-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
“MNA ‘MAJI MATAKATIFU’”
Mashahidi wa Yehova walifungwa kwenye kambi kwa sababu ya kazi ya kuhubiri. Nikolai Kalibaba aliyefungwa miaka mingi kwenye kambi hizo anakumbuka: “Wanne kati yetu walifungwa kwenye kambi katika kijiji cha Vikhorevka kwenye Wilaya ya Irkutsk, ambako ndugu 70 hivi walikuwa wamefungwa. Hakukuwa na maji safi ya kunywa; bomba pekee la maji safi lilikuwa limeunganishwa na bomba la maji machafu, kwa hiyo maji hayo yalikuwa hatari kwa afya. Pia chakula hakikufaa kuliwa, lakini Yehova alitusaidia. Katika kambi hiyo, ni Mashahidi tu waliotaka kufanya kazi. Tulikuwa wafanyakazi wenye bidii. Baada ya muda mfupi wasimamizi wa kambi walitambua hilo, na wakatutuma tukafanye kazi katika kambi nyingine. Hivyo tungeweza kuleta maji safi ya kunywa katika ndoo. Wafungwa wengi walikuwa wakitujia na kusema: ‘Tumesikia kwamba mna “maji matakatifu.” Tupeni angalau nusu glasi.’ Bila shaka tuliwapa maji.
“Kati ya wafungwa hao, kulikuwa na watu wenye nia njema. Baadhi yao walifungwa kwa sababu ya wizi na makosa mengine. Walijifunza kweli na wakawa Mashahidi wa Yehova. Wengine hawakupenda kweli na walitupinga waziwazi. Lakini wakati mmoja, msemaji alipokuja kambini kutoa hotuba dhidi ya Mashahidi wa Yehova, watu hao walitutetea kwa kusema kwamba hotuba hiyo iliwaharibia Mashahidi sifa.”
“TUTAWAJIA TUKIWA VIKUNDI”
Mara nyingi akina ndugu walimwomba Yehova hekima ya kujua jinsi ambavyo wangeweza kutumia hali zao kuendeleza mambo ya Ufalme. Nikolai anaendelea kusema: “Tulipata fununu kwamba tutapelekwa kwenye kambi nyingine huko Mordvinia karibu na Moscow. Kabla ya kuondoka jambo la kupendeza lilitukia. Tulishangaa wakati maofisa na wanyapara fulani ambao walikuwa wamewalinda Mashahidi wa Yehova kwa miaka kadhaa walipotujia na kusema: ‘Tungependa mtuimbie nyimbo zenu na mtueleze zaidi kuhusu mafundisho yenu. Tutawajia tukiwa vikundi vya watu 10 hadi 20, au hata zaidi.’
“Wakiogopa kile ambacho kingetokea iwapo tungegunduliwa, maofisa hao walisema kwamba wangeweka walinzi mahali ambapo tungekutania. Tuliwaambia kwamba kwa kuwa tuna uzoefu mwingi zaidi katika mambo hayo, tutaweka walinzi wetu pia. Walinzi wao walifanya kazi bega kwa bega na walinzi wetu: Kila baada ya hatua chache, kulikuwa na askari kati ya nyumba ya mlinzi na mahali tulipokutania. Unaweza kuwazia mandhari hiyo? Kikundi cha Mashahidi kiliwaimbia nyimbo maofisa na wanyapara, baada ya hapo ndugu alitoa hotuba fupi iliyotegemea kichwa fulani cha Biblia. Ilikuwa ni kana kwamba tuko kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova! Hivyo ndivyo tulivyoongoza mikutano kadhaa na vikundi vya wanyapara na maofisa waliopendezwa. Tuliona jinsi Yehova alivyotutunza sisi na watu hao wenye mioyo minyoofu.
“Tulibeba magazeti mengi kutoka katika kambi hiyo hadi kambi ya Mordvinia,” anasema Nikolai. “Kulikuwa na Mashahidi wengi katika kambi hiyo. Akina ndugu walinipa sanduku ambalo lilikuwa na mifuko ya ziada ndani ambamo vichapo vingeweza kuwekwa. Tulikuwa waangalifu ili wakati wa upekuzi, sanduku hilo lisivute uangalifu wa wanyapara hao. Katika kambi ya Mordvinia, tulipekuliwa kwa uangalifu sana. Mnyapara mmoja alichukua sanduku langu na kusema: ‘Sanduku hili ni zito sana! Lazima kuna hazina ndani!’ Bila kutarajia, aliweka sanduku langu pamoja na vitu vingine upande mmoja na akaanza kupekua mizigo ya watu wengine. Baada ya upekuzi, mnyapara mwingine aliniambia, ‘Chukua virago vyako na uende!’ Sanduku langu halikupekuliwa, kwa hiyo niliingiza kambini chakula kingi cha kiroho ambacho kilihitajika sana.
“Isitoshe, mara nyingi niliweka trakti zilizonakiliwa kwa mkono katika mabuti yangu. Kwa kuwa nilikuwa na miguu mikubwa, kila mara kulikuwa na nafasi ya kuhifadhi karatasi nyingi ndani ya viatu vyangu. Niliweka karatasi hizo chini ya soli ya ndani ya viatu, kisha nikapaka grisi nyingi. Grisi hiyo iliteleza na ilinuka vibaya sana, kwa hiyo wanyapara hawakupekua mabuti yangu.”
“WANYAPARA WALITUCHUNGUZA, NAMI NILIWACHUNGUZA PIA”
Nikolai anaendelea kusema: “Katika kambi ya Mordvinia, akina ndugu waliniweka nisimamie kazi ya kunakili vichapo. Jukumu langu moja lilikuwa kuwachunguza wanyapara ili wale walionakili vichapo kwa mkono wawe na muda wa kuficha kila kitu. Wanyapara walituchunguza, nami niliwachunguza pia. Baadhi ya wanyapara waliazimia kutukamata, na mara kwa mara wangeingia ghafula kwenye kambi. Ilikuwa vigumu sana kuwachunga. Wengine wangekuja kambini mara moja kwa siku. Hawakutuhangaisha.
“Katika nyakati hizo, tulinakili kutoka kwenye nakala halisi, ambazo tulizificha mahali salama. Nakala kadhaa halisi zilifichwa ndani ya jiko, hata kwenye jiko lililokuwa katika ofisi ya msimamizi wa kambi. Ndugu ambao walisafisha ofisi hiyo, walijenga sehemu maalumu katika jiko hilo ambako tuliweka nakala nyingi halisi za Mnara wa Mlinzi. Ingawa wanyapara walitupekua kwa uangalifu sana, sikuzote nakala halisi zilikuwa mahali salama, yaani, katika ofisi ya msimamizi.”
Akina ndugu walikuja kuwa na ustadi wa kuficha vichapo. Walipenda sana kuficha vichapo kwenye vizingiti vya madirisha. Ndugu hata walificha vichapo kwenye tyubu za dawa ya meno. Ni ndugu wawili au watatu tu waliojua mahali nakala halisi zilipowekwa. Kulipokuwa na uhitaji, mmoja wao alichukua nakala halisi na baada ya kuinakili kwa mkono aliirudisha mahali pake salama. Kwa njia hiyo, sikuzote nakala halisi zilibaki mahali salama. Ndugu wengi waliliona kuwa pendeleo kufanya kazi ya kunakili hata ingawa hilo lingemaanisha kuadhibiwa kwa kifungo cha upweke kwa siku 15. Viktor Gutshmidt anakumbuka hivi: “Kati ya miaka kumi niliyofungwa kambini, miaka mitatu hivi nilikuwa katika kifungo cha upweke.”
MNARA WA MLINZI WENYE MAANDISHI MADOGO SANA
Akina ndugu waliona kwamba wasimamizi wa kambi walikuwa wamebuni njia ya pekee ya kusaka vichapo vya Biblia kutoka kwa Mashahidi. Baadhi ya maofisa walifanya hivyo kwa makini sana. Ivan Klimko anasema hivi: “Wakati mmoja katika Kambi Na. 19 ya Mordvinia, askari wenye mbwa waliwaamuru akina ndugu watoke kambini na wakafanya msako mkali. Kila Shahidi alivuliwa nguo zote, kutia ndani matambara aliyokuwa amevaa miguuni. Lakini akina ndugu walibandika kwa gundi karatasi zilizonakiliwa kwa mkono chini ya nyayo za miguu, na hivyo karatasi hizo hazikugunduliwa. Pia walitengeneza vijitabu vidogo ambavyo vingeweza kutoshea katikati ya vidole. Walinzi walipowaamuru watu wote wainue mikono yao, vijitabu hivyo havikuanguka, na hivyo baadhi ya vichapo hivyo havikupatikana.”
Kulikuwa na njia nyingine za kulinda chakula cha kiroho. Aleksey Nepochatov anasema hivi: “Ndugu fulani waliweza kuandika kwa mwandiko mdogo kama utando wa buibui. Ncha ya kalamu ilichongwa na kuwa nyembamba sana hivi kwamba kwenye mstari mmoja wa karatasi mtu angeweza kuandika mistari mitatu au minne ya maandishi. Kasha dogo la kiberiti lingeweza kuwekwa nakala tano au sita za Mnara wa Mlinzi zilizoandikwa kwa mwandiko huo mdogo. Ili kuweza kuandika kwa mwandiko huo, mtu alihitaji kuwa na macho mazuri sana na alipaswa kuwa mvumilivu. Baada ya taa zote kuzimwa na watu wote kulala, ndugu hao waliandika wakiwa wamejifunika blanketi. Walitumia mwangaza wa taa iliyokuwa kwenye lango la kambi ambayo haikuwa inafanya kazi vizuri. Mtu alipofanya kazi hiyo kwa miezi kadhaa macho yake yaliharibika. Mara nyingine mlinzi angegundua, na ikiwa alitupenda angesema, ‘Bado mnaandika-andika tu, mtalala saa ngapi?’”
Ndugu Klimko anakumbuka hivi: “Pindi moja, tulipoteza vichapo vingi na hata Biblia. Vichapo hivyo vilikuwa vimefichwa katika mguu wa bandia wa ndugu mmoja. Baada ya kumlazimisha ndugu huyo atoe mguu wake, walinzi waliuvunja. Kisha walipiga picha kurasa zilizotawanyika na kuzichapisha kwenye gazeti la gereza hilo. Hata hivyo, hilo lilikuwa jambo zuri kwani lilionyesha kwamba Mashahidi wa Yehova walijihusisha katika utendaji wa kidini tu. Baada ya ugunduzi huo, msimamizi wa kambi aliwaambia akina ndugu hivi kwa kejeli, ‘Hii ndiyo Har–Magedoni yenu!’ Hata hivyo, siku iliyofuata, mtu fulani alimwambia kwamba Mashahidi wa Yehova wamekutana, wakaimba nyimbo, na kusoma kama ilivyo kawaida yao.”
KUZUNGUMZA NA MWENDESHA-MASHTAKA MKUU
Mwishoni mwa mwaka wa 1961, mwendesha-mashtaka mkuu wa Shirikisho la Muungano wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Sovieti ya Urusi, alikuja kukagua kambi ya Mordvinia. Alipokuwa akitembea katika kambi hiyo, aliingia mahali ambapo Mashahidi waliishi. Mwendesha-mashtaka mkuu aliwaruhusu ndugu wamuulize maswali machache. Viktor Gutshmidt anakumbuka hivi, “Niliuliza, ‘Je, unadhani dini ya Mashahidi wa Yehova ni hatari kwa watu wa Sovieti?’
“‘Sidhani,’ alisema mwendesha-mashtaka mkuu. Lakini baadaye alisema hivi bila kukusudia, ‘Katika mwaka wa 1959 pekee, rubo milioni tano zilitengwa kwa ajili ya Wilaya ya Irkutsk ili kuwachunguza Mashahidi.’
“Kwa kusema hivyo, alimaanisha kwamba serikali ilijua sisi ni nani, kwa kuwa Serikali ilikuwa imetenga rubo milioni tano zitumiwe katika magereza ili kuwachunguza Mashahidi wa Yehova. Hicho kilikuwa kiasi kikubwa sana cha pesa. Wakati huo, rubo elfu tano zingemwezesha mtu kununua gari au nyumba nzuri. Wenye mamlaka huko Moscow lazima walijua kwamba Mashahidi wa Yehova si watu hatari.
“Mwendesha-mashtaka mkuu aliendelea kusema, ‘Tukiwaambia watu wa Sovieti wawatendee vile wanavyotaka, watawafagilia mbali ninyi nyote.’ Alimaanisha kwamba watu wa Sovieti hawakuwapenda Mashahidi. Maneno yake yalionyesha kwamba mamilioni ya watu walikuwa wameathiriwa na propaganda ya kwamba hakuna Mungu.
“Tulimjibu hivi, ‘Mtaona uhalisi wa mambo wakati Mashahidi watakapofanya makusanyiko kutoka Moscow hadi Vladivostok.’
“Akasema: ‘Huenda watu nusu milioni ndio watakaokuwa upande wenu, wengine wote bado watakuwa upande wetu.’
“Mazungumzo yetu na mwendesha-mashtaka mkuu yaliishia hapo. Hakuwa amekosea. Leo, zaidi ya watu 700,000 wanahudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kotekote katika nchi zilizokuwa chini ya Muungano wa Sovieti. Huko watu wanasikiliza kweli safi za Biblia, badala ya propaganda.”
“UMEWATENGENEZEA MASHAHIDI MAHALI PA KUSTAREHE”
Viktor anaendelea kusema: “Msimamizi wa kambi alimwonyesha mwendesha-mashtaka mkuu maua na miti ambayo Mashahidi walipanda na pia vifurushi ambavyo walipokea na kuviweka katika kambi hiyo bila yeyote kuviiba. Alitazama kila kitu kwa mshangao. Hata hivyo, baadaye tuligundua kwamba mtu huyo aliamuru msimamizi wa kambi aharibu maua na miti yote. Alimwambia hivi msimamizi wa kambi, ‘Umewatengenezea Mashahidi mahali pa kustarehe badala ya kambi ya kazi ngumu.’ Pia aliamuru kwamba Mashahidi wasipokee vifurushi vyovyote na akafunga duka ambalo Mashahidi waliruhusiwa kwenda kununua chakula cha ziada.
“Hata hivyo, akina ndugu walifurahi wakati msimamizi hakufuata maagizo hayo yote. Kwa mfano, akina dada waliruhusiwa kuendelea kupanda maua kama zamani. Katika majira ya kuchipua, walikata maua hayo na kutengeneza mashada makubwa na kuwapa wafanyakazi wa kambi na watoto wao. Ilifurahisha hasa kuwaona watoto walipokutana na wazazi kwenye lango, wakichukua maua yao na kukimbia shuleni wakiwa na furaha. Waliwapenda Mashahidi.”
Viktor anakumbuka hivi: “Siku moja mwanzoni mwa 1964, mnyapara mmoja ambaye ndugu yake alifanya kazi kwenye shirika la KGB, alituambia kwamba Serikali ilikuwa ikipanga kampeni kubwa dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Lakini mwishoni mwa mwaka huo, Nikita Khrushchev aliyekuwa kiongozi wa Serikali, aliondolewa mamlakani kwa ghafula na mateso yakapungua.”
NYIMBO ZA UFALME KWENYE KAMBI YENYE ULINZI MKALI
Katika miaka ya 1960, wasimamizi wa kambi yenye ulinzi mkali huko Mordvinia waliruhusu wafungwa wapokee vifurushi mara moja kwa mwaka na hilo lilikuwa ni kama ‘tuzo la pekee.’ Msako ulifanywa kila mara. Ikiwa yeyote angeshikwa akiwa na karatasi yenye andiko, alifungwa kifungo cha upweke kwa siku kumi. Isitoshe, katika kambi hiyo wafungwa walipewa chakula kidogo kuliko katika kambi nyingine. Kazi ilikuwa ngumu zaidi katika kambi zenye ulinzi mkali; Mashahidi walihitaji kung’oa visiki vya miti mikubwa. Aleksey Nepochatov anasema hivi: “Mara nyingi, tulikuwa tumechoka kabisa. Lakini tulijaribu kuwa makini na hatukuvunjika moyo. Njia moja ambayo akina ndugu walijitia moyo ilikuwa ni kuimba nyimbo za Ufalme. Tuliunda kwaya yenye mpangilio mzuri wa sauti, hivi kwamba hata ingawa hakukuwa na sauti za akina dada, nyimbo hizo zilipendeza sana. Nyimbo hizo ziliwachangamsha Mashahidi na pia maofisa, nao waliwaomba akina ndugu waimbe walipokuwa wakifanya kazi. Pindi moja tulipokuwa tunakata miti, msimamizi alikuja na kutuambia: ‘Imbeni nyimbo chache. Ombi hili limetoka kwa ofisa mkuu mwenyewe!’
“Ofisa huyo alikuwa amewasikia akina ndugu wakiimba nyimbo za Ufalme mara nyingi. Ombi hilo lilikuja kwa wakati uliofaa kwani tulikuwa tumechoka sana. Kwa shangwe tulianza kumsifu Yehova kwa sauti zetu. Kwa kawaida tulipoimba katika kambi, wake za maofisa walitoka nyumbani mwao na kusimama kwenye varanda na kutusikiliza kwa muda mrefu. Walipenda sana wimbo namba 6, ‘Dunia na Itoe Utukufu,’ uliokuwa katika kitabu cha nyimbo cha zamani. Wimbo huo ulikuwa na maneno mazuri na sauti nzuri sana.”
ALIFIKA “NCHI NYINGINE”
Hata katika hali zisizotarajiwa, ilionekana Mashahidi wa Yehova ni watu wa aina gani. Viktor Gutshmidt anakumbuka: “Tulikuwa tumeketi bustanini wakati vifaa fulani vya bei ghali vya umeme vililetwa kambini. Dereva aliyevileta hakuwa ndugu yetu wa kiroho. Alikuwa mfungwa katika kambi yetu, na meneja wa ununuzi aliyemsindikiza alikuwa wa kambi nyingine. Kwa kuwa chumba cha kuhifadhia kilikuwa kimefungwa na msimamizi alikuwa likizoni, Mashahidi waliombwa wavikubali na kuvipakua.
“Tulipakua vifaa hivyo na kuvipanga nje ya chumba hicho kilichokuwa karibu na jengo ambalo akina ndugu walifungwa. Meneja wa ununuzi alikuwa na wasiwasi sana kuhusu kuacha vifaa hivyo bila sahihi ya kuvipokea ya meneja wa chumba cha kuhifadhia. Lakini dereva alimhakikishia: ‘Usiogope. Hakuna atakayevigusa. Umefika “nchi nyingine.” Sahau yanayofanyika nje ya kambi. Ukivua saa ya mkononi na kuiacha mahali popote, kesho utaipata hapohapo.’ Meneja wa ununuzi alisisitiza kuwa bidhaa hizo zina thamani ya rubo nusu milioni, hivyo hangeziacha bila sahihi ya mtu fulani.
“Wasimamizi wa kambi waliwasili na kuamuru gari hilo liondolewe kambini. Mmoja wao alimwambia aache hati ya kuwasilisha bidhaa na kuichukua siku inayofuata. Aliondoka shingo upande. Asubuhi iliyofuata alirudi na kuomba aruhusiwe kuingia kambini ili hati hiyo itiwe sahihi, lakini mlinzi alimpa hati hiyo ikiwa tayari imetiwa sahihi.
“Mlinzi alituambia kwamba meneja huyo alishindwa kuondoka. Kwa nusu saa, alisimama, akakodolea macho lango hilo, kisha akatazama hati zile, akageuka ili aondoke, kisha akageuka tena na kukodolea macho lango kwa mara nyingine. Huenda ilikuwa mara yake ya kwanza kuona jambo kama hilo. Vifaa vya bei ghali vilipokewa na hati ikatiwa sahihi bila yeye kuwapo, na kila kitu kilikuwa kimefanywa kwa unyoofu. Lakini jambo la kushangaza hata zaidi ni kwamba hilo lilitokea kwenye kambi yenye ulinzi mkali ambapo wafungwa wanatambulishwa kuwa ‘wahalifu hatari zaidi.’ Ndiyo, licha ya propaganda dhidi ya Mashahidi, matukio kama hayo yaliwafanya watu wajue Mashahidi wa Yehova ni watu wa aina gani.”
“WAMEANZA KUHUBIRI TENA”
Mnamo 1960, siku chache baada ya akina ndugu kujikuta pamoja katika kambi ya Mordvinia, zaidi ya Mashahidi 100 walichaguliwa ili wahamishwe kwenye Kambi Na. 10, gereza maalumu katika kijiji cha karibu cha Udarnyy. Lilikuwa gereza la kujaribu kuwafundisha upya Mashahidi. Wafungwa walivalia sare zenye mistari kama zilizovaliwa na wafungwa wa kambi za mateso za Wanazi. Mbali na kazi nyingine, Mashahidi walihitaji kuchimbua visiki vikubwa msituni. Kila mmoja alitazamiwa kuchimbua visiki 11 hadi 12 kwa siku. Lakini nyakati nyingine, hata kikundi kizima cha akina ndugu kikifanya kazi kwa siku nzima hawangeweza kuchimbua kisiki kimoja cha mwaloni mkubwa. Mara nyingi waliimba nyimbo za Ufalme ili kutiana moyo. Msimamizi wa kambi alipowasikia wakiimba, mara nyingine angewafokea hivi: “Ninyi Mashahidi mtalala njaa ili mwache kuimba. Nitawafundisha kufanya kazi!” Ndugu mmoja aliyekuwa katika kambi hiyo anakumbuka: “Lakini Yehova alitutegemeza. Licha ya hali ngumu tulikuwa macho kiroho. Sikuzote tulijitia moyo kwa kujikumbusha kuwa tumesimama upande wa Yehova katika suala la enzi kuu ya ulimwenguni pote.”—Met. 27:11.
Kulikuwa na walioitwa eti “walimu” wa gereza na kila seli ilikuwa na mmoja, na hakuna yeyote kati yao aliyekuwa na cheo cha chini kuliko kile cha kapteni. Kusudi lao lilikuwa kuwafanya Mashahidi wakane imani. Walisema yeyote anayekana imani angeachiliwa. Kila mwezi, walimu hao waliandika ripoti kuhusu tabia ya kila Shahidi, nayo ingetiwa sahihi na mfanyakazi wa gereza. Kwa kawaida ripoti ya kila Shahidi ilisema, “Hatendi kupatana na majaribio ya kumwelimisha upya, yuko imara katika imani yake.” Ivan Klimko anasema: “Kati ya miaka kumi niliyohukumiwa, nilitumia miaka sita katika gereza hilo na niliitwa ‘mfungwa hatari anayefanya makosa kwa kurudia’ sawa na ndugu wengine. Maofisa walituambia wenye mamlaka walifanya hali ziwe ngumu sana hasa kwa ajili ya Mashahidi ili watuchunguze.”
Wakati mmoja Iov Andronic aliyefungwa humo kwa miaka mitano alimuuliza kamanda wa kambi hivi, “Tutafungwa hapa mpaka lini?” Akielekeza msituni, kamanda huyo alimjibu, “Hadi nyote mtakapozikwa kule.” Iov anasema: “Tulitenganishwa na wengine ili tusiwahubirie. Tulichungwa sana. Ikiwa mmoja wetu alihitaji kwenda sehemu nyingine ya kambi, alisindikizwa na mnyapara. Miaka kadhaa baadaye tulipohamishwa kwenye kambi yenye ulinzi wa kadiri, wafungwa fulani ambao si Mashahidi walimwambia msimamizi wa kambi: ‘Mashahidi wa Yehova walishinda. Mliwatenga, lakini sasa wameanza kuhubiri tena.’”
OFISA ANAITAMBUA BIBLIA YAKE
Kuingiza kichapo chochote katika Kambi Na. 10 haukuwa mchezo wa watoto, sembuse Biblia. Akina ndugu waliona haiwezekani kuingiza Neno la Mungu humo. Ndugu mmoja aliyefungwa humo kwa miaka michache anasema: “Kwa Yehova hakuna jambo lisilowezekana. Mungu alisikiliza sala zetu. Tuliomba tupate angalau Biblia moja kwa ajili ya Mashahidi 100 waliofungwa humo na kwa kushangaza tukapata Biblia mbili!” (Mt. 19:26) Hilo liliwezekanaje?
Kanali fulani aliajiriwa kuwa mwalimu wa gereza. Lakini ingewezekanaje kwa mtu asiye na ujuzi wowote wa Biblia “kuwaelimisha” Mashahidi? Kwa njia fulani alipata Biblia iliyochakaa. Kabla ya kwenda likizo alimwomba mfungwa fulani mzee aliyekuwa Mbaptisti aijalidi. Aliwaambia wanyapara wasimnyang’anye Biblia hiyo. Mbaptisti huyo aliwaringia Mashahidi kuwa amepata Biblia, naye akakubali kuwapa waisome. Akina ndugu walipopata hazina hiyo yenye thamani, walifumua nyuzi za Biblia hiyo na kuwagawia wafungwa wote Mashahidi kurasa zake ili wazinakili. Siku chache zilizofuata, Mashahidi walitumia seli zao kunakili kurasa hizo. Walitoa nakala mbili za kila kurasa. Ndugu mmoja anakumbuka: “Kurasa zote zilipokusanywa, kulikuwa na Biblia tatu! Kanali alipewa nakala yake iliyojalidiwa upya, nasi tukabaki na zetu mbili. Tulisoma nakala moja na ile nyingine tuliificha kwenye transfoma yenye umeme mwingi. Tulikuwa tumetengeneza sehemu za pekee katika transfoma hizo. Wanyapara waliogopa kuzikaribia, hivyo hakuna aliyezichunguza. Umeme huo ulikuwa mlinzi wetu mwenye kutegemeka.”
Hata hivyo, wakati wa upekuzi mmoja, kanali aliona ukurasa wa Biblia iliyonakiliwa kwa mkono. Alipogundua kilichotokea, alifadhaika sana na akasema kwa mshangao, “Hii ni sehemu ya Biblia ambayo mimi mwenyewe niliingiza kambini!”
KUADHIMISHA UKUMBUSHO
Kila mwaka, akina ndugu walijaribu kuadhimisha Ukumbusho kambini. Miaka yote waliyokuwa katika kambi moja huko Mordvinia, hakuna ndugu aliyekosa tukio hilo. Bila shaka, wasimamizi wa kambi walijaribu kulizuia. Walijua tarehe ya Ukumbusho, na kwa kawaida waliwaambia walinzi wote wawe macho. Hata hivyo, walinzi wengi walichoka kuwachunguza akina ndugu ilipofika jioni kwa sababu hakuna aliyejua wakati na mahali ambapo Ukumbusho ungefanywa.
Akina ndugu walijitahidi kupata divai na mkate usiotiwa chachu. Wakati mmoja walinzi waligundua mifano hiyo kwenye droo siku ya Ukumbusho na wakaichukua. Baadaye, kikundi hicho kilibadilishwa, na ndugu aliyekuwa akisafisha ofisi ya kamanda alichukua mifano hiyo na kuwapa akina ndugu bila kuonekana. Jioni hiyo ndugu waliadhimisha Ukumbusho wakiwa na mifano wakati wa zamu ya kikundi cha tatu. Mifano hiyo ilihitajika sana kwani ndugu mmoja alikuwa mtiwa mafuta.
KUADHIMISHA UKUMBUSHO KATIKA KAMBI YA WANAWAKE
Kambi nyingine zilikuwa na tatizo hilohilo. Valentina Garnovskaya anakumbuka ilivyokuwa vigumu kuadhimisha Ukumbusho katika kambi ya wanawake huko Kemerovo. Anasema: “Kambi hiyo ilikuwa na dada 180. Tulikatazwa kukutana. Kwa miaka kumi tulifaulu kuadhimisha Ukumbusho mara mbili tu. Wakati mmoja tuliamua kuadhimisha Ukumbusho katika ofisi niliyopaswa kusafisha. Akina dada walianza kuingia ofisini bila kuonekana kwa muda wa saa kadhaa kabla ya Ukumbusho. Dada 80 hivi walifika. Tuliweka mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu mezani.
“Tuliamua kuanza bila kuimba, hivyo dada mmoja akatoa sala ya kufungua, na tukaanza kwa shangwe na kwa njia inayofaa. Lakini ghafula tulisikia kelele na tukagundua kuwa wanyapara walikuwa wakitutafuta. Kisha tukaona msimamizi wao akichungulia dirishani, ingawa dirisha hilo lilikuwa juu sana. Mlango ulibishwa kwa nguvu na wakatuamuru tuufungue. Wanyapara waliingia kwa kishindo na kumkamata dada aliyekuwa akitoa hotuba na kumpeleka katika kifungo cha upweke. Kwa ujasiri dada mwingine alisimama atoe hotuba hiyo, lakini wakamkamata pia. Alipochukuliwa, dada mwingine akajaribu kuendelea na hotuba hiyo, kwa hiyo wakatukusanya katika chumba kingine, wakitisha kutuadhibu kwa kifungo cha upweke. Hapo ndipo tulipomaliza mwadhimisho wa Ukumbusho kwa wimbo na kufunga kwa sala.
“Tuliporudi mahali pa kulala, wafungwa wengine walituambia, ‘Mlipotoweka ghafula, tulisema Har–Magedoni imekuja na Mungu amewachukua na kuwapeleka mbinguni akituacha hapa tuangamie!’ Tulikuwa na wafungwa hao kwa miaka kadhaa na hawakuwa wamekubali kweli. Lakini baada ya hapo, baadhi yao walianza kutusikiliza.”
“TULIJIKUSANYA PAMOJA”
Kambi moja huko Vorkuta ilikuwa na Mashahidi wengi kutoka Ukrainia, Moldova, maeneo ya Baltiki, na jamhuri nyingine za Muungano wa Sovieti. Ivan Klimko anakumbuka: “Yalikuwa majira ya baridi kali mwaka wa 1948. Ingawa hatukuwa na vichapo vya Biblia, tuliandika katika karatasi ndogo tulichokumbuka kutoka kwenye magazeti ya zamani na kuzificha ili wanyapara wasizipate. Lakini walijua tulikuwa nazo. Tungepekuliwa kwa muda mrefu na kwa uangalifu sana. Siku zenye baridi kali sana, tulipelekwa nje na kusimamishwa katika mistari ya watu watano. Mara nyingi tulihesabiwa tena na tena. Ilionekana walitazamia tuwape karatasi hizo badala ya kusimama katika baridi hiyo kali. Tulipokuwa tukihesabiwa tena na tena, tulijikusanya pamoja na kuzungumzia jambo fulani la Biblia. Sikuzote tulifikiria mambo ya kiroho. Yehova alitusaidia kuwa watimilifu. Baadaye, hata tuliingiza Biblia kambini. Tuliigawanya sehemu mbalimbali ili Biblia nzima isichukuliwe wakati wa upekuzi.
“Walinzi walielewa Mashahidi wa Yehova hawakustahili kuwa gerezani. Walitusaidia kwa njia yoyote waliyoweza. Baadhi yao ‘walifunga macho’ kila mara tulipoletewa barua. Kwa kawaida, barua hizo zilikuwa na ukurasa mmoja au mbili za Mnara wa Mlinzi. Kurasa hizo, hazikuwa na gramu nyingi, lakini zilikuwa na thamani kuliko kilo kadhaa za chakula. Ingawa Mashahidi walinyimwa chakula na vitu vingine katika kila kambi, walikuwa matajiri kiroho.”—Isa. 65:13, 14.
“ATAKIGAWANYA MARA 50!”
Akina ndugu waliongoza mafunzo ya Biblia kila juma na wale waliopendezwa na kweli. Wafungwa kadhaa—hata wale ambao hawakupendezwa na Biblia—walijua kwamba baada ya saa moja jioni, kulikuwa na mafunzo ya Biblia kambini nao walijaribu kunyamaza. Iov Andronic anakumbuka: “Ilikuwa wazi Yehova anatutunza na kuendeleza kazi yake. Isitoshe, tulijaribu kuonyeshana upendo wa Kikristo kwa kutumia kanuni za Biblia. Kwa mfano, tuligawana chakula tulichopokea, jambo ambalo halikuwa la kawaida kambini.
“Katika kambi moja, Mykola Pyatokha alikuwa na jukumu la kugawia akina ndugu chakula. Ofisa wa KGB alisema hivi wakati mmoja, ‘Mpe Mykola kipande cha peremende, naye atakigawanya mara 50!’ Hivyo ndivyo akina ndugu walivyofanya. Tuligawana kila kitu kilicholetwa kambini, chakula cha kimwili na cha kiroho. Hilo lilitusaidia na likawavutia watu wenye mioyo minyoofu waliopendezwa.”—Mt. 28:19, 20; Yoh. 13:34, 35.
WAONGEZEWA MISHAHARA KWA SABABU YA MWENENDO MZURI
Katika kambi moja wafanyakazi waliowashughulikia Mashahidi wa Yehova walipata nyongeza ya asilimia 30 ya mishahara. Kwa nini? Viktor Gutshmidt anaeleza: “Mweka-hazina wa zamani kambini alinieleza jambo hilo. Aliniambia kwamba katika kambi ambako ndugu wengi walifungwa, wafanyakazi waliambiwa wasikasirike au wasimtukane mtu na walipaswa kuwa wenye busara na watulivu nyakati zote. Wangepata nyongeza kwa mwenendo huo mzuri. Hilo lilifanywa kuonyesha kuwa si Mashahidi wa Yehova tu wanaoishi maisha mazuri na kwamba hakuna tofauti kati yao na watu wengine. Kwa hiyo, wafanyakazi walilipwa kwa mwenendo wao. Kulikuwa na wafanyakazi wengi kambini; wahudumu wa afya, vibarua, wahasibu, na wanyapara, watu 100 hivi. Hakuna aliyetaka kukosa nafasi ya kupata pesa zaidi.
“Siku moja ndugu aliyefanya kazi nje ya kambi alimsikia msimamizi wa kikundi akitoa matusi kwa sauti. Siku iliyofuata ndugu huyo alikutana na msimamizi huyo kambini na kusema: ‘Inaonekana mtu fulani katika nyumba ya walinzi alikukasirisha sana. Ulikuwa ukitoa matusi kwa sauti kubwa sana!’ Mtu huyo akasema: ‘Hapana, nilifadhaika tu siku hiyo. Kwa hiyo nilitoka nje ya kambi ili nijitulize.’ Kwa kweli, haikuwa rahisi kujiendesha kama Mashahidi wa Yehova.”
TULIHUBIRI TULIPOKUWA TUKIWEKA DIRISHA
Akina ndugu walitumia nafasi walizopata kuhubiri na mara nyingine walifanikiwa sana. Nikolai Gutsulyak anakumbuka: “Mara nyingi tulinunua chakula katika kioski cha kambini. Kila nilipochukua chakula, nilisema maneno machache kuhusu Biblia. Mwanamke aliyeuza chakula alisikiliza kwa makini na wakati mmoja aliniomba nimsomee kitu fulani. Siku tatu baadaye, ofisa mmoja aliniita langoni. Aliniambia mimi na Shahidi mwingine tukaweke dirisha kwenye nyumba ya kamanda wa kambi.
“Tuliandamana na askari kwenda jijini. Tulipofika katika nyumba hiyo, tulifunguliwa mlango na mwanamke yuleyule aliyefanya kazi katika kioski cha kambini. Kumbe alikuwa mke wa kamanda! Askari mmoja alisimama ndani, na wawili nje kwenye barabara iliyokuwa kando ya dirisha. Mwanamke huyo alitupa chai na kuomba tumweleze mengi kuhusu Biblia. Tulimwekea kioo dirishani na kumhubiria sana. Mazungumzo yetu yalipoisha, alisema: ‘Msiniogope. Wazazi wangu walimwogopa Mungu kama ninyi.’ Alisoma vichapo kwa siri, bila mume wake kujua kwani aliwachukia Mashahidi.”
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kuvitia Nguvu “Vigingi vya Hema” Letu
DMITRY LIVY
ALIZALIWA 1921
ALIBATIZWA 1943
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa kwenye Halmashauri ya Nchi ya Urusi kwa zaidi ya miaka 20 na sasa anatumikia akiwa mzee katika kutaniko huko Siberia.
ULIKUWA mwaka wa 1944, miezi sita kabla ya mwisho wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Nilikuwa nimesimama katika mahakama mbele ya jaji wa kijeshi kwa sababu ya msimamo wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote wa kisiasa. Nilihukumiwa kifo kwa kupigwa risasi, lakini baadaye hukumu ilibadilishwa na kuwa kifungo cha miaka kumi katika kambi ya kazi ngumu.
Mnamo Januari 1945, nilipelekwa kwenye kambi moja kaskazini mwa Urusi katika mji wa Pechora, katika Jamhuri ya Komi. Kati ya mamia ya wafungwa waliokuwa kambini, kulikuwa na ndugu kumi. Nasikitika kwamba gazeti pekee nililokuwa nimebeba la Mnara wa Mlinzi lilichukuliwa, kwa hiyo hatukuwa na chakula cha kiroho. Nilikuwa nimechoka sana hivi kwamba singeweza kufanya kazi. Tulipoenda kuoga bafuni, ndugu mmoja aliniambia kwamba nilionekana mifupa mitupu. Kwa kweli, nilikuwa mnyonge sana hivi kwamba nilipelekwa kwenye kambi ya matibabu huko Vorkuta.
Baada ya muda, nilianza kupata nafuu na nikapelekwa kufanya kazi ya kuchimba mchanga. Lakini kabla ya mwezi mmoja kwisha, kazi hiyo ngumu ilinifanya nikonde tena. Daktari alifikiri kwamba ninabadilishana chakula ili nipate sigara, lakini nikamwambia mimi ni Shahidi wa Yehova na sivuti sigara. Nilifanya kazi katika kambi hiyo kwa miaka miwili. Ingawa nilikuwa Shahidi pekee kambini, kila mara kulikuwa na watu waliotaka kusikiliza kweli, na wengine kati yao waliitikia habari njema.
Wakati mmoja, watu wa ukoo walinitumia gazeti la Mnara wa Mlinzi lililoandikwa kwa mkono. Nilifaulu jinsi gani kulipata ilhali kila furushi lilikaguliwa kwa uangalifu na mnyapara? Kurasa za gazeti hilo zilikuwa zimekunjwa mara mbili na kuwekwa chini ya mkebe wenye sehemu mbili na sehemu ya juu ikafunikwa na mafuta mengi. Msimamizi wa gereza alitoboa mkebe huo na kwa kuwa hakushuku chochote, akanipa. Chanzo hicho cha “maji yaliyo hai” kilinifaa kwa muda mrefu.—Yoh. 4:10.
Mnamo Oktoba 1949, niliachiliwa kabla ya kifungo changu kuisha, na katika mwezi wa Novemba nilirudi nyumbani nchini Ukrainia.
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Sikuwa na Mahali Pangu Pa Kuishi
VALENTINA GARNOVSKAYA
ALIZALIWA 1924
ALIBATIZWA 1967
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alifungwa gerezani na kwenye kambi za kazi ngumu kwa miaka 21, miaka 18 kati ya hiyo akiwa bado hajabatizwa. Valentina aliwasaidia watu 44 wajifunze kweli kabla ya kifo chake mnamo 2001.
MIMI na mama yangu tuliishi upande wa magharibi wa Belarus. Nilikutana na Mashahidi wa Yehova mnamo Februari 1945. Ndugu mmoja alikuja nyumbani kwetu mara tatu tu na kutufundisha mambo fulani katika Biblia. Ingawa sikumwona tena, nilianza kuwahubiria majirani na marafiki. Wenye mamlaka walinikamata, na nikahukumiwa kifungo cha miaka nane katika kambi. Walinipeleka kwenye kambi katika Wilaya ya Ulyanovsk.
Nikiwa kambini niliwachunguza wafungwa wengine na kusikiliza mazungumzo yao, nikitumaini kwamba nitakutana na Shahidi wa Yehova. Mnamo 1948, nilimsikia mfungwa mmoja mwanamke akizungumza kuhusu Ufalme wa Mungu. Mfungwa huyo aliitwa Asya. Nilifurahi sana kuzungumza naye kuhusu mambo ya kiroho. Muda si muda, dada wengine watatu waliletwa kambini. Tulikuwa na vichapo vichache, kwa hiyo tulijaribu kuwasiliana mara nyingi iwezekanavyo.
Mnamo 1953 niliachiliwa huru, lakini miaka mitatu na nusu baadaye, nilikamatwa kwa sababu ya kuhubiri na kufungwa kwa miaka kumi. Mwaka wa 1957 nilihamishiwa kwenye kambi ya Kemerovo, ambako kulikuwa na dada 180 hivi. Sikuzote tulikuwa na vichapo vya Biblia. Katika majira ya baridi kali, tulificha vichapo katika theluji, na katika majira ya kiangazi, tulivificha katika nyasi na kwenye mchanga. Wakati wa upekuzi, nilificha hati katika mikono yote miwili, nilijitanda kitambaa kikubwa mabegani na nilishikilia miisho ya kitambaa hicho kwa mikono yangu. Nilipohamishwa kutoka kambi moja hadi nyingine, nilivaa kofia ambayo nilikuwa nimeshona mwenyewe na kuficha magazeti kadhaa ya Mnara wa Mlinzi ndani yake.
Mwishowe nilihamishiwa kwenye kambi fulani huko Mordvinia. Huko kulikuwa na Biblia, ambayo ilifichwa mahali salama. Tungeisoma wakati tu dada mwenye kuitunza alikuwapo. Mara nyingine pekee ambayo nilikuwa nimewahi kuona Biblia ni wakati ilikuwa mikononi mwa ndugu aliyezungumza nami kuhusu kweli katika mwaka wa 1945.
Nilipoachiliwa mwaka wa 1967, nilihamia huko Angren, Uzibekistani. Hapo nilifaulu kuonyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Hii ndiyo mara yangu ya pili kukutana na akina ndugu tangu yule ndugu wa kwanza aliponihubiria. Hiyo ni kwa sababu nilikuwa nimefungwa katika kambi za wanawake peke yao. Ndugu na dada wote katika kutaniko walikuwa na bidii nami nikaja kuwapenda. Mnamo Januari 1969, ndugu wanane na dada watano katika kutaniko letu walikamatwa kwa sababu ya kuhubiri, mimi nilikuwa mmoja wao. Nilihukumiwa miaka mitatu na kuitwa “mhalifu hatari sana.” Mara nyingi nilifungwa kifungo cha upweke kwa sababu ya kuhubiri.
Niliongoza mafunzo ya Biblia na waliopendezwa tukiwa tumejifunika blanketi. Tulikatazwa kuwasiliana tulipotembea. Iwapo tungekutwa tukizungumza, tungeadhibiwa kwa kupewa kifungo cha upweke. Tulitumia vichapo vilivyonakiliwa kwa mkono, na tuliendelea kuvinakili kila mara.
Sikuwa na mahali pangu pa kuishi. Vitu vyangu vyote vilitoshea katika mfuko mmoja, lakini nilifurahi na kuridhika kwa kuwa nilimtumikia Yehova.
-