Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Alimmwagia Mungu Mahangaiko Yake Kupitia Sala
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Julai 1
    • Walipokuwa wakilikaribia, huenda Hana alitafakari yale ambayo angemwambia Yehova katika sala. Mara tu walipofika familia hiyo ilikula pamoja. Hana alipopata nafasi, mara moja aliondoka na kwenda kwenye maskani ya Yehova. Kuhani Mkuu Eli alikuwa ameketi karibu na mwimo wa mlango wa hekalu. Lakini Hana alikazia fikira Mungu wake. Alikuwa na uhakika kwamba angesikiwa akiwa katika maskani. Hata kama hakuna mwanadamu ambaye angeweza kuelewa hali yake yenye kufadhaisha, Baba yake aliye mbinguni angemwelewa. Uchungu ulimjaa moyoni hivi kwamba akaanza kulia.

      Huku mwili wake ukitetemeka kwa sababu ya kulia, Hana alimweleza Yehova shida zake kimoyomoyo. Midomo yake ilitetemeka akitafuta maneno ya kueleza uchungu wake. Alisali kwa muda mrefu, akimmwagia Baba yake yaliyokuwa moyoni mwake. Hata hivyo, alifanya mengi zaidi ya kumwomba Mungu atimize tamaa yake ya kupata mtoto. Hana hakutamani tu kupata baraka za Mungu bali pia alitaka kumpa Mungu chochote ambacho angeweza. Kwa hiyo, aliweka nadhiri akisema kwamba ikiwa angepata mtoto wa kiume angemtoa ili amtumikie Yehova.—1 Samweli 1:9-11.

      Hivyo, Hana anawawekea watumishi wote wa Yehova mfano mzuri kuhusu sala. Yehova anawaalika watumishi wake wawasiliane naye kwa uhuru, bila kusitasita, wakimmiminia mahangaiko yao kama vile tu ambavyo mtoto anayemwamini baba yake mwenye upendo hufanya. (Zaburi 62:8; 1 Wathesalonike 5:17) Mtume Petro aliongozwa na roho kuandika maneno haya yenye kufariji kuhusu kusali kwa Yehova: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’—1 Petro 5:7.

      Hata hivyo, tofauti na Yehova, wanadamu hawaelewi wala hawana huruma. Hana alipokuwa akilia na kusali alishtuka kusikia sauti ya mtu fulani. Ilikuwa sauti ya Eli, kuhani mkuu, ambaye alikuwa amemtazama. Eli alimwambia hivi: “Utaendelea kujiendesha kama mlevi mpaka wakati gani? Iondolee mbali divai yako.” Eli aliona midomo ya Hana ikitetemeka, huku akilia, na akiwa na huzuni nyingi. Badala ya kumwuliza tatizo lake, Eli alikata kauli haraka kwamba Hana alikuwa mlevi.—1 Samweli 1:12-14.

      Kushutumiwa bila msingi wowote, hasa na mwanamume aliye na cheo chenye kuheshimika kulimwumiza Hana sana, hasa wakati huu alipokuwa amefadhaika sana. Hata hivyo, aliweka tena mfano mzuri wa imani. Hakuruhusu kutokamilika kwa mwanadamu kumzuie kumwabudu Yehova. Alimjibu Eli kwa heshima na akamweleza hali yake. Eli alipotambua kuwa amekosea, alimjibu hivi kwa upole: “Nenda kwa amani, naye Mungu wa Israeli akupe ombi lako ambalo umemwomba.”—1 Samweli 1:15-17.

      Hana alipommiminia Yehova moyo wake na kumwabudu katika maskani, kulikuwa na matokeo gani? Simulizi hilo linasema: “Mwanamke huyo akaenda zake, akala chakula, na uso wake haukuonyesha tena kuhangaika.” (1 Samweli 1:18) Biblia Habari Njema inasema: “Hakuwa na huzuni tena.” Hana alihisi ametulia. Ni kana kwamba alikuwa amechukua mzigo wake wa hisia zilizokuwa zikimfadhaisha na kumtupia Yehova, Baba yake wa mbinguni mwenye nguvu. (Zaburi 55:22) Je, Yehova anaweza kushindwa na tatizo lolote? La—hakuna lolote lililomshinda jana, linaloweza kumshinda leo, wala kesho!

      Tunapohisi tumelemewa na hisia au kuhuzunika kupita kiasi, tunaweza kumwiga Hana na kuzungumza waziwazi na Yule ambaye Biblia inamwita “msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Tukisali kwa imani, huenda tukaacha kuhuzunika na badala yake tukawa na “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”—Wafilipi 4:6, 7.

  • Alimmwagia Mungu Mahangaiko Yake Kupitia Sala
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Julai 1
    • Kisha Hana akatoa sala ambayo Mungu aliona inastahili kutiwa katika Neno lake lililoongozwa na roho. Unaposoma maneno yake yaliyoandikwa katika 1 Samweli 2:1-10, utaona kwamba kila mstari unaonyesha kwamba alikuwa na imani yenye nguvu. Alimsifu Yehova kwa kutumia nguvu zake kwa njia ya ajabu—kwa uwezo wake usio na kifani wa kuwashusha wenye majivuno, kuwabariki walioonewa, na wa kuua au kuhifadhi uhai. Alimsifu Baba yake kwa utakatifu wake wa pekee, haki yake, na uaminifu wake. Hana angeweza kusema hivi akiwa na sababu nzuri: “Hakuna mwamba ulio kama Mungu wetu.” Yehova anategemeka kabisa, habadiliki, na ni kimbilio kwa ajili ya wote walioonewa na kukandamizwa na ambao wanamwomba msaada.

  • Alimmwagia Mungu Mahangaiko Yake Kupitia Sala
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Julai 1
    • [Sanduku katika ukurasa wa 17]

      Sala Mbili za Pekee

      Sala mbili za Hana zilizoandikwa katika 1 Samweli 1:11 na 2:1-10, zina mambo mengi yenye kupendeza. Fikiria mifano ifuatayo:

      ◼ Hana alielekeza sala yake ya kwanza kwa “Yehova wa majeshi.” Yeye ndiye mtu wa kwanza katika Biblia anayenukuliwa kuwa alitumia jina hilo la cheo. Jina hilo linapatikana mara 285 katika Biblia na linarejelea uwezo ambao Mungu anao juu ya jeshi kubwa la wana wa roho.

      ◼ Ona kwamba Hana alitoa sala ya pili, si wakati mwana wake alipozaliwa, bali wakati yeye na Elkana walipomtoa kwa ajili ya utumishi wa Mungu huko Shilo. Kwa hiyo, shangwe ya Hana haikutokana na kumnyamazisha mke mwenzake, Penina, lakini ilitokana na baraka za Yehova.

      ◼ Hana aliposema, “Pembe yangu kweli imeinuliwa katika Yehova,” huenda akilini alikuwa akimfikiria ng’ombe-dume, mnyama ambaye hutumia pembe zake kwa nguvu. Ni kana kwamba Hana alikuwa akisema: ‘Yehova, wewe ndiye unayenitia nguvu.’—1 Samweli 2:1.

      ◼ Maneno ya Hana kuhusu “mtiwa-mafuta” wa Mungu ni ya kinabii. Neno hilo ni sawa na “masihi,” naye Hana ndiye mtu wa kwanza katika Biblia kurejelea mfalme mtiwa-mafuta wa wakati ujao.—1 Samweli 2:10.

      ◼ Miaka 1,000 hivi baadaye, Maria, mama ya Yesu, alitumia maneno fulani ya Hana alipokuwa akimsifu Yehova.—Luka 1:46-55.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki