-
Mfalme na Wakuu WakeUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Kutawala kwa Uadilifu na Haki
3. Ni utawala gani unaotabiriwa katika kitabu cha Isaya na cha Ufunuo?
3 Isaya sura ya 32 inaanza kwa unabii wenye kusisimua ambao unatimizwa kwa njia ya pekee leo: “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki [“uadilifu,” “BHN”], na wakuu watatawala kwa hukumu [“haki,” “BHN”].” (Isaya 32:1) Naam, “Tazama”! Neno hilo latukumbusha neno kama hilo lililo kwenye kitabu cha mwisho cha unabii katika Biblia: “Yeye aketiye juu ya kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’” (Ufunuo 21:5) Kitabu cha Isaya kiliandikwa miaka ipatayo 900 kabla ya kuandikwa kwa kitabu cha Ufunuo. Vitabu vyote hivyo viwili vya Biblia vyafafanua vizuri utawala mpya—“mbingu mpya,” inayojumuisha Mfalme, Kristo Yesu, aliyetawazwa mbinguni mwaka wa 1914, na watawala-wenzi 144,000 ‘walionunuliwa kutoka miongoni mwa wanadamu’—pamoja na “dunia mpya,” familia ya kibinadamu iliyoungana duniani kote.a (Ufunuo 14:1-4; 21:1-4; Isaya 65:17-25) Dhabihu ya fidia ya Kristo ndiyo inayofanya mpango huo wote uwezekane.
4. Ni kiini gani cha dunia mpya kilichopo sasa?
4 Baada ya kuona katika maono kutiwa muhuri kwa mwisho kwa watawala-wenzi hao 144,000, mtume Yohana aripoti hivi: “Nikaona, na, tazama! umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha, wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo.” Hicho ndicho kiini cha dunia mpya—umati mkubwa ambao hesabu yake ni mamilioni, ambao wamekusanywa upande wa mabaki wachache kati ya wale 144,000 ambao wengi wao wamezeeka. Umati huo mkubwa utaokoka dhiki kubwa inayokaribia haraka halafu waaminifu waliofufuliwa na mabilioni ya wengine watakaopewa nafasi ya kudhihirisha imani watajiunga nao katika dunia Paradiso. Wote watakaodhihirisha imani hiyo watapewa baraka ya uhai udumuo milele.—Ufunuo 7:4, 9-17.
5-7. “Wakuu” waliotabiriwa wanatimiza wajibu gani katika kundi la Mungu?
5 Hata hivyo, maadamu ulimwengu wa sasa uliojaa chuki upo, washiriki wa umati mkubwa wahitaji ulinzi. Kwa jumla, “wakuu” ‘wanaotawala kwa haki,’ ndio wanaotoa ulinzi huo. Huo ni mpango bora kama nini! “Wakuu” hao wanafafanuliwa zaidi kwa maneno mazuri ya unabii wa Isaya: “Mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.”—Isaya 32:2.
6 Hivi sasa katika wakati huu wa taabu ya ulimwenguni kote, kuna uhitaji wa “wakuu,” yaani, wazee ‘wanaokazia uangalifu kwa kundi lote,’ wakitunza kondoo za Yehova na kutekeleza haki kupatana na kanuni za Yehova za uadilifu. (Matendo 20:28) Ni lazima “wakuu” hao wawe na sifa zilizo katika 1 Timotheo 3:2-7 na Tito 1:6-9.
7 Katika unabii wake mkubwa unaoeleza “umalizio wa mfumo wa mambo” wenye kujaa taabu, Yesu alisema: “Angalieni kwamba hamwogofishwi.” (Mathayo 24:3-8) Sababu gani hali hatari za ulimwengu wa leo haziwaogofishi wafuasi wa Yesu? Sababu moja ni kwamba “wakuu”—iwe ni watiwa-mafuta au “kondoo wengine”—wanalinda kundi kwa uaminifu-mshikamanifu. (Yohana 10:16) Wao huwatunza ndugu na dada zao bila woga, hata wanapokabiliwa na vitisho kama vita vya ukabila na maangamizi ya jamii nzima-nzima. Katika ulimwengu wenye njaa ya kiroho, wao huhakikisha kwamba nafsi zilizoshuka moyo zimefarijiwa kupitia kweli zinazojenga za Neno la Mungu, Biblia.
8. Ni kwa njia gani Yehova anawazoeza na kuwatumia “wakuu” ambao ni sehemu ya kondoo wengine?
8 Kwa miaka 50 iliyopita, “wakuu” hao wameonekana waziwazi. “Wakuu” walio sehemu ya kondoo wengine wanazoezwa wakiwa jamii ya “mkuu” inayozidi kukua ili baada ya dhiki kubwa, watu wanaostahili miongoni mwao wawe tayari kuteuliwa kutumikia wakiwa wasimamizi katika “dunia mpya.” (Ezekieli 44:2, 3; 2 Petro 3:13) Kwa kuandaa mwelekezo na burudisho la kiroho waongozapo katika utumishi wa Ufalme, wanajithibitisha wenyewe kuwa “kama kivuli cha mwamba mkubwa,” wakililetea kundi kitulizo katika eneo lake la ibada.b
9. Ni hali gani zinazoonyesha kwamba kuna uhitaji wa “wakuu” leo?
9 Katika siku hizi za mwisho zenye hatari za ulimwengu wa Shetani, Wakristo waliojiweka wakfu wahitaji sana ulinzi huo. (2 Timotheo 3:1-5, 13) Pepo kali za mafundisho yasiyo ya kweli na propaganda iliyopotoka zinavuma. Vita mithili ya dhoruba vinaendelea kati ya mataifa na ndani ya mataifa na vilevile kuna mashambulizi ya moja kwa moja dhidi ya waabudu waaminifu wa Yehova Mungu. Katika ulimwengu uliokaushwa na ukame wa kiroho, Wakristo wanahitaji sana vijito vya maji safi ya kweli yasiyoghushiwa ili wakate kiu yao ya kiroho. Yafurahisha kwamba Yehova ameahidi kwamba Mfalme wake anayetawala, kupitia ndugu zake watiwa-mafuta na “wakuu” wanaowasaidia kati ya kondoo wengine, ataandaa kitia-moyo na mwelekezo kwa watu walioshuka na kuvunjika moyo katika kipindi hiki chenye uhitaji. Hivyo basi, Yehova atahakikisha kuwa mambo ya uadilifu na ya haki yamedumu.
-
-
Mfalme na Wakuu WakeUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
[Picha katika ukurasa wa 333]
Kila ‘mkuu’ ni kama mahali pa kujificha na upepo, mahali pa kujisitiri na dhoruba, maji mahali pakavu, na kivuli cha kujikinga na jua
-