzi wako tayari kuwastarehesha wanyama wao kwa vitu vya bei ghali, wafanyabiashara huuza vitu mbalimbali vya wanyama.
Kwa mfano, kuna madaktari stadi wanaotibu magonjwa ya wanyama ya kila aina. Kuna madaktari wa akili wanaoweza kupendekeza dawa ya kumsaidia mnyama aliyeshuka moyo. Isitoshe, kuna mawakili, mawakala wa bima, na vilevile huduma za kuwasafisha na taasisi za kuwazoeza. Pia wanyama hao hufanyiwa mazishi. Vilevile kuna huduma za bei ghali za kuwazalisha wanyama kwa kutumia chembe za urithi!
Ni wazi kwamba wanyama wanapendwa sana. Katika kitabu chake The Animal Attraction, Dakt. Jonica Newby anasema hivi: “Mbwa anapotukimbilia akitikisa mkia wake na kuturamba kana kwamba kuja kwetu nyumbani ndilo jambo bora siku hiyo, unaweza kusema huo ni ‘upendo.’” Kwa hakika inaeleweka ni kwa nini watu wengi wenye wanyama-vipenzi huchochewa ‘kuwapenda’ wanyama wao pia.
Hata hivyo, kuwatendea wanyama kama wanadamu ni hatari. Hilo ni kweli kwa kuwa mnyama hawezi kumwandalia mtu mahitaji ambayo yanapaswa kuandaliwa na wanadamu. Isitoshe, kuwapatanisha wanyama-vipenzi na hali za jijini huwasababishia baadhi ya wanyama hao na wenyewe matatizo. Tutazungumzia mambo hayo katika makala inayofuata.
-
-
Dumisha Maoni Yanayofaa Kuhusu Wanyama- VipenziAmkeni!—2004 | Februari 22
-
-
Dumisha Maoni Yanayofaa Kuhusu Wanyama- Vipenzi
KAMA ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, wanadamu walipewa daraka la kutunza dunia na wanyama wote. Biblia inasema hivi: “Kila kitu [Mungu amekiweka] chini ya miguu yake: kondoo na mbuzi na ng’ombe, wote hao, na pia wanyama wa porini, ndege wa mbinguni na samaki wa baharini.”—Zaburi 8:6-8; 115:16.
Ni muhimu wanadamu wazingatie jinsi wanavyowatendea wanyama. Neno la Mungu linasema hivi: “Mwadilifu anatunza nafsi ya mnyama wake wa kufugwa.” (Methali 12:10) Kwa kweli, sheria ambazo Mungu aliwapa Waisraeli zilikazia uhitaji wa kuwajali wanyama. (Kumbukumbu la Torati 22:4, 10; 25:4) Kadiri wanadamu wanavyoendelea kutekeleza daraka lao, wamekuwa na uhusiano wa karibu na wanyama wa kufugwa na hata wamewafuga wanyama wa mwituni.—Mwanzo 1:24.
Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba Biblia huonyesha kuna tofauti kati ya wanadamu na wanyama. Wanadamu ndio walioumbwa ‘kwa mfano na sura ya Mungu’ wala si wanyama. (Mwanzo 1:26) Isitoshe, ingawa wanadamu waliumbwa waishi milele duniani, haikuwa hivyo kwa wanyama. (Mwanzo 3:22, 23; Zaburi 37:29) Yesu Kristo alisema kwamba ili tufurahie “uzima wa milele,” ni lazima tumwamini Mungu na tujifunze kumhusu—mambo ambayo wanyama hawawezi kuyafanya. (Yohana 3:36; 17:3) Isitoshe, Biblia inawalinganisha wale ambao hawastahili kufufuliwa na “wanyama wasiofikiri waliozaliwa kiasili ili kukamatwa na kuangamizwa.”—2 Petro 2:9-12.
Waliumbwa Kuwafaidi Wanadamu
Mungu aliwaumba wanyama kwa ajili ya wanadamu. Wanyama wanaweza kuwasaidia wanadamu kufanya kazi zao na wanaweza kuwa marafiki au wanyama-vipenzi. Pia wanaonyesha upendo na hekima ya Mungu. Ama kweli, inapendeza kuona uzuri wa wanyama na kujifunza mengi kumhusu Muumba kwa kuchunguza hekima yao ya kisilika yenye kustaajabisha. (Zaburi 104:24; Methali 30:24-28; Waroma 1:20) Wadudu ni mfano mmoja wa hekima hiyo. Inastaajabisha jinsi nyuki huwasiliana na kufuata harufu zinazoongoza kwenye chakula na kujenga mizinga iliyo tata sana.
