Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Biblia Inabadili Maisha
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Julai 1
    • “Nimekuwa Nikimtafuta Mungu Tangu Utotoni.”—SHINJI SATO

      MWAKA WA KUZALIWA: 1951

      NCHI: JAPANI

      HISTORIA: KUHANI WA DINI YA SHINTO

      MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika mji fulani wa mashambani katika Wilaya ya Fukuoka. Wazazi wangu walikuwa watu wa kidini sana, na tangu utotoni walinifundisha kuiheshimu miungu ya Shinto. Nikiwa mvulana mdogo, mara nyingi nilitafakari kuhusu wokovu wangu na nilikuwa na tamaa kubwa ya kuwasaidia watu wenye shida. Ninakumbuka wakati fulani nilipokuwa katika shule ya msingi, mwalimu alituuliza tungependa kufanya kazi gani tutakapokuwa watu wazima. Wanafunzi wenzangu walitaja mambo makubwa, kama vile kuwa wanasayansi. Lakini mimi nikasema kwamba ningependa kuwa mtumishi wa Mungu. Wote walinicheka.

      Baada ya kumaliza shule ya sekondari, nilijiunga na shule ya walimu wa dini. Katika shule hiyo, nilikutana na kuhani wa dini ya Shinto ambaye alitumia muda wake wa ziada kusoma kitabu fulani chenye jalada jeusi. Siku moja aliniuliza, “Sato, unajua hiki ni kitabu gani?” Nilikuwa nimeona jalada la kitabu hicho hivyo nikamjibu, “Biblia.” Naye akaniambia, “Yeyote anayetaka kuwa kuhani wa dini ya Shinto, anapaswa kusoma kitabu hiki.”

      Niliondoka mara moja na kwenda kununua Biblia. Niliiweka mahali pa pekee kwenye rafu ya vitabu na kuitunza sana. Hata hivyo, sikupata nafasi ya kuisoma, kwa sababu tulikuwa na mambo mengi sana ya kufanya shuleni. Nilipomaliza shule, nilianza kufanya kazi katika hekalu nikiwa kuhani wa dini ya Shinto. Ndoto yangu ya tangu utotoni ilikuwa imetimia.

      Hata hivyo, mambo hayakwenda kama nilivyotarajia kabla ya kuwa kuhani wa dini ya Shinto. Makuhani wengi hawakuwajali wala kuwapenda watu wengine. Pia, wengi wao hawakuwa na imani. Hata mmoja wa wasimamizi wangu aliniambia hivi: “Ikiwa unataka kufanikiwa hapa, unapaswa tu kuzungumzia mambo ya falsafa. Ni marufuku kuzungumza kuhusu imani.”

      Maneno hayo yalinivunja moyo kuhusiana na dini ya Shinto. Hata ingawa niliendelea kufanya kazi katika hekalu hilo, nilianza kuchunguza dini nyingine. Lakini hakuna yoyote iliyoonekana kuwa nzuri. Kadiri nilivyoendelea kuchunguza dini, ndivyo nilivyozidi kuvunjika moyo. Niliona kwamba dini zote hazina ukweli.

      JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mnamo 1988, nilikutana na Mbudha ambaye alinitia moyo nisome Biblia. Nilimkumbuka yule kuhani wa dini ya Shinto, ambaye miaka mingi awali alinitia moyo nifanye jambo hilohilo. Niliamua kutumia shauri hilo. Nilipoanza kusoma Biblia, ilinivutia sana. Nyakati nyingine ningeisoma usiku kucha.

      Yale niliyosoma yalinichochea nitamani kusali kwa Mungu wa Biblia. Nilianza na sala ya kielelezo inayopatikana katika Mathayo 6:9-13. Niliirudia-rudia kila baada ya saa mbili hata nilipokuwa nikiendesha ibada katika hekalu la Shinto.

      Nilikuwa na maswali mengi kuhusu yale niliyokuwa nikisoma. Kufikia wakati huo, nilikuwa nimeoa, na nilijua kuwa Mashahidi wa Yehova wanawafundisha watu Biblia kwa sababu walikuwa wamewahi kumtembelea mke wangu. Nilimtafuta Shahidi mmoja na kumuuliza maswali mengi. Nilivutiwa sana alipotumia Biblia kujibu maswali hayo yote. Alifanya mpango ili mwanamume mmoja Shahidi ajifunze Biblia pamoja nami.

      Muda mfupi baadaye, nilianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Wakati huo, sikutambua kwamba miongoni mwao kulikuwa na watu niliowatendea kwa ukali zamani. Hata hivyo, walinisalimia kwa uchangamfu na kunifanya nihisi nimekaribishwa.

      Katika mikutano hiyo, nilijifunza kwamba Mungu anatarajia waume wawapende na kuwaheshimu watu wao wa familia. Kufikia wakati huo, nilikuwa nimejishughulisha sana na kazi yangu ya ukuhani hivi kwamba nilimpuuza mke wangu na watoto wetu wawili. Nilianza kutambua kwamba nilikuwa nikiwasikiliza kwa makini watu waliokuja kuabudu kwenye hekalu, lakini sikuwa nimewahi kumsikiliza mke wangu hata siku moja.

      Nilipoendelea kujifunza, nilielewa mambo mengi kumhusu Yehova ambayo yalinivuta kwake. Nilivutiwa hasa na andiko la Waroma 10:13, linalosema: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” Nilikuwa nikimtafuta Mungu tangu utotoni, lakini sasa hatimaye nilikuwa nimempata!

      Nilianza kuhisi kuwa sikustahili tena kuwa hekaluni. Mwanzoni, nilikuwa na wasiwasi kuhusu jinsi ambavyo wengine wangeniona ikiwa ningeacha dini ya Shinto. Lakini nilikuwa nimeazimia kuiacha ikiwa ningemjua Mungu wa kweli. Hivyo, mnamo 1989, niliamua kutii dhamiri yangu. Niliacha kuhudumu hekaluni na kujikabidhi mikononi mwa Yehova.

      Haikuwa rahisi kuacha kazi yangu hekaluni. Wasimamizi wangu walinikemea na kujaribu kunilazimisha niendelee na kazi hiyo. Ilikuwa vigumu hata zaidi kuwaambia wazazi wangu kuhusu jambo hilo. Nilipokuwa njiani kwenda nyumbani kwa wazazi, nilikuwa na wasiwasi mwingi sana hivi kwamba niliumwa na kifua na miguu yangu ikakosa nguvu! Nilisimama mara nyingi njiani, nikisali kwa Yehova anipe nguvu.

      Nilipofika kwa wazazi wangu, sikuweza kuwaambia mara moja kilichonipeleka kwa kuwa niliogopa sana. Saa kadhaa zilipita. Mwishowe, baada ya kusali sana, nilimweleza baba yangu kila kitu. Nilimweleza kwamba nimempata Mungu wa kweli na kwamba nilikuwa nimeamua kuacha dini ya Shinto ili niweze kumtumikia. Baba yangu alishtuka na kuhuzunika. Watu wengine wa ukoo walikuja na kujaribu kunishawishi nibadili maoni yangu. Sikutaka kuiumiza familia yangu, lakini wakati huohuo, nilijua kwamba kumtumikia Yehova ndilo jambo linalofaa. Baada ya muda, familia yangu ilianza kuniheshimu kwa uamuzi niliofanya.

      Ingawa nilikuwa nimeondoka hekaluni kihalisi, bado nilikuwa nikiwaza sana kuhusu kazi yangu huko. Maisha ya ukuhani yalikuwa yametia mizizi sana ndani yangu. Nilijitahidi sana kuyasahau, lakini ilikuwa kana kwamba kila kitu kilichokuwa nyumbani mwetu kilinikumbusha maisha hayo ya zamani.

      Kuna mambo mawili yaliyonisaidia kukabiliana na hali hiyo. Kwanza, niliipekua nyumba yangu kwa makini ili kuondoa chochote kilichohusiana na dini yangu ya zamani. Halafu nikateketeza kila kitu—vitabu, picha, na hata vitu vya ukumbusho vyenye thamani. Pili, nilitumia wakati mwingi iwezekanavyo pamoja na Mashahidi. Urafiki na utegemezo wao ulinisaidia sana. Kisha, hatua kwa hatua, nikasahau maisha yangu ya zamani.

      JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nilikuwa nikimpuuza mke wangu na watoto wetu, jambo lililowafanya wajihisi wapweke sana. Lakini nilipoanza kutumia wakati pamoja nao, kama vile Biblia inavyowafundisha waume kufanya, uhusiano wetu ukawa mzuri. Baada ya muda, mke wangu alijiunga nami katika kumtumikia Yehova. Sasa mimi na mke wangu, mwana wetu, binti yetu, na mume wake, tumeungana pamoja katika ibada ya kweli.

      Ninapotafakari kuhusu ndoto yangu ya tangu utotoni ya kumtumikia Mungu na kuwasaidia wengine, ninatambua kwamba nimepata yote niliyokuwa nikitafuta—na hata zaidi. Sina maneno ya kueleza shukrani zangu kwa Yehova.

  • Biblia Inabadili Maisha
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Julai 1
    • [Picha katika ukurasa wa 13]

      Zamani niliabudu katika hekalu hili la Shinto

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki