-
Msifuni Mfalme wa Umilele!Mnara wa Mlinzi—1996 | Aprili 1
-
-
Hekima ya Hali ya Juu ya Yehova
Hekima ya Mfalme wa umilele inaonyeshwa kwa njia nyingi sana katika uumbaji wake mbalimbali duniani! Ona maneno ya Aguri: “Kila usemi wa Mungu umesafishwa. Yeye ni ngao kwa wale wapatao kimbilio katika yeye.” (Mithali 30:5, NW) Kisha Aguri arejezea viumbe vingi kati ya viumbe vyenye uhai vya Mungu, vikubwa kwa vidogo. Kwa kielelezo, katika mstari wa 24 hadi wa 28 (NW) yeye afafanua “vitu vinne vilivyo vidogo kuliko vyote vya dunia, lakini ni vyenye hekima kisilika.” Hivyo ni chungu, wibari, nzige, na mjusi.
“Vyenye hekima kisilika”—ndiyo, wanyama wameumbwa kwa njia hiyo. Wao hawasababu mambo kama wanadamu bali hutegemea hekima iliyotiwa ndani. Je, umepata wakati wowote kustaajabia hilo? Wao ni viumbe wenye utaratibu kama nini! Mathalani, chungu hujipanga katika jumuiya mbalimbali, zinazotia ndani malkia, chungu-vibarua, na chungu wa kiume. Katika jamii nyingine za chungu, chungu-vibarua hata hufuga wadudu afidi katika mashamba yenye kuta ambazo wamejenga. Humo wao huwakamua afidi hao, huku chungu-askari-jeshi wakiwafukuza maadui wowote wanaoshambulia. Onyo lenye upole linatolewa kwenye Mithali 6:6: “Ewe mvivu, mwendee chungu, zitafakari njia zake ukapate hekima.” Je, vielelezo hivyo havipaswi kutuchochea sisi wanadamu tuwe na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana”?—1 Wakorintho 15:58, NW.
Mwanadamu amejenga eropleni kubwa-kubwa. Lakini ndege (nyuni) ni hodari zaidi kama nini, kutia ndani yule ndege-mvumaji, mwenye uzani upunguao gramu 30! Eropleni aina ya Boeing 747 lazima ichukue lita 180,000 za mafuta, iendeshwe na watu waliozoezwa na itumie mifumo tata ya kusafiria hewani ili kuruka ng’ambo nyingine ya Bahari Kuu ya Pasifiki. Lakini, ndege-mvumaji mdogo hutegemea gramu moja tu ya shahamu kumwezesha aruke umbali ule wote kutoka Amerika Kaskazini, kuvuka Ghuba ya Mexico, hadi Amerika Kusini. Yeye hahitaji mzigo mzito wa mafuta, wala mazoezi ya kusafiria hewani, wala chati zenye mambo magumu wala kompyuta! Je, uwezo huo ulitokana na aksidenti fulani ya mageuzi? La, hasha! Ndege huyu mdogo ni mwenye hekima kisilika, akiwa ameratibiwa hivyo na Muumba wake, Yehova Mungu.
-
-
Msifuni Mfalme wa Umilele!Mnara wa Mlinzi—1996 | Aprili 1
-
-
Hekima ya Uumbaji wa Yehova
9, 10. (a) Ni kazi gani zenye utukufu Yehova alitimiza katika kutayarisha dunia iwe zawadi kwa wanadamu? (b) Hekima ya hali ya juu ya Yehova inaonyeshwaje katika uumbaji wake? (Ona sanduku.)
9 Fikiria ule urithi wa ajabu ambao Mfalme wa umilele ametuandalia sisi wanadamu. Zaburi 115:16 hutuambia hivi: ‘Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wanadamu.’ Je, hufikiri hiyo ni amana nzuri ajabu? Bila shaka! Nasi twathamini kama nini ule mwono wa kimbele wenye kutokeza wa Muumba wetu katika kuitayarisha dunia kuwa makao yetu ya wakati ujao!—Zaburi 107:8.
10 Mambo ya ajabu yalitendeka duniani wakati wa zile “siku” sita za uumbaji za Mwanzo sura ya 1, kila siku ikichukua muda wa maelfu ya miaka. Uumbaji huo mbalimbali wa Mungu hatimaye ungefunika dunia nzima kwa zulia la nyasi mbichi, misitu yenye fahari, na maua maridadi. Nayo ingejaa viumbe vingi mno vya baharini vya ajabu-ajabu, vikundi vya ndege wazuri wenye mabawa, na unamna-namna mwingi sana wa wanyama wa kufugwa na wasiofugwa, kila mmoja akizaa “kulingana na aina yake.” Baada ya ufafanuzi wa uumbaji wa mwanamume na mwanamke, Mwanzo 1:31 husimulia hivi: “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.” Ni mazingira yenye kupendeza kama nini yaliyozingira wanadamu hao wa kwanza! Je, hatuoni katika uumbaji huo wote, ile hekima, ule mwono wa kimbele, na utunzaji wa Muumba mwenye upendo?—Isaya 45:11, 12, 18.
11. Sulemani alitukuzaje hekima ya uumbaji ya Yehova?
11 Mmoja aliyestaajabia hekima ya Mfalme wa umilele ni Sulemani. Kwa kurudia-rudia alielekeza fikira kwa hekima ya Muumba. (Mithali 1:1, 2; 2:1, 6; 3:13-18) Sulemani atuhakikishia kwamba “dunia imesimama hata kwa wakati usiodhahiri.” Yeye alithamini maajabu mengi ya uumbaji, kutia ndani fungu la mawingu ya mvua katika kuiburudisha dunia yetu. Hivyo, aliandika hivi: “Mito yote huingia baharini, walakini bahari haijai; huko iendako mito, ndiko irudiko tena.” (Mhubiri 1:4, 7, linganisha NW.) Ndivyo inavyokuwa kwamba baada ya mvua na mito kuiburudisha dunia, maji yayo hurudi tena kutoka baharini hadi katika mawingu. Dunia hii ingekuwaje, nasi tungekuwa wapi, bila usafishaji huu na mzunguko wa maji?
12, 13. Twaweza kuonyeshaje uthamini kwa uumbaji wa Mungu?
12 Uthamini wetu kwa ajili ya usawaziko katika uumbaji wapaswa kuungwa mkono na matendo, kama vile Mfalme Sulemani alivyoonyesha katika maneno ya kumalizia ya Mhubiri: “Umalizio wa mambo, yote yakiwa yamekwisha kusikiwa, ni: Mhofu Mungu wa kweli na uzishike amri zake. Kwa maana huu ndio wajibu wote wa mwanadamu. Kwa maana Mungu wa kweli mwenyewe atahukumu kila aina ya kazi kuhusiana na kila jambo lililofichwa, kama ni njema au mbaya.” (Mhubiri 12:13, 14, NW) Twapaswa kuhofu kufanya jambo lolote lisilompendeza Mungu. Badala ya hivyo, twapaswa kujaribu kumtii tukiwa na kicho chenye staha.
13 Hakika, twapaswa tutake kumsifu Mfalme wa umilele kwa sababu ya kazi zake zenye utukufu za uumbaji! Zaburi 104:24 (NW) hutangaza hivi: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima. Dunia imejaa mazao yako.” Kwa shangwe, acheni tukubaliane na mstari wa mwisho wa zaburi hii kwa kujiambia wenyewe na wengine hivi: “Mbariki Yehova, Ee nafsi yangu. Msifuni Yah, enyi watu!”—NW.
Upeo wa Uumbaji wa Kidunia
14. Ni kwa njia zipi uumbaji wa kibinadamu wa Mungu washinda kwa mbali ule wa wanyama?
14 Uumbaji wote wa Yehova ni wenye ustadi. Lakini uumbaji wa kidunia wenye kutokeza zaidi ni sisi—wanadamu. Adamu halafu Hawa waliumbwa wakiwa upeo wa siku ya uumbaji ya sita ya Yehova—uumbaji ulio bora zaidi kuliko samaki, ndege, na wanyama! Ingawa wengi wa viumbe hawa ni wenye hekima kisilika, wanadamu wamepewa nguvu za kusababu, dhamiri iwezayo kupambanua kati ya mema na mabaya, uwezo wa kupangia wakati ujao, na tamaa iliyotiwa ndani ya kuabudu. Hayo yote yalitokeaje? Badala ya kuwa tokeo la mageuzi kutoka kwa hayawani wasio na akili, mwanadamu aliumbwa katika mfano wa Mungu. Kwa hiyo, ni mwanadamu pekee awezaye kuonyesha sifa za Muumba wetu, aliyejitambulisha kuwa “Yehova, Yehova, Mungu mwenye rehema na mwema, asiye mwepesi wa hasira na mwenye wingi wa fadhili-upendo na kweli.”—Kutoka 34:6, NW.
15. Kwa nini tumshangilie Yehova kwa unyenyekevu?
15 Acheni tumsifu na kumshukuru Yehova kwa sababu ya ubuni wa ajabu wa miili yetu. Mkondo wetu wa damu ulio muhimu kwa uhai huuzunguka mwili kwa kila sekunde 60. Kama vile Kumbukumbu la Torati 12:23 (NW) hutaarifu, “damu ndiyo nafsi”—uhai wetu—yenye bei sana machoni pa Mungu. Mifupa yenye nguvu, misuli yenye kunyumbuka, na mfumo wa neva wenye kuitikia vinakamilishwa na ubongo ulio mkuu zaidi kuliko ubongo wowote ule wa mnyama na ambao una uwezo mkubwa usioweza kufikiwa na kompyuta yenye ukubwa wa jengo refu sana. Je, hilo halikufanyi uhisi unyenyekevu? Lapaswa lifanye hivyo. (Mithali 22:4) Na ebu fikiria hili pia: Mapafu yetu, zoloto, ulimi, meno, na kinywa vyaweza kushirikiana ili kutoa usemi wa kibinadamu katika yoyote ya maelfu ya lugha. Daudi alimwimbia Yehova wimbo ufaao, akisema: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.” (Zaburi 139:14) Acheni tujiunge na Daudi katika kumsifu Yehova kwa shukrani, aliye Mbuni na Mungu wetu wa ajabu!
16. Ni wimbo gani mwana-muziki mashuhuri aliimba kwa kumsifu Yehova, na tuitikie mwaliko gani wenye kushurutisha?
16 Maneno ya wimbo wa kidini wa karne ya 18 uliotungwa na Joseph Haydn yasema hivi katika kumsifu Yehova: “Mpeni shukrani, enyi kazi Zake zote zilizo ajabu sana! Imbeni heshima Yake, imbeni utukufu Wake, barikini na kulitukuza Jina Lake! Sifa ya Yehova hudumu milele, Ameni, Ameni!” Na yenye uzuri hata zaidi ni yale maneno yaliyorudiwa sana katika Zaburi, kama ule mwaliko unaotolewa mara nne katika Zaburi ya 107 Zb 107:8, 15, 21, 31(NW): “Ee acheni watu wampe shukrani Yehova kwa sababu ya fadhili-upendo zake na kwa kazi zake za ajabu kwa wana wa wanadamu.” Je, wewe hujiunga katika sifa hiyo? Unapaswa, kwa kuwa kila kitu ambacho kwa kweli ni kizuri kina chanzo cha Yehova, Mfalme wa umilele.
-