-
Tazama! Mtumishi wa Yehova AliyekubaliwaMnara wa Mlinzi—2009 | Januari 15
-
-
Tazama! Mtumishi wa Yehova Aliyekubaliwa
“Tazama! Mtumishi wangu, . . . ambaye nafsi yangu imemkubali!” —ISA. 42:1.
1. Watu wa Yehova wanatiwa moyo kufanya nini hasa Ukumbusho unapokaribia, na kwa nini?
WAKATI wa kuadhimisha kifo cha Kristo unapozidi kukaribia, watu wa Mungu wanatiwa moyo kufuata shauri la mtume Paulo la ‘kumtazama kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.’ Paulo aliongeza hivi: “Kwa kweli, mfikirieni sana yeye ambaye amevumilia maneno ya aina hii yenye kupinga yanayotolewa na watenda-dhambi kinyume cha faida zao wenyewe, ili ninyi msichoke na kuzimia katika nafsi zenu.” (Ebr. 12:2, 3) Kuchunguza kwa makini maisha ya uaminifu ya Kristo, ambayo yalifikia upeo alipotoa dhabihu yake, kutawasaidia Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao wa kondoo wengine kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu na kuepuka ‘kuzimia katika nafsi zao.’—Linganisha na Wagalatia 6:9.
2. Tunaweza kujifunza nini kupitia unabii mbalimbali ambao Isaya aliandika kuhusu Mwana wa Mungu?
2 Yehova alimwongoza kwa roho nabii Isaya aandike unabii mbalimbali uliomhusu moja kwa moja Mwana wa Mungu. Unabii huo utatusaidia ‘kumtazama kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu,’ Kristo Yesu.a Unabii huo unatufunulia utu wake, mateso yake, na jinsi alivyotukuzwa kuwa Mfalme na Mkombozi wetu. Utatusaidia kuelewa zaidi Ukumbusho, ambao tutaadhimisha mwaka huu Alhamisi (Siku ya 4), Aprili 9, baada ya jua kushuka.
Mtumishi Anatambulishwa
3, 4. (a) Neno “mtumishi” linatumiwa jinsi gani katika kitabu cha Isaya? (b) Biblia yenyewe inamtambulisha jinsi gani Mtumishi anayetajwa katika Isaya sura ya 42, 49, 50, 52, na 53?
3 Neno “mtumishi” linatajwa mara nyingi katika kitabu cha Isaya. Nyakati nyingine, linamhusu nabii Isaya mwenyewe. (Isa. 20:3; 44:26) Pindi nyingine linahusu taifa lote la Israeli, au Yakobo. (Isa. 41:8, 9; 44:1, 2, 21) Lakini namna gani ule unabii wa pekee kuhusu Mtumishi anayetajwa katika Isaya sura ya 42, 49, 50, 52, na 53? Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanamtambulisha wazi Mtumishi huyo wa Yehova anayetajwa katika sura hizo. Inapendeza kwamba yule ofisa Mwethiopia anayetajwa katika kitabu cha Matendo alikuwa akisoma unabii mmoja kati ya unabii mbalimbali kumhusu Masihi wakati mweneza-injili Filipo alipoagizwa na roho aende mahali alipokuwa. Ofisa huyo alisoma kifungu cha Biblia kinachopatikana sasa katika Isaya 53:7, 8, kisha akamuuliza Filipo: “Ninakuomba, Nabii anasema hivyo juu ya nani? Juu yake mwenyewe au juu ya mtu mwingine?” Papo hapo, Filipo akamweleza kwamba Isaya alikuwa akizungumza kuhusu Masihi, Yesu.—Mdo. 8:26-35.
4 Yesu alipokuwa mtoto, mwanamume fulani mwadilifu aliyeitwa Simeoni alitangaza huku akiongozwa na roho takatifu kwamba “mtoto mchanga Yesu” atakuwa “nuru ya kuondoa utaji kwa mataifa,” kama ilivyotabiriwa katika Isaya 42:6 na 49:6. (Luka 2:25-32) Zaidi ya hayo, unabii ulio katika Isaya 50:6-9 ulitabiri mateso yenye kufedhehesha yaliyompata Yesu usiku ambao kesi yake ilifanywa. (Mt. 26:67; Luka 22:63) Baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., mtume Petro alimtambulisha Yesu waziwazi kuwa “Mtumishi” wa Yehova. (Isa. 52:13; 53:11; soma Matendo 3:13, 26.) Tunaweza kujifunza nini katika unabii huo mbalimbali kumhusu Masihi?
Yehova Anamzoeza Mtumishi Wake
5. Mtumishi huyo alipata mazoezi gani?
5 Unabii mmoja wa Isaya kuhusu Mtumishi wa Mungu unafunua uhusiano wa karibu ambao Yehova alikuwa nao pamoja na Mwana wake mzaliwa wa kwanza kabla ya Mwana huyo kuja duniani. (Soma Isaya 50:4-9.) Mtumishi huyo mwenyewe anafunua kwamba Yehova alimzoeza sikuzote, anaposema: “Yeye . . . huliamsha sikio langu ili lisikie kama wale waliofundishwa,” au wanafunzi. (Isa. 50:4) Wakati huo wote, Mtumishi wa Yehova alimsikiliza Baba yake na kujifunza kutoka kwake, na hivyo akawa mwanafunzi mwenye kujitiisha. Ni pendeleo la pekee kama nini kufundishwa na Muumba wa ulimwengu wote mzima!
6. Mtumishi huyo alionyesha jinsi gani kwamba anajitiisha kikamili kwa Baba yake?
6 Katika unabii huo, Mtumishi huyo anamtaja Baba yake kuwa “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” Hilo linaonyesha kwamba Mtumishi huyo alikuwa amejifunza ukweli wa msingi kuhusu enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote mzima. Ili kuonyesha kwamba anajitiisha kikamili kwa Baba yake, alisema hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amelifungua sikio langu, nami kwa upande wangu sikuwa mwasi. Sikugeuka upande ulio kinyume.” (Isa. 50:5) Alikuwa ‘kando ya Yehova akiwa stadi wa kazi’ wakati wa kuumbwa kwa mwanadamu na ulimwengu wote mzima. ‘Stadi huyo wa kazi’ alikuwa ‘akifurahi mbele za Yehova wakati wote, akifurahi kwa sababu ya dunia yake yenye kutoa mazao, na vitu ambavyo Mwana huyo wa Mungu alipenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.’—Met. 8:22-31.
7. Ni nini kinachoonyesha kwamba Mtumishi huyo alikuwa na uhakika kwamba Baba yake angemtegemeza wakati wa majaribu?
7 Mazoezi ambayo Mtumishi huyo alipokea na upendo wake kwa wanadamu ulimtayarisha kabisa kwa ajili ya maisha yake duniani na upinzani mkali aliokabili. Aliendelea kufurahia kufanya mapenzi ya Baba yake, hata alipoteswa vikali. (Zab. 40:8; Mt. 26:42; Yoh. 6:38) Katika majaribu yote aliyopata duniani, Yesu alikuwa na uhakika kwamba Baba yake alimkubali na angemtegemeza. Kama ilivyotabiriwa katika unabii wa Isaya, Yesu alisema: “Yeye anayenitangaza mimi kuwa mwadilifu yupo karibu. Ni nani anayeweza kushindana nami? . . . Tazama! Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe atanisaidia.” (Isa. 50:8, 9) Bila shaka, Yehova alimsaidia Mtumishi wake mwaminifu katika huduma yake yote duniani, kama unabii mwingine wa Isaya unavyoonyesha.
Huduma ya Mtumishi Huyo Duniani
8. Ni jambo gani linalothibitisha kwamba Yesu ndiye “mchaguliwa” wa Yehova aliyetabiriwa katika Isaya 42:1?
8 Biblia inasema jambo lililotukia Yesu alipobatizwa mwaka wa 29 W.K.: “Roho takatifu . . . ikashuka juu yake, na sauti ikatoka mbinguni: ‘Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali wewe.’” (Luka 3:21, 22) Hivyo, Yehova alimtambulisha waziwazi “mchaguliwa” wake aliyetajwa katika unabii wa Isaya. (Soma Isaya 42:1-7.) Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alitimiza unabii huo kwa njia ya pekee. Katika masimulizi yake ya Injili, Mathayo alinukuu maneno yanayopatikana katika Isaya 42:1-4 na kuonyesha jinsi yanavyomhusu Yesu.—Mt. 12:15-21.
9, 10. (a) Yesu alitimiza jinsi gani Isaya 42:3 wakati wa huduma yake? (b) Ni kwa njia gani Kristo ‘alileta haki’ alipokuwa duniani, na ni wakati gani ambapo ‘ataweka haki duniani’?
9 Viongozi wa kidini Wayahudi waliwadharau watu wa kawaida. (Yoh. 7:47-49) Watu hao walitendewa kwa ukali na wangeweza kulinganishwa na ‘matete yaliyovunjika’ au ‘tambi za kitani’ zilizo karibu kuzimika kabisa. Hata hivyo, Yesu aliwahurumia maskini na watu wanaoteseka. (Mt. 9:35, 36) Aliwaalika kwa fadhili watu wa aina hiyo aliposema: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi.” (Mt. 11:28) Zaidi ya hayo, Yesu ‘alileta haki’ kwa kufundisha kanuni za Yehova kuhusu mema na mabaya. (Isa. 42:3) Pia, alionyesha kwamba Sheria ya Mungu ilipaswa kutumiwa kwa usawaziko na rehema. (Mt. 23:23) Vilevile, Yesu alionyesha haki kwa kuwahubiria matajiri na maskini bila ubaguzi.—Mt. 11:5; Luka 18:18-23.
10 Pia, unabii wa Isaya unatabiri kwamba “mchaguliwa” wa Yehova ‘ataweka haki duniani.’ (Isa. 42:4) Atafanya hivyo hivi karibuni wakati atakapoharibu falme zote za kisiasa na kusimamisha utawala wake wenye uadilifu akiwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi. Ataleta ulimwengu mpya, ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Pet. 3:13; Dan. 2:44.
“Nuru” na “Agano”
11. Ni kwa njia gani Yesu alikuwa “nuru ya mataifa” katika karne ya kwanza, na leo pia?
11 Kwa kweli, Yesu alikuwa “nuru ya mataifa,” na hivyo akatimiza unabii wa Isaya 42:6. Wakati wa huduma yake duniani, alileta nuru ya kiroho hasa kwa Wayahudi. (Mt. 15:24; Mdo. 3:26) Lakini Yesu alisema hivi: “Mimi ndiye nuru ya ulimwengu.” (Yoh. 8:12) Alikuwa nuru kwa Wayahudi na kwa mataifa si tu kwa kuwapa nuru ya kiroho bali pia kwa kudhabihu uhai wake mkamilifu akiwa mwanadamu ili awe dhabihu ya ukombozi kwa ajili ya wanadamu wote. (Mt. 20:28) Baada ya ufufuo wake, aliwaagiza wanafunzi wake wawe mashahidi wake “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Wakati wa huduma yao, Paulo na Barnaba walitaja maneno “nuru ya mataifa” na kuutumia kuhusu kazi ya kuhubiri ambayo walikuwa wakifanya kati ya watu wasio Wayahudi. (Mdo. 13:46-48; linganisha na Isaya 49:6.) Kazi hiyo bado inafanywa na ndugu za Yesu watiwa-mafuta walio duniani na waandamani wao ambao wanasambaza nuru ya kiroho na kuwasaidia watu kumwamini Yesu, ambaye ndiye “nuru ya mataifa.”
12. Yehova amemtoa jinsi gani Mtumishi wake “kuwa agano la watu”?
12 Katika unabii huohuo, Yehova alimwambia hivi Mtumishi wake mchaguliwa: “Nitakulinda na kukutoa kuwa agano la watu.” (Isa. 42:6) Shetani alijitahidi sana kumwangamiza Yesu na kumzuia asimalize huduma yake duniani, lakini Yehova alimlinda mpaka wakati uliowekwa wa kifo chake. (Mt. 2:13; Yoh. 7:30) Kisha Yehova akamfufua Yesu na kumtoa kuwa “agano,” au ahadi, kwa watu walio duniani. Ahadi hiyo rasmi ilitoa uhakikisho wa kwamba Mtumishi huyo mwaminifu wa Mungu angeendelea kuwa “nuru ya mataifa,” na hivyo kuwaweka huru wale walio katika giza la kiroho.—Soma Isaya 49:8, 9.b
13. Ni kwa njia gani Yesu aliwakomboa “wale wanaoketi gizani” wakati wa huduma yake duniani, naye anaendelea kufanya hivyo jinsi gani?
13 Kupatana na ahadi hiyo, Mtumishi mchaguliwa wa Yehova ‘angeyafungua macho yenye upofu,’ ‘angemtoa mfungwa katika gereza la shimoni,’ na kuwakomboa “wale wanaoketi gizani.” (Isa. 42:7) Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alifanya hivyo kwa kufunua mapokeo ya uwongo ya kidini na kuhubiri habari njema ya Ufalme. (Mt. 15:3; Luka 8:1) Hivyo, aliwakomboa kutoka katika dini ya uwongo Wayahudi ambao walikuja kuwa wanafunzi wake. (Yoh. 8:31, 32) Vivyo hivyo, Yesu amewakomboa kiroho mamilioni ya watu wasio Wayahudi. Amewaagiza wafuasi wake ‘waende na kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ na kuahidi kwamba atakuwa pamoja na wafuasi wake “mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20) Akiwa katika cheo chake mbinguni, Kristo Yesu anasimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote.
Yehova Alimwinua “Mtumishi” Huyo
14, 15. Kwa nini Yehova alimwinua Mtumishi wake, naye alifanya hivyo jinsi gani?
14 Katika unabii mwingine kuhusu Mtumishi wake wa Kimasihi, Yehova anasema hivi: “Tazama! Mtumishi wangu atatenda kwa ufahamu. Atakuwa na cheo cha juu na hakika yeye atainuliwa na kutukuzwa sana.” (Isa. 52:13) Kwa kuwa Mwana wake alijitiisha kwa ushikamanifu chini ya enzi Yake kuu na akaendelea kuwa mwaminifu wakati wa jaribu kali zaidi, Yehova alimwinua.
15 Mtume Petro aliandika hivi kumhusu Yesu: “Yeye yuko mkono wa kuume wa Mungu, kwa maana alienda zake mbinguni; na malaika na mamlaka na nguvu vilitiishwa kwake.” (1 Pet. 3:22) Vivyo hivyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso. Kwa sababu hii pia Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya nchi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Flp. 2:8-11.
16. Yesu ‘alitukuzwa sana’ jinsi gani mwaka wa 1914, na ametimiza nini tangu wakati huo?
16 Katika mwaka wa 1914, Yehova alimwinua Yesu hata zaidi. ‘Alitukuzwa sana’ wakati Yehova alipomtawaza kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi. (Zab. 2:6; Dan. 7:13, 14) Tangu wakati huo, Kristo ‘ameenda akitiisha katikati ya adui zake.’ (Zab. 110:2) Kwanza, alimtiisha Shetani na roho wake waovu, kwa kuwatupa chini katika ujirani wa dunia. (Ufu. 12:7-12) Kisha, akitenda akiwa Koreshi Mkuu, Kristo aliwakomboa mabaki ya ndugu zake watiwa-mafuta walio duniani kutoka katika utekwa wa “Babiloni Mkubwa.” (Ufu. 18:2; Isa. 44:28) Amesimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote, na kupitia kazi hiyo, ndugu zake “waliobaki” wamekusanywa kwanza, halafu mamilioni ya “kondoo wengine” wamekusanywa pia, ambao ni waandamani washikamanifu wa “kundi dogo.”—Ufu. 12:17; Yoh. 10:16; Luka 12:32.
17. Tumejifunza nini kufikia sasa kwa kuchunguza unabii wa Isaya kuhusu “mtumishi” huyo?
17 Bila shaka, kujifunza unabii huo wa pekee katika kitabu cha Isaya kumetusaidia tumthamini zaidi Mfalme na Mkombozi wetu, Kristo Yesu. Utii wake akiwa Mwana wakati wa huduma yake duniani unaonyesha kwamba alizoezwa alipokuwa kando ya Baba yake kabla ya kuja duniani. Amejithibitisha kuwa “nuru ya mataifa” kupitia huduma yake mwenyewe na kazi ya kuhubiri ambayo ameisimamia mpaka leo hii. Kama tutakavyoona katika habari inayofuata, unabii mwingine kuhusu Mtumishi huyo wa Kimasihi ulifunua kwamba angeteseka na kudhabihu uhai wake kwa faida yetu. Hayo ni mambo ambayo tunapaswa ‘kuyatazama kwa makini’ kadiri Ukumbusho wa kifo chake unavyokaribia.—Ebr. 12:2, 3.
[Maelezo ya chini]
a Unabii huo unapatikana katika Isaya 42:1-7; 49:1-12; 50:4-9; na 52:13–53:12.
b Ili upate habari zaidi kuhusu unabii ulio katika Isaya 49:1-12, soma kitabu Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote II, ukurasa wa 136-145.
-
-
Mtumishi wa Yehova—‘Alichomwa kwa Silaha kwa Ajili ya Ukosaji Wetu’Mnara wa Mlinzi—2009 | Januari 15
-
-
Mtumishi wa Yehova—‘Alichomwa kwa Silaha kwa Ajili ya Ukosaji Wetu’
“Alikuwa akichomwa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu; alikuwa akipondwa kwa ajili ya makosa yetu. . . . Kwa sababu ya majeraha yake sisi tumeponywa.”—ISA. 53:5.
1. Tunapaswa kukumbuka nini tunapoadhimisha Ukumbusho, na ni unabii gani utakaotusaidia kufanya hivyo?
TUNAADHIMISHA Ukumbusho ili kukumbuka kifo cha Kristo na mambo yote yaliyotimizwa kupitia kifo chake na ufufuo wake. Mwadhimisho huo unatukumbusha kuhusu kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova, kutakaswa kwa jina lake, na kutimizwa kwa kusudi lake, kutia ndani wokovu wa wanadamu. Labda hakuna unabii mwingine katika Biblia ambao unazungumzia waziwazi dhabihu ya Kristo na mambo ambayo yalitimizwa na dhabihu hiyo kuliko ule ulioandikwa katika Isaya 53:3-12. Isaya alitabiri mateso ya Mtumishi huyo na kutoa habari hususa kuhusu kifo cha Kristo na baraka ambazo kifo hicho kingewaletea ndugu zake watiwa-mafuta na ‘kondoo wake wengine.’—Yoh. 10:16.
2. Unabii wa Isaya unathibitisha nini, nasi tutapata faida gani tunapouchunguza?
2 Miaka zaidi ya 700 kabla ya Yesu kuzaliwa duniani, Yehova alimwongoza Isaya kuandika kwamba Mtumishi Wake mchaguliwa atakuwa mwaminifu hata akijaribiwa mpaka mwisho. Jambo hilo la hakika linathibitisha kwamba Yehova alijua kabisa kuwa Mwana wake atabaki akiwa mshikamanifu. Tunapochunguza unabii huo, mioyo yetu itachangamshwa na imani yetu itatiwa nguvu.
“Alidharauliwa” na Kuhesabiwa “Kuwa Asiye na Maana”
3. Kwa nini Wayahudi walipaswa kumkaribisha Yesu, lakini walimpokea jinsi gani?
3 Soma Isaya 53:3. Hebu wazia jinsi Mwana wa Mungu alivyohisi alipolazimika kujinyima shangwe ya kutumikia kando ya Baba yake na kuja duniani na kudhabihu uhai wake ili kuwaokoa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo! (Flp. 2:5-8) Dhabihu yake ilikusudiwa kuleta msamaha wa kweli wa dhambi, nayo ilifananishwa na dhabihu za wanyama zilizotolewa chini ya Sheria ya Musa. (Ebr. 10:1-4) Je, si kweli kwamba alipaswa kukaribishwa na kuheshimiwa, angalau na Wayahudi, ambao walikuwa wakimtarajia Masihi aliyeahidiwa? (Yoh. 6:14) Badala yake, kama Isaya alivyotabiri, Kristo “alidharauliwa” na Wayahudi, nao ‘wakamhesabu kuwa mtu asiye na maana.’ Mtume Yohana aliandika hivi: “Alikuja nyumbani kwake mwenyewe, lakini watu wake mwenyewe hawakumkaribisha.” (Yoh. 1:11) Mtume Petro aliwaambia Wayahudi hivi: “Mungu wa mababu zetu . . . amemtukuza Mtumishi wake, Yesu, ambaye ninyi mlimpeleka na kumkana mbele ya uso wa Pilato, alipokuwa ameamua kumfungua. Ndiyo, ninyi mlimkana huyo aliye mtakatifu na mwadilifu.”—Mdo. 3:13, 14.
4. Yesu alizoeana na ugonjwa katika njia gani?
4 Pia, Isaya alitabiri kwamba Yesu alikusudiwa “kuzoeana na ugonjwa.” Wakati wa huduma yake, bila shaka Yesu alichoka mara kwa mara, lakini hakuna andiko linalosema kwamba aliwahi kuwa mgonjwa. (Yoh. 4:6) Hata hivyo, alijua na alizoea magonjwa ya watu aliowahubiria. Aliwasikitikia na kuwaponya wengi. (Marko 1:32-34) Hivyo, Yesu alitimiza unabii unaosema hivi: “Kwa kweli yeye mwenyewe aliyachukua magonjwa yetu; na kwa habari ya maumivu yetu, yeye aliyabeba.”—Isa. 53:4a; Mt. 8:16, 17.
Ni Kana Kwamba ‘Alipigwa na Mungu’
5. Wayahudi wengi walikuwa na maoni gani kuhusu kifo cha Yesu, na kwa nini jambo hilo lilimfanya ateseke hata zaidi?
5 Soma Isaya 53:4b. Watu wengi wa siku za Yesu hawakuelewa kwa nini aliteseka na kufa. Waliamini kwamba Mungu anamwadhibu, kana kwamba anampiga kwa ugonjwa wenye kuchukiza sana. (Mt. 27:38-44) Wayahudi walidai kwamba Yesu alikufuru. (Marko 14:61-64; Yoh. 10:33) Bila shaka, Yesu hakutenda dhambi wala kukufuru. Lakini kwa kuwa alimpenda sana Baba yake, ni wazi kwamba Mtumishi huyo wa Yehova aliteseka hata zaidi alipowazia kwamba angekufa kwa kushtakiwa kuwa amekufuru. Ingawa hivyo, alikuwa tayari kujitiisha kwa mapenzi ya Yehova.—Mt. 26:39.
6, 7. Ni katika maana gani Yehova ‘alimponda’ Mtumishi wake mwaminifu, na kwa nini jambo hilo ‘lilimpendeza’ Mungu?
6 Si vigumu kuelewa maneno ya unabii wa Isaya yanayoonyesha kwamba watu fulani wangefikiri kuwa Kristo ‘amepigwa na Mungu,’ lakini inaweza kuwa vigumu kuelewa maneno haya yaliyotabiriwa katika unabii huohuo: “Yehova alipendezwa kumponda.” (Isa. 53:10) Je, kweli Yehova ‘angependezwa kumponda’ mtumishi wake na tayari alikuwa amesema hivi: “Tazama! Mtumishi wangu, . . . mchaguliwa wangu, ambaye nafsi yangu imemkubali”? (Isa. 42:1) Jambo hilo lilimletea Yehova shangwe katika maana gani?
7 Ili tuelewe sehemu hiyo ya unabii huo, tunapaswa kukumbuka kwamba Shetani alipotilia shaka uhalali wa enzi kuu ya Yehova, alitilia shaka ushikamanifu wa watumishi wote wa Mungu mbinguni na duniani. (Ayu. 1:9-11; 2:3-5) Yesu alipoendelea kuwa mwaminifu kufikia kifo, alijibu kikamili dai la Shetani. Hivyo, ingawa Yehova aliruhusu maadui wamuue Kristo, bila shaka Yehova aliteseka alipomwona Mtumishi wake mchaguliwa akiuawa. Hata hivyo, Yehova alipendezwa sana alipomwona Mwana wake akidumisha uaminifu kikamili. (Met. 27:11) Zaidi ya hayo, Yehova alipata shangwe kubwa kwa sababu alijua faida ambazo kifo cha Mwana wake kingewaletea wanadamu wanaotubu.—Luka 15:7.
‘Alichomwa kwa Silaha kwa Ajili ya Ukosaji Wetu’
8, 9. (a) Yesu ‘alichomwa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu’ katika maana gani? (b) Petro alithibitisha jambo hilo jinsi gani?
8 Soma Isaya 53:6. Kama kondoo waliopotea, wanadamu wenye dhambi wameenda huku na huku, wakitafuta kukombolewa kutoka kwa magonjwa na kifo ambacho walirithi kutoka kwa Adamu. (1 Pet. 2:25) Kwa kuwa wazao wa Adamu si wakamilifu, hakuna hata mmoja wao ambaye angeweza kulipia kile ambacho Adamu alipoteza. (Zab. 49:7) Hata hivyo, akichochewa na upendo wake mwingi, “Yehova amefanya kosa letu sote likutane na huyo,” Mwana wake mpendwa na Mtumishi mchaguliwa. Kwa kukubali ‘kuchomwa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu’ na ‘kupondwa kwa ajili ya makosa yetu,’ Kristo alichukua dhambi zetu juu ya mti na kufa badala yetu.
9 Mtume Petro aliandika hivi: “Mliitwa kwenye mwendo huu, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu. Yeye mwenyewe alichukua dhambi zetu katika mwili wake mwenyewe juu ya mti, ili tuachane kabisa na dhambi na kuishi kwa uadilifu.” Kisha, akinukuu unabii wa Isaya, Petro aliongeza hivi: “Na ‘kwa mapigo yake mliponywa.’” (1 Pet. 2:21, 24; Isa. 53:5) Hilo liliwawezesha watenda-dhambi kupatanishwa na Mungu, kama maneno haya ya Petro yanavyoonyesha: “Kristo alikufa mara moja kwa wakati wote kuzihusu dhambi, mtu mwadilifu kwa ajili ya wasio waadilifu, ili awaongoze ninyi kwa Mungu.”—1 Pet. 3:18.
‘Aliletwa Kama Kondoo Machinjioni’
10. (a) Yohana Mbatizaji alisema nini kumhusu Yesu? (b) Kwa nini maneno ya Yohana yalifaa?
10 Soma Isaya 53:7, 8. Yohana Mbatizaji alipomwona Yesu akimjia, alisema hivi: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu!” (Yoh. 1:29) Yohana alipomtaja Yesu kuwa Mwana-Kondoo, huenda alikuwa akikumbuka maneno haya ya Isaya: “Alikuwa akiletwa kama kondoo [au, mwana-kondoo] machinjioni.” (Isa. 53:7) Isaya alitabiri hivi: “Aliimwaga nafsi yake mpaka kufa.” (Isa. 53:12) Ndiyo, usiku ambao Yesu alianzisha Ukumbusho wa kifo chake, aliwapa wale mitume 11 waaminifu kikombe cha divai na kusema hivi: “Hii inamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.”—Mt. 26:28.
11, 12. (a) Tendo la Isaka la kukubali kwa kupenda kutolewa kuwa dhabihu linaonyesha nini kuhusu dhabihu ya Kristo? (b) Tunapoadhimisha Ukumbusho, tunapaswa kukumbuka nini kumhusu Abrahamu Mkuu Zaidi, Yehova?
11 Kama Isaka, Yesu alikuwa tayari kutolewa akiwa dhabihu juu ya madhabahu ya mapenzi ya Yehova kwa ajili yake. (Mwa. 22:1, 2, 9-13; Ebr. 10:5-10) Ingawa Isaka alikubali kwa kupenda kutolewa kuwa dhabihu, Abrahamu ndiye aliyejaribu kutoa dhabihu hiyo. (Ebr. 11:17) Vivyo hivyo, Yesu alikubali kwamba atakufa, lakini Yehova ndiye Mwanzilishi wa mpango wa dhabihu ya ukombozi. Dhabihu ya Mwana wake ilionyesha kwamba Mungu anawapenda sana wanadamu.
12 Yesu mwenyewe alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Mtume Paulo aliandika hivi: “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Rom. 5:8) Kwa hiyo, tunapomheshimu Kristo kwa kukumbuka kifo chake, hatupaswi kamwe kusahau kwamba yule aliyeamua jinsi dhabihu hiyo itakavyolipwa si mwingine ila Abrahamu Mkuu Zaidi, Yehova. Tunaadhimisha Ukumbusho ili kumsifu.
Mtumishi Huyo Anawaletea “Watu Wengi Msimamo wa Uadilifu”
13, 14. Ni kwa njia gani Mtumishi wa Yehova amewaletea “watu wengi msimamo wa uadilifu”?
13 Soma Isaya 53:11, 12. Yehova alisema hivi kuhusu Mtumishi wake mchaguliwa: “Mtu mwadilifu, mtumishi wangu, atawaletea watu wengi msimamo wa uadilifu.” Jinsi gani? Sehemu ya mwisho ya mstari wa 12 inatoa wazo linalotusaidia kupata jibu. “[Mtumishi huyo] aliingilia kati kwa ajili ya wakosaji.” Wazao wote wa Adamu wanazaliwa wakiwa watenda-dhambi, au “wakosaji,” na hivyo wanapata “mshahara ambao dhambi hulipa,” yaani, kifo. (Rom. 5:12; 6:23) Ni lazima mwanadamu mwenye dhambi apatanishwe na Yehova. Sura ya 53 ya unabii wa Isaya inaeleza kwa njia yenye kuvutia sana jinsi ambavyo Yesu “aliingilia kati” au kuwa mpatanishi kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi, inaposema hivi: “Adhabu iliyokusudiwa kuleta amani yetu ilikuwa juu yake, na kwa sababu ya majeraha yake sisi tumeponywa.”—Isa. 53:5.
14 Kwa kubeba dhambi zetu na kufa kwa ajili yetu, Kristo aliwaletea “watu wengi msimamo wa uadilifu.” Paulo aliandika hivi: “Mungu aliona ni vema ujazo wote ukae katika yeye [Kristo], na kupitia yeye apatanishe tena kwake mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu aliyomwaga juu ya mti wa mateso, hata kama ni vitu vilivyo duniani au vitu vilivyo mbinguni.”—Kol. 1:19, 20.
15. (a) “Vitu vilivyo mbinguni” vilivyotajwa na Paulo ni akina nani? (b) Ni nani tu ambao wanastahili kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho, na kwa nini?
15 “Vitu vilivyo mbinguni” ambavyo vimepatanishwa na Yehova kupitia damu ya Kristo iliyomwagwa ni wale Wakristo watiwa-mafuta, walioitwa watawale pamoja na Kristo mbinguni. Wakristo ambao ni “washiriki wa mwito wa mbinguni” wanatangazwa kuwa “waadilifu kwa ajili ya uzima.” (Ebr. 3:1; Rom. 5:1, 18) Hivyo, Yehova anawakubali kuwa wana wake wa kiroho. Roho takatifu inawatolea ushahidi kwamba wao ni “warithi pamoja na Kristo,” walioitwa wawe wafalme na makuhani katika Ufalme wake wa mbinguni. (Rom. 8:15-17; Ufu. 5:9, 10) Wanakuwa sehemu ya taifa la Israeli la kiroho, “Israeli wa Mungu,” nao wanaingizwa katika “agano jipya.” (Yer. 31:31-34; Gal. 6:16) Wakiwa washiriki wa agano jipya, wanastahili kula na kunywa ile mifano ya Ukumbusho, ambayo inatia ndani kikombe cha divai nyekundu, ambacho Yesu alisema hivi kukihusu: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu, ambayo itamwagwa kwa ajili yenu.”—Luka 22:20.
16. “Vitu vilivyo duniani” ni akina nani, na ni kwa njia gani wanawezeshwa kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Yehova?
16 “Vitu vilivyo duniani” ni kondoo wengine wa Kristo, ambao wana tumaini la kuishi milele duniani. Mtumishi mchaguliwa wa Yehova anawawezesha pia kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Yehova. Kwa kuwa wana imani katika dhabihu ya ukombozi ya Kristo na “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” Yehova anawatangaza kuwa waadilifu, si ili wawe wana wa kiroho, bali ili wawe marafiki wake, na kuwapa tumaini zuri ajabu la kuokoka “ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:9, 10, 14; Yak. 2:23) Kwa kuwa hawako katika lile agano jipya na hawana tumaini la kuishi mbinguni, kondoo hao wengine hawali mkate wala kunywa divai wakati wa Ukumbusho bali wanahudhuria wakiwa watazamaji wenye heshima.
Tunamshukuru Sana Yehova na Mtumishi Wake Aliyekubaliwa!
17. Kuchunguza unabii mbalimbali wa Isaya kuhusu Mtumishi huyo kumetusaidia jinsi gani kutayarisha akili zetu kwa ajili ya Ukumbusho?
17 Kuchunguza unabii mbalimbali wa Isaya kuhusu Mtumishi huyo ni njia nzuri sana ya kutayarisha akili zetu kwa ajili ya Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kupitia uchunguzi huo, ‘tumemtazama kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu.’ (Ebr. 12:2) Tumejifunza kwamba Mwana wa Mungu si mwasi. Yeye si kama Shetani, bali anafurahia kufundishwa na Yehova, naye anamtambua kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu. Tumeona kwamba wakati wa huduma ya Yesu duniani, aliwahurumia watu aliowahubiria na kuwaponya wengi wao kimwili na kiroho. Hivyo, alionyesha mambo atakayofanya akiwa Mfalme wa Kimasihi katika mfumo mpya wa mambo wakati “atakapoweka haki duniani.” (Isa. 42:4) Bidii aliyoonyesha alipohubiri kuhusu Ufalme akiwa “nuru ya mataifa,” inawakumbusha wafuasi wake wahubiri habari njema kwa bidii katika dunia yote.—Isa. 42:6.
18. Kwa nini unabii wa Isaya unachochea mioyo yetu kumshukuru sana Yehova na Mtumishi wake mwaminifu?
18 Pia, unabii wa Isaya unatusaidia kuelewa vizuri zaidi jinsi Yehova alivyojidhabihu sana alipomtuma Mwana wake mpendwa duniani ateseke na kufa kwa ajili yetu. Yehova hakupendezwa kuona Mwana wake akiteseka, lakini alipendezwa kuona Yesu akiendelea kuwa mwaminifu kikamili mpaka kifo. Kama Yehova, tunapaswa pia kupendezwa na jambo hilo, na kutambua mambo yote ambayo Yesu alifanya ili kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo na kulitakasa jina la Yehova, na hivyo kutetea uhalali wa enzi Yake kuu. Zaidi ya hayo, Kristo alibeba dhambi zetu na kufa kwa ajili yetu. Kwa njia hiyo, aliwezesha kundi dogo la ndugu zake watiwa-mafuta na kondoo wengine kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Yehova. Tutakapokusanyika pamoja kwa ajili ya Ukumbusho, acheni mioyo yetu ichochewe kumshukuru sana Yehova na Mtumishi wake mwaminifu.
-