Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Habari Njema Wanazotaka Usikie
    Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini?
    • Habari Njema Wanazotaka Usikie

      YESU alipokuwa duniani, wanafunzi wake walimjia wakamwuliza: “Ni nini ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Alijibu kwamba kungekuwako vita kati ya mataifa mengi, njaa, magonjwa ya kipuku, matetemeko ya dunia, kuongezeka kwa uasi, walimu wa kidini wasio wa kweli wanaopoteza wengi, wafuasi wake wa kweli kuchukiwa na kunyanyaswa, na kupoa kwa upendo wa kutaka uadilifu. Wakati ambapo mambo hayo yangeanza kutukia, ingeonyesha Kristo angekuwapo bila kuonekana, na kwamba Ufalme wa mbinguni uko karibu. Hizo zingekuwa habari—habari njema! Hivyo Yesu aliongezea maneno haya kuwa sehemu ya ile ishara: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:3-14.

      Mambo yenyewe ambayo yametukia katika ulimwengu karibuni ni mabaya, lakini kile ambacho yanamaanisha ni chema, yaani, kuwapo kwa Kristo. Mambo hayo yaliyotajwa juu yalianza kutukia mwaka ule uliotangazwa kotekote wa 1914! Ulionyesha mwisho wa Nyakati za Mataifa na mwanzo wa kipindi cha badiliko kutoka utawala wa kibinadamu kuja kwenye Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu (Milenia).

      Zaburi ya 110, mistari 1 na 2, na Ufunuo 12:7-12 zaonyesha kwamba kungekuwapo kipindi cha mabadiliko. Inaonyeshwa humo kwamba Kristo angeketi kwenye mkono wa kulia wa Mungu mbinguni mpaka wakati wa kuwa kwake Mfalme. Ndipo vita mbinguni ingetokeza kufukuzwa kwa Shetani kuja kwenye dunia, kukileta ole duniani, na Kristo angetawala katikati ya maadui wake. Mwisho kamili wa uovu ungekuja kupitia “dhiki kubwa,” ikifikia upeo katika vita ya Har–Magedoni na kufuatwa na Utawala wa amani wa Kristo wa Miaka Elfu.—Mathayo 24:21, 33, 34; Ufunuo 16:14-16.

      “Lakini jua hili,” Biblia yasema, “kwamba katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu, wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakithibitika kuwa si kweli kwa nguvu ya hiyo; na geukia mbali kutoka kwa hawa.”—2 Timotheo 3:1-5.

      Huenda watu fulani wakabisha wakisema kwamba mambo hayo yametukia zamani katika historia ya kibinadamu, lakini ukweli ni kwamba hayajawahi kutukia kwa kadiri hii. Kama wanahistoria na wafafanuzi wanavyosema, haujapata kuwako wakati duniani kama ule ambao umekuwapo tangu mwaka wa 1914 na kuendelea. (Ona ukurasa wa 7.) Ole zimeenea zaidi ya zile zilizotangulia. Isitoshe, kwa habari ya sehemu nyingine za ishara ya Kristo ya siku za mwisho, mambo haya ya hakika yapasa kufikiriwa: Kutangazwa duniani pote kwa kuwapo kwa Kristo na Ufalme kumefanywa kwa kiasi kikubwa sana ambacho hakina kifani katika historia. Kunyanyaswa kwa sababu ya kuhubiri hakujapata kuwa na kifani kamwe kama kule ambako Mashahidi wa Yehova wamepata. Mamia ya Mashahidi waliuawa katika kambi za mateso za Nazi. Mpaka leo hii Mashahidi wa Yehova wamepigwa marufuku katika sehemu fulani-fulani, na katika nyingine wanakamatwa, wanafungwa gerezani, wanateswa, na kuuawa. Yote hayo ni sehemu ya ile ishara ambayo Yesu alitoa.

      Kama ilivyotabiriwa katika Ufunuo 11:18, ‘mataifa wamekuwa na hasira ya kisasi’ dhidi ya Mashahidi waaminifu wa Yehova, na hiyo inaonyesha kwamba “hasira ya kisasi” ya Yehova mwenyewe italetwa juu ya mataifa hayo. Andiko ilo hilo lasema kwamba Mungu ‘atawaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.’ Haujapata kamwe kuwako wakati mwingine wowote katika historia ya kibinadamu ambapo uwezo wa dunia kuendeleza uhai umekaribia kuharibiwa, kama ilivyo leo. Lakini, sasa ni tofauti! Wanasayansi wengi wameonya kwamba iwapo mwanadamu ataendelea kuichafua dunia, itakuwa isiyokalika. Lakini Yehova “aliiumba ili ikaliwe na watu,” naye atawaondoa wachafuzi hao kabla hawajamaliza kuiharibu dunia.—Isaya 45:18.

      BARAKA ZA KIDUNIA CHINI YA UFALME

      Huenda wazo la kwamba watu wataishi duniani wakiwa raia za Ufalme wa Mungu likaonekana kuwa la ajabu kwa waamini wengi wa Biblia wanaodhani kwamba watu wote waliookolewa wako mbinguni. Biblia yaonyesha kwamba ni wachache tu wanaoenda mbinguni na kwamba wale watakaoishi milele duniani watakuwa umati mkubwa usiohesabika. (Zaburi 37:11, 29; Ufunuo 7:9; 14:1-5) Unabii wa kitabu cha Biblia cha Danieli waonyesha kwamba Ufalme wa Mungu mikononi mwa Kristo utajaa duniani na kuitawala.

      Katika kitabu hicho, Ufalme wa Kristo unafananishwa na jiwe lililochongwa kutoka katika enzi kuu ya Yehova iliyo kama mlima. Lapiga na kuharibu sanamu inayofananisha mataifa ya dunia yenye nguvu, ‘nalo jiwe hilo likawa mlima mkubwa, likaijaza dunia yote.’ Unabii huo waendelea hivi: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:34, 35, 44.

      Ufalme huo na lile tumaini linalotegemezwa na Maandiko la uhai wa milele katika dunia iliyosafishwa na kurembwa ndiyo mambo ambayo Mashahidi wa Yehova wanataka kukuambia juu yake. Mamilioni ya watu wanaoishi sasa na mamilioni wengine wengi walio sasa katika makaburi yao watapata fursa ya kukaa humo milele. Ndipo kusudi la awali la Yehova la kuiumba dunia na kuweka ndani yake watu wawili wa kwanza litakapotimizwa, chini ya Utawala wa Kristo Yesu wa Miaka Elfu. Paradiso hiyo ya kidunia haitakuwa yenye kuchosha kamwe. Kama vile Adamu alivyopewa kazi katika bustani ya Edeni, vivyo hivyo jamii ya binadamu itakuwa na mipango itakayohitaji kufikiri kwingi katika kuitunza dunia na mimea na wanyama watakaokuwa juu yake. “Wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”—Isaya 65:22; Mwanzo 2:15.

      Maandiko mengi yangeweza kutolewa kuonyesha hali zitakazokuwako wakati ambapo ile sala ambayo Yesu alitufundisha itakapojibiwa: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:10) Lakini, acheni hili litoshe kwa sasa: “Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’ Na Yeye aketiye juu ya kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’ Pia, husema: ‘Andika, kwa sababu maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.’”—Ufunuo 21:3-5.

  • Njia Wanazotumia Kuhubiri Habari Njema
    Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini?
    • Njia Wanazotumia Kuhubiri Habari Njema

      WAKRISTO wameamriwa ‘wafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ lakini hiyo haimaanishi kwamba wanapaswa kutumia mkazo wala kugeuza imani za wengine kwa nguvu. Utume wa Yesu ulikuwa ‘kuwahubiria wanyenyekevu habari njema,’ “kuwaganga waliovunjika moyo,” “kuwafariji wote waliao.” (Mathayo 28:19; Isaya 61:1, 2; Luka 4:18, 19) Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufanya hivyo kwa kuzitangaza habari njema za Biblia. Kama nabii Ezekieli wa kale, Mashahidi wa Yehova leo hujaribu kutafuta wale “wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika.”—Ezekieli 9:4.

      Njia bora zaidi wanayotumia ili wawaone wale wanaosumbuliwa na hali za sasa ni kwa kwenda nyumba kwa nyumba. Kwa njia hiyo wanajitahidi kihakika wafikie umma, kama vile Yesu alivyofanya alipoanza “kusafiri kutoka jiji hadi jiji na kutoka kijiji hadi kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.” Wanafunzi wake wa mapema walifanya vivyo hivyo. (Luka 8:1; 9:1-6; 10:1-9) Leo, mahali inapowezekana, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kutembelea kila nyumba mara kadhaa kwa mwaka, wakitaka kuzungumza na mwenye nyumba kwa dakika chache juu ya habari fulani ya kwao au ya ulimwengu wote yenye kupendeza au kuhangaisha. Huenda andiko moja au mawili yakatolewa yazungumzwe, na mwenye nyumba akipendezwa, huenda Shahidi akafanya mpango wa kurudi wakati unaofaa ili kuzungumza zaidi. Biblia na vitabu vinavyoeleza juu ya Biblia hutolewa, na mwenye nyumba akitaka, funzo la Biblia la nyumbani huongozwa bila malipo. Mamilioni ya mafunzo hayo ya Biblia yenye kusaidia watu huongozwa kwa ukawaida pamoja na watu mmoja-mmoja na familia ulimwenguni kote.

      Njia nyingine ya kuwaambia wengine “habari njema ya ufalme” ni kupitia mikutano inayofanywa katika Majumba yao ya Ufalme. Mashahidi huongoza mikutano humo kila juma. Mkutano mmoja ni hotuba ya watu wote juu ya habari yenye kupendeza ya karibuni, ukifuatwa na funzo la habari au unabii wa Biblia, kwa kutumia gazeti la Mnara wa Mlinzi kuwa chanzo cha habari. Mkutano mwingine ni shule ya kuzoeza Mashahidi wawe watangazaji bora zaidi wa habari njema, ukifuatwa na sehemu ya kuzungumzia kazi ya kutoa ushahidi katika eneo la kwao. Pia, mara moja kwa juma Mashahidi hukusanyika katika nyumba za faragha, wakiwa vikundi vidogo, ili wajifunze Biblia.

      Watu wote wanakaribishwa kuhudhuria mikutano hiyo yote. Hakuna sadaka zinazokusanywa wakati wowote. Mikutano hiyo hunufaisha watu wote. Biblia yasema hivi: “Na acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.” Funzo la kibinafsi na kufanya utafiti ni mambo ya lazima, lakini kukutana na wengine huchangamsha: “Chuma hunoa chuma; ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake.”—Waebrania 10:24, 25; Mithali 27:17.

      Pia Mashahidi hutumia vizuri fursa za kuzungumza juu ya habari njema wanapokutana na watu wengine katika shughuli zao za kila siku. Huenda ni maneno machache ya kuongea pamoja na jirani au pamoja na msafiri mwingine katika basi au ndege, mazungumzo marefu zaidi pamoja na rafiki au mtu wa ukoo, au mazungumzo pamoja na mfanyakazi mwenzi wakati wa chakula cha mchana. Mwingi wa ushahidi aliotoa Yesu alipokuwa duniani ulikuwa wa aina hiyo—alipokuwa akitembea kando ya bahari, alipokuwa ameketi kando ya kilima, alipokuwa akila chakula nyumbani kwa mtu fulani, wakati wa arusi, au akisafiri katika mashua ya kuvulia samaki katika Bahari ya Galilaya. Alifundisha katika masinagogi na hekaluni Yerusalemu. Popote alipokuwa, alipata nafasi za kuzungumza juu ya Ufalme wa Mungu. Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuzifuata hatua zake kwa njia hiyo pia.—1 Petro 2:21.

      KUHUBIRI KUPITIA MFANO WAO

      Hakuna yoyote ya njia hizo za kukuambia habari njema ingekuwa ya maana kwako ikiwa mwenye kukuambia hafuati mwenyewe mambo anayokufundisha. Kusema jambo moja na kufanya kinyume ni unafiki, na unafiki wa kidini umeondoa mamilioni mbali na Biblia. Biblia hailaumiwi kwa haki. Waandishi na Mafarisayo walikuwa na Maandiko ya Kiebrania, lakini Yesu aliwashutumu vikali kuwa wanafiki. Alisema juu ya kusoma kwao Sheria ya Musa, kisha akaongeza kuwaambia wanafunzi hivi: “Mambo yote wawaambiayo nyinyi, yafanyeni na kuyashika, lakini msifanye kulingana na vitendo vyao, kwa maana wao husema lakini hawafanyi.” (Mathayo 23:3) Mkristo kuwa kielelezo cha maisha mema, husadikisha zaidi kuliko saa nyingi za kuhubiri. Hivyo ndivyo wake Wakristo waliokuwa na waume wasioamini walivyoambiwa hivi: “Wapate kuvutwa bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kuwa mashahidi wa kujionea mwenendo wenu ulio safi kiadili.”—1 Petro 3:1, 2.

      Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova hujaribu kupendekeza habari njema kwa wengine kwa njia hii pia: kwa kuwa vielelezo vyema katika mwenendo wa Kikristo wanaopendekezea wengine. Wao hujaribu ‘kuwatendea wengine kama vile wangetaka hao wawatendee.’ (Mathayo 7:12) Wao hujaribu kuwa hivyo kwa watu wote, si kwa Mashahidi wenzao, marafiki, majirani, au watu wa ukoo wao tu. Kwa vile si wakamilifu, hawafaulu kabisa kabisa nyakati zote kufanya hivyo. Lakini mioyo yao inataka sana kutendea watu wote mema, si kwa kuwaambia habari njema za Ufalme tu, bali pia kwa kutoa msaada iwezekanapo.—Yakobo 2:14-17.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki