-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
“Hakimu alitangaza kwamba Biblia na vichapo vilivyokuwa vimepatikana nyumbani kwetu vilikuwa ‘vinapinga Usovieti.’ Nilifurahi kwamba zaidi tu ya mimi na mume wangu kushtakiwa kuwa tunapinga Usovieti, mashtaka hayo yalihusu pia vichapo vyetu na Biblia! Tuliulizwa jinsi tulivyokutana na Mashahidi wa Yehova. Tuliposema tulikutana nao katika kambi huko Vorkuta, hakimu huyo alisema hivi kwa sauti, ‘Hebu oneni mambo yanayoendelea katika kambi zetu!’ Sote tulihukumiwa kifungo cha miaka kumi katika kambi za kazi ngumu.
“Pyotr alipelekwa kwenye kambi iliyoko Mordvinia, huko Urusi katikati. Nami nikawekwa katika kifungo cha upweke. Mnamo Machi 1958, nilijifungua mwana wetu. Katika kipindi hicho kigumu, Yehova alikuwa rafiki yangu wa karibu zaidi na msaidizi wangu. Mama yangu alimchukua mwana wetu na kumtunza. Nilipelekwa Kemerovo, Siberia, ambako nilifungwa katika kambi ya kazi ngumu.
“Baada ya miaka minane, niliachiliwa kabla ya muda kamili wa kifungo changu kwisha. Ninakumbuka kwamba katika majengo ya gereza, mnyapara wa jengo letu alitangaza kwa sauti kwamba sikuwahi kusema jambo lolote ‘linalopinga Usovieti’ na kwamba vichapo vyetu vilikuwa vya kidini kabisa. Nilibatizwa mnamo 1966, baada ya kuachiliwa.”
Biblia na vichapo vya Biblia vilikuwa vyenye thamani sana gerezani na kwenye kambi. Mnamo 1958, kwenye kambi huko Mordvinia, akina ndugu walikuwa wakiongoza mikutano kwa ukawaida. Ili wanyapara wasiwakamate, ndugu kadhaa waliwekwa wasimame kila baada ya hatua chache ili watoe onyo wengine walipokuwa wakijifunza Mnara wa Mlinzi. Mnyapara alipotokea ndugu aliyemwona angesema “anakuja,” kisha ujumbe huo ungepitishwa hadi kwa kikundi kilichokuwa kimekutana. Kila mtu angeondoka, na gazeti lingefichwa. Lakini mara nyingi wanyapara walitokea ghafula na bila kutarajiwa.
Wakati mmoja wanyapara walipowakuta ghafula akina ndugu, Boris Kryltsov aliamua kuwakengeusha ili wasilipate gazeti hilo. Alinyakua kitabu na kukimbia nje ya jengo. Wanyapara walimkimbiza kwa muda mrefu, lakini walipomkamata waliona alikuwa amebeba kitabu cha Lenin. Ingawa alitiwa katika kifungo cha upweke kwa siku saba, alifurahi kwamba alikuwa amesaidia gazeti lisichukuliwe.
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
“Nilipelekwa kwenye gereza lenye ulinzi mkali huko Vladimir. Nilipekuliwa kabisa, lakini nilishangaa kuwa nilifaulu kuingiza ndani ya gereza hilo matoleo manne ya Mnara wa Mlinzi niliyokuwa nimenakili katika karatasi nyembamba. Ilikuwa wazi kwamba Yehova alinisaidia. Nilinakili upya magazeti hayo manne kwenye seli yangu. Nilijua kwamba mbali na mimi, kulikuwa na Mashahidi wengine, na kwamba hawakuwa wamepata chakula cha kiroho kwa miaka saba. Nilimtumia dada aliyekuwa akisafisha ngazi kupitisha magazeti hayo.
“Ilitukia kwamba mtu aliyekuwa akishirikiana na akina ndugu aliwaambia askari kwamba kuna mtu anayesambaza vichapo vya Biblia. Mara moja walianza kumpekua kila mtu na kuchukua vichapo vyote. Walipokuja kwangu walipata vichapo katika godoro langu. Nilifungwa kwa siku 85 katika kifungo cha upweke. Hata hivyo, Yehova aliendelea kututunza.”
HOTUBA ZILIWASAIDIA WENGINE KUJIFUNZA KWELI
Hotuba zilitumiwa pia kupiga vita vya mawazo dhidi ya Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti. Viktor Gutshmidt anasema: “Kambi yetu ilitembelewa kwa ukawaida na wasemaji waliotoa hotuba zilizotetea wazo la kwamba hakuna Mungu. Kila mara akina ndugu waliuliza maswali. Nyakati nyingine wasemaji walishindwa kujibu maswali rahisi sana. Kwa kawaida jumba lilijaa na kila mtu alisikiliza kwa makini sana. Watu walikuja kwa wingi kwa kuwa walitaka kujua Mashahidi wa Yehova watasema nini mwishoni mwa hotuba.
“Wakati mmoja, kambi yetu ilitembelewa na msemaji ambaye hapo awali alikuwa kasisi katika Kanisa Othodoksi la Urusi. Kila mtu alijua kwamba alikana imani yake alipokuwa kambini na kujiunga na watu wanaoamini hakuna Mungu.
“‘Je, uliamini hakuna Mungu kabla ya kwenda gerezani, au ulianza kuamini hivyo baadaye?’ ndugu mmoja alimwuliza msemaji alipomaliza.
“‘Hebu fikiria,’ akajibu msemaji. ‘Mtu alisafiri kwenda anga za juu naye hakumwona Mungu huko.’
“‘Ulipokuwa kasisi, je, uliamini kwamba Mungu anawatazama wanadamu kutoka kilomita 200 hivi juu ya dunia?’ akauliza ndugu huyo. Msemaji hakujibu. Mahojiano hayo yaliwafanya wafungwa wengi wafikiri, na baadaye wengine walianza kujifunza Biblia pamoja nasi.
“Pindi moja dada mmoja aliomba ruhusa aseme jambo fulani. ‘Sema tu; huenda wewe ni Shahidi wa Yehova,’ akasema msemaji.
“‘Ungesemaje kuhusu mtu anayesimama uwanjani na kupaaza sauti, “Nitakuua!” na huku hakuna mtu yeyote karibu?’ akauliza dada huyo.
“‘Kwa kweli, huwezi kusema ana akili timamu,’ akajibu msemaji.
“‘Ikiwa hakuna Mungu, kwa nini mnapigana naye? Ikiwa hayuko, basi inamaanisha kuwa hakuna mtu wa kupigana naye.’ Wasikilizaji wote wakaangua kicheko.”
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 124, 125]
Kambi Na. 1 ya Mordvinia
Kati ya 1959 na 1966, akina ndugu zaidi ya 450, walitumikia kifungo chao kwenye kambi hiyo, ambayo ilikuwa na uwezo wa kuchukua wafungwa 600 kwa wakati mmoja. Ikiwa moja kati ya kambi 19 za kazi ngumu kwenye eneo la Mordvinia, kambi hiyo ilizungukwa na ua wa waya wenye umeme ambao ulikuwa na kimo cha mita tatu. Ua huo ulizungukwa na ua nyingine 13 za nyaya. Kila wakati udongo kuzunguka kambi hiyo ulitifuliwa ili kwamba yeyote atakayetoroka angeacha alama za miguu.
Kwa kuwatenga Mashahidi wa Yehova na watu wengine wa nje ya kambi, wenye mamlaka walijaribu kuwatiisha kwa nguvu au kisaikolojia. Hata hivyo, akina ndugu walifanikiwa kupanga mambo ya kitheokrasi ndani ya kambi hiyo.
Kambi hiyo ikawa mzunguko na ikawa na mwangalizi wake wa mzunguko. Mzunguko huo uliundwa na makutaniko manne yaliyoundwa na vikundi 28 vya funzo la kitabu. Ili kuwasaidia wote wawe imara kiroho, akina ndugu waliamua kufanya mikutano saba kwa juma. Mwanzoni kulikuwa na Biblia moja iliyokuwa ikitumiwa na makutaniko yote, hivyo kulikuwa na ratiba ya kusoma Biblia hiyo kutaniko moja hadi lingine. Nafasi ilipojitokeza, ndugu walinakili Biblia. Vitabu tofautitofauti vya Biblia vilinakiliwa kwenye madaftari na nakala halisi ya Biblia ilifichwa. Kwa njia hiyo akina ndugu waliweza kufuata ratiba iliyopangwa ya usomaji wa Biblia. Funzo la Mnara wa Mlinzi lilipangwa pia. Akina dada waliokuwa wanakuja kuwaona waume zao kambini walibeba nakala ndogo za magazeti. Waliweka nakala hizo midomoni mwao, kwenye visigino vya viatu vyao au walizisuka zikiwa nyembamba pamoja na nywele zao. Akina ndugu wengi walifungwa vifungo vya upweke kwa siku mmoja hadi siku 15 kwa ajili ya kunakili vichapo kwa mkono.
Hiyo ilikuwa sehemu ya upweke mbali na wafungwa wengine. Walinzi waliokuwa wakisimamia sehemu hizo walikuwa waangalifu ili Mashahidi wa Yehova wasisome kitu chochote walipokuwa hapo. Hata hivyo, baadhi ya akina ndugu walifikiria njia za kuwaandalia chakula cha kiroho. Ndugu mmoja angepanda juu ya paa la jengo lililokuwa likiangaliana na ua ambao wafungwa waliofungwa kifungo cha upweke waliruhusiwa kutembea-tembea. Aliandaa mapema vikaratasi vidogovidogo sana ambavyo vilikuwa na andiko fulani la Biblia vikiwa vimekunjwa katika umbo la duara vyenye kipenyo cha sentimita moja. Kisha ndugu huyo angeviweka vikaratasi hivyo vilivyokunjwa kwenye bomba lililokuwa wazi pande zote na kupuliza kuelekea upande alikokuwa ndugu yule aliye kwenye kifungo cha upweke. Ndugu huyo angeinama akijidai kana kwamba anafunga kamba za viatu vyake, na kuokota chakula cha kiroho bila kugundulika.
Kwa ajili ya kifungua kinywa na mlo wa jioni, wafungwa walipewa uji mwembamba uliochanganywa na mafuta kidogo ya mbegu za pamba. Kwa kawaida chakula cha mchana kilikuwa supu ya viazi sukari au mchuzi mwingine pamoja na mlo mkuu wa siku hiyo. Mkate ambao wafungwa walikula ulikuwa unaonekana kama kitambaa kigumu kilichokuwa kikitumiwa kutengenezea viatu! Ivan Mikitkov anakumbuka hivi: “Nilifungwa miaka saba kwenye kambi hiyo, na kila mara tulikuwa na maumivu makali ya tumbo.”
Ndugu walibaki imara katika imani. Kuwa mbali na ndugu zao waliokuwa nje, hakukuvuruga usawaziko wa kiroho wa watumishi hao waaminifu wa Mungu, ambao waliendelea kuonyesha imani na upendo kuelekea Mungu na majirani wao.—Mt. 22:37-39.
-