-
Je, Unapaswa Kuwa Mnyoofu Nyakati Zote?Mnara wa Mlinzi—2010 | Machi 1
-
-
Je, Ni Sawa Kuiba kwa Sababu ya Umaskini?
Mtawala mmoja wa Roma alisema hivi: “Umaskini ndio chanzo cha uhalifu.” Mtu maskini anaweza kufikiri kwamba ana haki ya kuiba. Huenda watazamaji wakaona kwamba ni sawa kwa maskini kuiba. Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu jambo hilo? Aliwatendea maskini kwa huruma. ‘Aliwasikitikia.’ (Mathayo 9:36) Hata hivyo, hakuunga mkono kamwe wizi kwa sababu yoyote. Basi, mtu maskini anapaswa kufanya nini?
Mungu anawahurumia wale ambao wanajitahidi kwa unyoofu kumtii, naye atabariki jitihada zao za kutosheleza mahitaji yao. (Zaburi 37:25) Biblia inaahidi hivi: “Yehova hataiacha nafsi ya mwadilifu iteswe na njaa, lakini atasukumia mbali tamaa ya waovu.” (Methali 10:3) Je, mtu maskini anaweza kuamini ahadi hiyo? Victorine anaamini kwamba ni ahadi ya kweli.
Maisha ya Victorine ni magumu kwa sababu ni mjane aliye na watoto watano wanaoenda shuleni. Anaishi katika nchi inayositawi ambamo hawapati msaada wa kutosha kutoka kwa serikali. Kuna nafasi nyingi za kuiba kwa sababu wengi wanafanya kazi katika mitaa. Hata hivyo, Victorine hakubali kamwe kushawishiwa kuiba. Badala yake, anajitahidi kupata mahitaji yake kwa unyoofu kwa kuuza vitu kando ya barabara. Kwa nini anaendelea kuwa mnyoofu?
“Kwanza, ninaamini kwamba Mungu ni mnyoofu na atanitendea kwa unyoofu ikiwa nitamwiga. Pili, watoto wangu watajifunza kuwa wanyoofu ikiwa tu wataniona nikiwa mnyoofu.”
Matokeo yamekuwa nini? Anasema hivi: “Tuna chakula, mavazi, na makao. Hata hivyo, nyakati nyingine ninalazimika kuwaomba marafiki wanisaidie, kwa mfano, ninapohitaji pesa za kulipia matibabu ya ugonjwa wa ghafula. Sijawahi kamwe kukosa ninachohitaji. Kwa nini? Kwa sababu marafiki wangu wanajua kwamba siwadanganyi ninapowaeleza hali zangu na sijaribu kujipatia faida.
“Watoto wangu wanajifunza kuwa wanyoofu wanapoendelea kukua. Hivi karibuni, jirani mmoja aliona sarafu chache kwenye meza yetu akaniuliza kwa nini sikuogopa kwamba watoto wangu watazichukua. Hakuamini kamwe nilipomwambia kwamba watoto wangu hawawezi kufanya hivyo. Aliamua kuwajaribu bila mimi kujua. Kwa siri aliweka sarafu mbili zenye thamani ya faranga 100 katika nyumba yetu mahali ambapo watoto wangeweza kuziona kwa urahisi. Aliporudi siku iliyofuata, alishangaa sana kuona kwamba bado sarafu hizo zilikuwapo. Kuwa na watoto wanyoofu ni jambo bora zaidi kuliko kuwa na vitu vingi vya kimwili.”
-
-
Je, Unapaswa Kuwa Mnyoofu Nyakati Zote?Mnara wa Mlinzi—2010 | Machi 1
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 14]
Je, Andiko la Methali 6:30 Linaunga Mkono Kuiba?
Andiko la Methali 6:30 linasema hivi: “Watu hawamdharau mwizi kwa sababu tu anaiba ili kushibisha nafsi yake akiwa na njaa.” Je, maneno hayo yanaunga mkono kuiba? Hapana. Mistari mingine katika kitabu hicho inaonyesha kwamba Mungu anamwona mwizi kuwa na hatia kwa sababu ya kosa lake. Mstari unaofuata unasema hivi: “Lakini, akipatikana, atalipa mara saba ya kiasi hicho; atatoa vitu vyote vyenye thamani vya nyumba yake.” (Methali 6:31) Ingawa mtu anayeiba kwa sababu ya njaa huenda asionekane kuwa mbaya kama yule anayeiba kwa sababu ya pupa au ili kumuumiza mwingine, bado anapaswa ‘kulipa’ au kurudisha. Wale wanaotaka kumpendeza Mungu hawapaswi kuwa na hatia ya kuiba kwa sababu yoyote.
-