Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Yehova, Mungu Mwenye Rehema na Neema”
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Oktoba 1
    • Yesu alisimulia kielezi chake cha tatu kwa kutumia mfano wenye somo.a Kielezi hicho kimeonwa na wengi kuwa simulizi fupi lililo bora zaidi lililowahi kusimuliwa. Kufikiria mfano huo wenye somo kutatusaidia kumthamini na kuiga rehema ya Mungu.—Luka 15:3-10.

      Mwana Mwasi Aondoka Nyumbani

      5, 6. Mwana aliye kijana zaidi katika kielezi cha tatu cha Yesu alionyeshaje ukosefu wa uthamini wenye kushtua?

      5 “Mtu fulani alikuwa na wana wawili. Na yule kijana zaidi kati yao akamwambia baba yake, ‘Baba, nipe sehemu ya mali iliyo fungu langu.’ Ndipo yeye akawagawia njia zake za kujipatia riziki. Baadaye, baada ya siku zisizokuwa nyingi, huyo mwana aliye kijana zaidi alikusanya pamoja vitu vyote akasafiri nchi ya nje akaingia katika nchi ya mbali, na huko akafuja mali yake kwa kuishi maisha ya ufasiki.”—Luka 15:11-13.b

      6 Hapa mwana aliye kijana zaidi alionyesha ukosefu wa uthamini wenye kushtua. Kwanza, alidai apewe urithi wake, kisha akaufuja “kwa kuishi maisha ya ufasiki.” Usemi “maisha ya ufasiki” umetafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki limaanishalo “maisha mapotovu.” Msomi mmoja asema kwamba neno hilo “laonyesha hali ya kuacha kabisa ubora wa kiadili.” Kwa sababu nzuri, mara kwa mara huyo mwanamume kijana katika mfano wa Yesu wenye somo huitwa mwana mpotevu, neno lifafanualo mtu ambaye hutumia mali ovyoovyo na kwa kuziharibu.

      7. Ni nani leo wanaofanana na mwana mpotevu, na ni kwa nini wengi wao hutafuta uhuru katika “nchi ya mbali”?

      7 Je, leo kuna watu wanaofanana na mwana mpotevu? Ndiyo. Kwa kusikitisha, idadi ndogo kwa kulinganishwa imeacha “nyumba” yenye usalama ya Baba wetu wa kimbingu, Yehova. (1 Timotheo 3:15) Baadhi yao huhisi kwamba hali katika nyumba ya Mungu ni yenye vizuizi vingi mno na kwamba jicho la Yehova lenye uangalifu ni kizuizi wala si ulinzi. (Linganisha Zaburi 32:8.) Fikiria mwanamke mmoja Mkristo aliyelelewa kulingana na kanuni za Biblia lakini baadaye akaanza kutumia vibaya kileo na madawa ya kulevya. Akikumbuka kipindi hicho chenye kuhuzunisha cha maisha yake, yeye asema: “Nilitaka kuthibitisha kwamba mimi binafsi ningeweza kuboresha maisha yangu. Nilitaka kufanya nilivyotaka, na sikutaka yeyote aniambie nifanye vinginevyo.” Kama mwana mpotevu, mwanamke huyu kijana alitafuta uhuru. Kwa kuhuzunisha, ilibidi aondoshwe kutoka katika kutaniko la Kikristo kwa sababu ya mazoea yake yasiyo ya Kimaandiko.—1 Wakorintho 5:11-13.

      8. (a) Ni msaada gani uwezao kutolewa kwa wale wanaotamani kuishi kinyume na viwango vya Mungu? (b) Kwa nini mtu apaswa kufikiria kwa makini chaguo analofanya kuhusiana na ibada?

      8 Inahuzunisha sana wakati mwamini mwenzi anapodhihirisha tamaa ya kuishi kinyume na viwango vya Mungu. (Wafilipi 3:18) Jambo hilo litokeapo, wazee na wengineo wenye sifa za ustahili za kiroho hujaribu kumrekebisha upya mkosaji. (Wagalatia 6:1) Hata hivyo, hakuna yeyote ambaye hulazimishwa kukubali nira ya uanafunzi wa Kikristo. (Mathayo 11:28-30; 16:24) Ni lazima hata vijana wafanye chaguo la kibinafsi kuhusiana na ibada wafikiapo umri wa utu mzima. Mwishowe, kila mmoja wetu ana uhuru wa kuchagua naye atatoa hesabu yake mwenyewe kwa Mungu. (Waroma 14:12) Bila shaka, ‘tutavuna pia tulilopanda,’ somo ambalo mwana mpotevu katika mfano wa Yesu wenye somo alikuwa ajifunze punde.—Wagalatia 6:7, 8.

      Kukata Tamaa Katika Nchi ya Mbali

      9, 10. (a) Mwana mpotevu alipatwa na badiliko gani la hali, naye alitendaje kulihusu? (b) Toa kielezi cha jinsi ambavyo wengine leo ambao huacha ibada ya kweli hupatwa na hali mbaya sawa na iliyompata mwana mpotevu.

      9 “Alipokuwa ametumia kila kitu, njaa kali sana ilitokea kotekote katika nchi hiyo, naye akaanza kuwa katika uhitaji. Hata alienda na kujiambatanisha mwenyewe kwa mmoja wa raia wa nchi hiyo, naye akamtuma aingie katika mashamba yake ili achunge mifugo ya nguruwe. Naye alikuwa na kawaida ya kutamani kushibishwa kwa matumba ya mkarobu ambayo hao nguruwe walikuwa wakila, na hakuna yeyote aliyekuwa akimpa kitu chochote.”—Luka 15:14-16.

      10 Ingawa alikuwa fukara, mwana mpotevu bado hakufikiria kurudi nyumbani. Badala yake, alifahamiana na raia fulani aliyemwajiri kazi ya kuchunga nguruwe. Kwa kuwa Sheria ya Kimusa ilisema kwamba nguruwe walikuwa wanyama wasio safi, yaelekea Myahudi hangekubali kazi kama hiyo. (Mambo ya Walawi 11:7, 8) Lakini ikiwa dhamiri ya mwana mpotevu ilimsumbua, ilimbidi aizime. Kwa vyovyote, hangeweza kumtarajia mwajiri wake, raia wa mahali hapo, ahangaishwe na hisia za mtoka-ugenini aliye fukara. Hali hiyo mbaya ya mwana mpotevu iko sawa na ile inayowapata watu wengi leo ambao huacha njia iliyonyoka ya ibada safi. Mara nyingi, watu hao hujishughulisha na mambo ambayo hapo awali wangeyafikiria kuwa yenye kushusha. Kwa kielelezo, akiwa na umri wa miaka 17, mwanamume mmoja kijana alikaidi malezi yake ya Kikristo. “Kukosa maadili na matumizi mabaya ya dawa za kulevya yalibatilisha miaka mingi ya mafundisho yaliyotegemea Biblia,” yeye akubali. Punde si punde, mwanamume huyo kijana alijipata gerezani kwa sababu ya unyang’anyi wa kutumia silaha na uuaji kimakusudi. Ingawa baadaye alipata nguvu tena kiroho, alipatwa na mateso makubwa kama nini kwa sababu ya “mfurahio wa muda wa dhambi”!—Linganisha Waebrania 11:24-26.

      11. Tatizo la mwana mpotevu lilifanywaje kuwa baya zaidi, na wengine leo wametambuaje kwamba vivutio vya ulimwengu ni “udanganyo mtupu”?

      11 Tatizo la mwana mpotevu lilifanywa kuwa baya zaidi na uhakika wa kwamba “hakuna yeyote aliyekuwa akimpa kitu chochote.” Marafiki aliokuwa amepata karibuni walikuwa wapi? Kwa vile sasa alikuwa hana hata ndururu, kwao alikuwa kama “kitu cha kuchukiwa.” (Mithali 14:20, NW) Hali kadhalika, watu wengi leo ambao hupotea njia na kuacha imani hutambua kwamba vivutio na maoni ya ulimwengu huu ni sawa na “udanganyo mtupu.” (Wakolosai 2:8) “Bila mwongozo wa Yehova, nilipatwa na maumivu na huzuni nyingi,” asema mwanamke mmoja kijana ambaye aliacha tengenezo la Mungu kwa muda fulani. “Nilijaribu kujipatanisha na ulimwengu, lakini kwa sababu kwa kweli nilikuwa tofauti na wengine, walinikataa. Nilijihisi kama mtoto aliyepotea ambaye alihitaji baba wa kumwongoza. Ndipo nilipotambua kwamba nilimhitaji Yehova. Sikutaka kamwe kuishi bila kumtegemea.” Mwana mpotevu katika kielezi cha Yesu alitambua jambo lililo sawa na hilo.

      Mwana Mpotevu Arudiwa na Fahamu Zake

      12, 13. Ni mambo gani ambayo yamesaidia watu fulani leo warudie fahamu zao? (Ona Sanduku.)

      12 “Aliporudiwa na fahamu zake, alisema, ‘Ni wanaume wangapi walioajiriwa wa baba yangu ambao wanazidi katika kuwa na mkate, na huku mimi ninaangamia hapa kutokana na njaa kali! Hakika mimi nitainuka nifunge safari niende kwa baba yangu na kumwambia: “Baba nimefanya dhambi dhidi ya mbingu na dhidi yako wewe. Sistahili tena kuitwa mwana wako. Unifanye kama mmoja wa watu wako walioajiriwa.”’ Kwa hiyo akainuka akamwendea baba yake.”—Luka 15:17-20.

      13 Mwana mpotevu ‘alirudiwa na fahamu zake.’ Kwa muda, mwana mpotevu alikuwa amejiingiza katika kutafuta anasa, kana kwamba alikuwa katika ulimwengu usio halisi. Lakini sasa alifahamu kabisa hali yake halisi ya kiroho. Ndiyo, hata ingawa alikuwa amejikwaa, bado kulikuwa na tumaini kwa mwanamume huyu kijana. Alikuwa na sifa fulani nzuri. (Mithali 24:16; linganisha 2 Mambo ya Nyakati 19:2, 3.) Namna gani wale wanaoliacha kundi la Mungu leo? Je, lingekuwa jambo lenye kupatana na akili kukata kauli kwamba, wote hao hawana tumaini kabisa, kwamba kwa vyovyote mwendo wao wa kuasi wathibitisha kwamba wamefanya dhambi dhidi ya roho takatifu ya Mungu? (Mathayo 12:31, 32) Si lazima iwe hivyo. Baadhi yao huumizwa sana na mwendo wao mkaidi, na hatimaye wengi wao hurudiwa na fahamu zao. “Sikumsahau Yehova kamwe, hata siku moja,” asema dada mmoja, akikumbuka muda aliokaa nje ya tengenezo la Mungu. “Sikuzote nilisali kwamba kwa njia fulani, siku moja angenikubali niirudie kweli.”—Zaburi 119:176.

      14. Mwana mpotevu aliazimia kufanya nini, naye alionyeshaje unyenyekevu katika kufanya hivyo?

      14 Lakini wale ambao wamepotea njia waweza kufanya nini kuhusu hali yao? Katika mfano wa Yesu wenye somo, mwana mpotevu aliamua kufunga safari ya kurudi nyumbani na kumwomba baba yake msamaha. “Unifanye kama mmoja wa watu wako walioajiriwa,” mwana mpotevu akaazimia kusema hivyo. Mtumishi aliyeajiriwa alikuwa kibarua, ambaye angeweza kufukuzwa baada ya kuarifiwa siku moja kimbele. Hiyo ilikuwa hali ya chini kuliko ya mtumwa ambaye, katika maana fulani, alikuwa kama mshiriki wa familia. Kwa hiyo, mwana mpotevu hakufikiria kuomba arudishwe kwenye hali yake ya zamani akiwa mwana. Angekuwa tayari kabisa kukubali hali ya chini zaidi, ili athibitishe upya uaminifu-mshikamanifu wake kwa baba yake siku kwa siku. Hata hivyo, mwana mpotevu alikuwa ashangae.

      Mapokezi Yenye Uchangamfu

      15-17. (a) Baba huyo alitendaje alipomwona mwana wake? (b) Kanzu, pete, na makubazi ambayo baba alimvika mwana wake vinamaanisha nini? (c) Baba anaonyesha nini kwa kutayarisha karamu?

      15 “Alipokuwa angali mbali sana, baba yake alimwona mara hiyo naye akasukumwa na sikitiko, naye akakimbia akaangukia shingo yake na kumbusu kwa wororo. Ndipo yule mwana akamwambia, ‘Baba, nimefanya dhambi dhidi ya mbingu na dhidi yako. Sistahili tena kuitwa mwana wako. Unifanye niwe kama mmoja wa wanaume wako walioajiriwa.’ Lakini yule baba akawaambia watumwa wake, ‘Upesi! leteni nje kanzu, iliyo bora zaidi, mmvike hiyo, na mtie pete mkononi mwake na makubazi miguuni mwake. Nanyi leteni fahali mchanga aliyenoneshwa, mchinjeni na acheni tule na kujifurahisha wenyewe, kwa sababu huyu mwana wangu alikuwa amekufa naye akaja tena kwenye uhai; alikuwa amepotea naye akapatikana.’ Nao wakaanza kujifurahisha wenyewe.”—Luka 15:20-24.

      16 Mzazi yeyote mwenye upendo angetamani sana mtoto apate nguvu tena kiroho. Kwa sababu hiyo, twaweza tu kuwazia baba ya mwana mpotevu akitazama kila siku njia iliyokuwa mbele ya nyumba yake, akitumaini kwa hamu kurudi kwa mwana wake. Sasa amwona mwana wake njiani akija! Bila shaka sura ya mvulana huyo ilikuwa imebadilika. Hata hivyo, baba anamtambua alipokuwa “angali mbali sana.” Yeye anapuuza mavazi yaliyorarukararuka na hali ya kushuka moyo; yeye anamwona mwana wake, naye anakimbia kumlaki!

      17 Baba alipomfikia mwana wake, alimwangukia shingoni na kumbusu kwa wororo. Kisha akaamuru watumwa wake wamvike kanzu, pete, na makubazi. Kanzu hiyo haikuwa vazi la kawaida tu, bali ilikuwa kanzu “iliyo bora zaidi,” labda aina ya vazi rasmi lililorembeshwa sana ambalo lilitolewa kwa mgeni mheshimiwa. Kwa kuwa kwa kawaida pete na makubazi hayakuvaliwa na watumwa, baba alikuwa akidhihirisha kwamba mwana wake alikuwa akikaribishwa arudi akiwa mshiriki kamili wa familia. Lakini baba alifanya mengi hata zaidi. Aliagiza kuwe na karamu ya kusherehekea kurudi kwa mwana wake. Kwa wazi, mwanamume huyu hakumsamehe mwana wake shingo upande au kwa sababu kurudi kwake kulimlazimisha afanye hivyo; alitaka kumsamehe. Jambo hilo lilimfanya ashangilie.

      18, 19. (a) Mfano wenye somo wa mwana mpotevu unakufunza nini kuhusu Yehova? (b) Yehova ‘hungojaje’ kurudi kwa mtenda-dhambi kama ionyeshwavyo na shughuli zake na Yuda na Yerusalemu?

      18 Kufikia hapo, mfano wenye somo wa mwana mpotevu hutufunza nini kuhusu Mungu ambaye tunapendelewa kumwabudu? Kwanza, tunajifunza kwamba Yehova “ni mwenye rehema na neema, asiye mwepesi wa hasira na mwingi wa fadhili-upendo na kweli.” (Kutoka 34:6, NW) Kwa kweli, rehema ni sifa kuu ya Mungu. Ni njia yake ya kawaida ya kuwaonyesha hisia walio na uhitaji. Basi, mfano wa Yesu wenye somo watufundisha kwamba Yehova yu “tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Yeye yu macho, kusema kitamathali, ili kuona badiliko lolote la maoni ya wanadamu wenye dhambi ambalo lingemwandalia msingi wa kuonyesha rehema.—2 Mambo ya Nyakati 12:12; 16:9.

      19 Kwa kielelezo, fikiria shughuli za Mungu pamoja na Israeli. Nabii Isaya alipuliziwa na Yehova afafanue Yuda na Yerusalemu kuwa na ‘ugonjwa tangu kichwani hadi wayo wa mguu.’ Hata hivyo, yeye pia alisema: “BWANA atangoja, ili awaonee huruma, na kwa ajili ya hayo atatukuzwa, ili awarehemu.” (Isaya 1:5, 6; 30:18; 55:7; Ezekieli 33:11) Kama yule baba katika mfano wenye somo wa Yesu, Yehova ‘hutazama njia,’ kusema kitamathali. Anatazamia kwa hamu kurudi kwa wowote wale ambao wameacha nyumba yake. Je, tusingetarajia baba mwenye upendo afanye hivyo?—Zaburi 103:13.

      20, 21. (a) Ni katika njia gani wengi leo huvutwa na rehema ya Mungu? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

      20 Kila mwaka, rehema ya Yehova huvuta wengi warudiwe na fahamu zao na kurudi kwenye ibada ya kweli. Hilo huletea wapendwa wao shangwe iliyoje! Kwa kielelezo, fikiria yule baba Mkristo aliyetajwa mwanzoni. Kwa kufurahisha, binti yake alipata nguvu tena kiroho na sasa hutumikia akiwa mhudumu wa wakati wote. “Ninafurahi kadiri iwezekanavyo mtu kufurahi katika mfumo huu wa mambo uliochakaa,” huyo baba asema. “Machozi yangu ya huzuni yamebadilishwa yakawa machozi ya shangwe.” Bila shaka, Yehova hushangilia pia!—Mithali 27:11.

      21 Lakini kuna mengi zaidi tuwezayo kujifunza kutokana na mfano wenye somo wa mwana mpotevu. Yesu aliendelea na simulizi lake ili aweze kutofautisha rehema ya Yehova na ule mtazamo mgumu wa kuhukumu uliokuwa wa kawaida miongoni mwa waandishi na Mafarisayo. Jinsi alivyofanya hivyo, na yale ambayo jambo hilo humaanisha kwetu, yatazungumziwa katika makala inayofuata.

  • Igeni Rehema ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Oktoba 1
    • Igeni Rehema ya Yehova

      “Endeleeni kuwa wenye rehema, sawa na vile Baba yenu ni mwenye rehema.”—LUKA 6:36.

      1. Mafarisayo walijionyeshaje kuwa bila rehema?

      MARA nyingi wanadamu hushindwa kuiga rehema ya Mungu ingawa waliumbwa kwa mfano wake. (Mwanzo 1:27) Kwa kielelezo, wafikirie Mafarisayo. Wakiwa kikundi, walikataa kushangilia wakati ambapo kwa rehema Yesu aliponya katika siku ya Sabato mkono wa mtu fulani ulionyauka. Badala yake, walifanya shauri dhidi ya Yesu “ili wapate kumwangamiza.” (Mathayo 12:9-14) Katika pindi nyingine, Yesu alimponya mtu aliyekuwa kipofu tangu kuzaliwa. Kwa mara nyingine tena, “baadhi ya Mafarisayo” walikosa sababu ya kushangilia huruma ya Yesu. Badala yake, walilalamika: “Huyu si mtu atokaye kwa Mungu, kwa sababu haishiki Sabato.”—Yohana 9:1-7, 16.

      2, 3. Yesu alimaanisha nini kwa taarifa, “Jiangalieni na chachu ya Mafarisayo”?

      2 Mtazamo usio na huruma wa Mafarisayo ulikuwa uhalifu dhidi ya jamii ya binadamu na dhambi dhidi ya Mungu. (Yohana 9:39-41) Akiwa na sababu nzuri, Yesu aliwaonya wanafunzi wake, “Jiangalieni na chachu” ya kikundi hiki chenye uwezo na wanadini wengine, kama vile Masadukayo. (Mathayo 16:6) Chachu hutumiwa katika Biblia kuwakilisha dhambi au ufisadi. Kwa hiyo, Yesu alikuwa akisema kwamba fundisho la “waandishi na Mafarisayo” lingeweza kufisidi ibada safi. Jinsi gani? Kwa kuwa lilifundisha watu waione Sheria ya Mungu kupatana tu na sheria na desturi zao ambazo hazikuwa na msingi maalum, huku wakipuuza “mambo yenye uzito zaidi,” kutia ndani rehema. (Mathayo 23:23) Aina hiyo ya dini ya kidesturi ilifanya ibada ya Mungu iwe mzigo wenye kulemea usioweza kuvumilika.

      3 Katika sehemu ya pili ya mfano wake wenye somo wa mwana mpotevu, Yesu alifichua kufikiri kwenye ufisadi kwa viongozi wa kidini Wayahudi. Katika mfano huo wenye somo, baba anayewakilisha Yehova alikuwa na hamu sana ya kumsamehe mwana wake mwenye kutubu. Lakini ndugu ya mvulana huyo aliye na umri mkubwa zaidi ambaye alifananisha “Mafarisayo na waandishi,” alikuwa na maoni tofauti kabisa juu ya jambo hilo.—Luka 15:2.

      Hasira ya Kisasi ya Ndugu

      4, 5. Ndugu ya mwana mpotevu alikuwa “amepotea” katika maana gani?

      4 “Sasa mwana wake mwenye umri mkubwa zaidi alikuwa katika shamba; naye alipokuja akaikaribia nyumba alisikia utumbuizo wa kimuziki na uchezaji-dansi. Kwa hiyo akaita mmoja wa watumishi kwake akaulizia habari mambo hayo yalimaanisha nini. Yeye akamwambia, ‘Ndugu yako amekuja, na baba yako amechinja fahali mchanga aliyenoneshwa, kwa sababu alimpata tena akiwa na afya njema.’ Lakini yeye akawa na hasira ya kisasi na hakutaka kuingia.”—Luka 15:25-28.

      5 Kwa wazi, katika mfano wa Yesu wenye somo, si mwana mpotevu pekee aliyekuwa na tatizo. “Wana wote wawili waliosimuliwa hapa wamepotea,” chasema kitabu kimoja cha marejezo, “mmoja kwa sababu ya ukosefu wa uadilifu ambao unamshusha, yule mwingine kwa sababu ya kujiona kuwa mwenye haki ambako kunampofusha.” Ona kwamba ndugu ya mwana mpotevu hakukataa kushangilia tu, bali pia “[aliku]wa na hasira ya kisasi.” Neno la msingi la Kigiriki limaanishalo “hasira ya kisasi” ladokeza, si mfoko tu wa hasira, bali hali inayodumu akilini. Yaonekana ndugu ya mwana mpotevu alikuwa na kinyongo cha kina kirefu, kwa hiyo hakuona kuwa ilifaa kusherehekea kurudi kwa mtu ambaye kwa kweli hakupaswa kamwe kuwa ameondoka nyumbani.

      6. Ndugu ya mwana mpotevu huwakilisha nani, na kwa nini?

      6 Ndugu ya mwana mpotevu anawakilisha vizuri wale walioonea uchungu huruma na uangalifu ambao Yesu aliwaonyesha watenda-dhambi. Watu hawa wenye kujiona kuwa waadilifu hawakuguswa moyo na rehema ya Yesu; wala hawakuonyesha shangwe ambayo hutokea mbinguni mtenda-dhambi anaposamehewa. Badala yake, rehema ya Yesu ilichochea hasira yao ya kisasi, nao wakaanza “[kufikiria] mambo maovu” mioyoni mwao. (Mathayo 9:2-4) Katika pindi moja hasira ya Mafarisayo fulani ilikuwa kali hivi kwamba walimwita mtu aliyekuwa ameponywa na Yesu, kisha “wakamfukuza nje” ya sinagogi, yaonekana wakimwondosha kabisa! (Yohana 9:22, 34) Kama ndugu ya mwana mpotevu ambaye “hakutaka kuingia,” viongozi wa kidini Wayahudi walisita walipopata fursa ya “[kushangilia] pamoja na watu washangiliao.” (Waroma 12:15) Huku akiendelea kusimulia mfano wake wenye somo, Yesu alifichua zaidi kusababu kwao kuovu.

      Kusababu Kwenye Kasoro

      7, 8. (a) Ndugu ya mwana mpotevu alishindwaje kuelewa maana ya uana? (b) Mwana mwenye umri mkubwa zaidi alikuwaje tofauti na baba yake?

      7 “Ndipo baba yake akatoka akaanza kumsihi sana. Kwa kujibu akamwambia baba yake, ‘Hii ni miaka mingi sana ambayo mimi nimekutumikia wewe kama mtumwa na kamwe hata mara moja sijakiuka amri yako, na bado kamwe hata mara moja hukunipa mwana-mbuzi ili mimi nijifurahishe mwenyewe pamoja na marafiki wangu. Lakini mara tu alipowasili huyu mwana wako aliyekula kabisa pamoja na makahaba njia zako za kujipatia riziki, ulimchinjia fahali mchanga aliyenoneshwa.’”—Luka 15:28-30.

      8 Kwa maneno hayo, ndugu ya mwana mpotevu alionyesha wazi kwamba alikuwa ameshindwa kuelewa maana halisi ya uana. Alimtumikia baba yake sawa na vile mwajiriwa anavyomtumikia mwajiri wake. Kama alivyomwambia baba yake: “Nimekutumikia wewe.” Ni kweli, mwana huyu mwenye umri mkubwa zaidi hakuwa amewahi kuondoka nyumbani au kukiuka amri ya baba yake. Lakini utii wake ulichochewa na upendo? Je, alipata shangwe ya kweli katika kumtumikia baba yake, au badala yake hatua kwa hatua alikuwa amekuwa mwenye kuridhika mno, akijiamini kuwa mwana mwema kwa sababu tu alitimiza wajibu wake mbalimbali “katika shamba”? Kama alikuwa mwana mwenye kujitoa, kwa nini alishindwa kuwa na maoni sawa na ya baba yake? Alipopewa fursa ya kumrehemu ndugu yake, kwa nini hakuwa na huruma yoyote moyoni mwake?—Linganisha Zaburi 50:20-22.

      9. Eleza jinsi viongozi Wayahudi walivyofanana na mwana mwenye umri mkubwa zaidi.

      9 Viongozi wa kidini Wayahudi walifanana na mwana huyo mwenye umri mkubwa zaidi. Waliamini kwamba walikuwa waaminifu-washikamanifu kwa Mungu kwa sababu walishikamana kabisa na mfumo wa sheria. Ni kweli, utii ni muhimu. (1 Samweli 15:22) Lakini kukazia kwao matendo kupita kiasi kuligeuza ibada ya Mungu ikawa kawaida isiyo na hisia, wonyesho wa nje tu wa ujitoaji usio na hali ya kiroho ya kweli. Akili zao zilijawa na mapokeo. Mioyo yao ilikuwa bila upendo. Kwani, waliwaona watu wa kawaida kama uchafu chini ya nyayo zao, hata wakiwarejezea kwa madharau kuwa “watu waliolaaniwa.” (Yohana 7:49) Mungu angewezaje kwa kweli kuvutiwa na matendo ya viongozi kama hao wakati ambapo mioyo yao ilikuwa imeondolewa mbali naye?—Mathayo 15:7, 8.

      10. (a) Kwa nini maneno, “Nataka rehema, wala si dhabihu” yalikuwa shauri lifaalo? (b) Ukosefu wa rehema ni jambo zito kadiri gani?

      10 Yesu aliwaambia Mafarisayo “nendeni . . . mjifunze kile ambacho hili lamaanisha, ‘Mimi nataka rehema, wala si dhabihu.’” (Mathayo 9:13; Hosea 6:6) Hawakupambanua mambo ya kutangulizwa, kwa maana bila rehema dhabihu zao zote zingekuwa zisizofaa kitu. Kwa kweli, jambo hilo ni zito, kwa maana Biblia yasema kwamba “wasio na rehema” huhesabiwa miongoni mwa wale wanaoonwa na Mungu kuwa “wanastahili kifo.” (Waroma 1:31, 32) Kwa hiyo, haishangazi kwamba Yesu alisema kwamba viongozi wa kidini wakiwa jamii walikusudiwa uharibifu wa milele. Kwa wazi, ukosefu wao wa rehema ulichangia sana kustahili kwao hukumu hiyo. (Mathayo 23:33) Lakini labda watu mmoja-mmoja kutoka katika jamii hiyo wangeweza kusaidiwa. Kwa kumalizia mfano huo wenye somo, Yesu alijitahidi kurekebisha upya kufikiri kwa Wayahudi hao kupitia mazungumzo ya baba na mwana wake mwenye umri mkubwa zaidi. Acheni tuone jinsi alivyofanya hivyo.

      Rehema ya Baba

      11, 12. Ni jinsi gani baba anajaribu kusababu na mwana wake mwenye umri mkubwa zaidi katika mfano wenye somo wa Yesu, naye huenda akawa alimaanisha nini kwa kutumia fungu la maneno “ndugu yako”?

      11 “Ndipo akamwambia, ‘Mtoto, wewe umekuwa pamoja nami sikuzote, na vitu vyote vilivyo vyangu ni vyako; lakini ilitupasa tu kujifurahisha wenyewe na kushangilia, kwa sababu huyu ndugu yako alikuwa amekufa naye akaja kwenye uhai, naye alikuwa amepotea naye akapatikana.’”—Luka 15:31, 32.

      12 Ona kwamba baba alitumia usemi “ndugu yako.” Kwa nini? Kumbuka kwamba hapo awali, alipozungumza na baba yake, huyo mvulana mwenye umri mkubwa zaidi alimwita mwana mpotevu “mwana wako,” wala hakumwita “ndugu yangu.” Hakuonekana kutambua kifungo cha kifamilia kilichokuwa kati yake mwenyewe na ndugu yake. Kwa hiyo, sasa kwa kweli baba anamwambia mvulana wake mwenye umri mkubwa zaidi hivi: ‘Huyu si mwana wangu tu. Yeye ni ndugu yako, mtu wa ukoo mmoja nawe. Una kila sababu ya kushangilia kurudi kwake!’ Ujumbe wa Yesu ulipaswa kuwa wazi kwa viongozi Wayahudi. Watenda-dhambi waliowadharau walikuwa kwa kweli “ndugu” zao. Kwa kweli, “hakuna mwanadamu mwenye haki hapa duniani, ambaye afanya mema, asifanye dhambi.” (Mhubiri 7:20) Basi, Wayahudi mashuhuri walikuwa na kila sababu ya kushangilia watenda-dhambi walipotubu.

      13. Kuisha ghafula kwa mfano wa Yesu wenye somo hutuacha na swali gani lenye kuamsha fikira?

      13 Baada ya sihi la baba, mfano huo wenye somo unaisha ghafula. Ni kana kwamba Yesu anawaalika wasikilizaji wake wafikie mkataa wao wenyewe. Hata iwe huyo mwana mwenye umri mkubwa zaidi aliitikiaje, kila msikilizaji alikabiliwa na swali, ‘Je, wewe utashiriki shangwe ipatikanayo mbinguni mtenda-dhambi anapotubu?’ Leo, Wakristo pia wana fursa ya kutoa jibu lao kwa swali hilo. Jinsi gani?

      Kuiga Rehema ya Mungu Leo

      14. (a) Twaweza kutumiaje shauri la Paulo lipatikanalo kwenye Waefeso 5:1 kuhusiana na rehema? (b) Ni kueleweka vibaya kupi kuhusu rehema ya Mungu ambako twahitaji kujilinda dhidi yake?

      14 Paulo aliwaonya Waefeso kwa upole hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa.” (Waefeso 5:1) Kwa sababu hiyo, tukiwa Wakristo twapaswa kuthamini rehema ya Mungu, tuikaze kikiki mioyoni mwetu, kisha tuonyeshe sifa hiyo katika kushughulika kwetu na wengine. Hata hivyo, inafaa tuwe wenye tahadhari. Rehema ya Mungu haipasi kufasiriwa kuwa kupunguza uzito wa dhambi. Kwa kielelezo, kunao wengine ambao huenda wakasababu hivi kwa kutojali: ‘Nikifanya dhambi, naweza kwa vyovyote kusali kwa Mungu kwa ajili ya msamaha, na atanirehemu.’ Mtazamo kama huo ungekuwa sawa na kile Yuda mwandikaji wa Biblia alichokiita “[ku]geuza fadhili isiyostahiliwa ya Mungu wetu kuwa sababu ya kujitetea kwa ajili ya mwenendo mlegevu.” (Yuda 4) Ingawa Yehova ni mwenye rehema, “si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe” anaposhughulika na wakosaji wasiotubu.—Kutoka 34:7; linganisha Yoshua 24:19; 1 Yohana 5:16.

      15. (a) Kwa nini wazee hasa wanahitaji kudumisha maoni yaliyosawazika kuhusu rehema? (b) Ingawa wazee hawavumilii ukosaji kimakusudi, wao wapaswa kujaribu kufanya nini, na kwa nini?

      15 Kwa upande mwingine, twahitaji kujihadhari vivyo hivyo ili tusiwe wenye kupita kiasi, yaani, tusiwe na mwelekeo wa kuwa wagumu na wenye kuhukumu wale wanaoonyesha toba ya kweli na huzuni ya kimungu juu ya dhambi zao. (2 Wakorintho 7:11) Kwa kuwa wazee wamekabidhiwa utunzaji wa kondoo wa Yehova, ni muhimu kwamba wadumishe maoni yaliyosawazika kuhusiana na jambo hilo, hasa wanaposhughulika na mambo ya kihukumu. Ni lazima kutaniko la Kikristo liendelezwe kuwa safi, na inafaa Kimaandiko “[kumwondoa] yule mtu mwovu” kwa kumtenga na ushirika. (1 Wakorintho 5:11-13) Wakati huohuo, ni vema kurehemu kunapokuwa na msingi dhahiri wa kufanya hivyo. Kwa hiyo, ingawa wazee hawavumilii ukosaji kimakusudi, wao hujitahidi kutafuta kutenda kwa upendo na rehema, bila kupita mipaka ya haki. Wao hutambua daima kanuni hii ya Biblia: “Yeye asiyezoea rehema atapata hukumu yake bila rehema. Rehema huchachawa kwa shangwe ya ushindi juu ya hukumu.”—Yakobo 2:13; Mithali 19:17; Mathayo 5:7.

      16. (a) Ukitumia Biblia, onyesha jinsi ambavyo Yehova kwa kweli hutaka wakosaji wamrudie. (b) Twaweza kudhihirishaje kwamba sisi pia twafurahia kurudi kwa watenda-dhambi wenye kutubu?

      16 Mfano wenye somo wa mwana mpotevu waonyesha wazi kwamba Yehova hutaka wakosaji wamrudie. Kwa kweli, yeye huwatolea mwaliko huo hadi wajithibitishapo kuwa hawawezi kutubu kabisa. (Ezekieli 33:11; Malaki 3:7; Waroma 2:4, 5; 2 Petro 3:9) Kama baba ya mwana mpotevu, Yehova huwatendea kwa adhama wanaorudi, akiwakubali warudi wakiwa washiriki kamili wa familia. Je, unamwiga Yehova kuhusiana na hilo? Wewe huitikiaje wakati mwamini mwenzi ambaye kwa muda fulani alikuwa ametengwa na ushirika anaporudishwa? Tayari tunajua kwamba kuna ‘shangwe mbinguni.’ (Luka 15:7) Lakini je, kuna shangwe duniani, kutanikoni mwako, hata moyoni mwako? Au, sawa na mwana mwenye umri mkubwa zaidi katika mfano wenye somo, je, kuna uchungu wa moyo, kana kwamba haustahili kukaribisha yule ambaye kwa kweli hakupaswa kamwe kuwa ameliacha kundi la Mungu?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki