Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Maskini Wanazidi Kuwa Maskini
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Agosti 1
    • Maskini Wanazidi Kuwa Maskini

      “Hakuna jamii inayoweza kusitawi na kuwa na furaha iwapo idadi kubwa ya raia zake ni maskini na hawana furaha.”

      MANENO hayo yalisemwa na mtaalamu wa uchumi, Adam Smith katika karne ya 18. Wengi wanasadiki kwamba ukweli wa yale aliyosema unaonekana wazi zaidi leo. Tofauti kati ya matajiri na maskini inaonekana wazi zaidi. Huko Ufilipino, theluthi moja ya watu hujitegemeza kwa kiasi kinachopungua dola moja ya Marekani kwa siku, kiasi ambacho mara nyingi huchumwa kwa dakika chache katika mataifa tajiri. Kichapo cha Umoja wa Mataifa, Human Development Report 2002 kinasema kwamba “mapato ya asilimia 5 ya watu matajiri sana ulimwenguni ni mara 114 zaidi ya asilimia 5 ya wale walio maskini sana.”

      Ingawa watu fulani wanaishi maisha ya starehe, mamilioni huishi wakiwa maskwota, wakijenga nyumba za mabanda mahali popote. Hali ya wengine ni mbaya zaidi; wanaishi barabarani, wakiwa wamelalia na kujifunika tu makaratasi. Wengi wao hujitegemeza kwa njia yoyote ile—huchakura takataka, hubeba mizigo mizito, au hutumia mikokoteni kuokota takataka wanazoweza kuuza kama vile makaratasi, mikebe na chupa.

      Ukosefu wa usawa kati ya matajiri na maskini hauko tu katika nchi zinazositawi, bali kama vile Benki ya Dunia inavyosema ‘kuna maskini katika nchi zote.’ Hata kama wengine ni matajiri sana, iwe ni huko Bangladesh au Marekani, kuna wale ambao wanashindwa kujipatia chakula cha kutosha na makao. Likinukuu ripoti ya Shirika la Marekani la Sensa ya 2001, gazeti The New York Times lilionyesha kwamba pengo kati ya matajiri na maskini huko Marekani linazidi kupanuka. Lilisema hivi: “Asilimia 20 ya watu walio matajiri sana ilipokea nusu ya mapato ya familia zote mwaka jana . . . Asilimia 20 ya walio maskini sana ilipokea asilimia 3.5.” Hali iko hivyo au ni mbaya hata zaidi katika nchi nyingine nyingi. Ripoti moja ya Benki ya Dunia inaonyesha kwamba asilimia 57 ya watu ulimwenguni hujitegemeza kwa kiasi kinachopungua dola mbili kwa siku.

      Kufanya hali iwe mbaya hata zaidi, katika mwaka wa 2002, watu wengi walikerwa na ripoti kuhusu wasimamizi wa makampuni ambao walitajirika kwa njia zenye kutiliwa shaka. Hata kama utajiri huo ulipatikana kwa njia halali, wengi wamehisi kwamba wasimamizi hao wa makampuni “walikuwa matajiri kupita kiasi, bila kujali wengine,” kama lilivyosema gazeti Fortune. Kwa kufikiria yale yanayotukia ulimwenguni, wengine hujiuliza kama kweli ni haki kwa watu fulani kuwa na pesa nyingi mno, ambazo zinakadiriwa kuwa mamilioni ya dola, huku wengine wakiishi katika umaskini.

      Je, Umaskini Utakuwapo Milele?

      Hii haimaanishi kwamba hakuna mtu anayefikiria kuwasaidia maskini. Bila shaka, maofisa wa serikali wenye nia nzuri na mashirika ya kutoa misaada yametoa mapendekezo ya kuleta mabadiliko. Hata hivyo, hali bado inasikitisha. Kichapo Human Development Report 2002 kinasema kwamba “nchi nyingi ni maskini kuliko zilivyokuwa miaka 10, 20 na katika visa vingine, miaka 30 iliyopita,” licha ya jitihada nzuri za kuboresha mambo.

      Je, hii inamaanisha kwamba maskini hawana tumaini lolote? Tunakukaribisha usome makala inayofuata ili uone jinsi kuwa na hekima kunavyoweza kuwasaidia maskini sasa na pia suluhisho ambalo labda hujawahi kulifikiria.

  • Kupata Suluhisho Lenye Kudumu la Umaskini
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Agosti 1
    • Kupata Suluhisho Lenye Kudumu la Umaskini

      IJAPOKUWA kuna ripoti mbaya kutoka sehemu mbalimbali ulimwenguni kuhusu umaskini, kuna wale ambao wana matumaini kwamba jambo fulani linaweza kufanywa. Kwa mfano, kulingana na kichwa kimoja katika gazeti la Manila Bulletin, Benki ya Maendeleo ya Asia ilisema kwamba “Asia inaweza kumaliza umaskini katika muda wa miaka 25.” Benki hiyo ilipendekeza ukuzi wa uchumi kuwa njia moja ya kuwatoa watu kutoka katika dimbwi la umaskini.

      Mashirika mengine na serikali zimetoa mapendekezo na miradi mingi ya kujaribu kutatua tatizo hilo. Baadhi ya mapendekezo hayo ni: mipango ya bima ya jamii, elimu bora, kufuta madeni ambayo nchi zilizositawi zinazidai nchi zinazositawi, kuondoa vizuizi vilivyowekwa ili mataifa yenye idadi kubwa ya watu maskini yaweze kuuza bidhaa zao katika nchi za nje, na kujenga nyumba za gharama ya chini kwa ajili ya maskini.

      Katika mwaka wa 2000, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa liliweka miradi inayopaswa kutimizwa kufikia mwaka wa 2015. Miradi hiyo ilitia ndani kukomeshwa kwa umaskini mkubwa na njaa, na vilevile tofauti kubwa ya mapato katika mataifa. Hata miradi hiyo iwe mizuri kadiri gani, wengi wanatilia shaka kwamba itatimizwa katika ulimwengu huu usio na umoja.

      Hatua Hususa za Kukabiliana na Umaskini

      Kwa kuwa hakuna tumaini la kutatua tatizo hilo ulimwenguni pote, tutapata wapi suluhisho? Kama ilivyotajwa hapo awali, kuna chanzo cha hekima ambacho kinaweza kuwasaidia watu sasa. Ni chanzo kipi? Ni Neno la Mungu, Biblia.

      Ni nini hufanya Biblia iwe tofauti na vichapo vingine vyote? Inatoka kwa Muumba wetu, aliye na mamlaka ya juu zaidi. Katika Biblia, Muumba wetu ametupa hekima na kanuni zinazofaa ambazo zinaweza kutumiwa na watu wote kila mahali, wakati wowote. Kanuni hizo zikifuatwa, zinaweza kuwasaidia maskini waishi maisha yenye kuridhisha hata sasa. Hebu tuchunguze baadhi ya kanuni hizo.

      Uwe na maoni yanayofaa kuhusu pesa. Biblia inasema: “Hekima ni ulinzi, kama vile fedha ilivyo ulinzi; na ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliye nayo.” (Mhubiri 7:12) Andiko hilo linamaanisha nini? Pesa haziwezi kutimiza kila kitu. Ni kweli kwamba pesa zinaweza kutoa usalama wa kadiri fulani. Hizo hutuwezesha tu kununua vitu fulani tunavyohitaji. Kuna vitu vyenye thamani sana visivyoweza kununuliwa kwa pesa. Tunapotambua jambo hilo, tutakuwa na maoni yanayofaa kuhusu vitu vya kimwili na hivyo kuepuka mahangaiko yanayowapata wale ambao huhangaikia urundikaji wa pesa. Pesa haziwezi kununua uhai, lakini kutenda kwa hekima kunaweza kulinda uhai sasa na hata kunaweza kutupa nafasi ya kuishi milele.

      Ishi kulingana na mapato yako. Vitu tunavyotaka si lazima viwe vitu tunavyohitaji. Tunapaswa kutanguliza mahitaji yetu. Tunaweza kufikiri kwamba tunahitaji kitu fulani, lakini kwa kweli kitu hicho si cha lazima. Mtu mwenye hekima atatenga mapato yake kwa ajili ya mahitaji ya lazima kwanza, kama vile chakula, mavazi, makao, na kadhalika. Kisha, kabla ya kununua chochote cha ziada, ataamua ikiwa pesa zilizobaki zinatosha kununua vitu vingine vya ziada. Katika mmoja wa mifano yake, Yesu alipendekeza kwamba mtu ‘aketi kwanza na kupiga hesabu ya gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha.’—Luka 14:28.

      Huko Ufilipino, Eufrosina, ambaye ni mzazi mwenye watoto watatu na hana mwenzi, amepata ugumu wa kujitegemeza na kutumia mapato yake kwa uangalifu tangu mume wake alipomwacha miaka kadhaa iliyopita. Ili kuishi katika hali hizo, amewazoeza watoto wake kutambua vitu vinavyopaswa kununuliwa kwanza. Kwa mfano, huenda watoto wakaona kitu fulani ambacho wangependa. Badala tu ya kukataa, mama huyo hutoa hoja hii: “Mkipenda mnaweza kupata kitu hiki, lakini mwamue. Tuna pesa za kutosha kununua kitu kimoja tu. Tunaweza kununua kitu hiki mnachopenda, au tunaweza kununua nyama kidogo au mboga iwe kitoweo cha wali kwa juma hili. Sasa mngependa tununue nini? Amueni.” Kwa kawaida, watoto hao huona hoja hiyo haraka na kukubali kwamba wangependa chakula badala ya kitu kingine.

      Ridhika. Kanuni nyingine ya Biblia inasema: “Tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.” (1 Timotheo 6:8) Pesa peke yake haziwezi kutuletea furaha. Kuna watu wengi matajiri ambao hawana furaha, ilhali kuna watu wengi maskini ambao wana furaha sana. Watu hao maskini wamejifunza kuridhika na vitu vichache vinavyohitajiwa maishani. Yesu alisema kuhusu kuwa na ‘jicho sahili’ ambalo linakazia mambo muhimu zaidi. (Mathayo 6:22) Jicho sahili humsaidia mtu aridhike. Watu wengi maskini huridhika sana kwa sababu wamesitawisha uhusiano mzuri na Mungu, nao wana familia zenye furaha. Mambo hayo hayawezi kununuliwa kwa pesa.

      Hiyo ni mifano michache tu inayoonyesha jinsi madokezo ya Biblia yanavyoweza kuwasaidia walio maskini kukabiliana na hali yao. Kuna madokezo mengine mengi. Kwa mfano, epuka mazoea mabaya ambayo huharibu pesa kama vile kuvuta sigara na kucheza kamari; tambua mambo yaliyo muhimu maishani, hasa miradi ya kiroho; mahali ambapo ni vigumu kuajiriwa kazi, jaribu kutoa huduma ambayo wengine wanaihitaji. (Mithali 22:29; 23:21; Wafilipi 1:9-11) Biblia inapendekeza tutumie “hekima kamili na busara” kwa sababu sifa hizo ‘zitakuwa uzima kwa nafsi yetu.’—Mithali 3:21, 22.

      Ingawa madokezo ya Biblia yanaweza kuwasaidia kwa njia fulani wale wanaopambana na umaskini, bado kuna maswali kuhusu wakati ujao. Je, maskini watabaki maskini milele? Je, pengo kubwa sana kati ya walio matajiri sana na walio maskini sana litapata kuzibwa? Hebu tuchunguze suluhisho ambalo wengi hawalijui.

      Biblia Inatupa Sababu ya Kuwa na Tumaini

      Watu wengi wanakubali kwamba Biblia ni kitabu kizuri. Hata hivyo, mara nyingi hawajui kwamba inataja mambo fulani hususa yatakayoleta mabadiliko makubwa hivi karibuni.

      Mungu ananuia kuchukua hatua ya kutatua matatizo ya wanadamu, kutia ndani umaskini. Kwa kuwa serikali za wanadamu zimeshindwa ama zimekataa kutatua matatizo hayo, Mungu ananuia kuziondoa. Jinsi gani? Biblia inasema hivi kwa mkazo katika Danieli 2:44: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”

      Baada ya kuondoa “falme” au serikali hizi, Mtawala aliyechaguliwa na Mungu atachukua hatua. Mtawala huyo si mwanadamu, bali ni kiumbe wa mbinguni aliye na nguvu kama Mungu, mwenye uwezo wa kufanya mabadiliko makubwa yanayohitajiwa ili kuondoa tofauti zilizopo leo. Mungu amemchagua Mwana wake mwenyewe kufanya hivyo. (Matendo 17:31) Andiko la Zaburi 72:12-14 linaeleza yale ambayo Mtawala huyo atafanya, lisemapo: “Atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaada. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, na damu yao ina thamani machoni pake.” Hilo ni tumaini zuri kama nini! Mwishowe kitulizo kitapatikana! Mtawala aliyechaguliwa na Mungu atawatetea maskini na walio dhaifu.

      Matatizo mengi yanayosababishwa na umaskini yataondolewa wakati huo. Andiko la Zaburi 72, mstari wa 16 linasema: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.” Hakutakuwapo tena upungufu wa chakula, ukosefu wa pesa, au usimamizi mbaya.

      Matatizo mengine yatatatuliwa pia. Kwa mfano, leo watu wengi ulimwenguni hawana nyumba zao wenyewe. Hata hivyo, Mungu anaahidi hivi: “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.” (Isaya 65:21, 22) Kila mtu atakuwa na nyumba yake mwenyewe na ataifurahia kazi yake. Kwa hiyo, Mungu anaahidi suluhisho kamili lenye kudumu la umaskini. Hakutakuwa tena na mapengo makubwa kati ya matajiri na maskini, watu hawatajitegemeza tena kwa shida.

      Mtu anaposikia kwanza ahadi hizi za Biblia, huenda akafikiri kwamba ni ndoto tu. Hata hivyo, kuchunguza Biblia kwa makini kunaonyesha kwamba ahadi zote za Mungu za zamani zimetimia. (Isaya 55:11) Suala hapa si ikiwa zitatimia, bali ni jambo unalopaswa kufanya ili kunufaika na ahadi hizo zitakapotimia.

      Je, Utakuwapo?

      Kwa kuwa serikali hiyo ni ya Mungu, ni lazima tuwe watu ambao Mungu atawakubali kuwa raia wa utawala huo. Ametupa kanuni katika Biblia ambazo zinatuonyesha jinsi tunavyoweza kustahili kuwa raia za serikali hiyo.

      Mtawala aliyechaguliwa, Mwana wa Mungu, ni mwadilifu. (Isaya 11:3-5) Kwa hiyo, wale watakaokubaliwa kuwa raia wa serikali hiyo watatarajiwa kuwa waadilifu pia. Andiko la Mithali 2:21, 22 linasema: “Wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”

      Je, kuna njia ya kujifunza jinsi ya kutimiza matakwa hayo? Ndiyo. Kwa kujifunza Biblia na kufuata mwongozo wake, unaweza kuwa na tumaini hilo zuri la wakati ujao. (Yohana 17:3) Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kujifunza Biblia. Tunakukaribisha uchukue nafasi hii ya kuwa sehemu ya jamii ambayo haitakuwa na umaskini wala ukosefu wa haki.

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      Eufrosina: “Kutumia mapato kwa uangalifu husaidia familia yangu kupata mahitaji yake”

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Kuwa na uhusiano mzuri na Mungu na kuwa na familia yenye furaha ni mambo ambayo hayawezi kununuliwa kwa pesa

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki