Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Sala Zako Zinafunua Nini Kukuhusu?
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Novemba 15
    • Sala Zako Zinafunua Nini Kukuhusu?

      “Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.”—ZAB. 65:2.

      1, 2. Kwa nini watumishi wa Yehova wanaweza kusali kwake wakiwa na hakika kwamba anawasikiliza?

      YEHOVA hapuuzi kamwe maombi ya watumishi wake waaminifu. Tunaweza kuwa na hakika kwamba anatusikiliza. Hata ikiwa mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wangesali kwa Mungu wakati uleule, bado angemsikiliza kila mmoja wao.

      2 Akiwa na hakika kwamba Mungu alisikiliza maombi yake, mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.” (Zab. 65:2) Sala za Daudi zilijibiwa kwa sababu alikuwa mwabudu mshikamanifu wa Yehova. Tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, dua zangu zinaonyesha kwamba ninamtumaini Yehova na kwamba ibada safi ndiyo hangaiko langu kuu? Sala zangu zinafunua nini kunihusu?’

      Sali kwa Yehova kwa Unyenyekevu

      3, 4. (a) Tunapaswa kusali kwa Mungu tukiwa na mtazamo gani? (b) Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunasumbuliwa na ‘fikira zinazofadhaisha’ kwa sababu ya dhambi nzito?

      3 Ili sala zetu zijibiwe, ni lazima tusali kwa Mungu kwa unyenyekevu. (Zab. 138:6) Tunapaswa kumwomba Yehova atuchunguze, kama Daudi alivyofanya aliposema hivi: “Unichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu. Unichunguze, na uzijue fikira zangu zinazofadhaisha, na uone kama ndani yangu mna njia yoyote yenye kuumiza, na uniongoze katika njia ya mpaka wakati usio na kipimo.” (Zab. 139:23, 24) Badala ya kusali tu tunapaswa pia kumruhusu Mungu atuchunguze na tunapaswa kutii mashauri ya Neno lake. Yehova anaweza kutuongoza kwenye “njia ya mpaka wakati usio na kipimo,” na kutusaidia kufuata njia inayoongoza kwenye uzima wa milele.

      4 Namna gani ikiwa tunasumbuliwa na ‘fikira zinazofadhaisha’ kwa sababu ya dhambi nzito? (Soma Zaburi 32:1-5.) Kujaribu kuinyamazisha dhamiri yenye hatia kunaweza kutufanya tunyauke kama mti ambao unapoteza maji yake wakati wa majira ya joto kali. Kwa sababu ya dhambi aliyotenda, Daudi alipoteza shangwe yake na hata labda akawa mgonjwa. Lakini alipata kitulizo kama nini alipoungama dhambi yake kwa Mungu! Fikiria shangwe ya Daudi alipohisi kwamba Yehova alikuwa ‘amemsamehe maasi yake.’ Kuungama dhambi kwa Mungu kunaweza kuleta kitulizo, na msaada wa wazee Wakristo utamsaidia mkosaji kuwa tena na hali nzuri ya kiroho.—Met. 28:13; Yak. 5:13-16.

      Msihi Mungu na Kumshukuru

      5. Kutoa dua kwa Yehova kunamaanisha nini?

      5 Ikiwa mambo fulani yanatufanya tuwe na mahangaiko mengi, tunapaswa kufuata shauri hili la Paulo: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.” (Flp. 4:6) “Kutoa dua” kunamaanisha “kusihi kwa unyenyekevu.” Tunapaswa kumsihi sana Yehova atusaidie na kutuongoza hasa wakati wa hatari au mateso.

      6, 7. Kwa nini tunapaswa kumshukuru Mungu katika sala zetu?

      6 Hata hivyo, tukisali tu wakati tunapohitaji kitu fulani, hilo linafunua nini kuhusu nia yetu? Paulo alisema kwamba tunapaswa kutoa maombi yetu ili yajulikane na Mungu “pamoja na kutoa shukrani.” Bila shaka, tuna sababu nzuri ya kumshukuru Mungu kutoka moyoni kama Daudi aliyesema hivi: “Ee Yehova, ukuu ni wako na nguvu na uzuri na utukufu na heshima; kwa maana kila kitu mbinguni na duniani ni chako. Ufalme ni wako, Ee Yehova, Wewe unayejiinua kuwa kichwa juu ya wote. . . . Ee Mungu wetu, tunakushukuru na kulisifu jina lako zuri.”—1 Nya. 29:11-13.

      7 Yesu alimshukuru Mungu kwa ajili ya chakula na kwa ajili ya mkate na divai ambayo ilitumiwa wakati wa Mlo wa Jioni wa Bwana. (Mt. 15:36; Marko 14:22, 23) Zaidi ya kuonyesha shukrani kama hiyo, tunapaswa ‘kumshukuru Yehova’ kwa ajili ya “kazi zake za ajabu kwa wana wa binadamu,” ‘maamuzi yake ya hukumu ya uadilifu,’ na kwa ajili ya neno lake, au ujumbe ambao unapatikana sasa katika Biblia.—Zab. 107:15; 119:62, 105.

      Sali kwa Ajili ya Wengine

      8, 9. Kwa nini tunapaswa kusali kwa ajili ya Wakristo wenzetu?

      8 Bila shaka, tunasali kwa ajili yetu wenyewe, lakini tunapaswa pia kusali kwa ajili ya wengine, hata Wakristo ambao hatuwajui kwa jina. Hata ingawa huenda mtume Paulo hakuwajua waamini wote huko Kolosai, aliandika hivi: “Sikuzote sisi humshukuru Mungu Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo tunaposali kwa ajili yenu, kwa kuwa tulisikia juu ya imani yenu kuhusiana na Kristo Yesu na upendo mlio nao kwa watakatifu wote.” (Kol. 1:3, 4) Paulo alisali pia kwa ajili ya Wakristo wa Thesalonike. (2 The. 1:11, 12) Sala za aina hiyo zinafunua mengi kutuhusu na kuhusu jinsi tunavyowaona ndugu na dada zetu katika imani.

      9 Sala zetu kwa ajili ya Wakristo watiwa-mafuta na kwa ajili ya waandamani wao wa “kondoo wengine” zinaonyesha wazi hangaiko letu kwa ajili ya tengenezo la Mungu. (Yoh. 10:16) Paulo aliwaomba waabudu wenzake wasali kusudi ‘apewe uwezo wa kusema ili ajulishe siri takatifu ya habari njema.’ (Efe. 6:17-20) Je, tunasali kibinafsi kwa njia hiyo kwa ajili ya Wakristo wengine?

      10. Kusali kwa ajili ya wengine huenda kukawa na uvutano gani juu yetu?

      10 Kusali kwa ajili ya wengine kunaweza kubadili mtazamo wetu kuwaelekea. Tukisali kwa ajili ya mtu ambaye hatumpendi sana inaelekea hilo litabadili mtazamo wetu kumwelekea mtu huyo. (1 Yoh. 4:20, 21) Sala za aina hiyo zinajenga na zinachangia umoja pamoja na ndugu zetu. Zaidi ya hayo, sala kama hizo zinaonyesha kwamba tuna upendo kama wa Kristo. (Yoh. 13:34, 35) Sifa hiyo ni sehemu ya matunda ya roho ya Mungu. Je, tunasali kibinafsi ili tupewe roho takatifu, tukimwomba Yehova atusaidie kuonyesha matunda ya roho, yaani, upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujizuia? (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23) Ikiwa ndivyo, maneno na matendo yetu yataonyesha kwamba tunatembea na kuishi kwa roho.—Soma Wagalatia 5:16, 25.

      11. Kwa nini unaweza kusema kwamba ni jambo linalofaa kuwaomba wengine wasali kwa ajili yetu?

      11 Tukipata habari kwamba watoto wetu wanashawishiwa kuiba mitihani shuleni, tunapaswa kusali kwa ajili yao na pia kutumia Maandiko ili kuwasaidia watende kwa unyoofu na kuepuka kufanya jambo lolote baya. Paulo aliwaambia Wakristo wa Korintho hivi: “Tunasali kwa Mungu kwamba msifanye kosa.” (2 Kor. 13:7) Sala za unyenyekevu za aina hiyo zinampendeza Yehova na zinafunua sifa zetu nzuri. (Soma Methali 15:8.) Tunaweza kuwaomba wengine wasali kwa ajili yetu, kama mtume Paulo alivyofanya. Aliandika hivi: “Endeleeni kusali kwa ajili yetu, kwa maana sisi tuna uhakika kwamba tuna dhamiri nyoofu, kwa kuwa tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Ebr. 13:18.

      Sala Zetu Zinafunua Mambo Mengi Zaidi Kutuhusu

      12. Ni mambo gani yanayopaswa kuwa ya maana sana katika sala zetu?

      12 Je, sala zetu zinaonyesha kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova wenye furaha na bidii? Je, dua zetu zinakazia hasa kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu, kuhubiriwa kwa ujumbe wa Ufalme, kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova, na kutakaswa kwa jina lake? Hayo yanapaswa kuwa mambo ya maana sana katika sala zetu, kama inavyoonyeshwa na sala ya Yesu ya kielelezo, ambayo inaanza kwa maneno haya: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mt. 6:9, 10.

      13, 14. Sala zetu zinafunua nini kutuhusu?

      13 Sala zetu kwa Mungu zinafunua nia, mapendezi, na tamaa zetu. Yehova anajua sisi ni watu wa aina gani. Andiko la Methali 17:3 linasema hivi: “Chungu cha kusafishia ni kwa ajili ya fedha na tanuru ni kwa ajili ya dhahabu, lakini Yehova ndiye mchunguzaji wa mioyo.” Mungu anaona yale yaliyo katika mioyo yetu. (1 Sam. 16:7) Anajua jinsi tunavyohisi kuhusu mikutano yetu, huduma yetu, na ndugu na dada zetu wa kiroho. Yehova anajua jinsi tunavyofikiri kuhusu “ndugu” za Kristo. (Mt. 25:40) Anajua ikiwa kwa kweli tunataka mambo tunayoomba katika sala au tunarudia-rudia tu maneno fulani. Yesu alisema: “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa wanavyofanya, kwa maana wao huwaza [kimakosa] watasikiwa kwa kutumia maneno mengi.”—Mt. 6:7.

      14 Mambo tunayosema katika sala yanafunua ni kwa kadiri gani tunamtegemea Mungu. Daudi alisema hivi: “[Yehova] umekuwa kimbilio langu, mnara wenye nguvu mbele ya uso wa adui. Nitakuwa mgeni katika hema lako mpaka nyakati zisizo na kipimo; nitakimbilia maficho ya mabawa yako.” (Zab. 61:3, 4) Kwa njia ya mfano, Mungu ‘anapotandaza hema lake juu yetu,’ tunafurahia usalama na ulinzi wake. (Ufu. 7:15) Inafariji kama nini kumkaribia Yehova katika sala tukiwa na uhakika wa kwamba yuko ‘upande wetu’ tunapokabili jaribu lolote la imani yetu!—Soma Zaburi 118:5-9.

      15, 16. Sala inaweza kutusaidia kutambua nini kuhusu tamaa yetu ya kufikia mapendeleo ya utumishi?

      15 Sala ya unyoofu kwa Yehova kuhusu nia yetu inaweza kutusaidia kutambua ukweli kuhusu nia hiyo. Kwa mfano, je, tunataka sana kutumikia katika pendeleo fulani la uangalizi kati ya watu wa Mungu kwa sababu tunatamani kwa unyenyekevu kusaidia na kufanya yote tunayoweza ili kuendeleza mambo ya Ufalme? Au je, inawezekana kwamba tunataka kuwa “mahali pa kwanza” au hata tunatamani ‘kupiga ubwana juu’ ya wengine? Mambo hayapaswi kuwa hivyo kati ya watu wa Yehova. (Soma 3 Yohana 9, 10; Luka 22:24-27.) Ikiwa tuna tamaa mbaya, kusali kwa unyoofu kwa Yehova Mungu kunaweza kufunua tamaa hizo na kutusaidia kubadilika kabla hazijatia mizizi.

      16 Huenda wake Wakristo wakatamani sana waume wao watumike wakiwa watumishi wa huduma na labda baadaye wakiwa waangalizi, au wazee. Dada hao wanaweza kutenda kupatana na hisia ambazo wanaeleza katika sala zao za faraghani kwa kujitahidi kujiendesha wenyewe kwa njia nzuri. Hilo ni jambo la maana kwa sababu maneno na mwenendo wa familia unaweza kumfanya mtu aonwe na kutaniko kwa njia inayofaa au isiyofaa.

      Kuwakilisha Wengine Katika Sala ya Watu Wote

      17. Kwa nini ni vizuri kuwa peke yetu tunaposali faraghani?

      17 Mara nyingi, Yesu alijitenga na umati wa watu ili asali kwa Baba yake faraghani. (Mt. 14:13; Luka 5:16; 6:12) Sisi pia, tunahitaji wakati fulani kuwa peke yetu. Tunaposali kwa utulivu katika mazingira yenye amani, inaelekea kwamba tutafanya maamuzi yatakayompendeza Yehova na ambayo yatatusaidia sana kubaki wenye nguvu kiroho. Hata hivyo, Yesu alisali pia hadharani, na ni vizuri kuchunguza jinsi tunavyoweza kusali hadharani kwa njia nzuri.

      18. Ni mambo gani ambayo ndugu wanapaswa kukumbuka wanapoliwakilisha kutaniko katika sala ya watu wote?

      18 Kwenye mikutano yetu, wanaume washikamanifu wanaliwakilisha kutaniko katika sala ya watu wote. (1 Tim. 2:8) Waamini wenzetu wanapaswa kusema “amina,” kumaanisha “na iwe hivyo,” mwishoni mwa sala hiyo. Hata hivyo, ili waseme “amina” ni lazima wakubaliane na yale yaliyosemwa. Katika ile sala ya kielelezo, Yesu hakusema jambo lolote lisilo la busara au lenye kushtua. (Luka 11:2-4) Zaidi ya hayo, hakutaja mahitaji yote au matatizo ya kila mtu kati ya wasikilizaji wake. Ni vizuri kutaja mahangaiko ya kibinafsi katika sala ya faraghani, bali si katika sala ya watu wote. Na tunapowakilisha kikundi cha watu katika sala, tunapaswa kuepuka kutaja mambo ya siri.

      19. Tunapaswa kujiendesha jinsi gani wakati wa sala ya watu wote?

      19 Tunapowakilishwa katika sala ya watu wote, tunapaswa kuonyesha heshima inayotokana na ‘kumwogopa Mungu.’ (1 Pet. 2:17) Kuna wakati unaofaa na mahali panapofaa pa kufanya mambo fulani ambayo si vizuri kuyafanya kwenye mkutano wa Kikristo. (Mhu. 3:1) Kwa mfano, tuseme kwamba mtu fulani anawahimiza watu wote katika kikundi washikane mikono wakati wa sala. Hilo linaweza kuwaudhi au kuwakengeusha wengine, kutia ndani wageni ambao si waamini wenzetu. Wenzi fulani wa ndoa wanaweza kushikana mikono kwa busara, lakini wakikumbatiana wakati wa sala ya watu wote, wanaweza kuwakwaza wale ambao wanaona mwenendo huo. Huenda wakafikiri au kuwa na maoni ya kwamba wenzi hao wanakazia fikira uhusiano wao wa kimahaba badala ya kumheshimu Yehova. Kwa sababu ya kumheshimu Mungu, acheni ‘tufanye mambo yote kwa utukufu wa Mungu’ na kuepuka mwenendo ambao unaweza kumkengeusha, kumshtua, au kumkwaza mtu yeyote.—1 Kor. 10:31, 32; 2 Kor. 6:3.

      Tusali kwa Ajili ya Mambo Gani?

      20. Unaweza kufafanua Waroma 8:26, 27 kwa njia gani?

      20 Nyakati nyingine, huenda tusijue jambo la kusema katika sala zetu za faraghani. Paulo aliandika hivi: “Lile tatizo kuhusu tunalohitaji kusali hatujui, lakini roho [takatifu] yenyewe hutuombea pamoja na kuugua kusikotamkwa. Lakini [Mungu] ambaye huichunguza mioyo anajua ni nini maana ya roho.” (Rom. 8:26, 27) Yehova aliongoza mambo ili sala nyingi ziandikwe katika Maandiko. Anakubali maombi hayo yaliyoongozwa na roho yake kana kwamba ni maombi yetu wenyewe na hivyo anayatimiza. Mungu anatujua na anajua pia maana ya mambo ambayo aliongoza roho yake iseme kupitia waandikaji wa Biblia. Yehova anajibu dua zetu wakati roho ‘inapoomba,’ au kusihi, kwa ajili yetu. Lakini kadiri tunavyojua vizuri zaidi Neno la Mungu, ndivyo tunavyokumbuka kwa urahisi zaidi mambo tunayohitaji kuomba.

      21. Tutachunguza nini katika habari ambayo inafuata?

      21 Kama tulivyoona, sala zetu zinafunua mengi kutuhusu. Kwa mfano, zinaweza kufunua jinsi tulivyo na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova na jinsi tunavyolijua vizuri Neno lake. (Yak. 4:8) Katika habari inayofuata, tutachunguza sala na maombi fulani yaliyoandikwa katika Biblia. Inaelekea uchunguzi huo wa Maandiko utaboresha jinsi gani sala zetu kwa Mungu?

  • Boresha Sala Zako Kupitia Funzo la Biblia
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Novemba 15
    • Boresha Sala Zako Kupitia Funzo la Biblia

      “Ah, tafadhali, Yehova, tega sikio lako kwa sala ya mtumishi wako.”—NEH. 1:11.

      1, 2. Kwa nini tutafaidika tukichunguza sala mbalimbali zilizoandikwa katika Biblia?

      SALA na funzo la Biblia ni mambo ya maana sana katika ibada ya kweli. (1 The. 5:17; 2 Tim. 3:16, 17) Bila shaka, Biblia si kitabu cha sala. Hata hivyo, ina sala nyingi, kutia ndani zile zinazopatikana katika kitabu cha Zaburi.

      2 Unaposoma na kujifunza Biblia, inaelekea utapata sala zinazohusu hali unazokabili. Kwa kweli, unapotumia mawazo yaliyo katika sala zilizoandikwa katika Maandiko unaboresha sala zako. Unaweza kujifunza nini kutokana na wale ambao maombi yao ya kutaka msaada yalijibiwa na kutokana na mambo waliyotaja katika sala zao?

      Tafuta na Kufuata Mwongozo wa Mungu

      3, 4. Mtumishi wa Abrahamu alitumwa kufanya nini, na tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyoongoza mambo?

      3 Funzo lako la Biblia linakusaidia kuona kwamba unapaswa sikuzote kuomba mwongozo wa Mungu. Ona yale yaliyotukia wakati mzee wa ukoo Abrahamu alipomtuma mtumishi wake mwenye umri mkubwa zaidi, inaelekea Eliezeri, kwenda Mesopotamia ili kumtafutia Isaka mke anayemwogopa Mungu. Wanawake walipokuwa wakichota maji kwenye kisima fulani, mtumishi huyo alisali hivi: “Yehova . . . , litakalotokea ni kwamba mwanamke kijana ambaye nitamwambia, ‘Tafadhali, shusha mtungi wako wa maji ili ninywe,’ na ambaye kwa kweli atasema, ‘Kunywa, na pia nitanywesha ngamia zako,’ huyo ndiye utakayemchagulia mtumishi wako, Isaka; na kwa hilo unijulishe kwamba umefanya upendo mshikamanifu kwa bwana wangu.”—Mwa. 24:12-14.

      4 Sala ya mtumishi wa Abrahamu ilijibiwa wakati Rebeka alipowanywesha ngamia wake. Baadaye, Rebeka alienda Kanaani pamoja na mtumishi huyo na hivyo akawa mke mpendwa wa Isaka. Bila shaka, huwezi kumtazamia Mungu akupe ishara ya pekee. Hata hivyo, atakuongoza maishani ikiwa unasali na kuazimia kuongozwa na roho yake.—Gal. 5:18.

      Sala Inasaidia Kupunguza Mahangaiko

      5, 6. Tunajifunza jambo gani kutokana na sala ambayo Yakobo alitoa alipokaribia kukutana na Esau?

      5 Sala inaweza kupunguza mahangaiko. Huku akiogopa hatari kutoka kwa ndugu yake pacha, Esau, Yakobo alisali hivi: “Ee Yehova, . . . Mimi sistahili fadhili zote zenye upendo na uaminifu wote ambao umemwonyesha mtumishi wako . . . Nakuomba, unikomboe kutoka katika mkono wa ndugu yangu, kutoka katika mkono wa Esau, kwa sababu mimi ninaogopa kwamba huenda akaja na kunishambulia, mama pamoja na watoto. Nawe, umesema, ‘Bila shaka nitakutendea vema nami nitaufanya uzao wako uwe kama chembe za mchanga wa baharini, usioweza kuhesabika kwa sababu ya wingi wake.’”—Mwa. 32:9-12.

      6 Ingawa Yakobo alichukua hatua za kujilinda, sala yake ilijibiwa wakati yeye na Esau walipopatana. (Mwa. 33:1-4) Soma sala au maombi hayo kwa makini, na utaona kwamba Yakobo hakuomba tu msaada. Alionyesha imani katika ule Uzao ulioahidiwa na alimshukuru Mungu kwa ajili ya fadhili zake zisizostahiliwa. Je, una ‘woga fulani ndani’ yako? (2 Kor. 7:5) Ikiwa ndivyo, basi huenda maombi ya Yakobo yakakukumbusha kwamba sala zinaweza kupunguza mahangaiko. Hata hivyo, sala hazipaswi tu kuwa na maombi bali pia maneno yanayoonyesha kwamba tuna imani.

      Sali Ili Upewe Hekima

      7. Kwa nini Musa alisali ili apewe ujuzi kuhusu njia za Yehova?

      7 Tamaa ya kutaka kumpendeza Yehova inapaswa kukuchochea kusali ili upewe hekima. Musa alisali ili apewe ujuzi kuhusu njia za Mungu. Alimsihi hivi: “Angalia, wewe [Yehova] unaniambia, ‘Waongoze watu hawa [kutoka Misri]’ . . . Na sasa, tafadhali, ikiwa nimepata kibali machoni pako, nijulishe, tafadhali, njia zako, . . . ili nipate kibali machoni pako.” (Kut. 33:12, 13) Mungu alijibu sala hiyo kwa kumpa Musa ujuzi mwingi zaidi kuhusu njia Zake. Musa alihitaji ujuzi huo ili awaongoze watu wa Yehova.

      8. Unaweza kufaidika jinsi gani ukitafakari juu ya andiko la 1 Wafalme 3:7-14?

      8 Daudi pia alisali hivi: “Nijulishe njia zako, Ee Yehova.” (Zab. 25:4) Sulemani, mwana wa Daudi alimsihi Mungu ampe hekima aliyohitaji ili kutimiza madaraka ya kifalme katika Israeli. Sala ya Sulemani ilimpendeza Yehova, naye akampa si tu kile alichoomba, bali pia utajiri na utukufu. (Soma 1 Wafalme 3:7-14.) Ikiwa umepata mapendeleo ya utumishi ambayo yanaonekana yanakulemea, sali ili upewe hekima na uonyeshe roho ya unyenyekevu. Hivyo, Mungu atakusaidia kupata ujuzi na kuwa na hekima unayohitaji ili utimize madaraka yako kwa njia nzuri na yenye upendo.

      Sali Kutoka Moyoni

      9, 10. Ni jambo gani la pekee unalojifunza katika maneno ambayo Sulemani anataja kuhusu moyo katika sala yake ya kuzindua hekalu?

      9 Ili sala yetu isikiwe, ni lazima itoke moyoni. Sulemani alitoa sala ya kutoka moyoni, iliyo katika 1 Wafalme sura ya 8, mbele ya umati wa watu uliokusanyika huko Yerusalemu kwa ajili ya kuzinduliwa kwa hekalu la Yehova katika mwaka wa 1026 K.W.K. Baada ya sanduku la agano kuwekwa katika Patakatifu Zaidi na wingu la Yehova kulijaza hekalu, Sulemani alimsifu Mungu.

      10 Ichunguze sala ya Sulemani na uone mambo anayotaja kuhusu moyo. Sulemani alitambua kwamba Yehova peke yake ndiye anayeujua moyo wa mwanadamu. (1 Fal. 8:38, 39) Sala hiyohiyo inaonyesha kwamba kuna tumaini kwa mtenda-dhambi ‘anayerudi kwa Mungu kwa moyo wake wote.’ Ikiwa adui angewateka nyara watu wa Mungu, maombi yao yangesikiwa ikiwa mioyo yao ilikuwa kamili kwa Yehova. (1 Fal. 8:48, 58, 61) Hivyo basi, sala zako zinapaswa kutoka moyoni.

      Jinsi Zaburi Zinavyoweza Kuboresha Sala Zako

      11, 12. Umejifunza nini kutokana na sala ya Mlawi mmoja ambaye kwa muda fulani hangeweza kwenda patakatifu pa Mungu?

      11 Kujifunza Zaburi kunaweza kuboresha sala zako na kukusaidia kumngojea Mungu ajibu sala hizo. Fikiria subira ambayo ilionyeshwa na Mlawi mmoja aliyekuwa uhamishoni. Ingawa kwa muda fulani hangeweza kwenda patakatifu pa Yehova, aliimba hivi: “Kwa nini umekata tamaa, Ee nafsi yangu, na kwa nini una msukosuko ndani yangu? Mngojee Mungu, kwa maana bado nitamsifu kuwa ndiye wokovu wangu mkuu na kuwa ndiye Mungu wangu.”—Zab. 42:5, 11; 43:5.

      12 Unaweza kujifunza nini kutokana na Mlawi huyo? Ikiwa kufungwa gerezani kwa ajili ya uadilifu kungekuzuia kwa muda fulani kuwa pamoja na waamini wenzako mahali pa ibada, mngojee Mungu kwa subira ili atende kwa ajili yako. (Zab. 37:5) Tafakari juu ya shangwe uliyopata wakati uliopita katika utumishi wa Mungu, na usali ili uweze kuvumilia ‘unapomngojea Mungu’ akufungulie njia ya kuendelea kushirikiana na watu wake.

      Sali kwa Imani

      13. Kulingana na Yakobo 1:5-8, kwa nini unapaswa kusali kwa imani?

      13 Hata uwe unakabili hali gani, sali sikuzote kwa imani. Ikiwa unakabili jaribu la utimilifu, fuata shauri la mwanafunzi Yakobo. Sali kwa Yehova, na usiwe na shaka kamwe kwamba anaweza kukupa hekima unayohitaji ili uvumilie jaribu lako. (Soma Yakobo 1:5-8.) Mungu anajua mahangaiko yote yanayokusumbua, naye anaweza kukuongoza na kukufariji kupitia roho yake. Mfungulie moyo wako ukiwa na imani kamili, “bila kutia shaka hata kidogo,” na ukubali mwongozo wa roho yake na mashauri ya Neno lake.

      14, 15. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Hana alisali na kutenda kwa imani?

      14 Hana, mmoja kati ya wake wawili wa Mlawi aliyeitwa Elkana, alisali na kutenda kwa imani. Hana ambaye hakuwa amezaa mtoto alidhihakiwa na mke mwenzake, Penina, ambaye alizaa watoto wengi. Kwenye maskani, Hana aliweka nadhiri kwamba ikiwa angezaa mwana, angemtoa kwa Yehova. Kwa kuwa midomo ya Hana ilikuwa ikitetemeka alipokuwa akisali, Kuhani Mkuu Eli alifikiri kwamba alikuwa mlevi. Lakini Eli alipojua kwamba Hana hakuwa mlevi, alimwambia hivi: “Mungu wa Israeli akupe ombi lako ambalo umemwomba.” Ingawa Hana hakujua matokeo yangekuwa nini, alikuwa na imani kwamba sala yake ingejibiwa. Kwa hiyo, “uso wake haukuonyesha tena kuhangaika.” Hakuendelea kuhuzunika au kuvunjika moyo.—1 Sam. 1:9-18.

      15 Baada ya Samweli kuzaliwa na kuachishwa kunyonya, Hana alimtoa kwa Yehova ili afanye utumishi mtakatifu kwenye maskani. (1 Sam. 1:19-28) Kutafakari kuhusu sala ya Hana katika pindi hiyo kunaweza kuboresha sala zako na kukusaidia kuona kwamba unaweza kushinda hata huzuni inayosababishwa na tatizo lenye kufadhaisha, ukisali ukiwa na imani ya kwamba Yehova atajibu sala yako.—1 Sam. 2:1-10.

      16, 17. Ni nini kilichotukia baada ya Nehemia kusali na kutenda kwa imani?

      16 Mwanamume mnyoofu Nehemia aliyeishi katika karne ya tano K.W.K. alisali na kutenda kwa imani. Alisihi hivi: “Ah, tafadhali, Yehova, tega sikio lako kwa sala ya mtumishi wako na kwa sala ya watumishi wako wanaofurahia kuliogopa jina lako; na, tafadhali, mpe mafanikio mtumishi wako leo na kumfanya ahurumiwe mbele ya mtu huyu.” “Mtu huyu” alikuwa nani? Alikuwa Mfalme Artashasta wa Uajemi, ambaye Nehemia alimtumikia akiwa mnyweshaji.—Neh. 1:11.

      17 Nehemia alisali kwa imani kwa siku nyingi baada ya kupata habari kwamba Wayahudi ambao waliachiliwa huru kutoka utekwani Babiloni walikuwa “katika hali mbaya sana na katika aibu; na ukuta wa Yerusalemu [ulikuwa] umebomoka.” (Neh. 1:3, 4) Sala za Nehemia zilijibiwa kupita alivyotazamia wakati Mfalme Artashasta alipomruhusu kwenda kujenga upya ukuta wa Yerusalemu. (Neh. 2:1-8) Baada ya muda mfupi, ukuta ulikuwa umejengwa. Sala za Nehemia zilijibiwa kwa sababu zilikazia ibada ya kweli na zilitolewa kwa imani. Je, ndivyo sala zako zilivyo?

      Kumbuka Kumsifu na Kumshukuru Mungu

      18, 19. Kwa nini mtumishi wa Yehova anapaswa kumsifu na kumshukuru?

      18 Kumbuka kumsifu na kumshukuru Yehova katika sala. Kuna sababu nyingi sana za kufanya hivyo! Kwa mfano, Daudi alikuwa na hamu kubwa ya kuusifu ufalme wa Yehova. (Soma Zaburi 145:10-13.) Je, sala zako zinaonyesha kwamba unathamini pendeleo la kutangaza Ufalme wa Yehova? Maneno ya watunga-zaburi yanaweza pia kukusaidia kusali kwa Mungu kutoka moyoni na kumshukuru kwa ajili ya mikutano ya Kikristo na makusanyiko yote.—Zab. 27:4; 122:1.

      19 Kuthamini uhusiano wako mzuri pamoja na Mungu kunaweza kukuchochea usali kutoka moyoni ukitumia mawazo kama haya: “Nitakusifu katikati ya vikundi vya watu, Ee Yehova; nitakupigia muziki katikati ya vikundi vya mataifa. Kwa maana fadhili zako zenye upendo ni kuu kufika mbinguni, na ukweli wako mpaka angani. Utukuzwe juu ya mbingu, Ee Mungu; utukufu wako na uwe juu ya dunia yote.” (Zab. 57:9-11) Ni maneno yenye kutia moyo kama nini! Je, hukubali kwamba maneno hayo yenye kugusa moyo ya Zaburi yanaweza kuwa na uvutano mzuri juu yako na kuboresha sala zako?

      Msihi Mungu kwa Heshima

      20. Maria alionyesha jinsi gani ujitoaji wake kwa Mungu?

      20 Sala zako zinapaswa kuonyesha wazi kwamba unamheshimu Mungu. Maneno ya heshima ambayo Maria alisema muda mfupi baada ya kujulishwa kwamba angekuwa mama ya Masihi yanalingana na yale ambayo Hana alisema alipokuwa akimpeleka kijana Samweli kwenye utumishi wa maskani. Maneno yafuatayo yaliyosemwa na Maria yanaonyesha wazi kwamba alimheshimu Mungu: “Nafsi yangu inamtukuza Yehova, na roho yangu haiwezi kuacha kumfurahia Mungu Mwokozi wangu.” (Luka 1:46, 47) Je, unaweza kuboresha sala zako na maneno kama hayo yenye hisia? Haishangazi kwamba Maria aliyemwogopa Mungu alichaguliwa kuwa mama ya Yesu yule Masihi!

      21. Sala za Yesu zilionyesha jinsi gani heshima na imani?

      21 Yesu alisali kwa heshima akiwa na imani kabisa. Kwa mfano, kabla ya kumfufua Lazaro, ‘Yesu aliinua macho yake kuelekea mbinguni na kusema: “Baba, ninakushukuru kwamba umenisikia. Kweli, nilijua kwamba sikuzote wewe hunisikia.”’ (Yoh. 11:41, 42) Je, sala zako zinaonyesha imani na heshima kama hiyo? Ukichunguza sala ya Yesu ya kielelezo yenye heshima, utaona kwamba mambo makuu katika sala hiyo hasa ni kutakaswa kwa jina la Yehova, kuja kwa Ufalme wake, na kutimizwa kwa mapenzi yake. (Mt. 6:9, 10) Fikiria kuhusu sala zako mwenyewe. Je, zinaonyesha kwamba unapendezwa sana na Ufalme wa Mungu, kufanya mapenzi yake, na kutakaswa kwa jina lake takatifu? Sala zako zinapaswa kuonyesha hivyo.

      22. Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakupa ujasiri wa kutangaza habari njema?

      22 Kwa sababu ya mateso au majaribu mengine, mara nyingi sala inatia ndani kumsihi Yehova atusaidie kumtumikia kwa ujasiri. Wakati Sanhedrini ilipowaamuru Petro na Yohana waache ‘kufundisha juu ya msingi wa jina la Yesu,’ kwa ujasiri mitume hao walikataa kufanya hivyo. (Mdo. 4:18-20) Baada ya kuachiliwa huru, waliwaeleza waamini wenzao yale yaliyotukia. Kisha, wote walimwomba Mungu awasaidie kusema neno lake kwa ujasiri. Lilikuwa jambo lenye kusisimua kama nini sala hiyo ilipojibiwa, kwa kuwa ‘walijazwa roho takatifu na wakawa wakisema neno la Mungu kwa ujasiri’! (Soma Matendo 4:24-31.) Kwa sababu hiyo, watu wengi wakawa waabudu wa Yehova. Sala inaweza pia kukutia nguvu ili utangaze habari njema kwa ujasiri.

      Endelea Kuboresha Sala Zako

      23, 24. (a) Taja mifano mingine inayoonyesha jinsi funzo la Biblia linavyoweza kuboresha sala zako. (b) Utafanya nini ili uboreshe sala zako?

      23 Tunaweza kutoa mifano mingine mingi inayoonyesha kwamba kusoma Biblia na kujifunza kunaweza kuboresha sala zako. Kwa mfano, katika sala yako unaweza kukiri kama Yona kwamba “wokovu ni wa Yehova.” (Yona 2:1-10) Ikiwa dhamiri inakusumbua kwa sababu ya dhambi nzito na umepata msaada kutoka kwa wazee, maneno ambayo Daudi alisema katika sala yanaweza kukusaidia kuonyesha toba katika sala zako za kibinafsi. (Zab. 51:1-12) Katika sala nyingine, unaweza kumsifu Yehova kama Yeremia alivyofanya. (Yer. 32:16-19) Ikiwa unatafuta mwenzi wa ndoa, kuchunguza sala iliyo katika Ezra sura ya 9 na kusali kibinafsi, kunaweza kutia nguvu azimio lako la kumtii Mungu kwa ‘kuoa katika Bwana tu.’—1 Kor. 7:39; Ezra 9:6, 10-15.

      24 Endelea kusoma, kujifunza, na kuichunguza Biblia. Tafuta mambo unayoweza kutia ndani ya sala zako. Unaweza kutumia mawazo fulani ya Kimaandiko katika dua na sala zako za kumshukuru na kumsifu Mungu. Ukifanya hivyo, bila shaka utamkaribia zaidi Yehova Mungu unapoendelea kuboresha sala zako kupitia funzo la Biblia.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki