-
Usitawi wa Muundo wa TengenezoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Tayari katika miaka ya 1870, Ndugu Russell alikuwa akizuru vile vikundi vya Wanafunzi wa Biblia—vya watu wawili na vya watatu pamoja na vikundi vikubwa zaidi—ili kuwajenga kiroho. Ndugu wengine wachache walishiriki katika miaka ya 1880. Halafu, katika 1894, mipango ilifanywa kwa Sosaiti ili wasemaji waliostahili vizuri wasafiri kwa ukawaida zaidi ili kusaidia Wanafunzi wa Biblia wakue katika ujuzi na uthamini kwa ajili ya kweli na kuwavuta karibukaribu zaidi.
Ikiwezekana, msemaji alikuwa akitumia siku moja au labda siku kadhaa pamoja na kikundi, akitoa hotuba moja au mbili za watu wote na kisha, kuzuru vile vikundi vidogo zaidi na watu mmoja-mmoja ili kuzungumza mambo yenye kina zaidi ya Neno la Mungu. Jitihada ilifanywa ili kila kikundi katika Marekani na Kanada kitembelewe mara mbili kwa mwaka, ingawa kwa kawaida si ndugu yuleyule alifanya hivyo. Katika kuteua wasemaji hao wasafirio, mkazo uliwekwa juu ya upole, unyenyekevu, na uelewevu mzuri wa kweli pamoja na ushikamano kwayo wa uaminifu-mshikamanifu na uwezo wa kuifundisha kwa uwazi. Wao hawakuwa jamii ya wahudumu wenye kulipwa. Waliandaliwa tu chakula na mahali pa kulala na ndugu wenyeji, na kwa kadiri ilivyohitajiwa, Sosaiti iliwasaidia kwa gharama za usafiri. Wakaja kujulikana kuwa “mapilgrimu” (wasafiri).
Wengi kati ya wawakilishi hao wa Sosaiti wasafirio walipendwa sana na wale waliotumikia. A. H. Macmillan, Mkanada, anakumbukwa kuwa ndugu ambaye kwake Neno la Mungu lilithibitika kuwa “kama moto uwakao.” (Yer. 20:9) Alilazimika kuongea juu yalo, naye aliongea, akisema kwa wasikilizaji katika Kanada na pia katika sehemu nyingi za Marekani na nchi nyinginezo. William Hersee, pilgrimu mwingine, hukumbukwa kwa shauku nyingi kwa sababu ya uangalifu wa pekee aliowapa vijana. Sala zake pia ziliacha uvutano wenye kudumu akilini mwao kwa sababu zilionyesha hali ya kiroho yenye kina iliyovuta sana mioyo ya wote vijana kwa wazee.
Usafiri haukuwa rahisi kwa mapilgrimu katika siku hizo za mapema. Kwa kielelezo, ili kutumikia kikundi karibu na Klamath Falls, Oregon, Edward Brenisen alisafiri kwanza kwa garimoshi, kisha usiku kwa gari la kukokotwa na farasi, na hatimaye kwa kigari chenye kutikisatikisa wasafiri kilipokuwa kikisafiri milimani kuelekea kwenye shamba ambako wangekutana. Mapema asubuhi, siku baada ya mkutano wao, ndugu mmoja alimpa farasi amwendeshe kilometa zipatazo 100 kwenda kwenye kituo cha garimoshi kilichokuwa karibu zaidi ili aweze kusafiri kwenda kwenye mgawo wake uliofuata. Yalikuwa maisha magumu, lakini jitihada za mapilgrimu zilikuwa na matokeo mazuri. Watu wa Yehova waliimarishwa, wakaunganishwa pamoja katika uelewevu wao wa Neno la Mungu, na wakavutwa pamoja karibu zaidi hata ingawa walitawanyika sana kijiografia.
Katika 1926, Ndugu Rutherford alianza kutumia mipango iliyobadili kazi ya mapilgrimu kutoka ile ya wasemaji wasafirio tu kuwa ile ya wasimamizi na waendelezaji wasafirio wa utumishi wa shambani wa makutaniko. Ili kukazia madaraka yao mapya, katika 1928 waliitwa waelekezi wa utumishi wa kimkoa.
-
-
Usitawi wa Muundo wa TengenezoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
a Kutoka 1894 hadi 1927, wasemaji wasafirio waliopelekwa na Sosaiti walijulikana kwanza kuwa wawakilishi wa Tower Tract Society, kisha kuwa mapilgrimu. Kutoka 1928 hadi 1936, kukiwa na mkazo ulioongezeka juu ya utumishi wa shambani, waliitwa waelekezi wa utumishi wa kimkoa. Kuanzia na Julai 1936, ili kukazia uhusiano wao ufaao na ndugu wenyeji, wakaja kujulikana kuwa watumishi wa kimkoa. Kutoka 1938 hadi 1941, watumishi wa kanda (eneo) ya dunia walipewa migawo kufanya kazi pamoja na idadi ndogo ya makutaniko kwa njia ya mzunguko, na hivyo kurudi kwenye vikundi vilevile kwa vipindi vya ukawaida. Baada ya kukatizwa kwa kama mwaka mmoja, utumishi huo ulianzishwa upya katika 1942 kukiwa na watumishi kwa akina ndugu. Katika 1948 maneno mtumishi wa mzunguko yalianza kutumiwa; sasa, mwangalizi wa mzunguko.
Kutoka 1938 kufika 1941, watumishi wa kimkoa, wakiwa na daraka jipya, walitumikia makusanyiko ya mahali kwa ukawaida, ambapo Mashahidi kutoka kanda ndogo ya dunia walikutana kwa ajili ya programu ya pekee. Kazi hiyo ilipoanzishwa upya katika 1946, waangalizi hao wasafirio walijulikana kuwa watumishi wa wilaya; sasa, waangalizi wa wilaya.
-