Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nguvu ya Sala
    Mnara wa Mlinzi—2000 | Machi 1
    • Nguvu ya Sala

      Jua linatua jijini Nahori huko Mashariki ya Kati. Msiria mmoja aitwaye Eliezeri afika na msafara wa ngamia kumi kwenye kisima fulani nje ya jiji hilo. Japo yaelekea ni mchovu na ana kiu, Eliezeri anahangaikia zaidi mahitaji ya wengine. Ametoka nchi ya kigeni kumtafutia mwana wa bwana-mkubwa wake mke. Isitoshe, ni lazima amtafute mke huyu kutoka kwa watu wa ukoo wa huyo bwana-mkubwa wake. Atatimizaje kazi hii ngumu?

      ELIEZERI anaamini kwamba sala ni yenye nguvu. Kwa imani yenye kutokeza, iliyo kama ya mtoto, yeye aomba hivi kwa unyenyekevu: “Ee BWANA, Mungu wa bwana wangu Ibrahimu, nakuomba mambo yangu uyajalie yawe heri leo, ukamfadhili bwana wangu Ibrahimu. Tazama! nimesimama karibu na kisima cha maji, na binti za watu wa mjini wanatoka kuteka maji, basi na iwe hivi; yule msichana nitakayemwambia, Tua mtungi wako, nakuomba, ninywe; naye akasema, Unywe, nami natawanywesha na ngamia zako pia; basi huyu na awe ndiye uliyemchagulia mtumishi wako Isaka; na kwa hayo nitajua ya kuwa umemfadhili bwana wangu.”—Mwanzo 24:12-14.

      Uhakika wa Eliezeri katika nguvu ya sala si wa bure. Kwani, kumbe mwanamke wa kwanza kabisa anayekuja kisimani ni mjukuu wa ndugu yake Abrahamu! Anaitwa Rebeka, naye ni mseja, safi kiadili, na mrembo. Jambo la kutokeza ni kwamba yeye anampa Eliezeri maji ya kunywa na pia anajitolea kwa fadhili kuwanywesha ngamia zake wote. Baadaye, baada ya mashauriano ya kifamilia, Rebeka anakubali kwa utayari kwenda na Eliezeri katika nchi ya mbali akawe mke wa Isaka, mwana wa Abrahamu. Sala ya Eliezeri inajibiwa kwa njia yenye kutokeza na dhahiri kama nini wakati huo ambapo Mungu aliingilia matukio kimwujiza mara moja moja!

      Tunaweza kujifunza mengi kutokana na sala ya Eliezeri. Sala hiyo ilionyesha imani yake yenye kutokeza, unyenyekevu, na kuhangaikia mahitaji ya wengine bila ubinafsi. Sala ya Eliezeri pia ilionyesha ujitiisho wake kwa njia ambayo Yehova hushughulika na wanadamu. Yaelekea alijua uhusiano wa pekee uliokuwapo kati ya Abrahamu na Mungu na vilevile ahadi Yake kwamba wanadamu wote wangebarikiwa wakati ujao kupitia Abrahamu. (Mwanzo 12:3) Hivyo, Eliezeri alianza sala yake kwa maneno haya: “Ee BWANA, Mungu wa bwana wangu Ibrahimu.”

      Yesu Kristo alikuwa mzao wa Abrahamu ambaye kupitia kwake wanadamu wote watiifu wangebarikiwa. (Mwanzo 22:18) Tukitaka sala zetu zijibiwe leo, tunahitaji kutambua kwa unyenyekevu njia ya Mungu ya kushughulika na wanadamu kupitia Mwana wake. Yesu Kristo alisema: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika muungano nami na semi zangu zakaa katika nyinyi, ombeni lolote lile mtakalo nalo litatukia kwenu.”—Yohana 15:7.

      Mfuasi wa Kristo aliyeona ukweli wa maneno hayo ya Yesu ni mtume Paulo. Hapana shaka kwamba imani yake katika sala haikuwa ya bure. Aliwatia moyo Wakristo wenzake wamtwike Mungu mahangaiko yao yote kupitia sala na kushuhudia hivi: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.” (Wafilipi 4:6, 7, 13) Je, hilo lamaanisha kwamba Paulo alipata majibu kwa maombi yake yote ya bidii? Ebu tuone.

