-
‘Jilinde na Kila Namna ya Tamaa’Mnara wa Mlinzi—2007 | Agosti 1
-
-
‘Jilinde na Kila Namna ya Tamaa’
“Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.”—LUKA 12:15.
1, 2. (a) Umeona watu leo wanapendezwa na wanafuatia nini? (b) Mitazamo hiyo inaweza kuwa na matokeo gani mabaya kwetu?
PESA, mali, sifa, kazi yenye mshahara mnono, na familia, ni kati ya mambo ambayo watu wengi wanafikiri yanaonyesha kwamba mtu amefanikiwa au yanamhamkikishia wakati ujao ulio salama. Ni wazi kwamba katika nchi tajiri na maskini, watu wengi wanapendezwa na wanafuatia vitu vya kimwili na mafanikio maishani. Kwa upande mwingine, ikiwa wanapendezwa na mambo ya kiroho kwa kadiri fulani, upendezi huo unazidi kupungua.
2 Hivyo ndivyo Biblia ilivyotabiri hasa. Inasema: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake.” (2 Timotheo 3:1-5) Kwa kuwa wanaishi kati ya watu hao kila siku, Wakristo wa kweli wanasukumwa kuwa na mtazamo na mtindo wa maisha kama wa watu hao. Ni nini kinachoweza kutusaidia kupinga jitihada za ulimwengu za ‘kutufinyanga katika muundo wake wenyewe’?—Waroma 12:2, The New Testament in Modern English, ya J. B. Phillips.
3. Sasa tutazungumzia shauri gani lililotolewa na Yesu?
3 Akiwa “Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu,” Yesu Kristo alitufundisha mambo muhimu sana kuhusiana na hilo. (Waebrania 12:2) Pindi moja, Yesu alipokuwa akiufundisha umati wa watu mambo fulani ya kiroho yenye kuelimisha, mtu fulani alikatiza mazungumzo hayo alipoomba hivi: “Mwalimu, mwambie ndugu yangu tugawane urithi.” Yesu alimjibu mtu huyo kwa kumpa yeye na wote waliokuwa wakisikiliza shauri zito. Alitoa onyo kali sana kuhusu kuepuka tamaa na akakazia onyo hilo kwa kutumia mfano wenye kuchochea fikira. Tunapaswa kutii shauri ambalo Yesu alitoa wakati huo na kuona jinsi tunavyoweza kufaidika kwa kulitumia katika maisha yetu.—Luka 12:13-21.
Ombi Lisilofaa
4. Kwa nini haikufaa mtu huyo kumkatiza Yesu?
4 Kabla ya mtu huyo kukatiza mazungumzo, Yesu alikuwa akizungumza na wanafunzi wake na watu wengine kuhusu kujihadhari na unafiki, kuwa na ujasiri wa kukiri kuwa na muungano pamoja na Mwana wa binadamu, na kuhusu kupata msaada wa roho takatifu. (Luka 12:1-12) Bila shaka, wanafunzi walipaswa kutia moyoni mambo hayo muhimu. Hata hivyo, alipokuwa akiendelea kutoa hotuba hiyo yenye kuchochea fikira, mtu huyo alikatiza mazungumzo ghafula na kumwomba Yesu asuluhishe mgogoro ambao ulionekana kuwa wa kifamilia kuhusu vitu vya kimwili. Hata hivyo, kuna jambo la maana ambalo tunaweza kujifunza kutokana na tukio hilo.
5. Ombi la mtu huyo lilionyesha nini kumhusu?
5 Inasemekana kwamba “kwa kawaida mambo ambayo mtu anafikiria wakati anaposikiliza mafundisho ya kidini yanaonyesha mwelekeo wake.” Wakati Yesu alipokuwa akizungumza kuhusu mambo mazito ya kiroho, inaelekea mtu huyo alikuwa akifikiria jambo ambalo angefanya ili apate faida fulani za kifedha. Hatuambiwi ikiwa mtu huyo alikuwa na sababu halali ya kulalamika kuhusu urithi huo. Labda alikuwa akijaribu kufaidika kutokana na mamlaka na sifa ya Yesu akiwa mwamuzi mwenye hekima katika shughuli za wanadamu. (Isaya 11:3, 4; Mathayo 22:16) Kwa vyovyote vile, swali lake lilionyesha kwamba alikuwa na tatizo ndani kabisa ya moyo wake, tatizo kubwa sana la kutothamini mambo ya kiroho. Je, hiyo si sababu nzuri ya kutufanya tujichunguze wenyewe? Kwa mfano, ni rahisi kuruhusu akili zetu zitangetange tunapokuwa katika mikutano ya Kikristo au kufikiria mambo tutakayofanya baadaye. Badala yake, tunapaswa kusikiliza kwa makini yale yanayosemwa na kufikiria njia za kutumia habari hiyo maishani ili tuboreshe uhusiano wetu pamoja na Baba yetu wa mbinguni, Yehova Mungu, na pamoja na Wakristo wenzetu.—Zaburi 22:22; Marko 4:24.
6. Kwa nini Yesu alikataa kutimiza ombi la mtu huyo?
6 Hata iwe mtu huyo alichochewa na nini kutoa ombi hilo, Yesu alikataa kulitimiza. Badala yake, Yesu alimwambia hivi: “Wewe mtu, nani aliyeniweka mimi kuwa mwamuzi au mgawaji juu yenu?” (Luka 12:14) Kwa kusema hivyo, Yesu alikuwa akizungumzia jambo fulani ambalo watu walijua vizuri, kwa sababu kulingana na Sheria ya Musa, waamuzi wa miji waliwekwa ili kuamua mambo hayo. (Kumbukumbu la Torati 16:18-20; 21:15-17; Ruthu 4:1, 2) Kwa upande mwingine, Yesu alihangaikia mambo ya maana zaidi, yaani, kutoa ushahidi kuhusu kweli ya Ufalme na kuwafundisha watu mapenzi ya Mungu. (Yohana 18:37) Tunafuata mfano wa Yesu kwa kutumia wakati na nguvu zetu kuhubiri habari njema na kufanya “wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,” badala ya kukengeushwa na mambo yasiyo na maana.—Mathayo 24:14; 28:19.
Jihadhari na Tamaa
7. Yesu alitambua jambo gani lililokuwa moyoni mwa mtu huyo?
7 Kwa kuwa alikuwa na uwezo wa kutambua mielekeo iliyo ndani kabisa ya moyo, Yesu alijua kwamba jambo lingine zito zaidi lilihusika katika ombi la mtu huyo la kumtaka aingilie jambo la kibinafsi. Kwa hiyo, badala ya kukataa tu kulitimiza , Yesu alitaja sababu kuu ya ombi hilo aliposema hivi: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila namna ya tamaa, kwa sababu hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.”—Luka 12:15.
8. Tamaa ni nini, na inaweza kuongoza kwenye nini?
8 Tamaa inatia ndani mengi zaidi ya kutaka kuwa na pesa au vitu fulani tu, ambavyo vinaweza kutumiwa kwa njia na kusudi linalofaa. Inatia ndani kutamani kupita kiasi utajiri, mali, au vitu vya mtu mwingine. Inaweza kutia ndani hamu isiyoweza kutoshelezwa, pupa ya kupata vitu, labda vitu vya mtu mwingine, ili tu kuwa navyo bila uhitaji wowote au bila kujali matokeo kwa wengine. Mtu mwenye tamaa anaruhusu kitu anachokitamani kitawale fikira na matendo yake hivi kwamba kinakuwa mungu wake. Kumbuka kwamba mtume Paulo anamlinganisha mtu mwenye pupa na mwabudu-sanamu, ambaye hana urithi katika Ufalme wa Mungu.—Waefeso 5:5; Wakolosai 3:5.
9. Tamaa inaweza kuonyeshwa kwa njia gani? Toa mifano.
9 Kwa kweli, Yesu alionya kuhusu “kila namna ya tamaa.” Tamaa inaonyeshwa kwa njia mbalimbali. Amri ya mwisho kati ya zile Amri Kumi inataja njia fulani kati ya hizo. Inasema hivi: “Usiitamani nyumba ya mwenzako. Usimtamani mke wa mwenzako, wala mtumwa wake wala kijakazi wake wala ng’ombe-dume wake wala punda wake wala chochote cha mwenzako.” (Kutoka 20:17) Biblia ina mifano mingi ya watu ambao wametenda dhambi nzito kwa sababu ya kuongozwa na tamaa fulani. Shetani alikuwa wa kwanza kutamani kitu ambacho kilikuwa cha mwingine, yaani, alitamani utukufu, heshima, na mamlaka ambayo ni ya Yehova peke yake. (Ufunuo 4:11) Hawa alitamani kupata haki ya kujiongoza, na alipodanganywa na tamaa hiyo aliwatumbukiza wanadamu katika dhambi na kifo. (Mwanzo 3:4-7) Roho waovu ni malaika ambao hawakutosheka na ‘mahali pao pa kwanza bali waliyaacha makao yao wenyewe yanayofaa’ na kufanya jambo ambalo hawakustahili kufanya. (Yuda 6; Mwanzo 6:2) Mfikirie pia Balaamu, Akani, Gehazi, na Yuda. Badala ya kutosheka na sehemu yao maishani, walitumia vibaya mapendeleo yao kwa sababu waliruhusu tamaa isiyotoshelezwa ya vitu vya kimwili iwaongoze katika maangamizo na uharibifu.
10. Kupatana na himizo la Yesu, tunapaswa ‘kuendelea kufungua macho yetu’ jinsi gani?
10 Inafaa kama nini kwamba kabla ya Yesu kutoa onyo kuhusu tamaa alisema maneno haya: “Endeleeni kufungua macho yenu”! Kwa nini? Kwa sababu ni rahisi sana kwa watu kuona kwamba mtu mwingine ana pupa au anatamani, lakini si rahisi wao wenyewe kukubali kwamba wana tatizo hilo. Hata hivyo, mtume Paulo anasema kwamba “kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.” (1 Timotheo 6:9, 10) Mwanafunzi Yakobo anaeleza kwamba tamaa isiyofaa, “wakati imetunga mimba, huzaa dhambi.” (Yakobo 1:15) Kupatana na himizo la Yesu, tunapaswa ‘kuendelea kufungua macho yetu,’ si kuangalia wengine kuona kama wana tamaa lakini kujichunguza wenyewe ili kuona mambo tunayotamani mioyoni mwetu kisha ‘tujilinde na kila namna ya tamaa.’
Kuwa na Vitu Vingi Maishani
11, 12. (a) Yesu alitoa onyo gani kuhusu tamaa? (b) Kwa nini tunahitaji kutii onyo la Yesu?
11 Tunapaswa kujilinda na tamaa kwa sababu nyingine. Angalia yale ambayo Yesu alisema baadaye: “Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Bila shaka, hilo ni jambo linalohitaji kufikiriwa kwa uzito katika nyakati zetu ambazo watu wanapenda mali na wanafikiri kwamba utajiri na ufanisi unaleta furaha na mafanikio. Yesu aliposema maneno hayo alikuwa akionyesha kwamba maisha yenye kusudi la kweli na yenye kuridhisha hayatokani au hayategemei vitu vya kimwili hata viwe vingi kadiri gani.
12 Hata hivyo, huenda watu fulani wakapinga hilo. Pengine wanaweza kudai kwamba vitu vya kimwili vinafanya maisha yawe yenye kustarehesha zaidi na kufurahisha, na hivyo yanakuwa yenye kusudi zaidi. Kwa hiyo, wanakazana kufuatia mambo ambayo yatawawezesha kupata vitu vya kimwili na vifaa vyote ambavyo wanatamani. Wanafikiri kwamba vitu hivyo vitawawezesha kuwa na maisha mazuri. Lakini kwa kufikiri hivyo, wanakosa kuelewa jambo ambalo Yesu alikuwa anakazia.
13. Tunapaswa kuwa na maoni gani yaliyosawazika kuhusu uhai na vitu tulivyo navyo?
13 Badala ya kuzungumza kuhusu ikiwa kuwa na vitu vingi ni sawa au si sawa, Yesu alikuwa akikazia kwamba uzima wa mtu hautokani na “vitu alivyo navyo,” yaani, vitu ambavyo tayari anavyo. Kuhusiana na hilo, sote tunajua kwamba kwa kweli hatuhitaji vitu vingi ili kuishi au kuendelea kuwa hai. Tunahitaji tu chakula kidogo, mavazi, na mahali pa kulala. Matajiri wana vitu hivyo vingi, nao maskini huenda wakalazimika kujitahidi sana ili kupata vitu wanavyohitaji. Hata hivyo, matajiri na maskini wanakuwa sawa wakati wanapokufa kwa sababu mambo yote yanaishia hapo. (Mhubiri 9:5, 6) Kwa hiyo, ili maisha yawe yenye kusudi na maana, hayawezi na hayapaswi kutegemea tu vitu ambavyo mtu anaweza kupata au kuwa navyo. Wazo hilo linaeleweka wazi zaidi tunapochunguza aina ya uzima ambao Yesu alikuwa akizungumzia.
14. Tunaweza kujifunza nini kutokana na neno linalotafsiriwa “uzima” katika Biblia?
14 Yesu alisema, ‘Uzima wa mtu hautokani na vitu alivyo navyo.’ Neno linalotafsiriwa “uzima” katika Injili ya Luka (Kigiriki, zo·eʹ) halimaanishi namna au mtindo wa maisha, bali uzima wenyewe, yaani, uhai.a Yesu alikuwa akisema kwamba tuwe matajiri au maskini, tuwe tunaishi maisha ya raha au tunapata riziki yetu kwa shida, hatuwezi kuamua urefu wa maisha yetu au hata hatuwezi kujua ikiwa kesho tutakuwa hai. Yesu alisema hivi katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?” (Mathayo 6:27) Biblia inaonyesha wazi kwamba Yehova peke yake ndiye “chemchemi ya uzima,” na ndiye peke yake anayeweza kuwapa wale walio waaminifu “uzima ulio wa kweli,” au “uzima wa milele,” uhai usio na mwisho, iwe mbinguni au duniani.—Zaburi 36:9; 1 Timotheo 6:12, 19.
15. Kwa nini watu wengi wanategemea vitu vya kimwili?
15 Maneno ya Yesu yanaonyesha jinsi ilivyo rahisi kwa watu kuwa na maoni yaliyopotoka au yasiyo sawa kuhusu maisha. Iwe ni matajiri au maskini, wanadamu wote si wakamilifu nao wana mwisho mmoja. Musa aliyeishi zamani alisema hivi: “Kwa maana siku za miaka yetu ni miaka 70; na ikiwa kwa sababu ya nguvu za pekee ni miaka 80, hata hivyo hizo husisitiza kuleta taabu na mambo yenye kuumiza; kwa maana lazima zipite upesi, nasi huruka na kwenda zetu.” (Zaburi 90:10; Ayubu 14:1, 2; 1 Petro 1:24) Kwa sababu hiyo, mara nyingi watu ambao hawajasitawisha uhusiano mzuri pamoja na Mungu wanakuwa na mtazamo ambao unatajwa na mtume Paulo wa kwamba “tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:32) Wengine wanapotambua kwamba maisha ni mafupi sana na hayategemeki, wanajaribu kutafuta usalama na maisha marefu kutokana na vitu vya kimwili. Labda wanafikiri kwamba wakiwa na vitu vingi vya kimwili, kwa njia fulani watakuwa na maisha salama zaidi. Hivyo, wanajikakamua kabisa kukusanya mali na utajiri, wakifikiri kimakosa kwamba vitu hivyo vinaleta usalama na furaha.—Zaburi 49:6, 11, 12.
Wakati Ujao Ulio Salama
16. Kusudi la kweli maishani halitegemei nini?
16 Huenda ni kweli kwamba mtu anayeishi maisha ya hali ya juu akiwa na chakula cha kutosha, mavazi, makao na vitu vingine vya kujifurahisha anaweza kuishi maisha yenye starehe zaidi au anaweza kupata matibabu mazuri zaidi na hivyo kurefusha maisha yake kwa miaka michache. Hata hivyo, je, kweli maisha ya aina hiyo yako salama zaidi na ni yenye kusudi zaidi? Kusudi la kweli maishani halitegemei miaka ambayo mtu anaweza kuishi au wingi wa vitu vya kimwili ambavyo anaweza kuwa navyo au kutumia. Mtume Paulo alionyesha hatari ya kutegemea sana vitu kama hivyo. Alimwandikia Timotheo hivi: “Uwape maagizo wale walio matajiri katika mfumo wa mambo wa sasa wasitake makuu, na waweke tumaini lao, si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie.”—1 Timotheo 6:17.
17, 18. (a) Tunapaswa kuiga mifano gani bora kuhusiana na vitu vya kimwili? (b) Ni mfano gani wa Yesu utakaozungumziwa katika habari inayofuata?
17 Si jambo la hekima kwa mtu kuweka tumaini lake katika utajiri kwa sababu ‘si hakika.’ Mzee wa ukoo Ayubu alikuwa tajiri sana, lakini msiba ulipotokea ghafula, utajiri wake haungeweza kumsaidia; utajiri wake ulipotea ghafula. Uhusiano wake mzuri sana pamoja na Mungu ndio uliomwezesha kuvumilia majaribu na mateso yote. (Ayubu 1:1, 3, 20-22) Abrahamu hakuruhusu utajiri wake umzuie kukubali mgawo mgumu kutoka kwa Yehova, naye alibarikiwa na kuwa “baba ya umati wa mataifa.” (Mwanzo 12:1, 4; 17:4-6) Tunapaswa kuiga mifano hiyo na mifano mingine. Sisi sote vijana kwa wazee, tunahitaji kujichunguza ili tuone ni nini kilicho cha maana zaidi katika maisha yetu na tumaini letu linategemea nini.—Waefeso 5:10; Wafilipi 1:10.
18 Maneno machache ambayo Yesu alisema kuhusu tamaa na maoni yanayofaa kuhusu uhai ni muhimu na kwa kweli yanafundisha. Hata hivyo, Yesu alikuwa na mambo mengine akilini, naye alisimulia mfano wenye kuchochea fikira kuhusu mtu tajiri ambaye hakutumia akili yake. Mfano huo unahusu maisha yetu leo jinsi gani, na tunaweza kujifunza nini kutokana nao? Habari inayofuata itajibu maswali hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Neno lingine la Kigiriki linalotafsiriwa “uhai” ni biʹos, ambalo linatokeza maneno ya Kiswahili kama vile “biografia” na “biolojia.” Kulingana na kamusi moja (Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words), neno biʹos linamaanisha “kipindi au urefu wa maisha,” “namna ya maisha,” na “riziki ya maisha.”
-
-
Je, Wewe Ni “Tajiri Kwa Mungu”?Mnara wa Mlinzi—2007 | Agosti 1
-
-
Je, Wewe Ni “Tajiri Kwa Mungu”?
“Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.”—LUKA 12:21.
1, 2. (a) Watu wamekuwa tayari kujidhabihu sana ili kupata nini? (b) Ni lazima Wakristo wakabili hatari na hali gani ngumu?
KUTAFUTA HAZINA si kama mchezo wa kutafuta kitu kilichofichwa ambao watoto wanapenda kucheza. Kwa miaka mingi sana na katika jamii nyingi watu wamekuwa wakitafuta hazina halisi. Kwa mfano, katika karne ya 19 juhudi za kuhamia katika maeneo yenye migodi ya dhahabu huko Australia, Afrika Kusini, Kanada, na Marekani ziliwavutia watu kutoka sehemu za mbali sana. Watu hao walikuwa tayari kuacha wapendwa wao na makao yao ili kutafuta utajiri katika nchi za kigeni ambazo nyakati nyingine zilikuwa na hali ngumu sana. Ndiyo, watu wengi wako tayari kujihatarisha kabisa na kujidhabihu sana ili kupata utajiri ambao mioyo yao inatamani.
2 Ingawa watu wengi leo hawatafuti hazina kihalisi, wanalazimika kujitahidi sana ili kupata mahitaji ya lazima. Kufanya hivyo katika mfumo huu wa mambo kunaweza kuwa jambo gumu, lenye kuchosha, na lenye kulemea sana. Ni rahisi kuhangaikia sana chakula, mavazi, na makao hivi kwamba tunapuuza au hata kusahau mambo yaliyo ya maana zaidi. (Waroma 14:17) Yesu alitoa mfano ambao unaonyesha wazi kabisa mwelekeo huo wa wanadamu. Mfano huo uko katika andiko la Luka 12:16-21.
3. Eleza kwa ufupi mfano wa Yesu katika Luka 12:16-21.
3 Yesu alitoa mfano huo wakati uleule alipozungumzia uhitaji wa kujilinda na tamaa, ambao tulizungumzia kwa undani katika habari iliyotangulia. Baada ya kutoa onyo kuhusu tamaa, Yesu alitoa mfano wa mtu tajiri ambaye hatosheki na maghala yaliyojaa vitu vyema ambavyo tayari alikuwa amekusanya, badala yake anabomoa maghala hayo na kujenga maghala makubwa zaidi ili akusanye vitu vyema vingi zaidi. Wakati tu anapofikiri kwamba sasa anaweza kupumzika na kujifurahisha, Mungu anamwambia kwamba uhai wake unafikia mwisho, na vitu vyote vyema ambavyo ameweka akiba vitachukuliwa na mwingine. Kisha Yesu anamalizia kwa maneno haya: “Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.” (Luka 12:21) Tunaweza kujifunza somo gani kutokana na mfano huo? Tunaweza kutumia jinsi gani somo hilo katika maisha yetu?
Mtu Mwenye Tatizo
4. Tunaweza kusema mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu alikuwa mtu wa aina gani?
4 Watu wengi wanajua mfano huo ambao Yesu alitoa. Tunaona kwamba Yesu alianza kusimulia mfano huo kwa maneno haya: “Shamba la mtu fulani tajiri lilizaa vizuri.” Yesu hakusema kwamba mtu huyo alipata utajiri wake kwa udanganyifu au kwa njia isiyo halali. Kwa maneno mengine, hakusema kwamba mtu huyo alikuwa mbaya. Kwa kweli, kutokana na maneno ya Yesu, ni jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba mtu huyo alikuwa amefanya kazi kwa bidii. Angalau inaweza kuonekana kwamba alikuwa mtu ambaye alifanya mipango na kuweka akiba kwa ajili ya wakati ujao, labda ili familia yake iwe na maisha mazuri. Hivyo, kwa maoni ya watu, anaweza kuonwa kuwa mtu mwenye bidii ambaye alichukua wajibu wake kwa uzito.
5. Mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu alikabili tatizo gani?
5 Kwa vyovyote vile, katika mfano huo Yesu alimwita mtu huyo tajiri, yaani, mtu ambaye tayari alikuwa na vitu vingi vya kimwili. Hata hivyo, kama Yesu alivyoeleza, tajiri huyo alikuwa na tatizo. Shamba lake lilizaa mazao mengi kuliko alivyotazamia, mengi zaidi kuliko kiasi alichohitaji au ambacho angeweza kutunza. Angefanya nini?
6. Watumishi wengi wa Mungu leo wanakabili maamuzi gani?
6 Watumishi wengi wa Yehova leo wanakabili hali ambayo inalingana sana na ya tajiri huyo. Wakristo wa kweli wanajitahidi kuwa wanyoofu, wenye bidii, na wafanyakazi wenye kutegemeka. (Wakolosai 3:22, 23) Iwe wameajiriwa kazi au wana biashara zao wenyewe, mara nyingi wanafaulu na hata kufanikiwa sana katika kazi yao. Wanahitaji kufanya uamuzi wanapopewa nafasi ya kupandishwa cheo au kupata nafasi mpya za biashara. Je, wakubali vyeo hivyo au nafasi hizo za kupata pesa zaidi? Vivyo hivyo, vijana wengi Mashahidi wanafanya vizuri shuleni. Kwa sababu hiyo, wanaweza kupewa nafasi ya kupata elimu ya juu katika vyuo maarufu. Je, wanapaswa kukubali tu nafasi hizo kama watu wengi wanavyofanya?
7. Mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu alitatua tatizo lake jinsi gani?
7 Tukichunguza tena mfano wa Yesu, yule mtu tajiri alifanya nini wakati shamba lake lilipozaa vizuri hivi kwamba hakuwa na mahali pa kuweka mavuno yake? Aliamua kubomoa maghala ambayo alikuwa nayo na kujenga makubwa zaidi ili aweke akiba nafaka yake yote ya ziada na vitu vyema. Inaonekana alitosheka na mpango huo na kujihisi akiwa salama hivi kwamba akawaza: “Nami nitaiambia nafsi yangu: ‘Nafsi yangu, una vitu vyema vingi vilivyokusanywa kwa miaka mingi; starehe, ule, unywe, na kujifurahisha.’”—Luka 12:19.
Kwa Nini ‘Hakuwa na Akili’?
8. Mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu alipuuza jambo gani la maana?
8 Hata hivyo, kama Yesu alivyoonyesha, mipango ya mtu huyo tajiri ilimfanya ahisi usalama usio wa kweli. Ingawa huenda mipango hiyo ilionekana kuwa mizuri, mtu huyo alipuuza jambo fulani la maana, yaani, mapenzi ya Mungu. Mtu huyo alikuwa akijifikiria mwenyewe tu, jinsi ambavyo angestarehe na kula, kunywa, na kujifurahisha. Alifikiri kwamba kwa sababu alikuwa na ‘vitu vingi vyema’ angeishi pia “miaka mingi.” Lakini inasikitisha kwamba mambo hayakuwa hivyo. Kama tu Yesu alivyosema mapema, “hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Usiku huohuo, jitihada zote za mtu huyo zilifikia mwisho ghafula, kwa sababu Mungu alimwambia hivi: “Wewe usiye na akili, usiku huu wanadai nafsi yako kutoka kwako. Basi, vitu ulivyoviweka akiba vitakuwa vya nani?”—Luka 12:20.
9. Kwa nini yule mtu katika mfano wa Yesu aliitwa asiye na akili?
9 Sasa tumefikia jambo kuu la mfano wa Yesu. Mungu alisema kwamba mtu huyo hakuwa na akili. Kamusi moja (Exegetical Dictionary of the New Testament) inaeleza kwamba namna mbalimbali za neno la Kigiriki linalotumiwa hapo “sikuzote zinamaanisha kutoelewa.” Kamusi hiyo inasema kwamba katika mfano huo, Mungu anatumia neno hilo ili kuonyesha kwamba “mipango ya wakati ujao ya tajiri haina maana yoyote.” Neno hilo linahusu “mtu ambaye anakataa kumtegemea Mungu” wala si mtu ambaye si mwerevu. Maelezo ya Yesu kumhusu yule mtu tajiri yanatukumbusha yale ambayo aliwaambia baadaye Wakristo wa kutaniko la karne ya kwanza la Laodikia, huko Asia Ndogo: “Unasema: ‘Mimi ni tajiri, nimejipatia utajiri na sihitaji kitu chochote hata kidogo,’ lakini hujui kwamba wewe ni mwenye taabu na wa kusikitikiwa na maskini na kipofu na uchi.”—Ufunuo 3:17.
10. Kwa nini kuwa na “vitu vyema vingi” si uhakikisho wa kuishi “miaka mingi”?
10 Tunapaswa kufikiria kwa uzito somo la mfano huo. Je, tunaweza kuwa kama mtu aliye katika mfano huo na kufanya kazi kwa bidii sana ili kuhakikisha kwamba tuna “vitu vyema vingi” lakini tukose kufanya yale tunayohitaji kufanya ili kuwa na tumaini la kuishi “miaka mingi”? (Yohana 3:16; 17:3) Biblia inasema hivi: “Vitu vyenye thamani havitakuwa na faida yoyote siku ya ghadhabu,” na “anayetegemea utajiri wake—yeye mwenyewe ataanguka.” (Methali 11:4, 28) Kwa hiyo, Yesu alimalizia mfano wake kwa himizo hili: “Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.”—Luka 12:21.
11. Kwa nini ni ubatili kuweka tumaini na usalama katika vitu vya kimwili?
11 Yesu aliposema “hivyo ndivyo huwa,” alikuwa akimaanisha kwamba mambo yaliyompata yule tajiri katika mfano huo yatawapata pia wale ambao wanajenga maisha yao, yaani, wanaweka tumaini lao na usalama wao katika vitu vya kimwili. Kosa si ‘kujikusanyia mwenyewe hazina’ lakini ni kutokuwa “tajiri kwa Mungu.” Mwanafunzi Yakobo alitoa onyo kama hilo alipoandika hivi: “Haya, basi, ninyi ambao husema: ‘Leo au kesho tutasafiri kwenda jiji fulani nasi tutakaa mwaka mmoja huko, tutafanya biashara na kupata faida,’ ingawa hamjui uzima wenu utakuwa namna gani kesho.” Wanapaswa kufanya nini? “Badala yake, mnapaswa kusema: ‘Yehova akipenda, tutaishi na pia kufanya hili au lile.’” (Yakobo 4:13-15) Hata mtu awe tajiri namna gani au awe na vitu vingi kadiri gani, vyote vitakuwa ubatili ikiwa yeye si tajiri kwa Mungu. Basi, ni nini maana ya kuwa tajiri kwa Mungu?
Kuwa Tajiri kwa Mungu
12. Tutakuwa matajiri kwa Mungu tukifanya nini?
12 Yesu alisema kwamba kuwa tajiri kwa Mungu ni tofauti kabisa na kujiwekea hazina za vitu vya kimwili, au kujitafutia utajiri wa kimwili. Hivyo, Yesu alikuwa akisema kwamba hangaiko letu kuu maishani halipaswi kuwa kukusanya utajiri wa kimwili au kufurahia vitu tulivyo navyo. Badala yake, tunapaswa kutumia mali zetu kwa njia ambayo itaboresha, au kujenga, uhusiano wetu pamoja na Yehova. Tukifanya hivyo, bila shaka tutakuwa matajiri kwa Mungu. Kwa nini? Kwa sababu tutaweza kupata baraka nyingi kutoka kwake. Biblia inatuambia hivi: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”—Methali 10:22.
13. Baraka ya Yehova “hutajirisha” namna gani?
13 Yehova anapowabariki watu wake, sikuzote anawapa vitu vilivyo bora. (Yakobo 1:17) Kwa mfano, Yehova alipowapa Waisraeli nchi, “ilikuwa nchi inayotiririka maziwa na asali.” Ingawa nchi ya Misri pia ilisemwa kuwa hivyo, nchi ambayo Yehova aliwapa Waisraeli ilikuwa tofauti angalau katika njia moja muhimu. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: Ni “nchi ambayo Yehova Mungu wako anaitunza.” Kwa maneno mengine, wangefanikiwa kwa sababu Yehova angewatunza. Maadamu Waisraeli waliendelea kuwa waaminifu kwa Yehova, aliwabariki sana na ni wazi kwamba waliishi kwa njia bora kuliko mataifa yote yaliyowazunguka. Ndiyo, baraka ya Yehova ndiyo “hutajirisha”!—Hesabu 16:13; Kumbukumbu la Torati 4:5-8; 11:8-15.
14. Wale walio matajiri kwa Mungu wanapata nini?
14 Maneno “tajiri kwa Mungu” yanatafsiriwa pia kuwa “tajiri mbele ya Mungu” (Biblia Habari Njema) au “tajiri machoni pa Mungu.” (The New Testament in Modern English, ya J. B. Phillips) Wale ambao ni matajiri kimwili kwa ujumla wanahangaikia jinsi ambavyo wanaonwa na wengine. Mara nyingi njia yao ya maisha inaonyesha hivyo. Wanataka kuwapendeza watu kwa ‘kujionyesha mali yao maishani’ kama Biblia inavyosema. (1 Yohana 2:16) Kinyume chake, wale ambao ni matajiri kwa Mungu wanapata kibali, upendeleo, na fadhili nyingi zisizostahiliwa kutoka kwa Mungu, na wana uhusiano wa karibu pamoja naye. Bila shaka, kuwa katika hali hiyo nzuri sana kunawaletea furaha na usalama, baraka nyingi ambazo utajiri wa kimwili hauwezi kuleta. (Isaya 40:11) Swali linalobaki ni, Ni lazima tufanye nini ili tuwe matajiri machoni pa Mungu?
Tajiri Machoni pa Mungu
15. Tunapaswa kufanya nini ili tuwe matajiri kwa Mungu?
15 Mtu anayetajwa katika mfano wa Yesu alipanga na kufanya kazi ngumu ili ajitajirishe, naye aliitwa asiye na akili. Kwa hiyo, ili tuwe matajiri kwa Mungu, tunapaswa kujitahidi kabisa kushiriki kikamili katika utendaji ambao ni wa maana na wenye thamani kikweli machoni pa Mungu. Utendaji huo unatia ndani amri hii ya Yesu: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mathayo 28:19) Kutumia wakati, nguvu, na vipawa vyetu katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi wala si kuboresha maisha yetu kunaweza kulinganishwa na kuwekeza pesa katika biashara. Wale ambao wamefanya hivyo wamepata baraka nyingi sana za kiroho, kama mambo yafuatayo yanavyoonyesha.—Methali 19:17.
16, 17. Unaweza kusimulia mambo gani yaliyoonwa ili kuonyesha njia ya maisha ambayo inamfanya mtu awe tajiri machoni pa Mungu?
16 Mfikirie mwanamume mmoja Mkristo katika nchi fulani ya Asia. Alikuwa fundi wa kompyuta naye alipata mshahara mnono. Hata hivyo, kazi yake ilichukua wakati wake wote na hivyo akadhoofika kabisa kiroho. Mwishowe, badala ya kujaribu kufanya maendeleo katika kazi hiyo, aliiacha na kuanza kutengeneza aiskrimu (glace) na kuiuza mitaani, ili awe na wakati zaidi wa kushughulikia mahitaji na wajibu wake wa kiroho. Wafanyakazi wenzake wa zamani walimdhihaki, lakini matokeo yalikuwa nini? Alisema hivi: “Kwa kweli, nilipata pesa nyingi zaidi kuliko nilizopata nilipokuwa nikifanya kazi ya kompyuta. Nimepata furaha zaidi kwa sababu sina mfadhaiko wala wasiwasi kama niliokuwa nao katika kazi yangu ya zamani. Jambo la maana zaidi ni kwamba sasa ninajihisi nikiwa karibu zaidi na Yehova.” Kubadili kazi kulimwezesha Mkristo huyo kuanza huduma ya wakati wote, na hivi sasa anatumika katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi yake. Kwa kweli, baraka ya Yehova ‘inatajirisha.’
17 Mfano mwingine ni wa mwanamke ambaye alilelewa katika familia ambayo ilithamini sana elimu. Alipata elimu katika vyuo vikuu nchini Ufaransa, Mexico, na Uswisi, naye alitumaini kupata kazi nzuri. Alisema hivi: “Nilifanikiwa; niliheshimiwa na kupewa mapendeleo ya pekee, lakini moyoni nilihisi kwamba maisha yangu hayana maana yoyote, nami sikutosheka hata kidogo.” Kisha alijifunza kumhusu Yehova. Anasema hivi: “Kadiri nilivyofanya maendeleo ya kiroho, tamaa yangu ya kumpendeza Yehova na kumshukuru angalau kidogo kwa ajili ya mambo aliyonipa ilinisaidia kuelewa wazi jambo nililopaswa kufanya, yaani, kumtumikia kwa wakati wote.” Aliacha kazi yake na muda si muda akabatizwa. Kwa miaka 20 iliyopita, amefurahi kutumika katika huduma ya wakati wote. Anasema: “Watu fulani wanafikiri kwamba nimepoteza vipawa vyangu, lakini wanatambua kwamba nina furaha, nao wanavutiwa na kanuni ambazo ninafuata maishani. Kila siku ninamwomba Yehova anisaidie kuwa mnyenyekevu ili nipate kibali chake.”
18. Kama Paulo, tunaweza kuwa matajiri kwa Mungu jinsi gani?
18 Sauli, ambaye alikuja kuwa mtume Paulo, alikuwa na nafasi ya kupata kazi nzuri sana. Hata hivyo, aliandika hivi baadaye: “Kwa kweli naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu Bwana wangu.” (Wafilipi 3:7, 8) Paulo aliona kwamba utajiri ambao alipata kupitia Kristo ulikuwa wenye thamani zaidi kuliko kitu chochote ambacho ulimwengu ungempa. Vivyo hivyo, tukiacha miradi ya kichoyo na kufuatia maisha ya ujitoaji-kimungu, sisi pia tunaweza kuwa matajiri machoni pa Mungu. Neno la Mungu linatuhakikishia hivi: “Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima.”—Methali 22:4.
-