Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Walimngoja Masihi
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Agosti 15
    • Walimngoja Masihi

      “Watu walikuwa wakingoja, na wote walikuwa wakiwaza mioyoni mwao juu ya Yohana, kama ndiye aliyekuwa Masihi.” —LUKA 3:15, THE EMPHATIC DIAGLOTT.

      1. Wachungaji fulani walisikia tangazo gani lililotolewa na malaika?

      USIKU umeingia. Wachungaji wako nje, wakichunga mifugo yao. Wanashtuka malaika wa Yehova anaposimama kando yao na utukufu wa Mungu unapowaangazia pande zote! Sikiliza! Malaika huyo anatoa tangazo hili la pekee: ‘Msiogope, kwa maana, tazama! ninawatangazia ninyi habari njema ya shangwe kubwa ambayo watu wote watakuwa nayo, kwa sababu leo, Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana, amezaliwa kwenu,’ yule ambaye atakuwa Masihi. Wachungaji watamkuta mtoto huyo akiwa amelazwa ndani ya hori katika mji wa karibu. Kwa ghafula, “umati wa jeshi la mbingu” unaanza kumsifu Yehova ukisema: “Utukufu katika vilele vilivyo juu kwa Mungu, na juu ya dunia amani kati ya watu wa nia njema.”—Luka 2:8-14.

      2. Neno “Masihi” linamaanisha nini, na anaweza kutambuliwa jinsi gani?

      2 Bila shaka, wachungaji hao Wayahudi wanajua kwamba neno “Masihi,” au “Kristo,” linamaanisha “Mtiwa-Mafuta” wa Mungu. (Kut. 29:5-7) Lakini watafanya nini ili wajifunze na wawasadikishe wengine kwamba mtoto ambaye ametajwa na malaika atakuwa Masihi aliyechaguliwa na Yehova? Ni kwa kuchunguza unabii unaopatikana katika Maandiko ya Kiebrania na kuulinganisha na utendaji na maisha ya mtoto huyo.

      Kwa Nini Watu Walikuwa Wakimngoja Masihi?

      3, 4. Tunaelewa jinsi gani andiko la Danieli 9:24, 25?

      3 Miaka mingi baadaye, Yohana Mbatizaji alianza kazi ya kuhubiri. Watu fulani waliposikia mambo aliyosema na kufanya walifikiri kwamba Masihi alikuwa amefika. (Soma Luka 3:15.) Inawezekana kwamba wengine walielewa kwa usahihi unabii wa Kimasihi unaohusu “majuma 70.” Ikiwa ndivyo, wangeweza kukadiria wakati ambapo Masihi angetokea. Kwa sehemu, unabii huo ulisema hivi: “Tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62.” (Dan. 9:24, 25) Wasomi mbalimbali wanakubali kwamba hayo ni majuma ya miaka. Kwa mfano, tafsiri moja ya Biblia (Revised Standard Version) inasema hivi: “Majuma 70 ya miaka yameamuriwa.”

      4 Leo, watumishi wa Yehova wanajua kwamba yale majuma 69, au miaka 483, ya Danieli 9:25 yalianza mwaka wa 455 K.W.K. wakati Mfalme Artashasta wa Uajemi alipomwamuru Nehemia arudishe na kujenga upya Yerusalemu. (Neh. 2:1-8) Majuma hayo yalimalizika miaka 483 baadaye, katika mwaka wa 29 W.K., wakati Yesu wa Nazareti alipobatizwa na kutiwa-mafuta kwa roho takatifu, na hivyo akawa Masihi.—Mt. 3:13-17.a

      5. Kwa sasa tutachunguza unabii gani mbalimbali?

      5 Acheni sasa tuchunguze unabii fulani kati ya unabii mwingi unaomhusu Masihi ambao ulitimia kuhusiana na kuzaliwa kwa Yesu, maisha yake ya utotoni, na huduma yake. Bila shaka, kufanya hivyo kutatia nguvu imani yetu katika neno la Mungu la kinabii. Na hilo litatusaidia kuona wazi kwamba Yesu alikuwa kwa kweli yule Masihi aliyengojewa kwa muda mrefu.

      Maisha Yake ya Utotoni Yalitabiriwa

      6. Eleza jinsi andiko la Mwanzo 49:10 lilivyotimia.

      6 Masihi angezaliwa Israeli katika kabila la Yuda. Mzee wa ukoo Yakobo aliwabariki watoto wake wa kiume kabla ya kifo chake na kutabiri hivi: “Fimbo ya enzi haitageuka kando kutoka kwa Yuda, wala fimbo ya kiongozi kutoka katikati ya miguu yake, mpaka Shilo aje; na vikundi vya watu vitamtii yeye.” (Mwa. 49:10) Wasomi wengi wa kale Wayahudi walisema kwamba maneno hayo yalimhusu Masihi. Kuanzia utawala wa Mfalme Daudi wa Yuda, fimbo (enzi ya kifalme) na fimbo ya uongozi (mamlaka ya kuongoza) ilikuwa katika kabila la Yuda. Neno “Shilo” linamaanisha “Yeye Ambaye Ni Yake; Yeye Ambaye Ni Mali Yake.” Ukoo wa kifalme wa Yuda ungefikia mwisho wake wakati ambapo “Shilo” angekuwa Mrithi wa kifalme wa kudumu, kwa sababu Mungu alimwambia Sedekia, mfalme wa mwisho wa Yuda, kwamba yule aliye na haki ya kisheria ndiye angepewa utawala huo. (Eze. 21:26, 27) Baada ya Sedekia, Yesu ndiye mzao pekee wa Daudi ambaye aliahidiwa ufalme. Kabla Yesu hajazaliwa, malaika Gabrieli alimwambia Maria hivi: “Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:32, 33) Ni lazima Shilo awe ni Yesu Kristo, ambaye alikuwa mzao wa Yuda na Daudi.—Mt. 1:1-3, 6; Luka 3:23, 31-34.

      7. Masihi alizaliwa wapi, na kwa nini hilo ni jambo la pekee?

      7 Masihi angezaliwa Bethlehemu. Nabii Mika aliandika hivi: “Nawe, Ee Bethlehemu Efratha, wewe uliye mdogo sana kuwa kati ya maelfu ya Yuda, kutoka kwako atanijia yeye atakayekuwa mtawala katika Israeli, ambaye asili yake ni kutoka nyakati za kale, kutoka siku za wakati usio na kipimo.” (Mika 5:2) Masihi angezaliwa katika mji wa Bethlehemu huko Yuda, na inaonekana kwamba zamani mji huo uliitwa Efratha. Ingawa Maria mama ya Yesu, na baba yake mlezi, Yosefu, waliishi huko Nazareti, mtawala wa Roma aliamuru watu wajiandikishe na hivyo wakarudi Bethlehemu, ambako Yesu alizaliwa mwaka wa 2 K.W.K. (Mt. 2:1, 5, 6) Kwa kweli, unabii kuhusu kuzaliwa kwa Yesu ulitimia kama ilivyotabiriwa!

      8, 9. Ni nini kilichotabiriwa kuhusu kuzaliwa kwa Masihi na matukio yaliyofuata?

      8 Masihi angezaliwa na bikira. (Soma Isaya 7:14.) Neno la Kiebrania bethu·lahʹ linamaanisha “bikira,” lakini neno lingine (ʽal·mahʹ) linapatikana katika Isaya 7:14. Katika andiko hilo, ilitabiriwa kwamba “mwanamwali [ha·ʽal·mahʹ]” angezaa mwana. Neno ʽal·mahʹ linatumiwa kumhusu mwanamwali Rebeka kabla ya kuolewa. (Mwa. 24:16, 43) Chini ya mwongozo wa roho ya Mungu, Mathayo alitumia neno la Kigiriki (par·theʹnos) linalomaanisha “bikira” alipoonyesha kwamba andiko la Isaya 7:14 lilitimia kuhusiana na kuzaliwa kwa Yesu. Waandikaji wa Injili, Mathayo na Luka, wanasema kwamba Maria alikuwa bikira aliyepata mimba kupitia nguvu za roho ya Mungu.—Mt. 1:18-25; Luka 1:26-35.

      9 Watoto wachanga wangeuawa baada ya kuzaliwa kwa Masihi. Jambo fulani linalofanana na hilo lilitukia karne nyingi mapema wakati Farao wa Misri alipoamuru kwamba watoto wa kiume Waebrania watupwe ndani ya Mto Nile. (Kut. 1:22) Lakini jambo kuu hasa linapatikana katika andiko la Yeremia 31:15, 16, ambalo linasema kwamba Raheli anawalilia wanawe ambao walipelekwa katika “nchi ya adui.” Maombolezo au kilio chake kilisikika mbali huko Rama, katika eneo la Benyamini upande wa kaskazini wa Yerusalemu. Mathayo anaonyesha kwamba maneno ya Yeremia yalitimia wakati Mfalme Herode alipoamuru watoto wote wachanga wa kiume wachinjwe huko Bethlehemu na katika maeneo ya karibu. (Soma Mathayo 2:16-18.) Fikiria huzuni ya watu katika eneo hilo!

      10. Eleza jinsi andiko la Hosea 11:1 lilivyotimia kumhusu Yesu.

      10 Kama Waisraeli, Masihi angeitwa kutoka Misri. (Hos. 11:1) Kabla Herode hajaamuru watoto wa kiume wauawe, malaika aliwaagiza Yosefu, Maria, na Yesu waende Misri. Walikaa huko “mpaka kufa kwa Herode, ili litimizwe lile lililosemwa na Yehova kupitia nabii [Hosea], akisema: ‘Kutoka Misri nilimwita mwanangu.’” (Mt. 2:13-15) Bila shaka, Yesu hangeweza kuongoza kwa ujanja mambo yaliyotabiriwa kuhusiana na kuzaliwa kwake na maisha yake ya utotoni.

      Masihi Anaanza Kutenda!

      11. Mtiwa-Mafuta wa Yehova alitayarishiwa njia jinsi gani?

      11 Njia ilipaswa kutayarishwa mbele ya Mtiwa-Mafuta wa Mungu. Malaki alitabiri kwamba “nabii Eliya” angefanya kazi hiyo ya kutayarisha mioyo ya watu kwa ajili ya kuja kwa Masihi. (Soma Malaki 4:5, 6.) Yesu mwenyewe alisema kwamba Yohana Mbatizaji ndiye aliyekuwa “Eliya.” (Mt. 11:12-14) Naye Marko alionyesha kwamba huduma ya Yohana ilitimiza unabii wa Isaya. (Isa. 40:3; Marko 1:1-4) Yesu hakumwambia Yohana afanye kazi kama ya Eliya ya kumtayarishia njia. Kazi ya huyo “Eliya” aliyetabiriwa ilifanywa kupatana na mapenzi ya Mungu ili kuwasaidia watu wamtambue Masihi.

      12. Ni kazi gani inayomtambulisha Masihi?

      12 Kazi aliyopewa na Mungu inamtambulisha Masihi. Katika sinagogi la Nazareti, mji ambako alilelewa, Yesu alisoma kitabu cha kukunjwa cha Isaya na kusema kwamba maneno yafuatayo yalimhusu: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema, alinituma kuhubiri kuachiliwa huru kwa mateka na kupata kuona tena kwa vipofu, kuacha waliopondeka waende zao wakiwa wameachiliwa huru, kuhubiri mwaka wa Yehova wenye kukubalika.” Na kwa kuwa yeye ndiye aliyekuwa Masihi, kwa kufaa Yesu alisema hivi: “Leo andiko hili ambalo mmesikia sasa hivi limetimizwa.”—Luka 4:16-21.

      13. Huduma ya hadharani ya Yesu huko Galilaya ilitabiriwa jinsi gani?

      13 Huduma ya hadharani ya Masihi huko Galilaya ilitabiriwa. Kuhusu “nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali . . . Galilaya ya mataifa,” Isaya aliandika hivi: “Watu waliokuwa wakitembea katika giza wameona nuru kuu. Kwa habari ya wale wanaokaa katika nchi yenye kivuli kizito, nuru imewaangazia.” (Isa. 9:1, 2) Yesu alianza huduma yake ya hadharani huko Galilaya, naye aliishi Kapernaumu, ambako wakaaji wengi wa Zabuloni na Naftali walifaidika na nuru ya kiroho ambayo aliwaletea. (Mt. 4:12-16) Huko Galilaya, Yesu alitoa Mahubiri yake ya Mlimani yenye kuchochea sana, aliwachagua mitume wake, alifanya muujiza wake wa kwanza, na inaelekea kwamba aliwatokea wanafunzi 500 hivi baada ya kufufuliwa. (Mt. 5:1–7:27; 28:16-20; Marko 3:13, 14; Yoh. 2:8-11; 1 Kor. 15:6) Hivyo, alitimiza unabii wa Isaya kwa kuhubiri katika “nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali.” Bila shaka, Yesu aliendelea kuhubiri ujumbe wa Ufalme katika maeneo mengine ya Israeli.

      Utendaji Mwingine wa Masihi Ulitabiriwa

      14. Yesu alitimiza unabii wa Zaburi 78:2 kwa njia gani?

      14 Masihi angesema kwa kutumia mifano. Mtunga-zaburi Asafu aliimba hivi: “Katika neno la kimethali nitakifungua kinywa changu.” (Zab. 78:2) Tunajua jinsi gani kwamba unabii huo ulimhusu Yesu? Mathayo anatueleza jambo hilo. Baada ya kueleza mifano ya Yesu ambayo ilifananisha Ufalme na chachu na pia mbegu ya haradali inayokua, Mathayo anasema hivi: “[Yesu] hakuwa akisema nao bila mfano; ili litimizwe lililosemwa kupitia nabii aliyesema: ‘Nitakifungua kinywa changu kwa mifano, nitatangaza mambo yaliyofichwa tangu kuwekwa msingi.’” (Mt. 13:31-35) Maneno ya kimethali au mifano, ni moja kati ya njia zenye matokeo ambazo Yesu alitumia kufundisha.

      15. Eleza jinsi unabii wa Isaya 53:4 ulivyotimia.

      15 Masihi angebeba udhaifu wetu. Isaya alitabiri hivi: “Kwa kweli yeye mwenyewe aliyachukua magonjwa yetu; na kwa habari ya maumivu yetu, yeye aliyabeba.” (Isa. 53:4) Mathayo alisema kwamba baada ya kumponya mama-mkwe wa Petro, Yesu aliwaponya wengine ili “litimizwe lile lililosemwa kupitia nabii Isaya, akisema: ‘Yeye mwenyewe aliyachukua magonjwa yetu na kuyachukua maradhi yetu.’” (Mt. 8:14-17) Na hilo ni simulizi moja tu kati ya masimulizi mengi yanayoonyesha kwamba Yesu aliwaponya wagonjwa.

      16. Mtume Yohana alionyesha jinsi gani kwamba Yesu alitimiza unabii wa Isaya 53:1?

      16 Watu wengi hawangemwamini Masihi hata ingawa angefanya mambo mengi mazuri. (Soma Isaya 53:1.) Akionyesha kwamba unabii huo ulitimia, mtume Yohana aliandika hivi: “Ijapokuwa [Yesu] alikuwa amefanya ishara nyingi sana mbele yao, hawakuwa wanamwamini, hata kwamba neno la nabii Isaya likatimizwa ambalo alisema: ‘Yehova, ni nani aliyeliamini jambo ambalo tumesikia? Na kwa habari ya mkono wa Yehova, umefunuliwa kwa nani?’” (Yoh. 12:37, 38) Hata wakati wa huduma ya mtume Paulo, ni watu wachache sana ambao waliamini habari njema ya kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi.—Rom. 10:16, 17.

      17. Yohana alisema unabii wa Zaburi 69:4 ulitimia jinsi gani?

      17 Masihi angechukiwa bila sababu. (Zab. 69:4) Mtume Yohana anataja maneno haya ya Yesu: “Kama singefanya kati [ya watu] kazi ambazo hakuna mwingine aliyezifanya, hawangekuwa na dhambi; lakini sasa wameniona na pia wamenichukia mimi na vilevile Baba yangu. Lakini ni ili neno lililoandikwa katika Sheria yao lipate kutimizwa, ‘Walinichukia bila sababu.’” (Yoh. 15:24, 25) Mara nyingi neno “Sheria” linamaanisha Maandiko yote kwa ujumla. (Yoh. 10:34; 12:34) Masimulizi ya Injili yanathibitisha kwamba Yesu alichukiwa, hasa na viongozi wa dini ya Kiyahudi. Zaidi ya hayo, Kristo alisema hivi: “Ulimwengu hauna sababu ya kuwachukia ninyi, lakini huo unanichukia mimi, kwa sababu ninatoa ushahidi juu yake kwamba kazi zake ni mbovu.”—Yoh. 7:7.

      18. Ni habari gani zaidi ambayo itatusaidia kusadiki kabisa kwamba Yesu ndiye Masihi?

      18 Wafuasi wa Yesu katika karne ya kwanza walikuwa na hakika kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi, kwa sababu kwa kweli alitimiza unabii mbalimbali kumhusu Masihi unaopatikana katika Maandiko ya Kiebrania. (Mt. 16:16) Kama tulivyoona, unabii fulani ulitimia wakati Yesu wa Nazareti alipokuwa mtoto na wakati wa huduma yake. Unabii mwingine kumhusu Masihi utazungumziwa katika habari inayofuata. Bila shaka, tukisali na kutafakari kuhusu unabii huo, tutasadiki kabisa kwamba kwa kweli Yesu Kristo ndiye Masihi aliyewekwa rasmi na Baba yetu wa mbinguni, Yehova.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa mazungumzo zaidi kuhusu yale “majuma 70,” ona sura ya 11 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!

  • Walimpata Masihi!
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Agosti 15
    • Walimpata Masihi!

      “Tumempata Masihi.”—YOH. 1:41.

      1. Ni nini kilichomfanya Andrea aseme: “Tumempata Masihi”?

      YOHANA MBATIZAJI amesimama pamoja na wawili kati ya wanafunzi wake. Yesu anapokaribia, Yohana anasema hivi kwa sauti kubwa: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu!” Papo hapo, Andrea na yule mwanafunzi mwingine wanamfuata Yesu na kukaa naye siku nzima. Baadaye, Andrea anampata ndugu yake, Simoni Petro, na kumpeleka kwa Yesu baada ya kusema hivi kwa msisimko: “Tumempata Masihi.”—Yoh. 1:35-41.

      2. Tutafaidika jinsi gani tunapoendelea kuchunguza unabii mbalimbali kumhusu Masihi?

      2 Kadiri wakati unavyopita, Andrea, Petro, na wengine watakuwa na nafasi nyingi za kujifunza kwa undani Maandiko na watasema kwa uhakika kabisa kwamba Yesu wa Nazareti ndiye Masihi aliyeahidiwa. Imani yetu katika Neno la Mungu na Mtiwa-Mafuta wake itatiwa nguvu tunapoendelea kuchunguza unabii mbalimbali kumhusu Masihi.

      “Tazama! Mfalme Wako Anakuja”

      3. Ni unabii gani ambao ulitimia Yesu alipoingia Yerusalemu kwa ushindi?

      3 Masihi angeingia Yerusalemu kwa ushindi. Unabii wa Zekaria ulisema hivi: “Shangilia sana, Ee binti Sayuni. Piga kelele za ushindi, Ee binti Yerusalemu. Tazama! mfalme wako anakuja kwako. Yeye ni mwadilifu, ndiyo, ameokolewa; ni mnyenyekevu, naye amepanda juu ya punda, juu ya mnyama mkomavu, mwana wa punda-jike.” (Zek. 9:9) Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Na abarikiwe Yeye anayekuja katika jina la Yehova.” (Zab. 118:26) Yesu hakuuambia umati jambo la kufanya. Hata hivyo, umati huo ulipaaza sauti kwa ghafula na kwa shangwe nyingi sana na hivyo kutimiza unabii huo. Unaposoma simulizi hilo, wazia tukio hilo na usikie sauti za furaha za umati huo.—Soma Mathayo 21:4-9.

      4. Eleza jinsi andiko la Zaburi 118:22, 23 lilivyotimia.

      4 Yesu ni mwenye thamani machoni pa Mungu, lakini watu wengi wangemkataa ingawa angetimiza mengi akiwa Masihi. Kama ilivyotabiriwa, Yesu ‘alidharauliwa na kuhesabiwa kuwa asiye na maana’ na watu ambao hawakuamini uthibitisho. (Isa. 53:3; Marko 9:12) Hata hivyo, Mungu alimwongoza kwa roho takatifu mtunga-zaburi kusema hivi: “Jiwe ambalo wajenzi walilikataa limekuwa jiwe kuu la pembeni. Hili limetokana na Yehova mwenyewe.” (Zab. 118:22, 23) Pindi moja, Yesu alizungumzia unabii huo alipokuwa akiongea na wapinzani wake wa kidini, na Petro alisema kwamba Kristo alitimiza unabii huo. (Marko 12:10, 11; Mdo. 4:8-11) Yesu akaja kuwa “jiwe la pembeni la msingi” la kutaniko la Kikristo. Ingawa watu wasiomwogopa Mungu walimkataa, yeye ni ‘mchaguliwa na mwenye thamani kwa Mungu.’—1 Pet. 2:4-6.

      Alisalitiwa na Kuachwa!

      5, 6. Ni jambo gani lililotabiriwa na kutimia kuhusu kusalitiwa kwa Masihi?

      5 Ilitabiriwa kwamba Masihi angesalitiwa na rafiki mwenye hila. Daudi alitabiri hivi: “Mtu mwenye kuwa na amani nami, ambaye nimemtegemea, ambaye alikuwa akila mkate wangu, amekiinua kisigino chake dhidi yangu.” (Zab. 41:9) Mtu ambaye alikula mkate pamoja na mwingine alionwa kuwa rafiki yake. (Mwa. 31:54) Hivyo, Yuda Iskariote alipomsaliti Yesu, alitenda kwa njia ya hila kabisa. Yesu alionyesha kwamba unabii wa Daudi ulitimia alipozungumza kuhusu msaliti wake na kuwaambia mitume wake hivi: “Mimi sisemi juu yenu nyote; ninawajua wale ambao nimewachagua. Lakini ni ili Andiko lipate kutimizwa, ‘Yule aliyekuwa akila mkate wangu amekiinua kisigino chake dhidi yangu.’”—Yoh. 13:18.

      6 Mtu ambaye angemsaliti Masihi angepokea vipande 30 vya fedha, yaani, bei ya mtumwa! Akitumia unabii wa Zekaria 11:12, 13, Mathayo alionyesha kwamba Yesu alisalitiwa kwa kiasi hicho kidogo cha fedha. Lakini kwa nini Mathayo alisema kwamba jambo hilo lilikuwa limetabiriwa “kupitia nabii Yeremia”? Katika siku za Mathayo, huenda kitabu cha Yeremia kilikuwa cha kwanza katika kikundi cha vitabu vya Biblia ambavyo vilitia ndani Zekaria. (Linganisha na Luka 24:44.) Yuda hakutumia kamwe pesa alizopata kwa hila, kwa kuwa alizitupa ndani ya hekalu na kwenda kujinyonga.—Mt. 26:14-16; 27:3-10.

      7. Unabii wa Zekaria 13:7 ulitimia jinsi gani?

      7 Hata wanafunzi wa Masihi wangetawanyika. Zekaria aliandika hivi: “Mpige mchungaji, na wale wa kundi watawanyike.” (Zek. 13:7) Katika Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninyi nyote mtakwazika kuhusiana nami usiku huu, kwa maana imeandikwa, ‘Nitampiga mchungaji, nao kondoo wa kundi watatawanyika huku na huku.’” Na hivyo ndivyo ilivyokuwa, kwa sababu Mathayo aliripoti kwamba “wanafunzi wote wakamwacha [Yesu] na kukimbia.”—Mt. 26:31, 56.

      Alishtakiwa na Kupigwa

      8. Unabii wa Isaya 53:8 ulitimia chini ya hali gani?

      8 Masihi angeshtakiwa na kuhukumiwa. (Soma Isaya 53:8.) Asubuhi ya Nisani 14, washiriki wote wa Sanhedrini walikutana, wakaamuru Yesu afungwe mikono, na kumpeleka kwa Gavana Mroma Pontio Pilato. Alimuuliza Yesu maswali lakini hakumpata na hatia yoyote. Hata hivyo, Pilato alipotaka kumwachilia Yesu, watu walipaaza sauti hivi: “Mtundike mtini!” na wakaomba Baraba aliyekuwa mhalifu aachiliwe. Akitaka kuupendeza umati huo, Pilato alimwachilia Baraba, akaamuru Yesu apigwe mijeledi, na kumtoa ili atundikwe mtini.—Marko 15:1-15.

      9. Ni jambo gani lililotukia katika siku za Yesu ambalo lilitabiriwa katika Zaburi 35:11?

      9 Mashahidi wa uwongo wangetoa ushahidi wa uwongo kumhusu Masihi. Mtunga-zaburi Daudi alisema hivi: “Mashahidi wenye jeuri husimama; huniuliza mambo nisiyojua.” (Zab. 35:11) Kama unabii ulivyosema, “wakuu wa makuhani na Sanhedrini nzima walikuwa wakitafuta ushahidi wa uwongo juu ya Yesu ili wamuue.” (Mt. 26:59) Kwa kweli, “wengi walikuwa wakitoa ushahidi wa uwongo juu yake, lakini ushuhuda wao haukupatana.” (Marko 14:56) Maadui wa Yesu wenye hasira ambao walitaka auawe hawakujali ushahidi wa uwongo uliotolewa kumhusu.

      10. Eleza jinsi unabii wa Isaya 53:7 ulivyotimia.

      10 Masihi angekaa kimya mbele ya wale waliomshtaki. Isaya alikuwa ametabiri hivi: “Alikazwa sana, naye alijiachilia ateswe; ingawa hivyo hakufungua kinywa chake. Alikuwa akiletwa kama kondoo machinjioni; na kama kondoo-jike ambaye amekuwa bubu mbele ya wakataji-manyoya wake, yeye pia hakufungua kinywa chake.” (Isa. 53:7) Yesu “alipokuwa akishtakiwa na wakuu wa makuhani na wanaume wazee, hakujibu.” Pilato akamuuliza: “Je, husikii ni mambo mangapi wanashuhudia juu yako?” Hata hivyo, Yesu “hakumjibu, hata neno moja, hivi kwamba gavana akastaajabu sana.” (Mt. 27:12-14) Yesu hakuwatukana wale waliokuwa wakimshtaki.—Rom. 12:17-21; 1 Pet. 2:23.

      11. Unabii wa Isaya 50:6 na Mika 5:1 ulitimia jinsi gani?

      11 Isaya alitabiri kwamba Masihi angepigwa. Nabii huyo aliandika: “Mgongo wangu niliwapa washambuliaji, na mashavu yangu nikawapa wale wenye kung’oa nywele. Uso wangu sikuuficha kutoka kwa mambo yenye kufedhehesha na mate.” (Isa. 50:6) Mika alitabiri hivi: “Watalipiga kwa fimbo shavu la mwamuzi wa Israeli.” (Mika 5:1) Akithibitisha kwamba unabii huo ulitimia, Marko, mwandikaji wa Injili alisema: “Wengine wakaanza kumtemea [Yesu] mate na kuufunika uso wake wote na kumpiga ngumi na kumwambia: ‘Toa unabii!’ Na, wakimpiga makofi usoni, watumishi wa mahakama wakamchukua.” Marko anasema kwamba askari-jeshi “wakawa wakimpiga kichwani kwa utete na kumtemea mate na kumsujudia [kwa dhihaka] wakiwa wamepiga magoti.” (Marko 14:65; 15:19) Bila shaka, Yesu hakutenda kosa lolote ambalo lingefanya astahili kutendewa hivyo.

      Mwaminifu Mpaka Kifo

      12. Unabii wa Zaburi 22:16 na Isaya 53:12 ulimhusu Yesu jinsi gani?

      12 Unabii ulitabiri jinsi ambavyo Masihi angetundikwa mtini. Mtunga-zaburi Daudi alisema hivi: “Kusanyiko la watenda-maovu limenizunguka. Wako kwenye mikono yangu na miguu yangu kama simba.” (Zab. 22:16) Akiripoti tukio ambalo wasomaji wa Biblia wanajua vizuri, Marko, mwandikaji wa Injili anasema: “Sasa ilikuwa saa tatu [karibu saa tatu asubuhi], nao wakamtundika mtini.” (Marko 15:25) Pia, ilikuwa imetabiriwa kwamba Masihi angehesabiwa pamoja na watenda-dhambi. Isaya aliandika hivi: “Aliimwaga nafsi yake mpaka kufa, naye alihesabiwa pamoja na wakosaji.” (Isa. 53:12) Na kama ilivyotabiriwa, “wanyang’anyi wawili wakatundikwa mtini pamoja [na Yesu], mmoja upande wake wa kuume na mwingine upande wake wa kushoto.”—Mt. 27:38.

      13. Unabii wa Zaburi 22:7, 8 ulitimia jinsi gani kuhusiana na Yesu?

      13 Daudi alitabiri kwamba Masihi angetukanwa. (Soma Zaburi 22:7, 8.) Yesu alitukanwa akiwa kwenye mti wa mateso, kwa kuwa Mathayo anaripoti hivi: “Wapita-njia wakaanza kumtukana, wakitikisa vichwa vyao na kusema: ‘Ewe uliyetaka kuliangusha hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe mwenyewe! Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, shuka kutoka kwenye mti wa mateso!’” Vivyo hivyo, wakuu wa makuhani, waandishi, na wanaume wazee walimcheka na kusema: “Aliwaokoa wengine; yeye mwenyewe hawezi kujiokoa! Yeye ni Mfalme wa Israeli; acheni sasa ashuke kutoka kwenye mti wa mateso nasi tutamwamini. Ameweka tegemeo lake katika Mungu; acheni Yeye sasa amwokoe ikiwa Yeye anamtaka, kwa maana alisema, ‘Mimi ni Mwana wa Mungu.’” (Mt. 27:39-43) Hata hivyo, Yesu alivumilia mateso hayo yote kwa heshima. Alituwekea mfano mzuri kama nini!

      14, 15. Eleza jinsi unabii ulivyotimia kuhusu mavazi ya Masihi na jinsi alivyopewa siki.

      14 Mavazi ya Masihi yangepigiwa kura. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Wanagawana mavazi yangu, nao wanalipigia kura vazi langu.” (Zab. 22:18) Hilo ndilo jambo lililotukia, kwa kuwa “[askari-jeshi Waroma] walipokuwa wamemtundika [Yesu] mtini wakagawa mavazi yake ya nje kwa kupiga kura.”—Mt. 27:35; soma Yohana 19:23, 24.

      15 Masihi angepewa siki na nyongo. Mtunga-zaburi alisema: “Walinipa mmea wenye sumu kuwa chakula, na kwa ajili ya kiu yangu wakajaribu kuninywesha siki.” (Zab. 69:21) Mathayo anatuambia hivi: “Wakampa [Yesu] divai iliyochanganywa na nyongo anywe; lakini, baada ya kuionja, akakataa kuinywa.” Baadaye, “mmoja wao akakimbia mara moja, akachukua sifongo akailowesha kwenye divai kali akaiweka juu ya utete na kuanza kumnywesha.”—Mt. 27:34, 48.

      16. Eleza jinsi unabii wa Zaburi 22:1 ulivyotimia.

      16 Ingeonekana kwamba Mungu amemwacha Masihi. (Soma Zaburi 22:1.) Kulingana na unabii huo, “saa tisa [karibu saa tisa mchana] Yesu akapaaza kilio kwa sauti kubwa: ‘Eli, Eli, lama sabakthani?’ maneno ambayo yanapotafsiriwa humaanisha: ‘Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?’” (Marko 15:34) Yesu hakuwa amepoteza imani katika Baba yake wa mbinguni. Mungu alimwacha Yesu mikononi mwa maadui wake kwa kuondoa ulinzi Wake ili utimilifu wa Kristo ujaribiwe kikamili. Na Yesu alipopaaza kilio, alitimiza unabii wa Zaburi 22:1.

      17. Maneno ya Zekaria 12:10 na Zaburi 34:20 yalitimia jinsi gani?

      17 Masihi angechomwa, lakini mifupa yake haingevunjwa. Wakaaji wa Yerusalemu ‘wangemtazama Yule waliyemchoma.’ (Zek. 12:10) Na andiko la Zaburi 34:20 linasema: “[Mungu] anailinda mifupa yote ya mtu huyo; hakuna hata mmoja uliovunjwa.” Akithibitisha maneno hayo, mtume Yohana aliandika hivi: “Mmoja wa hao askari-jeshi akauchoma ubavu wake [wa Yesu] kwa mkuki, na mara moja damu na maji vikatoka. Na [Yohana] ambaye ameona hilo ametoa ushahidi, nao ushahidi wake ni wa kweli . . . Mambo haya yalitendeka kusudi andiko litimizwe: ‘Hakuna mfupa wake hata mmoja utakaovunjwa.’ Na tena, andiko tofauti linasema: ‘Watamtazama Yule waliyemchoma.’”—Yoh. 19:33-37.

      18. Yesu alizikwa pamoja na matajiri jinsi gani?

      18 Masihi angezikwa pamoja na matajiri. (Soma Isaya 53:5, 8, 9.) Baadaye Nisani 14 wakati wa mchana, “mtu mmoja tajiri wa Arimathea, anayeitwa Yosefu,” alimwomba Pilato mwili wa Yesu, na ombi lake likakubaliwa. Simulizi la Mathayo linaongezea hivi: “Yosefu akauchukua mwili huo, akaufunga katika kitani safi kizuri, na kuulaza katika kaburi lake jipya, alilokuwa amechimba katika mwamba. Na, baada ya kuviringisha jiwe kubwa kwenye mlango wa lile kaburi, akaondoka.”—Mt. 27:57-60.

      Msifu Mfalme wa Kimasihi!

      19. Unabii wa Zaburi 16:10 ulitimia jinsi gani?

      19 Masihi angefufuliwa. Daudi aliandika hivi: “[Yehova] hutaiacha nafsi yangu katika Kaburi.” (Zab. 16:10) Fikiria jinsi wanawake waliokuja kwenye kaburi ambamo mwili wa Yesu ulikuwa umelazwa walivyoshangaa. Walimkuta malaika aliyejivika mwili wa kibinadamu, akawaambia hivi: “Acheni kufadhaika. Mnamtafuta Yesu Mnazareti, aliyetundikwa mtini. Alifufuliwa, hayupo hapa. Tazameni! Mahali walipomlaza.” (Marko 16:6) Siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K., mtume Petro aliuambia hivi umati uliokusanyika Yerusalemu: “[Daudi] aliona kimbele na kusema kuhusu ufufuo wa Kristo, kwamba hakuachwa katika Kaburi wala mwili wake haukuona uharibifu.” (Mdo. 2:29-31) Mungu hakuruhusu mwili wa nyama wa Mwana wake mpendwa uoze. Zaidi ya hayo, Yesu alifufuliwa kimuujiza na kupewa mwili wa roho!—1 Pet. 3:18.

      20. Unabii kuhusu utawala wa Masihi ulitimia jinsi gani?

      20 Kama ilivyotabiriwa, Mungu alitangaza kwamba Yesu ni Mwana wake. (Soma Zaburi 2:7; Mathayo 3:17.) Pia, umati wa watu ulimsifu Yesu na Ufalme ambao ungekuja, na kwa shangwe tunawahubiria watu kumhusu na kuhusu utawala wake uliobarikiwa. (Marko 11:7-10) Hivi karibuni, Kristo atawaharibu maadui wake ‘atakapopanda kwa kutetea kweli, unyenyekevu, na uadilifu.’ (Zab. 2:8, 9; 45:1-6) Ufalme wake utaleta amani na ufanisi duniani pote. (Zab. 72:1, 3, 12, 16; Isa. 9:6, 7) Tuna pendeleo kubwa sana la kutangaza kweli hizo tukiwa Mashahidi wa Yehova, ambaye Mwana wake mpendwa anatawala sasa mbinguni akiwa Mfalme wa Kimasihi!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki