-
“Nyumba ya Sala kwa Mataifa Yote”Mnara wa Mlinzi—1996 | Julai 1
-
-
“Nyumba ya Sala kwa Mataifa Yote”
“Je! haikuandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote?”—MARKO 11:17.
1. Mwanzoni Adamu na Hawa walifurahia uhusiano wa aina gani pamoja na Mungu?
ADAMU na Hawa walipoumbwa, walifurahia uhusiano wa karibu pamoja na Baba yao wa kimbingu. Yehova Mungu aliwasiliana nao na akaonyesha makusudi yake ya ajabu kwa ajili ya jamii ya kibinadamu. Kwa hakika, mara nyingi walisukumwa kububujika katika kumsifu Yehova kwa sababu ya kazi zake tukufu za uumbaji. Ikiwa Adamu na Hawa walihitaji mwongozo walipokuwa wakitafakari fungu lao la kuwa wazazi wa wakati ujao wa familia ya kibinadamu, wangeweza kumfikia Mungu wakiwa mwomwote katika makao yao ya Paradiso. Hawakuhitaji utumishi mbalimbali wa kuhani hekaluni.—Mwanzo 1:28.
2. Ni badiliko gani lililotokea Adamu na Hawa walipotenda dhambi?
2 Hali ilibadilika wakati malaika mwasi alipomshawishi Hawa afikiri kwamba hali yake maishani ingeboreka ikiwa angekataa enzi kuu ya Yehova, akitaarifu kwamba Hawa ‘angekuwa kama Mungu.’ Hivyo Hawa akala tunda la mti ambao Mungu alikuwa amewakataza wasile. Kisha Shetani akamtumia Hawa kumshawishi mumeye. Kwa kuhuzunisha, Adamu alimsikiliza mkeye mwenye dhambi, akionyesha kwamba alithamini uhusiano wake pamoja naye zaidi ya uhusiano wake pamoja na Mungu. (Mwanzo 3:4-7) Kwa kweli, Adamu na Hawa walimchagua Shetani kuwa mungu wao.—Linganisha 2 Wakorintho 4:4.
3. Ni matokeo gani mabaya yaliyotokana na uasi wa Adamu na Hawa?
3 Kwa kufanya hivyo, mume na mke wa kwanza wa kibinadamu walipoteza uhusiano wao wenye thamani pamoja na Mungu na pia taraja la kuishi milele katika paradiso ya kidunia. (Mwanzo 2:16, 17) Hatimaye miili yao yenye dhambi ilizorota hata wakafa. Wazao wao walirithi hali hii yenye dhambi. “Hivyo,” Biblia hueleza, “mauti ikawafikia watu wote.”—Warumi 5:12.
4. Ni tumaini gani lililotolewa na Mungu kwa wanadamu wenye dhambi?
4 Kitu fulani kilihitajiwa ili kupatanisha wanadamu wenye dhambi pamoja na Muumba wao mtakatifu. Alipokuwa akiwahukumu Adamu na Hawa, Mungu aliwatolea tumaini wazao wao wa wakati ujao kwa kuahidi “mbegu” ambayo ingeokoa wanadamu kutoka katika matokeo ya uasi wa Shetani. (Mwanzo 3:15, NW) Baadaye, Mungu alifunua kwamba ile Mbegu ya baraka ingekuja kupitia Abrahamu. (Mwanzo 22:18) Akifikiria kusudi hili lenye upendo, Mungu alichagua wazao wa Abrahamu, Waisraeli, wawe taifa lake teule.
5. Kwa nini tupendezwe na mambo madogo-madogo ya agano la Sheria la Mungu pamoja na Israeli?
5 Katika 1513 K.W.K., Waisraeli waliingia katika uhusiano wa agano pamoja na Mungu wakakubali kutii sheria zake. Agano hilo la Sheria lapaswa kuwa la upendezi mkubwa kwa wote watakao kumwabudu Mungu leo kwa kuwa lilielekezea Mbegu iliyoahidiwa. Paulo alisema lilitia ndani “kivuli cha mema yatakayokuwa.” (Waebrania 10:1) Paulo alipotoa taarifa hiyo, alikuwa akizungumzia utumishi wa makuhani wa Israeli kwenye tabenakulo lenye kuchukulika, au hema la ibada. Liliitwa “hekalu la BWANA” au “nyumbani kwa BWANA.” (1 Samweli 1:9, 24) Kwa kuchunguza utumishi mtakatifu uliofanywa kwenye nyumba ya Yehova ya kidunia, twaweza kuthamini kikamili zaidi mpango wenye rehema ambao kwa huo wanadamu wenye dhambi leo waweza kupatanishwa pamoja na Mungu.
Patakatifu Zaidi Sana
6. Ni nini kilichokuwa katika Patakatifu Zaidi Sana, na kuwapo kwa Mungu kuliwakilishwaje hapo?
6 “Yeye aliye juu hakai katika nyumba zilizofanywa kwa mikono,” Biblia hutaarifu. (Matendo 7:48) Hata hivyo, kuwapo kwa Mungu katika nyumba yake ya kidunia kuliwakilishwa na wingu katika chumba cha ndani zaidi cha Patakatifu Zaidi Sana. (Mambo ya Walawi 16:2) Kwa wazi, wingu hilo liling’aa kwa wangavu, likiandaa nuru katika Patakatifu Zaidi Sana. Lilikuwa juu ya sanduku takatifu lililoitwa “sanduku la ushuhuda,” lililokuwa na mabamba ya mawe yaliyonakshiwa baadhi ya amri ambazo Mungu aliwapa Waisraeli. Kwenye kifuniko cha hilo Sanduku kulikuwa na makerubi wawili wa dhahabu wenye mabawa yaliyonyooshwa, yaliyofananisha viumbe wa roho wa daraja la juu katika tengenezo la Mungu la kimbingu. Wingu la nuru la kimuujiza lilikuwa juu ya kifuniko na kati ya makerubi. (Kutoka 25:22) Hilo ilionyesha wazo la Mungu Mweza Yote akiwa ametawazwa juu ya gari la kimbingu linalotegemezwa na makerubi walio hai. (1 Mambo ya Nyakati 28:18) Hiyo ndiyo sababu Mfalme Hezekia alisali hivi: “Ee BWANA wa majeshi, Mungu wa Israeli, ukaaye juu ya makerubi.”—Isaya 37:16.
Patakatifu
7. Ni vitu vipi vilivyokuwamo katika Patakatifu?
7 Chumba cha pili cha tabenakulo kiliitwa Patakatifu. Ndani ya sehemu hii, kushotoni mwa mwingilio palisimama kinara cha taa chenye kupendeza kilichokuwa na matawi saba, na kuumeni palikuwa na meza ya mkate wa wonyesho. Mbele kabisa palisimama madhabahu ambayo kutoka kwayo harufu ya uvumba wenye kufukizwa ilipaa. Ilikuwa mbele ya pazia lililotenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi Sana.
8. Makuhani walitimiza wajibu gani mbalimbali kwa ukawaida katika Patakatifu?
8 Kila asubuhi na kila jioni, kuhani alipaswa kuingia ndani ya tabenakulo na kufukiza uvumba juu ya madhabahu ya uvumba. (Kutoka 30:7, 8) Asubuhi, huku uvumba ukifukizwa, zile taa saba zilizokuwa kwenye kinara cha dhahabu zilihitaji kuongezwa mafuta. Jioni hizo taa ziliwashwa ili kuandaa nuru katika Patakatifu. Kila Sabato kuhani alipaswa kuweka mikate mipya 12 kwenye meza ya mkate wa wonyesho.—Mambo ya Walawi 24:4-8.
Ule Ua
9. Kusudi la birika la maji lilikuwa nini, nasi twaweza kupata somo gani kutokana na hilo?
9 Tabenakulo pia lilikuwa na ua, uliozungukwa na uzio wa nguo za hema. Uani humu kulikuwa na birika kubwa ambapo makuhani waliosha mikono na miguu yao kabla ya kuingia ndani ya Patakatifu. Walipaswa pia kujiosha kabla ya kutoa dhabihu juu ya madhabahu iliyokuwa uani. (Kutoka 30:18-21) Takwa hilo la usafi ni kikumbusha chenye nguvu kwa watumishi wa Mungu leo kwamba lazima wajitahidi kuwa safi kimwili, kiadili, kiakili, na kiroho ikiwa wanataka ibada yao ikubalike kwa Mungu. (2 Wakorintho 7:1) Hatimaye, watumwa wa hekalu wasio Waisraeli ndio walileta zile kuni za ule moto ulio juu ya madhabahu na yale maji ya birika.—Yoshua 9:27.
10. Ni yapi baadhi ya matoleo yaliyofanywa juu ya madhabahu ya dhabihu?
10 Kila asubuhi na kila jioni, kondoo-dume mchanga wa kidhabihu alichomwa juu ya madhabahu pamoja na toleo la nafaka na la kinywaji. (Kutoka 29:38-41) Dhabihu nyingine zilitolewa katika siku za pekee. Nyakati fulani dhabihu ilipaswa kutolewa kwa sababu ya dhambi hususa ya kibinafsi. (Mambo ya Walawi 5:5, 6) Nyakati nyingine Mwisraeli angeweza kutoa dhabihu ya ushirika ya hiari ambayo kutoka hiyo visehemu vililiwa na makuhani na yule aliyefanya hilo toleo. Hilo lilionyesha kwamba binadamu watenda-dhambi wangeweza kuwa na amani na Mungu, wakifurahia mlo pamoja naye, kwa kusema kitamathali. Hata mkazi-mgeni angeweza kuwa mwabudu wa Yehova na awe na pendeleo la kutoa matoleo ya hiari nyumbani Kwake. Lakini ili kumwonyesha Yehova staha inayostahili, makuhani waliweza tu kukubali matoleo yaliyo bora kabisa. Unga wa matoleo ya nafaka ulipaswa kusagwa uwe mwembamba, na wanyama wa dhabihu walipaswa kuwa bila kasoro yoyote.—Mambo ya Walawi 2:1; 22:18-20; Malaki 1:6-8.
11. (a) Damu ya wanyama wa dhabihu ilifanywa nini, jambo hilo lilirejezea nini? (b) Mungu anaonaje damu ya binadamu na ya wanyama?
11 Damu ya dhabihu hizo ililetwa madhabahuni. Hiyo ilitumika ikiwa kikumbusha cha kila siku kwa taifa kwamba walikuwa watenda-dhambi wenye uhitaji wa mkombozi ambaye damu yake iliyomwagwa ingefunika dhambi zao kwa wakati wote na kuwaokoa na kifo. (Warumi 7:24, 25; Wagalatia 3:24; linganisha Waebrania 10:3.) Utumizi huu mtakatifu wa damu pia uliwakumbusha Waisraeli kwamba damu huwakilisha uhai na kwamba uhai ni mali ya Mungu. Sikuzote Mungu amewakataza wanadamu kutumia damu kwa njia nyingine yoyote.—Mwanzo 9:4; Mambo ya Walawi 17:10-12; Matendo 15:28, 29.
Siku ya Kufunika
12, 13. (a) Siku ya Kufunika ilikuwa nini? (b) Kabla ya kuhani wa cheo cha juu kuleta damu ndani ya Patakatifu Zaidi Sana, alipaswa kufanya nini?
12 Mara moja kwa mwaka katika ile iliyoitwa Siku ya Kufunika, taifa lote la Israeli, kutia ndani wakazi-wageni waliomwabudu Yehova, lilipaswa kuacha kazi zote na kufunga. (Mambo ya Walawi 16:29, 30) Kwenye siku hii yenye umaana, taifa lilisafishwa lisiwe na dhambi kwa njia ya kielezi ili lifurahie mahusiano yenye amani pamoja na Mungu kwa mwaka mwingine. Acheni tuwazie hiyo mandhari na kuchunguza baadhi ya mambo makuu.
13 Kuhani wa cheo cha juu yumo uani mwa tabenakulo. Baada ya kujiosha kwenye birika la maji, yeye achinja fahali kwa ajili ya dhabihu. Damu ya huyo fahali inamwagwa bakulini; itatumiwa kwa njia ya pekee ili kufunika dhambi za kabila la kikuhani la Lawi. (Mambo ya Walawi 16:4, 6, 11) Lakini kabla ya kuendelea kutoa dhabihu, kuna jambo ambalo kuhani wa cheo cha juu lazima afanye. Yeye achukua uvumba wenye marashi (yaelekea akiuweka ndani ya kijiko cha kupakulia) na makaa-mawe yenye moto kutoka madhabahu ndani ya kishikio cha moto. Sasa aingia ndani ya Patakatifu na kutembea kuelekea lile pazia la Patakatifu Zaidi Sana. Anapita polepole kuzunguka pazia na kusimama mbele ya sanduku la agano. Baadaye, bila kuonekana na mwanadamu mwingine yeyote, anamwaga uvumba kwenye yale makaa-mawe yenye moto, na Patakatifu Zaidi Sana panajawa na wingu lenye kunukia.—Mambo ya Walawi 16:12, 13.
14. Kwa nini kuhani wa cheo cha juu alipaswa kuingia ndani ya Patakatifu Zaidi Sana akiwa na damu ya wanyama wawili walio tofauti?
14 Sasa Mungu yu tayari kuonyesha rehema na kuridhishwa kwa njia ya kielezi. Kwa sababu hiyo kifuniko cha lile Sanduku kiliitwa “kiti cha rehema” au “kifuniko cha kufunikia.” (Waebrania 9:5, NW, kielezi chini) Kuhani wa cheo cha juu aondoka Patakatifu pa Patakatifu, atwaa damu ya fahali, na kuingia tena ndani ya Patakatifu Zaidi Sana. Kama ilivyoamuriwa katika Sheria, achovya kidole chake ndani ya hiyo damu na kuinyunyiza mara saba mbele ya kifuniko cha Sanduku. (Mambo ya Walawi 16:14) Halafu arudi uani na kuchinja mbuzi, ambaye ni toleo la dhambi “kwa ajili ya watu.” Aleta kiasi fulani cha damu ya huyo mbuzi ndani ya Patakatifu Zaidi Sana na kufanya jambo lilelile alilofanya na damu ya fahali. (Mambo ya Walawi 16:15) Pia utumishi mwingine mbalimbali muhimu ulifanywa Siku ya Kufunika. Kwa kielelezo, kuhani wa cheo cha juu alipaswa kuweka mikono yake juu ya kichwa cha mbuzi wa pili na kuungama juu yake “uovu wote wa wana wa Israeli.” Kisha mbuzi huyo aliye hai alipelekwa aende jangwani ili achukue dhambi za taifa kwa njia ya kitamathali. Kwa njia hiyo ufuniko ulifanywa kila mwaka “kwa ajili ya makuhani, na kwa ajili ya watu wote wa kusanyiko.”—Mambo ya Walawi 16:16, 21, 22, 33.
15. (a) Hekalu la Sulemani lilifananaje na tabenakulo? (b) Kitabu cha Waebrania chasema nini kuhusu utumishi mtakatifu uliofanywa kwenye tabenakulo na pia hekaluni?
15 Kwa miaka 486 ya kwanza ya historia ya Israeli wakiwa watu wa agano wa Mungu, tabenakulo lenye kuchukulika lilitumika kwao likiwa mahali pa ibada kwa Mungu wao, Yehova. Kisha, Sulemani wa Israeli akapewa pendeleo la kujenga jengo la kudumu. Ingawa hekalu hilo lilitazamiwa kuwa kubwa zaidi na lenye madoido zaidi, ramani iliyotolewa kimungu ilifuata kiolezo kilekile cha tabenakulo. Kama tabenakulo, lilikuwa kielezi cha mpango mkuu zaidi na wenye matokeo zaidi wa ibada ambao Yehova ‘angeuweka wala si mwanadamu.’—Waebrania 8:2, 5; 9:9, 11.
Hekalu la Kwanza na la Pili
16. (a) Sulemani alifanya ombi gani lenye upendo alipokuwa akiweka wakfu hekalu? (b) Yehova alionyeshaje kukubali kwake sala ya Sulemani?
16 Alipokuwa akiliweka wakfu hekalu hilo tukufu, Sulemani alitia ndani ombi hili lililopuliziwa: “Hata na mgeni naye, asiyekuwa mmoja wa watu wako Israeli, atakapokuja kutoka nchi iliyo mbali sana kwa ajili ya jina lako kuu, . . . ; hao watakapokuja na kuomba wakiielekea nyumba hii; basi usikie huko mbinguni, toka makaoni mwako, ukatende yote atakayokuomba huyo mgeni; ili watu wote wa dunia wapate kulijua jina lako, na kukuacha wewe, kama watu wako Israeli, tena wajue ya kuwa nyumba hii niliyoijenga imeitwa kwa jina lako.” (2 Mambo ya Nyakati 6:32, 33) Kwa njia ya wazi, Mungu alionyesha kukubali kwake sala ya Sulemani ya kuweka wakfu. Mwali wa moto ulianguka kutoka mbinguni, ukateketeza dhabihu za wanyama juu ya madhabahu, nao utukufu wa Yehova ukalijaza hekalu.—2 Mambo ya Nyakati 7:1-3.
17. Ni nini hatimaye kilicholipata hekalu lililojengwa na Sulemani, na kwa nini?
17 Kwa kuhuzunisha, Waisraeli walipoteza hofu yao ifaayo kwa Yehova. Hatimaye, walichafua jina lake kuu kupitia matendo ya umwagaji wa damu, ibada ya sanamu, uzinzi, ngono ya maharimu, na kupitia kuwatenda vibaya mayatima, wajane, na wageni. (Ezekieli 22:2, 3, 7, 11, 12, 26, 29) Kwa njia hiyo, katika mwaka wa 607 K.W.K., Mungu alitekeleza hukumu kwa kuleta majeshi ya Babiloni yapate kuliharibu lile hekalu. Waisraeli waliookoka walichukuliwa mateka Babiloni.
18. Kwenye hekalu la pili, ni mapendeleo gani yaliyofunguliwa kwa baadhi ya wanaume wasio Waisraeli waliotegemeza ibada ya Yehova kwa moyo wote?
18 Baada ya miaka 70 baki la Kiyahudi lenye kutubu lilirudi Yerusalemu nalo likapewa pendeleo la kujenga upya hekalu la Yehova. Kwa kupendeza, kulikuwa na upungufu wa makuhani na Walawi wa kutumikia katika hekalu hili la pili. Likiwa tokeo, Wanethini, waliokuwa wazao wa watumwa wa hekaluni wasio Waisraeli, walipewa mapendeleo makubwa zaidi wakiwa watumishi wa nyumba ya Mungu. Hata hivyo, hawakuwa sawa na makuhani na Walawi kamwe.—Ezra 7:24; 8:17, 20.
19. Mungu alitoa ahadi gani kuhusiana na hekalu la pili, na maneno hayo yalikujaje kuwa kweli?
19 Mwanzoni ilionekana kwamba hekalu la pili halingeweza kulinganishwa na lile la awali. (Hagai 2:3) Lakini Yehova aliahidi: “Nami nitatikisa mataifa yote, na vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote vitakuja; nami nitaijaza nyumba hii utukufu, . . . Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza.” (Hagai 2:7, 9) Kama ilivyotabiriwa, hekalu la pili kwa kweli lilifikia utukufu mkuu zaidi. Lilidumu miaka 164 zaidi, na waabudu wengi zaidi kutoka nchi nyingi zaidi walimiminika kwenye nyua zalo. (Linganisha Matendo 2:5-11.) Kurekebishwa kwa hekalu la pili kulianza katika siku za Mfalme Herode, na nyua zalo zilipanuliwa. Likiwa juu ya jukwaa kubwa sana la mawe na kuzungukwa na safu za nguzo zenye kupendeza, lililingana kwa uzuri na hekalu la kwanza lililojengwa na Sulemani. Lilitia ndani ua mkubwa wa nje kwa ajili ya watu wa mataifa waliotaka kumwabudu Yehova. Ukuta wa kuzuia wa mawe ulitenganisha Ua huo wa Wasio Wayahudi na nyua za ndani zilizokuwa za Waisraeli peke yao.
20. (a) Ni tofauti gani yenye kutokeza iliyotia alama hekalu lililojengwa upya? (b) Ni nini kilichoonyesha kwamba Wayahudi walikuwa na maoni yasiyofaa juu ya hekalu, na Yesu alifanya nini kwa kuitikia hilo?
20 Hekalu hilo la pili liliheshimiwa kuwa na Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, akifundisha katika nyua zalo. Lakini sawa na hekalu la kwanza, Wayahudi kwa ujumla hawakuwa na mtazamo ufaao wa pendeleo lao la kuwa watunzaji wa nyumba ya Mungu. Hata waliruhusu wafanya-biashara kufanya biashara katika ua wa Wasio Wayahudi. Zaidi ya hayo, watu waliruhusiwa kulitumia hekalu kuwa njia ya mkato walipokuwa wakichukua vitu huku na huku Yerusalemu. Siku nne kabla ya kifo chake, Yesu alisafisha hekalu lisiwe na mazoea hayo yasiyo ya kidini, huku akifuliza kusema: “Je! haikuandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote? Bali ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang’anyi.”—Marko 11:15-17.
Mungu Aiacha Nyumba Yake ya Kidunia Milele
21. Yesu alionyesha nini kuhusu hekalu la Yerusalemu?
21 Kwa sababu ya tendo la Yesu lenye moyo mkuu katika kutegemeza ibada safi ya Mungu, viongozi wa kidini Wayahudi waliazimia kumuua. (Marko 11:18) Akijua kwamba angeuawa kimakusudi karibuni, Yesu aliwaambia viongozi wa kidini Wayahudi hivi: “Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:37, 38) Kwa njia hiyo alionyesha kwamba upesi Mungu asingekubali tena namna ya ibada iliyozoewa kwenye hekalu halisi katika Yerusalemu. Lisingeendelea tena kuwa “nyumba ya sala kwa mataifa yote.” Wanafunzi wake walipomwonyesha Yesu yale majengo matukufu ya hekalu, alisema hivi: “Hamyaoni haya yote? . . . Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa.”—Mathayo 24:1, 2.
22. (a) Maneno ya Yesu juu ya hekalu yalitimizwaje? (b) Badala ya kukazia matumaini yao jiji la kidunia, Wakristo wa mapema walitafuta nini?
22 Unabii wa Yesu ulitimizwa miaka 37 baadaye katika mwaka wa 70 W.K., majeshi ya Roma yalipoharibu Yerusalemu na hekalu lalo. Hilo liliandaa ithibati yenye kutokeza ya kwamba Mungu kwa kweli alikuwa ameacha nyumba yake halisi. Yesu hakutabiri kamwe kujengwa upya kwa hekalu jingine Yerusalemu. Kuhusu jiji hilo la kidunia, Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania hivi: “Maana hapa hatuna mji udumuo, bali twautafuta ule ujao.” (Waebrania 13:14) Wakristo wa mapema walitazamia kuwa sehemu ya “Yerusalemu la kimbingu”—Ufalme wa Mungu ulio kama jiji. (Waebrania 12:22, NW) Kwa njia hiyo, kitovu cha ibada ya kweli ya Yehova hakiko tena katika hekalu halisi duniani. Katika makala yetu ifuatayo, tutachunguza mpango ulio bora zaidi ambao Mungu amewawekea wote wanaotamani kumwabudu yeye “katika roho na kweli.”—Yohana 4:21, 24.
-
-
Hekalu Kubwa la Kiroho la YehovaMnara wa Mlinzi—1996 | Julai 1
-
-
Hekalu Kubwa la Kiroho la Yehova
“Tunaye kuhani mkuu [“wa cheo cha juu,” “NW”] wa namna hii, . . . mhudumu wa patakatifu, na wa ile hema ya kweli, ambayo Bwana aliiweka wala si mwanadamu.”—WAEBRANIA 8:1, 2.
1. Mungu alifanya uandalizi gani wenye upendo kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi?
KWA sababu ya upendo wake mkubwa kwa wanadamu, Yehova Mungu aliandaa dhabihu ili kuondolea mbali dhambi za ulimwengu. (Yohana 1:29; 3:16) Hilo lilitaka kuhamisha uhai wa Mwana wake mzaliwa wa kwanza kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira Myahudi aitwaye Mariamu. Malaika wa Yehova alimweleza Mariamu kwa wazi kwamba kitoto ambacho angechukua mimba kingeitwa “kitakatifu, Mwana wa Mungu.” (Luka 1:34, 35) Yusufu, aliyekuwa mchumba wa Mariamu, aliambiwa juu ya kuchukuliwa mimba kwa Yesu kimuujiza, na akapata kujua kwamba huyo ‘angewaokoa watu wake na dhambi zao.’—Mathayo 1:20, 21.
2. Yesu alifanya nini alipokuwa na umri wa miaka ipatayo 30, na kwa nini?
2 Yesu alipokuwa akikua, lazima awe alielewa baadhi ya mambo hayo ya hakika kuhusu kuzaliwa kwake kimuujiza. Alijua kwamba Baba yake wa kimbingu alikuwa na kazi ya kuokoa uhai aliyotaka afanye duniani. Kwa hiyo akiwa mtu mzima kabisa mwenye umri wa miaka ipatayo 30, Yesu alimjia Yohana nabii wa Mungu, ili abatizwe katika Mto Yordani.—Marko 1:9; Luka 3:23.
3. (a) Yesu alimaanisha nini kwa maneno, “Dhabihu na toleo hukutaka”? (b) Ni kielelezo gani chenye kutokeza alichoweka Yesu kwa wote wanaotaka kuwa wanafunzi wake?
3 Wakati wa ubatizo wake Yesu alikuwa akisali. (Luka 3:21) Kwa hakika, kuanzia wakati huo maishani mwake na kuendelea, alitimiza maneno ya Zaburi 40:6-8, kama ionyeshwavyo baadaye na mtume Paulo: “Dhabihu na toleo hukutaka, lakini mwili uliniwekea tayari.” (Waebrania 10:5) Kwa njia hiyo Yesu alionyesha kujua kwake kwamba Mungu ‘hakutaka’ dhabihu za wanyama ziendelee kutolewa kwenye hekalu la Yerusalemu. Badala ya hilo, alitambua kwamba Mungu alikuwa amemtayarishia yeye, Yesu, mwili mkamilifu wa kibinadamu, apate kuutoa ukiwa dhabihu. Hilo lingeondoa uhitaji wowote zaidi wa dhabihu za wanyama. Akionyesha tamaa yake yenye kuhisiwa moyoni ya kunyenyekea mapenzi ya Mungu, Yesu aliendelea kusali: “Tazama, nimekuja (katika gombo la chuo nimeandikiwa) niyafanye mapenzi yako, Mungu.” (Waebrania 10:7) Ni kielelezo kitukufu kama nini cha moyo mkuu na ujitoaji usio na ubinafsi alichoweka Yesu siku hiyo kwa wote ambao baadaye wangekuwa wanafunzi wake!—Marko 8:34.
4. Mungu alionyeshaje kukubali kwake kule kujitoa mwenyewe kwa Yesu?
4 Je, Mungu alionyesha kukubali sala ya Yesu ya ubatizo? Acheni mmoja wa mitume wateule wa Yesu atupe jibu: “Yesu alipokwisha kubatizwa mara akapanda kutoka majini; na tazama, mbingu zikamfunukia, akamwona Roho wa Mungu akishuka kama hua akija juu yake; na tazama, sauti kutoka mbinguni ikisema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.”—Mathayo 3:16, 17; Luka 3:21, 22.
5. Ni nini kilichofananishwa na madhabahu halisi ya hekalu?
5 Kukubali kwa Mungu kule kutolewa kwa mwili wa Yesu utumiwe ukiwa dhabihu kulimaanisha kwamba, katika maana ya kiroho, madhabahu iliyo kubwa zaidi ya ile iliyokuwa katika hekalu la Yerusalemu ilichukua sehemu ya kwanza. Madhabahu halisi ambapo wanyama walitolewa kwa ajili ya dhabihu ilitangulia kuonyesha madhabahu hiyo ya kiroho, ambayo kwa kweli ilikuwa “mapenzi” au mpango wa Mungu wa kukubali uhai wa Yesu wa kibinadamu ukiwa dhabihu. (Waebrania 10:10) Hiyo ndiyo sababu mtume Paulo aliweza kuwaandikia Wakristo wenzake: “Tuna madhabahu ambayo wale waihudumiao ile hema hawana ruhusa kula vitu vyake.” (Waebrania 13:10) Kwa maneno mengine, Wakristo wa kweli hufaidika kutokana na dhabihu ya kufunika dhambi iliyo bora zaidi, ambayo makuhani Wayahudi walio wengi walikataa.
6. (a) Ni nini kilichochukua sehemu ya kwanza wakati wa ubatizo wa Yesu? (b) Jina la cheo Mesiya, au Kristo, humaanisha nini?
6 Kutiwa mafuta kwa Yesu kwa roho takatifu kulimaanisha kwamba sasa Mungu alikuwa ametokeza mpango wake kamili wa hekalu la kiroho, Yesu akitumikia akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu. (Matendo 10:38; Waebrania 5:5) Mwanafunzi Luka alipuliziwa kutaja mwaka wa tukio hilo kubwa kuwa “mwaka wa kumi na tano wa kutawala kwake Kaisari Tiberio.” (Luka 3:1-3) Huo walingana na mwaka wa 29 W.K.—majuma ya miaka 69 kamili, au miaka 483, tangu wakati Mfalme Artashasta alipokuwa ametoa amri kwamba kuta za Yerusalemu zijengwe upya. (Nehemia 2:1, 5-8) Kulingana na unabii, “masihi aliye mkuu” angetokea katika mwaka huo uliotabiriwa. (Danieli 9:25) Kwa hakika Wayahudi wengi walijua hilo. Luka aripoti kwamba ‘watu walikuwa wakingoja’ kutokea kwa Mesiya, au Kristo, majina ya cheo yanayotokana na maneno ya Kiebrania na Kigiriki yaliyo na maana sawa, yaani “mtiwa-mafuta”—Luka 3:15.
7. (a) Mungu alitia mafuta “Patakatifu pa Patakatifu” lini, na hilo lilimaanisha nini? (b) Ni nini kingine kilichompata Yesu wakati wa ubatizo wake?
7 Wakati wa ubatizo wa Yesu, makao ya kimbingu ya Mungu yalitiwa mafuta, au kutengwa, kuwa “Patakatifu pa Patakatifu” (NW) katika ule mpango wa hekalu kubwa la kiroho. (Danieli 9:24) “Ile hema ya kweli [au hekalu], ambayo Bwana aliiweka wala si mwanadamu” ilikuja kutenda. (Waebrania 8:2) Pia, kupitia ubatizo wake kwa maji na roho takatifu, yule mwanamume Yesu Kristo alizaliwa mara ya pili akiwa Mwana wa kiroho wa Mungu. (Linganisha Yohana 3:3.) Hilo lilimaanisha kwamba kwa wakati ufaao Mungu angemrudisha Mwanaye kwenye uhai wa kimbingu, ambapo angetumikia kwenye mkono wa kuume wa Babaye akiwa Mfalme na Kuhani wa Cheo cha Juu “hata milele kwa mfano wa Melkizedeki.”—Waebrania 6:20; Zaburi 110:1, 4.
Patakatifu Zaidi Sana pa Kimbingu
8. Kiti cha ufalme cha Mungu mbinguni kilikuwa kimepata sehemu gani mpya sasa?
8 Katika siku ya ubatizo wa Yesu, kiti cha ufalme cha Mungu cha kimbingu kilikuwa kimepata sehemu mpya mbalimbali. Kuainishwa kwa dhabihu kamilifu ya kibinadamu ya kufunika dhambi za ulimwengu kulikazia utakatifu wa Mungu kwa kutofautishwa na hali yenye dhambi ya mwanadamu. Rehema ya Mungu pia ilikaziwa kwa njia ya kwamba sasa alionyesha kuwa kwake tayari kutulizwa, au kuridhishwa. Kwa njia hiyo kiti cha ufalme cha Mungu mbinguni kilikuwa kumekuwa sawa na chumba cha ndani cha hekalu, mahali ambapo kuhani wa cheo cha juu aliingia mara moja kwa mwaka akiwa na damu ya wanyama ili kufunika dhambi kwa njia ya kielezi.
9. (a) Pazia kati ya Patakatifu na Patakatifu Zaidi Sana lilifananisha nini? (b) Yesu aliingiaje ndani kupita lile pazia la hekalu la kiroho la Mungu?
9 Lile pazia lililotenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi Sana lilifananisha mwili wa Yesu wenye nyama. (Waebrania 10:19, 20) Lilikuwa kizuizi kilichomzuia Yesu asiingie mbele ya Babaye alipokuwa mwanadamu duniani. (1 Wakorintho 15:50) Wakati wa kifo cha Yesu, ‘pazia la hekalu lilipasuka vipande viwili toka juu hata chini.’ (Mathayo 27:51) Hilo lilionyesha kwa njia yenye kutokeza kwamba kizuizi kilichomzuia Yesu asiingie mbinguni sasa kilikuwa kimeondolewa. Siku tatu baadaye, Yehova Mungu alifanya muujiza wenye kutokeza. Alimfufua Yesu kutoka kwa wafu, si akiwa mwanadamu awezaye kufa mwenye nyama na damu, bali akiwa kiumbe kitukufu cha kiroho, ‘akaaye milele.’ (Waebrania 7:24) Siku arobaini baadaye, Yesu alipaa kwenda mbinguni akaingia “Patakatifu pa Patakatifu” (NW) palipo halisi, “aonekane sasa usoni pa Mungu kwa ajili yetu.”—Waebrania 9:24.
10. (a) Ni nini kilichotendeka baada ya Yesu kumtolea Babaye wa kimbingu thamani ya dhabihu yake? (b) Kutiwa mafuta kwa roho takatifu kulimaanisha nini kwa wanafunzi wa Kristo?
10 Je, Mungu alikubali thamani ya damu ya Yesu iliyomwagwa kuwa ufuniko kwa ajili ya dhambi za ulimwengu? Kwa kweli aliikubali. Ithibati ya kukubali huko ilikuja siku 50 kamili baada ya ufufuo wa Yesu, kwenye siku ya msherehekeo wa Pentekoste. Roho takatifu ya Mungu ilimwagwa juu ya wanafunzi wa Yesu 120 waliokusanyika pamoja katika Yerusalemu. (Matendo 2:1, 4, 33) Sawa na Kuhani wao wa Cheo cha Juu, Yesu Kristo, sasa walikuwa wametiwa mafuta ili watumikie wakiwa ‘ukuhani mtakatifu, watoe dhabihu za roho’ chini ya mpango wa Mungu wa hekalu kubwa la kiroho. (1 Petro 2:5) Zaidi ya hayo, hawa watiwa-mafuta walifanyiza taifa jipya, “taifa takatifu” la Mungu la Israeli wa kiroho. Kuanzia wakati huo na kuendelea, unabii wote mbalimbali wa mambo mazuri juu ya Israeli, kama ile ahadi ya “agano jipya” iliyorekodiwa kwenye Yeremia 31:31, ungehusu kutaniko la Kikristo la watiwa-mafuta, “Israeli wa Mungu” walio halisi.—1 Petro 2:9; Wagalatia 6:16.
Sehemu Nyinginezo za Hekalu la Kiroho la Mungu
11, 12. (a) Ni nini kilichofananishwa na ua wa kikuhani katika kisa cha Yesu, nao ni nini katika kisa cha wafuasi wake watiwa-mafuta? (b) Birika la maji lafananisha nini, nalo latumiwaje?
11 Ingawa Patakatifu Zaidi Sana palifananisha “mbinguni hasa,” mahali ambapo Mungu ana kiti chake cha ufalme, sehemu nyingine zozote za hekalu la kiroho la Mungu zinahusu vitu vilivyo duniani. (Waebrania 9:24) Hekaluni Yerusalemu, kulikuwa na ua wa ndani wa kikuhani uliokuwa na madhabahu ya dhabihu na birika kubwa la maji, ambalo makuhani walitumia ili kujisafisha wenyewe kabla ya kufanya utumishi mtakatifu. Vitu hivyo hufananisha nini katika mpango wa Mungu wa hekalu la kiroho?
12 Katika kisa cha Yesu Kristo, ua wa ndani wa kikuhani ulifananisha hali yake ya kutokuwa na dhambi akiwa Mwana mkamilifu wa kibinadamu, wa Mungu. Kupitia kudhihirisha imani katika dhabihu ya Yesu, wafuasi wa Kristo watiwa-mafuta wanahesabiwa uadilifu. Kwa njia hiyo, Mungu aweza kushughulika nao kwa haki kana kwamba hawana dhambi. (Warumi 5:1; 8:1, 33) Kwa hiyo, ua huo pia hufananisha kuhesabiwa hali ya uadilifu ya kibinadamu ambayo washiriki mmoja-mmoja wa ukuhani mtakatifu hufurahia mbele ya Mungu. Wakati huohuo, Wakristo watiwa-mafuta bado si wakamilifu nao wana hali ya kutenda dhambi. Birika la maji uani hufananisha Neno la Mungu, ambalo Kuhani wa Cheo cha Juu hutumia kusafisha ukuhani mtakatifu hatua kwa hatua. Kwa kunyenyekea usafishaji huo, wamefikia mwonekano wenye adhama unaomheshimu Mungu na unaovuta watu wa nje kwenye ibada yake safi.—Waefeso 5:25, 26; linganisha Malaki 3:1-3.
Patakatifu
13, 14. (a) Patakatifu pa hekalu hufananisha nini katika kisa cha Yesu na wafuasi wake watiwa-mafuta? (b) Kinara cha dhahabu hufananisha nini?
13 Chumba cha kwanza cha hekalu hufananisha hali iliyo bora zaidi kuliko ile ya ua. Katika kisa cha mwanadamu mkamilifu Yesu Kristo, hicho hufananisha kuzaliwa kwake tena akiwa Mwana wa kiroho wa Mungu mwenye taraja la kurudia uhai wa kimbingu. Baada ya kutangazwa kuwa waadilifu kwa msingi wa imani yao katika damu ya Kristo iliyomwagwa, wafuasi hao watiwa-mafuta pia wanapatwa na utendaji huo wa pekee wa roho ya Mungu. (Warumi 8:14-17) Kwa “maji [yaani, ubatizo wao] na kwa Roho” wao ‘wanazaliwa mara ya pili’ wakiwa wana wa kiroho wa Mungu. Hivyo, wana tumaini la kufufuliwa kwenye uhai wa kimbingu wakiwa wana wa kiroho wa Mungu, maadamu tu wanaendelea kuwa waaminifu mpaka kifo.—Yohana 3:5, 7; Ufunuo 2:10.
14 Makuhani waliotumikia ndani ya Patakatifu pa hekalu la kidunia hawakuonekana na waabudu waliokuwa nje. Vivyo hivyo, Wakristo watiwa-mafuta wanapatwa na hali ya kiroho ambayo wengi wa waabudu wa Mungu, ambao tumaini lao ni kuishi milele kwenye dunia iliyo paradiso, hawashiriki wala hawaifahamu kikamili. Kile kinara cha dhahabu cha tabenakulo hufananisha hali ya kutiwa nuru ya Wakristo watiwa-mafuta. Utendaji wa roho takatifu ya Mungu, sawa na yale mafuta katika zile taa, huelimisha juu ya Biblia. Wakristo hawaukalii tu uelewevu wanaopata kutokana nao. Badala ya hivyo, wao humtii Yesu, aliyesema: “Ninyi ni nuru ya ulimwengu. . . . Nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.”—Mathayo 5:14, 16.
15. Ni nini kinachofananishwa na mkate kwenye meza ya mkate wa wonyesho?
15 Ili kubaki katika hali hiyo ya kutiwa nuru, ni lazima Wakristo watiwa-mafuta wajilishe kwa ukawaida kile kifananishwacho na mkate kwenye meza ya mkate wa wonyesho. Chanzo chao cha msingi cha chakula cha kiroho ni Neno la Mungu, ambalo wanajitahidi kusoma na kutafakari juu yalo kila siku. Pia Yesu aliahidi kuwaandalia “chakula kwa wakati wake” kupitia “mtumwa [wake] mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45) “Mtumwa” huyo ni jamii nzima ya Wakristo watiwa-mafuta walio duniani kwa wakati wowote ule. Kristo ametumia jamii hiyo ya watiwa-mafuta ili kutangaza habari juu ya utimizo wa unabii mbalimbali wa Biblia na kutoa mwelekezo kwa wakati ufaao juu ya matumizi ya kanuni za Biblia katika maisha ya kila siku ya siku ya kisasa. Kwa hiyo, Wakristo watiwa-mafuta hujilisha maandalizi yote hayo kwa uthamini. Lakini kuendelea kwa uhai wao wa kiroho hutegemea mengi zaidi ya kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Mungu akilini mwao na mioyoni mwao. Yesu alisema hivi: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.” (Yohana 4:34) Vivyo hivyo, Wakristo watiwa-mafuta huwa na uradhi kwa kujihusisha wenyewe kila siku katika kufanya mapenzi ya Mungu yaliyofunuliwa.
16. Ni nini kinachofananishwa na utumishi kwenye madhabahu ya uvumba?
16 Asubuhi na jioni, kuhani alimtolea Mungu uvumba juu ya madhabahu ya uvumba katika Patakatifu. Wakati huohuo, waabudu wasio makuhani walikuwa wakisali kwa Mungu wakiwa wamesimama katika nyua za nje ya hekalu lake. (Luka 1:8-10) “Uvumba,” yaeleza Biblia, “wamaanisha sala za watakatifu.” (Ufunuo 5:8, NW) “Sala yangu ipae mbele zako kama uvumba,” akaandika mtunga-zaburi Daudi. (Zaburi 141:2) Wakristo watiwa-mafuta pia huthamini sana pendeleo lao la kumfikia Yehova katika sala kupitia Yesu Kristo. Sala zenye bidii zinazotoka moyoni ni kama uvumba wenye kunukia. Wakristo watiwa-mafuta pia humsifu Mungu katika njia nyingine, wakitumia midomo yao kufundisha wengine. Uvumilivu wao wakabilipo magumu na uaminifu-maadili wao chini ya majaribu hasa humpendeza Mungu.—1 Petro 2:20, 21.
17. Ni nini kilichohusishwa katika utimizo wa ufananisho wa kiunabii ulioandaliwa na kuingia mara ya kwanza kwa kuhani wa cheo cha juu ndani ya Patakatifu Zaidi Sana katika Siku ya Kufunika?
17 Katika Siku ya Kufunika, kuhani wa cheo cha juu wa Israeli alipaswa kuingia ndani ya Patakatifu Zaidi Sana na kufukiza uvumba kwenye chombo cha dhahabu cha kufukizia uvumba kilichokuwa na makaa-mawe yenye moto. Hilo lilipaswa kufanywa kabla hajaingiza ile damu ya matoleo ya dhambi. Katika utimizo wa mandhari hii ya kiunabii, mwanadamu Yesu alidumisha uaminifu-maadili kabisa kwa Yehova Mungu kabla ya kutoa uhai wake kuwa dhabihu moja yenye kudumu kwa ajili ya dhambi zetu. Kwa njia hiyo, alionyesha kwamba mwanadamu mkamilifu angeweza kudumisha uaminifu-maadili wake kwa Mungu licha ya mikazo yoyote ile ambayo Shetani alimletea. (Mithali 27:11) Alipojaribiwa, Yesu alitumia sala “pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu.” (Waebrania 5:7) Kwa njia hiyo alimtukuza Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu mwadilifu na mwenye haki wa ulimwengu wote mzima. Mungu alimthawabisha Yesu kwa kumfufua kutoka kwa wafu hadi kwenye uhai usioweza kufa wa kimbingu. Katika wadhifa huo wa juu, Yesu hutolea uangalifu sababu ya pili ya kuja kwake duniani, yaani, kupatanisha pamoja na Mungu wanadamu watenda-dhambi wenye kutubu.—Waebrania 4:14-16.
Utukufu Mkuu Zaidi wa Hekalu la Kiroho la Mungu
18. Yehova ameletaje utukufu wenye kutokeza kwenye hekalu lake la kiroho?
18 “Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza,” akatabiri Yehova. (Hagai 2:9) Kwa kumfufua Yesu kuwa Mfalme na Kuhani wa Cheo cha Juu asiyeweza kufa, Yehova alileta utukufu wenye kutokeza kwenye hekalu lake la kiroho. Sasa Yesu aweza kuleta “wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii.” (Waebrania 5:9) Wa kwanza kuonyesha utii wa aina hiyo walikuwa wale wanafunzi 120 waliopokea roho takatifu kwenye Pentekoste katika 33 W.K. Kitabu cha Ufunuo kilitabiri kwamba wana hawa wa kiroho wa Israeli hatimaye wangefikia idadi ya 144,000. (Ufunuo 7:4) Baada ya kufa, wengi wao walihitaji kulala katika kaburi la kawaida la wanadamu, wakingojea wakati wa kuwapo kwa Yesu katika nguvu za kifalme. Kronolojia ya kiunabii iliyo kwenye Danieli 4:10-17, 20-27 huelekeza kwenye 1914 kuwa ndio wakati wa Yesu kuanza kutawala katikati ya adui zake. (Zaburi 110:2) Kwa miongo mingi mapema, Wakristo watiwa-mafuta waliungojea kwa hamu mwaka huo. Vita ya ulimwengu ya kwanza na ole juu ya wanadamu zilizoambatana nayo ilitoa ithibati ya kwamba Yesu kwa kweli alitawazwa kuwa Mfalme katika 1914. (Mathayo 24:3, 7, 8) Muda mfupi baadaye, wakati ulipokuwa umefika wa “hukumu kuanza katika nyumba ya Mungu,” Yesu angetimiza ile ahadi kwa wanafunzi wake watiwa-mafuta waliokuwa wamelala katika kifo: “Nitakuja tena niwakaribishe kwangu.”—1 Petro 4:17; Yohana 14:3.
19. Baki la 144,000 litaingiaje kwenye Patakatifu Zaidi Sana pa kimbingu?
19 Si wote wa wale washiriki 144,000 wa ukuhani mtakatifu ambao wametiwa muhuri wa mwisho na kukusanywa kwenda kwenye makao yao ya kimbingu. Baki lao lingali laishi duniani katika hali ya kiroho iliyofananishwa na Patakatifu, palipotenganishwa na kuwapo kutakatifu kwa Mungu, kwa lile “pazia,” au kizuizi, cha miili yao yenye nyama. Hao wafapo katika uaminifu, wanafufuliwa mara moja wakiwa viumbe vya roho visivyoweza kufa wapate kujiunga na wale wa 144,000 walio mbinguni tayari.—1 Wakorintho 15:51-53.
20. Wabakio wa ukuhani mtakatifu wanafanya kazi gani muhimu sasa, kukiwa na matokeo yapi?
20 Kukiwa na makuhani wengi namna hiyo wanaotumikia pamoja na Kuhani mkubwa wa Cheo cha Juu mbinguni, hekalu la kiroho la Mungu limepokea utukufu zaidi. Wakati huohuo, wanaobaki wa ukuhani mtakatifu wanafanya kazi yenye thamani duniani. Kupitia kuhubiri kwao, Mungu ‘anatikisa mataifa yote’ kwa semi za hukumu zake, kama ilivyotabiriwa kwenye Hagai 2:7. Wakati huohuo, mamilioni ya waabudu yafafanuliwayo kuwa “vitu vinavyotamaniwa na mataifa” yanamiminika kuingia kwenye nyua za kidunia za hekalu la Yehova. Hao hufaanaje na mpango wa Mungu kwa ajili ya ibada, na ni utukufu gani wa wakati ujao tuwezao kutarajia kwa ajili ya hekalu lake kubwa la kiroho? Maswali hayo yatachunguzwa katika makala ifuatayo.
-
-
Ushindi wa Ibada ya Kweli WakaribiaMnara wa Mlinzi—1996 | Julai 1
-
-
Ushindi wa Ibada ya Kweli Wakaribia
“BWANA atakuwa Mfalme juu ya nchi yote.”—ZEKARIA 14:9.
1. Wakristo watiwa-mafuta walipatwa na nini wakati wa Vita ya Ulimwengu 1, na jambo hilo lilitabiriwaje?
WAKATI wa vita ya ulimwengu ya kwanza, Wakristo watiwa-mafuta walipatwa na magumu mengi na vifungo vingi vya gerezani mikononi mwa mataifa yenye kupigana. Dhabihu zao za sifa kwa Yehova zilizuiliwa vikali, nao wakatumbukia katika hali ya utekwa wa kiroho. Yote hayo yalitabiriwa kwenye Zekaria 14:2, lifafanualo shambulio la kimataifa juu ya Yerusalemu. Jiji la unabii huo ni “Yerusalemu la kimbingu,” Ufalme wa kimbingu wa Mungu na mahali pa “kiti cha enzi cha Mungu na cha Mwana Kondoo.” (Waebrania 12:22, 28; 13:14; Ufunuo 22:3, linganisha NW.) Watiwa-mafuta wa Mungu duniani waliwakilisha jiji hilo. Walio waaminifu miongoni mwao walisalimika hilo shambulio, wakidinda kujiruhusu wapelekwe uhamishoni “kutoka hilo jiji.”a
2, 3. (a) Ibada ya Yehova imeshindaje tangu 1919? (b) Tangu 1935, ni jambo gani limetukia?
2 Katika 1919 watiwa-mafuta waaminifu waliachiliwa huru kutoka katika hali yao ya utekwa, nao mara moja wakatumia kwa faida yao kile kipindi cha amani kilichofuata vita. Wakiwa mabalozi wa Yerusalemu la kimbingu, walinyakua fursa tukufu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu na kusaidia katika kukusanya washiriki wa mwisho wa wale 144,000. (Mathayo 24:14; 2 Wakorintho 5:20) Katika 1931 walikubali kirasmi kutumia lile jina lifaalo la Kimaandiko Mashahidi wa Yehova.—Isaya 43:10, 12.
3 Tangu wakati huo, Mashahidi wa Mungu watiwa-mafuta wameendelea kusonga mbele bila kuacha. Hata Hitler na tengenezo lake la Nazi la kisiasa na kijeshi hakuweza kuwanyamazisha. Licha ya mnyanyaso wa ulimwenguni pote, kazi yao imezaa matunda duniani kote. Hasa tangu mwaka wa 1935, “umati mkubwa” wa kimataifa, uliotabiriwa katika kitabu cha Ufunuo, umejiunga nao. Wao pia ni Wakristo waliojiweka wakfu na kubatizwa, nao “wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” Yesu Kristo. (Ufunuo 7:9, 14, linganisha NW.) Hata hivyo, wao si watiwa-mafuta, wenye tumaini la uhai wa kimbingu. Tumaini lao ni kurithi kile kilichopotezwa na Adamu na Hawa, yaani, uhai mkamilifu wa kibinadamu kwenye dunia iliyo paradiso. (Zaburi 37:29; Mathayo 25:34) Leo, idadi ya umati mkubwa yafikia nafsi zaidi ya milioni tano. Ibada ya kweli ya Yehova inashinda, lakini ushindi wayo wa mwisho bado utakuja.
Wageni Katika Hekalu la Mungu la Kiroho
4, 5. (a) Umati mkubwa humwabudu Yehova wapi? (b) Wao hufurahia mapendeleo gani, na ni kwa kutimiza unabii upi?
4 Kama ilivyotabiriwa, ule umati mkubwa “[Unamwabudu Mungu] mchana na usiku katika hekalu lake.” (Ufunuo 7:15, ona NW, kielezi chini.) Kwa kuwa wao si Waisraeli wa kikuhani wa kiroho, yaelekea Yohana aliwaona wakiwa wamesimama hekaluni katika ua wa nje wa Wasio Wayahudi. (1 Petro 2:5) Hekalu la Yehova la kiroho limekuwa tukufu kama nini, ua walo ukiwa umejawa na umati huu mkubwa unaomsifu yeye, pamoja na baki la Israeli la kiroho.
5 Ule umati mkubwa haumtumikii Mungu katika hali iliyofananishwa na ua wa ndani wa kikuhani. Hawatangazwi kuwa waadilifu kwa kusudi la kuwa wana wa Mungu wa kiroho, waliofanywa kuwa wana. (Warumi 8:1, 15) Hata hivyo, kwa kudhihirisha imani katika fidia ya Yesu, wana msimamo safi mbele ya Yehova. Wanatangazwa kuwa waadilifu kwa kusudi la kuwa rafiki zake. (Linganisha Yakobo 2:21, 23.) Wao pia wamependelewa kutoa dhabihu zenye kukubalika juu ya madhabahu ya kiroho ya Mungu. Kwa njia hiyo, kuhusu umati huo mkubwa, unabii huu wa Isaya 56:6, 7 unaendelea kupata utimizo mtukufu: “Wageni, walioandamana na BWANA ili wamhudumu, na kulipenda jina la BWANA, . . . Nitawaleta hao nao hata mlima wangu mtakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala; makafara yao na dhabihu yao zitakubaliwa juu ya madhabahu zangu; kwa maana nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote.”
6. (a) Wageni hutoa aina gani ya dhabihu? (b) Chombo cha maji katika ua wa kikuhani huwakumbusha nini?
6 Kati ya dhabihu ambazo wageni hao hutoa ni “tunda la midomo [sawa na matoleo ya nafaka yaliyotayarishwa yawe membamba] iliungamayo jina lake” na “kutenda mema na kushirikiana.” (Waebrania 13:15, 16) Kile chombo kikubwa cha maji ambacho makuhani walipaswa kutumia ili kujiosha wenyewe pia ni kikumbusha muhimu kwa wageni hao. Wao pia lazima wanyenyekee usafishaji wa kiroho na kiadili kadiri Neno la Mungu linavyodhihirishwa kwao hatua kwa hatua.
Patakatifu na Vyombo Vyapo
7. (a) Umati mkubwa huonaje mapendeleo ya ukuhani mtakatifu? (b) Wageni wengine wamepata mapendeleo gani ya ziada?
7 Je, Patakatifu na vyombo vyapo vina maana yoyote kwa umati huo mkubwa wa wageni? Hawatapata kamwe kuwa katika hali iliyofananishwa na Patakatifu. Hawazaliwi mara ya pili kuwa wana wa kiroho wa Mungu wenye uraia wa kimbingu. Je, hilo huwafanya wawe na wivu au uchoyo? La. Badala ya hivyo, wanashangilia katika pendeleo lao la kuunga mkono baki la wale 144,000, nao wanaonyesha uthamini wenye kina kwa ajili ya kusudi la Mungu la kuwafanya wana hao wa kiroho kuwa wana, watakaoshiriki na Kristo katika kuinua wanadamu hadi ukamilifu. Pia, umati mkubwa wa wageni huthamini fadhili zisizostahiliwa za Mungu zilizo kubwa katika kuwapa tumaini la kidunia la uhai udumuo milele katika Paradiso. Baadhi ya wageni hao, sawa na Wanethini wa kale, wamepewa mapendeleo ya usimamizi katika kuusaidia ukuhani mtakatifu.b (Isaya 61:5) Yesu huweka rasmi baadhi yao kuwa “wakuu katika nchi zote.”—Zaburi 45:16.
8, 9. Umati mkubwa hupata manufaa zipi kutokana na kuchunguza vyombo vya Patakatifu?
8 Ingawa hautapata kamwe kuingia ndani ya Patakatifu pa ufananisho, umati mkubwa wa wageni hujifunza masomo yenye thamani kutokana na vyombo vyapo. Sawa na jinsi kinara cha taa kilivyohitaji kuongezwa mafuta kwa ukawaida, ndivyo wale wageni wahitajivyo roho takatifu iwasaidie kushika kweli za hatua kwa hatua kutoka Neno la Mungu, zinazotolewa kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45-47) Zaidi ya hayo, roho ya Mungu huwasaidia waitikie mwaliko huu: “Roho na Bibi-arusi [baki la watiwa-mafuta] wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.” (Ufunuo 22:17) Kwa njia hiyo, kinara cha taa ni kikumbusha kwa wale wa umati mkubwa cha wajibu wao wa kung’aa wakiwa Wakristo na kuepuka mtazamo wowote, wazo lolote, neno lolote, au tendo lolote liwezalo kuhuzunisha roho takatifu ya Mungu.—Waefeso 4:30.
9 Meza ya mkate wa wonyesho huukumbusha umati mkubwa kwamba ili ubaki ukiwa wenye afya kiroho, ni lazima ujilishe kwa ukawaida chakula cha kiroho kutoka Biblia na kutoka vichapo vya “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 4:4) Madhabahu ya uvumba huwakumbusha umaana wa kusali kwa Yehova kwa bidii ili kupata msaada waweze kudumisha uaminifu-maadili wao. (Luka 21:36) Sala zao zapaswa kutia ndani semi za sifa na shukrani zenye kuhisiwa moyoni. (Zaburi 106:1) Madhabahu ya uvumba huwakumbusha pia uhitaji wa kumsifu Mungu katika njia nyinginezo, kama kupitia kuimba kwao nyimbo za Ufalme kwa moyo wote kwenye mikutano ya Kikristo na kwa kutayarisha kwao vizuri ili kutoa “tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.”—Warumi 10:10, NW.
Ushindi Kamili wa Ibada ya Kweli
10. (a) Twaweza kutazamia taraja gani tukufu? (b) Ni jambo gani lazima litukie kwanza?
10 Leo “jamii za watu wengi” kutoka mataifa yote zinamiminika kwenye nyumba ya Yehova ya ibada. (Isaya 2:2, 3, NW) Likihakikisha hilo, Ufunuo 15:4 lataarifu hivi: “Ni nani asiyekucha, Ee Bwana, na kulitukuza jina lako? kwa kuwa wewe peke yako u Mtakatifu; kwa maana mataifa yote watakuja na kusujudu mbele zako; kwa kuwa matendo yako ya haki yamekwisha kufunuliwa.” Zekaria sura ya 14 hufafanua linalofuata. Katika wakati ujao ulio karibu, mtazamo mbaya wa wengi wa watu walio duniani utafikia upeo huku wakikusanyika kwa mara ya mwisho ili kupigana dhidi ya Yerusalemu—wawakilishi wa Yerusalemu la kimbingu walio duniani. Kisha Yehova atatenda. Akiwa Mungu-Mpiganaji, yeye “atapigana na mataifa hayo” yanayothubutu kufanya shambulio hilo.—Zekaria 14:2, 3.
11, 12. (a) Yehova ataitikiaje shambulio lijalo la tufeni pote juu ya wale waabuduo hekaluni mwake? (b) Tokeo la vita ya Mungu litakuwa nini?
11 “Hii ndiyo tauni, ambayo BWANA atawapiga watu wote waliofanya vita juu ya Yerusalemu; nyama ya mwili wao itaharibika, wasimamapo juu ya miguu yao, na macho yao yataharibika ndani ya vichwa vyao, na ndimi zao zitaharibika vinywani mwao. Tena itakuwa siku hiyo, ya kwamba mashaka makubwa yatokayo kwa BWANA yatakuwa kati yao; na kila mmoja wao atakamata mkono wa jirani yake, na mkono wake utainuliwa ili kushindana na mkono wa jirani yake.”—Zekaria 14:12, 13.
12 Ni lazima tungoje ili tuone ikiwa tauni hii ni halisi au ya kitamathali. Hata hivyo, jambo moja ni hakika. Huku adui za Mungu wakichukua hatua ili kufanya shambulio lao la tufeni pote juu ya watumishi wa Yehova, watazuiwa na maonyesho yenye kutisha ya nguvu za Mungu zenye uweza wote. Vinywa vyao vitanyamazishwa. Itakuwa ni kana kwamba ndimi zao za kudharau zilikuwa zimeoza. Mradi wao wa muungano utatiwa kiwi uwezo wao wa kuona, kana kwamba macho yao yalikuwa yameoza. Nguvu zao za kimwili, zilizowapa ujarisi wa kufanya hilo shambulio, zitapotelea mbali. Katika vurugu, watageukiana kwa uchinjaji mkubwa. Kwa njia hiyo maadui wa kidunia wote wa ibada ya Mungu watafutiliwa mbali. Hatimaye, mataifa yote yatakuwa yamelazimishwa kutambua enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote mzima. Huu unabii utatimizwa: “BWANA atakuwa Mfalme juu ya nchi yote.” (Zekaria 14:9) Baada ya hapo, Shetani na roho waovu wake watafungwa huku Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo uanzapo ukiwa na baraka kubwa akibani kwa ajili ya wanadamu.—Ufunuo 20:1, 2; 21:3, 4.
Ufufuo wa Kidunia
13. Ni nani wale ‘watakaosalia kutoka kwa mataifa yote’?
13 Unabii wa Zekaria waendelea kwenye sura ya 14, mstari wa 16 hivi: “Hata itakuwa, ya kwamba kila mtu aliyesalia wa mataifa yote, waliokuja kupigana na Yerusalemu, atakwea mwaka baada ya mwaka ili kumwabudu Mfalme, BWANA wa majeshi, na kuishika sikukuu ya Vibanda.” Kulingana na Biblia, watu wote walio hai leo waendeleao kuishi hadi mwisho wa mfumo huu mwovu na wanaohukumiwa kuwa maadui wa ibada ya kweli ‘wataadhibiwa kwa maangamizi ya milele.’ (2 Wathesalonike 1:7-9; ona pia Mathayo 25:31-33, 46.) Hawatapata ufufuo. Basi, yaelekea kwamba ‘wanaosalia’ hutia ndani washiriki wa mataifa waliokufa kabla ya vita ya mwisho ya Mungu walio na tumaini la ufufuo lenye msingi wa Biblia. “Saa yaja,” Yesu aliahidi, “ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu.”—Yohana 5:28, 29.
14. (a) Ni lazima watakaofufuliwa wafanye nini ili wapate uhai udumuo milele? (b) Ni nini kitakachowapata wowote wakataao kujiweka wakfu kwa Yehova na kuzoea ibada ya kweli?
14 Wote hao waliofufuliwa ni lazima wafanye kitu fulani ili ufufuo wao uwe wa uzima wala si wa hukumu kali. Lazima waje kwenye nyua za kidunia za hekalu la Yehova na kuinama chini katika wakfu kwa Mungu kupitia Yesu Kristo. Wowote waliofufuliwa wakataao kufanya hivyo watapatwa na tauni ileile iyapatayo mataifa ya siku ya sasa. (Zekaria 14:18) Ni nani ajuaye ni wangapi wa wale watakaofufuliwa watakaojiunga na umati mkubwa kwa furaha katika kuadhimisha Sikukuu ya Vibanda ya ufananisho? Bila shaka, watakuwa wengi, na hekalu kubwa la kiroho la Yehova litakuwa tukufu hata zaidi kwa sababu hiyo!
Sikukuu ya Vibanda ya Ufananisho
15. (a) Ni zipi baadhi ya sehemu zenye kutokeza za Sikukuu ya Vibanda ya Israeli la kale? (b) Kwa nini fahali 70 walitolewa wakiwa dhabihu wakati wa hiyo sikukuu?
15 Kila mwaka, Israeli la kale lilitakwa kuadhimisha Sikukuu ya Vibanda. Iliendelea kwa juma moja nayo ilianza mwishoni-mwishoni mwa kule kukusanya pamoja kwa mavuno yao. Ulikuwa wakati wenye shangwe wa kutoa shukrani. Kwa juma hilo lote, walipaswa kuishi katika vibanda vya muda vilivyoezekwa kwa majani ya miti, hasa matawi ya mitende. Sikukuu hiyo ililikumbusha Israeli jinsi Mungu alivyookoa babu zalo wa kale kutoka Misri na jinsi alivyowatunza walipokuwa wakiishi katika vibanda huku wakizungukazunguka kwa miaka 40 jangwani hata walipofika Bara Lililoahidiwa. (Mambo ya Walawi 23:39-43) Wakati wa hiyo sikukuu fahali 70 walitolewa wakiwa dhabihu juu ya madhabahu ya hekalu. Kulingana na uthibitisho, sehemu hiyo ya sikukuu ilikuwa unabii wa kazi ya Yesu Kristo ya kuokoa uhai iliyo kamilifu na ya ujumla. Manufaa za dhabihu yake ya fidia hatimaye zitawafikia wazao wa zile familia 70 za wanadamu zilizotokana na Nuhu.—Mwanzo 10:1-29; Hesabu 29:12-34; Mathayo 20:28.
16, 17. (a) Sikukuu ya Vibanda ya ufananisho ilianza lini, nayo iliendeleaje? (b) Umati mkubwa hushirikije katika huo mwadhimisho?
16 Kwa njia hiyo Sikukuu ya Vibanda ya kale ilielekezea kule kukusanywa kwenye shangwe katika hekalu kubwa la kiroho la Yehova, kwa watenda-dhambi wenye kukombolewa. Utimizo wa sikukuu hiyo ulianza kwenye Pentekoste katika 33 W.K. na mwanzo wa kule kukusanywa kwenye shangwe kwa Waisraeli wa kiroho katika kutaniko la Kikristo. (Matendo 2:41, 46, 47) Watiwa-mafuta hao waling’amua kwamba walikuwa “wakaaji wa kigeni” katika ulimwengu wa Shetani kwa sababu ‘uraia wao halisi uko katika mbingu.’ (1 Petro 2:11; Wafilipi 3:20, linganisha NW.) Hiyo sikukuu yenye shangwe ilifunikwa kwa muda na uasi-imani uliotokeza kufanyizwa kwa Jumuiya ya Wakristo. (2 Wathesalonike 2:1-3) Hata hivyo, hiyo sikukuu ilianzishwa tena katika 1919 kukiwa na kule kukusanywa kwenye shangwe kwa washiriki wa mwisho wa wale Waisraeli wa kiroho 144,000, kukifuatwa na kule kukusanywa kwa umati mkubwa wa kimataifa wa Ufunuo 7:9.
17 Ule umati mkubwa unaonyeshwa ukiwa na matawi ya mitende mikononi mwao, jambo lionyeshalo kwamba wao pia ni waadhimishaji wenye shangwe wa Sikukuu ya Vibanda ya ufananisho. Wakiwa Wakristo waliojiweka wakfu, wao hushiriki kwa shangwe katika kazi ya kukusanya waabudu zaidi katika hekalu la Yehova. Zaidi ya hilo, wakiwa watenda-dhambi, wanang’amua kwamba hawana haki za kukaa duniani daima. Wao, pamoja na watakaofufuliwa wakati ujao, lazima waendelee kudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo hata wafikie ukamilifu wa kibinadamu mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo.—Ufunuo 20:5.
18. (a) Ni nini kitakachotukia mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo? (b) Ibada ya kweli ya Yehova itashindaje hatimaye?
18 Kisha, waabudu wa Mungu duniani watasimama mbele yake katika ukamilifu wa kibinadamu bila ya uhitaji wa ukuhani wa kimbingu. Wakati wa Yesu Kristo ‘kumpa Mungu Baba ufalme wake’ utakuwa umefika. (1 Wakorintho 15:24) Shetani atafunguliwa “muda mchache” ili kuwajaribu binadamu waliofanywa wakamilifu. Wowote wasio waaminifu wataharibiwa milele, pamoja na Shetani na roho waovu wake. Wale waendeleao wakiwa waaminifu watapewa uhai udumuo milele. Watakuwa wakazi wenye kudumu katika Paradiso ya kidunia. Kwa njia hiyo Sikukuu ya Vibanda ya ufananisho itakuwa imefikia umalizio mtukufu na wenye mafanikio. Ibada ya kweli itakuwa imeshinda kwa utukufu udumuo milele wa Yehova na kwa furaha ya milele ya wanadamu.—Ufunuo 20:3, 7-10, 14, 15.
-