Wanadamu wanaweza kula wanyama. Mwanzoni Mungu aliwaruhusu wanadamu wale mimea tu. Lakini zaidi ya miaka 1,600 baadaye—kufuatia Furiko la siku ya Noa—Mungu alisema hivi: “Kila mnyama anayetembea ambaye yuko hai anaweza kuwa chakula chenu. Kama nilivyowapa mimea ya majani, nawapeni hao wote.” (Mwanzo 1:29; 9:3) Hivyo, Mungu aliwaruhusu wanadamu kula wanyama. Inaonekana Mungu aliwaruhusu wanadamu wale nyama kwa faida yao ijapokuwa hakuwa ameruhusu jambo hilo mwanzoni.
Matatizo Kati ya Wanyama-Vipenzi na Wanadamu
Inaonekana kwamba katika historia yote, wanyama-vipenzi hawakufugwa ndani ya nyumba na ndivyo ilivyo katika sehemu nyingi duniani. Hata hivyo, siku hizi watu wamehamia mijini na wamekuwa matajiri, hivyo wanafuga wanyama-vipenzi ndani ya nyumba. Jambo hilo limeleta matatizo katika nchi zilizoendelea.
Inakadiriwa kwamba kuna wanyama-vipenzi milioni 500 duniani, na asilimia 40 hivi wanapatikana Marekani. Mbwa milioni 59 hivi na paka milioni 75 hufugwa huko. Lakini idadi ya wanyama wanaofugwa katika kila nyumba huko London na Paris ni kubwa kuliko ya New York City!
Miaka michache iliyopita huko Paris, pikipiki ndogo 70 zilikodishwa kusafisha kinyesi cha mbwa barabarani. Ilikadiriwa kwamba mbwa 250,000 wanaopatikana Paris walikunya tani 25 za kinyesi kila siku, na ni kiasi kidogo sana kilichoondolewa na pikipiki. Inasemekana kwamba kila mwaka, mamia ya watu walijeruhiwa na kulazwa hospitalini baada ya kuteleza juu ya kinyesi.
Isitoshe kuna tatizo la kelele. Watu fulani wenye mbwa huvumilia tabia za wanyama hao kuliko wanavyoweza kuvumilia za wanadamu. Kulingana na kituo cha Internet kinachoitwa Utunzaji wa Wanyama-Vipenzi, “inaonekana watu wenye mbwa wanaobweka sana wamezoea kelele hizo.” Kwa mfano, wengine hawawazuii mbwa wao kubweka hata kama kelele hiyo inazuia mazungumzo muhimu.
Kwa upande mwingine, mbwa anaweza kuwa mtulivu na mwenye furaha akiwa pamoja na bwana wake, lakini mwenye kusumbua majirani sana wakati bwana wake hayuko. Ni kweli kwamba watu wanaofuga wanyama huenda wakawapenda licha ya kasoro hizo, lakini jirani anayefanya kazi kwa zamu au mama anayejaribu kumbembeleza mtoto alale huenda asielewe jambo hilo. Isitoshe, wanyama wanaweza kusitawisha tabia mbaya na hata kuwa wakali wanapohuzunika.
Tatizo lingine la wanyama-vipenzi jijini ni kwamba wanazaana haraka. Inakadiriwa kwamba mbwa milioni 17 na paka milioni 30 huzaliwa kila mwaka huko Marekani. Mamilioni ya wanyama hao huishi kwenye vituo vya kutunza wanyama ambako inakadiriwa kwamba kila mwaka wanyama milioni nne hadi sita huuawa.
Kwa nini wanyama wengi hupelekwa kwenye vituo hivyo? Mara nyingi ni kwa sababu watu humpenda mnyama kwa muda mfupi tu. Kitoto maridadi cha mbwa au cha paka hukua na kuhitaji utunzaji. Lakini hakuna yeyote nyumbani mwenye wakati na subira ya kucheza au kumzoeza mnyama huyo. Dakt. Jonica Newby, ambaye ni mwandishi na mtaalamu wa wanyama, anasema hivi: “Tofauti na wengi wanavyodhani, uchunguzi uliofanywa ulimwenguni pote unaonyesha kwamba nusu ya mbwa wanaopelekwa katika vituo vya utunzaji hawajatupwa, bali wamepelekwa huko na wenyewe ambao hawawezi kuvumilia tena kelele, uharibifu, na usumbufu wao.”
Habari moja kuhusu idadi kubwa ya wanyama-vipenzi inasema hivi kuhusu hali hiyo: “Wanyama wamekuwa kama takataka, wanakumbatiwa wanapokuwa wachanga na kutupwa wanaposumbua. Kutowajali wanyama jinsi hiyo kumeongezeka na kunaharibu utamaduni wetu.”
Mambo Muhimu Tunayopaswa Kufikiria
Tunapaswa kufikiria sana kabla ya kufuga wanyama, hasa mjini. Wanyama wenye afya wanahitaji mazoezi kila siku. “Uchunguzi wa Kitaifa Kuhusu Wanyama-Vipenzi na Wanadamu” nchini Australia ulisema hivi: “Mbwa anahitaji kutembea na kufanya mazoezi mengine ili awe na afya na kuchochea ubongo wake. Inaweza kuwa vigumu kushughulika na mbwa wasiopata mazoezi ya kutosha.” Lakini wengi wanaofuga mbwa huwa wamechoka sana baada ya kufanya kazi ngumu mchana hivi kwamba hawawezi kuwatembeza ili watumie nguvu zao.
Hivyo wale wanaotaka kufuga wanyama-vipenzi wanapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, nitaweza kumtunza vizuri mnyama huyo? Je, maisha yangu ya kila siku yatamfanya awe peke yake kwa muda mrefu? Je, nitapata wakati wa kumtembeza au kucheza naye? Iwapo mbwa wangu anahitaji mazoezi, niko tayari kumzoeza au kumpeleka katika shule ya kuwazoeza mbwa? Je, kuwa na mnyama kutanizuia kufanya mambo muhimu zaidi?’
Jambo lingine la kuzingatia ni kwamba kuwa na mnyama kunaweza kugharimu sana. Uchunguzi uliofanywa kuhusu watu wanaofuga wanyama ulionyesha kwamba gharama za kumtibu mbwa mmoja kila mwaka huko Marekani zilikuwa dola 196 na za paka dola 104. Hiyo haitii ndani gharama za chakula na mahitaji ya kila siku. Isitoshe katika maeneo fulani kuna gharama za kuwasajili wanyama.
Ni Vigumu Kuwa na Maoni Yanayofaa
Muumba wetu hufurahi tunapopendezwa na kuwatunza wanyama aliowaumba. Basi je, hukubali kwamba ni vibaya kuwatesa wanyama? Lakini watu wengine hufurahi kuwaona wanyama kama vile fahali, mbwa, na kuku wakiteseka na kuuana wanapopigana. Inasikitisha kwamba wanadamu hawawatendei wanyama kwa huruma kama vile Mungu alivyokusudia.
Kwa upande mwingine, watu wengine huwahangaikia wanyama sana na kupuuza mambo muhimu zaidi. Kwa kweli, wanyama wanapopendwa kupita kiasi, huenda uhai wao ukaonwa kuwa muhimu kuliko wa wanadamu. Kwa mfano, moto ulipotokea katika hospitali moja ya wanyama, wenyewe walikusanyika nje na inasemekana wengine “walijaribu kuwapita wazimamoto wakisema kwamba eti wanataka kufa na wapenzi wao.”
Bila shaka ni jambo la kuhuzunisha sana kumwona mnyama-kipenzi akifa. Lakini hata katika hali hiyo, tunapaswa kuwa na maoni yanayofaa. Kama tulivyoona mapema, wanyama hawakuumbwa kwa mfano wa Mungu wala hawakukusudiwa waishi milele kama wanadamu. Biblia inasema hivi kuhusu jinsi Mungu alivyowaumba wanadamu: “Tena ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao.” Lakini haisemi hivyo kuhusu wanyama.—Mhubiri 3:11, Union Version.
Hivyo, Biblia haisemi kwamba ni kosa kuwaua wanyama. Ama kweli, wao huliwa na mamilioni ya watu. Lakini vipi kumwua mnyama-kipenzi anayeugua na kuteseka? Huo ni uamuzi mgumu na wenye kuhuzunisha! Mwenyewe anaweza kuamua kwamba kufanya hivyo haraka bila kumuumiza ni bora kuliko kurefusha maisha ya mnyama-kipenzi kwa matibabu yanayogharimu sana na kumfanya ateseke zaidi. Na huenda kurefusha maisha yake kukasababisha hali ngumu ya kifedha katika familia.
Kwa kuwa Mungu anawapenda wanadamu sana, je, hatupaswi kuwapenda na kuwajali wanyama ambao ametupatia tuwatunze? Wale walio na upendo kama huo wamevutiwa na tumaini la kufurahia wanyama kama vile Muumba wetu alivyokusudia mwanzoni. Makala ya kumalizia katika mfululizo huu itazungumzia jambo hilo.
-
-
Furahia Wanyama MileleAmkeni!—2004 | Februari 22
-
-
Furahia Wanyama Milele
KUNA wanyama wengi wa aina mbalimbali, na inaonekana kila mmoja ana tabia na sifa tofauti! Kuwapenda na kuwahurumia wanyama humfanya mtu amkaribie Muumba wao. Maria alijionea jambo hilo.
Karibu miaka mitatu iliyopita, wakati Maria alipoishi Lisbon, Ureno, mbwa wake kipenzi alipotea na kutangazwa kwenye redio. Shahidi mmoja wa Yehova alikuwa na uhakika kwamba alimwona mbwa kama yule aliyetajwa, basi akawasiliana na Maria. Walipokutana, walienda na kumpata mbwa. Shahidi huyo alimwambia Maria kwamba kwa kuwa anawapenda wanyama, atafurahia kuishi katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. Alimweleza kwamba wakati huo wanadamu wataishi kwa amani na wanyama.
Maria alikubali mwaliko wa kuhudhuria mkutano wa Mashahidi. Mambo aliyosikia na kuona huko yalimchochea hivi kwamba akataka kujifunza Biblia. Funzo lilipoendelea, Maria alichochewa sana na yale aliyojifunza kumhusu Yehova Mungu na ahadi yake ya uzima wa milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. (Zaburi 37:29; Yohana 17:3) Mwishowe alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa katika Februari 16, 2002.
Kusudi la Mungu la Awali
Kama Maria, wengi wamefurahi kutambua kwamba kusudi la awali la Mungu la kwamba wanadamu waishi milele katika paradiso duniani na kuwatunza wanyama wote, litatimizwa hatimaye. (Mwanzo 1:28) Biblia inasema kwamba Mungu “hakuiumba [dunia] tu bila sababu,” lakini “aliiumba ili ikaliwe na watu.” Hivyo kulingana na ahadi ya Biblia, wanadamu walipaswa kufurahia dunia pamoja na wanyama milele.—Isaya 45:18.
Biblia pia inakazia kwamba Mungu anakusudia kutimiza kusudi lake la awali la kufanya dunia kuwa paradiso. Anasema hivi, “Mimi nimesema hilo,” na kuongezea, “pia nitalitenda.” Yehova anasema hivi: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 46:11; 55:11.
Ni wazi kwamba mwanzoni Mungu alikusudia wanadamu wafurahie paradiso duniani milele. Tuna hakika kabisa kwamba hatimaye kusudi hilo litatimia. Hebu tuchunguze jinsi Biblia inavyoelezea maisha katika ulimwengu mpya wa Mungu. Tutaona kwamba wanyama wote, wawe ni wa kufugwa au wa mwituni, wataishi kwa amani wao kwa wao na pamoja na wanadamu.—Isaya 65:17, 21-25; 2 Petro 3:13.
Wanyama-Vipenzi Katika Ulimwengu Mpya
Katika ulimwengu mpya wa Yehova, watu watagusa manyoya ya simba, wataipapasa ngozi ya simbamarara, na hata kulala msituni bila kuogopa kushambuliwa na wanyama. Ona ahadi hii ya Mungu: “Hakika mimi nitamkomesha katika nchi mnyama-mwitu mwenye kudhuru, nao [wanadamu] kwa kweli watakaa nyikani kwa usalama na kulala katika misitu.”—Ezekieli 34:25; Hosea 2:18.
Wakati huo wanyama wa mwituni watawatii hata watoto wachanga! Biblia inasema hivi: “Mbwa-mwitu kwa kweli atakaa pamoja na mwana-kondoo kwa muda fulani, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi, na ndama na mwana-simba mwenye manyoya shingoni na mnyama aliyelishwa vizuri wote pamoja; na mvulana mdogo atakuwa kiongozi juu yao.”
Lakini mambo bado! Andiko hilo linaendelea kusema hivi: “Ng’ombe na dubu watakula pamoja; watoto wao watalala pamoja. Na hata simba atakula majani kama ng’ombe. Na mtoto anayenyonya hakika atacheza juu ya shimo la nyoka; na mtoto aliyeachishwa kunyonya atatia mkono wake juu ya tundu la kupitishia nuru la nyoka mwenye sumu. Hawatasababisha madhara yoyote wala kusababisha uharibifu wowote katika mlima wangu wote mtakatifu; kwa maana dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:6-9.
Katika ulimwengu mpya wa Yehova, hakutakuwa na tatizo la msongamano wa watu katika majiji makubwa ambayo hayawafai wanadamu na wanyama wao. Ni kweli kwamba hata leo watu wengi wanafurahia wanyama wao na wengi wana maoni yanayofaa kuwahusu na wanawatunza. Lakini hebu wazia taraja zuri la kufurahia wanyama-vipenzi milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu! Utunzaji bora watakaopata utamtukuza sana Muumba Mtukufu wa vitu vyote vilivyo hai.
Iwapo bado hujajifunza kuhusu mambo mazuri ambayo Mungu amekusudia—kama Maria alivyokuwa kabla ya kujifunza—tunakuomba kwa uchangamfu uwasiliane na wachapishaji wa gazeti hili au Shahidi wa Yehova ambaye atafurahia kukufundisha mambo hayo.
-