      Si Sala Zote Zinazojibiwa

      Katika huduma yake isiyo na ubinafsi, Paulo aliugua kile alichokiita “mwiba katika mwili.” (2 Wakorintho 12:7) Huenda mwiba huo ulikuwa msononeko wa kiakili na wa kihisia-moyo uliosababishwa na wapinzani na “ndugu wasio wa kweli.” (2 Wakorintho 11:26; Wagalatia 2:4) Au huenda ulikuwa hali yenye kusumbua iliyosababishwa na ugonjwa wa macho wa kudumu. (Wagalatia 4:15) Hata iweje, “mwiba [huo] katika mwili” ulimdhoofisha Paulo. “Mara tatu nilimsihi sana Bwana kwamba upate kuniondoka,” yeye akaandika. Lakini ombi la Paulo halikujibiwa. Paulo alielezwa kwamba manufaa za kiroho ambazo alikuwa amekwisha pata kutoka kwa Mungu, kama vile nguvu za kuvumilia majaribu, zilitosha. Isitoshe, Mungu alisema: “Nguvu yangu inafanywa kamilifu katika udhaifu.”—2 Wakorintho 12:8, 9. 

      Tunajifunza nini kutokana na mifano ya Eliezeri na Paulo? Yehova Mungu kwa kweli husikiliza sala za wale wanaojitahidi kwa unyenyekevu kumtumikia. Lakini hilo halimaanishi kwamba yeye hujibu sala zao sikuzote kwa sababu Mungu hujua mambo yatakayotukia muda mrefu baadaye. Yeye anajua kutushinda yale yanayotufaa zaidi. La maana zaidi ni kwamba sikuzote yeye hutenda kulingana na makusudi yake kama yalivyoandikwa katika Biblia.

      Wakati wa Uponyaji wa Kiroho

      Mungu anaahidi kuponya wanadamu magonjwa yote ya kimwili, ya kiakili, na ya kihisia-moyo wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Mwana wake juu ya dunia. (Ufunuo 20:1-3; 21:3-5) Wakristo wa kweli wanangoja kwa hamu wakati huo ujao ulioahidiwa wakiwa na imani kamili kwamba Mungu ana uwezo wa kuuleta. Ingawa hawatarajii kuponywa kimuujiza leo, wao husali kwa Mungu wapate faraja na nguvu zake ili kuvumilia majaribu. (Zaburi 55:22) Wanapokuwa wagonjwa wanaweza pia kusali kupata mwongozo wa Mungu ili wapate matibabu yafaayo zaidi kulingana na uwezo wao wa kifedha.

      Dini kadhaa huwatia wagonjwa moyo wasali ili waponywe sasa, wakitaja maponyo ya kimuujiza ambayo Yesu na mitume wake walifanya. Lakini miujiza hiyo ilifanywa kwa kusudi la pekee. Ilifanywa kuthibitisha kwamba Yesu Kristo alikuwa Mesiya wa kweli na kudhihirisha kwamba Mungu alipendelea kutaniko changa la Kikristo bali si taifa la Kiyahudi. Wakati huo, zawadi za kimuujiza zilihitajika ili kuimarisha imani ya kutaniko la Kikristo lililokuwa limefanyizwa karibuni. Zawadi hizo za kimuujiza ‘ziliondolewa mbali’ wakati kutaniko hilo changa lilipoimarika na kukomaa.—1 Wakorintho 13:8, 11.

      Katika wakati huu muhimu, Yehova Mungu anawaelekeza waabudu wake katika kazi yenye maana zaidi ya uponyaji wa kiroho. Maadamu wangali na wakati, watu wanahitaji kuitikia haraka ombi hili: “Mtafuteni BWANA, maadamu anapatikana, mwiteni, maadamu yu karibu; mtu mbaya na aache njia yake, na mtu asiye haki aache mawazo yake; na amrudie BWANA, naye atamrehemu; na arejee kwa Mungu wetu, naye atamsamehe kabisa.”—Isaya 55:6, 7.

      Uponyaji huo wa kiroho wa watenda-dhambi wenye kutubu unatimizwa kupitia kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Kwa kuwatia nguvu watumishi wake watekeleze kazi hii ya kuokoa uhai, Yehova Mungu anasaidia mamilioni ya watu wa mataifa yote watubu dhambi zao na kuwa na uhusiano wenye upendeleo pamoja naye kabla ya mwisho wa mfumo huu mwovu. Sala za wote wanaosali kwa unyofu ili wapate ponyo hilo la kiroho na za wote wanaosali kupata msaada wa kufanya kazi hii ya kuponya zinajibiwa kwelikweli.

  • Mungu Hujibu Sala
    Mnara wa Mlinzi—2000 | Machi 1
    • Mungu Hujibu Sala

      Kornelio alitafuta upendeleo wa Mungu kwa kusali kwa ukawaida kutoka moyoni. Isitoshe, alitumia vizuri cheo chake akiwa ofisa wa jeshi. Kulingana na Biblia ‘yeye aliwafanyia watu wenye uhitaji zawadi nyingi za rehema.’—Matendo 10:1, 2.

      WAKATI huo, kutaniko la Kikristo lilifanyizwa na Wayahudi wenye kuamini, wageuzwa-imani, na Wasamaria. Kornelio, mtu asiye Myahudi na asiyetahiriwa, hakuwa mshiriki wa kutaniko la Kikristo. Je, jambo hilo lamaanisha kwamba alisali bure? La. Yehova Mungu alimsikiliza Kornelio na kuona kazi zake za bidii.—Matendo 10:4.

      Kornelio alielekezwa na malaika kupata kutaniko la Kikristo. (Matendo 10:30-33) Hivyo, yeye na watu wa nyumbani kwake wakapendelewa kuwa watu wa kwanza, wasio Wayahudi na wasiotahiriwa, kukubalika katika kutaniko la Kikristo. Yehova Mungu aliona inafaa kwamba mambo yaliyompata Kornelio yaandikwe katika Biblia. Yaelekea alifanya mabadiliko mengi ili kupatanisha maisha yake na viwango vya Mungu. (Isaya 2:2-4; Yohana 17:16) Mambo yaliyompata Kornelio yapaswa kuwatia moyo sana watu wa mataifa yote wanaotafuta upendeleo wa Mungu leo. Ona mifano kadhaa.

      Mifano ya Siku Hizi

      Mwanamke mmoja kijana nchini India alihitaji sana faraja. Aliolewa akiwa na umri wa miaka 21 na alikuwa na watoto wawili. Lakini punde tu baada ya mtoto wa pili kuzaliwa, mume wake akafa. Kwa ghafula, akiwa na umri wa miaka 24, akawa mjane mwenye binti wa umri wa miezi 2 na mwana wa umri wa miezi 22. Si ajabu kwamba alihitaji faraja! Angemwendea nani? Usiku mmoja, akiwa amesononeka sana, alisali akisema, “Baba wa mbinguni, tafadhali nifariji kupitia Neno lako.”

      Asubuhi iliyofuata akapata mgeni. Mgeni huyo alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Siku hiyo, huduma ya Shahidi huyo ya nyumba hadi nyumba ilikuwa ngumu kwa sababu watu wachache tu ndio waliomkaribisha. Akiwa amechoka na kuvunjika moyo, akataka kwenda nyumbani, lakini kwa sababu fulani asiyoijua akahisi anasukumwa azuru nyumba nyingine moja tu. Alimkuta mjane huyo mchanga kwenye nyumba hiyo. Akamkaribisha ndani na kuchukua kichapo kilichofafanua Biblia. Mwanamke huyo alifarijika sana kwa kusoma kichapo hicho na kwa kuzungumza na Shahidi huyo. Alijifunza juu ya ahadi ya Mungu ya kufufua wafu na juu ya Ufalme wa Mungu, ambao karibuni utafanya dunia kuwa paradiso. Jambo la maana zaidi ni kwamba alipata kumjua na kumpenda yule Mungu mmoja wa kweli, Yehova, aliyejibu sala yake.

      Nora, ambaye anaishi jijini George, Afrika Kusini, alitenga mwezi mmoja ili ashiriki katika kazi ya wakati wote ya kueneza evanjeli. Kabla ya kuanza, alisali kwa Yehova kwa bidii ili amsaidie kupata mtu ambaye alipendezwa kikweli na funzo la Biblia. Eneo alilogawiwa kuhubiri lilikuwa na nyumba ya mtu mmoja ambaye alikuwa mkali sana Nora alipozuru hapo awali. Kwa ujasiri, Nora akazuru nyumba hiyo tena. Alishangaa kukuta mpangaji mpya aitwaye Noleen. Isitoshe, Noleen na mama yake walikuwa wakisali kwa Mungu wapate msaada wa kuielewa Biblia. “Nilipowatolea funzo la Biblia,” aeleza Nora, “walifurahi sana.” Noleen na mama yake walifanya maendeleo haraka. Halafu, wote wawili wakaanza kushiriki pamoja na Nora katika kazi ya uponyaji wa kiroho.

      Mfano mwingine unaoonyesha nguvu za sala ni ule wa mume na mke wake wanaoishi jijini Johannesburg, Afrika Kusini. Jumamosi moja usiku mwaka wa 1996, ndoa ya Dennis na Carol ilikuwa karibu kuvunjika. Ikiwa hatua ya mwisho, wakaamua kusali kupata msaada, jambo walilofanya tena na tena hadi usiku wa manane. Saa 5:00 asubuhi iliyofuata, Mashahidi wa Yehova wawili wakabisha mlango wao. Dennis alifungua mlango na kuwaambia wangoje mpaka amwite mke wake. Kisha Dennis akamwonya Carol kwamba akiwakaribisha Mashahidi hao, inaweza kuwa vigumu kuwaondoa. Carol akamkumbusha Dennis kwamba walikuwa wakisali kupata msaada na kusema kwamba huenda Mungu anajibu sala zao. Basi Mashahidi hao wakakaribishwa, na funzo la Biblia likaanzishwa katika kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Dennis na Carol walifurahia sana yale waliyojifunza. Alasiri hiyohiyo, wakahudhuria mkutano kwa mara ya kwanza kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la huko. Kwa kutumia ujuzi waliojifunza katika Biblia, Dennis na Carol walitatua matatizo yao ya ndoa. Sasa wao ni wasifaji wa Yehova wenye furaha waliobatizwa na wao huzungumza na majirani wao kwa ukawaida juu ya itikadi zao zinazotegemea Biblia.

      Vipi Ukihisi Hustahili Kusali?

      Huenda watu fulani wenye mioyo myeupe wakahisi kwamba hawastahili kusali kwa sababu ya njia yao mbaya ya maisha. Yesu Kristo alisimulia juu ya mtu kama huyo, mkusanya-kodi aliyedharauliwa. Alipoingia kwenye ua wa hekalu, mtu huyu alihisi kwamba hastahili kwenda mahali pa kawaida pa sala. “Akiwa amesimama kwa umbali fulani . . . alifuliza kupiga kifua chake, akisema, ‘Ee Mungu, uwe mwenye fadhili kwangu mimi mtenda-dhambi.’” (Luka 18:13) Kulingana na Yesu, mtu huyu alisikilizwa kwa upendeleo. Jambo hilo lathibitisha kwamba Yehova Mungu kwa kweli ni mwenye neema na hutaka kuwasaidia watenda-dhambi wanaotubu kikweli.

      Fikiria mwanamume mmoja kijana wa Afrika Kusini aitwaye Paul. Akiwa mvulana, Paul alikuwa akihudhuria mikutano ya Kikristo pamoja na mama yake. Lakini wakati wa ujana, akaanza kushirikiana na vijana ambao hawakufuata njia za Mungu. Baada ya kumaliza shule, alitumikia katika jeshi la serikali ya awali ya ubaguzi wa rangi ya Afrika Kusini. Kisha, kwa ghafula rafiki yake wa kike akakatiza uhusiano wao. Maisha hayo yasiyoridhisha yakamvunja Paul moyo sana. “Jioni moja,” yeye akumbuka, “nikasali kwa Yehova anisaidie, hata ingawa kwa miaka mingi sikuwa nimemfikia Mungu kwa moyo mweupe.”

      Muda mfupi baada ya sala hiyo, mama ya Paul akamwalika ahudhurie Ukumbusho wa kifo cha Kristo wa kila mwaka. (Luka 22:19) Kwa kuwa Paul alikuwa mkaidi na hakupendezwa na Biblia, alishangaa kwamba mama yake alimwalika. “Niliona mwaliko huo kuwa jibu la Yehova kwa sala yangu na kuhisi kwamba ni lazima nihudhurie.” Tangu wakati huo na kuendelea, Paul akaanza kuhudhuria mikutano yote ya Kikristo. Baada ya kujifunza Biblia kwa miezi minne, akabatizwa. Isitoshe, aliacha masomo yake ya uhandisi na kuchagua kazi-maisha ya mweneza-evanjeli wa wakati wote. Leo, Paul ni mwenye furaha na maisha yake ya zamani hayafanyi ashuke moyo. Kwa miaka 11, ametumikia kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower Society huko Afrika Kusini.

      Kwa kweli, Yehova Mungu hujibu sala kwa neema na “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Karibuni siku kubwa ya Yehova itafika na kukomesha uovu wote. Wakati huohuo, Yehova anawajibu watu wake wanaposali kupata nguvu na mwelekezo wanaposhiriki kwa bidii katika kazi ya kutoa ushahidi. Hivyo, mamilioni ya watu kutoka mataifa yote wanaletwa kwenye kutaniko la Kikristo na wanabarikiwa kwa ujuzi wa Biblia uongozao kwenye uhai udumuo milele.—Yohana 17:3.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki