-
Yesu Anatufundisha KusaliJifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
-
-
Sura Ya 12
Yesu Anatufundisha Kusali
JE, WEWE huzungumza na Yehova Mungu?— Yehova anataka uzungumze naye. Unazungumza na Mungu unapotoa sala. Mara nyingi Yesu alizungumza na Baba yake wa mbinguni. Wakati mwingine alitaka awe peke yake ili azungumze na Mungu. Biblia inasema kwamba wakati mmoja ‘alipanda kwenda mlimani akiwa peke yake ili kusali. Ingawa ilikuwa jioni, alikuwa huko peke yake.’—Mathayo 14:23.
Unaweza kwenda wapi ukiwa peke yako ili usali kwa Yehova?— Unaweza kuzungumza na Yehova ukiwa peke yako usiku kabla ya kulala. Yesu alisema: “Wewe unaposali, ingia ndani ya chumba chako cha faragha na, baada ya kufunga mlango wako, sali kwa Baba yako.” (Mathayo 6:6) Je, wewe husali kila usiku kabla ya kwenda kulala?— Unapaswa kufanya hivyo.
Yesu alisali akiwa na watu wengine pia. Rafiki ya Yesu, Lazaro, alipokufa, Yesu alisali akiwa na watu wengine mahali ambapo Lazaro alizikwa. (Yohana 11:41, 42) Yesu alisali pia alipokuwa na mikutano na wanafunzi wake. Je, wewe huenda mikutanoni ambapo sala hutolewa?— Kwa kawaida mtu mzima ndiye husali huko. Sikiliza kwa makini anachosema kwa sababu anazungumza na Mungu kwa niaba yako. Kisha utaweza kusema “Amina” baada ya sala. Kusema “Amina” baada ya sala kunamaanisha nini?— Kunamaanisha unapenda sala hiyo, unakubaliana nayo, na unataka iwe sala yako pia.
Yesu alisali pia wakati wa chakula. Alimwambia Yehova asante kwa chakula. Je, wewe husali kwa ukawaida kabla ya kula? Ni vizuri kumwambia Yehova asante kwa chakula kabla ya kuanza kula. Mnapokula pamoja na wengine mtu mwingine anaweza kusali. Lakini namna gani unapokula peke yako? Au namna gani ikiwa unakula pamoja na watu ambao hawamwambii Yehova asante?— Basi unahitaji kutoa sala yako mwenyewe.
-
-
Yesu Anatufundisha KusaliJifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
-
-
Sasa fikiria. Je, unapaswa kuinamisha kichwa unaposali? Au kupiga magoti? Unaonaje?— Wakati mwingine Yesu aliposali alipiga magoti. Wakati mwingine alisimama. Na wakati mwingine alitazama mbinguni aliposali, kama alivyofanya aliposali kwa ajili ya Lazaro.
Kwa hiyo, hii inamaanisha nini?— Inamaanisha kwamba jambo la maana si kusali ukiwa umekaa kwa njia fulani hususa. Wakati mwingine ni vizuri kuinamisha kichwa na kufunga macho. Wakati mwingine hata unaweza kupiga magoti, kama Yesu alivyofanya. Lakini kumbuka kwamba tunaweza kusali kwa Mungu wakati wowote mchana au usiku, naye atatusikiliza. Jambo la maana kuhusu sala ni kuamini kabisa kwamba Yehova anasikiliza. Je, unaamini kwamba Yehova anasikiliza sala zako?
Tunapaswa kusema nini tunaposali kwa Yehova?— Hebu niambie: Unaposali, unamwambia Mungu nini?— Yehova ametupatia vitu vingi vizuri na inafaa kumwambia asante, sivyo?— Tunaweza kumwambia asante kwa chakula. Lakini umewahi kumwambia asante kwa kutupatia anga la buluu, miti ya kijani, na maua mazuri?— Aliviumba vyote hivyo pia.
Wakati fulani, wanafunzi wa Yesu walimwambia awafunze jinsi ya kusali. Mwalimu Mkuu aliwafundisha na kuwaonyesha mambo muhimu ya kusema katika sala. Unajua mambo hayo?— Hebu chukua Biblia yako na ufungue Mathayo sura ya 6. Katika mstari wa 9 hadi 13, tunapata ile inayoitwa na watu wengi, Sala ya Bwana. Hebu tuisome pamoja.
Hapa tunajifunza kwamba Yesu alisema tusali kuhusu jina la Mungu. Alisema tusali kwamba jina la Mungu litakaswe, au lionwe kuwa takatifu. Jina la Mungu ni nani?— Ndiyo, ni Yehova na sisi tunapaswa kulipenda jina hilo.
Pili, Yesu alitufundisha tusali kwamba Ufalme wa Mungu uje. Ufalme huo ni wa maana kwa sababu utaleta amani duniani na kuifanya dunia iwe paradiso.
Tatu, Mwalimu Mkuu alisema tusali mapenzi ya Mungu yatendeke duniani kama vile mbinguni. Iwapo tunasali Ufalme uje, basi tunapaswa kufanya mapenzi ya Mungu.
Baadaye, Yesu alitufundisha tusali kwa ajili ya chakula cha kila siku. Pia alisema tunapaswa kumwomba Mungu msamaha tunapokosea. Lakini kabla ya kumwomba msamaha, ni lazima tuwasamehe wengine iwapo wametukosea. Je, ni rahisi kwako kufanya hivyo?—
Kwa kumalizia, Yesu alisema tunapaswa kumwomba Yehova Mungu atulinde kutokana na yule mwovu, Shetani Ibilisi. Hayo yote ni mambo mazuri ya kutaja tunaposali kwa Mungu.
-