Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • “ACHA HAR-MAGEDONI IJE!”

      Ndugu na dada wengi walitumikia vifungo virefu gerezani. Grigory Gatilov alitumikia miaka 15 gerezani naye anakumbuka hivi: “Gereza la mwisho nililofungwa lilikuwa na jina la kupendeza: Liliitwa Bata-Maji Mweupe. Gereza hilo lilikuwa katika eneo linalopendeza huko Caucasus juu ya moja kati ya milima mitano iliyo karibu na mji wa kitalii wa Pyatigorsk. Katika gereza hilo, nilipata nafasi kuwahubiria watu mbalimbali mwaka mzima. Seli yangu ilikuwa ‘eneo’ zuri la kuhubiri na sikuhitaji kwenda popote. Askari wa gereza waliwaleta watu wapya kwenye seli yangu na kuwahamisha baada ya siku kadhaa lakini mimi nilibaki. Ni mara chache sana nilihamishiwa katika seli nyingine. Nilijaribu kumhubiria kila mtu kuhusu Ufalme wa Yehova. Watu wengi walikuwa na maswali kuhusu Har–Magedoni. Wafungwa fulani walishangaa kwamba mtu anaweza kufungwa kifungo kirefu hivyo kwa sababu ya imani yake. ‘Kwa nini usikane imani yako na kwenda nyumbani?’ waliuliza wafungwa wenzangu na mara nyingine hata askari wa gereza. Nilifurahi sana kila wakati mtu fulani alipopendezwa na kweli. Wakati mmoja mtu fulani aliandika kwenye kuta za seli, ‘Acha Har–Magedoni ije!’ Ingawa maisha ya gerezani hayakuwa yenye kufurahisha, nilifurahi kwamba niliweza kuzungumza kuhusu kweli.”

      “JE, KUNA WAYONADABU KATI YENU?”

      Dada wengi Wakristo wenye bidii katika utumishi wa Yehova walifungwa gerezani pia. (Zab. 68:11) Zinaida Kozyreva anakumbuka jinsi akina dada walivyokuwa na upendo kati yao na kuelekea wafungwa wengine: “Mnamo 1959, muda usiozidi mwaka mmoja tangu nilipobatizwa, mimi, Vera Mikhailova, na Lyudmila Yevstafyeva, tulipelekwa kwenye kambi huko Kemerovo, Siberia. Kambi hiyo ilikuwa na wafungwa 550. Tulipofika tulikuta wanawake kadhaa wamesimama kwenye lango.

      “Wakauliza hivi: ‘Je, kuna Wayonadabu kati yenu?’

      “Tuligundua kwamba hao walikuwa dada zetu wapendwa. Mara moja walitupa chakula na kutuuliza maswali. Nyuso zao zilionyesha uchangamfu na upendo wa kweli, jambo ambalo sikuwa nimeliona katika familia yangu. Kwa kuwa walijua kwamba sisi ni wageni kambini, dada hao walitutegemeza. (Mt. 28:20) Baada ya muda mfupi tulitambua kwamba mambo ya kiroho yalikuwa yamepangwa vizuri katika kambi hiyo.

      “Tukawa kama familia ya kweli. Tulifurahia hasa kipindi cha kiangazi tulipokuwa tukikata nyasi kavu. Wasimamizi wa kambi hawakuwa na hofu kwamba tungetoroka au kuvunja sheria za kambi. Askari mmoja angewalinda dada 20 au 25, ingawa kwa kweli, sisi ndio tuliomlinda! Mtu alipokaribia tungemwamsha ili asiadhibiwe kwa kulala kazini. Alipokuwa amelala, tulizungumzia mambo ya kiroho katika kipindi cha mapumziko. Mpango huo ulikuwa mzuri kwetu na kwake pia.

      “Mwishoni mwa mwaka wa 1959, mimi na dada wengine tulipelekwa katika kambi yenye ulinzi mkali. Tulifungiwa kwenye seli yenye baridi ambayo haikuwa na kioo kwenye dirisha. Usiku tulilala kwenye mbao na mchana tulifanya kazi. Wenye mamlaka walitupa kazi ya kuchambua mboga huku wakichunguza tabia zetu. Punde si punde walipoona kwamba hatukuiba kama wafungwa wengine, walituletea nyasi za kulalia na wakaweka kioo kwenye dirisha. Tulikaa kwenye kambi hiyo kwa mwaka mmoja kisha akina dada wote tulihamishiwa kwenye kambi isiyo na ulinzi mkali huko Irkutsk.

      “Kambi hiyo ilikuwa na dada 120 hivi. Tulikaa humo kwa mwaka mmoja na miezi mitatu. Majira ya baridi ya kwanza tukiwa huko yalikuwa na baridi kali na theluji nyingi. Tulifanya kazi ngumu katika kiwanda cha mbao. Wanyapara walitupekua mara nyingi wakitafuta vichapo. Ni kama hawakuwa na jambo lingine la kufanya. Tulikuwa na ustadi wa kuficha vichapo hivi kwamba hata nyakati nyingine tulisahau mahali tulipoviweka. Pindi mmoja, mimi na Vera tulificha vikaratasi vilivyokuwa na andiko la siku kwenye makoti yetu ya kazi hivi kwamba sisi wenyewe hatungeweza kuvipata. Lakini mnyapara alivipata na tukafungwa kifungo cha upweke kwa siku tano. Nje kulikuwa na baridi ya nyuzi 40 selsiasi chini ya sufuri na barafu ilifunika kuta za seli hiyo ambayo haikuwa na mfumo wa kupashia joto.

      “Kulikuwa na mabenchi yaliyotengenezwa kwa saruji ambayo mtu angeweza kukalia. Tulipohisi baridi sana, tulikunja miguu yetu ukutani tukaketi migongo yetu ikiwa imeshikana na tukalala tukiwa hivyo. Tulipoamka ghafula tulisimama haraka tukihofia kuganda hadi kufa tukiwa tumelala. Tulipewa glasi yenye maji moto na mkate mweusi wa gramu 300 kila siku. Licha ya hayo tulikuwa na furaha kwa kuwa Yehova alitupa ‘nguvu zinazopita zile za kawaida.’ (2 Kor. 4:7) Akina dada walitutendea kwa fadhili tuliporudi kambini. Walitupikia chakula na kutupashia maji moto ili tuweze kuoga.”

      “ANAWEZA KUISHI NA WENGINE KWA AMANI”

      Zinaida anaendelea kusema hivi: “Ilikuwa vigumu kuhubiri kwenye kambi hiyo kwa sababu kulikuwa na wafungwa wachache na kila mtu aliwajua Mashahidi. Kanuni inayopatikana kwenye 1 Petro 3:1 ilifaa katika hali hiyo. Tuliiita kuhubiri pasipo maneno. Tuliweka kambi yetu ikiwa safi na nadhifu na tulikuwa wenye urafiki na tulishirikiana kwa ukaribu na dada zetu. (Yohana 13:34, 35) Isitoshe tulikuwa na uhusiano mzuri na wafungwa wengine ambao hawakuwa Mashahidi. Tulijitahidi kujiendesha kulingana na Neno la Mungu na tuliwajali wengine. Nyakati nyingine tuliwasaidia kwa njia mbalimbali watu ambao si Mashahidi. Kwa mfano, dada mmoja aliwasaidia wafungwa wengine kufanya hesabu ilipohitajika. Watu wengi walitambua kuwa Mashahidi walikuwa tofauti na watu wa dini nyingine.

      “Mnamo 1962, tulihamishwa kutoka kambi ya Irkutsk na kupelekwa hadi kambi moja huko Mordvinia. Tukiwa huko tulijaribu pia kuwa safi na nadhifu. Vitanda vyetu vilikuwa safi na nadhifu kila wakati. Kambi hiyo ilikuwa na wafungwa 50 hivi, wengi wao wakiwa dada zetu. Dada zetu ndio waliofanya kazi ya usafi kwa kuwa wafungwa wengine hawakuipenda kazi hiyo. Sakafu za kambi hiyo zilisafishwa na kusuguliwa kila mara, na wasimamizi wa kambi walitupa vifaa tulivyohitaji. Kulikuwa na watawa wa kike na watu wenye elimu kambini lakini walikataa kufanya kazi hiyo. Kwa hiyo usafi wa kambi ulitegemea jitihada zetu. Kila mara mmoja wa dada zetu alipoachiliwa huru, ripoti kuhusu tabia yake ilisema kwamba yeye ‘anaweza kubadilikana kulingana na hali na anaweza kuishi na wengine kwa amani.’”

      MAUA MAREFU YANAKUWA MAHALI PA KUJIFICHA

      Zinaida anasema hivi: “Wakati mmoja, dada kadhaa waliziandikia familia zao barua wakiomba mbegu za mimea inayochanua maua makubwa. Tuliwaambia wasimamizi wa kambi kwamba tulitaka kupanda maua maridadi na kuomba tupewe udongo mweusi wenye rutuba kwa kusudi hilo. Tulishangaa walipokubali mara moja. Tulipanda maua ndani ya kambi na kwenye vijia vya kambi hiyo. Muda si muda kambi hiyo ilikuwa na vichaka virefu vya maua ya waridi na maua mengine maridadi na marefu. Bustani iliyokuwa katikati ya kambi ilikuwa na maua maridadi ya dalia na vichaka virefu vya maua ya daisy yenye rangi mbalimbali. Tulitembea huko, tukajifunza Biblia nyuma ya maua na kuficha vichapo vyetu katika vichaka vya waridi.

      “Tulifanya mikutano yetu tulipokuwa tukitembea. Tulijigawa katika vikundi vya watu watano. Kila mmoja wa akina dada alikariri mapema fungu moja kati ya mafungu matano kutoka katika kichapo kinachozungumzia Biblia. Kisha baada ya kufungua kwa sala, tungerudia mafungu tuliyokariri na kuyazungumzia. Baada ya kumaliza kwa sala, tuliendelea na matembezi yetu. Magazeti yetu ya Mnara wa Mlinzi yalikuwa vijitabu vidogo [kama picha inayoonyeshwa kwenye ukurasa wa 161]. Kila siku tulijifunza jambo fulani, hasa andiko la siku na kukariri mafungu katika mikutano yetu ambayo tulifanya mara tatu kwa juma. Na si hayo tu, tulijitahidi kukariri sura nzima-nzima za Biblia na kuzirudia ili kutiana nguvu. Kwa njia hiyo hatukuathirika sana vichapo vyetu vilipotwaliwa wakati wa msako.

      “Ingawa wasimamizi wa kambi walijaribu kuwauliza wafungwa wengine jinsi ambavyo utendaji wetu ulivyokuwa ukiendeshwa kambini, wafungwa wengi walishirikiana nasi. Kwenye kambi hiyo tulifungwa pamoja na Olga Ivinskaya, ambaye alikuwa rafiki ya mtunga-mashairi na mwandishi maarufu Boris Pasternak, aliyepokea Tuzo la Nobeli kwa vitabu vyake. Olga Ivinskaya, alikuwa mwandishi na kwa kuwa aliwapenda Mashahidi alifurahia kuona jinsi utendaji wao ulivyoendeshwa kambini. Yehova alitupa hekima hasa ili tuweze kuwa na chakula cha kiroho kambini.”—Yak. 3:17.

      “IMETOSHA!”

      “Tulipata vichapo katika njia mbalimbali,” Zinaida anaendelea kusema. “Ilikuwa wazi kwamba Yehova mwenyewe alikuwa akisimamia utendaji huo kwa kuwa alikuwa ametuahidi: ‘Sitawaacha wala kuwatupa hata kidogo.’ (Ebr. 13:5) Wakati mwingine aliwapofusha walinzi. Pindi moja wakati wa majira ya baridi kali, kikundi chetu kilipokuwa kikiingia kambini baada ya kazi, walinzi walitupekua kama kawaida wakituamuru tutoe nguo zote. Niliingia mwisho nikiwa nimebeba vichapo vipya ndani ya suruali mbili nilizovaa.

      “Kwa sababu kulikuwa na baridi, nilikuwa nimevaa nguo nyingi sana. Kwanza, mnyapara wa kike alipekua koti langu la baridi, kisha koti lisilo na mikono ambalo nilivaa ndani yake. Niliamua kuvua nguo hizo polepole nikitumaini kwamba atachoka. Taratibu nikatoa sweta moja, kisha nyingine. Alipokuwa akizipekua nguo hizo kwa uangalifu, nilitoa skafu kadhaa taratibu, kisha nikatoa vesti, kisha shati moja, halafu nyingine. Nilibaki na suruali mbili na viatu vya manyoya. Polepole nilivua kiatu kimoja kisha kingine, halafu nikaanza kutoa suruali ya nje. Kisha nikajiuliza: ‘Nitafanya nini sasa? Akiniambia nivue suruali hii iliyobaki, nitakimbia na kuwatupia akina dada vichapo.’ Nilipomaliza kutoa tu suruali ya nje, mwanamke huyo aliniambia hivi akiwa amekasirika: ‘Imetosha! Toka hapa!’ Mara moja nikavaa nguo zangu na kukimbilia kambini.

      “Tulipata wapi vichapo hivyo? Akina ndugu waliviacha mahali fulani tulipokubaliana mapema, nasi tulivichukua kwa zamu na kuviingiza kambini. Vilipoingia kambini, tulivificha mahali salama, na mara kwa mara tulibadili mahali hapo. Pia tulikuwa tukinakili vichapo kwa mkono na kuficha nakala hizo. Tulinakili vichapo hivyo tukiwa tumejifunika blanketi tukitumia mwangaza kutoka kwenye taa ya barabarani ulioingia kupitia dirishani na kupenya kwenye matundu madogo ya blanketi. Sikuzote, tulikuwa na shughuli nyingi ili tusipoteze wakati. Kila tulipokuwa tukienda kwenye chumba cha kulia chakula, sote tulibeba karatasi zenye andiko fulani.”

  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Niliachwa Nikiwa Shahidi Pekee Kambini

      KONSTANTIN SKRIPCHUK

      ALIZALIWA 1922

      ALIBATIZWA 1956

      MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alijifunza kweli mnamo 1953 katika kambi ya kazi ngumu na akabatizwa humo mnamo 1956. Alifungwa kwa miaka 25 mfululizo kwa sababu ya kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alikufa mnamo 2003.

      NILIKUTANA na ndugu anayeitwa Vasily mapema katika mwaka wa 1953 katika seli. Alisema alikuwa amefungwa kwa sababu ya imani yake katika Mungu. Sikuelewa mtu angefungwa jinsi gani kwa sababu ya imani yake. Jambo hilo lilinisumbua sana hivi kwamba singeweza kulala. Siku iliyofuata alinieleza zaidi kuhusu jambo hilo. Hatua kwa hatua, nikasadiki kwamba Biblia ni kitabu kutoka kwa Mungu.

      Nilibatizwa mnamo 1956. Mwishoni mwa mwaka huo, wanyapara walitupekua na kupata vichapo vingi vya Biblia. Uchunguzi uliendelea kwa karibu mwaka mmoja, na mnamo 1958 mahakama ilinihukumu kifungo cha miaka 23 kwa ajili ya utendaji wa kidini. Kufikia wakati huo, tayari nilikuwa nimefungwa kwa miaka mitano na nusu katika kambi. Muda wa miaka 28 na miezi 6 ulipita nikiwa gerezani bila hata kuonja uhuru.

      Mnamo Aprili 1962, mahakama ilinitangaza kuwa “mhalifu hatari sana,” nami nikahamishwa kwenye gereza lenye ulinzi mkali, ambako nilifungwa kwa miaka 11. Kuna mambo mengi ambayo yalifanya kambi kama hiyo iwe “ya pekee.” Kwa mfano, chakula ambacho mtu alipewa kwa siku kilikuwa cha pesa chache sana (kopeck 11), pesa ambazo hazikutosha hata kununua mkate mmoja wakati huo. Nikiwa na kimo cha sentimita 192, nilikuwa na uzani wa kilo 59 tu. Ngozi yangu ilikuwa inabambuka.

      Kwa kuwa nilikuwa mjenzi stadi, mara nyingi nilitumwa kurekebisha nyumba za maofisa. Hakuna mtu aliyeniogopa, na watu walioishi humo hawakushughulika kuficha vitu katika nyumba zao. Mke wa ofisa mmoja alipojua kwamba ningefanya kazi katika nyumba yao, hakumpeleka mtoto wake mwenye umri wa miaka sita kwenye shule ya nasari. Lilikuwa jambo la kushangaza: “mhalifu hatari sana” alikuwa ameachwa peke yake ndani ya nyumba na mtoto mwenye umri wa miaka sita! Ilikuwa wazi kwamba hakuna mtu aliyeamini eti mimi ni mhalifu, na isitoshe, eti mhalifu “hatari sana.”

      Hatua kwa hatua, akina ndugu wote kambini waliachiliwa. Mnamo 1974, mimi ndiye niliyekuwa Shahidi pekee kambini. Nilikaa humo kwa miaka mingine saba hadi nilipoachiliwa mnamo Agosti 1981. Yehova aliendelea kunitegemeza kiroho. Jinsi gani? Kwa miaka hiyo saba, nilipokea Mnara wa Mlinzi katika barua. Ndugu mmoja alinitumia barua hizo kwa ukawaida akiwa ameandika makala za kila toleo jipya kwa mkono. Kila wakati, ofisa aliyewekwa kambini kuzuia vitu visiingie alinipa barua hizo zikiwa tayari zimefunguliwa. Mimi na yeye tulijua ujumbe uliokuwa katika barua hizo. Hadi leo, sina uhakika ni nini kilichomchochea ajihatarishe hivyo, lakini ninafurahi kwamba alifanya kazi hapo kwa miaka yote saba. Zaidi ya yote, ninamshukuru Yehova. Katika miaka hiyo yote, nilijifunza kumtegemea Yehova na nikapata nguvu kutoka kwake.—1 Pet. 5:7.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki