Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nilimtumikia Mungu Licha ya Magumu
    Amkeni!—2005 | Aprili 22
    • Nakamatwa na Kufungwa

      Plasta niliyokuwa nayo iliondolewa mwaka wa 1953. Licha ya kujitahidi kuwa mwangalifu, polisi wa KGB waligundua utendaji wangu wa kiroho pamoja na kazi yangu ya kunakili vichapo vya Biblia. Mwishowe, nilihukumiwa miaka 12 katika kambi ya gereza pamoja na Mashahidi wengine. Hata hivyo, wakati wa kesi, sote tulitoa ushahidi mzuri kumhusu Mungu wetu, Yehova, na makusudi yake ya upendo kwa wanadamu.

      Mwishowe tulipelekwa kwenye kambi mbalimbali karibu na Irkutsk, mamia ya kilometa upande wa mashariki. Watu ambao walionwa kuwa maadui wa Serikali ya Sovieti waliteswa katika kambi hizo. Kuanzia Aprili 8, 1954, hadi mapema mwaka wa 1960, nilifungwa katika kambi 12 za kazi ngumu. Baadaye, nilisafirishwa zaidi ya kilometa 3,000 kuelekea magharibi kwenye kambi kubwa za Mordovia za wafungwa kilometa 400 hivi kusini-mashariki mwa Moscow. Nilipata fursa ya kukutana na Mashahidi waaminifu kutoka sehemu nyingi za Muungano wa Sovieti.

      Wasovieti waligundua kwamba Mashahidi waliporuhusiwa kuchangamana na wafungwa wengine wasio Mashahidi, baadhi ya wafungwa hao pia walikuja kuwa Mashahidi. Kwa hiyo, katika magereza makubwa ya Mordovia yaliyofikia umbali wa kilometa 30 au zaidi, ambayo yalikuwa na kambi nyingi za kazi ngumu, walijaribu kututenga na wafungwa wengine. Zaidi ya Mashahidi 400 waliwekwa pamoja katika kambi yetu. Dada Wakristo wapatao 100 au zaidi walikuwa katika kambi nyingine kubwa umbali wa kilometa kadhaa.

      Nilijitahidi sana kusaidia kupanga mikutano ya Kikristo katika kambi yetu, vilevile kunakili vichapo vya Biblia ambavyo vililetwa kambini kisiri. Bila shaka wasimamizi wa kambi waligundua jambo hilo. Muda mfupi baadaye, mnamo Agosti 1961, nilihukumiwa mwaka mmoja katika gereza maarufu la Vladimir la enzi ya utawala wa Zari, kilometa 200 hivi kaskazini-mashariki mwa Moscow. Rubani Mmarekani Francis Gary Powers, ambaye alikuwa akiendesha ndege iliyopigwa risasi Mei 1, 1960, ilipokuwa ikipeleleza Urusi, alifungwa pia katika gereza hilo hadi Februari 1962.

      Nilipokuwa katika Gereza la Vladimir, nilipewa chakula kidogo tu cha kuniwezesha kuishi. Nilistahimili njaa kwa sababu nikiwa kijana nilizoea hali hiyo, lakini nilishindwa kuvumilia baridi kali sana ya mwaka wa 1961 na 1962. Mabomba ya kupasha joto gereza yaliharibika, na hivyo chumba changu kilikuwa na baridi kali kupindukia. Daktari mmoja aliona hali yangu yenye kusikitisha na kufanya mipango ili nipelekwe kwenye chumba kingine kilichokuwa afadhali katika majuma ya kwanza ya baridi kali.

      Naimarishwa Kuvumilia Magumu

      Mawazo yasiyofaa yanaweza kumvunja mtu moyo baada ya kukaa peke yake kwa miezi kadhaa, na wasimamizi wa gereza hutaka hivyo. Hata hivyo, nilisali daima nikaimarishwa na roho ya Yehova pamoja na maandiko niliyokumbuka.

      Nilipokuwa katika Gereza la Vladimir nilikumbuka maneno ya mtume Paulo kwamba “tunakazwa katika kila njia, lakini hatubanwi kupita kiasi cha kuweza kusonga,” na “tunafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa.” (2 Wakorintho 4:8-10) Baada ya mwaka mmoja, nilirudishwa katika kambi kubwa ya Moldova. Nikakamilisha kifungo changu cha miaka 12 katika kambi hizo mnamo Aprili 8, 1966. Baada ya kuachiliwa huru, walisema kwamba mimi ni mtu “asiyeweza kubadilika.” Kwangu, huo ulikuwa uthibitisho wa wazi kwamba nilidumisha uaminifu wangu kwa Yehova.

      Mara nyingi nimeulizwa jinsi tulivyopata na kunakili vichapo vya Biblia katika kambi za Sovieti licha ya jitihada za kutuzuia kufanya hivyo. Si watu wengi waliojua siri hiyo, kama anavyosema mfungwa mmoja wa kisiasa kutoka Latvia ambaye alifungwa miaka minne katika kambi ya wanawake ya Potma. Aliandika hivi baada ya kufunguliwa mwaka wa 1966: “Kwa njia fulani Mashahidi waliendelea kupata vichapo vingi.” Amalizia hivi: “Ni kana kwamba malaika waliruka kambini na kudondosha vichapo hivyo.” Kwa kweli, tulitimiza kazi hiyo kwa msaada wa Mungu tu!

  • Nilimtumikia Mungu Licha ya Magumu
    Amkeni!—2005 | Aprili 22
    • Kisha, mwaka wa 1983 Lidia alipokuwa na umri wa miaka kumi, mtu mmoja aliyekuwa Shahidi zamani alinisaliti kwa polisi wa KGB. Kufikia wakati huo, nilikuwa nimetumikia nikiwa mwangalizi anayesafiri kwa miaka kumi hivi kotekote mashariki mwa Ukrainia. Wale waliopinga utendaji wetu wa Kikristo waliwakusanya watu fulani ili watoe ushahidi wa uwongo wakati wa kusikizwa kwa kesi, nikahukumiwa kifungo cha miaka mitano.

      Nilipokuwa gerezani sikuruhusiwa kushirikiana na Mashahidi wengine. Hata hivyo, hakuna kitu au mtu yeyote angeweza kunizuia kumfikia Yehova, na sikuzote alinitia nguvu. Zaidi ya hayo, nilipata nafasi za kuwahubiria wafungwa wengine. Hatimaye, baada ya kukaa gerezani kwa miaka minne, niliachiliwa na kuungana tena na mke na binti yangu, ambao walidumisha uaminifu wao kwa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki