-
Yule Mfinyanzi Mkuu na Kazi YakeMnara wa Mlinzi—1999 | Februari 1
-
-
Yule Mfinyanzi Mkuu na Kazi Yake
“[Uwe] chombo kwa kusudi lenye kuheshimika, . . . kilichotayarishwa kwa kila kazi njema.”—2 TIMOTHEO 2:21.
1, 2. (a) Uumbaji wa Mungu wa mwanamume na mwanamke ulikuwaje kazi yenye kutokeza? (b) Mfinyanzi Mkuu aliwatokeza Adamu na Hawa kwa kusudi gani?
YEHOVA ndiye Mfinyanzi Mkuu. Kuumbwa kwa Adamu, mzazi wetu wa kwanza, kulikuwa kazi yenye kutokeza zaidi kati ya uumbaji wake. Biblia hutuambia: “Yehova Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai,” yaani, “kiumbe kinachopumua.” (Mwanzo 2:7, NW, kielezi-chini) Mwanadamu wa kwanza kuumbwa alikuwa mkamilifu, amefanyizwa hasa kwa mfano wa Mungu, uthibitisho wa hekima Yake ya kimungu na kupenda kwake uadilifu wa kweli na pia haki.
2 Akitumia ubavu wa Adamu, Mungu pia alifinyanga—mwanamke—kikamilisho na msaidizi wa mwanamume. Urembo wa Hawa usio na dosari ulipita kabisa hata ule wa wanawake ambao ni warembo zaidi siku hizi. (Mwanzo 2:21-23) Isitoshe, wenzi wa kwanza wa kibinadamu walipewa miili na uwezo mbalimbali uliobuniwa kikamilifu ili kutimiza mradi waliogawiwa wa kufanya dunia hii kuwa paradiso. Walipewa pia uwezo wa kutekeleza amri ya Mungu iliyotolewa kwenye Mwanzo 1:28: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.” Hatimaye, mabilioni ya wanadamu wenye shangwe wangekuwa wakazi wa bustani hii ya ulimwenguni pote, wakiwa wameunganishwa pamoja katika aina ya upendo ambao ni “kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:14.
3. Wazazi wetu wa kwanza walikuja kuwa vyombo visivyoheshimika jinsi gani, na matokeo yakawa nini?
3 Kwa kusikitisha, wazazi wetu wa kwanza waliamua kuasi dhidi ya mamlaka ya Muumba wao Mwenye Enzi Kuu, Mfinyanzi Mkuu. Mwenendo wao ukawa kama ifafanuliwavyo kwenye Isaya 29:15, 16: “Ole wao wanaojitahidi kumficha BWANA mashauri yao, na matendo yao yamo gizani, nao husema, Ni nani atuonaye? nani atujuaye? . . . . Je! mfinyanzi ahesabiwe kuwa kama udongo; kitu kilichofinyangwa kimnene yeye aliyekifinyanga, Hakunifinyanga huyu; au kitu kilichoumbwa kimnene yeye aliyekiumba, Yeye hana ufahamu?” Upotovu wao ulitokeza msiba—hukumu ya kifo cha milele. Isitoshe, jamii yote ya kibinadamu iliyotokana nao ilirithi dhambi na kifo. (Waroma 5:12, 18) Uzuri wa uumbaji wa Mfinyanzi Mkuu ukatiwa dosari kubwa.
4. Sisi twaweza kutumikia kusudi gani lenye kuheshimika?
4 Hata hivyo, hata tukiwa katika hali yetu ya sasa isiyo kamilifu, sisi wazao wa Adamu mwenye dhambi twaweza kumsifu Yehova kwa maneno ya Zaburi 139:14: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.” Ingawa hivyo, inasikitisha kama nini kwamba kazi ya mikono ya awali ya Mfinyanzi Mkuu imetiwa dosari kubwa hivyo!
Mfinyanzi Apanua Kazi Yake
5. Ustadi wa Mfinyanzi Mkuu ungetumikaje?
5 Kwa kufurahisha, mbali na uumbaji wake wa kwanza wa wanadamu, Muumba wetu angetumia ustadi wake akiwa Mfinyanzi Mkuu kwa kiwango kikubwa hata zaidi. Mtume Paulo atuambia: “Basi, Ewe mtu, kwa kweli wewe ni nani hata uwe ukimjibu Mungu? Hakika je, kitu kilichofinyangwa kitamwambia yeye aliyekifinyanga, ‘Kwa nini ulinifanya mimi kwa njia hii?’ Ama je, mfinyanzi hana mamlaka juu ya udongo wa mfinyanzi kufanya kutokana na donge lilelile chombo kimoja kwa utumizi wenye kuheshimika, kingine kwa utumizi usio wenye kuheshimika?”—Waroma 9:20, 21.
6, 7. (a) Wengi leo huamuaje kufinyangwa kwa ajili ya kutoheshimika? (b) Waadilifu hufinyangwa namna gani kwa utumizi wenye kuheshimika?
6 Naam, baadhi ya vyombo vya Mfinyanzi Mkuu vitafinyangwa kwa utumizi wenye kuheshimika, ilhali vingine vitafinyangwa kwa utumizi usio wenye kuheshimika. Wale wanaoamua kufuatana na ulimwengu unapoingia ndani zaidi na zaidi katika hali ya kutomcha Mungu wanafinyangwa kwa njia ya kuwatambulisha ili waharibiwe. Wakati Mfalme mtukufu, Yesu Kristo, ajapo kuhukumu, vyombo hivyo visivyoheshimika vitatia ndani wanadamu wakaidi walio kama mbuzi ambao, kama vile andiko la Mathayo 25:46 lisemavyo, “wataondoka kuingia katika kukatiliwa-mbali kudumuko milele.” Lakini “waadilifu” walio kama kondoo ambao walifinyangwa kwa utumizi “wenye kuheshimika,” watarithi “uhai udumuo milele.”
7 Kwa unyenyekevu, waadilifu hao watakuwa wamejitiisha chini ya ufinyanzi wa kimungu. Wameingia katika njia ya Mungu ya maisha. Wamekubali shauri hili lipatikanalo kwenye 1 Timotheo 6:17-19: ‘Weka tumaini lako, si juu ya mali zisizo hakika, bali juu ya Mungu, ambaye hututolea sisi vitu vyote kwa utajiri kwa ajili ya ufurahio wetu.’ Wamejitahidi “kufanya mema, kuwa matajiri katika kazi zilizo bora, kuwa wakarimu, tayari kushiriki, wakijiwekea wenyewe kuwa hazina salama msingi bora kwa ajili ya wakati ujao, ili wao wapate kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi.” Kweli ya kimungu huwafinyanga nao hudhihirisha imani thabiti katika uandalizi wa Yehova kupitia Kristo Yesu, “aliyejitoa mwenyewe kuwa fidia inayolingana” ili arudishe kilichopotea kwa sababu ya dhambi ya Adamu. (1 Timotheo 2:6) Basi, twapaswa kunyenyekea kwa utayari ulioje shauri la Paulo la “[kujivika] wenyewe utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya [unafinyangwa] kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba”!—Wakolosai 3:10.
Wewe Utakuwa Chombo cha Aina Gani?
8. (a) Ni nini kinachoamua mtu anakuwa chombo cha aina gani? (b) Ni mambo gani mawili ambayo huelekeza jinsi mtu atavyofinyangwa?
8 Ni nini kinachoamua mtu anakuwa chombo cha aina gani? Ni mtazamo wake na mwenendo wake. Hizo husababishwa kwanza na tamaa na mielekeo ya moyo. Mfalme Solomoni mwenye hekima alisema: “Moyo wa mtu huifikiri njia yake; bali BWANA huziongoza hatua zake.” (Mithali 16:9) Pili, husababishwa na mambo yaliyosikiwa na kuonwa, mashirika na pia mambo yaliyompata mtu. Kwa hiyo, ni muhimu jinsi gani kusikiza shauri hili: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Kama vile andiko la 2 Petro 1:16 lituonyavyo, twapaswa kuepuka kufuata “hadithi zisizo za kweli zilizotungwa kwa usanifu mwingi,” au kulingana na tafsiri ya Katoliki ya Roma ya Knox, “hekaya zilizobuniwa na mwanadamu.” Hadithi hizo zingetia ndani mengi ya mafundisho na misherehekeo ya Jumuiya ya Wakristo iliyoasi.
9. Twaweza kuitikiaje kwa njia ifaayo kufinyangwa na Mfinyanzi Mkuu?
9 Basi, Mungu aweza kutufinyanga kulingana na itikio letu. Twaweza kurudia kwa unyenyekevu mbele za Yehova sala ya Daudi: “Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu, unijaribu, uyajue mawazo yangu; uone kama iko njia iletayo majuto ndani yangu, ukaniongoze katika njia ya milele.” (Zaburi 139:23, 24) Yehova anafanya ujumbe wa Ufalme uhubiriwe. Mioyo yetu imeitikia kwa uthamini habari njema na miongozo zaidi kutoka kwake. Kupitia tengenezo lake yeye hututolea mapendeleo mbalimbali yanayohusiana na kuhubiri habari njema; acheni tuyapokee mapendeleo hayo na kuyathamini sana.—Wafilipi 1:9-11.
10. Twapaswa kujitahidije katika kufuata programu za kiroho?
10 Ni muhimu sana kwamba tukazie Neno la Mungu uangalifu daima, tukifuata programu ya kila siku ya usomaji wa Biblia na kufanya Maandiko na utumishi wa Yehova uwe msingi wa mazungumzo katika familia zetu na miongoni mwa marafiki wetu. Programu ya ibada ya asubuhi, ambayo hufanywa wakati wa kifungua-kinywa na kila familia ya Betheli na pia wamishonari wanaoishi kwenye makao ya wamishonari ya Mashahidi wa Yehova, kwa kawaida hutia ndani usomaji mfupi wa Biblia au kitabu Yearbook cha wakati huo, kila kimoja kikisomwa katika juma tofauti. Je, familia yako yaweza kuwa na mpango kama huo? Sote pia hupokea manufaa zilizoje, kupitia ushirika katika kutaniko la Kikristo, kukutana kwetu pamoja, na hasa kushiriki katika funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma!
Waliofinyangwa Kukabiliana na Majaribu
11, 12. (a) Twaweza kutumiaje shauri la Yakobo kuhusu majaribu katika maisha yetu ya kila siku? (b) Jambo lililompata Yobu latutiaje moyo kushika uaminifu-maadili?
11 Katika maisha yetu ya kila siku, Mungu huruhusu hali fulani zitokee na huenda tukaziona baadhi ya hali hizo kuwa ngumu. Twapaswa kuzionaje? Kama andiko la Yakobo 4:8 linavyoshauri, na tusiwe na uchungu kamwe, bali acheni tumkaribie Mungu, tukimtumaini kwa moyo wetu wote, tukiwa na uhakika kwamba ‘tunapomkaribia, atatukaribia.’ Ni kweli kwamba tutavumilia shida na majaribu, lakini yanaruhusiwa ili yasaidie katika kufinyangwa kwetu, kukiwa na matokeo yenye furaha. Andiko la Yakobo 1:2, 3 latuhakikishia hivi: “Fikirieni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mkutanapo na majaribu ya namna mbalimbali, kama mjuavyo kwamba ubora huu uliojaribiwa wa imani yenu hutokeza uvumilivu.”
12 Yakobo pia asema: “Wakati yuko chini ya jaribu, acheni yeyote asiseme: ‘Mimi ninajaribiwa na Mungu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote. Lakini kila mmoja hujaribiwa kwa kuvutwa na kutongozwa na tamaa yake mwenyewe.” (Yakobo 1:13, 14) Majaribu yetu yaweza kuwa mengi na ya namna mbalimbali, lakini kama hali ya Yobu ilivyokuwa, hayo yote hutimiza fungu fulani katika kufinyangwa kwetu. Ni uhakikisho mkubwa jinsi gani ambao Maandiko yanatutolea kwenye Yakobo 5:11: “Tazameni! Twawatamka kuwa wenye furaha wale ambao wamevumilia. Nyinyi mmesikia juu ya uvumilivu wa Yobu na mmeona tokeo alilotoa Yehova, kwamba Yehova ni mwenye wororo sana katika shauku na mwenye rehema.” Tukiwa kama vyombo mikononi mwa Mfinyanzi Mkuu, na tushike uaminifu-maadili nyakati zote, tukiwa na uhakika kama wa Yobu katika lile litakalotokea!—Ayubu 2:3, 9, 10; 27:5; 31:1-6; 42:12-15.
Kufinyanga Vijana Wetu
13, 14. (a) Wazazi wapaswa kuanza kufinyanga watoto wao lini, wakitazamia matokeo gani hatimaye? (b) Waweza kutaja matokeo gani yenye furaha?
13 Wazazi wanaweza kushiriki kufinyanga vijana wao, tangu utotoni, nao vijana wetu wanaweza kushika uaminifu-maadili kwa njia nzuri kama nini! (2 Timotheo 3:14, 15) Hilo limepata kuwa hivyo hata wakati ambapo majaribu yamekuwa makali mno. Miaka kadhaa iliyopita, mnyanyaso ulipokuwa mkali sana katika nchi fulani ya Afrika, familia yenye kutumainika ilishughulikia uchapaji wa Mnara wa Mlinzi katika kibanda kilichokuwa nyuma ya nyumba yao. Siku moja askari-jeshi walikuwa wakija barabarani, wakiwasaka wanaume vijana kutoka nyumba hadi nyumba ili wawaingize jeshini. Wakati ulikuwa ungali upo kwa wavulana wawili wa familia hiyo kujificha, lakini msako wa askari-jeshi ambao ungefuata ungefichua hiyo matbaa kwa hakika. Jambo hilo lingesababisha kuteswa au labda kuuawa kwa familia yote. Ni nini kingeweza kufanywa? Hao wavulana wawili walisema bila woga, wakitaja kwa ujasiri Yohana 15:13: “Hakuna aliye na upendo mkubwa zaidi kuliko huu, kwamba mtu fulani aisalimishe nafsi yake kwa niaba ya marafiki wake.” Walisisitiza kuendelea kukaa sebuleni. Askari-jeshi hao wangewapata na yaelekea wangewatesa au hata kuwaua wakikataa kuingizwa jeshini. Lakini hawangeendelea na msako wao. Matbaa na washiriki wengine wa familia wangenusurika. Hata hivyo, kulikuwa na matokeo yenye kutokeza. Kwa kweli, askari-jeshi hao waliruka nyumba hiyo na kuelekea kwenye nyumba nyingine! Vyombo hivyo vya kibinadamu ambavyo viliundwa kwa utumizi wenye kuheshimika vilinusurika, pamoja na matbaa na kuendelea kuchapisha chakula cha kiroho kwa wakati ufaao. Mmojawapo wa wavulana hao wawili na dada yake, sasa wanatumikia katika Betheli; na mvulana huyo angali anaendesha mashine hiyo iliyozeeka.
14 Vijana wanaweza kufunzwa namna ya kusali, naye Mungu hujibu sala zao. Mfano wenye kutokeza wa jambo hilo ulitokea wakati wa mauaji ya kinyama ya Rwanda. Wakati binti mwenye umri wa miaka sita na wazazi wake walipowekwa tayari na waasi ili wauawe kwa kombora la kutupwa kwa mkono, binti huyo alisali kwa Yehova kwa sauti kubwa na kwa bidii waweze kunusurika ili waendelee na utumishi wao kwa Yehova. Wale ambao wangewaua kimakusudi walisukumwa kuwanusuru, wakisema, “Hatuwezi kuwaua kwa sababu ya huyu msichana mdogo.”—1 Petro 3:12.
15. Paulo alionya juu ya uvutano gani wenye kufisidi?
15 Vijana wetu walio wengi hawalazimiki kukabiliana na hali ngumu kama hizo ambazo zimefafanuliwa hapo juu, lakini kuna majaribu mengi ambayo siku hizi wanakabiliana nayo shuleni na katika jamii zenye ufisadi: lugha chafu, ponografia, vitumbuizo vilivyoshuka, na kusongwa na marika ili washiriki mazoea mabaya yameenea mahali pengi. Mtume Paulo alionya tena na tena juu ya uvutano huo.—1 Wakorintho 5:6; 15:33, 34; Waefeso 5:3-7.
16. Mtu aweza kuwaje chombo kwa utumizi wenye kuheshimika?
16 Baada ya kuvirejezea vyombo vinavyowekwa ‘baadhi yavyo kwa kusudi lenye kuheshimika lakini vingine kwa kusudi lenye kukosa heshima,’ Paulo asema: “Kwa hiyo, ikiwa yeyote ajiepusha kabisa na hawa wa mwisho, atakuwa chombo kwa kusudi lenye kuheshimika, kilichotakaswa, chenye mafaa kwa mmiliki wacho, kilichotayarishwa kwa kila kazi njema.” Kwa hiyo acheni tuwatie moyo vijana wetu wawe waangalifu kuhusu mashirika yao. Acheni ‘wakimbie tamaa zenye kutukia ujanani, lakini wafuatie uadilifu, imani, upendo, amani, pamoja na wale wamwitiao Bwana kutokana na moyo safi.’ (2 Timotheo 2:20-22) Programu ya familia kwa ajili ya “kujengana” yaweza kuwa yenye manufaa sana katika kufinyanga vijana wetu. (1 Wathesalonike 5:11; Mithali 22:6) Kusoma na kujifunza Biblia kila siku, ukitumia vichapo vya Sosaiti vifaavyo kwaweza kuwa msaada mzuri.
Kufinyangwa kwa Watu Wote
17. Nidhamu itatufinyanga namna gani, kukiwa na matokeo gani yenye shangwe?
17 Ili kutufinyanga, Yehova hututolea shauri kutoka katika Neno lake na kupitia tengenezo lake. Usikinze kamwe shauri hilo la kimungu! Liitikie kwa hekima, na acha likufinyange kwa ajili ya kutumiwa na Yehova katika utumizi wenye kuheshimika. Andiko la Mithali 3:11, 12 latushauri: “Mwanangu, usidharau kuadhibiwa na BWANA, wala usione ni taabu kurudiwa naye. Kwa kuwa BWANA ampendaye humrudi, kama vile baba mwanawe ampendezaye.” Isitoshe, shauri la kibaba latolewa kwenye Waebrania 12:6-11: “[Yule] ambaye Yehova ampenda humtia nidhamu . . . Kweli, hakuna nidhamu ionekanayo kwa wakati wa sasa kuwa yenye shangwe, bali yenye kihoro; lakini baadaye kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo hutoa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” Lazima Neno la Mungu lililopuliziwa liwe ndilo njia kuu ya kutolea nidhamu kama hiyo.—2 Timotheo 3:16, 17.
18. Kuhusu toba, twajifunza nini kutokana na Luka sura ya 15?
18 Yehova pia ni mwenye rehema. (Kutoka 34:6) Toba ya kutoka moyoni ionyeshwapo hata ikiwa dhambi nzito sana imetendwa, yeye husamehe. Hata ‘wapotevu’ wa siku hizi waweza kufinyangwa kuwa vyombo kwa utumizi wenye kuheshimika. (Luka 15:22-24, 32) Huenda dhambi zetu zisiwe nzito kama zile za mwana mpotevu. Lakini itikio letu la unyenyekevu kwa shauri la Kimaandiko litafanya sikuzote tufinyangwe kuwa vyombo kwa utumizi wenye kuheshimika.
19. Twaweza kuendeleaje kutumikia tukiwa vyombo vyenye kuheshimika mikononi mwa Yehova?
19 Tulipojifunza kweli mara ya kwanza, tulionyesha utayari wa kumwacha Yehova atufinyange. Tuliacha njia za kilimwengu, tukaanza kuvaa utu mpya, tukawa Wakristo waliojiweka wakfu na kubatizwa. Tulitii shauri la Waefeso 4:20-24, ‘tukiweka mbali utu wa hapo zamani uliofuatana na njia yetu ya kwanza ya mwenendo, pamoja na tamaa zake za udanganyifu, na kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.’ Sisi binafsi na twendelee kuwa wenye kupindika kwa urahisi mikononi mwa Yehova, Mfinyanzi Mkuu, tukitumikia sikuzote kama vyombo kwa utumizi wenye kuheshimika!
-
-
Hazina Yetu Katika Vyombo vya UdongoMnara wa Mlinzi—1999 | Februari 1
-
-
Hazina Yetu Katika Vyombo vya Udongo
“Sisi tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili nguvu ipitayo iliyo ya kawaida ipate kuwa ya Mungu na si ile ya kutoka katika sisi wenyewe.”—2 WAKORINTHO 4:7.
1. Kielelezo cha Yesu chapaswa kututiaje moyo?
ALIPOKUWA akifinyangwa na Yehova hapa duniani, Yesu alipata kujua moja kwa moja udhaifu mbalimbali wa wanadamu. Kielelezo chake cha kushika uaminifu-maadili chapaswa kututia moyo kama nini! Mtume atuambia: “Kwa kweli, kwenye mwendo huu mliitwa, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia kigezo ili nyinyi mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Kwa kunyenyekea chini ya kufinyangwa huko, Yesu aliushinda ulimwengu. Pia, aliwajasirisha mitume wake wawe washindi. (Matendo 4:13, 31; 9:27, 28; 14:3; 19:8) Na ni kitia-moyo kikubwa kama nini alichotoa katika umalizio wa hotuba yake ya mwisho! Alitangaza hivi: “Nimewaambia nyinyi mambo haya ili kupitia mimi mpate kuwa na amani. Ulimwenguni mnakuwa na dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.”—Yohana 16:33.
2. Tofauti na hali ya upofu ya ulimwengu, sisi tuna mmuliko gani?
2 Vilevile, baada ya kutofautisha hali ya upofu iliyoletwa na “mungu wa huu mfumo wa mambo” na “mmuliko wa habari njema yenye utukufu,” mtume Paulo alisema hivi kuhusu huduma yetu yenye thamani: “Sisi tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili nguvu ipitayo iliyo ya kawaida ipate kuwa ya Mungu na si ile ya kutoka katika sisi wenyewe. Twasongwa katika kila njia, lakini hatufinywi kupita tuwezavyo kusonga; twafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa; twateswa, lakini hatuachwi kabisa bila msaada; twaangushwa chini, lakini hatuangamizwi.” (2 Wakorintho 4:4, 7-9) Ingawa sisi ni “vyombo vya udongo” vilivyo dhaifu, Mungu ametufinyanga sana kwa roho yake takatifu hivi kwamba twaweza kuushinda kabisa ulimwengu wa Shetani.—Waroma 8:35-39; 1 Wakorintho 15:57.
Kufinyanga Katika Israeli la Kale
3. Isaya alifafanuaje kufinyangwa kwa taifa la Kiyahudi?
3 Yehova hufinyanga watu mmoja-mmoja na pia mataifa mazima-mazima. Kwa kielelezo, Israeli la kale liliponyenyekea ufinyanzi wa Yehova, lilisitawi. Lakini hatimaye likajifanya kuwa gumu na kukosa kutii. Tokeo lilikuwa kwamba Mfinyanzi wa Israeli alileta “ole” juu ya taifa hilo. (Isaya 45:9) Katika karne ya nane K.W.K., Isaya alizungumza na Yehova kuhusu hali yenye dhambi ya Israeli iliyokuwa dhahiri, akisema: “Ee BWANA, wewe u baba yetu; sisi tu udongo, nawe u mfinyanzi wetu; sisi sote tu kazi ya mikono yako. . . . Vitu vyetu vyote vyenye kupendeza vimeharibika.” (Isaya 64:8-11) Israeli lilikuwa limefinyangwa kuwa chombo kilichofaa tu kuharibiwa.
4. Ni kielezi kipi ambacho kiliigizwa na Yeremia?
4 Karne moja baadaye, siku ya kutoa hesabu ilipokaribia, Yehova alimwambia Yeremia achukue gudulia la udongo na aende pamoja na wanaume wazee wa Yerusalemu kwenye Bonde la Hinomu, akimwagiza hivi: “Hapo utalivunja gudulia lile, mbele ya macho ya watu wale waendao pamoja nawe, na kuwaambia, BWANA wa majeshi asema hivi, Hivyo ndivyo nitakavyowavunja watu hawa, na mji huu, kama mtu avunjavyo chombo cha mfinyanzi, kisichoweza kutengenezwa tena na kuwa kizima.”—Yeremia 19:10, 11.
5. Hukumu ya Yehova dhidi ya Israeli ilikuwa kubwa kadiri gani?
5 Katika 607 K.W.K., Nebukadneza aliharibu Yerusalemu kabisa pamoja na hekalu lake na kuwapeleka Wayahudi walionusurika utekwani huko Babiloni. Lakini baada ya miaka 70 uhamishoni, Wayahudi wenye kutubu waliweza kurudi na kujenga upya Yerusalemu na hekalu lake. (Yeremia 25:11) Hata hivyo, kufikia karne ya kwanza W.K., taifa hilo lilikuwa limemwacha tena Mfinyanzi Mkuu, na hatimaye hali yake ya kiadili ikashuka kufikia kiwango cha kufanya uhalifu mbaya sana wa kumwua Mwana wa Mungu. Katika 70 W.K., Mungu alitumia Serikali ya Ulimwengu ya Roma kama mfishaji wake katika kufutilia mbali mfumo wa mambo wa Kiyahudi na kuponda tikitiki Yerusalemu na hekalu lake. Taifa la Israeli halingefinyangwa tena kamwe kwa mkono wa Yehova likiwa kitu ‘kitakatifu na kizuri.’a
Kufinyanga Taifa la Kiroho
6, 7. (a) Paulo anafafanuaje kufinyangwa kwa Israeli wa kiroho? (b) Idadi kamili ya “vyombo vya rehema” ni gani, nayo ilifanyizwaje?
6 Wayahudi waliomkubali Yesu walifinyangwa wakawa washiriki wa msingi wa taifa jipya, “Israeli wa Mungu” wa kiroho. (Wagalatia 6:16) Basi, maneno haya ya Paulo yanafaa: “Ama je, mfinyanzi hana mamlaka juu ya udongo wa mfinyanzi kufanya kutokana na donge lilelile chombo kimoja kwa utumizi wenye kuheshimika, kingine kwa utumizi usio wenye kuheshimika? . . . Mungu, ingawa anayo nia ya kuonyesha hasira ya kisasi yake na kujulisha nguvu yake, alivumilia kwa ustahimilivu mwingi vyombo vya hasira ya kisasi vilivyofanywa vifae kuharibiwa, ili apate kujulisha utajiri wa utukufu wake juu ya vyombo vya rehema, alivyotayarisha kimbele kwa ajili ya utukufu.”—Waroma 9:21-23.
7 Yesu aliyefufuliwa alijulisha baadaye kwamba idadi ya “vyombo [hivyo] vya rehema” ingekuwa 144,000. (Ufunuo 7:4; 14:1) Kwa kuwa Israeli la asili halikuwa limetoa idadi hiyo ikiwa kamili, Yehova aliwaonyesha watu wa mataifa rehema. (Waroma 11:25, 26) Kutaniko jipya la Kikristo lilipanuka haraka. Katika muda wa miaka 30 habari njema ilikuwa “[iki]hubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.” (Wakolosai 1:23) Jambo hilo lilihitaji kuyaweka makutaniko mengi ya mahali hapo yaliyokuwa yametawanyika chini ya uangalizi ufaao.
8. Ni nani waliofanyiza baraza linaloongoza la kwanza, na kikundi hicho kilikuaje?
8 Yesu alikuwa ametayarisha mitume 12 ili wawe baraza linaloongoza la kwanza, akiwazoeza mitume hao pamoja na watu wengine kwa ajili ya huduma. (Luka 8:1; 9:1, 2; 10:1, 2) Siku ya Pentekoste 33 W.K., kutaniko la Kikristo lilianzishwa, na kwa wakati upasao baraza lake linaloongoza likapanuliwa kutia ndani “mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu.” Yaonekana, Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, alitumikia kwa kipindi kirefu akiwa mwenyekiti, ingawa yeye hakuwa mtume. (Matendo 12:17; 15:2, 6, 13; 21:18) Kulingana na mwanahistoria Eusebius, mitume walikuwa shabaha ya pekee ya mnyanyaso nao walitawanyika katika maeneo mengine. Muundo wa baraza linaloongoza ulirekebishwa kulingana na hali.
9. Ni tukio gani lenye kusikitisha ambalo Yesu alitabiri lingetokea?
9 Mwishoni mwa karne ya kwanza, ‘yule adui, ambaye ni Ibilisi,’ alianza ‘kupanda magugu’ miongoni mwa warithi wa “ufalme wa mbingu” walio kama ngano. Yesu alikuwa ametabiri kwamba tukio hilo lenye kusikitisha lingeruhusiwa hadi wakati wa kuvuna katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” Ndipo, ‘waadilifu wangeng’aa tena kwa uangavu kama jua katika ufalme wa Baba yao.’ (Mathayo 13:24, 25, 37-43) Huo ungekuwa wakati gani?
Kufinyanga Israeli la Mungu Leo
10, 11. (a) Kufinyangwa kwa Israeli wa Mungu wa siku hizi kulianzaje? (b) Ni mafundisho gani yenye kutofautiana ambayo yangepatikana katika Jumuiya ya Wakristo na miongoni mwa Wanafunzi wa Biblia wenye bidii?
10 Katika mwaka wa 1870, Charles Taze Russell alifanyiza kikundi cha kujifunza Biblia katika Pittsburgh, Pennsylvania, Marekani. Katika mwaka wa 1879 alianza kuchapisha gazeti la kila mwezi ambalo leo laitwa Mnara wa Mlinzi. Punde si punde, wanafunzi hao wa Biblia, kama walivyoitwa, walifahamu kwamba Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imekubali mafundisho ya kipagani yasiyo ya Kimaandiko, kama vile kutokufa kwa nafsi, moto wa helo, purgatori, mungu wa Utatu, na ubatizo wa vitoto vichanga.
11 Ingawa hivyo, jambo la muhimu zaidi ni kwamba hawa wapenda-kweli ya Biblia walirudisha mafundisho ya msingi ya Biblia, kama vile ukombozi kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu, na kufufuliwa kwenye uhai udumuo milele katika dunia paradiso yenye amani chini ya Ufalme wa Mungu. Zaidi ya yote, mkazo uliwekwa juu ya kutetewa karibuni kwa Yehova Mungu kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu. Wanafunzi wa Biblia waliamini kwamba Sala ya Bwana ilikuwa karibu kujibiwa: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe. Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:9, 10) Walikuwa wakifinyangwa na roho takatifu ya Mungu kuwa jamii ya ulimwenguni pote ya Wakristo wapenda-amani.
12. Wanafunzi wa Biblia walikuja kufahamuje tarehe fulani muhimu?
12 Funzo barabara la Danieli sura ya 4 na unabii mwingine mbalimbali uliwasadikisha Wanafunzi wa Biblia kwamba kuwapo kwa Yesu akiwa Mfalme wa Kimesiya lazima kulikuwa kumekaribia. Walifahamu kwamba mwaka wa 1914 ungekuwa tarehe ya kumalizika kwa “nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa.” (Luka 21:24; Ezekieli 21:26, 27) Hao Wanafunzi wa Biblia walipanua utendaji wao kwa haraka, wakifanyiza madarasa ya Biblia (ambayo baadaye yaliitwa Makutaniko) kotekote Marekani. Mwanzoni mwa miaka ya 1900, kazi yao ya kufundisha Biblia ilipanuliwa hadi Ulaya na Australasia. Kuwepo kwa mpango mzuri kukawa jambo la lazima.
13. Wanafunzi wa Biblia walipata uhalali gani wa kisheria, naye msimamizi wa kwanza wa Sosaiti alitoa utumishi gani wenye kutokeza?
13 Ili kuwapa Wanafunzi wa Biblia uhalali wa kisheria, Zion’s Watch Tower Tract Society lilifanywa kuwa shirika mwaka wa 1884 huko Marekani, makao makuu yakiwa Pittsburgh, Pennsylvania. Waelekezi wake walitumika wakiwa Baraza kuu Linaloongoza, wakisimamia kuhubiriwa tufeni pote kwa Ufalme wa Mungu. Msimamizi wa kwanza wa Sosaiti, Charles T. Russell, aliandika mabuku sita ya Studies in the Scriptures na kufanya safari ndefu za kuhubiri. Pia alichanga fedha nyingi alizokuwa amekusanya kabla ya kuanza kujifunza Biblia, kwa ajili ya kazi ya Ufalme ya ulimwenguni pote. Katika mwaka wa 1916, huku Vita Kuu ikiendelea vikali huko Ulaya, Ndugu Russell aliyekuwa mchovu alikufa akiwa katika safari ya kuhubiri. Alikuwa ametoa kila kitu kwa ajili ya kupanua kutolewa kwa ushahidi kuhusu Ufalme wa Mungu.
14. J. F. Rutherford ‘alipiganaje pigano bora’? (2 Timotheo 4:7)
14 Joseph F. Rutherford, ambaye kwa muda alikuwa hakimu katika Missouri, akawa msimamizi aliyefuata. Kwa sababu ya kutetea kwake kweli ya Biblia bila hofu, makasisi wa Jumuiya ya Wakristo waliungana na wanasiasa katika ‘kutunga madhara kwa njia ya sheria.’ Katika Juni 21, 1918, Ndugu Rutherford na Wanafunzi wa Biblia wengine saba wenye kuongoza walifungwa jela, wakiwa wamehukumiwa vifungo mbalimbali vya miaka 10 au 20 ambavyo wangetumikia wakati uleule. Wanafunzi hao wa Biblia walijitetea. (Zaburi 94:20; Wafilipi 1:7) Walipokata rufani, waliachiliwa Machi 26, 1919, na baadaye shtaka la uwongo la uchochezi likaondolewa kabisa.b Jambo hilo lililowapata liliwafinyanga wakawa watetezi hodari wa ile kweli. Kwa msaada wa Yehova walijaribu kila njia iwezekanayo kushinda katika pigano la kiroho la kuhubiri habari njema, licha ya upinzani wa Babiloni Mkubwa. Pigano linaloendelea hadi mwaka huu wa 1999.—Linganisha Mathayo, sura ya 23; Yohana 8:38-47.
15. Kwa nini mwaka wa 1931 ulikuwa muhimu kihistoria?
15 Katika miaka ya 1920 na 1930 Israeli watiwa-mafuta wa Mungu waliendelea kufinyangwa chini ya mwelekezo wa Mfinyanzi Mkuu. Nuru ya kiunabii kutoka katika Maandiko iliangaza, ikitoa utukufu kwa Yehova na kukazia Ufalme wa Kimesiya wa Yesu. Katika mwaka wa 1931 Wanafunzi wa Biblia walishangilia kupokea jina jipya, Mashahidi wa Yehova.—Isaya 43:10-12; Mathayo 6:9, 10; 24:14.
16 na sanduku kwenye ukurasa wa 19. Idadi kamili ya wale 144,000 ilikamilika lini, na kuna uthibitisho gani wa jambo hilo?
16 Katika miaka ya 1930, idadi ya “wale walioitwa na waliochaguliwa na walio waaminifu,” wale 144,000, ilionekana kuwa imekamilika. (Ufunuo 17:14; ona sanduku kwenye ukurasa wa 19.) Hatujui ni wangapi wa watiwa-mafuta waliokusanywa katika karne ya kwanza na waliokusanywa kutoka miongoni mwa “magugu” wakati wa karne za giza za uasi-imani mkubwa wa Jumuiya ya Wakristo. Lakini mwaka wa 1935 kulikuwa na jumla ya wahubiri 52,465 ulimwenguni pote, kati ya kilele cha wahubiri 56,153, walioonyesha tumaini lao la kimbingu kwa kushiriki mifano ya Ukumbusho. Je, ni nini ingekuwa hali ya baadaye ya wengi ambao walikuwa bado wakusanywe?
“Tazama! Umati Mkubwa”
17. Ni tukio gani la kihistoria lililotokea mwaka wa 1935?
17 Kwenye mkusanyiko uliofanywa kutoka Mei 30 hadi Juni 3, 1935, huko Washington, D.C., Marekani, Ndugu Rutherford alitoa hotuba muhimu yenye kichwa “Ile Halaiki Kubwa.”c Kikundi hiki, ‘ambacho hakuna mtu aliyeweza kukihesabu,’ kingetokea wakati ambapo kutiwa muhuri kwa wale 144,000 wa Israeli wa kiroho kungekuwa kukikaribia kukamilika. Hao wa kikundi hicho pia wangedhihirisha imani katika nguvu za kufidi za “damu ya Mwana-Kondoo,” Yesu, na kutoa utumishi mtakatifu katika mpango wa hekalu wa Yehova wa ibada. Wakiwa kikundi, ‘wangetoka katika dhiki kubwa’ wakiwa hai, ili kurithi Paradiso ya kidunia ambapo “kifo hakitakuwapo tena.” Miaka kadhaa kabla ya mkusanyiko huo, kikundi hiki kilikuwa kimesemwa kuwa cha Wayonadabu.—Ufunuo 7:9-17; 21:4; Yeremia 35:10.
18. Mwaka wa 1938 ulikuwa muhimu katika njia zipi?
18 Mwaka wa 1938 ulikuwa muhimu katika kutambulisha waziwazi jamii hizi mbili. Matoleo ya Mnara wa Mlinzi (ya Kiingereza) ya Machi 15 na Aprili 1, 1938, yalikuwa na funzo lenye sehemu mbili lenye kichwa “Kundi Lake” na lilionyesha wazi mahali panapowahusu mabaki watiwa-mafuta na waandamani wao, umati mkubwa. Kisha matoleo ya Juni 1 na Juni 15 (ya Kiingereza) yalikuwa na makala za kujifunza juu ya “Tengenezo,” zilizotegemea Isaya 60:17. Makutaniko yote yaliombwa yatoe ombi kwa Baraza Linaloongoza ili liweke rasmi watumishi katika makutaniko yao, hivyo wakianzisha mpango wa kitheokrasi ulioboreka, wenye kuagizwa na Mungu. Makutaniko yalifanya vivyo hivyo tu.
19 na kielezi-chini. Ni mambo gani ya hakika yathibitishayo kwamba mwito wa kijumla wa “kondoo wengine” umekuwa ukiendelea sasa kwa zaidi ya miaka 60?
19 Ripoti iliyo katika 1939 Yearbook of Jehovah’s Witnesses ilisema: “Wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo Yesu waliomo duniani leo ni wachache, na idadi yao haitaongezeka kamwe. Hawa wanatambulishwa katika Maandiko kuwa ‘mabaki’ ya wazao wa Zayoni, tengenezo la Mungu. (Ufu. 12:17) Sasa Bwana anajikusanyia ‘kondoo wengine,’ ambao watafanyiza ile ‘halaiki kubwa.’ (Yohana 10:16) Wale wanaokusanywa sasa ni waandamani wa mabaki, ambao wanafanya kazi pamoja na mabaki. Tangu sasa na kuendelea, idadi ya wale wanaofanyiza ‘kondoo wengine’ itaongezeka hadi pale ‘halaiki kubwa’ itakapokusanywa.” Mabaki watiwa-mafuta walikuwa wamefinyangwa ili kushughulikia kukusanywa kwa umati mkubwa. Hao pia lazima sasa wafinyangwe.d
20. Ni mabadiliko gani ya kitengenezo ambayo yametokea tangu mwaka wa 1942?
20 Katika Januari 1942, wakati Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipokuwa imechacha zaidi, Joseph Rutherford alikufa naye Nathan Knorr akachukua mahali pake akiwa msimamizi. Msimamizi wa tatu wa Sosaiti anakumbukwa kwa shauku kwa kuanzisha shule za kitheokrasi makutanikoni na Shule ya Gileadi ya kuzoeza wamishonari. Kwenye mkutano wa kila mwaka wa Sosaiti katika 1944, yeye alitangaza kwamba hati ya katiba ya Sosaiti ilikuwa ikisahihishwa ili uanachama utegemee, si michango ya vitu vya kimwili, bali hali ya kiroho. Kipindi cha miaka 30 iliyofuata, idadi ya wafanyakazi wa shambani iliongezeka kutoka watu 156,299 hadi watu 2,179,256 duniani pote. Katika mwaka wa 1971-1975 mabadiliko zaidi ya kitengenezo yalihitajiwa. Haingewezekana tena kwa mtu mmoja aliyetumikia akiwa msimamizi atoe uangalizi kamili wa kazi ya Ufalme ulimwenguni pote. Baraza Linaloongoza, likiwa na mwenyekiti aliyetumika kwa zamu, lilipanuliwa kuwa na washiriki 18, ambao karibu nusu yao sasa wamemaliza mwendo wao duniani.
21. Ni nini kimewafanya washiriki wa kundi dogo wastahili Ufalme?
21 Washiriki wanaobaki wa kundi dogo wamefinyangwa kupitia miongo mingi ya majaribu. Wao ni wenye moyo mkuu, wakiwa wamepokea waziwazi ‘ushahidi wa roho.’ Yesu amewaambia: “Nyinyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami nafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu amefanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme, ili mpate kula na kunywa kwenye meza yangu katika ufalme wangu, na kuketi juu ya viti vya ufalme kuyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.”—Waroma 8:16, 17; Luka 12:32; 22:28-30.
22, 23. Kundi dogo na kondoo wengine wanafinyangwa namna gani?
22 Kwa kuwa idadi ya mabaki waliotiwa mafuta kwa roho imepungua, ndugu wakomavu wa umati mkubwa wamepewa usimamizi wa karibu makutaniko yote duniani pote. Na wakati Mashahidi watiwa-mafuta wa mwisho walio wazee wamalizapo mwendo wao wa kidunia, sa·rimʹ, yaani, wakuu wa kifalme wa kondoo wengine watakuwa wamezoezwa vizuri kutekeleza wajibu mbalimbali wa kiutawala wakiwa jamii ya mkuu duniani.—Ezekieli 44:3; Isaya 32:1.
23 Kundi dogo na vilevile kondoo wengine wanaendelea kufinyangwa kuwa vyombo kwa utumizi wenye kuheshimika. (Yohana 10:14-16) Tumaini letu liwe katika “mbingu mpya” au liwe katika “dunia mpya,” na tuitikie kwa moyo wote mwaliko wa Yehova: “Furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha.” (Isaya 65:17, 18) Acheni sisi viumbe dhaifu tutumikie sikuzote kwa unyenyekevu, tukifinyangwa na “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida”—nguvu ya Mungu ya roho takatifu!—2 Wakorintho 4:7; Yohana 16:13.
-