-
Afrika Kusini2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
MSIMAMO WA KUTOKUWAMO UNAJARIBIWA
Afrika Kusini ilijitenga na Jumuiya ya Madola ya Uingereza na kuwa jamhuri Mei 1961. Wakati huo, kulikuwa na msukosuko wa kisiasa na ongezeko la jeuri nchini. Ili kudhibiti hali, serikali ilichochea roho ya uzalendo, na jambo hilo liliwaletea shida Mashahidi wa Yehova katika miaka iliyofuata.
Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova hawakulazimishwa watumikie katika jeshi. Lakini hali ilibadilika mwishoni mwa miaka ya 1960, Afrika Kusini ilipohusika zaidi katika shughuli za kijeshi nchini Namibia na Angola. Sheria mpya ilisema kwamba kila kijana mzungu mwenye afya anapaswa kutumikia jeshini. Ndugu waliokataa walihukumiwa kifungo cha siku 90 katika kambi ya kijeshi.
Mike Marx alikuwa miongoni mwa ndugu waliofungwa na kuagizwa wavae mavazi na kofia za kijeshi. Anakumbuka hivi: “Kwa sababu hatukutaka kuonwa kuwa wanajeshi, tulikataa. Basi, ofisa mkuu, ambaye alikuwa kapteni, akaamuru tunyimwe haki zetu, kila mmoja afungwe peke yake, na kupata chakula kidogo tu.” Kwa hiyo, akina ndugu hawangeweza kuandika wala kupokea barua, kupata wageni, wala kuwa na vichapo vyovyote ila Biblia. Chakula hicho kidogo, kilichokusudiwa hasa wafungwa wenye vichwa vigumu, kilikuwa maji na nusu-mkate kila siku kwa siku mbili halafu chakula cha kawaida cha wanajeshi kwa siku saba, kisha maji na mkate kwa siku mbili tena. Mara nyingi, hata chakula hicho cha kawaida kilikuwa kibovu, nacho hakikutosha.
Utimilifu wa akina ndugu ulijaribiwa vikali. Kila mmoja wao alifungiwa katika chumba kidogo. Wakati mmoja, hawakuruhusiwa kuoga kwa maji yanayotiririka kutoka kwenye mfereji. Badala yake, kila ndugu alipewa ndoo mbili, moja ya kuendea haja na nyingine ya kuogea. Baada ya muda, waliruhusiwa tena kuoga kwa maji yanayotiririka kutoka kwenye mfereji.
Keith Wiggill anakumbuka hivi: “Siku moja, baada ya kuoga kwa maji baridi katika majira ya baridi kali, walinzi walitunyang’anya magodoro na mablanketi yetu. Hawakuturuhusu tuvae mavazi yetu ya raia, hivyo tukavaa suruali fupi na fulana tu. Tulilalia taulo iliyolowa maji kwenye sakafu baridi kama barafu. Asubuhi, ofisa mmoja wa kijeshi alishangaa kuona kwamba tulikuwa wazima na wenye furaha. Alikubali kwamba Mungu wetu alitutunza usiku huo wenye baridi kali.”
Muda mfupi kabla ya kumaliza kifungo chao cha siku 90, ndugu hao walipelekwa mahakamani tena kwa sababu walikataa kuvaa mavazi ya kijeshi na kufanya mazoezi pamoja na wafungwa wengine wa kijeshi. Kisha wakarudishwa gerezani. Wenye mamlaka walisema wazi kwamba lengo lao ni ndugu hao wafungwe tena na tena mpaka watakapokuwa na umri wa miaka 65, wakati ambapo hawangestahili tena kutumikia jeshini.
Mwaka wa 1972, sheria ilibadilishwa baada ya raia na wanasiasa kuteta vikali. Akina ndugu walihukumiwa kifungo kimoja ambacho kinalingana na muda wa kupata mazoezi ya kijeshi. Mwanzoni, kifungo hicho kilikuwa cha kati ya miezi 12 na 18. Halafu, muda huo ukaongezwa kufikia miaka mitatu na mwishowe miaka sita. Baadaye, wenye mamlaka walilegeza mambo kidogo, na ndugu hao wakaruhusiwa kufanya mkutano mmoja kwa juma.
Walipokuwa gerezani, akina ndugu hawakusahau amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Waliwahubiria wafungwa wenzao, wenye mamlaka, na watu wengine waliokutana nao. Kwa kipindi fulani, kila Jumamosi alasiri waliruhusiwa kuhubiri habari njema kwa kuandika barua.
Wakati mmoja, wenye mamlaka katika jeshi waliwaamuru Mashahidi hao 350 kula pamoja na wafungwa 170 wa kijeshi. Ni katika kambi hiyo ya kijeshi tu ambapo kulikuwa na Mashahidi wawili kati ya kila mtu mmoja ambaye si Shahidi, na baada ya muda wenye mamlaka waliamua akina ndugu wawe wakila peke yao.
JUMUIYA YA WAKRISTO NA MSIMAMO WA KUTOKUWAMO
Jumuiya ya Wakristo ilionaje suala la kulazimishwa kutumikia jeshini? Mnamo Julai 1974, Baraza la Makanisa la Afrika Kusini (SACC) lilipitisha azimio la kukataa kutumikia jeshini kwa sababu ya dhamiri. Hata hivyo, badala ya kuzungumzia suala hilo kwa upande wa kidini tu, azimio hilo liliingilia mambo fulani ya kisiasa. Liliunga mkono haki ya kukataa kutumikia jeshini kwa sababu jeshi lilikuwa likilinda “jamii isiyofuatia haki na yenye ubaguzi” na hivyo lilikuwa likipigana vita visivyo vya haki. Dini za Kiafrikana, na dini nyingine pia, hazikuunga mkono azimio la baraza hilo.
Kanisa la Dutch Reformed liliunga mkono shughuli za kijeshi za serikali. Kanisa hilo lilipinga azimio la Baraza la Makanisa la Afrika Kusini na kusema kwamba linavunja amri iliyo katika Waroma sura ya 13. Msimamo wa baraza hilo ulipingwa pia na makasisi waliotumikia katika Jeshi la Afrika Kusini, ambalo lilikuwa na makasisi wa makanisa yaliyo katika baraza hilo. Katika taarifa fulani waliyoitayarisha pamoja, makasisi wa makanisa ya Kiingereza walishutumu azimio hilo na kusema: “Tunamsihi kila mfuasi wa makanisa yetu, na hasa vijana, wajitoe kuilinda nchi yetu.”
Isitoshe, makanisa mojamoja ya baraza hilo hayakuchukua msimamo ulio wazi kuhusu suala la kutokuwamo. Kitabu kimoja (War and Conscience in South Africa) kinasema hivi: “Makanisa mengi . . . hayakuwatangazia wafuasi wao msimamo wao wala kuwahimiza wasishiriki vita kwa sababu ya dhamiri.” Kitabu hicho kinasema makanisa yaliogopa kutetea msimamo wao kwa sababu serikali ilipinga vikali azimio la baraza hilo na kutunga sheria kali. Kinasema hivi: “Haikuwezekana kulifanya kanisa lichukue hatua.”
Kwa upande mwingine, kitabu hicho kinasema: “Idadi kubwa ya waliofungwa kwa kukataa kutumikia jeshini kwa sababu ya dhamiri ni Mashahidi wa Yehova.” Kisha kinaongeza hivi: “Mashahidi wa Yehova walitetea haki za mtu za kupinga vita vyote kwa sababu ya dhamiri yake.”
Msimamo wa Mashahidi ulitegemea sababu za kidini tu. Ingawa Mashahidi wanakubali kwamba “mamlaka zilizopo zimesimamishwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri,” hawaungi mkono upande wowote wa siasa. (Rom. 13:1) Wao wanamtii kwanza Yehova, ambaye katika Neno lake Biblia anasema kwamba waabudu wake wa kweli hawapaswi kushiriki vita.—Isa. 2:2-4; Mdo. 5:29.
Baada ya mfumo huo wa kuwafunga watu wanaokataa kutumikia jeshini kuendelea kwa miaka kadhaa, ilionekana wazi kwamba Mashahidi wa Yehova hawawezi kukana msimamo wao wa kutokuwamo ili waepuke kutendewa kwa ukatili. Zaidi ya hayo, magereza katika kambi za kijeshi yalijaa kupita kiasi na kupata sifa mbaya. Maofisa fulani wa serikali walisisitiza akina ndugu wapelekwe katika magereza ya raia.
Maofisa fulani wa kijeshi wenye nia nzuri walikataa. Waliwaheshimu ndugu zetu vijana kwa sababu ya maadili yao mema. Ikiwa akina ndugu wangepelekwa katika gereza la raia, ingesemekana kuwa wamewahi kutenda uhalifu. Pia, wangefungiwa pamoja na wahalifu wabaya zaidi na kukabili hatari ya kunajisiwa. Basi, ilipangwa wafanye kazi ya kujitolea katika wizara za serikali ambazo si za kijeshi. Hali ya kisiasa ya Afrika Kusini ilipobadilika katika miaka ya 1990, haikuwa lazima tena kutumikia jeshini.
Ndugu zetu vijana waliathiriwaje walipofungwa kwa muda mrefu katika kipindi cha maana maishani mwao? Wengi wao walimtumikia Yehova kwa ushikamanifu na kutumia nafasi hiyo kwa hekima kujifunza Neno la Mungu na kukua kiroho. “Maisha yangu yalibadilika nilipokuwa gerezani katika kambi ya kijeshi,” asema Cliff Williams. “Kuona waziwazi jinsi Yehova alivyonilinda na kunibariki nilipokuwa gerezani kulinichochea nifanye mengi zaidi kuendeleza kazi ya Ufalme. Nilianza upainia wa kawaida muda mfupi baada ya kuachiliwa mwaka wa 1973, kisha mwaka uliofuata nikaingia Betheli, ambako ninaendelea kutumikia hadi leo hii.”
Stephen Venter, ambaye alikuwa na umri wa miaka 17 alipofungwa katika kambi ya kijeshi, alisema hivi: “Nilikuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, nami sikuwa na ujuzi mwingi kuhusu kweli. Nilivumilia kwa sababu ya msaada wa kiroho niliopata kupitia mikutano, kufundishwa Biblia na ndugu mwenye uzoefu, na mazungumzo ya andiko la kila siku ambayo tulifanya asubuhi tulipokuwa tuking’arisha sakafu. Ingawa kulikuwa na nyakati ngumu, ni ajabu kwamba sikumbuki sana pindi hizo! Huenda hata ile miaka mitatu niliyokaa gerezani ndiyo miaka bora ya maisha yangu. Mambo niliyokabili wakati huo yalinisaidia kukomaa. Nilipata kumjua Yehova, na hilo lilinichochea kuanza utumishi wa wakati wote.”
Kuna faida iliyotokana na kuwafunga ndugu zetu isivyo haki. Gideon Benade, ambaye aliwatembelea ndugu hao walipokuwa gerezani katika kambi ya kijeshi, aliandika hivi: “Ninapokumbuka yaliyopita, ninatambua kwamba ushahidi mkubwa sana ulitolewa.” Uvumilivu wa ndugu zetu na ripoti nyingi za habari kuhusu kesi na hukumu waliyopata zilionyesha kwa njia isiyosahaulika msimamo wa kutokuwamo wa Mashahidi wa Yehova, ambao ulitambuliwa jeshini na kotekote nchini.
-
-
Afrika Kusini2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 114-117]
Kudumisha Utimilifu Gerezani
MAHOJIANO NA ROWEN BROOKES
ALIZALIWA 1952
ALIBATIZWA 1969
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa gerezani kuanzia Desemba 1970 hadi Machi 1973 kwa sababu ya kutokuwamo kwa Kikristo. Alianza upainia wa kawaida mwaka wa 1973 na kwenda Betheli mwaka wa 1974. Sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi.
Hali zilikuwaje gerezani?
Kambini kulikuwa na majengo makubwa, kila moja likiwa na safu mbili za vyumba 34, na mtaro wa maji katikati ya majengo. Katika vifungo vya upweke, kila mmoja wetu alikuwa na chumba chenye urefu wa mita 2 na upana wa mita 1.8. Tuliruhusiwa kutoka katika vyumba vyetu mara mbili tu kwa siku: asubuhi ili kunawa, kunyoa ndevu, na kuosha ndoo zetu tulizotumia kama vyoo na wakati wa alasiri ili kuoga. Hatukuruhusiwa kuandika wala kupokea barua. Hatukuruhusiwa kuwa na vitabu vyovyote ila Biblia na hatukuruhusiwa kuwa na kalamu wala penseli zozote. Hatukuruhusiwa kuwa na wageni wowote.
Kabla ya kufungwa, ndugu wengi walikuwa na Biblia zilizounganishwa na vitabu vingine, kama vile Aid to Bible Understanding. Walinzi hawakutambua kwa kuwa zilifanana na Biblia zao za zamani za Kiafrikana au Kidachi.
Je, mlikuwa mkipata vichapo vya Biblia?
Ndiyo, wakati wowote ambapo ingewezekana, tuliviingiza kisiri. Vitu vyote tulivyokuwa navyo, kutia ndani sabuni, mafuta, dawa ya meno, na kadhalika, vilikuwa ndani ya mifuko katika mojawapo ya vyumba ambavyo havikuwa na mtu. Mara moja kwa mwezi, mlinzi alituruhusu kwenda katika jela hilo kuchukua vitu tulivyohitaji. Pia, tuliweka vichapo katika mifuko hiyo.
Mmoja wetu alimkengeusha mlinzi kwa kuzungumza naye, huku ndugu mwingine akificha kitabu ndani ya suruali au fulana. Tuliporudi katika vyumba vyetu tulitenganisha visehemu vidogo-vidogo vya vitabu hivyo, ili iwe rahisi kuvificha. Tulipokezana visehemu hivyo ili wote wavisome. Tulipata sehemu nyingi za kuvificha. Vyumba kadhaa vilikuwa vimeharibika sana, navyo vilikuwa na mianya kila mahali.
Vyumba vyetu vilipekuliwa kila wakati, nyakati nyingine hata usiku wa manane. Sikuzote walinzi walipata baadhi ya vichapo lakini kamwe hawakupata kila kitu. Mara nyingi askari mmoja aliyetujali alitutahadharisha wakati ambapo upekuzi ungefanywa. Kisha, tungefunga vichapo hivyo katika plastiki na kuvishindilia katika mabomba ya kuondoa maji machafu. Siku moja kulikuwa na mvua kubwa, na ajabu ni kwamba kifurushi kimoja kilikuja kikielea katika mtaro uliokuwa katikati ya majengo. Baadhi ya wafungwa waliokuwa wanajeshi walianza kukichezea kama mpira. Ghafula mlinzi alikuja na kuwaambia warudi katika vyumba vyao. Tulifurahi kwamba hakuna mtu aliyejishughulisha na kifurushi hicho, na hivyo tuliweza kukichukua tuliporuhusiwa kutoka nje ya majela yetu muda mfupi baadaye.
Je, utimilifu wenu ulijaribiwa mlipokuwa gerezani?
Wakati wote. Kila wakati maofisa wa gereza walijaribu njama fulani. Kwa mfano, wangejifanya wazuri kwetu, yaani, wangetupatia chakula cha ziada, wangetupeleka kufanya mazoezi, na hata kuturuhusu tuote jua. Kisha, baada ya siku chache wangetuamuru tuvae nguo za kijeshi. Tulipokataa, walitutendea kikatili kama mwanzoni.
Baada ya hayo, tuliambiwa tuvae kofia za plastiki za kijeshi, nasi tukakataa. Msimamizi alikasirika sana hivi kwamba kuanzia wakati huo hata hakuturuhusu tuoge kwa maji yanayotiririka. Kila mmoja wetu alipewa ndoo ambayo angetumia kuoga ndani ya chumba chake.
Kwa sababu hatukuwa na viatu, miguu ya akina ndugu fulani ilikuwa na vidonda. Ilitubidi tujitengenezee viatu. Tuliokota vipande vya mablanketi makuukuu yaliyotumiwa kung’arisha sakafu. Halafu tukapata waya wa shaba, tukatandaza mwisho mmoja, na kunoa ule mwingine. Tulitumia pini kutoboa shimo katika sehemu iliyotandazwa ya waya na kuitumia waya hiyo kama sindano ya kushonea. Tulitoa nyuzi kwenye mablanketi yetu na kuzitumia kushona viatu tukitumia vipande vya blanketi.
Bila kujua sababu, tuliamuriwa tukae watatu-watatu katika chumba kimoja. Ingawa tulisongamana, tulifaidika. Tulipanga kwamba ndugu walio dhaifu kiroho wakae na wenye uzoefu. Tuliongoza mafunzo ya Biblia na kufanya mazoezi ya kuhubiri. Msimamizi alishangaa kuona kwamba tulikuwa na uhakika zaidi.
Alipotambua kwamba mbinu hiyo iliambulia patupu, msimamizi huyo aliamuru kwamba kila Shahidi akae na watu wawili wasio Mashahidi. Ingawa walikuwa wameonywa vikali wasizungumze nasi, walianza kuuliza maswali na tulikuwa na wakati wa kutosha kutoa ushahidi. Matokeo yakawa kwamba mmoja au wawili kati ya wafungwa wenzetu walikataa kujihusisha katika utendaji fulani wa kijeshi. Punde si punde, tulianza tena kuishi kila mtu katika chumba chake.
Je, mliweza kufanya mikutano?
Tulifanya mikutano yetu kwa ukawaida. Juu ya mlango wa kila chumba kulikuwa na dirisha lenye wavu wa waya na fito saba zilizo wima. Tulikalia kiti cha kuning’inia tulichotengeneza kwa kufunga miisho miwili ya blanketi kwenye fito mbili. Tukiwa huko juu tungeweza kumwona ndugu katika chumba kilichokuwa upande ule mwingine, nasi tungeweza kupaaza sauti na kusikiwa na wengine katika jengo hilo. Tulichunguza andiko la kila siku, na pia tulijifunza Mnara wa Mlinzi iwapo tungekuwa na gazeti hilo. Kila siku tulimalizia kwa sala ya hadharani tuliyotoa kwa zamu. Hata tulijitayarishia programu ya kusanyiko la mzunguko.
Hatukuwa na uhakika iwapo mzee angeruhusiwa kuja kuhudhuria Ukumbusho pamoja nasi. Hivyo, tulifanya matayarisho yetu wenyewe. Tulitengeneza divai kwa kulowesha zabibu kadhaa ndani ya maji, na kutandaza na kuukausha mkate tuliopokea. Wakati mmoja tuliruhusiwa kupokea chupa ndogo ya divai na mikate kadhaa isiyotiwa chachu kutoka kwa akina ndugu huko nje.
Je, mambo yalibadilika?
Ndiyo, baada ya muda mambo yalikuwa afadhali. Sheria ilibadilishwa na kikundi chetu kikaachiliwa. Kuanzia wakati huo na kuendelea, watu waliokataa kutumikia jeshini kwa sababu ya dini walihukumiwa kifungo kimoja kwa kipindi hususa bila kuhukumiwa tena. Baadaye, baada ya kikundi chetu cha ndugu 22 kuachiliwa, ndugu 88 waliobaki gerezani walitendewa kama wafungwa wengine. Wangeweza kutembelewa mara moja kwa mwezi na hata kuandika na kupokea barua.
Je, baada ya kuachiliwa, ilikuwa rahisi kurudia maisha ya kawaida?
Hapana, ilichukua muda kuzoea maisha tukiwa huru. Kwa mfano, hatukuhisi huru tulipokuwa mahali penye watu wengi. Hatua kwa hatua wazazi na ndugu zetu walitusaidia kwa fadhili kukubali mapendeleo zaidi kutanikoni.
Ingawa huo ulikuwa wakati mgumu, tulifaidika kutokana na mambo tuliyokabili. Majaribu ya imani tuliyokabili yalituimarisha kiroho na kutufunza uvumilivu. Kwa kweli, tulijifunza kuithamini Biblia na kuona faida ya kuisoma na kuitafakari kila siku. Na bila shaka tulijifunza kumtegemea Yehova. Baada ya kujidhabihu hivyo ili kubaki waaminifu kwa Yehova, tuliazimia kuendelea kuvumilia, tukijitoa kabisa kwake kwa kutumikia katika utumishi wa wakati wote ilipowezekana.
-