-
“Kiongozi Wenu Ni Mmoja, Kristo”Mnara wa Mlinzi—2010 | Septemba 15
-
-
Kristo Anaanzisha Kazi ya Kuhubiri
9, 10. Kristo aliongoza mambo jinsi gani katika kueneza habari njema ya Ufalme?
9 Tangu mwanzoni, Yesu mwenyewe aliongoza kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri na kufundisha. Aliweka utaratibu ambao ungefuatwa katika kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa wakaaji wa dunia. Wakati wa huduma yake, aliwaagiza hivi mitume wake: “Msiende katika barabara ya mataifa, na msiingie katika jiji la Wasamaria; bali, badala ya hivyo, nendeni kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. Mnapoenda, hubirini, mkisema, ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’” (Mt. 10:5-7) Walihubiri ujumbe huo kwa bidii kati ya Wayahudi na watu waliogeuzwa imani, hasa baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.—Mdo. 2:4, 5, 10, 11; 5:42; 6:7.
10 Baadaye, kupitia roho takatifu, Yesu alieneza kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme kwa Wasamaria na kisha kwa watu wengine wasio Wayahudi. (Mdo. 8:5, 6, 14-17; 10:19-22, 44, 45) Akiwa na nia ya kueneza habari njema katikati ya mataifa, Yesu mwenyewe alimchochea Sauli wa Tarso kuwa Mkristo. Yesu alimwagiza hivi mwanafunzi wake Anania: “Ondoka, uende kwenye barabara inayoitwa Nyoofu, na kwenye nyumba ya Yuda tafuta mtu anayeitwa jina Sauli, kutoka Tarso. . . . Ondoka uende, kwa sababu mtu huyu ni chombo kilichochaguliwa kwangu ili kupeleka jina langu kwa mataifa na vilevile kwa wafalme na wana wa Israeli.” (Mdo. 9:3-6, 10, 11, 15) “Mtu huyu” alikuja kuwa mtume Paulo.—1 Tim. 2:7.
11. Kristo alipanua jinsi gani kazi ya kuhubiri akitumia roho takatifu?
11 Wakati ulipofika wa kupanua kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme katikati ya mataifa yasiyo ya Kiyahudi, Paulo alipata mwongozo kutoka mbinguni wa kwenda katika Asia Ndogo na Ulaya kwa ajili ya safari za umishonari. Simulizi la Luka katika Matendo linasema hivi: “Walipokuwa [manabii na walimu Wakristo katika kutaniko la Antiokia ya Siria] wakimhudumia Yehova hadharani na kufunga, roho takatifu ikasema: ‘Kati ya watu wote wekeni kando Barnaba na Sauli kwa ajili yangu kwa kazi ambayo nimewaitia wao.’ Ndipo wakafunga na kusali na kuweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.” (Mdo. 13:2, 3) Yesu mwenyewe alimwita Sauli wa Tarso kuwa “chombo [Chake] kilichochaguliwa” ili kulipeleka jina Lake kwa mataifa; hivyo, nguvu hiyo mpya kwa kazi ya kutoa ushahidi ilitoka kwa Kristo, ambaye ni Kiongozi wa kutaniko. Wakati wa safari ya pili ya Paulo ya umishonari ilikuwa wazi kwamba Yesu alikuwa akitumia roho takatifu ili kuongoza kazi ya kuhubiri. Simulizi hilo linasema kwamba “roho ya Yesu,” yaani, Yesu alimwongoza Paulo na wasafiri wenzake kupitia roho takatifu, kuamua wakati na mahali ambapo wangeenda, na walipata maono ambayo yaliwaelekeza Ulaya.—Soma Matendo 16:6-10.
-
-
“Kiongozi Wenu Ni Mmoja, Kristo”Mnara wa Mlinzi—2010 | Septemba 15
-
-
15 Kupitia roho takatifu, mwishowe Yesu angepanua kazi ya kutoa ushahidi mpaka kwenye miisho ya dunia. Kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8; soma 1 Petro 1:12.) Chini ya mwongozo wa Kristo, ushahidi mkubwa ulitolewa katika karne ya kwanza.—Kol. 1:23.
16 Lakini Yesu mwenyewe alionyesha kwamba kazi hiyo ingeendelea mpaka wakati wa mwisho. Baada ya kuwaamuru wafuasi wake wahubiri na kufanya wanafunzi kutoka katika mataifa yote, Yesu aliwaahidi hivi: “Mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20)
-