-
Msifuni Mfalme wa Umilele!Mnara wa Mlinzi—1996 | Aprili 1
-
-
Msifuni Mfalme wa Umilele!
“Yehova ndiye Mfalme kwa wakati usiodhahiri, hata milele.”—ZABURI 10:16, NW.
1. Ni maswali gani yazukayo kwa habari ya umilele?
UMILELE—wewe ungesema huo ni nini? Je, wafikiri kwa kweli wakati waweza kuendelea milele? Naam, hakuna shaka lolote kwamba wakati hutanuka milele katika wakati uliopita. Kwa hiyo kwa nini usitanuke milele katika wakati ujao? Kwa kweli, Biblia ya New World Translation humrejezea Mungu kuwa mwenye kusifiwa “kutoka wakati usiodhahiri hadi wakati usiodhahiri.” (Zaburi 41:13, NW) Usemi huo unamaanisha nini? Huenda tukasaidiwa kuuelewa kwa kurejezea habari inayohusiana nao—anga.
2, 3. (a) Ni maswali gani yenye kuhusu anga, yatusaidiayo kufahamu umilele? (b) Kwa nini tutake kumwabudu Mfalme wa umilele?
2 Anga huenea kotekote kadiri gani? Je, ina mpaka wowote? Kufikia miaka 400 iliyopita, dunia yetu ilifikiriwa kuwa kitovu cha ulimwengu wote mzima. Kisha Galileo akaunda darubini, ikiwezesha sehemu kubwa zaidi ya mbingu kuonekana. Sasa Galileo angeweza kuona nyota nyingi zaidi naye akaweza kuonyesha kwamba dunia na sayari nyinginezo huzunguka jua. Njia ya Maziwa haikuonekana tena kuwa ya maziwa-maziwa. Ilithibitika kuwa galaksi yenye nyota, zikiwa karibu bilioni mia moja. Hatuwezi kamwe kuhesabu wingi huo wa nyota halisi, hata katika muda wote wa maisha. Baadaye, waastronomia wakaanza kuvumbua mabilioni ya galaksi. Hayo huenea angani bila mpaka, kupita umbali ambao darubini zenye nguvu zaidi zaweza kuona. Yaonekana kana kwamba anga haina mipaka. Ndivyo ilivyo na umilele—huo hauna mipaka!
3 Yaonekana kwamba wazo la umilele hupita uelewevu wa bongo zetu za kibinadamu zilizo dhaifu. Hata hivyo, kuna Mtu Fulani anayelielewa kikamili. Yeye aweza kuhesabu, ndiyo, na hata kuita kwa majina, yale mabilioni na mabilioni mengi ya nyota katika mabilioni ya galaksi! Huyo asema hivi: “Inueni macho yenu juu sana na kuona. Ni nani ameumba vitu hivi? Ni Yeye anayetokeza jeshi lavyo hata kwa hesabu, navyo vyote huviita hata kwa jina. Kwa sababu ya wingi wa nishati zenye msukumo, yeye akiwa pia mwenye kutenda kwa uwezo, hakuna kimoja chavyo kinachokosekana. Je, wewe hujapata kujua au hujapata kusikia? Yehova, Muumba wa ncha za mbali zaidi za dunia, ndiye Mungu kwa wakati usiodhahiri. Yeye hachoki wala hazimii. Uelewevu wake hauchunguziki.” (Isaya 40:26, 28, NW) Ni Mungu wa ajabu kama nini! Kwa hakika, yeye ndiye Mungu ambaye twapaswa kutaka kumwabudu!
“Mfalme kwa Wakati Usiodhahiri”
4. (a) Daudi alionyeshaje uthamini kwa Mfalme wa umilele? (b) Mmojawapo wanasayansi wakubwa zaidi katika historia alikata kauli gani juu ya chanzo cha ulimwengu wote mzima?
4 Kwenye Zaburi 10:16 (NW) Daudi asema hivi juu ya Mungu huyu aliye Muumba: “Yehova ndiye Mfalme kwa wakati usiodhahiri, hata milele.” Na kwenye Zaburi 29:10 (NW) yeye arudia hivi: “Yehova huketi akiwa mfalme kwa wakati usiodhahiri.” Ndiyo, Yehova ndiye Mfalme wa umilele! Zaidi ya hayo, Daudi ashuhudia kwamba Mfalme huyu aliyetukuka ndiye Mbuni na Mfanyi wa vyote tunavyoona angani, akisema hivi kwenye Zaburi 19:1: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.” Miaka ipatayo 2,700 baadaye, yule mwanasayansi mashuhuri Sir Isaac Newton alikubaliana na Daudi, akiandika hivi: “Mfumo huu mzuri sana wa jua, sayari na nyota zenye mikia ungeweza kutokana tu na kusudi na enzi kuu ya mtu mwenye akili na mwenye uweza.”
5. Isaya na Paulo waliandika nini kuhusu Chanzo cha hekima?
5 Twapaswa kunyenyekea kama nini kwa kujua kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ambaye hata ‘mbingu zenye nafasi kubwa sana hazimtoshi, wala mbingu za mbingu,’ huishi kwa umilele! (1 Wafalme 8:27) Yehova, afafanuliwaye kwenye Isaya 45:18 kuwa “aliyeziumba mbingu, . . . aliyeiumba dunia na kuifanya,” ndiye Chanzo cha hekima ipitayo kwa mbali sana uwezo wa ufahamu wa bongo za binadamu wanaokufa. Yehova alisema, kama vile ikaziwavyo kwenye 1 Wakorintho 1:19 (NW): “Hakika nitafanya hekima ya watu wenye hekima iangamie, na akili ya watu wenye akili hakika nitaisukuma kando.” Mtume Paulo aliongezea hivi katika mstari wa 20 (NW): “Yuko wapi mtu mwenye hekima? Wapi mwandishi? Wapi mshindania-maneno wa mfumo huu wa mambo? Je, Mungu hakuifanya hekima ya ulimwengu iwe pumbavu?” Ndiyo, kama vile Paulo alivyoendelea kusema kwenye sura ya 3, mstari wa 19 (NW) “hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu kwa Mungu.”
6. Mhubiri 3:11 (NW) laonyesha nini kuhusu “wakati usiodhahiri”?
6 Magimba ya kimbingu ni sehemu ya uumbaji ambao Mfalme Sulemani alirejezea: “Kila kitu [Mungu] amekifanya kizuri kwa wakati wacho. Hata wakati usiodhahiri yeye ameuweka moyoni mwao, ili wanadamu wasipate kamwe kutambua kazi ambayo Mungu wa kweli ameifanya tangu mwanzo hadi mwisho.” (Mhubiri 3:11, NW) Kwa kweli, kujaribu kutambua maana ya “wakati usiodhahiri,” yaani, umilele, kumetiwa moyoni mwa mwanadamu. Lakini je, kweli aweza kupata ujuzi huo?
Tazamio Zuri Ajabu la Uhai
7, 8. (a) Ni tazamio gani zuri ajabu la uhai lililo mbele ya wanadamu, nalo laweza kupatikanaje? (b) Kwa nini tushangilie kwamba elimu ya kimungu itaendelea kwa umilele wote?
7 Yesu Kristo alisema hivi katika sala yake kwa Yehova: “Hii yamaaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3, NW) Twaweza kupataje ujuzi huo? Twahitaji kujifunza Neno la Mungu, Biblia Takatifu. Hivyo twaweza kupata ujuzi sahihi juu ya makusudi matukufu ya Mungu, kutia ndani uandalizi uliofanywa kupitia Mwana wake kwa ajili ya uhai udumuo milele katika dunia iliyo paradiso. Huo utakuwa “uhai ulio kwelikweli” urejezewao kwenye 1 Timotheo 6:19 (NW). Huo utapatana na kile kifafanuliwacho na Waefeso 3:11 kuwa “kusudi la milele alilolikusudia [Mungu] katika Kristo Yesu Bwana wetu.”
8 Ndiyo, sisi wanadamu wenye dhambi twaweza kupata uhai udumuo milele kupitia elimu ya kimungu na imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. Elimu hiyo itaendelea muda mrefu kadiri gani? Itaendelea kwa umilele wote kadiri wanadamu waendeleavyo kuagizwa hatua kwa hatua katika hekima ya Muumba wetu. Hekima ya Yehova haina mipaka. Akitambua hilo, mtume Paulo alipaaza sauti hivi: “Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu! Hukumu zake hazichunguziki, wala njia zake hazitafutikani!” (Warumi 11:33) Kwa kweli, yafaa kwamba 1 Timotheo 1:17 (NW) humwita Yehova “Mfalme wa umilele”!
Hekima ya Uumbaji wa Yehova
9, 10. (a) Ni kazi gani zenye utukufu Yehova alitimiza katika kutayarisha dunia iwe zawadi kwa wanadamu? (b) Hekima ya hali ya juu ya Yehova inaonyeshwaje katika uumbaji wake? (Ona sanduku.)
9 Fikiria ule urithi wa ajabu ambao Mfalme wa umilele ametuandalia sisi wanadamu. Zaburi 115:16 hutuambia hivi: ‘Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wanadamu.’ Je, hufikiri hiyo ni amana nzuri ajabu? Bila shaka! Nasi twathamini kama nini ule mwono wa kimbele wenye kutokeza wa Muumba wetu katika kuitayarisha dunia kuwa makao yetu ya wakati ujao!—Zaburi 107:8.
10 Mambo ya ajabu yalitendeka duniani wakati wa zile “siku” sita za uumbaji za Mwanzo sura ya 1, kila siku ikichukua muda wa maelfu ya miaka. Uumbaji huo mbalimbali wa Mungu hatimaye ungefunika dunia nzima kwa zulia la nyasi mbichi, misitu yenye fahari, na maua maridadi. Nayo ingejaa viumbe vingi mno vya baharini vya ajabu-ajabu, vikundi vya ndege wazuri wenye mabawa, na unamna-namna mwingi sana wa wanyama wa kufugwa na wasiofugwa, kila mmoja akizaa “kulingana na aina yake.” Baada ya ufafanuzi wa uumbaji wa mwanamume na mwanamke, Mwanzo 1:31 husimulia hivi: “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.” Ni mazingira yenye kupendeza kama nini yaliyozingira wanadamu hao wa kwanza! Je, hatuoni katika uumbaji huo wote, ile hekima, ule mwono wa kimbele, na utunzaji wa Muumba mwenye upendo?—Isaya 45:11, 12, 18.
11. Sulemani alitukuzaje hekima ya uumbaji ya Yehova?
11 Mmoja aliyestaajabia hekima ya Mfalme wa umilele ni Sulemani. Kwa kurudia-rudia alielekeza fikira kwa hekima ya Muumba. (Mithali 1:1, 2; 2:1, 6; 3:13-18) Sulemani atuhakikishia kwamba “dunia imesimama hata kwa wakati usiodhahiri.” Yeye alithamini maajabu mengi ya uumbaji, kutia ndani fungu la mawingu ya mvua katika kuiburudisha dunia yetu. Hivyo, aliandika hivi: “Mito yote huingia baharini, walakini bahari haijai; huko iendako mito, ndiko irudiko tena.” (Mhubiri 1:4, 7, linganisha NW.) Ndivyo inavyokuwa kwamba baada ya mvua na mito kuiburudisha dunia, maji yayo hurudi tena kutoka baharini hadi katika mawingu. Dunia hii ingekuwaje, nasi tungekuwa wapi, bila usafishaji huu na mzunguko wa maji?
12, 13. Twaweza kuonyeshaje uthamini kwa uumbaji wa Mungu?
12 Uthamini wetu kwa ajili ya usawaziko katika uumbaji wapaswa kuungwa mkono na matendo, kama vile Mfalme Sulemani alivyoonyesha katika maneno ya kumalizia ya Mhubiri: “Umalizio wa mambo, yote yakiwa yamekwisha kusikiwa, ni: Mhofu Mungu wa kweli na uzishike amri zake. Kwa maana huu ndio wajibu wote wa mwanadamu. Kwa maana Mungu wa kweli mwenyewe atahukumu kila aina ya kazi kuhusiana na kila jambo lililofichwa, kama ni njema au mbaya.” (Mhubiri 12:13, 14, NW) Twapaswa kuhofu kufanya jambo lolote lisilompendeza Mungu. Badala ya hivyo, twapaswa kujaribu kumtii tukiwa na kicho chenye staha.
13 Hakika, twapaswa tutake kumsifu Mfalme wa umilele kwa sababu ya kazi zake zenye utukufu za uumbaji! Zaburi 104:24 (NW) hutangaza hivi: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima. Dunia imejaa mazao yako.” Kwa shangwe, acheni tukubaliane na mstari wa mwisho wa zaburi hii kwa kujiambia wenyewe na wengine hivi: “Mbariki Yehova, Ee nafsi yangu. Msifuni Yah, enyi watu!”—NW.
Upeo wa Uumbaji wa Kidunia
14. Ni kwa njia zipi uumbaji wa kibinadamu wa Mungu washinda kwa mbali ule wa wanyama?
14 Uumbaji wote wa Yehova ni wenye ustadi. Lakini uumbaji wa kidunia wenye kutokeza zaidi ni sisi—wanadamu. Adamu halafu Hawa waliumbwa wakiwa upeo wa siku ya uumbaji ya sita ya Yehova—uumbaji ulio bora zaidi kuliko samaki, ndege, na wanyama! Ingawa wengi wa viumbe hawa ni wenye hekima kisilika, wanadamu wamepewa nguvu za kusababu, dhamiri iwezayo kupambanua kati ya mema na mabaya, uwezo wa kupangia wakati ujao, na tamaa iliyotiwa ndani ya kuabudu. Hayo yote yalitokeaje? Badala ya kuwa tokeo la mageuzi kutoka kwa hayawani wasio na akili, mwanadamu aliumbwa katika mfano wa Mungu. Kwa hiyo, ni mwanadamu pekee awezaye kuonyesha sifa za Muumba wetu, aliyejitambulisha kuwa “Yehova, Yehova, Mungu mwenye rehema na mwema, asiye mwepesi wa hasira na mwenye wingi wa fadhili-upendo na kweli.”—Kutoka 34:6, NW.
15. Kwa nini tumshangilie Yehova kwa unyenyekevu?
15 Acheni tumsifu na kumshukuru Yehova kwa sababu ya ubuni wa ajabu wa miili yetu. Mkondo wetu wa damu ulio muhimu kwa uhai huuzunguka mwili kwa kila sekunde 60. Kama vile Kumbukumbu la Torati 12:23 (NW) hutaarifu, “damu ndiyo nafsi”—uhai wetu—yenye bei sana machoni pa Mungu. Mifupa yenye nguvu, misuli yenye kunyumbuka, na mfumo wa neva wenye kuitikia vinakamilishwa na ubongo ulio mkuu zaidi kuliko ubongo wowote ule wa mnyama na ambao una uwezo mkubwa usioweza kufikiwa na kompyuta yenye ukubwa wa jengo refu sana. Je, hilo halikufanyi uhisi unyenyekevu? Lapaswa lifanye hivyo. (Mithali 22:4) Na ebu fikiria hili pia: Mapafu yetu, zoloto, ulimi, meno, na kinywa vyaweza kushirikiana ili kutoa usemi wa kibinadamu katika yoyote ya maelfu ya lugha. Daudi alimwimbia Yehova wimbo ufaao, akisema: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.” (Zaburi 139:14) Acheni tujiunge na Daudi katika kumsifu Yehova kwa shukrani, aliye Mbuni na Mungu wetu wa ajabu!
16. Ni wimbo gani mwana-muziki mashuhuri aliimba kwa kumsifu Yehova, na tuitikie mwaliko gani wenye kushurutisha?
16 Maneno ya wimbo wa kidini wa karne ya 18 uliotungwa na Joseph Haydn yasema hivi katika kumsifu Yehova: “Mpeni shukrani, enyi kazi Zake zote zilizo ajabu sana! Imbeni heshima Yake, imbeni utukufu Wake, barikini na kulitukuza Jina Lake! Sifa ya Yehova hudumu milele, Ameni, Ameni!” Na yenye uzuri hata zaidi ni yale maneno yaliyorudiwa sana katika Zaburi, kama ule mwaliko unaotolewa mara nne katika Zaburi ya 107 Zb 107:8, 15, 21, 31(NW): “Ee acheni watu wampe shukrani Yehova kwa sababu ya fadhili-upendo zake na kwa kazi zake za ajabu kwa wana wa wanadamu.” Je, wewe hujiunga katika sifa hiyo? Unapaswa, kwa kuwa kila kitu ambacho kwa kweli ni kizuri kina chanzo cha Yehova, Mfalme wa umilele.
Kazi Zenye Uweza Hata Zaidi
17. ‘Wimbo wa Musa na wa Mwana-Kondoo’ wamtukuzaje Yehova?
17 Katika miaka elfu sita iliyopita, Mfalme wa umilele ameanzisha kazi zenye uweza hata zaidi. Katika kitabu cha mwisho cha Biblia, kwenye Ufunuo 15:3, 4 (NW) twasoma juu ya wale walio mbinguni ambao wamepata ushindi dhidi ya maadui walio roho waovu: “Wanaimba wimbo wa Musa mtumwa wa Mungu na wimbo wa Mwana-Kondoo, wakisema: ‘Ni kubwa na za ajabu sana kazi zako, Yehova Mungu, Mweza-Yote. Ni za uadilifu na za kweli njia zako, Mfalme wa umilele. Ni nani ambaye kwa kweli hatakuhofu wewe, Yehova, na kulitukuza jina lako, kwa sababu wewe peke yako ni mwaminifu-mshikamanifu? Kwa maana mataifa yote yatakuja na kuabudu mbele yako, kwa sababu maagizo yako ya uadilifu yamefanywa kuwa dhahiri.’” Kwa nini huo waitwa ‘wimbo wa Musa na wa Mwana-Kondoo’? Acheni tuone.
18. Ni kazi gani yenye uweza inayokumbukwa katika wimbo ulio katika Kutoka sura 15?
18 Miaka ipatayo 3,500 iliyopita, wakati jeshi la Farao lenye uweza lilipoangamia katika Bahari Nyekundu, Waisraeli walimsifu Yehova kwa shukrani katika wimbo. Twasoma hivi kwenye Kutoka 15:1, 18 (NW): “Wakati huo Musa na wana wa Israeli walianza kuimba wimbo huu kwa Yehova na kusema yafuatayo: ‘Acha nimwimbie Yehova wimbo, kwa maana ametukuka sana. Farasi na mpanda-farasi wake yeye ametumbukiza baharini. Yehova atatawala akiwa mfalme kwa wakati usiodhahiri, hata milele.’” Amri za uadilifu za huyu Mfalme wa umilele zilidhihirika katika kuhukumu na kuangamiza kwake maadui waliokaidi enzi kuu yake.
19, 20. (a) Kwa nini Yehova alifanyiza taifa la Israeli? (b) Mwana-kondoo na wengine wamejibuje ushindani wa Shetani?
19 Kwa nini hilo lilikuja kuhitajiwa? Ni katika bustani ya Edeni yule nyoka mwenye hila aliwaongoza wazazi wetu wa kwanza watende dhambi. Tokeo la hilo likawa kupitishwa kwa hali ya kutokamilika yenye dhambi kwa wanadamu wote. Hata hivyo, kwa kupatana na kusudi lake la kwanza, Mfalme wa umilele alichukua hatua mara iyo hiyo, ambazo zingeongoza kwenye kuondolea mbali maadui wake wote kutoka kwenye makao ya dunia na kurudisha hali za kiparadiso. Mfalme wa umilele alifanyiza taifa la Israeli na kuandaa Sheria yake ili kuonyesha kimbele jinsi ambavyo angetimiza hilo.—Wagalatia 3:24.
20 Lakini, baada ya wakati fulani, Israeli lenyewe lilididimia katika hali ya kutokuwa jaminifu, na hali hiyo yenye kuhuzunisha ilifikia upeo wakati watawala walo walipokabidhi Waroma Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu ili ateswe vibaya sana na kuuawa. (Matendo 10:39; Wafilipi 2:8) Hata hivyo, uaminifu-maadili wa Yesu hadi kifo, akiwa “Mwana-Kondoo wa Mungu” aliyedhabihiwa, ulijibu kwa njia yenye kutokeza lile suala lililotolewa na Mpinzani wa kale wa Mungu, Shetani—kwamba hakuna mtu duniani ambaye angeendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu akiwa chini ya jaribu kali sana. (Yohana 1:29, 36; Ayubu 1:9-12; 27:5) Ingawa wamerithi kutokamilika kwa Adamu, mamilioni ya wanadamu wengine wamhofuo Mungu wamefuata hatua za Yesu kwa kushika uaminifu-maadili wakabiliwapo na mashambulio ya kishetani.—1 Petro 1:18, 19; 2:19, 21.
21. Kwa kupatana na Matendo 17:29-31, ni nini litakalofuata kuzungumzwa?
21 Sasa siku imewasili kwa Yehova kuthawabisha waaminifu hao na kuhukumu maadui wote wa kweli na uadilifu. (Matendo 17:29-31) Hilo litatendekaje? Makala yetu ifuatayo itaeleza.
-
-
Msifuni Mfalme wa Umilele!Mnara wa Mlinzi—1996 | Aprili 1
-
-
Hekima ya Hali ya Juu ya Yehova
Hekima ya Mfalme wa umilele inaonyeshwa kwa njia nyingi sana katika uumbaji wake mbalimbali duniani! Ona maneno ya Aguri: “Kila usemi wa Mungu umesafishwa. Yeye ni ngao kwa wale wapatao kimbilio katika yeye.” (Mithali 30:5, NW) Kisha Aguri arejezea viumbe vingi kati ya viumbe vyenye uhai vya Mungu, vikubwa kwa vidogo. Kwa kielelezo, katika mstari wa 24 hadi wa 28 (NW) yeye afafanua “vitu vinne vilivyo vidogo kuliko vyote vya dunia, lakini ni vyenye hekima kisilika.” Hivyo ni chungu, wibari, nzige, na mjusi.
“Vyenye hekima kisilika”—ndiyo, wanyama wameumbwa kwa njia hiyo. Wao hawasababu mambo kama wanadamu bali hutegemea hekima iliyotiwa ndani. Je, umepata wakati wowote kustaajabia hilo? Wao ni viumbe wenye utaratibu kama nini! Mathalani, chungu hujipanga katika jumuiya mbalimbali, zinazotia ndani malkia, chungu-vibarua, na chungu wa kiume. Katika jamii nyingine za chungu, chungu-vibarua hata hufuga wadudu afidi katika mashamba yenye kuta ambazo wamejenga. Humo wao huwakamua afidi hao, huku chungu-askari-jeshi wakiwafukuza maadui wowote wanaoshambulia. Onyo lenye upole linatolewa kwenye Mithali 6:6: “Ewe mvivu, mwendee chungu, zitafakari njia zake ukapate hekima.” Je, vielelezo hivyo havipaswi kutuchochea sisi wanadamu tuwe na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana”?—1 Wakorintho 15:58, NW.
Mwanadamu amejenga eropleni kubwa-kubwa. Lakini ndege (nyuni) ni hodari zaidi kama nini, kutia ndani yule ndege-mvumaji, mwenye uzani upunguao gramu 30! Eropleni aina ya Boeing 747 lazima ichukue lita 180,000 za mafuta, iendeshwe na watu waliozoezwa na itumie mifumo tata ya kusafiria hewani ili kuruka ng’ambo nyingine ya Bahari Kuu ya Pasifiki. Lakini, ndege-mvumaji mdogo hutegemea gramu moja tu ya shahamu kumwezesha aruke umbali ule wote kutoka Amerika Kaskazini, kuvuka Ghuba ya Mexico, hadi Amerika Kusini. Yeye hahitaji mzigo mzito wa mafuta, wala mazoezi ya kusafiria hewani, wala chati zenye mambo magumu wala kompyuta! Je, uwezo huo ulitokana na aksidenti fulani ya mageuzi? La, hasha! Ndege huyu mdogo ni mwenye hekima kisilika, akiwa ameratibiwa hivyo na Muumba wake, Yehova Mungu.
-
-
“Msifuni Yah, Enyi Watu!”Mnara wa Mlinzi—1996 | Aprili 1
-
-
“Msifuni Yah, Enyi Watu!”
“Kila kitu kipumuacho—na kimsifu Yah.”—ZABURI 150:6, NW.
1, 2. (a) Ni kwa kadiri gani Ukristo wa kweli ulisitawi katika karne ya kwanza? (b) Mitume walitoa onyo gani la kimbele? (c) Uasi-imani ulisitawije?
YESU aliwapanga kitengenezo wanafunzi wake kuwa kutaniko la Kikristo, lililositawi katika karne ya kwanza. Ujapokuwa upinzani mkali, ‘habari njema ilihubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.’ (Wakolosai 1:23, NW) Lakini baada ya kifo cha mitume wa Yesu Kristo, Shetani alichochea kwa hila ukuzi wa uasi-imani.
2 Mitume walikuwa wametoa onyo la kimbele juu ya uasi-imani huo. Kwa kielelezo, Paulo aliwaeleza wazee kutoka Efeso: “Kazieni uangalifu kwenu wenyewe na kwa kundi lote, ambalo miongoni mwalo roho takatifu imewaweka nyinyi rasmi kuwa waangalizi, kulichunga kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe. Mimi najua kwamba baada ya kwenda zangu mbwa-mwitu wenye kuonea wataingia miongoni mwenu na hawatalitendea kundi kwa wororo, na kutoka miongoni mwenu nyinyi wenyewe watu watainuka na kusema mambo yaliyopotoka ili kuvuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Matendo 20:28-30, NW; ona pia 2 Petro 2:1-3; 1 Yohana 2:18, 19.) Hivyo, katika karne ya nne, Ukristo wenye kuasi imani ulianza kujiunga na Milki ya Roma. Karne kadhaa baadaye, Milki Takatifu ya Roma, kwa ushirikiano na papa wa Roma, ilikuja kutawala sehemu kubwa ya wanadamu. Baada ya wakati fulani, Warekebishaji wa Kidini wa Kiprotestanti waliasi dhidi ya mambo maovu yenye kupita kiasi ya Kanisa Katoliki, lakini wakashindwa kurudisha Ukristo wa kweli.
3. (a) Ni lini na jinsi gani habari njema ilihubiriwa kwa viumbe vyote? (b) Ni matazamio gani yenye kutegemea Biblia yaliyotimizwa katika 1914?
3 Hata hivyo, mwisho wa karne ya 19 ulipokuwa ukikaribia, kikundi chenye moyo mweupe cha wanafunzi wa Biblia kilikuwa chenye shughuli tena kikihubiri na kueneza kwa ‘viumbe vyote chini ya mbingu tumaini la habari njema.’ Kwa msingi wa funzo la unabii wa Biblia, kikundi hiki kilielekeza mbele kwenye miaka zaidi ya 30 hadi 1914 kuwa mwaka wenye kutia alama mwisho wa “nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa,” kipindi cha “nyakati saba,” au miaka 2,520, kilichoanza na kufanywa ukiwa kwa Yerusalemu katika 607 K.W.K. (Luka 21:24, NW; Danieli 4:16) Kwa utimizo wa matazamio yao, 1914 ulithibitika kuwa mwaka wenye kuleta badiliko la maana katika mambo ya wanadamu duniani. Mbinguni pia, mambo ya maana kihistoria yalitendeka. Ndio wakati Mfalme wa umilele alipomweka Mfalme-Mshirika wake, Yesu Kristo, juu ya kiti cha utawala cha kimbingu, kwa utayarishaji wa kufagilia mbali uovu wote kutoka kwenye uso wa dunia hii na kuanzisha Paradiso tena.—Zaburi 2:6, 8, 9; 110:1, 2, 5.
Tazama Mfalme wa Kimesiya!
4. Yesu alijipatanishaje na maana ya jina lake Mikaeli?
4 Katika 1914 Mfalme huyu wa Kimesiya, Yesu, alianza kuchukua hatua. Katika Biblia yeye huitwa pia Mikaeli, kumaanisha “Ni Nani Aliye Kama Mungu?,” kwa maana amenuia kutetea enzi kuu ya Yehova. Kama ilivyorekodiwa kwenye Ufunuo 12:7-12, mtume Yohana alifafanua katika ono kile ambacho kingetendeka: “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake; nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni. Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.” Ni anguko kubwa kwelikweli!
5, 6. (a) Baada ya 1914, ni mbiu gani yenye kusisimua iliyotangazwa kutoka mbinguni? (b) Mathayo 24:3-13 yaambatanaje na hiyo?
5 Ndipo sauti kuu sana mbinguni ikapiga mbiu hivi: “Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa maana ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu, mchana na usiku. Nao [Wakristo waaminifu] wakamshinda kwa damu ya Mwana-Kondoo [Kristo Yesu], na kwa neno la ushuhuda wao; ambao hawakupenda maisha yao hata kufa.” Hilo lamaanisha ukombozi kwa washika uaminifu-maadili, ambao wamedhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu yenye thamani.—Mithali 10:2; 2 Petro 2:9.
6 Hiyo sauti kuu mbinguni ikaendelea kutangaza hivi: “Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” Huo “ole” uliotabiriwa hivyo kwa dunia hii umekuwa dhahiri katika vita vya ulimwengu, njaa kali, magonjwa ya kuambukiza, matetemeko ya dunia, na uasi-sheria ambao umeikumba dunia katika karne hii. Kama vile Mathayo 24:3-13 (NW) husimulia, Yesu alitabiri kwamba hayo yangekuwa sehemu ya ‘ishara ya umalizio wa mfumo wa mambo.’ Kwa utimizo wa unabii huo, tangu 1914 wanadamu wamepatwa na ole duniani usio na kifani katika historia yote ya kibinadamu iliyotangulia.
7. Kwa nini Mashahidi wa Yehova huhubiri kwa uharaka?
7 Katika enzi hii ya ole wa kishetani, je, wanadamu waweza kupata tumaini kwa wakati ujao? Ndiyo, kwa kuwa Mathayo 12:21 husema hivi juu ya Yesu: “Na jina lake Mataifa watalitumainia”! Hali zenye kufadhaisha zilizo miongoni mwa mataifa hazionyeshi tu ‘ishara ya umalizio wa mfumo wa mambo’ bali pia zaonyesha ‘ishara ya kuwako kwa Yesu’ akiwa Mfalme wa Ufalme wa Kimesiya. Kuhusu Ufalme huo, Yesu asema zaidi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Ni kikundi kipi kimoja cha watu duniani leo kinachohubiri tumaini tukufu la utawala wa Ufalme wa Mungu? Mashahidi wa Yehova! Kwa uharaka, wao hupiga mbiu nyumba kwa nyumba kwamba Ufalme wa Mungu wenye uadilifu na amani uko karibu kutwaa usimamizi wa mambo ya dunia. Je, wewe unashiriki katika huduma hiyo? Huwezi kupata pendeleo kubwa kuliko hili!—2 Timotheo 4:2, 5.
“Mwisho” Unakujaje?
8, 9. (a) Hukumu ilianzaje “katika nyumba ya Mungu”? (b) Jumuiya ya Wakristo imekiukaje Neno la Mungu?
8 Wanadamu wameingia katika kipindi cha hukumu. Tunajulishwa kwenye 1 Petro 4:17 kwamba hukumu ilianza “katika nyumba ya Mungu”—hukumu juu ya matengenezo yanayodai eti kuwa ya Kikristo ambayo imeonekana wazi tangu “siku za mwisho” zilipoanza kwa machinjo ya Vita ya Ulimwengu 1 katika kipindi cha 1914-1918. Jumuiya ya Wakristo imehukumiwaje katika hukumu hiyo? Naam, fikiria msimamo wa makanisa katika kutegemeza vita tangu 1914. Je, makasisi hawajatiwa “alama za damu za nafsi maskini zisizo na hatia” ambazo walizihimiza ziende vitani?—Yeremia 2:34, NW.
9 Kulingana na Mathayo 26:52, Yesu alisema: “Wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.” Hilo limekuwa kweli kama nini katika vita vya karne hii! Makasisi wamehimiza vijana wachinje vijana wengine, hata wale wa dini yao—Mkatoliki akimuua Mkatoliki na Mprotestanti akimuua Mprotestanti. Utukuzo wa taifa umekuzwa juu ya Mungu na Kristo. Majuzi, katika baadhi ya mataifa ya Afrika, mahusiano ya kikabila yametangulizwa mbele ya kanuni za Biblia. Katika Rwanda, ambako idadi kubwa ya watu ni Wakatoliki, angalau watu nusu milioni walichinjwa ovyo-ovyo katika ujeuri wa kikabila. Papa alikiri hivi katika gazeti la habari la Vatikani L’Osservatore Romano: “Haya ni maangamizi ya moja kwa moja ya kabila zima, ambayo inasikitisha kwamba hata Wakatoliki wameshiriki.”—Linganisha Isaya 59:2, 3; Mika 4:3, 5.
10. Ni hukumu gani ambayo Yehova atatekeleza juu ya dini bandia?
10 Mfalme wa umilele huzionaje dini zinazotia watu moyo wachinjane au zinazosimama kando tu huku washiriki wa kundi lazo wakiua washiriki wengine? Kuhusu Babiloni Mkubwa, mfumo wa ulimwenguni pote wa dini bandia, Ufunuo 18:21, 24 (NW) hutuambia hivi: “Malaika mwenye nguvu akainua jiwe kama jiwe kubwa la kusagia na kulivurumisha ndani ya bahari, akisema: ‘Hivyo kwa mtupo wa kasi sana atavurumishwa chini Babiloni lile jiji kubwa, na hatapatikana tena kamwe. Ndiyo, katika yeye ilipatikana damu ya manabii na ya watakatifu na ya wote wale ambao wamechinjwa juu ya dunia.’”
11. Ni mambo gani yenye kuchukiza ambayo yamekuwa yakitendeka katika Jumuiya ya Wakristo?
11 Kwa utimizo wa unabii wa Biblia, mambo yenye kuchukiza yamekuwa yakitendeka katika Jumuiya ya Wakristo. (Linganisha Yeremia 5:30, 31; 23:14.) Kwa sababu hasa ya mtazamo wenye uendekevu wa makasisi, makundi yao yamejawa ukosefu wa adili. Katika Marekani, linaloonwa kuwa taifa la Kikristo, karibu nusu ya ndoa zote huishia kwenye talaka. Mimba za matineja na ugoni-jinsia-moja umepita kiasi miongoni mwa washiriki wa kanisa. Mapadri wanawatenda vibaya kingono watoto wachanga—na si katika visa vichache tu. Imesemwa kwamba malipo ya mahakamani yanayohusiana na kesi hizo yanaweza kugharimu Kanisa Katoliki katika Marekani dola bilioni moja katika mwongo mmoja. Jumuiya ya Wakristo imepuuza onyo la mtume Paulo kwenye 1 Wakorintho 6:9, 10 (NW): “Ama! Je, hamjui kwamba watu wasio waadilifu hawatarithi ufalme wa Mungu? Msiongozwe vibaya. Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume watunzwao kwa makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume walalao pamoja na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawatarithi ufalme wa Mungu.”
12. (a) Mfalme wa umilele atachukuaje hatua dhidi ya Babiloni Mkubwa? (b) Tofauti na Jumuiya ya Wakristo, ni kwa sababu gani watu wa Mungu wataimba korasi za “Haleluya”?
12 Hivi karibuni, Mfalme wa umilele, Yehova, akitenda kupitia Amiri Mkuu wa kimbingu, Kristo Yesu, ataanzisha dhiki kubwa. Kwanza, Jumuiya ya Wakristo na sehemu nyinginezo za Babiloni Mkubwa zitapatwa na utekelezaji wa hukumu ya Yehova. (Ufunuo 17:16, 17) Wamejionyesha kutostahili wokovu ambao Yehova ameandaa kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu. Wamedharau jina takatifu la Mungu. (Linganisha Ezekieli 39:7.) Ni dhihaka iliyoje kwamba wanaimba korasi za “Haleluya” katika majengo yao ya kidini yenye kuvutia! Wanaondoa jina la Yehova lenye thamani kutoka tafsiri zao za Biblia lakini inaonekana hawajui kamwe jambo la kwamba “Haleluya” humaanisha “Msifuni Yah”—“Yah” ikiwa ni ufupisho wa “Yehova.” Kwa kufaa, Ufunuo 19:1-6 hurekodi korasi za “Haleluya” zitakazoimbwa karibuni katika sherehe ya utekelezaji wa hukumu ya Mungu juu ya Babiloni Mkubwa.
13, 14. (a) Ni matukio gani makubwa yatakayofuata kutukia? (b) Ni yapi matokeo yenye furaha ya wanadamu wenye kumhofu Mungu?
13 Jambo linalofuata kutukia ni ‘kuwasili’ kwa Yesu ili kutangaza na kutekeleza hukumu juu ya mataifa na watu. Yeye mwenyewe alitoa unabii hivi: “Wakati Mwana wa binadamu [Kristo Yesu] awasilipo katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake [cha hukumu] cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote [duniani] yatakusanywa mbele yake, naye atatenganisha watu, kama vile mchungaji atenganishavyo kondoo na mbuzi. Naye atawaweka kondoo kwenye mkono wake wa kuume, lakini mbuzi kwenye mkono wake wa kushoto. Ndipo mfalme atakapowaambia wale walio kwenye mkono wake wa kuume, ‘Njoni, nyinyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, rithini ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu ulimwengu kuwekwa msingi.’” (Mathayo 25:31-34, NW) Mt 25 Mstari wa 46 (NW) waendelea kusimulia kwamba jamii ya mbuzi “wataondoka kuingia katika kukatiliwa-mbali kudumuko milele, lakini waadilifu kuingia katika uhai udumuo milele.”
14 Kitabu cha Biblia cha Ufunuo chaendelea kufafanua jinsi ‘Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,’ Bwana wetu wa kimbingu, Yesu Kristo, atakavyoendesha farasi kuingia katika pigano kwenye Har–Magedoni, akiharibu sehemu ya kisiasa na ya kibiashara ya mfumo wa Shetani. Hivyo Kristo atakuwa ameimwaga “ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi” juu ya makao yote ya kidunia ya Shetani. Mambo haya ‘ya kwanza yapitapo,’ wanadamu wenye kumhofu Mungu wataingizwa katika ulimwengu mpya wenye utukufu ambamo Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao.”—Ufunuo 19:11-16; 21:3-5.
Wakati wa Kumsifu Yah
15, 16. (a) Kwa nini ni muhimu kwamba tutii neno la Yehova la kiunabii? (b) Manabii na mitume waonyesha ni lazima tufanye nini ili tupate wokovu, na hilo laweza kumaanisha nini kwa wengi leo?
15 Siku hiyo ya kutekeleza hukumu iko karibu! Kwa hiyo yafaa tutii neno la kiunabii la Mfalme wa umilele. Kwa wale ambao wangali wamenaswa na mafundisho na desturi za dini bandia, sauti ya kimbingu yatangaza hivi: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.” Lakini ni lazima wenye kuponyoka waende wapi? Kwaweza kuwa na kweli moja tu, kwa hiyo kwaweza kuwa na dini ya kweli moja tu. (Ufunuo 18:4; Yohana 8:31, 32; 14:6; 17:3) Kupata uhai wa milele hutegemea kupata dini hiyo na kutii Mungu wayo. Biblia hutuelekeza kwake kwenye Zaburi 83:18, ambalo lasema hivi: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.”
16 Hata hivyo, twahitaji kufanya zaidi kuliko kujua tu jina la Mfalme wa umilele. Twahitaji kujifunza Biblia na kupata kujua juu ya sifa na makusudi yake matukufu. Kisha twahitaji kufanya mapenzi yake kwa wakati huu, kama inavyoonyeshwa katika Warumi 10:9-13 (NW). Mtume Paulo alinukuu manabii waliopuliziwa na kumalizia kwa kusema: “Kila mtu aitaye jina la Yehova ataokolewa.” (Yoeli 2:32; Sefania 3:9) Kuokolewa? Ndiyo, kwa kuwa wengi leo wanaodhihirisha imani katika uandalizi wa Yehova wa fidia kupitia Kristo watakombolewa kutoka katika dhiki kubwa inayokuja, wakati hukumu itakapotekelezwa juu ya ulimwengu wa Shetani wenye ufisadi.—Ufunuo 7:9, 10, 14.
17. Ni tumaini gani tukufu lipaswalo kutuchochea tujiunge sasa katika kuimba wimbo wa Musa na wa Mwana-Kondoo?
17 Mapenzi ya Mungu ni nini kwa wale wanaotazamia kuokoka? Ni kwamba tujiunge hata sasa katika kuimba wimbo wa Musa na wa Mwana-Kondoo, tukimsifu Mfalme wa umilele katika kutazamia kwa hamu ushindi wake. Twafanya hivyo kwa kuambia wengine juu ya makusudi yake matukufu. Tufanyapo maendeleo katika uelewevu wa Biblia, twaweka maisha zetu wakfu kwa Mfalme wa umilele. Hilo litafanya tuishi kwa umilele wote chini ya mpango ambao Mfalme huyu mwenye uweza afafanua, kama upatikanavyo kwenye Isaya 65:17, 18 (NW): “Kwa maana hapa mimi naumba mbingu mpya [Ufalme wa Kimesiya wa Yesu] na dunia mpya [jamii mpya yenye uadilifu ya wanadamu]; na vitu vya kwanza havitakumbukwa akilini, wala havitakumbukwa moyoni. Lakini chachaweni, enyi watu, na mwe wenye shangwe milele katika kile ninachoumba.”
18, 19. (a) Maneno ya Daudi katika Zaburi 145 yapasa yatuchochee kufanya nini? (b) Twaweza kutarajia nini kwa uhakika kwenye mkono wa Yehova?
18 Mtunga-zaburi Daudi alimfafanua Mfalme wa umilele kwa maneno haya: “Yehova ndiye mkuu na mwenye kusifiwa sana, na ukuu wake hauchunguziki.” (Zaburi 145:3, NW) Ndiyo, ukuu wake hauchunguziki kama vile mipaka ya anga na ya umilele! (Warumi 11:33) Huku tukiendelea kutwaa ujuzi juu ya Muumba wetu na juu ya uandalizi wake wa fidia kupitia Mwana wake, Kristo Yesu, sisi tutazidi kutaka kumsifu Mfalme wetu wa milele. Tutataka kufanya kama vile Zaburi 145:11-13 huonyesha: “Wataunena utukufu wa ufalme wako, na kuuhadithia uweza wako. Ili kuwajulisha watu matendo yake makuu, na utukufu wa fahari ya ufalme wake. Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote, na mamlaka yako ni ya vizazi vyote.”
19 Twaweza kutazamia kwa uhakika kwamba Mungu wetu atatimiza hili tangazo: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.” Mfalme wa umilele atatuongoza kwa wororo hadi ukomo wa siku hizi za mwisho, kwa kuwa Daudi alituhakikishia hivi: “BWANA huwahifadhi wote wampendao, na wote wasio haki atawaangamiza.”—Zaburi 145:16, 20.
20. Twaitikiaje mwaliko wa Mfalme wa umilele, kama ulivyotolewa katika zaburi tano za mwisho?
20 Kila moja ya zile zaburi tano za kumalizia katika Biblia hufungua na kufunga kwa mwaliko wa “Haleluya.” Hivyo, Zaburi 146 (NW) hutualika hivi: “Msifuni Yah, enyi watu! Msifu Yehova, Ee nafsi yangu. Nitamsifu Yehova muda wa maisha yangu. Nitamwimbia Mungu wangu maadamu nipo.” Je, wewe utaitikia wito huo? Kwa hakika wapaswa kutaka kumsifu! Na uwe miongoni mwa wale wanaofafanuliwa kwenye Zaburi 148:12, 13 (NW): “Wanaume vijana na pia enyi mabikira, enyi wanaume wazee pamoja na wavulana. Acheni walisifu jina la Yehova, kwa maana jina lake pekee ni juu lisiweze kufikika. Adhama yake ni juu ya dunia na mbingu.” Na tuitikie kwa moyo wote mwaliko: “Msifuni Yah, enyi watu!” Acheni tumsifu kwa umoja Mfalme wa umilele!
-